Anaandika Tito Magoti.
Mheshimiwa Waziri Mkuu,Nakuandikia barua ya wazi kwa heshima kubwa sana!
Ni mwaka wa saba tangu uwe Mtendaji Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (CEO JTM hapa chini). Kuna mambo mengi unayojivunia. Pengine ndio maana umedumu katika nafasi yako hadi sasa.
Lakini Mheshimiwa, umewahi kujiuliza wananchi wanasemaje kuhusu utendaji wako kama Waziri Mkuu? Je, umewahi kutathmini umuhimu wa nafasi yako, unachofanya dhidi ya ufanisi unaotarajiwa?
Mhe Waziri Mkuu, bila mpangilio, niruhusu nikukumbushe yafuatayo:
Mwaka 2018 watu zaidi ya 130 walifariki katika ajali ya MV Nyerere, Ukerewe. Ukiwa CEO wa JMT, ulisitisha uokoaji kwakuwa giza liliingia. Serikali ikaenda kulala. Lakini Wananchi walipanda mitumbwi wakawasha ‘karabai’ zao kwenda kuwatafuta na kuwaokoa ndugu zao. Serikali ilikwenda kulala kwa udhuru wa giza, kana kwamba hilo lingesitisha maafa hata kwa nukta moja. Uliunda Tume. Ripoti unayo. Hakuna aliyewajibika.
Nov ‘22, ukiwa CEO JTM, ndege (Precision Air) imepata ajali ziwa Viktoria, Bukoba. Badala ya kuharakisha kuokoa uhai wa abiria, wewe na Serikali yako yote mliamua kuwapa adhabu ya kifo kwa uzembe na kutojali. Watu 19 walikufa kikatili huku wakitarajia msaada wako.
Ni kweli na inasikitisha kwamba haukujali hata kidogo. Uliendelea na shughuli zako. Baadaye sana ukaenda Kagera kupiga picha na manusura wa ajali. Na kusimamia mazishi. Ulionesha utayari na mamlaka katika kusimamia ‘sherehe ya mazishi’ kuliko kuokoa maisha ya watu. Ni sahihi kusema kwamba, ukiwa CEO JMT, kwa uzembe na kutojali, uliruhusu maisha ya watu 19 yadhulumiwe. Inasikitisha!
Ndege ya shirika la Precision Air ikiwa imezama ndani ya ziwa Viktoria, Kegera.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, sio hayo tu!
Mlima Kilimanjaro umeriporiwa kuungua moto majuzi. Haukuitikia tukio hilo kwa wakati. Kuna haja ya kuliandikia UNESCO kuhusu uzembe huu unaojirudia.
Sept 2022 Polisi waliua raia watatu nyumbani kwetu Mara. Pia walimdhalilisha kingono binti mmoja kwa kumvua nguo wakimtaka afanya mapenzi na baba yake aliyevuliwa nguo vilevile. Binti yuko wapi? Serikali ambayo wewe ni CEO wake imefanya nini kando ya ule mzaha wa polisi?
Jan 2022 mfanyabiashara wa madini aliuliwa na Polisi Mtwara. Uliunda Tume. Ripoti yake haijulikani ilipo. Zipo taarifa kuwa makachero waliofunguliwa kesi watakuwa huru, ni suala la muda. Ripoti iko wapi. Nini kimefanyika zaidi?
Mheshimiwa Waziri Mkuu,
Una mamlaka makubwa sana kama CEO JMT. Lakini umekuwa ukitoa maagizo mengi ambayo ni maigizo. Mazingaombwe! Ni maigizo kwakuwa hayatekelezwi kwa vitendo. Kauli zako hazipewi uzito wowote, nikwambie ukweli.
Tangu uwe CEO JMT, umeunda Tume nyingi sana. Ni mara chache utasikia ama kuona Ripoti ya Tume hii ama ile imewekwa wazi kwa umma kusoma na kushiriki utekelezaji. Maagizo yako yanakuwa maigizo kwa mtindo huu.
Machi 2021, wakati wananchi wanamtafuta kiongozi wao, ulilitangazia Taifa kuwa Rais Magufuli ni mzima anachapa kazi. Ulisema ukiwa msikitini. Kumbe Rais alikuwa mgonjwa mahututi. Ukikumbuka tukio hili huwa unajiambia nini?
Mwaka 2016/20 mlitangazia vita ya kiuchumi. Sheria za ulinzi wa rasilimali zikaandikwa ghafla. Mkawaweka wafanyabiashara jela. Mkaunda Tume. Mkaanzisha kampuni ya madini. Juzi mmekiri sehemu ya ulaghai mliofanya katika vita ya kiuchumi. Baadhi ya sheria mmerekebisha. Ulikuwa CEO JMT na bado unadumu.
Profesa Kabudi akikiri kwamba vita ya kiuchumi ilikuwa ni ulaghai
Mwaka 2018/19 na kuendelea, ukiwa CEO JMT, ulishuhudia serikali yako ikifanya dhuluma dhidi ya wakulima wa zao la korosho. Biashara ya korosho hadi leo ni mazingaombwe matupu.
Mwaka 2019 kulitokea tetemeko la ardhi Kagera. Hakuna jambo la maana linalokumbukwa zaidi ya matumizi mabaya fedha za waathirika na kauli za kizembe kama: ‘sikuleta tetemeko,’ na nyingine za ajabu. Ulikuwa CEO JMT.
Tangu 2015 mmetunga Sheria lukuki kwa hati ya dharura. Sheria nyingi zinazobana ufurahiwaji wa haki za kisiasa na kiraia na kiuchumi. Mmeweka rekodi ya kuwa Serikali iliyotunga na kurekebisha baadhi ya sheria hizohizo ndani ya muda mfupi. Ukiwa CEO JMT, jiulize, mlibeba maslahi ya nani?
