peno hasegawa
JF-Expert Member
- Feb 24, 2016
- 12,775
- 21,335
Zile zama za makampuni ya nje kupiga hela kwa mgongo wa ushauri zimerudi.
TPDC imeingia mkataba ya kampuni ya Uingereza za Baker Botts kwa ajili ya ushauriwa kisheria kwenye mikataba ya gesi.
Hivi Tanzania bado hatuna kampuni zenye uwezo wa kutoa ushauri wa kisheria hadi tutoe Ulaya?
View attachment 2095378
UPDATE: Jan 25, 2022
TPDC yalazimika kutoa ufafanuzi
UFAFANUZI KUHUSU UPATIKANAJI WA MSHAURI ELEKEZI (TRANSACTION ADVISOR) WA SERIKALI KATIKA MRADI WA KUCHAKATA NA KUSINDIKA GESI ASILIA (LIQUEFIED NATURAL GAS [LNG] PROJECT)
25 Januari, 2022
Mnamo tarehe 25 Januari 2022, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) na Kampuni ya Baker Botts (UK) LLP walisaini Mkataba wa Huduma ya Ushauri wa Kitaalam na Kampuni ya Baker Botts (UK) LLP ya Uingereza ili kushirikiana na Serikali katika majadiliano ya kutekeleza Mradi wa LNG.
Mchakato wa kumpata Mshauri Elekezi ulianza tarehe 12 Aprili 2018 ambapo TPDC ilitoa tangazo katika magazeti na tovuti mbalimbali kwa ajili ya kualika kampuni mbalimbali kuonesha nia ya kutekeza jukumu hilo kwa Serikali.
Tangazo hili lilichapishwa katika gazeti la Dailynews la tarehe 12 Aprili 2018 pamoja na kuwekwa katika tovuti za TPDC, UNDP na AfDB. Hadi kufikia tarehe 4 Mei 2018, kampuni 64 ziliwasilisha nia ya kushiriki katika zabuni tajwa.
Tathmini ya maombi yote ilifanyika kwa mujibu wa Sheria ya Manunuzi ya Mwaka ya 2011 ambapo Kampuni 3 kati ya 64 zilifanikiwa kutimiza vigezo vyote vilivyotumika katika tathmini na hivyo kuendelea na hatua zinazofuata ambayo ilihusisha ufunguzi wa mapendekezo ya kifedha (Financial Proposal). Hata hivyo, mchakato wa zabuni ulisimama kutokana na kusimamishwa kwa majadiliano baina ya Serikali na Wawekezaji.
Mwezi Novemba 2021, Serikali na Wawekezaji walikubaliana kuendeleza majadiliano. Hivyo, TPDC ilihuisha mchakato wa kumpata Mshauri Elekezi baada ya kushauriana na taasisi mbalimbali zinazosimamia manunuzi ya umma na mikataba. Mchakato huu ulikamika na kupelekea TPDC na Mzabuni aliyeshinda kusaini Mkataba tarehe 25 Januari, 2022.
Ikumbukwe kuwa Mradi wa LNG, ni mradi mkubwa na wa kwanza kutelekezwa hapa nchini. Mradi huu unahusisha kuvuna gesi asilia kutoka kwenye kina kirefu cha Bahari takribani kilometa tano kutoka usawa wa Bahari na kuisafirisha takribani kilometa 200 mpaka ufukwe wa Bahari ya Hindi katika eneo la Likong’o, Lindi kwa ajili ya kuichakata na kuisindika ili kuisafirisha kwenye masoko ya kimataifa na gesi nyingine kutumika kwa mahitaji ya ndani na ya kikanda. Mradi huu unatarajiwa kuwa na gharama ya takribani Shilingi trilioni sabini (70).
Kutokana na ukubwa na upekee wa Mradi huu, Serikali iliona umuhimu wa kushirikana na Mshauri Elekezi mwenye uzoefu wa utekelezaji wa miradi ya aina hii duniani ili kushauri kuhusu masuala ya kiufundi, kiuchumi, kifedha na kisheria.
Serikali ina lengo la kumtumia Mshauri Elekezi kwa ajili ya kupata ushauri stahiki hususani katika masuala ya teknolojia, kifedha na masoko ya kimataifa ili kuuza gesi iliyogundulika katika misingi ya ushindani na kulinda maslahi ya Taifa.
Kampuni ya Baker Botts (UK) LLP ni moja ya kampuni kubwa Duniani yenye uzoefu wa kimataifa wa kutoa ushauri wa kitaalam kwenye miradi ya aina hii. Kampuni hii itashirikiana na kampuni nyingine za kimataifa zenye ubobezi wa masuala ya teknolojia, kifedha na masoko. Vilevile, Kampuni hiyo itafanya kazi na Kampuni ya Kitanzania ya Apex Attorneys Advocates. Pia Kampuni hiyo itatoa mafunzo maalum kwa watanzania katika mada mbalimbali kuhusu Mradi ili kuwajengea uwezo wakati wa utekelezaji wa Mradi.
Imetolewa na:
Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano SHIRIKA LA MAENDELEO YA PETROLI TANZANIA