Uchaguzi Kenya ghali zaidi Afrika, namba mbili duniani

Majs

JF-Expert Member
Dec 21, 2012
229
485
SIKU 10 tangu kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa Kenya, imeelezwa kuwa nchi hiyo ndiyo inayoongoza kwa kufanya uchaguzi ghali zaidi barani Afrika.

Aidha, kwa duniani imeshika nafasi ya pili, ikitanguliwa na Papua New Guinea inayotajwa kuwa kinara duniani, kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali vya habari. Wakati Papua NewGuinea ikitajwa kumgharimu kila mpigakura Dola za Marekani 63 (Sh 132,300 za Tanzania), Kenya imetajwa kumgharimu kila raia wake dola 25.4 (Sh 53,340) ili kulipia gharama za kila kura katika mchakato huo wa kidemokrasia.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha ya Kenya, Kamau Thugge katika taarifa yake kabla ya Uchaguzi Mkuu wa Agosti 8, mwaka huu, makadirio ya fedha za uchaguzi yalikuwa Shilingi za Kenya bilioni 49.9, sawa na dola za Marekani milioni 499 (Sh trilioni 1.04 za Tanzania). “Ni gharama za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja katika uchaguzi.

Kenya.jpg

Gharama za moja kwa moja ni Shilingi za Kenya bilioni 33.3 (Dola milioni 333, sawa na Sh za Tanzania bilioni 700). Kwa mujibu wa mchanganuo uliokuwa umetolewa, dola milioni 429 zilitakiwa kwenda Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), huku kiasi kingine kikisambazwa kwa ajili ya mahakama, taasisi za usalama na msajili wa vyama vya siasa.

Hii ina maana kwamba, kwa dola 25.4 kwa kila mpigakura kati ya Wakenya milioni 19.6 waliojiandikisha, imetia fora kwa kufanya uchaguzi ghali zaidi katika Bara la Afrika. Inaelezwa kuwa, mwaka 2013 Kenya ilitumia Sh bilioni 26 za nchi hiyo, sawa na Dola za Marekani milioni 260 (Sh bilioni 540) kwa ajili ya uchaguzi mkuu uliomweka madarakani kwa mara ya kwanza Uhuru Kenyatta.

Kiasi hicho ni takribani mara mbili ya uchaguzi wa mwaka huu. Uchaguzi Mkuu wa Kenya mwaka huu pia umevutia idadi kubwa ya wagombea, ambapo kulikuwa na wagombea 16,259 wakiwania nafasi mbalimbali 1,882 huku katika kiti cha urais kilichowaniwa na wagombea wanane, Uhuru Kenyatta (55) alirejea madarakani baada ya kuvuna asilimia 54 ya kura milioni 15.6 zilizopigwa, akimbwaga kwa mara nyingine mshindani wake, Raila Odinga aliyepata asilimia 44.4 ya kura zote.

Hata hivyo, Raila aliyewania urais kwa tiketi ya Muungano wa Vyama vya Upinzani (NASA), ikiwa ni mara yake ya nne kuisaka Ikulu ya Kenya, lakini bila mafanikio, amegomea matokeo ya uchaguzi huo akidai haukuwa huru na wa haki, licha ya waangalizi wa kimataifa kuusifia uchaguzi huo kuwa haukuwa na dosari. Raila mwenye umri wa miaka 72, amekwenda mahakamani kupinga rasmi matokeo ya uchaguzi huo.

Katika Afrika Mashariki, Rwanda ambayo pia imefanya uchaguzi wake mkuu mapema mwezi huu uliomrejesha Rais Paul Kagame madarakani, hivyo kuendelea kuongoza kwa muhula wa tatu, imeelezwa gharama zake za uchaguzi kuwa zimemgharimu kila mpigakura Dola ya Marekani 1.05 (sawa na Sh 2,205 za Tanzania). Ilikuwa na wapigakura waliojiandikisha milioni 6.8.

Katika mwaka 2010, inakadiriwa kila mpigakura wa Rwanda aliigharimu nchi yake dola 1.71 (Sawa za Shilingi za Tanzania 3,591). Gharama za Uchaguzi Mkuu wa Uganda wa mwaka jana, 2016 zinaonesha zilikuwa sawa na Dola 4 za Marekani (Shilingi za Tanzania 8,400), wakati Uchaguzi Mkuu wa Tanzania wa mwaka 2015 uliomweka madarakani Rais mchapakazi na `kioo’ cha nchi nyingi, Dk John Magufuli ulimgharimu kila mpigakura dola 5.16 (Shilingi za Tanzania 10,836).

Uchaguzi wa Ghana wa mwaka jana umetajwa ndiyo uliokuwa na gharama za chini zaidi barani Afrika, kwa wastani wa dola 0.70 (Sh 1,050 za Tanzania), wakati kiwango cha chini duniani ni wastani wa dola 5 (Sh 10,500 za Tanzania). Nigeria, taifa lenye watu milioni 186 ambalo lina wapigakura takribani milioni 70, mwaka 2015 lilitajwa kutumia dola milioni 603 (Sh za Tanzania trilioni 1.26), sawa na dola 8.61 (Sh 18,081) kwa kila mpigakura.

Tume ya Uchaguzi Tanzania Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Ramadhan Kailima amesema kuna mambo ambayo Tanzania inaweza kujifunza kwa namna ambavyo uchaguzi nchini Kenya umefanyika. Aidha, ameipongeza Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka nchini Kenya (IEBC) kwa kufanya vizuri katika uchaguzi mkuu uliofanyika Agosti 8, mwaka huu na Rais Kenyatta kurejea madarakani akiwabwaga washindani wake saba, akiwemo wa karibu, Odinga.

“Tume imefanya mambo mazuri sana na wamekuwa mfano hata kuna taasisi zimesema hivyo ikiwemo AU (Umoja wa Afrika) na EU (Jumuiya ya Ulaya), hivyo nina kila sababu ya kumpongeza mtendaji mwenzangu,” alisema Kailima. Alisema utaratibu waliotumia hauna tofauti na utaratibu uliotumika nchini katika uchaguzi mkuu uliopita, lakini kuna baadhi ya mambo yanapaswa kuigwa kutoka kwao. “Mfano matumizi makubwa ya teknolojia, utoaji wa elimu ya mpigakura ambapo wao wameanza kipindi cha maandalizi ya kuboresha daftari la kupigia kura, lakini sisi tutafanya kwa mwaka mzima, kufanya midahalo baina ya Tume na wananchi ili wapate nafasi ya kuuliza maswali na kujibiwa,” alisema Kailima.

CHANZO: Habari Leo
 
Back
Top Bottom