Ukweli kuhusu vurugu Zanzibar: Serikali ya Umoja hatarini kuvunjika wakati wowote

Zak Malang

JF-Expert Member
Dec 30, 2008
5,404
234
CCM, CUF jino kwa jino




Na Jabir Idrissa

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha Wananchi (CUF) vimeanza kufarakana; na serikali yao ya pamoja inaweza kusambaratika wakati wowote, MwanaHALISI limeelezwa.

Kila chama kinakishutumu kingine kwa kuanzisha, kuendesha na kuchochea mazingira ya vurugu Zanzibar.

Kauli za viongozi waandamizi wa vyama hivyo, katika mahojiano na gazeti hili juzi, Jumatatu, zinathibitisha kushutumiana, kutoaminiana na hatimaye uwezekano wa kufarakana.

Kwa upande mmoja, CCM inaituhumu CUF kwa kuunga mkono Jumuia ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu, ambayo imejiapiza kuongoza juhudi za kupinga ukusanyaji maoni ya katiba mpya hadi ifanyike kura ya maoni ya kuuliza Wazanzibari iwapo bado wanataka Muungano.

Kwa upande mwingine, CUF inaituhumu CCM kwa kuendesha mikutano, ambayo viongozi wake "wamemimina vitisho na matusi" kwa viongozi wa chama hicho cha upinzani ndani ya serikali ya pamoja.

Mkurugenzi wa habari wa CUF, Salim Abdalla Bimani amesema viongozi wa CCM wilaya ya mjini, mkoa wa Mjini Magharibi, wakiongozwa na mwenyekiti wao, Borafya Mtumwa Silima, wamekuwa wakiendesha mikutano ya vitisho dhidi ya wapinzani wa Muungano.

Amesema viongozi hao wamefika mbali zaidi; wakimhusisha Makamu wa Kwanza wa Rais, ambaye pia ni katibu mkuu wa CUF, Maalim Seif Shariff Hamad kuwa anaunga mkono Uamsho.

Viongozi wa CCM wanaelezwa kufanya mikutano mitano katika mkoa wa Mjini Magharibi.

Katika mikutano hiyo, Bimani anasema walitukana viongozi wa Uamsho huku wakiwatisha waliowaita ‘wapinga muungano' kwa kuwaambia "watakatwa vichwa na janjaweed."

Janjaweed ni jina walilojiita vijana nchini Sudan waliokuwa wakifadhiliwa na chama tawala cha nchi hiyo, ili wapambane na wanamgambo waliokuwa wakishinikiza kuundwa kwa taifa la Sudan Kusini.

Kwa Zanzibar, jina hilo walipewa vijana waliokuwa wanadaiwa kufadhiliwa na CCM ili kuendesha vitisho – kuvamia kwenye makazi, vijiwe na hata nyumbani – na kuwajeruhi "wapinzani" kwa mapanga na vipande vya nondo.

Vurugu hizi zilionekana zaidi wakati wa uchaguzi mkuu hasa mwaka 1995. Zilisitishwa kabla ya uchaguzi mkuu 2010 baada ya muwafaka kati ya CCM na CUF.

"Wewe unawajua janjaweed ni nani. Unaposikia matamshi kama haya jukwaani, unapata tafsiri gani, kama siyo kwamba wanaoyatoa wamekusudia kuleta vurugu nchini petu?" anahoji Bimani.

"Hawa siyo kwamba wamechoka au hawana akili. Hata kidogo. Tatizo lao kubwa hawapendi maridhiano. Wanataka Zanzibar irudi kusherehekea siasa za fitna na mauaji," ameeleza.

Lakini Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai amesema CCM haihusiki na vitendo vinavyochochea vurugu.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa simu juzi Jumatatu, Vuai kwanza alijibu kwa ufupi, "Hili jambo unajua lipo mahakamani. Nisingependa kutoa kauli yangu. Tusubiri vyombo husika ambavyo vinafanya uchunguzi. Ukweli utajulikana."

Bali alipoelezwa kuwa tuhuma kwa viongozi wa CCM kufanya mikutano ya hadhara na kutishia wanaoitwa "wapinga Muungano" hazina uhusiano na shauri lililoko mahakamani, alisema "…ukweli unajulikana ila wenzetu wanajaribu kuuficha."

Vuai amesema wao wanajua kuwa CUF wanaunga mkono shughuli za Uamsho na ndio wanaohusika na vurugu "zilizosababisha fadhaa kwa nchi na uharibifu wa mali za wananchi."

