Ukatili kwa Watoto Wadogo! KWA KWELI INANIUMA SANA!!!

mizambwa

JF-Expert Member
Oct 8, 2008
4,422
1,790
Makala

Ukatili kwa watoto washika kasi Geita
Imeandikwa na David Azaria; Tarehe: 6th May 2012 @ 14:59

Ukatili kwa Watoto Geita.jpg

Mtoto Deus Juma (7) akiwa ameunguzwa vibaya kwa maji ya moto na mama yake baada ya kumtuhumu kumuibia shilingi 6,000.



MUSWADA wa Sheria ya Mtoto ya Mwaka 2009 ulipitishwa na bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Novemba, 2009.

Ilikuwa ni miaka 20 tangu Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Mtoto (UNCRC) upitishwe na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mwaka 2009 na miaka 19 tangu kupitishwa kwa Mkataba wa Kimataifa wa Haki na Ustawi wa Mtoto (ACRWC) 1990.

Kutungwa kwa Sheria ya Mtoto ni matunda ya juhudi za muda mrefu za Kitaifa na Kimataifa
kuona kuwa Tanzania inakuwa na Sheria mahususi ya mtoto kwa ajili ya kuendeleza na kulinda haki za mtoto Tanzania.

Pamoja na jitihada zote hizo katika kuhakikisha kwamba haki za watoto zinalindwa na kusimamiwa kikamilifu, Vitendo vya ukatili dhidi ya watoto wadogo bado vinaonekana kuchukua kasi katika maeneo mbalimbali hapa nchini na hivyo kuwaumiza na kuwanyima watoto haki zao za msingi.

Mfano mzuri wilayani Geita mkoani Geita vitendo vya ukatili dhidi ya watoto vinaendelea kuchukua kasi, baada ya mtoto mmoja mwenye umri wa miaka (9) ambaye ni mwanafunzi wa darasa la tatu kujeruhiwa vibaya baada ya kuchomwa moto na mama yake mzazi kwa tuhuma za kula chakula kwa majirani.

Tukio hilo la aina yake limetokea hivi karibuni katika mtaa wa Ihayabuyaga kata ya Kalangalala Tarafa ya Geita ambapo mtoto aliyejeruhiwa ametambuliwa kwa jina la Amina Said, huku Mama mzazi akitambuliwa kwa jina la Rahabu Alphonce (38).

Mtoto huyo amejeruhiwa vibaya mikono yote miwili, mgongoni na tumboni baada ya kuunguzwa na moto na mama yake, hivi sasa anaendelea kupata matibabu nyumbani na hiyo ni kutokana na kuokolewa na majirani ambao walimuwahi muda mfupi baada ya kuchomwa moto na kumpaka dawa ya asili iliyochanganywa na asali.

Akizungumzia tukio hilo katika mahojiano maalumu na gazeti hili mtoto huyo alisema siku ya tukio alifika nyumbani na kumkuta mama yake mzazi ambaye alianza kumuuliza ni kwa nini anakula kwenye miji ya watu.

“Nilifika nyumbani nikamkuta mama anagomba, akanishika na kuanza kuniuliza kwamba ni kwa nini nakula kwenye miji ya watu, ndipo akaanza kunichapa na fimbo, lakini baadaye akanitoa nje ambapo kulikuwa na jiko nililokuwa nimewasha akanishika mikono na kuiingiza ndani ya jiko.’’

Alisema mtoto huyo huku machozi yakimtoka kwa uchungu. “Pamoja na kunichoma mikono lakini mama aliona haitoshi akaamua kunyanyua jiko na kuniwekea kichwani kwa lengo la kunichoma nikapiga kelele kwa nguvu sana za kuomba msaada nikafanikiwa kukimbia ndiyo maana unaona nimeungua huku tumboni na mgongoni kwa sababu baadhi ya mikaa ya moto ilinidondokea’’.

Kwa upande wake mama mzazi wa mtoto huyo katika mahojiano alikiri kumuadhibu mtoto huyo kwa kumchapa fimbo, lakini akakanusha kumchoma kwa moto, huku akiwatupia lawama baadhi ya majirani aliodai kuwa hawampendi kutokana na hali yake ya kutokujiweza (maskini) kwamba ndio waliomfundisha mtoto huyo namna kutoa maelezo.

Alisema aliamua kumuadhibu mtoto huyo baada ya kupata malalamiko kutoka kwa bibi yake na mtoto huyo kwamba watoto wake wamekuwa na mazoea ya kula kwenye miji ya watu hali inayofanya baadhi ya familia kushindwa kushiba chakula.

“Kweli nilimuadhibu kwa fimbo kwa sababu kuna jirani yangu mmoja ambaye alikuja kunitukana kwamba niwe nawapikia watoto wangu chakula wanashiba, kwa sababu wamesababisha mume wake azire kula kutokana na chakula alichokuwa amemtengea kuwa kidogo cha kumtosha lakini watoto wake wameingia kula na kusababisha mumewe kuzira kula kwa vile asingeweza kushiba’’.

“Maneno hayo yalinitia hasira sana ndio maana nikaamua kumwadhibu kama ni suala la kumchapa fimbo ni kweli nilifanya hivyo na nilikuwa na hasira sana kwa sababu watoto wangu wamekuwa wakilalamikiwa sana kwenye mtaa huu kwamba wanapenda kula kwenye miji ya watu, lakini suala la kusema kwamba nilimchoma moto hilo si kweli,’’ alisema mama huyo.

Balozi aliyemuokoa mtoto huyo na kumpeleka kwenye ofisi ya serikali ya kijiji George Makaranga alilithibitishia gazeti hili kwamba mtoto huyo aliunguzwa na moto na mama yake mzazi.

Balozi huyo alilithibitishia gazeti hili kwamba mtoto huyo aliunguzwa na moto na mama yake mzazi.

Anasema siku ya tukio alikimbiliwa na mtoto huyo akipiga kelele kwamba anauawa na mama yake huku akidai amemuunguza kwa moto, ambapo baadhi ya majirani walimuwahi na kumpaka dawa ya kienyeji iliyochanganywa na asali ambapo baada ya kufanya mahojiano ya kina na mtoto huyo aliamua kumpeleka kwenye ofisi ya serikali ya kijiji.

Baadhi ya majirani walioshuhudia tukio hilo walisema mama huyo alimchoma moto mtoto huyo kwa lengo la kumkomesha tabia yake ya kupenda kula kwenye miji ya watu, ambapo alikuwa akidai kuwa watoto wake wamekuwa na tabia ya kula kwenye miji hiyo na kumsababishia lawama kwa majirani.

“Siku hiyo alimpiga sana baada ya kulalamikiwa na mmoja wa majirani zetu hapa kwamba wamemaliza chakula cha mumewe hatua iliyoleta misukosuko kwenye ndoa yake, lakini tatizo lake ni kwamba amekuwa hawapatii chakula kuna wakati wanashinda njaa na sisi kama majirani ndio tunawapatia chakula huku yeye akiwa hayupo…..’’ alieleza mmoja wa majirani aliyejitambulisha kwa jina la mama Rahma.

Tayari mama huyo ametiwa mbaroni na kuhojiwa na jeshi la polisi, hata hivyo polisi wamempatia dhamana kutokana na kuwa na mtoto mdogo mwenye umri wa mwaka mmoja na nusu, pamoja na wengine ambao hawana mtu wa kuwalea wala kuwapikia chakula.

Mkuu wa polisi wa wilaya ya Geita, OCD Paul Kasabago amethibitisha mama huyo kukamatwa
lakini akafafanua kwamba wameamua kumpa dhamana wakati wakiendelea na uchunguzi wa tukio hilo, kutokana na mama huyo kuishi na watoto hao peke yake kwa sababu baba yao anafanya kazi ya kukata mkaa msituni.

Hata hivyo kwa mujibu wa mkuu huyo wa polisi wilaya kutokana na mazingira ya kesi hiyo wanatarajia kumfikisha mama huyo mahakamani Jumatatu hii kwa ajili ya hatua zaidi za kisheria, kwani kitendo kilichofanywa na mama huyo ni ukatili dhidi ya watoto ambao umekuwa ukipigiwa kelele na serikali pamoja na wadau mbalimbali wa haki za watoto.

Tukio hili linakuja huku kukiwa na matukio mengine ya aina yake huko nyuma ambapo katika moja ya matukio hayo katika hali isiyokuwa ya kawaida mwanamke mmoja aliyetambuliwa kwa jina la Mary Dominic alimjeruhi vibaya mtoto wake wa kuzaa baada ya kumuunguza kwa maji ya moto mikono yote miwili na kisha kumfunga na manati kwa siku tatu mfululizo ndani ya nyumba.

Mwanamke huyo ambaye ni mkazi wa Mtaa wa Msalala Road Mjini Geita anadaiwa kumtendea unyama huo mtoto wake wa kumzaa mwenyewe, baada ya kumtuhumu kumuibia shilingi 6,000 ambazo alikuwa ameuza karanga ambayo ni biashara yake inayomuwezesha kuishi na familia yake.

Katika mahojiano na mwandishi wa makala haya, mtoto huyo Deus Juma (7) anayesoma darasa la kwanza katika shule ya msingi Kivukoni, alisema alikumbwa na mkasa huo baada ya kuchukua fedha hizo kwa ajili ya kwenda kununulia chakula kutokana na yeye kukosa chakula mara kwa mara na hasa wakati anapotoka shuleni.

