Rev. Kishoka
JF-Expert Member
- Mar 7, 2006
- 4,526
- 1,529
Ukahaba Wetu Unatuponza
Tafsiri ya Sanifu ya Kahaba, ni mtu ambaye anajiuza mwili ili ajipatie kipato. Ni mtu ambaye amekubuhu katika fani ya Umalaya na aliyekata shauri kuwa kamwe yeye hata fanya lolote lile bali kujiuza.
Kuna msemo wa Kiswahili unaosema kizuri chajiuza na kibaya chajitembeza.
Ukahaba wetu unaotuponza ni ule wa kujitembeza tukijiuza na kulazimisha kila tunayemhisi kuwa ana pesa au anaweza kutupa pesa, basi sisi humkimbilia na kwa ulegevu mkubwa tunajisalimisha kwake, alimradi katuahidi pesa.
Hatujali wala kupima kama mtu huyu kweli anatujali, ana hata hisia na kuvutiwa nasi na kama dhamira yake ni kuwa na mapenzi ya kweli na sisi. Sisi tunachojali ni zile pesa atakazotupa, ambazo zitatusaidia kununua kitumbua na chai ya rangi, siku inayofuata na kusubiri mtu mwingine atupe pesa kwa ajili ya chakula na malazi kwa siku nyingine.
Jinsi mwili wetu ulivyoumbwa na Mungu, hatuuthamini wala kuupa thamani ya maana ambayo yaweza kutufanya tuwe kile Kizuri kinahojiuza na kujipatia si pesa ya hai tuu, bali ni mtaji mkubwa wa hata kuwalisha vitukuu na vilembwe.
Ni Ukahaba huu wa kukimbilia kujitembeza na kukubali kulaghaiwa na kila mtu hata wale wasio na pesa, ndio unaokomaza umasikini wetu.
Tanzania ni nchi tajiri sana. Tuna Rasilimali za kila aina, bwelele, tele, topu, kedekede, lakini badala ya kuzitunza vizuri na kuzitumia vizuri, sisi tumeamua kwa nguvu moja na kwa kauli moja kuwaachia mabwana wapitao wanaotuahidi hela, nasi tunawagawia hazina na rasilimali yetu kwa dezo, sawa na mtu kahaba asiyethamini mwili, nguvu na akili zake alizopewa na Mwenyezi Mungu.
Inashangaza sana, kwa nchi yetu ambayo mwaka 1967, tulitaifisha kila kitu kutoka mikono ya wageni na kuvifanya mali zetu ili sisi wenyewe tufaidi matunda ya maliasili na rasilimali tulizoneemeshwa na Mungu, leo hii tumegeuka nyuma abautani na kuanza kukimbilia kila anayepita tukiomba aje alime, apalilie na kuvuna kwenye shamba letu na sisi tunachoomba ni kakipande cha muhogo na kopo la mbaazi kujisitiri!
Ni lini tuliingia uvivu na ujuvi wa namna hii, kwamba kila kitu kinatushinda tena kwa hiari na kwa kushindwa kuwa na tija na motisha kufanya kazi na kujitosheleza?
Je tutawalaumu Wakoloni kama vile Wakorea walivyodai kuwa waliondoka bila kutufundisha jinsi ya kusindika matunda?
Tumekuwa huru kwa miaka karibu 50 sasa, na kila kazi inatushinda ila tunayoiweza ni kuombaomba na kutumia mpaka tuishiwe!
Sasa Ukahaba wetu umetufanya tuwe manyang'au, tukikimbilia kuuza kila kitu, kunyang'anyana tonge mdomoni, kuzidiana ujanjaujanja wa nani auze handaki haraka na apate kamisheni yake ya haraka ili aweze kutanua na kurubuni kura za kumfanya awe mtawala wa maisha!
Hebu tafakari unaposikia kauli kutoka kwa viongozi wan chi wakidai kuwa ni lazima tuweke mazingira mazuri ili wawekezaji waje, halafu linganisha na kauli za wawekezaji ambao wanajiingiza kwa ahadi nyingi, ilhali hata mtaji hawana, ila wanategemea kutuzidi maarifa na ujanja na kutumia mali zetu wenyewe kuwa mtaji wa walichoahidi kuja kuzalisha.
Hivi karibuni kumekuwa na msukumo mkubwa unaodai kuwa Tanzania ina sera mpya ya "Kilimo Kwanza" ikiwa ni namna eti ya kufufua shughuli za kilimo ambacho tulishadai siku nyingi kuwa ndio uti wa mgongo wa Uzalishaji mali wetu.
Lakini, ukikaa chini na kutafakari kauli mbiu hii, utabaini kuwa mlengwa na mnufaika wa Kilimo Kwanza si Yule mkulima wa Kisiju au Kingolwira, hata Yule wa Chake Chake na Busanda!
Mlengwa wa kauli mbiu hii ni Yule Yule Bwana mtanashati, anayetembea akijidai ana pesa za kuja kuwekeza ndani ya nchi yetu.
Tunadanganyana kuwa eti Mwekezaji atakuja kutufundisha mbinu bora za kilimo na kuinua ubora wa shughuli za kilimo, lakini jiulizeni, Chuo Kikuu cha Kilimo ha Sokoine kinafanya nini? Je vile vyuo vingine vya kilimo vya Uyole, Ukiliguru, Tengeru na kazwalika, vimeshindwa nini kumfundisha Mkulima wa Tanzania ukulima wa kisasa?
