Unaifahamu JamiiForums?

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,790
288,006
Unaifahamu Jambo Forums?

Kama jibu lako ni ndiyo, basi huna haja ya kuendelea kusoma makala hii kwani wewe ni miongoni mwa Watanzania wachache wanaojua hazina hii ya lulu iliyofichika. Hata hivyo unaweza kujisomea kujipa ujuzi zaidi wa tovuti yako uipendayo. Kama jibu lako ni hapana, basi bora ulinunue gazeti hili na ujitafutie mahala pa utulivu utakapoweza kujisomea makala hii bila bughdha wala kelele kwani ukimaliza kuisoma, utakuwa umepata ufahamu juu ya tovuti yenye mvuto wa sumaku, ushawishi wa akili, uzito wa hoja, na kina cha habari kuliko tovuti nyingine nyingi za Watanzania. Ukimaliza kusoma utakuwa ni miongoni mwa wale wanaofahamu kuhusu Jambo Forums, na mtu akikuuliza "unaifahamu Jambo Forums" unaweza kumjibu kwa madaha, kiburi, mbwembwe, na umakini wote na kusema "ndiyo naifahamu". Atakupa mkono wa kufahamiana. Haya lipia hilo gazeti kwanza. Ukiamua kuingia Jambo Forums utakutana na wachangiaji mahiri ambao wamejibandika majina kama haya Aljazeera, Alfa na Omega, DrWho, Jasusi, Kamundu, Lunyungu, na Yebo Yebo. Kumbuka nyuma ya majina hayo ni watu halisi wenye nafasi mbalimbali katika serikali, vyama, na sekta binafsi. Na wengine ni wakulima kama mimi.

Kwa maneno machache, Jambo Forums (JFs) ni baraza la kwenye mtandao ambapo Watanzania kutoka sehemu mbalimbali duniani hushiriki katika kubadilishana mawazo kuhusu mambo mbalimbali yanayohusu nchi yao masaa 24. Katika baraza hilo, Watanzania huzungumza kwa uhuru, uwazi, umakini, na kina ambacho hakina mfano wake.

Ingawa ni forum mpya zaidi ukilinganisha na forum kama hizo zilizotangulia, JFs imetokea kuvutia watu wa rika mbalimbali, vyama na itikadi tofauti, dini tofauti na
mitazamo tofauti tena kwa muda mfupi zaidi. Wakati forum nyingine zinasusua na nyingine zimekufa kwa sababu mbalimbali JFs imeonesha uthabiti wake na mvuto wake kwa kuhimili mikimiki ya teknolojia na majaribio ya hapa na pale ya kuinyamazisha
forum hiyo. Ni mvuto huu basi ndio umewavutia wafanyakazi wa kawaida na viongozi serikalini, maafisa wa taasisi mbalimbali, walimu wa vyuo vikuu, wafanyakazi wa mashirika binafsi, wanafunzi na watu wengine wa kila aina. Hata hivyo, hii siyo tovuti ya wasomi, siyo ya wapinzani, na siyo ya CCM; ni tovuti inayokaribisha maoni ya Watanzania wote.

Kuna mambo kadhaa ambayo ni mazuri yanayowavutia watanzania kutoka kila kona duniani kutembelea tovuti hiyo kila siku na kuhakikisha kuwa hawakosi kupitia hapo angalau mara moja.

Miongoni mwa faida unazoweza kuzipata hapo Jambo Forums ni hizi:
Kwanza, utakuwa ni miongoni mwa Watanzania wachache wanaopata habari za udadisi, uchambuzi, udaku, burudani na maoni yenye kina mapema kabla hazijaifikia radio au televisheni yako! Na utakuwa unapata habari mapema kabla hazijaifikia hadhara
ya Tanzania.

Wakati Watanzania wanaambiwa kuhusu uteuzi wa Dr. Migiro kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa au habari za Prof. Mahalu kufikishwa mahakamani wanajambo walishanong'onezwa mapema kuhusu uteuzi huo! Habari za kugundulika mabomu kule Kurasini zilitangazwa kwanza kwenye JFs kabla habari hizo hazijatangazwa RTD.

Hivyo, kuwa mwanachama wa JFs ni kuwa karibu na habari za matukio mbalimbali yanahusu Tanzania au yanayotea Tanzania kuliko kuwa karibu na radio au kukodolea macho televisheni yako. Ni huko Jambo Forums utakutana na wachangiaji na wachambuaji wa mambo kama kina Mwanagenzi, Mwanasiasa, Mwawado, Rufiji, Mkandara na Zanaki. Pili, Jambo Forums inawapa watu mbalimbali nafasi ya kuweza kutoa mawazo yao bila ya kulazimika kujitambulisha wao ni nani.

Ni kwa sababu hiyo basi mtu yeyote anaweza kuja na habari, wazo, au maoni na kuyatoa bila ya hofu ya kujulikana au kulazimika kujitambulisha. Ni kwa sababu hii basi watu wenye habari nyeti wanaweza kuingia na "kumwaga vitu" – wenyewe wanaita kumwaga data - kwenye JFs na kutokomea kama ukungu wa asubuhi. Habari walizotoa zinaweza kuthibitishwa au kukanushwa na watu wengine. Uking'ang'ania watu walete ushahidi, utapoteza muda, Hata hivyo hakuna sheria au utaratibu unaolazimisha watu kutumia majina bandia. Kuna baadhi ya watu ambao wameamua kujitambulisha na hivyo basi kujulikana wao ni akina nani. Miongoni mwao ni pamoja na Freeman Mbowe, John Mnyika na Dr. Augustine Mosha. Wale wanaojitambulisha hata hivyo mara nyingi wanazungumza wakiwa katika nafasi ya vyeo vyao au wanazungumza rasmi zaidi (hawazungumzi utumbo). Na usishangae watu hao hao wakawa na majina mengine wanapozungumza kama wao binafsi. Huo ni utamu wa jambo forums.

Jambo la tatu ni kuwa JFs ni mahali ambapo maswali hujibiwa au hujaribu kujibiwa na hoja huchambuliwa. Kwa watu wengi jambo forums imekuwa ni mahali pa kuhakikisha habari walizonazo zina ukweli na kujaribu kutafuta mawazo tofauti juu ya masuala mbalimbali ambayo yanahitaji upezu wa mawazo. Hivyo, utakuta mtu anaingia na kuuliza juu ya jambo fulani, na baada ya muda anaweza kupewa majibu au kuzua maswali zaidi na hivyo kupatia mwanga zaidi. Ni mahali ambapo panachangamsha akili, na kuchochea udadisi na utafiti wa hoja.

Usitegemee kusema neno kwenye Jambo Forums na watu wakalikubali kwa vile tu linaonekana linavutia. Watu watalichambua (wakati mwingine mistari kwa mistari) na kuonesha uzuri wake au udhaifu wake. Ni kwa sababu hiyo basi kila anayeandika anajikuta analazimika kuandika vitu vyenye mantiki na vinavyokubalika kiakili na vyenye maana ndani yake. Usishangae kupata majibu kutoka kwa mtu anayejiita Mzee ES, au kina Philemon Mikael, Mgonjwa wa Ukimwi, Tabasamu, Wambandwa, na Washawasha. Wakianza kumwaga data, unaweza kujikuta unapatwa na kigugumizi cha ghafla au akili yako ukahihisi inaanza kuganda kama barafu.

Jambo jingine kubwa ambalo linawavutia watu wengi kwenye baraza hili ni uhuru wa mawazo na maoni ambao mara nyingi unaonekana kukosekana katika vyombo vya kawaida vya habari. Waandishi wengi wa vyombo vingi vya kawaida vya habari hawana uhuru wa kusema mawazo yao katika vyombo vyao bila mhariri kukubali. Wakati mwingine mhariri hutupa kapuni mawazo asiyoafikiana nayo. Hivyo habari, maoni, mawazo, na hoja ni lazima vihaririwe kwanza ili kuweza kuchapishwa au kutangazwa kwenye vyombo hivyo. Kwenye JFs hata hivyo, hakuna Mhariri au msimamizi wa maoni., au mtu anayeangalia nani kaandika nini na kwanini.

Chochote utakachosema kitahukumiwa na wasomaji na wapiti njia wa JFs! Ni kwa sababu hiyo utakuta maoni, mawazo, na mapendekezo mengi mazuri na pia utakuwa mawazo ambayo huwezi kuamini yametolewa na binadamu! Ni uzuri huo basi watu wanajifunza kuvumiliana na kuheshimiana hata kama mawazo yao yanatofautiana, na wako tayari kupingana bila kupigana.

Faida nyingine pia ni kuwa kama wewe huna hamu na haja ya kuzungumzia mambo ya kisiasa, basi JFs inakupa vyumba kadha wa kadha ambapo unaweza kuchagua cha kuzungumzia. Kuna maeneo ya Lugha, Mapenzi, Michezo na Burudani, Dini na Imani, Ushauri kwa Viongozi na Vichekesho na Udaku. Hivyo wewe unachagua wapi unataka kuchangia na ni eneo gani ambalo binafsi unajiona uko fit kuzungumzia. Kwa hili JF ni kama chuo ambacho kina madarasa mengi, na wewe unachagua kozi.

Pia zipo faida nyingine nyingi ambazo sijazitaja hapo na utazigundua wewe mwenyewe pindi ukiamua kuchukua hatua ya imani na kutembelea tovuti hiyo. Hata hivyo nitakuwa si mkweli nikikupa uzuri tu bila kukuonesha ubaya wake au udhaifu wa forum hiyo ili unapoamua kutembelea au kujiunga basi ujue utarajie nini.

Udhaifu wa kwanza kabisa wa JFs ni kuwa kama una roho ndogo basi hakukufai huko. Unaweza kujikuta unapata kiharusi cha ghafla na watu wakaandaa ibada ya kukuaga! Huko JFs hakuna mtu anayeogopwa kuzungumzwa na hakuna mada isiyozungumzika. Wakati mwingine mambo ya binafsi ya watu mbalimbali hasa viongozi hujadiliwa waziwazi na hicho hupandisha watu "pressure".

Kama ni kiongozi mwenye kimada asishangae kuna mtu ameweka hadi jina la mtaa aliko kimada huyo! Hivyo ukiwa na roho nyepesi unaweza kujikuta unachukizwa kirahisi na ukaapa hutorudi tena na kujikuta unatishia watu kwenda mahakamani. Na kama wewe ni ndugu wa karibu wa kiongozi, ujifunze "kula jiwe" Unayoyaona Jambo Forums, yabakie Jambo Forums usiyalete nyumbani! Ni kwa sababu hii basi haja ya kujipa jina mbadala inapokuja kwani hakuna anayejua anayeandika ni nani na anayesoma ni nani. Ndio maana utakuta watu wamejibatiza majina kama Invincible, Invisible, Mgumu, Sam, Sara, Mama Lu, Wacha, Brutus, Mswahili, na Mlalahoi. Hao wote ni watu halisi, wengine ni wasomi na wahadhiri wa vyuo vikuu vya Tanzania! Na Wengine ni vijana walio shule za sekondari. Wote wanakutana kwenye uwanja sawa wa Jambo Forums. Udhaifu wa pili wa tovuti hiyo ni kuvutia sana watu wenye mawazo ya upinzani kuliko watu wa chama tawala.Ingawa tovuti yenyewe haina upande,utaona kuwa mengi yanayozungumziwa ni dhidi ya serikali, CCM au viongozi wake. Ni kwa sababu hiyo basi kwa mtu anayeingia mara ya kwanza anaweza kufikiri kuwa hiyo ni tovuti ya wapinzani (hasa wapenzi wa Chadema). Ukweli wa mambo ni kuwa baraza hilo halina dini, chama, au itikadi ya kisiasa na halifungamani na upande wowote.

Ili kuushinda udhaifu huu, wana CCM na viongozi toka serikalini hawana budi na wenyewe kujiunga kwa wingi ili kutetea hoja za serikali, kupinga maneno ambayo hayana ukweli, na kusahihisha mitazamo yenye makosa. Pamoja na hivyo wale watakaotaka kushirikia kutoka CCM, serikalini au wapenzi wa serikali hawana budi kuja na hoja zenye nguvu ama sivyo utakutana na watu kama kina Fikiraduni, Tafiti then Jadili, Lorditcal Jnr, Abdallah Issa, Husnaclara, Halisi na Eric Ongara ambao hawatachelewa kuanza kuuliza maswali na kuvunja vunja hoja dhaifu kama mtu anavyovunja bua la muwa.

Udhaifu mwingine wa tatu ni hilo la watu kujificha nyuma ya majina bandia. Kuna watu wengi ambao wanatoa hoja na mawazo mengi na wakati mwingine inawapa watu majaribu ya kutaka kujua nani ni nani hapo kwenye tovuti. Kama umeamua kutumia jina bandia na ukakuta yanayozungumzwa yanakugusa au yanagusa maslahi yako binafsi, usipoteze muda kujaribu kutafuta aliyesema ni nani kwani utaumiza kichwa. Ni kwa sababu ya hili, tovuti hii iko katika vitisho vya kufungiwa na kushtakiwa licha ya kusema wazi kuwa yote yanayozungumzwa ni maoni ya wazungumzaji. Baraza ni kama Ukumbi mkubwa ambao wote wanaotaka kuzungumza wanazungumza. Itachekesha na ni kinyume na akili kutaka kufunga ukumbi au kuushtaki ukumbi kwa vile muziki unaopigwa watu fulani hawaufurahii.

Yanayozungumzwa katika JFs mengi ni burudani na kupoteza muda na mengine ni mambo muhimu na nyeti hivyo kutishia kuufunga ni kuchezea na mahali ambapo watu wanajisikia huru kuzungumza wanayotaka kuzungumzwa bila kulazimishwa kujitambulisha. Uzuri wa mtandao ni kuwa hata tovuti hiyo ikifungwa, watu watafungua tovuti nyingine tena wakiwa na hasira zaidi na hisia ya kutaka kuwakomoa waliofunga.

Kuna tovuti ambazo zimewahi kufungwa na kuvamiwa lakini watu wameendelea kuunganisha nguvu katika sehemu nyingine. Hivyo, kwa wale ambao tovuti hii inawaudhi ni bora wajifunze kuishi nayo, kwani wachangiaji hawaendi popote na mada zitaendelea kujadiliwa hata kwenye mabaraza mengine ambayo siyo maarufu kama Jambo Forums.

Na udhaifu mkubwa ambao uko wazi ni kuwa kuweza kuwa mchangiaji na kujua nini kinachoendelea ni lazima uwe na mtandao au uwe na nafasi ya kutumia mtandao (intaneti). Kwa kweli hiki ni kikwazo kikubwa kwa Watanzania wengi kujiunga. Ni kwa
sababu hiyo basi utakuta wengi ya wachangiaji wa mara kwa mara hawako nyumbani, wako nje ya nchi. Hata hivyo, huhitaji mtandao nyumbani, hata ukiingia mara moja kwa wiki utakutana na habari nyingi ambazo vinginevyo usingejua.

Ni kwa sababu hiyo basi wengi ya wanaoalikwa kujiunga ni wale ambao wana nafasi ya kutumia mtandao shuleni au wale wenye kuweza kutumia mtandao maofisini. Na hata wale ambao wanaweza kuingia mara moja moja, haichukui muda mrefu kusoma mada au kupost kitu na kurudi siku nyingine kuona watu wamechangia nini. Jambo Forum inahifadhi mada kwa kutumia kurasa mbalimbali hivyo hata ukija baada ya wiki, unaweza kupekuwa kurasa mbalimbali na kusoma kutoka pale ulipoachia.

Usishangae utakaporudi utakuta watu kama kina Jafar, Shemzigwa, Mudywalker, Mkuu, na Chief wakiwa wamekujibu. Baada ya kusema hayo yote bila ya shaka unataka kujua ni wapi utaikuta tovuti hii ili na wewe usiwe mmoja wa watu wasiofahamu nini kinaendelea karibu na ofisi yako, au ndani ya nchi yako. Tovuti hii inapatikana kwenye kiungio hiki http://www.jamboforums.com na gharama ya kujiunga ni bure kabisa. Kujiandikisha haichukui zaidi ya dakika tano na itachukua muda mfupi kujifunza jinsi tovuti hiyo navyofanya kazi.

Bila ya shaka sasa umeelewa uwepo wa tovuti hiyo ambayo kila mtanzania, kila mwanasiasa, na kila kiongozi ambaye anataka kujiweka kwenye "kundi la wasiopitwa na mambo" lazima awe na ufahamu nayo na ajiunge bila kusita. Kutokufahamu tovuti hiyo, ni kutokufahamu nini kinaendelea Tanzania. Ila kama unataka kufahamu usichelewe, jiunge. Na ukifika waambie "Mzee wa Kijijini" kanielekeza hapa. Utakaribishwa kwa mikono miwili.

Wana Jambo Forums
Msemaji wa Jambo: - jamboforums@klhnews.com
Simu: 1 248 556 6748

 
hope & soon invincible utakuwa unainvite wajuzi kama kina Shivji and his likes waje hapa wakate issue zao tuzijadili ili tujue mchele upi na pumba ni zipi,invite watu wanao make sense na CV za maana waandike editorial/opinions ili kuongeza forum legitimacy maana hii anonymous ya kila member inabidi ipungue kidogo...ni maoni tuu!
 
wow! the history can be wiped out in a second! No sam in your story?
 
FIRST RULE OF JAMBO FORUMS, WE DO NOT TALK ABOUT JAMBO FORUMS

SECOND RULE OF JAMBO FORUMS,WE DO NOT TALK ABOUT JAMBO FORUMS
 
FIRST RULE OF JAMBO FORUMS, WE DO NOT TALK ABOUT JAMBO FORUMS

SECOND RULE OF JAMBO FORUMS,WE DO NOT TALK ABOUT JAMBO FORUMS

LOL! Brazameni...Wewe huchoki kuangalia nonino!?....:) Haya rudi kwenye anga zako za kujidai huku kwenye siasa unaona mauzauza tu!
 
wow! the history can be wiped out in a second! No sam in your story?

usijisikie vibaya ndugu!! kwikwikwikwi kuna member 4000 humu, ingekuwa shughuli kama ingebidi kila mtu atajwe!!!.
 
usijisikie vibaya ndugu!! kwikwikwikwi kuna member 4000 humu, ingekuwa shughuli kama ingebidi kila mtu atajwe!!!.

Kama unajua historia ya JF huwezi kabisa kuliacha jina la sam. Na kama tunavyofahamu sam siyo mtu na siyo mimi nililolianzisha. Kumbuka BSC ilipokufa watu walitawanyika huyo mwanakijiji akaanzisha gumzo, wengine wakaenda maoni na forums nyingine. Mkandara mwenyewe ilimchukua muda kuhamia hapa na sababu najua zilikuwa nini kuna siku nitawaelezeni. Baada ya muda na kutafakari niliamua kutangaza kuwa kwenye ile forums kwenye website ya Iddi Simba na baadaye ikaamishwa kuwa jamboforums. Kuna mambo mengi sana yalikuwa yanaendelea behind the scene wakati jambo inakuwa. Nawashukuru sana watu walioichukua ilipofikia na kuivusha kwenye another level hasa Mwanakijiji ambaye naye alihusika sana kuiwekea mizizi hii forum. Unajua kuna members wengi sana walikuwa YoungAfrican.com ambao wengi ni wazoefu wa hizi forums walianzai nyenzi.com kama mnaikumbuka mimi na Nyani tulienda kule tukajitambulisha in our style na wengi wao walitaja kujua tunatokea wape as the result tuko nao hapa nao as partners na kusahau yaliyotokea YA. Hii part ya story imeachwa na mwandishi. The roots and history of Jamboforums. Kuna watu humu wanaogopa kama JF itafungiwa au kufa, it is just a matter a seconds kuiinua forums nyingine. Kwa mfano sam akisema http://haki-hakingowi.blogspot.com/ ni bog bora kwa picha nenda kaone number of clicks zitapoongezeka. Au siyo mzee wa bongo radio www.bongoradio.com mambo ya promo 24/7 au siyo. Wengi hawajui wanachokosa www.bongoradio.com
 
usijisikie vibaya ndugu!! kwikwikwikwi kuna member 4000 humu, ingekuwa shughuli kama ingebidi kila mtu atajwe!!!.

Nadhani inapungua kidogo maana kuna wengine wana ID zaidi ya moja namkumbuka Hasara nadhani yupo hapa JF na ID mpya
 
Sam

Ndugu yangu na wewe umepotea sana. Vijana hawawezi kukukumbuka ndugu yangu, ila mie na akina Nyani na ES, Mwanakijiji, tabasamu, Mkandara, Invicible, Pedro, etc tunakumbuka sana.

Kweli tupo wengi kuliko ilivyokuwa BCS lakini ule moto wa BCS ulikuwa mkali sana, JF imepaa sana zaidi ya BCS lazima tukubali, kwa sasa tupo mbali.

Me against Kikwete, unakumbuka ile topic yako maarufu ya Nchimbi?

Uliona mbali ndugu yangu SAM angalia miaka michache baadaye huyu huyu uliekuwa against naye (Nchimbi) amefanya madudu kibao! na yet ni naibu waziri.

Acha tu. Uliangalia san utaona baadhi ya wanachama wa BCS wamepungua kasi, naona vijana wanachukua usukani ndio maendeleo acha tupumzike kidogo, hizi harakati tumeanza zamani sana toka Nyenzi.com ya Majaaliwa.

Ila usipotee sana mshkaji. Umeadimika.

FD
 
been visiting JF as a guest over the months...hats off 2 every1,finally joined officially and it feels like coming home. Its 1 of a kind...like no other! IDUMU!
 
Nadhani inapungua kidogo maana kuna wengine wana ID zaidi ya moja namkumbuka Hasara nadhani yupo hapa JF na ID mpya

Una maanisha members 4000 minus wenye double ID? Duh! kula deki, sasaaa...! Kwani dhambi jamani, au hii sawa na kuwa na uraia wa nchi mbili? No hapana nadhani hii ni sawa na jamaa wa kisonjo I mean kisomali(!?) yah wasomali wa london a.k.a bajuni, majina na miaka yao imerudishwa nyuma...! Ah ah ah... Yote maisha lakini... Nah I think kuwa na ID mbili JFs ni kutaka kuchangia zaidi au kutafuta suport za kulazimisha, any way JFs is bomba, Ila Thikubaliani na mwandishi wa makala haya ktk jamboforums moja, I mean jambo moja, yaani yanayo zungumzwa hapa yaachwe hapa hapa, basi aina maana ya kuchangia na kuwaeleza wana jamii ufisadi na udhandiki wa viongozi wetu na jamii kwa ujumla, jamii inatakiwa kurekebishwa na hapa JFs ni sehemu mojawapo ya Watanganyika na Wazanzibar a.k.a Watanzania Bin' Wabongo, kuelezea yale yanayojiri na yanayo wakera na kuwasumbuwa kwenye maisha yao ya kila siku... Je hatupaswi kujifunza na kuyafanyia kazi yale yanayo jadiliwa hapa? Hapana...! Tusiwe wanafiki wa nafsi zetu wenyewe... Nani anakumbuka kile kipindi cha Mazungumzo baada ya habari enzi zile za aliyekuwa eti baba wa taifa la wabongo....? Mambo yaliyokuwa yakizungumzwa kwenye kipindi kile yalikuwa mazuri sana kinadharia, lakini hakuna ambaye aliyatekeleza au hata kujaribu kuyafanyia kazi...! Na hatukuwa na huwezo wa kukosoa, japo hata kumkosoa mjumbe wa nyumba kumi kumi tu ilikuwa dhambi kubwa. (Thubutu umkosoe... kama hakukunyima sukari na unga wa muogo kwenye duka la kaya) Je na humu JFs ina maana tuwe hivyo? Sina maana kila kinacho zungumzwa humu kina manufaa ktk jamii la hasha, ila kwa kila jambos ambalo tuna hisi kuwa ni msaada au la manufaa kwa jamii ya wabongo, linafaa kulifanyia kazi. Kijamii au hata mmoja mmoja.

Wewe unafikiri wale waliotaka kuifungia JFs Wajinga? La hapana si wajinga ila Wanaweza kuwa ni w4pumb4fu, kwa maana mjinga anaweza kuelevuka ila mpumb4fu ina kuwa kazi kweli kweli kumuelimisha...!

Jambo moja nalitaka kulisahau hivi humu ndani ya JFs kuna uhuru wa mawazo na wa kutoa maoni kwa kiwango gani? Nimeshawahi kuona mada au makala ikifungiwa bila kutolewa maelezo just kimya kimya tu, na kuna makala zina yale maneno tunayaita matusi au pale inapotokea mtu kukosa hoja akaamua kmtukana mtu au kumuita jina ambalo si lake, just kwa niya ya kumchokoza hili naye ayamwage matusi aliyokuwa nayo kwenye kamusi yake ya kichwani, sasa kwa sisi ambao kamusi zetu zimeshafuta matusi yote inakuwa kazi kweli kweli, kurejesha matusi, kwani kila ukitafuta database yako inakuonyesha kuwa hakuna neno kama hilo, basi inakuwa raha kwa kwenda`mbele....!

Wana JFs tujitahidi tu kuvumiliana maana JFs imekusanya wengi, wazuri na wabaya, wema na waovu, wenye imani za dini na kinyume chake wote wapo humu, na kila mmoja ana jambo lake na uhuru wake, lakini UHURU usio na mipaka ni chaka lisili pendeza, ni sawa na jaa la taka...! Kila mwenye uchafu wake atautupa humo. Itawapa tabu wale wenye kutaka kuyachukuwa yenye manufaa, maana watakatishwa tamaa na yale machafu. yanayoletwa na wachache wenye malengo machafu, ya kutaka kuchafua kurasa za JFs zionekane chafu, kama kijiwe cha mafisi na manyangau walio tayari kumraruwa yeyote apitaye barabarani....!

Tuwe wastaarabu na wakomavu wa akli, tutoe hoja na tuwache viroja. Na
Tujihadhari na maneno au mambo tusio yajua mwendo wake wala ukweli wake, kwani maneno yako huonyesha akili yako, na maneno yako hudhihirisha maarifa yako.

Kwani Maisha ni adui usiyemfanyia uadui, na dhalimu usiyemdhulumu, na mchokozi usiyemchokoza.
 
Back
Top Bottom