Alisema siku ya tukio baada ya mama yake kurejea nyumbani akitokea kwenye shughuli zake alimuita na kuanza kumpiga huku akimtuhumu kuiba shilingi 6,000 alizokuwa ameziacha ndani ya nyumba, na kwamba pamoja na kujitetea kwa muda mrefu kwamba yeye hakuhusika kwenye wizi huo, lakini aliendela kupokea kipigo kutoka kwa mama yake.

Katika mwendelezo wa matukio hayo ya unyanyasaji dhidi ya watoto yanayofanywa na wazazi wao wa kuwazaa ama walezi mama wa kambo aliyetambuliwa kwa jina la Dafroza Masilu (25) alidaiwa kumuadhibu mtoto wake kwa kumning’iniza juu ya mti kichwa chini miguu juu kwa siku saba huku akimcharaza viboko.

Tukio hilo la aina yake lilitokea katika kijiji na kata ya Kharumwa wilayani Nyangh’wale ambapo iliwalazimu polisi kuwakamata wazazi wote wawili wa mtoto huyo aliyetambuliwa kwa jina la Dickson Majarifu (8) na kuwasweka rumande ambapo hadi sasa wanakabiliwa na shitaka la ukatili dhidi ya mtoto katika mahakama ya wilaya ya Geita.

Mtoto huyo aliokolewa na wanafunzi wenzake ambao walibahatika kumuona siku moja baada ya kupita nyumbani kwao wakitokea shuleni baada ya kutomuona shuleni siku nyingi ambapo walimkuta akiwa amening’inizwa juu ya mti huku akiwa amefungwa kwa kamba.

Kifungu cha 13.(1) kinachozungumzia ulinzi wa mtoto kinasema mtoto hatateswa au kutendewa vitendo vya kikatili, adhabu za kinyama au zinazoshusha utu wake pamoja na vitendo vya kimila/kiutamaduni vinavyoshusha hadhi yake.

Kifungu cha 13.(2) kinaeleza kuwa Hakuna adhabu atakayopewa mtoto ambayo ni kali na isiyo ya kiungwana kulingana na hali ya mtoto kimwili na kiakili, na kupewa adhabu ambayo kulingana na umri wake hatambui maana ya adhabu hiyo.

Ni vyema wazazi na walezi wakazifahamu sheria hizi kuhakikisha kwamba wanasimamia na kulinda haki za watoto mahali popote pale, kwa sababu ni wajibu kufanya hivyo ili watoto waweze kutimiziwa haki zao za msingi, lakini pia serikali isimamie sheria hiyo kwa kuhakikisha kwamba watoto hawatumbukii katika ukatili.

Source: Gazeti "HABARI LEO"



MIZAMBWA
INANIUMA SANA!!!
 
Inakuwaje kina mama wana roho ya ukatili kiasi hiki kwa mtoto wake mwenyewe aliyebeba Ujauzito kwa miezi isiyopungua 9!!!!!


MIZAMBWA
INANIUMA SANA!!!
 
katika binadamu ninayempenda na kumuheshimu duniani hapa ni MTOTO na MAMA yng, haitatokea siku nimfanyie mtoto ukatili kama huo.
 
Imeandikwa "enendeni duniani mkazaane muijaze dunia" lakini ni dhambi kuzaa watoto wengi na kushindwa kuwahudumia. NDUGU TAFAKARI NA UCHUKUE HATUA.
 
Inakuwaje kina mama wana roho ya ukatili kiasi hiki kwa mtoto wake mwenyewe aliyebeba Ujauzito kwa miezi isiyopungua 9!!!!!


MIZAMBWA
INANIUMA SANA!!!
Haya ni matokeo ya ugumu wa maisha ulioletwa na ccm na serikali yake. Mama ameponda kokoto wiki nzima kapata hiyo 6,000 na hana kitu kingine cha kutegemea halafu inatoweka, kwa nini asichanganyikiwe??
 
Haya ni matokeo ya ugumu wa maisha ulioletwa na ccm na serikali yake. Mama ameponda kokoto wiki nzima kapata hiyo 6,000 na hana kitu kingine cha kutegemea halafu inatoweka, kwa nini asichanganyikiwe??

Mmmhhhhhhhhhhhh!!!!!!!!Lakini sasa kumuhukumu mtoto kiasi kikubwa hivi ambaye hana hatia.

Kwa nini tusiandamane tuwachome moto viongozi wetu walioleta maisha magumu.

Tuangalie adhabu nyingine.

Majuto mjuu daima!!!


MIZAMBWA
INANIUMA SANA!!!
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom