Tujikumbushe:Na Saed Kubenea

WENYELE

JF-Expert Member
Apr 2, 2012
1,415
1,379
MBUNGE WA UBUNGO SAED KUBENEA ALIVYOELEZA UNAFIKI NA UFISADI WA LOWASSA KATIKA KAMPUNI HEWA YA RICHMOND.

Lowassa anajua uzalendo au ni machozi ya mamba?


Na Saed Kubenea - Imechapwa 18 January 2012

Printer-friendly version
Gumzo la Wiki
EDWARD Lowassa, yule aliyejiuzulu nafasi ya waziri mkuu kutokana na kashifa ya kuingiza nchi kwenye mkataba wa kinyonyaji wa makampuni ya Richmond/Dowans, sasa anasaka utakaso.

Katika kasi yake, anakemea hata asiostahili kukemea na anasema yale ambayo wengi wanajenga shaka kama anaweza kuyasimamia.

Akiwa mkoani Kigoma, kwenye harambee ya ujenzi wa Sekondari ya Kanisa la FPCT Bigabiro, Lowassa amenukuliwa akisema, “Nguvu ya umma inayotumiwa na baadhi ya vyama vya siasa kushinikiza serikali kutekeleza mambo mbalimbali, haiwezi kuleta maendeleo wala tija kwa taifa.”

Mbunge huyo wa Monduli, alifika mbali zaidi. Alidai kuwa hivi sasa wananchi wengi hawataki kujitolea kwa sababu “wamepoteza uzalendo.” Alisema kila wanachokifanya, ikiwamo kutekeleza miradi ya maendeleo kwenye maeneo yao, wanataka kulipwa fedha.”

Jumla ya Sh. 125 milioni zikiwamo ahadi, zilichangwa kwenye harambee hiyo, huku taarifa zikisema Lowassa na wale aliowaita “marafiki zake,” walitoa Sh. 60.5 milioni.

Lowassa hakutaja jina la chama cha siasa ambacho ametaka kiachane na matumizi ya nguvu ya umma yanayolenga kushinikiza serikali kutekeleza matakwa ya wananchi. Wala hakutaja chama ambacho amekitaka kitumie nguvu ya umma kushinikiza wananchi kufanya kazi za kujitolea.

Bali kila mmoja anajua kuwa Lowassa amelenga Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA). Hiki ndicho kinajitambulisha kwa kauli mbiu ya nguvu ya umma – “People’s Power.”

Je, Lowassa anaamini anachokisema? Anastahili kueneza anachokihubiri? Kama haamini anachokisema na anahubiri asichostahili kuhubiri, nini kimemsukuma kueleza haya sasa?

Kwanza, Lowassa haamini kwenye kujitolea “nguvu kazi.” Ndiyo maana kila anakopita, hakuna ambako aliweka nguvu kazi yake. Hakuna alikotoa jasho lake. Bali kote alikopita, kuanzia mkoani Singida, Mwanza, Arusha, Dar es Salaam, Pwani, Kilimanjaro na Kigoma, Lowassa amemwaga fedha, badala ya kujitolea nguvu kazi.

Pili,Lowassa anajua sababu za wananchi kupoteza uzalendo na kutaka kulipwa ujira kwa kazi wanayoifanya. Ni kwa sababu, wamechoshwa na vitendo vya viongozi wao waliowapa dhamana.

Kwa mfano, baraza la mawaziri liliagiza mkataba kati ya serikali na makampuni ya Richmond/Dowans uwe wa mwaka mmoja. Lakini baadhi ya viongozi, Lowassa akiwa miongoni mwao, walibadilisha maelekezo ya baraza la mawaziri na kuliamuru Shirika la Umeme la Taifa (TANESCO), kujifunga kwenye mkataba wa miaka miwili.

Aidha, kwa kisingizio cha nchi kutaka kuingia gizani, Lowassa aliamuru kubadilishwa kwa vigezo vya utoaji wa zabuni kutoka 24 vilivyowekwa awali hadi vinne ili kuweza kuibeba Richmond.

Pale alipoona Richmond imeshindwa kukidhi hata kigezo kimoja kutoka miongoni mwa vigezo vinne vipya vilivyowekwa, kikiwamo kile kinachoweka sharti la kampuni kuwa na uzoefu wa angalau mwaka mmoja katika miradi ya umme, aliamuru kazi ya kutafuta mzabuni ifanywe na kamati ya serikali, badala ya Bodi ya Tenda ya TANESCO.

Mbali na hayo, Lowassa anafahamu thamani halisi ya mitambo ya Richmond/Dowans; si zaidi ya dola za Marekani 40 milioni. Lakini kwa makusudi alikubali serikali kujifunga kwenye mkataba unaowalazimisha kuilipa kampuni hiyo, kwa kila siku, kama malipo ya kuweka mitambo – Capacity Charge – dola za Marekani 100,000; karibu Sh. 152 milioni.

Kiasi hiki ni nje ya fedha zinazotumika kununulia umeme; zitakazolipia matengenezo ya mashine na zitakazotumiwa kugharamia usafirishaji mafundi kutoka nje ya nchi.

Katika kipindi cha miezi 21 ya uhai wa mkataba, tayari Richmond/Dowans walishavuna kutoka serikalini, zaidi ya dola za Marekani 66.4 milioni (karibu Sh. 90 bilioni). Kiasi hiki cha fedha, ni mara mbili ya bei halisi ya mitambo.

Baadaye wanaojiita wamiliki wa Dowans wakaenda mahakamani kudai serikali kwa kisingizio cha kuvunjwa kwa mkataba wake wa miezi 24. Mahakama bila kuhoji uhalali wa fedha inayodaiwa; bila kuhoji sababu za Richmond/Dowans kutaka kulipwa mkataba wote, wakati uhai wa mkataba ulibaki miezi mitatu, ikaamuru TANESCO kulipa kiasi cha Sh. 90 bilioni.

Mahakama ikaweka hata sharti jingine la serikali kulipa riba ya karibu asilimia 30 kwenye viwango vya dola. Sasa deni linaendelea kukua siku hadi siku hadi kufikia Sh. 120 bilioni.

Ukichua kiasi ambacho mahakama imeamuru kilipwe kwa Dowans, ukakichanganya na fedha ambayo tayari serikali imelipa katika kipindi cha miezi 21 ya uhai wa mkataba, utapata jibu moja: Mashine zenye thamani ya dola za Marekani 40 bilioni, tayari zimevuna ama zinatarajiwa kuvuna dola za Marekani 258 milioni (Sh. 397 bilioni) ndani ya muda mfupi wa miaka mitano.

Kama hiyo haitoshi, serikali ikakubali kujifunga kwenye mkataba mwingine wa milele na milele na kampuni ileile iliyojibadili jina tu na kujiita Symbon Power LLC, lakini ikiwa inatumia mitambo ileile ambayo italipwa Sh. 365 bilioni.

Hadi hapa, nani anaweza kuitikia wito wa Lowassa wa “kujitolea?” Nani anaweza kumsikiliza? Kama kujitolea, mbona ni yeye aliyekuwa anatakiwa kufanya hivyo kwenye kipindi cha kusaini mkataba na kutafuta mzabuni?

Lowassa ameshindwa nini, wakati alikuwa analipwa na serikali; analishwa na serikali na anavishwa na serikali? Hata sabuni ya kufulia mto wa kitandani kwake, shuka la kujifunika, sabuni na makochi anayotumia, vyote vinalipiwa kwa fedha za wananchi?

Yule aliyeshitaki serikali; aliyelipwa mabilioni ya shilingi na serikali kwa mashine zenye thamani ya Sh. 60 bilioni; na ambaye sasa anashinikiza kulipwa mabilioni mengine, ni mmoja wa maswahiba wakuu wa Lowassa na mshirika wake mkubwa kisiasa, Rais Jakaya Kikwete.

Rostam Aziz, mwanachama mashuhuri na muhimu ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), ndiye aliyeshitaki, aliyeajiri mawakili, ndiye alidai na ndiye anayepokea na atakayepokea malipo yoyote ya fedha kwa niaba ya makampuni ya Dowans Holding SA, Dowans Tanzania Limited (DTL) na Richmond Development Company (LLC).

Lakini kuna hili pia. Lowassa anafahamu jinsi katibu wa TANESCO, Subira Wandiba, alivyojitolea kwa taifa lake. Alieleza kwa ufasaha ubatili wa hatua ya Richmond ya kuhamisha mkataba.

Wandiba alikuwa akiandikia mwenyekiti wa bodi ya TANESCO, Balozi Fulgence Kazaura, tarehe 28 Novemba 2006, kwamba “…kufuatana na mkataba wa 23 Juni 2006, Richmond hairuhusiwi kuhamisha mkataba wao kwenda kampuni nyingine yeyote.” Hii ilikuwa kabla ya mkataba kumilikishwa kwa Dowans.

Lakini nani alimsikiliza Wandiba? Nani alisikiliza ushauri wake, kwamba Richmond – kampuni iliyopewa mkataba kwa upendeleo, ikiwa haina fedha, haina utaalam wala historia ya kufua umeme – haikupaswa kuhamisha mkataba wake kama ilivyofanya tarehe 23 Desemba 2006. Ilikuwa kinyume cha sheria za nchi.

Akiwa nchini Canada, Nazir Karamagi aliyekuwa waziri wa nishati na madini, aliamuru Richmond kuruhusiwa kuhamisha mkataba wao. Leo hii, Wandiba ameondolewa kwenye nafasi yake hiyo. Je, uzalendo ambao Lowassa anasema uko wapi, ikiwa wale ambao wameonyesha uzalendo ndio wanasakamwa na hata kuondolewa kazini?

Nani anaweza kuwa mzalendo, wakati wale ambao wamesababisha haya, wanaendelea kupeta? Wanalipwa na serikali. Wanahudumiwa na serikali. Wanatumia magari ya serikali; wanakaa nyumba za serikali na wanatibiwa nje ya nchi kwa gharama za walipa kodi wa hapa?

Nani ataweza kuwa na moyo wa kujitolea, wakati Lowassa mwenyewe anaendelea kulipwa mafao ya waziri mkuu mstaafu, wakati ukweli ni kuwa hakustaafu?

Nani anaweza kujitolea nguvu kazi yake wakati anaona rasilimali za taifa zinatumika kugharamia watu walioshindwa kazi; waliongiza nchi kwenye mikataba yenye utata na wanaoendelea kulipwa, wao na wasaidizi wao, kwa fedha za walalahoi?

Nani ataweza kutumia nguvu kazi yake kufanya kazi ya maendeleo, wakati nguvu walizotumia kufanya kazi zao binafsi na kulipa kodi kubwa isiyo na kipimo, inatumiwa na wale waliosaidia kufikisha taifa hapa lilipo?

Nani atakubali kumwaga jasho lake kufanya kazi za kujitolea, wakati wanaona kiongozi wao – Waziri Mkuu Mizengo Pinda – anayelipiwa kila kitu na serikali akisaini posho ya Sh.250,000 kwenye semina ya Bunge?

Ilitegemewa badala ya Lowassa kuwaalani na kuwadhihaki wanaoshinikiza wananchi kupinga udhalimu huu; wanaotaka serikali kuwajibika kwa wananchi wake; wanaotaka kupunguzwa kwa ugumu wa maisha; angesimama pamoja nao – hata kama yeye si miongoni mwa wanaojua bei ya sukari, mafuta, chuvi, umeme na kibiriti – kuhimiza serikali kutekeleza wajibu wake.

Angalau angefanya hivyo, angeweza kusamehewa kwa dhambi hii aliyosababishia taifa hili. Lakini kwa hatua yake ya kusema wananchi – wenye njaa, wanaopunjwa bei ya mazao yao, wanaolazimishwa kutoa rushwa kwa kila huduma wanayostahili – wamepoteza uzalendo; basi amefanya dhihaka ambayo inahitaji toba.

Wananchi waandamanaji ambao Lowassa anawalaani wanataka kuona taifa lao linatokomeza ufisadi; linakuwa taifa huru kwa watu huru. Wanaoandamana wanataka kuona heshima, utu wao na mali za taifa vikirejeshwa.

Wanaoandamana wanataka kuona misingi ya haki inatolewa kwa raia wote, bila kujali kipato cha mtu, umaarufu wa mtu au nasaba yake. Wananchi wanaoandamana wanataka kuona utawala wa matabaka nchini unatokomezwa. Hakuna tena mabwana na watwana.

Wanataka kuona tofauti kubwa ya kipato kati ya masikini na matajiri inaondoka. Huduna zinapatikana katika hospitali za umma. Karo kwenye shule za msingi, sekondari na vyuo, zinalipwa na serikali, tena bila ubaguzi.

Wananchi wanataka kuona wote walioiba au walioshiriki wizi, ukwapuzi na ufisadi wa aina yoyote ile lakini bado wamejificha nyuma ya siasa au wanalindwa na watawala, wamekamatwa na kufikishwa mahakamani.

Wanataka kuona walioshiriki kuuza nchi kwa njia ya kunadi raslimali za taifa kwa bei ya karanga, wakichukuliwa hatua na jeuri yao inakoma mbele ya nguvu ya umma.

Wanaotetea nguvu ya umma wanataka kuona walioingiza taifa hili katika mikataba ya kinyonyaji wanaswekwa mahakamani na wanazuiwa hata kugombea uongozi wa ngazi yoyote.

Kuchukuliwa kwa hatua hizi ndiko pekee kunakoweza kurejesha uzalendo; chini ya watawala wapya ambao mikono yao haihusiki hata kidogo na ukamuaji jasho na damu ya wananchi.

Moyo wa utaifa – uzalendo – utarejea chini ya watawala wapya ambao wanathamini nguvu kazi ya umma; wale ambao hawahusiki hata kidogo na wala hawajawahi
kushiriki ufisadi na ukamuaji jasho na damu ya wananchi.

Copy and paste from Mwanahalisi online.
 
Kubenea mchumia tumbo, haoni haya kutapika halafu kuyazoa matapishi ni kurudisha kichwani ha ha haaaaaaa
 
Back
Top Bottom