Tuzungumze biashara: Weka kumbukumbu ya unachodaiwa

Majs

JF-Expert Member
Dec 21, 2012
229
485
TUMEZOEA kuona wateja wakidaiwa na mara nyingi kuamini kwamba, kwa sababu mwenye duka ndiye anayemiliki bidhaa ziuzwazo, uwezekano wa kudaiwa na mteja haupo au ni kwa asilimia ndogo sana.

Mtandao wa maswali Www.ask. com unasema kwa nchi zilizoendelea, suala la mteja kumdai mmiliki wa biashara ni la kawaida na huruhusiwa katika mazingira fulani ya kibiashara, ilimradi kuwe na utaratibu.

Hata hivyo, mtandao huo unasema kuwa inapotokea kutoelewana kati ya mteja anayemdai mmiliki na hasa ikiwa kuna mikataba ya madai au maandishi ya kuthibitisha kudaiana au kumbukumbu zozote zinazoonesha kuwa A anamdai B, ni rahisi kusuluhisha na kuruhusu maisha ya kibiashara yasonge mbele.

Kwa mujibu wa mtandao mwingine, Www.answers.com unaotambulika kuwa ni mtandao wa majibu, mitafaruku katika biashara inayoibuka kati ya mteja anayemdai muuzaji au mmiliki wa biashara na mmiliki husika au muuzaji hutokea pindi zinapokosekana taarifa za kudaiana kwao.

“Wateja wengi wamepoteza fedha zao kwa kukataliwa kulipwa kwa sababu ya kutokuwa na kumbukumbu za makubaliano ya kukopeshana fedha au bidhaa... “Kwa kawaiđa binadamu wasio waaminifu hawaonekani usoni, hivyo kutojulikana endapo watakuwa wasumbufu kulipa wanachodaiwa au kama watakataa jambo lolote linalohusishwa na kulipa wanachodaiwa,” unasema mtandao huo.

Unaongeza: “Cha msingi mteja ahakikishe anatunza kumbukumbu za makubaliano ya kudaiana ili asikanwe.” Mtandao huo unaeleza kuwa yapo mazingira ambayo mmiliki wa biashara anaweza kudaiwa na mteja wake na kwamba jambo hilo si la ajabu na wala si kosa.

Www.answers.com inaeleza kuwa katika mazingira ambapo mteja analipa gharama ndipo aandaliwe bidhaa au huduma, uwezekano wa kuwepo deni ni mkubwa hasa inapotokea kuwa malighafi kwa ajili ya kuitengeneza bidhaa hiyo hazipatikani kwa wakati au ni lazima ziagizwe kutoka mbali, mfano nje ya nchi.

Kadhalika, inaelezwa kuwa mmiliki wa biashara anaweza kudaiwa na mteja wake ikiwa atahitaji amkopeshe kiasi fulani cha fedha, huduma au malighafi, jambo ambalo si baya kibiashara, kwa sababu linalenga kuchangia kukuza mtaji. “Kinachotakiwa ni uaminifu wa mdaiwa (mmmiliki wa biashara), kwa sababu anapoupoteza uaminifu alionao kwa jambo kubwa au dogo, anakuwa amewapa wateja wake tiketi ya kumkimbia.

Www.ask.com inaweka wazi kuwa biashara nyingi hufanikiwa kwa sababu ya uaminifu wa wanaoziendesha,hasa kwa wateja wanaowaamini, wa zamani na wapya. Www.ask.com inasema, ili mfanyabiashara asijichanganye na kukataa deni la kweli, analazimika kuweka kumbukumbu sahihi kuhusu watu wanaomdai na anaowadai.

Mtandao huo unaeleza zaidi kuwa mfanyabiashara hapaswi kuchukulia kila jambo kuwa ni mzaha, kwa sababu wateja wanaojitambua huweza kuamua kumchukulia hatua.

CHANZO: Habari Leo
 
Back
Top Bottom