Ubovu wa filamu za bongo tatizo ni ubinafsi wa waandaaji

Jumakidogo

R I P
Jul 16, 2009
1,851
417
Nimekuwa nikifuatilia kwa makini sana maoni ya wadau mbalimbali kuhusu ubora wa filamu zetu za kibongo. Wengi wamekuwa wakitoa changamoto badala ya kupongeza kazi za sanaa hiyo ya filamu kwa sababu ya kuchoshwa na kile ambacho kinaandaliwa na waigizaji hao hasa kwa upande wa hadithi za filamu hizo. Kwa bahati nzuri mimi ni mwandishi wa riwaya na simulizi za kusisimua hapa nchini. Binafsi nimekuwa nikifuatilia hadithi za filamu mbali mbali na kugundua kuwa waigizaji wetu wametawaliwa na tamaa ya kutaka sifa pamoja na ubinafsi wa kutaka kuonekana kuwa kila kitu kimefanywa na yeye. Matokeo kinachofanyika hakitokani na hadithi bali ubabaishaji wa maneno na mionekano yao ya kutaka kujiweka katika hali ya juu kwa kila filamu wanazoigiza. Ifahamike kuwa, msingi mkubwa wa filamu nzuri ni hadithi, hadithi ndiyo inayompa muigizaji muongozo wa nini kinachotakiwa katika muonekano wa filamu hiyo. Utunzi wa hadithi ni kipaji maalumu. Si kweli kwa sababu mtu anao uwezo mkubwa na kipaji cha kuigiza basi ajipe na kipaji cha utunzi wa hadithi. Hadithi ni kitu kingine na, uigizaji nao ni kitu kingine. Matokeo yake ndio haya, kila pembe ya nchi kumekuwa na malalamiko ya mashabiki wa filamu kuwa wanachoshwa na aina ya filamu zinazochezwa bongo. Napenda nikili tu kwamba, kwa sasa waandishi na watunzi wa hadithi hapa nchini wamebaki wachache sana. Lakini hilo lisiwe kikwazo kwa sababu waliopo wanafahamika na, kazi zao nzuri zinaonekana. Ikiwa ni lazima mwigizaji aonekane yeye ndiye mtunzi, ni kazi rahisi. Kwani si lazima mtunzi ajulikane, zungumza na mwandishi wa hadithi kisha mwisho wa kazi bandika jina lako. nani atajua? kuliko kuwalisha watu makapi. Nikiwa kama mwandishi na mtunzi wa riwaya hapa nchini, nawapa fursa waigizaji. Msiogope, leteni aidia zenu za kile mnachotaka kufanya. Si kazi kwa mtunzi mwenye kipaji kuandika hadithi za filamu. Acheni ukiritimba, sisi sote ni wasanii wenye jukumu la kuendeleza sanaa hapa nchini.
 
Juma, kumbuka kuwa filamu ni zao la muongozaji wa filamu (film director) na si
zao la mtunzi wa hadithi, mwandishi wa script, mwigizaji au mtayarishaji. kumbuka
kuwa hata kama utakuwa na hadithi nzuri lakini kama muongozaji ni boya usitegemee
kupata filamu nzuri, lakini pia haidithi nzuri inamhitaji mwandishi mzuri wa script ambaye
ataiwasilisha vizuri kwa kufuata misingi ya uandishi wa script ndipo utakapopata zao zuri.
Usiangalie kuhusu hadithi tu ukasahau mambo mengine ya msingi kwani mwisho wa yote
kazi huishia kwa muongozaji wa filamu...

Endapo hadithi ni mbovu lakini ikampata muongozaji mzuri anayeijua vyema kazi yake,
hataitumia hadithi hiyo hadi ahakikishe kuwa imetimiza kiwango anachokitaka...
Mi' nadhani badala ya kukimbilia kwenye kuongelea hadithi (najua unapiga debe kwa
kuwa unaandika hadithi, ingawa nakushauri ujifunze kuandika script), hadithi nzuri bado
haikuhakikishii kupata zao zuri endapo mwandishi wa script atakuwa mbovu. Tungeongelea
ubora wa script (muswada andishi wa filamu) na uongozaji kwani ni miongoni mwa mambo
makuu matano yanayotajwa kuifanya filamu iwe bora, mengine yakiwa ni uigizaji mzuri,
upigapicha mzuri na uhariri mzuri.

Jifunze kuandika script kwani utunzi haukusaidii kwa kuwa kiasili kila binadamu ni mtunzi
na kwenye tasnia ya filamu mtunzi anahesabika kama ni mtoa wazo tu...
 
Sawa Bishop...
Sasa kila mtu akitaja kaeneo kamoja na kutaka kujenga hoja kuwa hako ni muhimu kuliko kengine itakuwa nini? Si itakuwa sawa na kuanza kulinganisha umuhimu wa viungo vya binadamu wakati kumbe kila kiungo kina umuhimu katika kumkamilisha binadamu! Hoja kubwa ni SANAA YETU kwa ujumla,
Tuna tatizo kubwa sana kwenye sanaa kwa ujumla wake ambapo pia kwa umuhimu wa sanaa inakuwa rahisi kusema tuna tatizo KIJAMII..!
Ila kwa kurudi kwenye topic, pia ni ngumu kufanya hvyo vitu ambavyo wote tutasema kwenye tasnia hii katika ubora ule unaotamaniwa kama SOKO linavuja kiasi hichi... Mwisho wa siku filamu nzuri ni uwekezaji, nani atawekeza kwenye soko lenye matundu kama hili letu? Tutatafuta mchawi sana lakini bila uratibu sahihhi wa kidola (serikali) kwenye sanaa hamna kitu kikubwa sana na cha kimataifa tutaweza kufanya. Tupeane mifano ya nchi ambayo imesogea kisanaa bila mkono wa serikali....
Ntarudi
 
jouneGwalu,
Nashukuru kwa kuliona hili, nakubaliana kabisa na wewe kuhusu mifano uliyotoa
hasa pale ulipoifananisha tasnia ya filamu na mwili wa binadamu. Kimantiki
ndivyo ilivyo. Pia nakupongeza kwa kuliona suala la umuhimu wa serikali yetu
kushiriki kwenye tasnia hii kwa maendeleo ya soko la filamu ndani na nje ya nchi.
Ikumbukwe kuwa serikali iliunda Wizara ya Utamaduni wa Taifa na Vijana mwaka 1962,
muda mfupi tu baada ya uhuru wa nchi yetu, rais wa wakati huo, Mwalimu Julius Nyerere,
alitamka wazi kuwa Utamaduni ndiyo kiini na roho ya Taifa, na nchi inayokosa utamaduni
wake ni sawa na mkusanyiko wa watu usiokuwa na roho na hivyo kukosa sifa ya kuitwa
taifa kamili.
Lakini katika miaka hii hamsini ya uhuru nchi yetu inashuhudia mmomonyoko mkubwa
wa maadili katika jamii huku tasnia ya sanaa/utamaduni ikionekana kutelekezwa kabisa
na serikali yetu bila kujali kuwa tasnia hii imesheheni utajiri mkubwa ambao kama ungetiliwa
maanani ungeliingizia taifa hili pato kubwa.
Ingawa sekta ya sanaa na utamaduni imekuwa katika mfumo wa serikali tangu 1962
nafasi yake katika maendeleo ya taifa bado haijatambuliwa kikamilifu. Cha kushangaza
pamoja na umuhimu uliopo katika suala la sanaa na utamaduni kwa maisha ya watu,
bado sera ya utamaduni imepewa nafasi finyu sana katika serikali yetu tangu ilipoanzishwa
wizara ya kushughulikia masuala ya sanaa na utamaduni.
Sera ya utamaduni ilizinduliwa Agosti 23, 1997 mjini Dodoma, hii ilikuwa ni hatua ya pili
muhimu baada ya ile ya kwanza ya kuundwa kwa Wizara ya Utamaduni wa Taifa na Vijana
mwaka 1962.
 
Back
Top Bottom