Wiki iliyopita (26 na 27 Mei), vijana waliosadikiwa kuwa wafuasi wa Uamsho, walifanya maandamano, kuchoma matairi na kuziba barabara; kuchoma moto makanisa mawili na kuvunja majumba ya kuuza bia – baa.

Vuai amesema wana imani kuwa "Uamsho ni wing ya CUF. Si unajua sisi CCM tuna wing ya vijana? Basi wenzetu wao Uamsho ni wing yao. Wanaunga mkono shughuli zao… wanaunga mkono yanayofanywa na Uamsho. Hili linajulikana," amesema.

Amesema watu wasihangaike kusaka wahusika; vyombo vya dola vinafuatilia kila kitu ili ukweli uwekwe wazi licha ya watu "kujitahidi kuuficha."

"Chukua CD za mihadhara ya Uamsho; chukua CD za hiyo mikutano mitano ya CCM; halafu ziweke hadharani watu waone na kusikiliza. Waache waamue ni nani aliyechochea vurugu," ameeleza Vuai kwa sauti ya upole.

Vuai alikana kutetea au kulinda viongozi wa chini yake wanaotuhumiwa "kutukana" viongozi wa serikali na "kutishia wapinga Muungano."

Lakini Bimani anasema viongozi wa CCM wamenukuliwa wakisema, "…janjaweed wangalipo, tena wana kontena za nondo ambazo watatumia kukata vichwa vya wapinga Muungano."

Akiongea kwa hamasa, Bimani anasema, "Usidhani hawa wanafanya utani; janjaweed wanajulikana kukata vichwa na kuchanja watu. Hawa ndio watu wabaya ambao tungependa serikali ikabiliane nao."

Bimani ametaja majina ya viongozi waliopanda jukwaani katika mikutano ya CCM na kudai kuwa wametumwa na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar kutoa salamu kuwa wapinga Muungano watashughulikiwa (orodha ya viongozi hao tunaihifadhi kwa sasa).

Amesema yote hayo yametokea bila CCM kukemea na kuongeza kuwa hata alipomfuata ofisini, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohamed Aboud Mohamed na kumjulisha juu ya suala hilo, hakuchukua hatua.

"Nilikwenda ofisini kwake. Nikampa taarifa za uhuni unaofanywa na wasaidizi wao katika chama. Nikaonya kuwa uhuni huu utaleta vurugu. Lakini hakuchukua hatua," ameeleza Bimani.

Bimani amesema CUF inajua kuna viongozi waliochukizwa na maridhiano; wanatumia kila mbinu kutaka kuchafua amani na utulivu uliopo.

Kiongozi huyo wa CUF amesema chama chake kinaachia vyombo vya dola kuchunguza na kuchukua hatua ila anasisitiza, "…wafanye kazi yao kitaalamu; asionewe mtu, asipendelewe mtu wala asibambikizwe kesi mtu."

Maalim Seif hajasema lolote kuhusu hali hii. Kiongozi mmoja wa CUF ngazi ya taifa amesema, "…ukiona huyu kaingia kwenye mabishano haya, ujue ndoa yao inavunjika."

"Alichokwambia mwenezi wa CUF ndiyo maoni na msimamo wa chama chetu. Hapa tayari kuna ‘jino kwa jino' ya kimyakimya. Tuombe isilipuke," ameeleza kiongozi huyo akiomba kutotajwa gazetini.

Tayari viongozi wakuu wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu (JUMIKI) wamekutana na uongozi wa juu wa jeshi la polisi Zanzibar.

Mkutano huo ulifanyika makao makuu ya polisi Zanzibar, Ziwani juzi Jumapili.

Gazeti hili limeelezwa kuwa Sheikh Farid Ahmed Hadi, Amir wa Uamsho, ndiye aliongoza viongozi wenzake kukutana na polisi kwa ushauriano.

Katika kikao hicho, Uamsho walitoa orodha ya viongozi wa CCM ngazi ya wilaya wakiwatuhumu kutoa kauli zilizochochea vurugu.

Amir Farid ameiambia MwanaHALISI kuwa amekabidhi orodha hiyo kwa kamishna wa polisi. Orodha hiyo pia ina maelezo ya mikutano ambako CCM walitolea vitisho kwa viongozi wa Uamsho kwa madai kuwa wanapinga Muungano.

Uamsho wameshaendesha mihadhara ipatayo 50 kuelezea umuhimu wa kuitisha kura ya maoni kwanza ili Wazanzibari watoe kauli iwapo wanataka Muungano.

