Tume ya Warioba yatupiwa lawama, Zanzibar

jamesbond007

Member
Jun 27, 2012
36
8
Tume ya Warioba yatupiwa lawama

Tume ya kukusanya maoni ya Katiba inayoongozwa na ya Jaji Joseph Warioba, imetupiwa lawama kwa kushindwa kuchukua hatua za kisheria dhidi ya baadhi ya viongozi wa CCM wanaowatisha wanachama wasitoe maoni ambayo yanatofautiana na msimamo wa chama hicho.

Waziri wa Miundombinu na Mwasiliano wa Zanzibar, Rashid Seif Suleiman, alisema tume hiyo ina kila sababu za kuchukuliwa hatua za kisheria kwa sababu wanachofanya ni kosa chini ya Sheria ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

Alisema kitendo hicho kinapora uhuru wa wananchi kutoa maoni juu ya aina ya mfumo wa Muungano wanaoutaka.

Seif alikuwa anachangia mada juu ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba iliyowasilishwa katika semina ya wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na Waziri wa Katiba na Sheria wa Zanzibar, Aboubakar Khamis Bakary, mjini hapa.

“Nadhani Sheria ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba inakataza mtu au taasisi kumzuia mtu mwingine kutoa maoni yake au kumlazimisha aseme anavyotaka yeye, sasa hawa viongozi wa CCM wanaotaka kuwanyang’anya kadi wawakilishi wao wanakiuka sheria hii,” alisema Waziri Seif.

Alisema ataendelea kuishangaa Tume ikiwa itaendelea kushindwa kukemea au kuwachukulia hatua wale wote wanaotoa vitisho dhidi ya watu wenye mitazamo tofauti na ya CCM katika Katiba mpya.

Seif alisema kila mtu yuko huru kutoa maoni yake mbele ya tume hiyo na kwamba si haki kwa mtu au chama chochote cha siasa kuwakataza wanachama wake kutoa maoni yanayogusa mitazamo yao binafsi tofauti na ya vyama vyao.

Makamu Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT) Zanzibar, Asha Bakar Makame, aliwataka viongozi wenzake ndani ya CCM kutowatisha wanachama wenye maoni tofauti na chama hicho katika suala la mabadiliko ya Katiba.

Asha alisema ni jambo la kushangaza katika ukuaji wa demokrasia wanapojitokeza watu kuwazuia wengine kuwa na mawazo huru kwenye mchakato wa kupata Katiba mpya. "Jamani tusitishane, kama CCM kila mtu ni CCM hapa hakuna mtu asiyenijua msimamo wangu kuhusu Chama, ninakipenda na nitakitetea, lakini si vizuri kuanza kutishana kwa kuambiana huyu hivi huyu vile, haifai jamani,” alisema.

Asha alikumbusha kwamba wakati wa kutafuta maridhiano ya kisiasa Zanzibar, wapo wana-CCM na viongozi waliopinga suala hilo, lakini hakuna mtu aliyeadhibiwa kwa kuvuliwa uanachama na kuwataka viongozi kuwavumilia wanachama na wafuasi wengine wa CCM katika suala zima la maoni tofauti kuhusu Muungano.

Mwakilishi wa Kwamtipura, Hamza Hassan Juma, alisema Rais Kikwete, hajazuia kutoa maoni tofauti na msimamo wa CCM juu ya suala hilo na kuwataka viongozi wengine kuiga mfano huo na kuwa wavumilivu.

Hamza aliongeza kwamba CCM bado ni bora, hivyo kisiogope mageuzi kama ilivyotokea wakati wa mageuzi kutoka demokrasia ya chama kimoja kuingia mfumo wa vyama vingi vya siasa mwaka 1992.
 
Back
Top Bottom