Tujadili vifungu vibovu vya katiba

fige

JF-Expert Member
Jul 4, 2010
376
61
Kwa hakika hakuna mtanzania anayeilewa na kusoma katiba iliyopo na mwenye mapenzi mema na Nji hii anayepinga KATIBA MPYA.
Kwa busara na hekima ya wanaoisoma Katiba yetu naomba tuainishe mapungufu yake ikiwezekana kuanzia na utangulizi unaosema sisi wananchi wa JMT wakati ukweli ni kwamba sio sisi ila ni viongozi ndio walioiandaa na si wananchi wote walioiandaa katiba ilyopo wala hawakutoa ridhaa yao.

Ni vema tuka ainisha vipengele hivyo ili watu wajue kinachodaiwa .Natoa wito kwa waandishi wa makala mbalimbali magazetini na mada mbalimbali kwenye runinga au redioni zijikite katika kujadili vifungu hivyo kuliko ku site moja kwa moja katika kudai katiba mpya bila kutaja mapungufu ya katiba iliyopo.

kufanya hivyo kutafanya hata wale wanaopinga mabadiliko hayo kuchangia au kuona aibu kuendelea kupinga.Vilevile itatusaidia tulio wengi kuijua katiba ya nchi yetu vizuri.

Nawasilisha wakuu.
 
hapo mmenena mkuu maana wengine wanafikiri huu ni ushabiki tu,mfano kile kipengele kinachosema kuwa matokeo ya urais hayawezi kupingwa kwenye mahakama yoyote,wananchi hawalijui hili wanahoji kama Dr. Slaa alionewa kwa nini asiende mahakamani.ukimwambia mwananchi wa kawaida kwamba tatizo ni katiba inabidi umfafanulie kivipi. mkuu kweli magazeti na vyombo vingine vya habari badala ya kujadili mambo yasiyokuwa na tija wafanye mijadala ya namna hii.katiba si swala la kisiasa tu bali linaathiri nyanja zote za kiuchumi na kijamii hivyo lipewe kipao mbele.
 
Nashukuru kwa kuunga hoja mkono Mkuu.
Ukweli kuna vipengele vingi vya katika vinatia kichefuchefu.
Mfano mwingine wa HII INAYOITWA TZ BARA zamani ikiitwa Tanganyika kutokuwa na kiongozi pale Raisi anapochaguliwa toka visiwani.
Soma katiba 34(i)
Inasema,
Kutakuwa na serikali ya JMT ambayo itakuwa na mamlaka juu mambo yote ya muungano ktk JMT na pia juu ya mambo mengine yahusiyo Tz bara.
 
nikiwa mdau wa somo la URAIA/CIVICS....hapa naona ni wakati muafaka kutoa yangu moyoni......nawashukuru viongozi waliopita kwa kuibadili katiba iliyopo kwani bila wao tusingekuwa na katiba hii tuliyonayo.....! angalizo: NI VYEMA KILA ATAKAYE KUCHANGIA AWE ANAIJUA NA PIA AWE AMEISOMA KATIBA ILI KUEPUSHA MIZOZO WENGI WANAOPIGA KELELE HATA KATIBA YENYEWE HAWAJAWAHI KUIONA SEMBUSE KUISOMA...NA WENGI WAO HAWAJUI HISTORIA YA KATIBA ILIYOPO KWANI HUDANGANYWA KUWA HAIJAWAHI KUBADILISHWA WAKATI NI UONGO WA WANASIASA KUJITAFUTIA UMAARUFU TOKA KWA LAYMEN
 
Fige, umenena vyema.

Sifurahi kabisa ninapoona kila mtu anaimba wimbo wa Katiba Mpya'' bila kutaja katika huo upya tunataka kubadilisha nini!

Watu wengi hawaijui Katiba ya sasa. Unaweza kukuta hata Mawaziri wetu hawajawahii hata kuiona/juisoma. Ya nini sasa wakati mwanasheria mkuu yupo au wizara ina mwanasheria??:teeth:

Vifungu vibovu vikishaainishwa (vyoooote kama inawezekana), tutaweza sasa kujadili na kuamua kama ni muhumu kuandika katiba mpya au ni sawasawa tu kuvirekebisha hivyo kwenye katiba ya sasa.

Kwa kuwa Kenya wameweza kuandika katiba yao mpya, sasa tunachachawa na tunataka kucopy na kupaste huku!
 
Kwa hakika hakuna mtanzania anayeilewa na kusoma katiba iliyopo na mwenye mapenzi mema na Nji hii anayepinga KATIBA MPYA.
Kwa busara na hekima ya wanaoisoma Katiba yetu naomba tuainishe mapungufu yake ikiwezekana kuanzia na utangulizi unaosema sisi wananchi wa JMT wakati ukweli ni kwamba sio sisi ila ni viongozi ndio walioiandaa na si wananchi wote walioiandaa katiba ilyopo wala hawakutoa ridhaa yao.

Ni vema tuka ainisha vipengele hivyo ili watu wajue kinachodaiwa .Natoa wito kwa waandishi wa makala mbalimbali magazetini na mada mbalimbali kwenye runinga au redioni zijikite katika kujadili vifungu hivyo kuliko ku site moja kwa moja katika kudai katiba mpya bila kutaja mapungufu ya katiba iliyopo.

kufanya hivyo kutafanya hata wale wanaopinga mabadiliko hayo kuchangia au kuona aibu kuendelea kupinga.Vilevile itatusaidia tulio wengi kuijua katiba ya nchi yetu vizuri.

Nawasilisha wakuu.
Ungefanya uungwana kwa kuiweka na hapa kwenye bandiko lako ili watu wajadili wakiisoma.
 
Joseph Mihangwa, Disemba 8, 2010
KAMA kuna waziri katika Baraza jipya la Mawaziri la Rais Jakaya Mrisho Kikwete, aliyeanza kazi kwa mikwara na mikakati iliyoshindwa kabla ya kuanza, waziri huyo ni Celina Kombani anayeongoza Wizara ya Sheria na Katiba.

Tamko la waziri huyo, hivi karibuni, kwamba suala la Katiba mpya nchini halizungumziki; kwa sababu ni la gharama kubwa, ni ishara kwamba waziri huyo anapiga jaramba kupigana na wakati asijue kwamba "wakati ukuta".

Kama ningekuwa mkufunzi msimamizi wake wa tasnifu [thesis] juu ya wizara yake, tayari ningemkata alama kabla ya kuisoma ili ashindwe mtihani hima.

Kombani anashindwaje kusoma maandishi ukutani na matukio nchini Kenya yaliyozaa Katiba mpya? Na aukubali usemi wa wahenga kwamba "ukiona mwenzio akinyolewa, wewe tia maji".

Suala la Katiba mpya haliepukiki nchini kwa mazingira ya sasa, na kujaribu kulizuia ni sawa na mtu kujaribu kutemea mate anga. Na kwa kufanya hivyo, hawezi kukwepa kujichafua uso wake mwenyewe. Au anajaribu kuzuia mafuriko ya mto kwa viganja vya mikono?

Historia ya nchi yetu inaonyesha kwamba, mabadiliko ya Katiba hayakwepeki kila panapotokea mabadiliko makubwa ya kiuchumi na kijamii; na hivyo kwamba, yanayoendelea nchini sasa yatashinikiza Katiba mpya. Kwa nini?

Katiba ya nchi ni ramani ya madaraka na ni kielelezo cha demokrasia nchini kwa sababu ni tunda la uamuzi wa dhati wa wananchi wenyewe. Kudumu kwa Katiba bila marekebisho ya mara kwa mara ni ishara ya Katiba makini; kinyume chake ni Katiba isiyozingatia matakwa ya wananchi na mabadiliko ya nyakati.

Katiba kama ile ya Marekani ambako ndiko tumeazima mfumo wa demokrasia wa sasa, imerekebishwa si zaidi ya mara nne katika kipindi cha miaka 222 tangu ianze kutumika rasmi mwaka 1788, tofauti na Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano ambayo katika kipindi cha miaka 13 pekee imefanyiwa marekebisho 14, sawa na wastani wa rekebisho moja kila mwaka!