Ikiwa taasisi kama Magereza na SUMA-JKT ambazo kwa miaka mingi zimekuwa na ufanisi mkubwa katika uzalishaji hasa kilimo na kasoro yao kubwa si ukosefu wa Wafanyakazi au Wataalamu bali ni uongozi mbovu, leo hii zinadai eti zinatafuta wawekezaji ili wakodishe ardhi na kuzalisha Chakula, je hamuoni kuwa kuna kasoro kubwa?
Ni mdudu gani huyu aliyewaingilia viongozi wa Tanzania kwa kila ngazi kuwa kila mmoja keshajisalimisha na kuanza kukimbilia kudai Uwekezaji ndio suluhisho?
Mbona wawekezaji wa ndani tunao na wataalamu tunao wengi sana lakini iweje tuwanyime ardhi Watanzania wenzetu na tuende kukodisha kwa Saudi Arabia, Korea, India na China?
Kama lengo ni kusisimua kilimo ha kisasa, je ile program ya mpunga Rufiji iliyofanywa na Wa-Irani wa Uajemi miaka zaidi ya 15 iliyopita haikuzaa matunda?
Je ule mradi wa Mahindi ya Sasakawa na hata wa Konoike kule Kilimanjaro havikutufundisha ustadi wa kuzalisha mahindi na mpunga wa kutosha?
Sasa kama tulifundishwa miaka 16-20 iliyopita kulima kwa kisasa na kina Sasakawa, halafu leo tunadai lazima tutafute wawekezaji wan je watufundishe kilimo bora na cha mashine, je tulirudi nyuma na kujiuliza ni kwa nini mradi wa Sasakawa haukuwa na mafanikio?
Ardhi, ni kitu muhimu sana na mgongano wa ardhi, siku zote ndio umekuwa chimbuko la vita zote duniani. Ndani ya ardhi, iwe ina rutuba au la, kuna hazina kubwa sana ya kutosha. Kuna madini, gesi, mafuta, malisho, maji, na kila unachoweza kufikiri. Mwanadamu mwenyewe aliumbwa kwa udongo ambao ni ardhi!
Sasa kama hatujajifunza kwa wenzetu, wanavyopigania ardhi kila siku na sisi tunaigawa hovyohovyo kisa mpango wa maendeleo ya Mwekezaji na si Mwananchi wa Tanzania, basi iko siku kitone kimoja ha damu kama kile kilichomwagika kule Buzwagi, Bulyanhulu, Loliondo na Grumeti, kitageuka kuwa mto wa damu, tukichinjana kugombania ardhi.
Ubaya zaidi ni jinsi Serikali yetu ilivyoamua kushupalia mambo na kukimbilia kulinda maslahi ya mwekezaji na si ya Watanzania Sawa na Kahaba anayempa kipaumbele mtu anayemhonga na kutokujali watoto wake.
Sasa kama tumeshindwa kuzalisha mali na tunahoweza zaidi ya kuombaomba misaada ni kukimbilia Uwekezaji uchwara uliotuletea TRL,TICTS, ATCL, IPTL, Richmond, Buzwagi na hata kupanua mianya ya uhujumu na ufisadi kama EPA, Meremeta na Rada, kwa nini basi tusiamue kutafuta mwekezaji atakaye kuwa nyapara kwetu sote kuanzia Ikulu na sisi tumtumikie?
Kuna maana gani kudai tuna Uhuru na tunajitawala ikiwa hatuna hata chembe moja ya kuamsha Uzalishaji?
Ikiwa Mkorea kafikia hatua ya kutukebehi kuwa hatukufundishwa kusindika matunda na Mkoloni, je tuaminije kuwa huyu anakuja kwa nia nzuri?
Inasikitisha na inahuzunisha kuwa tumekosa mbinu za kujizatiti na kuzalisha na tunakimbilia kudai tunahitaji wawekezaji. Kama Mzungu, Mwarabu, Mchina, Mhindi na hata Mwafrika mwingine ambaye si Mtanzania anaweza kuja Tanzania na kuzalisha marudufu na kila mmoja wetu akaitika wito na kufanya kazi kwa bidii hini ya mgeni huyu, kwa nini basi tusirudishe Mkoloni ili tuweze kulijenga Taifa letu tukilambwa bakora na mijeledi?
Ikiwa kwa hiari yetu, tu wavivu na hatutaki kufanya kazi na kwa ufanisi, si heri basi aje nyapara au turudi Utumwani tujue moja kama Wana-Israeli walivyoyakumbuka masufuria ya Pharao walipoondoka utumwani Misri?
Leo tunakimbilia kuanzisha makongamano, warsha, semina na kila namna ya kijimkutano na si kwamba tunania ya kujifunza na kufanyia kazi tunachokizungumza, bali tunakwenda kupata alaunsi tujenge nyumba ya pili na ya tatu.
Tumebakia kuwa watu wa mikutano na misafara kutwa kuchwa, tukijilipa mifedha ya ziada ili kutimiza sehemu ya wajibu wetu. Kisha tukishamaliza mikutano hiyo, tunakimbilia kutafuta mwekezaji.
Mwisho wa haya ni mwili wetu kuchoka na kukosa thamani kutokana na kutumiwa na kila mtu, maana hata pesa tutakuwa hatupokei tena bali tutakuwa tukijiuza bure, tukiwa tumekubuhu na kuchujika!