Unapenda MOVIES? (SESSION 03) Usikose hizi wiki hii...

Oya naweza zipataje
Niaje wazee? Natumai mnaendelea vema huku mkiendeleza mapambano dhidi ya janga hili la Corona. Tafadhali usipuuzie, ni serious na inaua. Usingoje serikali ikuchukulie hatua, bali chukua mwenyewe kwa ajili ya familia yako.

Basi kama ilivyo kawaida, leo hii nitajaribu kushirikiana nanyi baadhi ya filamu ambazo waweza tumia muda wako kuzitama. Filamu hizo, moja baada ya nyingine, nitazielezea kadiri ya uelewa wangu na hivyo basi kama ikikuvutia, waweza itafuta kutazama. Kama kutakuwa na maswali ruksa kuuliza maana filamu wote twaweza itazama lakini tukaelewa tofauti ama mwingine akashindwa kuelewa kabisa akaishia kusema filamu ile hamna kitu, kumbe uelewa wake ndo tatizo.

Kwa wale ambao ni wageni, mnaweza pitia session 1 na 2 hapa...

Unapenda movies? Pitia hapa kidogo - JamiiForums

Unapenda movies? Tazama hizi weekend hii! - JamiiForums

Basi na tuanze...

1. SHUTTER ISLAND ya 2014.

"Which would be worse: to live as a monster or to die as a good man?"
(Kipi kitakuwa kibaya zaidi: kuishi kama dubwana ama kufa kama mtu mwema?)
View attachment 1427391
Ndani ya filamu hii kuna mtu mzima Leonardo Dicaprio, mzee ambaye hana historia ya kuchafua wasifu wake inapokuja kwenye swala la kazi. Humu pia, kama ilivyo ada, 'katisha' sana. Ameutendea haki uhusika wake.

Hii ni filamu ambayo hutuonyesha ni namna gani hisia za ukosefu (guilty) zinavyoweza kumpagawisha mtu kiasi kwamba maisha yake yakawa tafarani ya nyoka, kujongea na tumbo kusikia na ulimi!

Ni filamu ambayo hutuonyesha namna gani matendo tunayoyafanya yanavyoweza kuathiri akili zetu kiasi kwamba katika kupambana na kutokuyaridhia tuliyoyafanya, sababu si mazuri na yanatisha, tunajikuta tena tukiwa tumevaa uhusika wa uongo kujiridhisha na kupoozesha nafsi zetu na hata kuwapendeza wale wanaotutazama.

IPO HIVI: Bwana Teddy, mpelelezi wa kiserikali, anajikuta katika kazi ya kupeleleza kisa cha mfungwa mwanamke mwenye ugonjwa wa akili aliyetoroka toka kwenye mahifadhi maalum yaliyotengwa mbali katika kisiwa cha Shutter.

Katika kisiwa hicho, tofauti na visiwa vingine, kumekaliwa na taasisi moja tu ya serikali ambayo huonekana ni ya siri ikiwa inahusika na kuwatunza wafungwa ambao si wa kawaida bali waliotenda matukio makubwa na ya kutisha na pia wanasumbuliwa na matatizo ya akili!

Bwana huyo Teddy akiwa anaelekea huko kisiwani anapata kujuana na mtu mtiifu ambaye anajinasibu ni msaidizi wake ambaye ametumwa kuja kumsaidia kwenye operesheni yake anayoenda kufanya. Wanapofika kisiwani huko wanaanza kazi na kubaini mazingira tatanishi kuhusu mlengwa wao, mosi haijulikani ametorokea wapi kwani mlango ulikuwa umefungwa na madirisha pia yamepambwa na nondo. Lakin pia vilevile, hali ya hewa ilikuwa ya mvua kubwa na pasipo kujali mawe na miiba, mfungwa alitoroka pasi na viatu.
Kama haitoshi napo aliyekuwa anasimamia kwa siku hiyo alikuwapo koridoni lakini anasema hakuona mtu yeyote akikatiza!

Bwana Teddy na mwenzake wanahaha kutafuta majibu. Kwa bahati mbaya ama nzuri ndani ya chumba cha mfungwa wanapata kuona karatasi iliyoandikwa kwa mwandiko wa mfungwa aliyepotea, kikisomeka - MGONJWA No. 67.