Ukiwa CEO JMT, maelfu wametupwa jela kwa kesi za uongo. Wapo waliotekwa, walioteswa na kupewa ulemavu wa kudumu. Kuna waliouwawa kikatili. Kuna waliofutiwa kesi baada ya kukaa jela muda mrefu. Yamefanyika ukiwa CEO JMT. Sijawahi kukusikia ukiomba radhi, kujuta ama kuhofia.
Ukiwa CEO JMT, wananchi wengi wamepotezwa. Hawajulikani walipo. Wamo wakosoaji wa serikali. Haujawahi kujishughulisha kuwatafuta ama kuomba msaada wa kuwatafuta.
Sep 2017, Wakili Mwandamizi Tundu Lissu alipigwa risasi 36 jijini Dodoma na ‘watu wasiojulikana.’ Jaribio la kudhulumu uhai wa mtu kiasi kile lilifanywa ukiwa CEO JMT. Hakuna jambo lolote la maana umewahi kufuatia tukio hilo.
Tangu 2016 ukiwa CEO JMT uliruhusu uwepo wa kundi la ‘watu wasiojulikana.’ Waliendesha ‘oparesheni’ dhidi ya wakosoaji wa serikali na zaidi. Watu walitekwa, kuuwawa na wengine hawajulikani walipo.
Ukiwa CEO JMT, umeshuhudia uporaji wa fedha za watu waliopewa kesi za uongo kwa jina la ‘plea bargain.’ Ukiwa CEO JMT, juzi mmeunda tume kuchunguza mwenendo wa zoezi la plea baragain. Unawezaje kuwa na ufanisi?
Waendesha Mashitaka wakiwa na lundo la fedha za ‘plea bargain.’
Ripoti za CAG kila mwaka zinaonesha ubadhilifu wa fedha za umma uliokithiri. Hakuna jambo lolote la maana umewahi kulifanya juu ya ripoti hizo. Hata maazimio ya Bunge kufuatia Ripoti za CAG haufuatilii utekelezaji wake. Haujawahi kujisikia vibaya kufuatia uzembe katika usimamizi unaopelekea wizi unaoandikwa na CAG kila mwaka tangu uwe CEO JTM. Ujasiri wa kipekee sana!
Ukiwa CEO JMT na mshirika wa CCM, kati ya 2016/20, ulishiriki jitihada zote za kuua demokrasia nchini Tanzania. Leo hatuna Bunge sababu ya ubinafsi wenu. Mahakama hali kadhalika. Utamaduni wa ‘uchawa’ nchini ni matokeo ya hofu zenu. Si jambo unalohofia ama kujutIa. Maana hadi leo mnalea viongozi wanaotishia na kuhujumu uhuru wa fikra nchini. Hii ni mbaya sana.
Matukio ya raia kuuwawa wakiwa chini ya polisi ni mengi. Mauaji yanatekelezwa na Polisi. Ukiwa CEO JMT, haujawahi kuitisha uchunguzi wowote huru dhidi ya matukio haya, wala kuchukua hata hatua za kisiasa.
Mwaka 2018 ukiwa CEO JTM, ulishuhudia polisi wakimuua mwanafunzi Akwilina Aqwilini kwa kumpiga risasi. Mliwashitaki ila baaadaye mkawafutia kesi. Hii ndiyo heshima mliyomchagulia Aqwilina. Hakustahili zaidi?
MKIRU na zaidi na matishio ya ugaidi yamedhulumu uhai wa watu wengi sana. Hakuna taarifa yoyote rasmi ya serikali ambayo wewe ni CEO wake kuhusu oparesheni ya MKIRU, idadi ya watu waliopoteza maisha na mwito wa usalama zaidi. Watu waliofunguliwa kesi za ugaidi kufuatia matukio haya wengi hawajashitakiwa. Wako mahabusu miaka sasa. Azory Gwanda aliuwawa katika muktadha huo pia. Tumejifunza nini. Ufanisi wenu kama Serikali ni upi?
Ukiwa CEO JMT, watumishi wa umma wamefukuzwa kwa uhakiki wa vyeti. Hivi karibuni mmeahidi kuwalipa fidia. Nani alisikiliza hizi kesi, kuna uhalifu, na kwanini fidia? Hamjawahi kuwa na umakini hata kidogo.
Ukiwa CEO JMT, watumishi wa umma wamedhulumiwa stahiki zao kwa miaka sita na zaidi, wakiwemo wastaafu. Hivi, Mheshimiwa, wewe umewahi kuishi bila mshahara ama marupurupu kwa angalau siku moja?
Mwaka 2019/20 Ukiwa CEO JMT, mlifuta haki ya Wananchi na AZAKI kufungua mashauri katika Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, hata bila aibu kwamba Mahakama hii muhimu ipo nchini, Arusha. Uamuzi huu umelisaidia nini taifa?
Ukiwa CEO JMT, umeshiriki kupuuza utekelezaji wa hukumu za Mahakama za Kimataifa, ikiwemo ya Afrika na ya Afrika Mashariki ambazo Tanzania ni mshirika. Mmeiweka nchi yetu sawa na mataifa yasiyojua wajibu wao kimataifa.
Mheshimiwa Waziri Mkuu,
Kwakuwa orodha ni ndefu, ninaomba nikuulize tena, Mheshimiwa, unajisikiaje na unawezaje kuwa kiongozi wa Serikali iliyofeli, japo kwa haya machache?
Ninajua sina umri wa kukushauri ujiuzulu. Lakini nafurahi kukumbusha tulikotoka!