Katika kukabiliana na wana-Uamsho, yapata wiki mbili sasa, polisi walimkamata mmoja wa viongozi wao, jambo ambalo linadaiwa kuamsha hasira za wafuasi wao.

Kwa siku mbili mfululizo, polisi walikabiliana na vijana waliokuwa wakirusha mawe wakishinikiza kiongozi wao aachiwe.

Watu 30 wamekamatwa na kufikishwa mahakamani kwa mashitaka yanayohusiana na vurugu hizo. Wote walikana kuhusika na wapo nje kwa dhamana.

Vuta nikuvute iliyopo hivi sasa kati ya Zanzibar na serikali ya Muungano, ni kuanza kutumika kwa sheria ya kukusanya maoni ya katiba kabla sheria hiyo haijaridhiwa na Baraza la Wawakilishi (BLW).

Kikatiba na kiutaratibu, sheria yoyote inayotungwa na bunge kuhusu mambo ya Muungano na ikikusudiwa kutumika Zanzibar, sharti iwasilishwe katika BLW kabla ya kuanza kutumika.

Kuibuka kwa hoja hiyo sasa, ambayo inatokana ama na kupitiwa au kudharau, kumetajwa kuwa sababu kuu ya Tume ya Katiba chini ya Jaji Joseph Warioba kuchelewa kuanza kazi yake.

Tume ilitarajiwa kuanza kazi tarehe 1 Mei. Jaji Warioba amekuwa akiwaambia waandishi wa habari kuwa tume yake ikiwa tayari, atawaita wao kwanza na kuwaleleza utaratibu.

Taarifa ambazo hazijathibitishwa ambazo zimefikia MwanaHALISI zinasema huenda baraza la wawakilishi, ambalo linaanza kikao chake cha bajeti wiki ijayo, likashughulikia uridhiaji wa sheria hiyo.

Tangu Rais Jakaya Kikwete atangaze utaratibu wa kupatikana katiba mpya ya Muungano, kumekuwa na harakati nyingi zikiwemo asasi za kiraia kuhamasisha watu kutoa maoni wakati utakapofika.

Lakini kwa Zanzibar, asasi zinaongeza vionjo kwa kushinikiza serikali iitishe kwanza kura ya maoni ili watu waamue iwapo bado wanapenda na kuridhika na Muungano.

Wiki iliyopita, akiongea na waandishi wa habari ikulu Zanzibar, Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein aliwasihi Wazanzibari kuwa watulivu na kusubiri Tume ya Katiba kuchukua maoni yao.

Naye Rais Kikwete, katika hotuba yake ya mwisho wa mwezi Mei amesema, Muungano hauwezi kuvunjwa kwa maandamano.

Amesema Watanzania wako huru kutoa maoni yao juu ya Muungano.

Chanzo: Mwanahalisi


My take: Jabir Idrissa aliwahi kuwa afisa habari ktk kampeni ya Maalim Seif uchaguzi 2010 hivyo haya aliyoandika yana ukweli mkubwa kuhusu wasemayo CUF.

 


Stori hiyo na hii hapa chini ya mwandishi huyo huyo na gazeti hilo hilo zimeibuwa masuala mazito kuhusu kuhusika kwa serikali ya CCM (bila shaka kupitia kitengo chake cha Usalama wa Taifa - UWT) katika vurugu zilizotokea.

Nimejaribu kuonyesha kwenye red sehemu husika. Inakuwaje hadi sasa hakuna hata mmoja baina ya wale 30 waliokamatwa aliefungulkiwa shitaka la uharibifu wa mali na uchomaji wa makanisa?

Hakuna anayeweza kuamini hili na mwandishi amekumbusha yale ya zamani (wakati wa uchaguzi wa 2010)kuhusu utiwaji kinyesi katika visima na ulipuaji wa mabomu hujuma zilizoelekezwa kwa wafuasi wa CUF kwa kusema hadi leo hakuna yeyote aliyekamatwa na kufunguliwa mashitaka kuhusu hujuma zile.

Hii ina maana moja tu: Kuhusika kwa serikali ya CCM katika hujuma hizo kuonyesha kwamba CUF ni chama cha vurugu. Safari hii serikali ya CCM inafikiria kuwa imefanikiwa kuonyesha kwamba Uamsho haukuwa na lengo la kuuhoji Muungano, suala ambalo ni shubiri sana kwa CCM, bali lengo ni udini tu dhidi ya makanisa.

CCM wanaufyata hata kuunda Tume huru kubaini ni akina nani waliochoma makanisa, kwani ni watu wao. Ingekuwa kweli siyo wao saa hizi wangekuwa wameisha kamatwa.




KALAMU YA JABIR:


Mpanga ubaya mwisho humrudia



Na Jabir Idrissa

KUNA uhalifu umefanywa Zanzibar. Ni katika matukio mabaya yaliyoanza usiku wa tarehe 26 Mei 2012. Watu wamechochewa kupambana na dola. Hili halijaelezwa na serikali.

Polisi wamevamia nyumba za viongozi wa Uamsho na kuvunja milango huku wakiwatukana matusi ya nguoni viongozi na familia zao sambamba na kuwatishia maisha. Polisi hawajalieleza hili.

Amir (kiongozi) wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu (JUMIKI), Sheikh Farid Ahmed Hadi anasema usiku wa Jumamosi hiyo, akiwa kwake, alipata taarifa anafuatwa na polisi wa kuzuia fujo (FFU).

Akajiandaa. Mnamo saa 7.30 kweli wakafika. Wakataka mlango ufunguliwe. Hakuna aliyewatii. Wakarusha risasi hewani. Hakuna aliyetoka. Hakuna aliyepiga kelele kutokea ndani.

Lakini, baada ya kuona vishindo vimezidi, Sheikh Farid akasema kwa sauti, "Nipo ndani na familia yangu tumepumzika. Kama mpo tayari, fanyeni chochote nje ila, ninaapa kwa jina la Allah, anayekuja ndani, tutakabiliana mimi sina bunduki."

Polisi hawakujali. Wakafyatua mabomu. Wakavunja mlango na kuvuruga walivyovikuta nje. Wakataka kuingia ndani. Wakakatazana, "hapana. Mnajua nani wamo ndani? Tuondokeni."

Wakaondoka, anasimulia Sheikh Farid. Amepata simulizi kama hizo kwa viongozi wenzake wa Uamsho. Lakini sokomoko kama lililomkuta, lilitokea nyumbani kwa naibu wake, Sheikh Azzan Khalid Hamdan, wakati mwenyewe akiwa nje ya nchi kwa matibabu.

Sheikh Azzan aliporudi Ijumaa, akapewa taarifa na familia yake kuwa walifika polisi wa FFU na kufanya fujo. Walifyatua risasi nje, wakavunja mlango. Wakapiga mayowe ya kumtukana matusi yeye na familia. Wakaondoka.

Hakutulia. Alikwenda kupiga ripoti kituo cha polisi Mfenesini, karibu na anapoishi. Wakuu wakakana kufika kwake. Wakasema askari waliomfuata walitoka Mwembemadema.

Mwembemadema ni makao makuu ya polisi mkoa wa Mjini Magharibi. Hawa ndio waliotuma makachero Jumamosi ile wakamshike Ustadhi Mussa Juma Issa, mmoja wa wahadhir wakuu wa Uamsho, kipenzi cha wahudhuriaji wa mihadhara ya jumuiya hii inayohamasisha Wazanzibari kuukataa muungano.

Wapo watu wamejitokeza kutoa ushahidi wa walivyoona polisi wanalipua nyumba na mali za vitegauchumi za raia wema, zikiwemo gari zilizoegeshwa Kisiwandui na Michenzani.

Mwanamke anayefanya kazi shirika la ndege la Kenya Airways, gari yake iliteketezwa kwa bomu lililorushwa na polisi. Matukio yote hayo katika siku mbili – Jumamosi na Jumapili.

Leo, taarifa zimepatikana za uhalifu wa Polisi uliofanywa Jumatatu, 28 Mei, muda mfupi baada ya watuhumiwa 30 wa fujo, walipoachiwa kwa dhamana na Mahakama ya Mwanakwerekwe, mjini Zanzibar. Kati yao wapo viongozi wawili, akiwemo Ustadhi Mussa, wa Uamsho.

Wakati wakili wao, Abdalla Juma akiwa Mahakama ya Ardhi, Vuga, vijana wa FFU walivamia ofisi zake Amani, yapata kilomita tano kutoka Vuga. Wakapitisha mitutu ya bunduki madirishani na kufyatua risasi na mabomu ya machozi.



Hawakujali wafanyakazi waliokuwa ndani. Ni mchana kweupe. Hapana, ni mchana wa mola muumba mbingu na ardhi siku ya kazi, Jumatatu.



