nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
JUMAPILI, SEPTEMBA 16, 2012 08:21 NA MWANDISHI WETU, TANGA
*Mpambanaji wa ufisadi agawa fedha kwa makatibu
*Afadhiliwa na mmoja wa wagombea urais 2015
*Adaiwa kutoa rushwa ya Sh 200,000 hadi Sh 500,000
HALI ya siasa ndani ya Jumuiya ya Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) imezidi kuchafuka baada ya mmoja wanachama wanaowania nafasi ya uenyekiti wa umoja huo kutuhumiwa kugawa fedha kwa makatibu wa wilaya wa umoja huo.
Mgombea huyo ambaye pia ni mpambanaji wa ufisadi, anadaiwa amekuwa akigawa fedha kwa makatibu hao kama njia ya kushawishi achaguliwe katika nafasi hiyo nyeti na ya juu ndani ya jumuiya hiyo.
Kwa mujibu wa chanzo chetu cha habari cha kuaminika kutoka ndani ya UWT, mgombea huyo ambaye pia ni mbunge, amekuwa akifanya vitendo hivyo vya kugawa hongo kwa makatibu hao wa UWT sambamba na kuwalisha viapo wapambe wake.
Chanzo hicho kilisema kuwa tangu yalipopitishwa majina ya wagombea wa nafasi hiyo mjini Dodoma na vikao vya UWT, mgombea huyo aliwakusanya baadhi ya makatibu wa UWT wilayani Korogwe kwa lengo la kuweka mikakati huku akimwaga fedha kuanzia Sh 200,000 hadi Sh 500,000 kwa kila aliyehudhuria kikao hicho.
Kikao hicho ambacho kilifanyika katika hoteli ya Transit kilitoa na azimio huku mgombea huyo akiweka mikakati yake ya kuhakikisha anatumia mikutano ya uchaguzi kupitia mgongo wa makatibu hao.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa mpambanaji huyo wa ufisadi alimtumia Katibu wa UWT Wilaya moja mkoani Kilimanjaro kufanikisha mkakati wake huo.
Katibu huyo wa UWT, alipewa kazi hiyo pamoja na fungu la fedha ambako alitakiwa kugawa kwa kila wilaya Sh 500,000 lakini hakufanya hivyo na kulazimika kugawa Sh 200,000.
"Unajua ndugu yangu kwa muda mrefu UWT ilikuwa na utulivu mkubwa lakini katika kipindi cha uchaguzi wa mwaka huu fedha zimekuwa zikimwaga mno tofauti na miaka iliyopita.
"Mimi pamoja na makatibu wenzangu wa wilaya wa UWT kutoka katika mkoa wa Kilimanjrao tumepewa kila mtu Sh 200,000 badala ya Sh 500,000 tuliyokuwa tumekubaliana tangu awali.
"…, hata hivyo bado fedha tulizopewa sisi ni tofauti na wenzetu wa mkoa wa Arusha ambao kila mmoja amepewa Sh 500,000.
"Tunajua wazi tunachukua hizi fedha kuna kundi la mgombea mmoja wa urais amekuwa akimpa fedha huyu mama aweze kupambana katika uchaguzi Mkuu wa UWT.
"Kwa hali hizi Sh 200,000 tulipopewa tuliahidiwa kumaliziwa kiasi kilichobaki kama tulivyokubaliana pamoja na kwa hali hii sasa ninakiomba chama changu cha CCM kifanye uchunguzi ya kina katika hili," alisema na kuhoji mtoa habari huyo ambaye pia ni Katibu wa UWT katika moja ya wilaya za mkoa wa Kilimanjaro.
Inaelezwa kuwa mgombea huyo wa UWT mbaye pia ni Mbunge amesoma alama za nyakati baada ya kuona hali ya siasa imebadilika katika jimbo lake hali inayoonyesha huenda asirejee bungeni mwaka 2015.
"Jimbo lake huyu mgombea hivi sasa lina upinzani mkali kwa sababu upepo wa siasa umebadilika, CHADEMA waliingilia na kufanya kazi ya ushawishi hivyo kuna hatihati ya kutorejea tena mjengoni mpambanaji huyo.
"….hivi sasa hata anapoitisha mikutano ya wananchi amekuwa akitumia lugha za ubabe dhidi ya wapinzania wake wa ndani ya chama na nje ya chama hali inayodhihirisha wazi kuwa na wakati mgumu," analisema mtoa habari huyo na kuongeza:
"Kwa muda mrefu UWT imekuwa ni injini kubwa ndani ya CCM hasa kila inapofika uchaguzi mkuu wa nchi au wa majimbo ambako huwa na kazi ya kuomba kura za chama kwa wanawake.
"Na katika kipindi chote tulikuwa na utulivu wa hali ya juu ndani ya UWT lakini uchaguzi wa mwaka huu umekuwa na fujo na fitina za kila aina hasa kutoka kwa mmoja wa wagombea wa uenyekiti wa taifa."
Alipotafutwa Katibu wa UWT wa anayetuhumiwa, alikana akisema jambo hilo halina ukweli wowote huku akimtaka mwandishi wa habari hizi kwenda ofisi kwake.
"Duh! ndugu yangu ninakuomba uje ofisini kutokana na jambo hilo kuwa kubwa. Binafsi niseme katika wilaya yangu sijapewa fedha na mgombea yoyote ila ninakuomba uje ofisini tuzungumze zaidi.
"Pamoja na hali hiyo lakini napenda kusema ….Sina uhusiano na fedha zilizokuja ndani ya wilaya yangu zilitoka makao makuu ya chama ndugu yangu," alisema.
MTANZANIA Jumapili ilipomtafua Katibu wa Halmashauri Kuu, Itikadi na Uenezi Nape Nnauye kujua namna chama hicho kinavyopambana na wagombea wanaotoa rushwa, alisema katu chama hicho hakiwezi kuvumilia vitendo vya rushwa.
Aliweka wazi kuwa ikiwa kuna wagombea watabainika wanafanya hivyo watachukuliwa hatua hata kama watafanikiwa kushinda katika uchaguzi.
Katika vikao vya Baraza Kuu la UWT ililofanyika mkoani Dodoma hivi karibuni, majina matatu yalipitishwa kuwania uenyekiti wa UWT.
Hao ni Mwenyekiti wa sasa anayetetea nafasi yake, Sophia Simba, Mbunge wa Same Mashariki Anne Kilango na Meryrose Magige.
Hata hivyo upinzani mkali unatarajiwa kuwa kati ya Sophia Simba ambaye anaonekana kuungwa mkono na kundi kubwa la wajumbe wa mkutano mkuu kwa kusimamia sera yake ya viti maalum kuwekewa kikomo ili kila mwanamke aweze kupata nafasi ya ubunge huku Anne Kilango, akisimami sera yake ya kuondoa ukomo katika ubunge wa Viti Maalum ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
| ||
|