Wanapofuatilia idadi ya wagonjwa ndani ya hiyo hospitali nzima wanabaini ni 66, je huyo wa 67 ni nani? ... kadiri bwana huyu anavyozidi kutafuta majibu ndivyo anavyozidi kuamini kuna kitu kiovu mno na cha siri kuu kinafanyika hapa kisiwani juu ya hawa wafungwa wenye magonjwa ya akili ... kwanini baadhi ya nyaraka zinafichwa? Na mbona ushirikiano wa utawala kwa wapelelezi ni finyu sana?

Bwana Teddy anahisi kabisa kuna kitu hakipo sawa wanafanyiwa wahanga hawa wasiojitambua ... lakini zaidi ya yote, anakuja kujivumbua yeye mwenyewe sie yule aliyekuwa anajidhania... hata hilo jina analolitumia si lake .... Aisee... ni hatari ya kishada fukweni!

Sasa Je, bwana Teddy anapojivumbua, ataikubali 'new identity' yake? Mfungwa huyo nambari 67 ni nani? Huyo mtu aliyekutana naye kwa usafiri wakielekea shutter island ni kweli wa kuaminika? Na nini haswa kinachoendelea kisiwani?

Tafuta miwa kabisa maana popcorn haitakutosha!

2. COUNTDOWN ya 2020.

"If you could find out exactly when you're going to die...would you want to know?"
(Kama ungaliweza kujua haswa ni lini utakufa ... je ungalitaka kujua?)
View attachment 1427390
Kifo ni fumbo la siri. Na kuwa hivyo kama fumbo ndo' kunafanya tuishi kwa amani kabisa, tunakula na tunakunywa hata kama tutakufa kesho, alimradi tunakuwa hatujui basi hamna noma! Laiti kama watu wangelikuwa wanajua wanakufa lini, hakika maisha haya yasingekuwa hivi yalivyo sasa.

Huenda yangekuwa tafrani zaidi kwa sababu ya hofu ya kifo kiasi kwamba watu wasingefurahia maisha kabisa, au kwa wengine yangekuwa mtafutano wa amani mapema kujiandaa na maisha ya baada ya kifo hivyo kuondoa kabisa maana ya maisha, kwani badala ya kuyaishi watu watakuwa wapo tu kwa ajili ya vijavyo.

Kumbe kwa kiasi hicho, ladha ya maisha ni fumbo la siri ya kifo eti?

IPO HIVI: Hapo zamani sana kuna mwanamfalme ambaye alikaimu jeshi la himaya yao baada ya baba yake (mfalme) kuumwa hoi kitandani. Hivyo mwanamfalme huyo akatakiwa kuongoza jeshi lao kwenda kupigana dhidi ya adui.
Kwa kutaka kufahamu hatma yake, mwanafalme akamtafuta 'mtaalamu' na kumuuliza kama je, atarejea nyumbani akiwa hai? Mtaalamu akamweka bayana kwamba aweza kumwambia ukweli lakini kwa sharti moja, hatakiwi kubadili hatma yake hiyo!

Baada ya hapo akamwelezea kuwa atakufa huko vitani. Mwanamfalme kwa kutaka kujiokoa na nafsi yake, akaepuka kwenda vitani. Matokeo yake akawa amevunja masharti, akawa amejipa laana na hivyo basi kifo chake kikaja kudai haki yake kwa njia ya kikatili zaidi!

Sasa hiyo ilikuwa ni zamani huko. Sasa kutokana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia, hakuna tena mtaalamu wa kuonana naye kukwambia hatma yako, badala yake kuna 'application' ambayo sio kwamba inabashiri bali inakupa muda halisi wa kifo chako!

Punde unapopakua app hiyo, hutaweza kuifuta tena. Hata kama ukibadili simu na 'line' bado itakuwa palepale mpaka kifo chako. Sasa shida inakuja wapi? Pale penye kujua unakufa lini tena muda ukiwa ni mfupi tu baadae!

Je, utaamini kwanza kama utakufa? Na kama ukiamini utakaa kungoja kwa amani kifo chako ama ndo utataka upambane kujinasua na hatma yako?

Kumbuka hii app haikupi muda wako halisi wa kufa ili uuepuke bali tu uufahamu na hivyo basi unapofanya namna yoyote kuepuka hatma yako hapo ndo shida huanzia, kwani kuna kiumbe kitahusika na wewe kama adhabu mpaka pale muda wako halisi uliokuwa umepangiwa utimie!

Alafu sasa, kila kitu kilikuwa kimeandikwa kwenye 'Terms and Agreements' ya application hiyo ila si unajua sasa sie huwa hatusomagi, hahahh! ukidownload wewe ni kuweka tiki tu uende zako kumbe unajiweka kwenye mikataba!

Sasa mwanadada fulani, nesi, anajikuta katika kisanga hiki. Anashuhudia kesi mbalimbali za app hii na hivyo anaamua kuipakua ashuhudie, tahamaki anaona muda wake ni mchache mno! na si tu yeye peke yake, bali na mdogo wake vilevile. Je, wapo tayari kufanya nini kuepuka hatma yao?

Ni checherumba bwana!

3. IN TIME ya 2011.

"For a few to be immortal. Many must die."
(Kwa wachache kuishi milele. Wengi lazima wafe.)
View attachment 1427389
Maisha yetu haya ni bure kabisa. Ndio kuna wanaoishi kwenye majumba ya kifahari na wengine kwenye mbavu za mbwa, ndio kuna wanaokula na kusaza ingali wengine kupata mlo ni ngekewa, lakini kati yetu sote hakuna anayelipia ili apate kuishi na ndo' mana uwe tajiri ama maskini, wote tutakufa tu. Huwezi kuhonga uongezewe muda wa kuishi. Hata pesa zina kikomo cha kukupa huduma.

Sasa vipi kama maisha haya yangekuwa ya kununua? Yani kama uendavyo dukani na kusema nipewe umeme wa buku nawe uende kusema niongezewe maisha ya buku nisogeze siku kadhaa? Ingekuaje mzee? ... si mchezo! Yani huku ndo mtu akikwambia 'Dont waste my time' basi ujue anamaanisha kweli asemacho.

IPO HIVI: Katika miaka ya mbele kabisa, watu wanazaliwa wakiwa na kikomo cha muda wa kuishi wa miaka ishirini na tano tu! Baada ya hapo unapewa muda wa mwaka mmoja wa ziada ambapo ndo unakuwa mwisho wa 'dezo', baada ya huo mwaka inakuwa sasa ni juu yako juu ya wapi utapata muda uendelee kuishi zaidi.
Katika hii jamii muda ndo pesa. Yani mtu anafanya kazi na kulipwa muda wa kuishi. Hivyo kwa matajiri wao wanaishi milele lakini kwa hawa masikini, pangu pakavu tia mchuzi, ni mahangaiko na mateso. Wanalazimika kukopa, kuomba, kuiba na hata kuua alimradi waupate muda. MUDA NI MALI!

Mwenye muda ndo tajiri. Mwenye muda ndo anatawala jamii, humu wanawaita 'Time Keepers'.

Basi bwana mmoja aitwaye Will Salas (Justin Timberlake) anafanikiwa kumwokoa kigogo mmoja dhidi ya genge la wahalifu, na kwenye kumtunuku shukrani, bwana huyo anampatia Will miaka yake mia moja na kitu ya kuishi duniani.

Lakini sababu tajiri ni tajiri, fukara hathaminiki (in professor Jay's voice kwenye Zali la mentali) bwana Will anaonekana mwivi akituhumiwa kumuua kigogo ili avune muda wake, hivyo anaanza kutafutwa!

Siku moja akiwa kwenye tafrija anapata kuongea na msichana aliyevutiwa naye, kwa jina Sylvia. Lakini akiwa hapo anataka kukamatwa na mtunza muda kwa tuhuma zake za wizi, bwana Will anamteka binti huyo na kutoroka naye mpaka kwake kabisa.

Huko Will na Sylvia wanapata kutengeneza 'combo' matata sana inayodhamiria kuiba muda mwingi sana kutoka kwa mabwanyenye wanaowakandamiza maskini, na kwa wakati huohuo kupambania maisha yao.
Will they be in time? (Je, watakuwa ndani ya muda?)

Bwana bwana.... huwaga unadhani ka-Justin Timberlake ni kamwanaume ka-mapenzi tu enh? Katazame uone kazi yake humo ndani.

4. TRUTH OR DARE ya 2017.

"We are not playing the game, it's playing us."
(Hatuuchezi mchezo bali ni wenyewe ndo unatucheza sisi.) - Olivia.
View attachment 1427384
Kilichonifanya nikaipenda hii filamu ni namna walivyoigeuza game ya truth or dare (ukweli ama kuthubutu) kuwa katika wazo linalofanya mtu afuatilie akitaka kujua nini hatma ya washiriki katika huu mchezo.