Ipo taarifa ya Chama cha Wanasheria wa Zanzibar (ZLS) kulalamikia kitendo hicho. Wamemtumia barua Kamishna wa Polisi wa Zanzibar, Mussa Ali Mussa, na kumtaka asake wahusika na kuwashitaki.



ZLS wamekiita kitendo hicho cha makusudi kilicholenga kutisha mawakili wasiwe imara katika kazi yao ya kutetea wananchi wanaposhitakiwa. Polisi wanatuhumiwa sasa kushiriki vitendo vya uhalifu katika kipindi kilekile ambacho wao wanatuhumu Uamsho kuzusha ghasia mjini Zanzibar.



Ninayaeleza haya ili kukumbusha historia ya kisiasa Zanzibar inayochefua. Siasa za maridhiano zilizoanza kustawi tangu 2010 mwishoni, zinachafuliwa kwa nguvu.



Ni kama zilivyokuwa zikipandikizwa na kustawishwa siku zile za giza, mara tu mfumo wa siasa za vyama vingi, siasa za ushindani, uliporudishwa chini ya sheria ya Tanzania.



Sasa wapo wasiotaka amani Zanzibar idumu. Wapo. Pengine wanampenda Amani Abeid Karume, kiongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Shariff Hamad, ambao walizijenga, bali wanachukia matunda ya maridhiano.



Polisi. Polisi. Polisi. Polisi. Polisi. Polisi. Polisi. Polisi. Polisi. Hapana; si peke yao. Kwa jumla, vyombo vya dola, vya dola, vya dola. Dola, dola, dola, dola, dola, dola, dola, dola, dola.



Vyote vilitajwa kupandikiza chuki kwa wananchi, mgongo ukiwa vyama vingi na uimara wa CUF. Visima vikapakwa kinyesi, ofisi za umma zikawashwa kwa viberiti na makanisa yakachomwa kiajizi. Kanisa linawashwa, dakika mbili tu hao walinzi wamefika.


Ushetani ule ukakoma pale wananchi wa Shengejuu, kaskazini Pemba, walipovizia usiku kutafuta nani hasa wakihusika na vitendo vile vya kiharamia. Waliokutwa mpaka leo Polisi hawajawataja.

Ni askari polisi na mashushushu ndani ya Landrover iliyosheheni madumu ya petroli, mapipa ya kinyesi na viberiti vya kuwashia mabomu ya chupa.

Kutaka kuzubaisha umma wa Watanzania na ulimwengu, IGP Omari Mahita akaunda kikosi kuchunguza. Akamteua Robert Manumba, kachero aliyekuwa msaidizi mkuu wa DCI Adadi Rajabu, kukiongoza.

Alitaka wachunguze chimbuko, sababu na wahusika wa milipuko ile ya kishetani pamoja na vitendo haramu vya kupaka kinyesi madarasa na kukimwaga kwenye visima vya maji wanayotumia wananchi.

Tangu wakati ule, karibu miaka kumi sasa, si DCI Manumba ambaye sasa ndiye DCI, si IGP Mahita wala serikali iliyotoa ripoti ya uchunguzi huo. Wananchi waseme nini hapo? Lakini kwa sababu wahusika walijulikana na kufikia kukamatwa Shengejuu, zile fitna kuwa CUF walikuwa wahusika, zilifutika.

Tungalinao wakorofi wasiopenda maridhiano. Wahafidhina ndani ya CCM wameibuka upya wakitaka kuharibu amani na utulivu. Hawawezi kuitaja CUF moja kwa moja maana wanashirikiana nacho kuendesha serikali.

Wametafuta pa kuingilia – Uamsho. Kwa kuwa taasisi hii imechukua jukumu la kupigania haki za wananchi wasioridhishwa na mwenendo wa muungano, wanawapakazia kuwa wanavunja amani.

Kumbe bado kuujadili Muungano wa Tanzania ni uhaini. Pamoja na serikali kuruhusu Watanzania watoe maoni yatakayotumika kuandika katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, watawala hawapendi watu wafikiri tofauti na wao.

Tunaona kila viongozi wa polisi wanavyojitahidi kupotosha ukweli wa kilichotendeka mjini Zanzibar, ile dhamira yao ya kupotosha inawarudia. Wanatajwa baada ya kuonekana wazi wakivamia na kuharibu mali ikiwemo ofisi za wanasheria.


Mpanga ubaya mwisho humrudia. Hawajajisafisha, wamejiumbua. Na ndiyo matokeo ya polisi nchini kushabikia siasa. Wanasubiriwa watamshika nani mchoma makanisa. Bado watafute ushahidi kuthibitisha kesi ya watu 30, pamoja na wafadhili wa Uamsho.


Source: Mwanahalisi


 

Ni vigumu CCM kukwepa kuhusika kwake katika sakata hili la vurugu Zanzibar kwani kuna mengi tu yanawasuta.

Nilishangaa juzi JK aliwasifia polisi kwa 'kazi nzuri' kuzima vurugu Zanzibar! Kazi nzuri ipi? ya Kutembeza virungu ovyo, kupiga watu na kuwalipua kwa mabomu ya machozi?

Kazi nzuri ambayo JK angeweza kuwasifia ingekuwa ni kwa polisi kufanya uchunguzi wa kina na wa kitaalamu wa kuwabaini waliochoma makanisa na kuwafikisha mahakamani kwa hujuma hiyo. badala yake wamekamata kamata watu tu kijuu juu na kuwapeleka mahakani kwa kosa la uzururaji -- na kisha kuwaachia kwa dhamana!

Ni aibu kubwa sana hii kwa polisi wetu, ni wavivu na hawana utaalamu wa kuchunguza hujuma kama hizi na wanachojuwa ni kufata amri za wakubwa wao katika kupiga watu ovyo.
 
Wiki iliyopita kulikuwapo thread moja iliyoelezea hili, kwamba ni mbinu chafu za CCM kuwapakazia uamsho kwamba ndiyo wao waliochoma makanisa? Thread hiyo iliondolewa na kulikuwa malalamiko humu JF kwa nini iliondolewa. Baadaye iliwekwa kwenye back burner, yaani Jukwaa la habari Mchanganyiko bila sababu za msingi ili hali ilikuwa ni ya siasa 100%.

Ukweli sasa waanza kudhihirika nani kashitakiwa kwa kuchoma makanisa, au hata kwa uharibifu wa mali? Utawala wa CCM wasicheze na akili za Watz.
 
Wiki iliyopita kulikuwapo thread moja iliyoelezea hili, kwamba ni mbinu chafu za CCM kuwapakazia uamsho kwamba ndiyo wao waliochoma makanisa? Thread hiyo iliondolewa na kulikuwa malalamiko humu JF kwa nini iliondolewa. Baadaye iliwekwa kwenye back burner, yaani Jukwaa la habari Mchanganyiko bila sababu za msingi ili hali ilikuwa ni ya siasa 100%.

Ukweli sasa waanza kudhihirika nani kashitakiwa kwa kuchoma makanisa, au hata kwa uharibifu wa mali? Utawala wa CCM wasicheze na akili za Watz.

Hilo la kuminywa hiyo thread lilinishangaza mimi pia. Lakini nadhani maaskaofu walifanya haraka mno kutoa lile tamko lao, wangesubiri kidogo kupata ukweli ni akina nani hasa waliochoma makanisa. Nashangaa Maaskofu wanaamini mara moja wasemayo serikali ya CCM.
 
Kilichobakia ni kwa serikali zote mbili ku-come up clean on this issue. Maelezo yao na mambo yalivyokuwa hayaendani kabisa -- ni usanii mtupu.

Na ndiyo maana serikali ya Zenj haraka haraka imekimbilia kusema italipa uharibifu uliotokana na uchomaji wa makanisa, bila hata kutaka kujuwa ni akina nani waliochoma.

Kwa maana nyingine hela za walipa kodi zinatumika kulipia uharibifu bila kumbaini nani aliyeharibu! This is a big SHAME!
 
Aina hii ya mamichezo ya serikali ya CCM ndiyo huletaga farakano na vita ya wenyewe kwa wenyewe katika nchi nyingi humu Barani Afrika.
 
Majungu tu haya hamna lolote!

Siyo majungu -- mbona hawataki kuwabaini waliochoma makanisa ili washitakiwe? Wanafunika funika tu na kukimbilia kusema serikali itafidia!

Isitoshe ni ukweli kwamba waliokamatwa na kufikishwa mahakamani walichajiwa kwa uzuraraji tu na siyo kuharibu mali.

Ndugu yangu ukilipa suala hili fikira kidogo tu utakuta kuna kitu kikubwa kinafichwa.
 
Serikali ya CCM inafikiri imewakomoa Wazenji kumbe ndo inazidi kupandikiza chuki miongoni mwa jamii.
 
Back
Top Bottom