Tumbiliwaulaya
JF-Expert Member
- Nov 22, 2020
- 280
- 435
RAIS mstaafu wa awamu ya pili, Ali Hassan Nwinyi, amebainisha kuwa wakati wa uongozi wake, aliepuka kubishana hadharani
na mtangulizi wake, Hayati Mwalimu Julius Nyerere, akiwaonya viongozi wa sasa kujaribu kupata uhalali wa wanayoyafanya
kwa kutupia lawama viongozi waliopita.
Katika kitabu chake cha 'Mzee Rukhsa, Safari ya Maisha Yangu', Mwinyi anasema aliona ilikuwa muhimu kwake kuepuka kubishana na Mwalimu Nyerere hadharani wala kukosoa uamuzi na yote yaliyofanyika wakati wa uongozi wake. "Ipo hulka ya kibinadamu ya viongozi wapya kujaribu kupata uhalali wa wanayoyafanya kwa kutupa kila aina ya lawama kwa viongozi waliopita.
Hayo, kwa maoni yangu ni makosa makubwa. "Hakuna kitu rahisi kama kukosoa wengine, lakini wananchi hawachagui kiongozi ili akaorodheshe lawama. Ukichaguliwa na wenzako kuwaongoza unakuwa umepewa dhamana kubwa kupeleka taifa mbele. "Wananchi wanataka kuona matokeo chanya ya unachokifanya wewe uliye na serikali kwa wakati huo, wakitambua kuwa kila awamu ya uongozi ina nafasi yake na inachokifanya ni sehemu ya mradi usioisha wa ujenzi wa nchi na kutumikia wananchi," anasihi.
Mwinyi anafafanua kuwa mageuzi mengi yaliyofanyika wakati wa awamu yake hayakuwa ya kutafuta umaarufu, bali kuwaondolea wananchi adha mbalimbali. "Hatukuandika waraka, hatukubuni itikadi mpya na wala hatukutumia majukwaa kujinasibu. Mengi tuliyafanya kimya kimya, kwa ujasiri lakini na hekima pia. "Na siku zote nilijitahidi kupata maoni na baraka za chama na kusikiliza
na kupokea ushauri kwa dhati kabisa na kuuzingatia, si kutimiza wajibu tu.
"Kutoka kwa Mwalimu niliimarishwa hulka yangu ya kusikiliza kwa makini maoni na ushauri wa wengine kabla ya kufanya uamuzi na kuutekeleza. Na baada ya kuelewana na wenzangu tulisambaa nchi nzima kuwafahamisha wananchi," anasema. Mwinyi anabainisha kikwazo kikubwa kilichomkumba wakati wa kufanya mageuzi hayo kilitokana na kundi analiloliita la uhafidhina ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), viongozi wenzake walioona vigumu kukubali haja na hoja ya mabadiliko, hasa pale ambapo hawakuwa na
uhakika na msimamo wa Mwalimu Nyerere kuhusu mageuzi.
Katika kitabu chake hicho, Mwinyi pia anabainisha namna hali ya uchumi wa nchi ilivyokuwa mbaya wakati anakadhibiwa kijiti huku akisifu mchango wa Mwalimu Nyerere katika kurekebisha hali hiyo. Mwinyi anaweka wazi kuwa hata shinikizo IMF na Benki ya Dunia (WB) kwa Tanzania kukubaliana na masharti yao kama nchi inataka fedha (misaada na mikopo) kutoka kwao na wahisani wengine kutoka nchi za Magharibi, lilitatuliwa kwa ushauri wa Mwalimu Nyerere.
Anafafanua kuwa Mwalimu Nyerere hakukubaliana na baadhi ya masharti hayo na aliweka msimamo mkali na hivyo makubaliano hayakufikiwa mpaka anaondoka madarakani. Katika kutatua suala hilo, Mwinyi anarejea ushauri wa Mwalimu Nyerere akimnukuu: "Tazameni, pesa bado tunazihitaji ili tukwamue uchumi wetu uende mbele. Hali ni mbaya kweli. Maadamu mimi nimeng'atuka, sikserikalini, huu ndiyo wakati mzuri wewe Sheikh Ali na timu yako mkamilishe mazungumzo hayo na ninaamini yatakwenda vizuri maana
wakubwa hao wanajua kuwa yule mkorofi keshaondoka".
Mwinyi anasema ataendelea kumshukuru Mwalimu kwa uamuzi wake wa kuitisha kikao cha Kamati Kuu ya CCM (kilifanyika Zanzibar) na kutoa kauli ile mbele ya Kamati Kuu na hivyo kumpa rukhsa ya kuendelea na kazi hiyo ya kuimarisha uchumi wa nchi.
Chanzo: Nipashe