Che Guevara
JF-Expert Member
- May 22, 2009
- 1,236
- 346
BoT yatumia Sh1bilioni kukarabati nyumba ya Gavana Ndulu
Na James Magai
WAKATI tuhuma za matumizi mabaya ya Sh1.4 bilioni kwa ajili ya ukarabati wa nyumba za Tanesco zikiendelea kuchunguzwa, Benki Kuu (BoT) inadaiwa kutumia Sh1 bilioni kukarabati nyumba moja ya gavana wake, Profesa Benno Ndulu, Mwananchi imeelezwa.
Habari zilizolifikia gazeti hili jana zimeeleza kuwa taasisi hiyo ya fedha imetumia kiasi hicho kukarabati nyumba ya gavana katika mradi wa ukarabati wa nyumba za vigogo wake wanne ambao ni gavana na manaibu wake watatu.
Kwa mujibu wa habari hizo, nyumba iliyokarabatiwa kwa fedha hizo iko Oysterbay eneo la Morogoro Stores, jirani na nyumbani kwa katibu mkuu wa mstaafu wa CCM, Philip Mang'ula jijini Dar es Salaam.
Uchunguzi wa gazeti hili umebaini pia kwamba kigogo anayestahili kuishi kwenye nyumba hiyo (gavana), tayari amehamia na kuishi humo tangu Desemba Mosi mwaka huu.
Hata hivyo, habari zaidi za kiuchunguzi zinabainisha kuwa ukarabati wa nyumba hiyo umetumia gharama mara mbili zaidi ya bei ya kununulia nyumba hiyo. Nyumba hiyo ilinunuliwa kwa dola 400,000 za Kimarekani ambazo ni sawa na takriban Sh500 milioni.
Mbali na nyumba hiyo, nyumba nyingine zinazodaiwa kutafuna fedha za walipa kodi katika ukarabati wake ni ya naibu gavana wa kwanza, Juma Reli iliyo Masaki, Mtaa wa Chole. Nyumba hiyo ilikuwa ikitumiwa na gavana wa zamani, Dk Daud Balali.
Habari zaidi zinadai kuwa Reli alihamia kwenye nyumba hiyo baada ya Gavana Ndulu kuikataa kwa madai kuwa haina bwawa la kuogelea (swimming-pool).
Nyumba nyingine iliyo kwenye tuhuma hizo za kashfa ya ufujaji mamilioni ya walipa kodi ni ile inayotumiwa na naibu gavana wa pili (Bukuku), iliyo Oysterbay pamoja na ya naibu gavana wa tatu (Makila) iliyo Masaki.
Afisa uhusiano wa BoT, Emmanuel Mwero, alipotafutwa na Mwananchi kutoa ufafanuzi wa tuhuma hizo jana, hakutaka kujibu moja kwa moja na badala yake aliweka urasimu wa kutaka maswali yaandikwe kwenye karatasi iliyo na nembo ya gazeti hili ndpo aandae majibu.
"Ahh, kwa hilo, wewe lete maswali yako kwenye 'headed paper (barua yenye nembo)' ya Mwananchi hata leo (jana) au kesho (Leo) utajibiwa kiofisi," alisema Mwero.
BoT ni taasisi ya pili kutuhumiwa kuhusika na ufisadi huo katika mradi wa ukarabati wa nyumba za vigogo wake ndani ya kipindi cha mwaka mmoja.
Tayari Tanesco imekumbwa na tuhuma kama hizo ambazo bado hazijapoa. Wizara ya Nishati na Madini imeeleza kuwa inaendelea kuzifanyia kazi.
Hata hivyo, tuhuma za ufisadi ndani ya BoT zinadaiwa kuwa kubwa na za kutisha ikilinganishwa na kiwango cha pesa kinachodaiwa kutumika kwa ukarabati kwa nyumba za Tanesco.
Wakati Tanesco inatuhumiwa kutumia Sh.1.4bilioni kwa ajili ya ukarabati wa nyumba saba za vigogo wake, taarifa za kuaminika kutoka vyanzo mbalimbali vya habari zilizolifikia Mwananchi zinaeleza kuwa BOT imetumia zaidi ya Sh1bilioni kukarabati nyumba moja, kati ya nyumba nne zilizokuwa katika mradi huo wa ukarabati.
Kiasi hicho cha fedha unaweza kununua nyumba mbili mpya nje ya maeneo ya Jiji la London, Uingereza. Kwa sasa bei ya nyumba katika maeneo ya Cardiff ni Sh450milioni kwa nyumba moja.
Chanzo: Mwananchi 12/22/2009