Uhakiki Wa Mali Za Vigogo: Wapewa amri kuwasilisha nyaraka za kibenki, magari

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797

Mwandishi Wetu

Toleo la 241
30 May 2012

WAKATI joto la ufisadi uliofichuliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovick Utouh, kiasi cha kuibua shinikizo la kutaka baadhi ya viongozi kujiuzulu likiwa halijapoa, uhalali wa mali za viongozi wanane wa kitaifa umezua utata na tayari viongozi hao wamepewa siku 30 kuwasilisha nyaraka ili kuthibitisha umiliki wao, Raia Mwema, limeleezwa.

Viongozi hao wametakiwa kuwasilisha nyaraka zao zikiwamo taarifa za kibenki ndani ya siku hizo 30, kuanzia Mei 21 hadi Juni 19, mwaka huu.


Katibu wa Utumishi wa Sekretariati ya Maadili ya Umma, Tixon Nzunda, amethibitisha taarifa hizo na kwamba, muda huo utakapofika bila viongozi hao kuwasilisha nyaraka zao, watapelekwa katika Baraza la Maadili la Tume hiyo.


Katika maelezo yake kwa mwandishi wetu, Nzunda anazungumzia uhakiki wa mali za viongozi uliofanywa katika awamu ya pili kwa kuzingatia ratiba ya Sekretariati ya Maadili ya Viongozi wa Umma akisema; "Awamu ya pili ya uhakiki, ilihusisha orodha ya viongozi 81, lakini ni 76 tu ambao mali zao zilihakikiwa.


"Kati ya viongozi hao (76) ni viongozi 68 ambao walitimiza matakwa ya sheria ya maadili kuhusu tamko la mali. Viongozi wanane wanahitajika kuwasilisha baadhi ya nyaraka muhimu kuthibitisha tamko lao la mali."


Nyaraka wanazohitajika kuwasilisha viongozi hao ni pamoja na za kibenki na kadi za umiliki wa magari yao.


Idadi hiyo ya viongozi wanane ambao wamekutwa na kasoro inaungana na idadi ya viongozi wengine watano waliokutwa na kasoro katika awamu ya kwanza ya uhakiki wa mali zao.


Akizungumzia uhakiki wa chombo hicho chenye dhima ya kusimamia maadili ya viongozi wa umma Nzunda anasema: "Tulifanya uhakiki kwa awamu mbili, awamu ya kwanza tulitakiwa tuhakiki viongozi 60. Lakini kutokana na viongozi watatu kuwa nje ya nchi tulishindwa kuhakiki mali zao na kwa hiyo, waliohakikiwa katika awamu hiyo ni viongozi 57."


Akizungumzia matokeo ya uhakiki huo alisema katika awamu ya kwanza, imebainika kuwa ni viongozi watano ambao mali zao zinalingana na matamko yao lakini kasoro iliyopo ni kwamba, hawajawasilisha nyaraka mbalimbali kuthibitisha mazingira ya matamko hayo.


"Kwa mfano, nyaraka hizo ni pamoja na taarifa za kibenki pamoja na kadi za magari na hao watano tumewapa mwezi mmoja wawe wamewasilisha nyaraka hizo, vinginevyo tutawapeleka kwenye Baraza la Maadili," anasema.


Ukata wakwamisha watendaji

Katika hatua nyingine, Nzunda alimweleza mwandishi wetu kwamba Sekretarieti ya Maadili imeweza kuhakiki mali za viongozi 133 tu, kwa kada ya mawaziri hadi madiwani kati ya idadi kamili ambayo ni viongozi 1,000 pande zote mbili za Muungano.

Kutokana na mazingira hayo ya ufinyu wa bajeti, Nzunda alisema mchakato mwingine wa kuhakiki mali za vigogo utaendelea katika mwaka wa fedha ujao.


"Tunaomba kupewa uwezo zaidi wa rasilimali watu na fedha ili kuweza kutekeleza majukumu yetu kikamilifu. Tayari tumepeleka mapendekezo kwa Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, kuhusu kufanyia marekebisho mfumo wa uendeshaji shughuli zetu kisheria ili tuwe na nguvu zaidi kiutendaji kuliko ilivyo sasa.


"Katika maombi yetu tunataka taasisi ipewe uwezo zaidi wa rasilimali fedha, rasilimali watu pamoja na kufanyia marekebisho mfumo wa kisheria ili uweze kuwa na nguvu katika kusimamia majukumu yetu," alisema.


Kitendawili cha siasa na biashara

Kwa upande mwingine, nia ya kutengeneza sheria itakayotenganisha shughuli za kisiasa na kibiashara kwa lengo la kuwalazimisha wanasiasa wanaotaka uongozi wa umma kujitenga na biashara, imeendelea kuwa kitendawili.

Nia hiyo iliwahi kuonyeshwa na Rais Jakaya Kikwete katika muhula wa kwanza alipoingia madarakani.


Kwa mujibu wa taarifa za Sekretariati ya Maadili, nia hiyo bado inafanyiwa uchunguzi ili kupima athari za matokeo ya utekelezaji wake.


Nzunda amemweleza mwandishi wetu: "Ni dhana mpya (kutenganisha shughuli za siasa na biashara). Ni moja ya maeneo ambayo yanapunguza migongano ya masilahi na kwa hiyo, unapohitaji kufanya hivyo ni vema kufanya utafiti wa kina.


"Lazima tufanye utafiti kwanza ili kuepuka kuingiza nchi kwenye migongano, zipo nchi ambazo nilizungumza nazo mfano, nchi ya Srilanka, Trinidad & Tobago, Marekani na Canada. Zipo changamoto kabla hujaingiza nchi kwenye mfumo huo lazima ujiulize unayo taasisi inaweza kusimamia mfumo huo?


"Tunaendelea kuiomba Serikali ili ituwezeshe kwenda kuangalia nchi za wenzetu ni kwa vipi zimefanikiwa kuendesha mfumo huo.


"Katika utafiti mdogo tulioufanya tumegundua ni nchi tatu tu duniani zimefanikiwa kuendesha mfumo huo, miongoni mwa nchi hizo ni Canada. Kwa upande wa Afrika, Tanzania itakuwa ni nchi ya kwanza".











 
Too much bureaucracy Ni nini tena Baraza la Maadili la Tume ya Mahesabu ya Serikali (CAG) kwanini wasipelekwe Mahakamani Moja kwa Moja?

Ni sawa, sawa kabisa na kuweka juhudi kumbadilisha tabia kichaa.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom