Tunaomboleza janga hili, lakini tutajifunza lini?

jamadari

JF-Expert Member
Feb 13, 2010
295
92










KATUNI(530).jpg

Maoni ya katuni


Taifa linaomboleza msiba mkubwa wa vifo vya takribani watu 240 waliopoteza maisha katika ajali mbaya ya meli ya Spice Islander iliyotokea usiku wa kuamkia Jumamosi, ikisafiri kutoka Unguja kwenda Pemba. Pia kiasi cha watu 521 hivi wameokolewa.

Ajali hii imeacha machungu na maombolezo kwa familia nyingi za Wazanzibari. Walioumia kwa njia mbalimbali kutokana na ajali hii si Wazanzibari tu, Watanzania kwa ujumla wetu tumeumia, tumepoteza raia wenzetu, nguvu kazi ya taifa imepotea na ni machungu kwa taifa zima.

Tunachukua nafasi hii kuwapa pole wote waliopoteza ndugu, jamaa au marafiki katika janga hili baya. Mahususi, tunazipa pole familia zilizofiwa na kuziomba ziwe na moyo wa subira katika kipindi hiki kigumu, kadhalika tunawapa pole majeruhi wote wa ajali hii, tunawatakia uponaji wa haraka ili wawe na afya njema ya kurejea katika shughuli zao za ujenzi wa taifa.

Mengi hadi sasa yamezungumzwa juu ya chanzo cha ajali hii, hata hivyo, hadi sasa hakuna taarifa rasmi kamili ya chanzo hasa cha ajali hiyo, kuna taarifa tu ambazo si rasmi. Wapo wanaosema kuwa kupakia abiria na mizigo kupita uwezo wa meli ni chanzo cha janga hilo.

Wapo wasafiri waliosafiri na meli hii ambao wameshuhudia kwamba mara baada ya meli hiyo kung’oa nanga bandari ya Malindi, Zanzibar, ilianza kuonyesha dalili kwamba kila kitu hakikuwa sawa. Wapo walioshuhudia kwamba ilifika wakati nahodha wa meli hiyo akawataka abiria kuhamia upande mmoja wa meli baada ya kuona ikiegemea upande mwingine ili kuweka mzania sawa.

Abiria hawa wanasema wakati hayo yakitokea hakukuwa na hatua zozote za dharura zilizochukuliwa na wahudumu wa meli hiyo kama vile kugawa maboya ya kujiokolea wakati wa dharura kama ilivyotokea.

Ndiyo maana kila anaeeleza alivyopona anasema ama alishikilia godoro au gunia la mchele au unga vitu ambavyo vilikuwa ni mizigo ndani ya meli hiyo; kwa kifupi walionusurika katika ajali hii iliyotokea saa saba usiku walijitahidi kijinusuru kwa kutumia vitu ambavyo si rasmi kujiokoa kwa kuelea baharini zaidi ya saa saba. Wengi walianza kuokolewa saa mbili asubuhi.

Kila tunapoitazama ajali hii, tunajawa na woga mkubwa kwamba ni kwa nini hali hii tena nchini? Sote tunakumbuka kwamba mwaka 2009 meli ya MV. Fatihi ilizama baharini Zanzibar na kusababisha vifo vya watu saba; iliundwa Tume kuchunguza janga hilo lakini hakuna hatua za maana zilizochukuliwa kuadhibu wote waliozembea hadi meli hiyo ikaleta maafa hayo.

Tukiwa katika hofu hii, tunakumbuka kwamba Mei, 1996, meli ya MV. Bukoba ilizama katika ziwa Victoria na kuua zaidi ya watu 800. Hawa walikuwa ni abiria waliokuwa wanasafiri kutoka Bukoba kwenda Mwanza. Meli hiyo ilizama umbali mfupi kabla ya kutia nanga katika bandari ya Mwanza.

Walionusurika kwenye MV. Bukoba walisema meli hiyo ilianza kuonyesha dalili mbaya tangu mapema wakati wanaondoka bandari Kemondo, Bukoba. Ilikuwa imeegemea upande mmoja, chanzo kikielezwa ni kuzidisha mizigo na abiria kuliko uwezo wake. Taifa liliomboleza kwa machungu mengi, watawala waliunda tume kuchunguza, hatua za maana zilizochukuliwa kwa maana ya kuzuia uzembe katika vyombo vya usafiri vya majini.

Tunajua Serikali ya Mapinduzi Zanzibar au kama inavyoitwa siku hizi, Serikali ya Umoja wa Kitaifa, itachunguza ajali hii. Tunaamini uchunguzi huu hautakuwa kama ule wa MV. Fatihi, kwamba fedha za walipa kodi zinatumika kufanya uchunguzi wa mambo yaliyokwaza na kutatiza jamii, lakini hakuna hatua zinazochukuliwa hata pale ripoti ya uchunguzi inapoonyesha dhahiri kuwa kulikuwa na uzembe.

Mwaka 1996 MV. Bukoba ilipoteketeza maisha ya Watanzania wenzetu karibia 1,000 hakuna yeyote aliyewajibika kwa maana ya wenye dhamana ya kusimamia sekta ya usafiri wa majini, si watendaji wala wanasiasa.

Utamaduni huu wa watu wenye dhamana kuwajibika kwa makosa yanayotokea katika maeneo wanayosimamia bado haujakubalika nchini; wengi wanaona kuwa matukio kama haya ya ajali ni kawaida hivyo hawana sababu ya kuwajibika kwayo.

Ni hakika katika mazingira ya uwajibikaji uliotukuka, mambo ya meli kujaza kupita kiasi hayawezi kutokea kwa sababu kuna vyombo vingi vya ukaguzi, inawezekana tu kama mambo yameachwa yajiendeshe yenyewe, hakuna usimamizi, hakuna uwajibikaji. Ni katika mazingira kama haya ndipo tunapoona kwamba leo mwaka 2001 miaka 15 baada ya ajali ya MV.

Bukoba, bado Watanzania wanaomboleza tena kwa staili ile ile, ndiyo maana tunasema kuwa tumeshindwa kujifunza hata kwa makosa yetu wenyewe? Ni kweli tuna machungu na tunaomboleza lakini msaada wetu sasa utatoka wapi kukosesha majanga haya?




CHANZO: NIPASHE

 
Nimejifunza kuwa nchi yangu inangojea watu wafe kwenye ajali ndipo inapoanza mikakati ya kudhibiti vyombo vya usafiri.
 
Back
Top Bottom