Kwa watu wasiofahamu mchezo huu ni upo hivi, kila mtu anakuwa na machaguzi mawili ambapo atatakiwa kuchagua kimoja kati ya kusema jambo fulani la kweli kabisa kutokana na alichoulizwa ama basi athubutu kufanya jambo fulani atakaloagizwa pasipo kupinga.

Game hii ni maarufu sana ulimwenguni na kwakupitia hiyo, kampuni ambayo huwekeza sana kwenye filamu za 'horror' - BLUMHOUSE -wakaona fursa nzuri ya kuifanyia kitu kwa kuongezea hiki na kile kama vionjo na ladha. Na kweli wakafanikiwa kutoa kigongo hiki.

S'kiza hapa ...

Kikundi cha vijana kadhaa wanafunga safari kwenda zao Rosarito, Mexico. Wakiwa huko katika namna ya kipekee, wanakutana na kijana mmarekani anayejitambulisha kwa jina la Carter, ndani ya muda mfupi Carter anafanikiwa kushawishi kikundi hiki waongozane naye kwenda kwenye ghofu fulani wanywe na kufurahia.

Wakiwa huko, Carter anaanzisha mchezo wa 'Truth or Dare' ambapo anawataka wenzake washiriki. Wakiwa wanaucheza mchezo huo, Carter anafikiwa zamu yake na anaulizwa kwanini amewaleta watu kwenye jengo hilo, kwakuwa mchezo hautaki mtu adanganye (hapa bado anajua yeye mwenyewe tu kuhusu uhalisia wa mchezo huu ya kwamba ukienda kombo ni kifo) anasema ukweli kuwa amewarubuni ili waje wachukue nafasi yake katika mchezo huu wa laana na kifo ili sasa naye awe huru!

Bwana Carter anawapa maelekezo kwamba mchezo huu sio wa kupuuza. Endapo swali likiulizwa basi lijibiwe kweli, na mtu akipewa thubutu basi afanye kweli, la sivyo ni KIFO!

Anaongezea kwa kusema wenzake wote walishakufa akabakia yeye peke yake.
Kuanzia hapo sasa ndo mambo yanaanza kubadilika. Tayari kundi hili linakuwa limesajiliwa katika mchezo wa kifo ambapo hauwezi kutoka ukitoka hai ... mchezo ambao umetwaliwa na kuendeshwa na jini aitwaye Calax! Akiuliza maswali ya siri kubwa yanayotetemesha watu kuyajibu na kuwafanya washiriki wathubutu kufanya mambo ya hatari kupita kiasi!

Je, haya yametokea wapi? Nakugusia kidogo...

Hapo nyuma kulikuwa na kanisa ambalo mchungaji wake alikuwa akiwaonea na kuwaendesha 'masister' kwa njia ya uovu. Kwa kumkomesha, mmoja wa masister akafanya kusudi kufanya ibada ya kumwita jini Calax kwa kukata ulimi wake na kuufungia ndani ya chungu.

Baada ya muda mchungaji akapata fundisho lake kwa kufa na hata hatimaye kanisa likatelekezwa kuwa ghofu. Basi siku moja ingali watu walivyoenda kutembelea ghofu hilo, pasipo kujua, wakavunja chungu kile kilichokuwa kimemshikilia jini Calax, na kwasababu watu hao walikuwa wanacheza mchezo huo wa 'Truth or dare', jini hilo likajimilikisha mchezo huo na kuutumia kumaliza wahusika mmoja baada ya mwingine!

Na kumbuka kua katika mchezo huu, maswali ya kusema ukweli yanaulizwa mara mbili tu, baada ya hapo hata kama ukisema upewe jaribio la kusema ukweli, mchezo utakataa. Utatakiwa uthubutu kufanya jambo!! ... jambo la HATARI!
Je, kundi hili lililorubuniwa na Carter litaenda mpaka wapi? Nani atafanikiwa kuvunja laana ya mchezo huu? Na kwa namna gani?

Usikose utamu huu ndugu yangu. Jifungie utazame zako usiku, yani utasahau hata kama kuna Corona.

5. WHAT HAPPENED TO MONDAY ya 2017.

"What happens to one of you, happens to all of you."
(Kitachomtokea mmoja wenu, kitawatokea wote.)
View attachment 1427383
Kuna baadhi ya watu wanaamini kuna programu (au kutakuwa na programu) maalumu ya kupunguza idadi ya watu waliopo na watakaokuwepo duniani.
Programu hizo, kama inavyoaminika na baadhi ya watu, zitakuwa zinashikiliwa na kuendeshwa na baadhi ya taasisi na serikali zenye nguvu wakishinikizwa na uhaba wa rasilimali endapo watu wakizidi kuzaliana ndani ya ulimwengu huu.

Watu hao, kama waaminivyo, kuongezeka kwa idadi ya watu ni tishio sana kwani itakuja kuchochea uhaba mkubwa wa rasilimali na hatimaye kusababisha machafuko, uhalifu na migogoro kuongezeka ndani ya jamii kupita kiasi cha kuweza kumudu.

Hivyo wanasihi kuongezeka kwa idadi ya watu kuwe 'controlled and manipulated' kwa hisani ya nanufaa ya watu wa sasa na haswa wa baadae ili kuepusha majanga zaidi.

Kwa mtazamo huo basi, sera mbalimbali za uzazi wa mpango zinaasisiwa na kusimamiwa ili kupunguza uzao wa watu, mathalani China kuanzia miaka ya 1960 na kitu ambapo walianza na sera ya watoto wawili (two children policy) na baadae kuanzia mwaka 1979 wakaiboresha makali na kuwa sera ya mtoto mmoja tu, sera ambayo ilidumu tokea mwaka huo na kuja kukomea 2015.
Sasa je, vipi ikatokea sera kali na namna hiyo katika nchi yako na wewe ukawa hauko tayari kupoteza watoto wako kwa hali yoyote ile? Alafu ubaya zaidi, si watoto wawili basi, sita!!

S'kiza hapa...

IPO HIVI; Katika ya miaka ya mbele huko, 2040's, kunakuwa na janga kubwa la watu kuwa wengi kupita kiasi kutokana na madhara ya GMO foods (Genetic Modified), yani vyakula vilivyokuzwa kisayansi.

Watu hao kuwa wengi kupita maelezo inapelekea serikali kuanzisha sera kali ya kila familia kuwa na mtoto mmoja tu, na endapo ikitokea wakawa zaidi basi hutengwa na familia zao na kwenda kuhifadhiwa kwenye mashine maalum ya usingizi ili waje kuamka miaka ya baadae mambo yakiwa yamebadilika, lakini kiuhalisia hiyo ilikuwa ni danganya toto tu, watu hao walikuwa wakiuawa.

Sasa familia moja bwana katika ulimwengu huu, inabahatika kupata watoto saba (septuplets). Mama anafariki katika uzazi na kuwaacha watoto mikononi mwa babu yao ambaye anawalea kwa siri mpaka kukua kwao.
Watoto hao wamefanana sana, hivyo basi sababu za kuwalinda, babu yao anawapa majina kutokana na siku za juma, yani kuna Monday, Tuesday mpaka Sunday. Na wote hao wanatakiwa kuigiza kuwa mtu mmoja tu, hivyo wapeane siri zao na kujuzana kilakitu, na kila mmoja anatoka siku ya jina lake tu.

Sasa mambo yanakuwa 'peace' tu mpaka pale siku moja Monday anapotoka na harudi tena nyumbani. Na ubaya ni kwamba kuna baadhi ya mambo hakuwashirikisha wenzake, mathalani kuwa na kijimahusiano na afisa wa serikali.

Sasa hapa inabidi kila mtu katika siku yake atoke kwenda kutafuta nini kimemkumba Monday. Yupo wapi akifanya nini. Na kumbuka wakiwa wanafanya hivyo ni hatari wakionekana wapo zaidi ya mmoja nje kwa wakati mmoja!

Na zaidi, huyo aliyemkamata Monday akingoja kuona kama kuna wengine wanaofanania na Monday kupata kuthibitisha kuwa familia hii inavunja sheria kali ilowekwa na serikali.

Je, familia hii ita-survive vipi dhidi ya mkono mkali wa serikali? Na ni wapi alipo Monday? Na siri zake zitawaathiri vipi wengine wasio na hili wala lile?

6. THE RING ya 2002.

"ever since that girl's been gone, things have been better."
(Tangu binti huyo alipoondoka, hali imekuwa bora zaidi.)
View attachment 1427380
Filamu hii ni Horror (ya kutisha) lakini sio kutisha kwa kiwango kile cha INSIDIOUS ama DRAG ME TO HELL, hivyo hata watu waoga waoga wanaweza kutazama tu pasi na shaka.

Ni filamu ambayo imetokana na story maarufu nchini Japan kumhusu binti aitwaye Samara ama Sadako ambaye alikuwa akiaminika kuwa na nguvu za ajabu akiwaua watu kwa kupitia runinga.
Hii filamu ina migawanyo mitatu kama si miwili, nitajitahidi kukuelezea hapa ili kwa kuitazama tu hii moja upate kukidhi haja yako. So usistaajabu endapo ukaenda tazama hii usione haya nloelezea lakini yatakusaidia sana kwenye kuelewa filamu hii.

Funga mkanda ...

Binti mmoja aitwaye Samara alizaliwa na mwanamke aitwaye Evelyn. Baba yake na Samara alikuwa ni mchungaji ambaye alimbaka Evelyn na kumtia mateka mpaka pale alipofikisha mimba ya miezi nane.

Samara anazaliwa lakini ni bayana haonekani kuwa mtoto wa kawaida, basi mama yake anajikuta akitaka kumzamisha maji na anapokamatwa anasema alikuwa na nia ya kumsafisha mwanaye na roho ya kishetani.

Basi mama anashikiliwa na kupelekwa kwenye hospitali ya watu wenye ugonjwa wa akili huku mtoto, Samara, akiwekwa kwenye wazi kwa mtu yoyote kuja kumuasili awe mwanaye.

Hapo ndo tunaona wazazi hawa wapya sasa, familia ya Morgan, wakiwa tayari wameshamuasili huyu mtoto kutokana na matatizo ya kupata mtoto, lakini kama iwavyo, chui habadiliki madoa bwana. Samara baada ya muda akaanza kusumbua wazazi wake waliomuasili kwa vihoja na viroja.

Baba akaamua kumfungia kwenye banda la kufugia farasi, chumba cha juu kabisa, ambako huko sasa kutokana na kutokuwa na cha kufanya akitengwa, Samara akawa anaonyesha nguvu zake za ajabu kama vile kuunguza picha ya mti ukutani na kama haitoshi akaanza kufanya farasi wachanganyikiwe, wavunje banda na kukimbilia kufia baharini!

Alooooh!

Kuona kwamba haya hayawezi vumilika, sasa mama anaamua kumuua mtoto huyo kwa kumtupia ndani ya kisima kirefu. Humo Samara anadumu kwa siku saba kabla ya kufa ... lakini kifo chake ndo' kinaleta balaa zaidi kuliko uhai wake.
Yule jini alokuwepo ndani ya chombo mwili cha Samara, sasa anakuwa huru akiwatesa watu wanaotazama mkanda wenye ishara mbalimbali za matukio na visa vya Samara na familia yake ingali akiwa hai.

Na ukitazama mkanda huo, kama ilivyokuwa kwa Samara ndani ya kisima, utakuwa na siku saba tu za kuishi kabla hajaja kudai roho yake.

Sasa basi mwaandishi mmoja wa habari anajikuta katika kisanga hiki akijaribu kutafuta majibu ya kifo cha ajabu cha mpwa wake.

Dada huyo anapofanya utafiti wake anapata eneo ambapo mpwa wake na rafiki zake walifikia kwa ajili ya 'vacation', huko anapata kuutwaa mkanda wa ajabu na anautazama. Punde simu inaita na anaambiwa ana siku saba tu za kuishi!
Sasa dada huyu anapambana kujua yote haya yametokea wapi. Na kama haitoshi, mtoto wake anautazama mkanda huu. Hivyo kazi inakuwa kubwa zaidi, moja ya kupambania maisha yake na pili ya mwanae kabla siku hazijaisha!

Nilichopenda zaidi ndani ya hii movie ni kitendo cha kujidanganya cha dada huyu alipodhania kwamba akimpata Samara na kumfanyia wema basi watakuwa huru na laana ya mkanda, kumbe sio!

Bali njia ya kuvunja laana ilikuwa ni ...... katazame movie ujionee mwenyewe mzee!


IMETAYARISHWA NA,
Steve, BM.
A Freelance Journalist.
And a Literary critic.
0685 758123 (Whatsapp)

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Naipenda sana hii movies season 7 hutojutia
leemaudaku-20200424-0001.jpg
 

Similar Discussions

19 Reactions
Reply
Back
Top Bottom