Dhumuni kuu la kurekebisha Katiba ya nchi ni kutaka kukidhi matakwa ya jamii inayobadilika kwa lengo la kutekeleza demokrasia, haki ya kijamii utawala wa sheria na maendeleo ya nchi. Misingi yote ya Katiba huongozwa na uzalendo na si kwa mizengwe ya siasa za vyama vya siasa kwani Katiba ya nchi iko juu ya vyama vya siasa.

Katiba inayozingatia malengo haya ina uwezo mkubwa wa kuhimili mitafaruku nchini inayoambatana na mabadiliko ya jamii ya mara kwa mara na kudumu kwa muda mrefu kuliko inayokiuka malengo haya, na hivyo kusababisha mabadiliko au marekebisho ya mara kwa mara. Katiba yetu iko katika Katiba za kundi la pili. Nitaelezea kwa nini tumefikia hapo.

Tangu tupate Uhuru Desemba 9, 1961 hadi sasa, Tanzania imepata kuwa na Katiba mpya tano ambazo katika uhai wake zimeweza kufanyiwa marekebisho mara kwa mara kwa kuzingatia mazingira ya kisiasa, kijamii na kiuchumi ya nchi.

Kila Katiba mpya, na kila rekebisho au marekebisho ya Katiba yalitanguliwa na mitafaruku au migongano ya kijamii na kiuchumi iliyotishia mustakabali wa Taifa na uhusiano wa kimataifa.

Katiba ya kwanza iliyojulikana kama "Katiba ya Uhuru" [The Independence Constitution] ya mwaka 1961, ilitungwa na kutumika katika mazingira yaliyoashiria kumalizika kwa ukoloni mkongwe nchini Tanganyika.

Ilifuatiwa na Katiba ya Jamhuri [The Republican Constitution] ya mwaka 1962 iliyoashiria Watanganyika kuchukua madaraka ya nchi kutoka kwa wakoloni.

Nitafafanua kidogo. Katiba ya Uhuru ndiyo iliyotoa uhuru na ramani ya madaraka kwa Tanganyika huru bila madaraka kamili ya ndani kwa sababu nchi ilikuwa bado inasimamiwa na Uingereza kupitia mteule wake - Gavana wa Tanganyika.

Na kusema kweli, Katiba hiyo haikuwa tunda la Watanganyika; bali ilitungwa na kutolewa kwenye Ofisi ya Makoloni nchini Uingereza na kushushwa kwetu kama "Torati" yenye ukakasi bila kutoa uhuru kamili.

Kwa hiyo ilizua nguvu ya hoja kwamba uhuru kwa Watanganyika bila kuwa na Serikali yenye madaraka ya ndani [Jamhuri] lilikuwa debe tupu, na huo ukawa msingi wa kudai Serikali hiyo na Katiba mpya; madai ambayo ndiyo yaliyozaa Jamhuri.

Kwa bahati mbaya, Katiba zote mbili za kwanza – Katiba ya Uhuru na Katiba ya Jamhuri, tofauti na Katiba za nchi zingine zilizokuwa zilizokuwa makoloni ya Uingereza, hazikuwa na tamko kuhusu Haki za Binadamu.

Huo ndio ulikuwa mwanzo wa mfumo wa utawala wa rais dikteta, mwenye imla [imperial presidency], asiyeambilika au kushaurika; kwani chini ya kifungu cha 3 (3) cha Katiba hiyo, Rais alipewa mamlaka na uwezo wa kuongoza nchi atakavyo kwa vile hakulazimika kusikiliza au kupokea ushauri kutoka kwa mtu yeyote kuhusu masuala ya uongozi wa nchi.

Hali hiyo haijabadilika hadi sasa kama inavyobainishwa kwa maneno yale yale katika ibara ya 37 (1) ya Katiba yetu ya 1977 inayoendelea kutumika.

Kama kweli tunataka demokrasia ionekane kufanya kazi, tunapendekeza Rais atende kazi kwa ushauri wa Baraza la Mawaziri, na Bunge la nchi [sauti ya watu] lipewe mamlaka zaidi ya kutoa maelekezo kwa Rais bila hofu ya kuvunjwa na yeye kwa mamlaka aliyo nayo chini ya ibara ya 97 (4) ya Katiba ya sasa.

Katiba ya tatu [nayo ilikuwa ya muda] ya Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ya 1964, ilianzishwa kwa kusudi la kukidhi matakwa ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, pale nchi mbili hizo zilipoungana, Aprili 26, 1964.

Katiba hii ilikuwa ni maboresho tu ya Katiba ya Jamhuri ya Tanganyika ya 1962 kupitia Agizo la Rais [Presidential Decree] na kuitwa "Katiba ya Muda ya Jamhuri ya Muungano", wakati huo Jamhuri ya Muungano ikijiandaa kupata Katiba yake kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa na Mkataba wa Muungano pamoja na Sheria ya Muungano.

Katiba ya Nne iliitwa "Katiba ya Muda ya Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar" ya mwaka 1965 ambayo, kwa kutumia Kikao cha kawaida cha Bunge la kawaida [badala ya Bunge la Katiba kama ilivyotakiwa], ilipitishwa na kuanzisha Utawala wa Chama kimoja cha siasa badala ya vyama vingi, tofauti na ilivyokuwa kwa Katiba zilizotangulia.

Na chini ya marekebisho ya Katiba hiyo yaliyofanywa mwaka 1975, Chama cha Tanganyika African National Union [TANU], kilitangazwa "kushika hatamu" za uongozi wa nchi, ambapo vyombo vyote vya Serikali vilifanywa kuwajibika kwa Chama.

Katiba ya kudumu iliyofuata mwaka 1977 ilipitishwa mahsusi kukidhi matakwa ya vyama viwili vilivyoungana – TANU cha Tanzania Bara na Afro Shirazi Party [ASP] cha Tanzania Zanzibar, na kuimarisha zaidi "utukufu" wa Chama kipya kilichoshika hatamu za utawala wa nchi - "Chama cha Mapinduzi" [CCM] kilichozaliwa kwa ndoa ya TANU na ASP.

Katiba hii ilikamilisha zoezi la kuhodhi siasa za nchi kwa njia ya Chama kimoja ambapo jukumu la kufikiri, kutoa hoja na mawazo ya kimaendeleo liliondolewa kwa wananchi na kuwekwa mikononi mwa Chama pekee.

Yeyote aliyehoji juu ya mwenendo wa Serikali [mwanachama au si mwanachama wa CCM] aliitwa mpinga maendeleo, mpinzani wa Chama na hivyo mpinzani wa Serikali. Sheria kandamizi, ikiwamo Sheria ya Usalama wa Taifa na Mamlaka ya Rais ya kumtia mtu kizuizini, zilitumika kunyamazisha wananchi wenye hoja na maoni.

Katiba ya Kudumu ya 1977 ilianzishwa na kusimama kwenye mihimili [mafiga] mikuu mitatu: Kwanza, Rais mwenye imla, asiyeambilika au kushaurika kama sehemu ya masalia ya Katiba ya 1962. Pili, Serikali mbili – Tanganyika na Zanzibar; na tatu, Utawala wa Chama kimoja na siasa ya Ujamaa na Kujitegemea.

Katiba hii, kama ilivyokuwa Katiba ya Uhuru, si matunda ya mjadala wala maoni ya wananchi. Ni Katiba iliyopendekezwa na Tume ya Chama iliyoteuliwa kuandaa rasimu ya kuunganishwa kwa vyama vya TANU na ASP, badala ya kupendekezwa Tume ya Katiba iliyotajwa katika ibara ya 7 ya Hati ya Muungano, na kifungu cha 9 cha Sheria zote mbili za Muungano, za Tanganyika na Zanzibar.

Je, Katiba ya aina hii inakidhi matakwa na mazingira ya nchi ya sasa? Je, inakidhi matakwa ya Muungano yaliyokusudiwa?


Hatuna cha kutumaini kutokana na ukweli kwamba baadhi ya mihimili iliposimamia Katiba hii imekwishavunjika. Ukiondoa mhimili pekee wa Rais asiyeambilika uliosalia katika Katiba ya 1977 [angalia ibara ya 37, 46 na 63 ya Katiba], mihimili mingine miwili imevunjika: Itikadi ya Ujamaa na Kujitegemea imeuawa na Azimio la Zanzibar la 1992, na nafasi ya mfumo wa Utawala wa Chama kimoja imenyakuliwa na mfumo wa vyama vingi vya siasa tangu 1992.

