Tume ya warioba zanzibar

abdul 28

JF-Expert Member
May 29, 2012
325
38
Maofisa wake Z'bar watumia vifaa vya CCM mikutanoni
*Mwenyekiti na Makamishna waduwaa, wapiga stop

WAKATI Tume ya Mabadiliko ya Katiba ipo katika hatua za mwisho kupokea maoni ya wananchi wa Zanzibar juu ya mabadiliko ya katiba mpya, maofisa wake wameiingiza katika kashfa baada ya makamishina wake kudaiwa kutumia vifaa vya Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika mikutano yao ya kuratibu maoni ya wananchi.

Vifaa hivyo ni meza, viti na maturubai, ambavyo vimeandikwa neno 'CCM' na hivyo kutoa tafsiri kwamba Tume hiyo iko chini ya Chama Cha Mapinduzi katika kufanya kazi zake.

Habari za uhakika ambazo RAI imezipata kutoka ndani ya Tume hiyo, zimebainisha kuwa uzembe huo umefanywa na maofisa wake wa Wilaya ya Mjini, ambao ndio waratibu wa zoezi hilo.

Imeelezwa kwamba hali hiyo imechangia kuwapo vurugu zinazoendelea kwenye maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Mjini Zanzibar, ambako hivi sasa zoezi la kuchukua maoni ya wananchi linaendelea, huku wananchi sehemu mbalimbali wakilalamikia kuwapo hali ya vitisho miongoni mwao.

Hali hiyo imetafsiriwa kuwa siyo 'image' nzuri kwa Tume inayoongozwa na watu waadilifu na wanaoheshimika katika ngazi za uamuzi nchini, ambao ni Jaji Joseph Warioba na Jaji Augustine Ramadhan.

Uzembe uliofanywa na maofisa hao umesababisha baadhi ya wafuasi wa CCM kujiona wako juu ya Tume na hivyo kuzua sintofahamu kwa wananchi na wafuasi wa vyama vingine.

Tayari Tume hiyo imepiga marufuku matumizi ya vifaa vya CCM katika mikutano yao, baada ya kubaini ndio chanzo cha vurugu zinazotokea katika mikutano yao katika maeneo mbali mbali ya Wilaya ya Mjini.

Mmoja wa Makamishina hao (jina tunalo), ameiambia RAI kuwa, vurugu zilizotokea hivi karibuni, zimechangiwa na wananchi kutojua mipaka yao katika zoezi la kutoa maoni.

"Vurugu hizi zimekuja kwa sababu kila kundi hawajui mipaka yao, kila mmoja linafikiri lina haki kuliko jingine.

"Jambo la pili, wote hawajui sheria kama inasema kuwa kila mtu aliyeifuata Tume ana haki ya kutoa maoni, mbona Wilaya ya Magharibi mambo yalikuwa mazuri, lakini tumekuja Mjini mambo yameharibika.

"Kuna tatizo, hawajui kuwa Mtanzania yeyote ana haki kutoa maoni popote anapoikuta Tume, lakini utasikia watu wengine wanalalamikia watu kuletwa na magari.

"Lakini wapo wanaopanga nani atoe maoni na nani asitoe hili pia ni tatizo, hawa watu zaidi ya wiki mbili wanatufuata na wanao ushawishi mkubwa, lakini kibaya zaidi wanakuja kukaa kwenye viti ambavyo sisi makamishna tumekaa.

"Na kama umesikia mwenzetu mmoja alishambuliwa kwa maneno makali na mmoja wa wabunge na sababu kubwa tunatumia viti, meza na maturubai yao. Hii si 'image' nzuri kwa Tume, ni uzembe uliofanywa na waliopewa kufanya kazi hiyo.

"Tume haijapanga kufanya hivyo kutumia vifaa vya CCM, kazi hiiimefanya ma maofisa wa wilaya, lakini tayari imepiga marufuku kutumia vifaa vya CCM," alisema mjumbe huyo.

Hata hivyo Mratibu wa zoezi la ukusanyaji maoni Zanzibar, Assah Rashid, alipotafutwa na RAI kwa njia ya simu ya kiganjani kuzungumzia hali inavyoendelea katika mikutano hiyo, na nini kinafanyika, alisema yuko kwenye kikao na kumtaka Mwandishi ampigie simu baada ya saa moja, lakini baada ya saa kupita alipopigiwa hakupokea simu yake.

Vurugu zilizotokea katika mikutano ya kukusanya maoni ya Katiba mpya kwenye baadhi ya maeneo Zanzibari, zinadaiwa kuchochewa na wanasiasa na zimesababisha baadhi ya watu kujeruhiwa kwa kuchomwa visu.

Juzi makamishina wa Tume, walilazimika kusitisha mikutano ya wananchi baada ya kuibuka vurugu za kisiasa zilizosababisha watu kurushiana mawe.

Maeneo yaliyokumbwa na vurugu hizo na kusababisha mikutano kuvunjika, ni kwenye Shehia za Magomeni na Mpendae, katika Wilaya ya Mjini Unguja.

Tume ipo katika hatua za mwisho kumaliza kazi ya kupokea maoni ya wananchi, juu ya marekebisho ya katiba kwa upande wa Zanzibar.

Tume hiyo inapokea maoni ya mwisho kwa wananchi wa Mkoa wa Mjini Unguja, chini ya Mwenyekiti wake Profesa Mwesiga Baregu.

Wakati Tume ikiwa katika hatua za mwisho kumaliza kazi yake, maoni ya wananchi wa Zanzaibar yamejielekeza kwenye suala la Muungano.

Wafuasi wa CCM wakitaka Serikali mbili na hadhi ya Rais wa Zanzibar kwenye Muungano irejeshwe, huku wafuasi wa CUF wakitaka Muungano wa Mkataba na Zanzibar kuwa na mamlaka kamili katika Umoja wa Mataifa.
 
Back
Top Bottom