Aidha, mfumo wa vyama vingi vya siasa na uchumi huria havikuwa katika mawazo ya Katiba ya 1977 wakati ikitungwa, na kwa sababu hiyo haujapewa nafasi inayostahili kwa tafsiri sahihi ya mfumo huo.

Kwa hiyo, nchi sasa inaendeshwa kwa kauli mbiu ya "Chama Dola" kana kwamba wananchi wengine wasio na vyama au wale wa vyama vingine ni ‘raia daraja la pili' katika nchi yao wenyewe.

Kuna tofauti kubwa kati yetu na nchi zenye demokrasia iliyokomaa. Kwa mfano katika Marekani na Afrika Kusini, rais anaweza kumteua mtu yeyote bila kujali tofauti za itikadi za siasa kushiriki katika uongozi wa nchi au katika kusimamia maslahi ya nchi. Kwa wenzetu; ni nchi kwanza, vyama vya siasa baadaye tofauti na sisi ambapo ni "Chama kwanza, maslahi ya nchi baadaye".

Nao utekelezaji wa mfumo na muundo wa Muungano uliokuwa ukifanyika kwa nguvu za Chama zaidi kuliko kutumia misingi ya sheria zilizoanzisha Muungano huo, sasa unahojika kuliko hapo zamani; na kwamba kuna kila hali kuonyesha kwamba busara inahitajika ili utekelezaji huo utazamwe upya kuondoa kero kwa manufaa ya nchi.

Vivyo hivyo kujaribu kujenga demokrasia na utawala bora nchini kwa kutumia Katiba ya sasa, ni sawa na mbio za mbilikimo katika kuisaka demokrasia. Ni mbio zisizoweza kuhimili wala kufua dafu kwa hatua ndefu za mabadiliko makubwa yanayotokea katika nyanja zote za maisha ya jamii.

Kwa hiyo; bila kuzingatia mambo haya ya kihistoria, mabadiliko yoyote ya Katiba [kwa njia ya kuweka viraka] hayatakidhi matakwa ya demokrasia, na Katiba yetu itaendelea kuwa adha kubwa kwa wananchi.

Tunapashwa kurefuka kimawazo, akili na kwa vitendo ili tusiachwe nyuma na ulimwengu wa kidemokrasia kwa maendeleo ya watu wetu. Tusikubali kubakia "mbilikimo" wakati dunia inapiga hatua ndefu katika uwanja wa demokrasia; tutasahaulika na kubaki nchi yenye udikteta unaopitwa na wakati haraka.
Itaendelea

SOURCE: Raia Mwema

Simu: 0713-526 972
Barua-pepe: jmihangwa@yahoo.com
 
Kwa idhini ya JM, naomba kuweka nukuu hiyo hapo.

Ni waraka mzuri wa kuanzia na kuendelea mbele ktk kujifunza juu ya mabadiliko ya katiba yanayohitajika Tz.
Elimu haina mwisho, nafurahi tuna wataalam wa fani mbalimbali JM.

Hivyo endeleea kutega sikio na kuwa na hali ya uwazi (open-mindedness) katika kujifunza, kutafakari na kuamua.
 
Katiba mpya must waache udikiteta tutatengeneza rasimu inayoonesha mapungufu ya katiba ya sasa
 
Ukisoma http://sw.radiovaticana.va/doc/RASIMU_final.pdf haizungumzii kabisa kuhusu wananchi kuelimishwa na kutengenezewa utaratibu wa kulipia michango ya bima ya afya na pensheni ya uzeeni ili huduma hii isiishie kwa waajiriwa tu bali hata wakulima na wafugaji wajiwekee akiba ili tuondokane na msemo wa fainali uzeeni. Kwa maoni yangu kila mtanzania anayejishughulisha na kazi yoyote atengenezewe kautaratibu ka hiari ka kuchangia akiba yake ya uzeeni. Kwa upande vifungu ambavyo vina walakini ni vile vinavyozungumzia namna ya kuboresha uchumi wa Tanzania. Ili tuweze kutoka katika lindi hili la umasikini ni lazima tujitengenezee utaratibu wa namna ya kujitegemea wenyewe. Tusitegemee London au Washington. Vifungu vya uchumi, rushwa, raslimali za taifa navyo havijakaa vizuri.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom