THE LAST SUMMER IN TANZANIA

Abdallahking

JF-Expert Member
Mar 19, 2018
3,983
10,804
1.jpg



SIMULIZI HII IMEKAMILIKA
IMEANDIKWA NA : NYEMO CHILONGANI
CHANZO : BURE SERIES


SEHEMU YA KWANZA


Matangazo yalikuwa yamebandikwa kila kona ndani ya Jiji la Dar es Salaam yaliyokuwa yakihusu ujio wa mjasiriamali mkubwa, Potter Mickey aliyejulikana duniani kote kutokana na mafundisho yenye nguvu ya kuwafanya watu kujishughulisha na biashara na mwisho wa siku kufanikiwa.
Huyu alikuwa mjasiriamali mwenye nguvu kubwa ya ushawishi, mjasiriamali aliyejitengenezea jina kubwa duniani kote kutokana na masomo yake yaliyoleta mabadiliko makubwa katika jamii.
Mickey alikuwa miongoni mwa watu mashuhuri duniani, kazi yake kubwa ilikuwa ni kuwahamasisha watu wengi kuweka nguvu kubwa katika biashara na hatimae kufanikiwa kwa kiasi kikubwa.
Japokuwa alikuwa Mmarekani lakini hakuwa mtu wa kutulia tu nchini mwake, leo alikuwa Afrika Kusini, wiki ijayo Uingereza, mara Urusi na sehemu nyingine duniani zikiwepo nchi za Kiarabu.
Ingawa lilikuwa ni jambo gumu kwa Waarabu kuwaruhusu Wamarekani kuingia nchini mwao kiholela lakini kwa bwana Mickey lilikuwa jambo jepesi sana, kila alipotaka kuingia katika nchi hizo zilizokuwa katika Umoja Waarabu wa Emirate, aliruhusiwa bila tatizo lolote lile.
Alizunguka kuanzia Dubai, Fujairah, Abu Dhabi, Ajman na sehemu nyingine katika nchi zilizokuwa katika umoja wa Kiarabu wa Emirate, huko kote alikuwa akihubiri kuhusiana na namna ambavyo mtu anaweza kufanya ili kufanikiwa katika biashara zake.
Mbali na nchi hizo, pia Mickey alitembelea nchi zilizokuwa Asia kama Iran, Iraq, China na sehemu nyingine, kote huko bado alikuwa akihubiri kuhusu ujasiriamali katika kufanikiwa.
Mickey alipendwa, mahubiri yake yalimfurahisha kila mtu aliyekuwa akimsikiliza, mara kwa mara alikuwa akipokea mialiko kutoka katika nchi za Kiarabu, wote walikuwa wakinufaishwa na mahubiri yake na hivyo kuyatumia katika biashara zao za mafuta.
Baada ya kuzunguka katika nchi za Kiarabu kwa kipindi kirefu, bwana Mickey akahama na kuhamia barani Ulaya, kama kawaida yake bado mahubiri yake yalikuwa gumzo kwa kila mtu aliyeyasikia.
Aliendelea kuwasisitizia watu kwamba paundi moja waliyokuwa nayo ambayo ilikuwa ni kiasi kidogo cha fedha kingeweza kuyabadilisha maisha yao na kuwagawia mabilioni ya paundi.
Kwa maneno yake ya harakaharaka, ilionekana kuwa ngumu sana lakini alipokuwa akifafanua namna ambavyo hiyo paundi moja ilivyotakiwa kutumika na kuzalisha mabilioni, kila mtu alibaki akishangaa na kukubaliana naye.
“This is the man of God,” (Huyu ni mtu wa Mungu) alisikika jamaa mmoja akiwaambia wenzake.
“Yes! His words change me positively from one step to another” (Ndiyo! Maneno yake yamenibadilisha kutoka hatua moja kwenda nyingine) alisema jamaa mwingine.
Kila alipokwenda, Mickey aliacha sifa kubwa, watu walikuwa wakimpenda huku wengi wakimuita mhamasishaji wa utajiri kwa masikini bila kuwa na ubaguzi wowote ule. Sifa zake hizo ndizo zilizomfanya kupokea mialiko mingi katika nchi nyingine nyingi.
Kila alipokuwa akienda, aliongozana na mkewe, Elizabeth ambaye alionekana kuwa mtu muhimu kuliko wengine. Kupitia mafundisho yake, akajikuta akijiingizia kiasi kikubwa cha fedha, vitabu vya ujasiriamali kama Think like A Businessman, Walking With Success vilimuingizia fedha nyingi ambazo alizitumia kuwasaidia watu waliokuwa na matatizo mbalimbali kama umasikini na wagonjwa.
Baada ya kuzunguka duniani kwa kipindi kirefu, akahitaji muda wa kupumzika, akili yake ilichoka, hakutaka tena kusafiri na kwenda sehemu nyingine kufanya mafundisho yake, kwa wakati huo, alihitaji kuipumzisha akili yake tu.
Kichwa chake kikalifikiria Bara la Afrika, sehemu ambayo ilikuwa na vivutio vingi. Alichokifanya ni kufungua kompyuta yake ili kuangalia ni nchi gani alitakiwa kwenda kwa ajili ya mapumziko hasa katika majira ya joto kama hayo, akaichagua nchi ya Tanzania.
“We are going to Tanzania once again” (Tunakwenda Tanzania kwa mara nyingine) alisema Mickey, alikuwa akimwambia mke wake, Elizabeth.
“What am I suppose to do?” (Natakiwa kufanya nini?) aliuliza Elizabeth.
“You have to tell Victor that we are going to meet with him there,” (Unatakiwa kumwambia Victor kwamba tunakwenda kukutana naye huko) alisema bwana Mickey.
“No problem.” (Hakuna tatizo)
Victor alikuwa mtoto wao aliyekuwa akisoma katika Chuo cha Mississippi nchini Marekani. Kama alivyokuwa baba yake, hata naye alikuwa akisomea mambo ya biashara ili baadae aje kuwa mfanyabiashara mzuri na mhamasishaji kuhusu ujasiriamali.
Uwezo wake chuoni haukuwa mdogo, Victor alikuwa akifaulu sana masomo yake, alikuwa miongoni mwa watu waliokuwa wakifanya vizuri kabisa katika masomo yote. Kila siku alikuwa akitumia dakika ishirini kuwaambia wanachuo wengine ni kwa namna gani walitakiwa kuyabadilisha maisha yao na mwisho wa siku kuwa mabilionea.
Kama alivyokuwa baba yake, naye alitokea kupendwa na kuwa mhubiri mzuri kuhusu mambo ya biashara kiasi kwamba wanachuo wengine walisema kwamba Victor alikuwa zaidi ya baba yake.
Ingawa alipanga kuja Tanzania kupumzika na mkewe lakini mara baada ya maprofesa wa Chuo Kikuu kusikia kwamba bwana Mickey alikuwa akija ndani ya nchi hiyo, wakaandaa tamasha lake kwa ajili ya mafundisho ya ujasiriamali kwa ajili ya wanachuo wa chuo hicho.
“Kuna kazi nimepewa,” alisema bwana Mickey.
“Kazi gani?”
“Natakiwa kwenda kuwafundishi wanachuo kuhusu ujasiriamali.”
“Wapi? Uarabuni kama kawaida?”
“Hapana. Hukohuko Tanzania tunapokwenda.”
“Mmmh! Lakini hiki si ndiyo kipindi chetu cha mapumziko mpenzi!”
“Najua hilo, lakini haina jinsi, sijawahi kufundisha nchini Tanzania, mara nyingi tumekuwa tukienda kule na kupumzika, naomba uniruhusu tu nifanye kitu kama hicho,” alisema Mickey kwa sauti ya upole.
“Mpenziiiiiii...”
“Naomba uniruhusu, siku mbili tu.”
“Lakini kw.....”
“Si zaidi ya siku mbili mpenzi, naomba uwape nafasi watu wengine nao watajirike.”
“Sawa. Ila niahidi, siku mbili!”
“Nakuahidi.”
Mickey akamsogelea mke wake, Elizabeth na kumkumbatia. Alikuwa akifanya mambo mengi katika maisha yake lakini mengi aliyokuwa akiyafanya, ilikuwa ni lazima kumshirikisha mkewe. Alimpenda mwanamke huyo, alimthamini na kumjali kwa kila kitu.
Ingawa alikuwa na ndugu, marafiki lakini mke wake ndiye alikuwa kila kitu, kila nchi aliyokwenda kufundisha ilikuwa ni lazima aende na mke wake huyo aliyekuwa mtu muhimu kuliko watu wote katika maisha yake.
Baada ya wiki moja safari ya kwenda nchini Tanzania ikaanza. Ndani ya ndege, kila mmoja alionekana kuwa na furaha, kila wakati walikuwa wakikumbatiana tu, hakukuwa na kitu ambacho kwao kilionekana kuwa cha thamani kama kuwa karibu.
Waliishi pamoja kwa miaka thethini na tano, walizoeana na mapenzi yao kukua kadiri siku zilivyozidi kwenda mbele, hawakuwa watu wa kugombana mara kwa mara, kila mmoja alipokuwa akifanya kosa, alikubali kwamba alikosea na aliomba msamaha.
Baada ya wiki moja, safari ya kuelekea nchini Tanzania ikaanza. Ilikuwa ni safari ndefu na yenye kuchosha lakini baada ya masaa ishirini na tano, ndege ya Shirika la Ndege la American Airlines ilikuwa ikitua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.
Hali ya hewa ilikuwa ni ya joto sana, kwa kuwa safari hiyo ilihusiana na ufundishaji wa ujasiriamali chuoni, maprofesa walikuwa uwanjani hapo kwa ajili ya kuwapokea. Mapokezi yalifanyika vizuri, walipoona kila kitu kimekamilika, wakawachukua na kuelekea hotelini kwa ajili ya mapumziko kabla ya kuanza kwa semina ya ujasiriamali iliyokuwa ikitangazwa sehemu zote jijini Dar es Salaam kwa kubandika matangazo mbalimbali.
****
Wanachuo wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam walikuwa wamejiandaa kwa ajili ya kusikiliza mafundisho juu ya namna ya kuwa bilionea kutoka kwa mhamasishaji mashuhuri aliyekuwa akifanya ziara zake mbalimbali duniani, bwana Potter Mickey.
Kila mmoja alikuwa na kiu ya kufanikiwa, kitendo cha kuambiwa kwamba shilingi elfu moja waliyonayo inaweza kuwafanya kutajirika na kuwa na mabilioni ya shilingi, kuliwachanganya watu.
Siku iliyofuata, wanafunzi wengi walikuwa wamekusanyika katika Jengo la Nkurumah kwa ajili ya kumsikiliza mhamasishaji huyo aliyetarajiwa kuingia chuoni hapo muda mchache ujao.
Idadi hiyo kubwa ya watu waliokuwa wamekusanyika ndani ya jengo hilo, liliufanya ukumbi huo kuwa mdogo kwani si wanachuo peke yao waliokuwa mahali hapo bali hata watu wengine kutoka sehemu nyingine walikuwa ndani ya jengo hilo.
Vitabu vyake vya ujasiriamali vya bwana Mickey viliendelea kuuzwa ukumbini, kila mtu alitaka kuwa navyo, kutoa shilingi elfu ishirini kwa ajili ya kuwa na vitabu hivyo viwili wala haikuonekana kuwa tatizo hata kidogo.
Baada ya dakika thelathini, bwana Mickey akafika chuoni hapo huku akiwa na mkewe. Watu wakaanza kushangilia, kuonekana tu ndani ya chuo hicho, tayari watu wakapata matumaini mapya, wale wasiokuwa na fedha wakajiona kuanza kupata utajiri.
“Daah! Huyu jamaa ni noma sana, unajua nilianza kufuatilia mafundisho yake kwa njia ya vitabu toka mwaka juzi, jamaa anatisha, amenifanya na mimi kuwa mtu miongoni mwa watu kwa kuwa na biashara nyingi,” alisikika mwanachuo mmoja, alikuwa kijana lakini mwenye biashara nyingi.
“Kumbe ulipata ujuzi kutoka kwa huyu jamaa?” aliuliza mwanachuo mmoja.
“Ndiyo! Yaani ukimsikiliza na kuvisoma vitabu vyake, utapenda.”
“Hebu ngoja na mimi nimsikilize, naweza kupata kitu,” alisema jamaa huyo.
Siku hiyo, watu walijifunza mambo mengi kuhusiana na biashara, kila neno alilokuwa akilizungumza bwana Mickey, lilionekana kuwa msingi mkubwa kwa wanachuo waliokusanyika mahali hapo.
Alijua kuzungumza na watu, kadiri alivyoendelea kuongea na ndivyo ambavyo watu walitamani aendelee kuzungumza zaidi na zaidi. Alionekana ni mtu mwenye mafanikio makubwa ambaye alikuwa akitaka kuwaona watu wakifanikiwa na kuwa mamilionea wakubwa duniani.
Hakutaka kuwaona watu wakiwa masikini, aliamini kwamba kila mtu duniani alikuwa na uwezo mkubwa wa kupata fedha kwa kufanya biashara, hivyo nafasi hiyo alikuwa akiitumia vilivyo kwa kuwaambia watu ni kwa namna gani walitakiwa kuanza na kiasi kidogo cha fedha walichokuwa nacho.
Siku hiyo, kila mtu akaonekana kumuelewa bwana Mickey ambaye alikuwa akizungumza hatua kwa hatua kama ambavyo mtu anaweza kumuhadithia mtoto mdogo kitu fulani. Baada ya kufanya semina hiyo kwa saa moja na nusu, akamaliza na kuomba kuondoka.
“Nitakwenda kuwa tajiri, nipe miaka miwili,” alisema mwanachuo mmoja.
“Mawazo yako ni kama mimi, pia nitakwenda kuwa tajiri mkubwa,” alisema jamaa mwingine.
Maneno yake yakawatia watu hamasa, kila mmoja alijiona kuwa na uwezo mkubwa wa kufanya biashara na kufanikiwa na mwisho wa siku kuwa mfanyabiashara mkubwa nchini, yaani ilikuwa ni sawa na mtu aliyeangalia filamu za mapigano za kina Jackie Chan na mwisho wa picha, akitoka nje kujiona kuwa na uwezo wa kupigana kama mcheza filamu huyo.
Siku hiyo bwana Mickey na mkewe wakarudi hotelini ambapo wakafanya mambo yao na kujiandaa kwa ajili ya siku ya pili na ya mwisho ya semina hiyo iliyotakiwa kufanyika palepale chuoni ili waendelee na ishu zao za mapumziko kama walivyotarajia.
Siku hiyo ilipofika, bwana Mickey akaonekana kuwa tofauti kabisa, hakuwa na furaha kama siku iliyopita, kila wakati alionekana mtu wa mawazo kupita kawaida kitu kilichomtia hofu mke wake, bi Elizabeth.
“Kuna nini?”
“Hakuna kitu mke wangu!”
“Hapana, niambie kuna nini, umebadilika sana!”
“Sijajua kwa nini, lakini kiukweli hakuna kitu, endapo kungekuwa na kitu, nisingeweza kukuficha mke wangu!” alisema bwana Mickey.
Japokuwa aliambiwa na mume wake kwamba hakukuwa na kitu chochote kibaya lakini moyo wake haukuonekana kuridhika hata kidogo, naye akajikuta akiingia katika huzuni.
“Unakumbuka kwamba Victor anaingia leo usiku?” aliuliza bi Elizabeth.
“Yeah! Nakumbuka sana kipenzi. Tutakwenda kumpokea na vitu vingine viendelee, kwanza tumalize hii semina,” alisema bwana Mickey.
Siku hiyo ya pili na ya mwisho ndiyo ilionekana kuwa balaa. Watu walifurika mara mbili ya siku iliyopita, zaidi ya watu elfu moja walihitaji kumsikia mhamasishaji huyo kutoka nchini Marekani.
Ukumbi wa Nkurumah ukawa mdogo kiasi kwamba kwa haraka sehemu ikabadilishwa na kupelekwa katika uwanja wa mpira chuoni hapo ili kila mtu apate nafasi ya kumsikiliza mtu huyo.
“Hapa poa sasa, hewa safi na ukitaka hata juu ya mti unakaa, full kujiachia tu,” alisema jamaa mmoja.
Kutokana na sehemu hiyo kuwa na miti mingi, wapo wanachuo ambao walipanda juu ya miti na kuanza kumsikiliza bwana Mickey aliyekuwa akiongea kwa uchungu wa kuwataka watu watoke pale walipokuwa na kusonga mbele.
Siku hiyo alizungumza mambo mengi ambayo yote yalionekana kuwa faida kwa kila mtu aliyekuwa akimsikiliza.
“One day my father gave me fifty cent that changed my life forever. I know, it is very difficult to believe me but let me tell you what I did. I asked myself abo.....” (Siku moja baba yangu alinipa senti hamsini iliyobadilisha maisha yangu milele. Najua ni vigumu mno kuniamini lakini acha nikwambie kile nilichokifanya. Nilijiuliza kuh....) alisema bwana Mickey lakini hata kabla hajamaliza sentensi yake, ukasikika mlio wa risasi mahali hapo.
“Paaaaaa.....” mlio mkubwa wa risasi ukasikika, bwana Mickey akaangua chini, damu zikaanza kumtoka kichwani kwake, kama alivyokuwa ameanguka, aliishia hivyohivyo na hakuweza kuutingisha mwili wake.
Watu waliokuwa mahali hapo, mara baada ya kusikia mlio wa risasi ile, wakaanza kukimbia hovyo, wale waliokuwa juu ya miti, ghafla wakajikuta wakiwa chini bila kujua wameshukaje na kuanza kukimbia.
Lilikuwa ni moja ya tukio lililoogopesha, mlio wa risasi uliokuwa umesikia, haukuonekana kuwa wa kawaida, ulikuwa na sauti kubwa kiasi kwamba baadhi ya watu walihisi kwamba lilikuwa bomu.
Kila mmoja akakimbia na ni bi Elizabeth peke yake ndiye aliyekuwa amebaki mahali hapo, aliuhisi mwili wake ukiwa umepigwa ganzi, picha aliyokuwa akiiona kwamba mume wake alikuwa chini, damu zilikuwa zikimtoka kichwani baada ya risasi kupenya kwenye paji la uso wake na kutokea nyuma, ilikuwa ni moja ya picha yenye kutisha ambayo hakuwahi kuiona maishani mwake.
Hapohapo akaanza kumkimbilia mume wake pale chini, hakukuwa na wa kumsaidia, kila mtu alikuwa amekimbia kuyaokoa maisha yake.
“Mickey...Mickey...please wake up, dont’t leave me alone, wake up my husband...wake up and look at me....” (Mickey...Mickey...tafadhali amka, usiniache peke yangu, amka mume wangu...amka na uniangalie...) alisema bi Elizabeth huku akilia kama mtoto.
Aliushika mwili wa mume wake pale chini, hakuwa akiamini kile kilichokuwa kimetokea, wakati mwingine alifikiri kwamba alikuwa ndotoni na baada ya dakika chache angeamka na kujikuta akiwa kitandani, chumbani na mumewe lakini ukweli ulibaki palepale kwamba hakuwa kwenye maisha ya njozi, kila kilichokuwa kikitokea, kilitokea katika maisha halisi.
Baada ya dakika tano kuona kwamba kila kitu kilikuwa shwari, wale watu waliokuwa wamekimbia wakaanza kujikusanya mahali hapo ili kuona ni kitu gani kilikuwa kimetokea.
Bi Elizabeth alikuwa jukwaani, bado alikuwa ameushika mwili wa mume wake huku akilia kama mtoto, muda wote alikuwa akimtaka aamke kwani hakuwa akiamini kama alikuwa amefariki dunia.
“Kuna nini?” aliuliza jamaa mmoja, alikuwa akiangalia huku na kule, hakuwa akijiamini.
“Mmmh! Sijui, mimi nilisikia paaa, baada ya hapo nikajikuta nipo barabarani,” alisema jamaa mwingine.
“Hivi ilikuwa risasi au bomu?”
“Mmmh! Wala sijui!”
Bi Elizabeth alikuwa akiendelea kulia, moyo wake ulikuwa kwenye maumivu makali, bado hakuwa akiamini kile kilichokuwa kimetokea, kila aliyekuwa akimwangalia mahali hapo, alimuonea huruma, wala hazikupita dakika nyingi, akaanguka chini na kupoteza fahamu, hakujua ni kitu gani kiliendelea baada ya hapo.
****
Mwili wa bwana Mickey ulikuwa chini, damu zilikuwa zimetapakaa katika jukwaa lile, watu walibaki wakishangaa tu kana kwamba hawakuwa wakifahamu ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea mahali hapo.
Maprofesa wakapiga hatua mpaka katika jukwaa lile, pembeni ya mwili wa bwana Mickey kulikuwa na mke wake ambaye alipoteza fahamu kutokana na mshtuko mkubwa alioupata baada ya kushuhudia mume wake kipenzi akiwa amepigwa risasi mbele ya macho yake.
Gari la mtu binafsi likasogezwa na kumchukua bi Elizabeth na kuondoka naye huku wakiuacha mwili wa bwana Mickey palepale ulipokuwa. Ndani ya dakika kadhaa, polisi wakafika na baadhi ya watu kutoka katika kitengo cha upelelezi, walichokifanya ni kuupiga picha mwili ule na kuchukua vipimo vyote ambavyo walitakiwa kuvichukua, baada ya hapo, wakauchukua na kuondoka nao.

Ilikuwa ni taarifa iliyoshtua mno, hakukuwa na mtu aliyeamini kama kweli mhamasishaji huyo kutoka nchini Marekani alikuwa ameuawa nchini Tanzania. Taarifa hizo ziliendelea kusambazwa na ndani ya kipindi kichache tu, dunia nzima ikafahamu kile kilichokuwa kimetokea katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Dunia nzima ikaanza kuilalamikia Tanzania kwa kutokuwa makini katika kudumisha ulinzi wa nchi yao, kitendo kilichokuwa kimetokea kilimsikitisha kila mtu na kuendelea kuilaumu nchi hiyo.
Marekani haikutaka kukaa kimya, wakatoa tamko ambalo walitaka litelekezwe mara moja na nchi ya Tanzania kwamba muuaji aliyemuua bwana Mickey anapatikana na kufikishwa katika vyombo vya sheria.
“Kimenuka!”
“Kuna nini?”
“Umewasikia wakina Obama huko?”
“Wamesemaje?”
“Wamesema wanataka kumjua muuaji, sijui kama ataweza kupatikana.”
Tamko la Marekani walilokuwa wamelitoa likaanza kuwa gumzo, kila mtu alilizungumzia kitu ambacho kwa kiasi kikubwa kikaleta hofu katika serikali ya Tanzania. Magazeti yakaandika sana kuhusu agizo hilo lililotakiwa kufanyiwa kazi mara moja na ripoti kutolewa.
“Mmesikia kilichosemwa?” aliuliza kamanda wa jeshi la polisi, bwana Kizota.
“Tumesikia.”
“Tunahitaji kumpata huyu mtu, iwe isiwe, ni lazima apatikane. Naliacha jukumu hili kwenu, nataka ndani ya siku mbili, muuaji ajulikane, na ndani ya wiki moja, muuaji huyo apatikane! Mmenielewa?” aliuliza kamanda Kizota.
“Tumekuelewa mkuu.”
Taarifa zikapelekwa mpaka katika kitengo cha upelelezi, TISS (Tanzania Internal Security Service) ambapo huko wakaandaa watu wawili kwa ajili ya kupeleleza na kujua ni mahali gani mtu huyo alipokuwa.
Mtu mmoja miongoni mwa wale waliokuwa wamechaguliwa aliitwa Martin Subian, alipewa jukumu la kumjua mtu huyo, alikuwa akiishi wapi na mtu wa pili ambaye naye alichaguliwa katika jukumu hilo la kumtafuta muuaji alikuwa ni Mathias Jonathan, kazi yake kubwa ilikuwa ni kumpata mtu huyo na kumtia nguvuni.
Siku iliyofuata, asubuhi na mapema Martin akaanza safari ya kuelekea chuo kikuu kwa lengo la kupata taarifa zote zilizokuwa zikimhusu mtu huyo, alikuwa nani, alikuwa katika eneo gani alipokuwa akimpiga risasi bwana Mickey na kwa nini alifanya hivyo.
Alipofika chuoni, moja kwa moja akaunganisha mpaka kwa Professa Ahmed Mitimingi na kuanza kuzungumza naye. Kwa kumwangalia Martin, hakuonekana kama alikuwa kijana shupavu, mwenye nguvu, alionekana kuwa hohehahe ambaye hata kama ungemuona basi ungeweza kusema kwamba una uwezo mkubwa wa kupambana naye na ukampiga.
“Ninaitwa Martin Subian kutoka TISS,” alisema Martin huku akitoa kitambulisho chake na kumkabidhi Professa Mitimingi. Akakichukua na kukiangalia, aliporidhika, akamtaka kuendelea kuzungumza.
“Ninataka kufahamu eneo alilouliwa bwana Mickey,” alisema Martin.
“Hakuna tatizo, twende.”
Wawili hao wakainuka na kutoka nje, hakukuwa na mtu aliyegundua kwamba mtu aliyekuwa akiongozana na Profesa Mitimingi alikuwa mtu hatari kwa kupambana na watu hata kama walikuwa watano.
Alionekana nadhifu, suti nyeusi lakini kiunoni alikuwa na bunduki iliyofichwa ambapo kama hali ingechafuka bunduki hiyo ingeingia katika matumizi wakati wowote ule. Hawakuchukua muda mrefu, wakafika uwanjani hapo.
“Hapa ndipo alipouawa.”
“Sawa. Jukwaa lilikuwa wapi na aligeukia wapi?” aliuliza Martin.
“Twende nikupeleke jukwaa lilipokuwa.”
Wakaendelea kupiga hatua mpaka sehemu kulipowekwa jukwaa lile, bado alama za vyuma vilivyokuwa vimechimbwa kwa chini zilionekana. Martin akasimama sehemu ile na kuangalia upande ambao bwana Mickey alikuwa akiangalia.
Muda wote huo Martin alikuwa kimya, alikuwa akiangalia huku na kule huku akionekana kujifikiria kitu. Kichwa chake kikianza kuivuta picha ya bwana Mickey, aliikumbuka vilivyo kwamba risasi ilipenya katika paji lake la uso na kutokea kichogoni.
Alisimama usawa mzuri na kuanza kuangalia sehemu ambayo ilikuwa ni nyepesi kwa mpigaji kupiga risasi ile.
“Bunduki iliyotumika ni Rifle yenye uwezo mkubwa wa kumpiga hata mtu aliyekuwa umbali wa mita mia mbili, ni bunduki iliyotengenezwa nchini Urusi ambayo mara nyingi hutumiwa na watu watunguaji wajulikanao kama snipers,” alisema Martin huku akiangalia kila kona maeneo hayo.
“Umejuaje?”
“Hakuna bunduki inayoweza kupiga umbali mrefu kama Rifle, hii ni bunduki iliyotengenezwa mahususi kwa ajili ya maadui wanaokaa kwa umbali mkubwa, na hii ndiyo iliyotumika mahali hapa,” alijibu Martin.
“Kulikuwa na watu wengi mahali hapa, sasa inawezekana vipi mpigaji kuwa karibu na mlengwa?”
“Mpigaji alikuwa mbali na ndiyo maana nilisema alitumia bunduki hii kwa kuwa ilikuwa na uwezo wa kupiga kitu kilichokuwa hata umbali wa mita mia mbili. Kama bwana Mickey alisimama hapa na kupigwa risasi upande huu, ina maana mpiga alisimama kule,” alisema Martin.
“Mmh! Huku kote kulijaa watu!”
“Najua, atakuwa alisimama kule porini. Unapaona?”
“Napaona, ila sidhani.”
“Twende nikuonyeshee.”
Wakatoka mahali hapo na kuelekea katika kichaka kilichokuwa umbali wa mia mia moja. Baadhi ya wanachuo walikuwa wakiwaangalia tu. Kila walipokuwa wakipiga hatua, waliwafuatilia kwa ukaribu pasipo kujulikana.
Prosefa Mitimingi na Martin wakafika katika kichaka kile kile kidogo na kuingia ndani. Martin akasimama na kuanza kuangalia kule kulipowekwa jukwaa, alipaangalia kwa umakini, alipoona amekosea, akasimama pembeni kidogo, alipoona hajakaa sawa, akaelekea pembeni kidogo mpaka alipojiona amekaa sawa na sehemu ile aliyosimama bwana Mickey kule jukwaani.
“Mpigaji alikuwa mahali hapa,” alisema Martin maneno yaliyomfanya Profesa Mitimingi kushtuka.
“Umejuaje?”
“Subiri.”
Martin akainama chini na kuanza kuyaangalia majani vizuri. Hali ya utofauti ilionekana katika majani yale. Majani ya upande mwingine yalikuwa yamesimama lakini majani ya pale alipokuwa ameinama yalikuwa yamelala kuonyesha kwamba kulikuwa na mtu aliyalalia.
“Unaona...majani yamelala, kuna mtu alikuwa mahali hapa, bila shaka ndiye huyo muuaji,” alisema Martin.
“Mmmh.”
“Subiri.”
Martin akaanza kutafuta kitu mahali pale, hakutulia, kila wakati alikuwa akipekua huku na kule, alionekana kuwa bize kupita kawaida. Wala haukuchukua muda mrefu, akakuta ganda la risasi likiwa mahali hapo, akalichukua na kuanza kuliangalia, Professa Mitimingi alikuwa kimya akimwangalia.
“Nini hicho?”
“Hili ni ganda la risasi, lisome lilivyoandikwa,” alisema Martin huku akimpa ganda lile na kuliangalia, liliandikwa Rifle 07T, bunduki kali iliyotoka nchini Urusi.
Kila kitu alichokuwa akikisema Martin mahali pale, Professa Mitimingi alikuwa akishangaa na kujikuta akimkubali kijana huyo kwamba alitoka TISS. Waliendelea kukaa kule huku akiambiwa vitu vingi, baada ya hapo, wakarudi ofisini.
“Nadhani nimekuonyeshea mengi na kukufundisha mengi, nahitaji kitu kimoja kutoka kwako,” alisema Martin.
“Kitu gani?”
“Kumjua mtu aliyepiga risasi hiyo.”
“Mmmh! Ni vigumu kufahamu.”
“Ulikuwepo wakati wa tukio?”
“Ndiyo! Nilikuwepo.”
“Hukumuona?”
“Hapana, sikumuona.”
“Hapana! Hebu vuta kumbukumbu, kumbuka vizuri, kumbuka kuanzia mwanzo mpaka mwisho,” alisema Martin.
“Kweli sikuweza kumuona.”
“Hapana. Hebu jaribu kukumbuka, vuta picha, kumbuka kuhusu kichaka kile, jaribu kukumbuka, nahisi nitapata picha. Kumbuka vizuri.”
Profesa Mitimingi akabaki kimya, ni kweli alijitahidi kuvuta picha zaidi, kila alipokuwa akikumbuka, hakukumbuka kumuona mtu kama huyo.
“Unasema ulikuwa jukwaani?”
“Ndiyo!”
“Hebu kumbuka vizuri, hakuna mtu aliyekwenda kule kichakani? Kumbuka, vuta kumbukumbu,” alisema Martin.
Prosessa akabaki kimya, alionekana kujifikiria kitu. Alijitahidi kukumbuka kila kitu kilichotokea siku ile katika uwanja ule. Alivuta kumbukumbu, alizivuta zaidi na zaidi mpaka akaonekana kushtuka.
“Mmmh!” alibaki akiguna.
“Niambie umekumbuka nini.”
“Kuna mtu alikwenda katika pori lile kukojoa, namkumbuka sana, alikuwa akiishikashika zipu ya suruali yake, mgongoni alibeba begi,” alisema Professa.
“Unamfahamu mtu huyo?”
“Mmmh! Hapana.”
“Bado! Jaribu kukumbuka.”
“No! Kuna mtu nilimuona akielekea kule, lakini sikuwa nikimfahamu kabisa, nilipomuona akiishikashika zipu ya suruali yake, niligundua kwamba alitaka kukojoa, nilitaka kumtuma mtu akamwambie kwamba hairuhusiwi kukojoa vichakani, sasa sijui kwa nini nilipuuzia,” alisema Professa Mitimingi.
“Umesema alibeba begi, alibeba begi rangi gani?”
“Lilikuwa jekundu, sikumbuki lilikuwa la aina gani.”
“Sawa. Kidogo maelezo yako yanaweza kufaa. Alivaa nguo za aina gani?’
“Nakumbuka ilikuwa jinzi nyeusi na fulana nyekundu.”
“Hivyo tu?”
“Hapana, alikuwa na kofia nyeupe,” alijibu professa.
“Sawa.
Professa akabaki akijiuliza, ni kwa jinsi gani Martin alikuwa amemwambia akumbuke kitu fulani mpaka kumfahamu mtu aliyeingia ndani ya kichaka kile na wakati hakuwa akikumbuka kitu chochote kile, mpaka hapo, alijipa uhakika kwamba mtu aliyesimama mbele yake alikuwa hatari sana na hakuwa na mchezo hata kidogo.
“Umejuaje kama ningeweza kukumbuka?”
“Hakuna siri. Kwenye tukio lolote linalotokea jukwaani, wale watu waliokaa mbele ambao wanawaona watu wengi, ni lazima muuaji au mtu aliyefanya tukio fulani walikuwa wakimuona ila walimpuuzia, ndiyo inavyotokea kila siku. Hata ukimfuata mtu mwingine aliyekuwa jukwaani siku ile, atakwambia kwamba alimuona ila alipuuzia na ndicho kilichotokea kwako!” alisema Martin.
“Mmmh! Ni hatari sana. Kwa hiyo nini kinafuata?”
“Kumtafuita mtu huyo aliyevalia jinzi nyeusi, begi jekundu na kofia nyeupe.”
“Tunampataje?”
“Ni kazi nyepesi sana. Ila jua huyo mtu si Mtanzania.”
“Mmmh!”
“Ndiyo. Kwa sisi Watanzania hakuna mtu anayeweza kuitumia Rifle vizuri mpaka awe komandoo, ni moja ya bunduki zinazosumbua sana. Kama umeona mtu kaitumia na mpigo mmoja tu aliweza kumuua mhusika, jua huyo si Mtanzania, atakuwa mtu wa nje ya Tanzania, na kama ni Mtanzania, jua kwamba atakuwa komandoo kitu ambacho hakiniingii akilini,” alisema Martin.
“Mmmh! Sasa utampata vipi?”
“Ni kitu chepesi sana, kama kumsukuma mlevi mlimani, usiwe na wasiwasi, nataka kuonana na rais wa chuo hiki,” alisema Martin.
“Unadhani atakusaidia?”
“Ndiyo. Asilimia mia moja.”
“Hakuna tatizo.”

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA PILI


Ilikuwa saa 11 jioni, Ndege ya Shirika la Ndege la British Airlines ilikuwa ikitua katika Uwanja wa Kimataifa wa Julius Nyerere uliokuwa jijini Dar es Salaam. Ndege hiyo iliposimama, abiria wakaanza kuteremka na miongoni mwa abiria hao alikuwepo Victor, mtoto wa marehemu Mickey.
Victor akaanza kupiga hatua kuelekea katika sehemu ya jengo la uwanja huo na kisha kuelekea katika sehemu ya kuchunguzia mizigo, akaliacha begi lake na lilipopita katika mashine maalumu ya kuchunguzia mizigo na kuonekana hakuwa na tatizo lolote lile, akalichukua na kuondoka nalo.
Mwendo wake ulikuwa ni wa taratibu, alipofika nje ya jengo hilo, akachukua teksi na kuondoka nayo kuelekea hotelini. Kichwa chake kilikuwa na mawazo lukuki, kila alipokuwa akiwafikiria wazazi wake, hakupata jibu.
Alikumbuka kuwa walimwambia kwamba wangewasiliana katika kipindi atakachokuwa ameshuka kutoka kwenye ndege lakini kitu cha ajabu, kila alipokuwa akiwapigia simu, hawakuwa wakipatikana.
Hakujua ni kitu gani kilichokuwa kimetokea, lakini hakutaka kujipa kazi kubwa ya kufikiria sana, yote hayo, hakuona kama kulikuwa na tatizo lolote lile, alikuwa na uhakika kwamba angewasiliana nao.
“Where to, my brother?” (Unaelekea wapi kaka yangu?) aliuliza dereva teksi kwa lugha ya kihuni.
“Take me to Serena Hotel,” (Nipeleke katika Hoteli ya Serena) alisema Victor, dereva akapiga gia na kuanza kuelekea huko.
Walichukua dakika arobaini mpaka kufika katika hoteli hiyo ambapo Victor akateremka na kuanza kuelekea katika sehemu ya mapokezi, akalipia kiasi cha fedha kilichohitajika, akapanda lifti na kuanza kuelekea katika chumba alichoelekezwa.
Kila wakati kichwa chake kilikuwa kikiwafikiria wazazi wake, baada ya simu zao kutokupokelewa kwa kipindi kirefu, sasa hivi hazikuwa zikipatikana kabisa. Alichokifanya ni kupumzika kwa kuamini kwamba baadae angeweza kuwatafuta kwa mara nyingine.
Ilipofika saa kumi na mbili jioni, akasikia simu yake ikiwa imelia mlio mfupi uliomaanisha kwamba kuna ‘breaking news’ ilikuwa imetumwa kutoka katika Kituo cha Habari cha CNN ambacho alikuwa amejiunga nacho.
Hakutaka kuifuata simu yake, alibaki kitandani pale huku akionekana kuwa mwingi wa mawazo. Baada ya kuhisi kwamba kulikuwa na umuhimu wa kuiona habari hiyo ilihusu nini, akaamka na kuanza kuifuata simu yake, alipoifikia, akaichukua na kukiangalia kioo cha simu hiyo.
‘POTTER MICKEY HAS BEEN KILLED IN TANZANIA’ (POTTER MICKEY AUAWA NCHINI TANZANIA) ilisema sehemu ya taarifa hiyo huku ikiwa imeambatanishwa na picha ya bwana Mickey.
Victor akahisi kutetemeka, hakuamini kile alichokuwa akikisoma, akaliangalia jina lile vizuri, aliporidhika nalo, akayaamisha macho yake na kutazama picha iliyokuwa imeambatanishwa na taarifa ile, alikuwa baba yake mzazi.
Moyo wake ukashindwa kuvumilia, ghafla, machozi yakaanza kumbubujika mashavuni, hakutaka kuendelea kubaki mahali hapo, akatoka chumbani mule.
Hoteli ilikuwa na lifti lakini hakutaka kuitumia, aliona kama zingemchelewesha, alichokifanya ni kuanza kuteremsha ngazi, tena kwa kasi. Mwendo wake ulikuwa wa harakaharaka, alijiona akichelewa kufika chini, moyo wake ulikuwa kwenye maumivu makali kwani hakutegemea kupokea taarifa kama ile aliyokuwa ameipokea.
Alipofika chini, hakutaka kusimama, akatoka nje ya hoteli hiyo na kuifuata moja ya teksi zilizokuwa eno hilo na moja kwa moja kuingia.
“Take me to University of Dar es Salaam,” (Nipeleke katika Chuo cha Dar es Salaam)
“Thirty thousand shillings bro,” (Shilingi elfu thelathini kaka)
“No problem” (Hakuna tatizo) alisema Victor.
Bado alionekana kuchanganyikiwa, kichwa chake kilimzunguka na kujiona akikaribia kuwa kichaa, taarifa aliyokuwa ameipata kwamba baba yake kipenzi alikuwa ameuawa ilikuwa imemchanganya mno.
Hawakuchukua muda mrefu wakafika katika eneo la chuo hicho. Katika kila kona watu walikuwa wakilizungumzia tukio hilo ambalo halikuwahi kutokea kabla chuoni hapo. Hakujua amuulize nani, akajikuta akipiga hatua mpaka katika Jengo la Utawala na kupandisha juu.
“Samahani,” alisema Victor, alikuwa amemsimamisha mwanachuo mmoja.
“Bila samahani.”
“Nimepata taarifa kuna mtu alipigwa risasi leo hii mahali hapa, ni kweli?”
“Ndiyo! Kuna Mzungu alikuja kwa ajili ya masomo ya ujasiriamali, bahati mbaya kapigwa risasi,” alijibu jamaa yule.
“Kapigwa risasi wapi?”
“Hapa kichwani.”
“Hapana, namaanisha eneo gani.”
“Kule uwanjani.”
“Unaweza kunipeleka?”
“Hakuna tatizo. Twende!”
Wakaanza kuondoka mahali hapo, bado Victor alionekana kutokuwa sawa. Mwendo wao ulikuwa wa harakaharaka, bado watu walikuwa wakilizungumzia tukio lile lililotokea kipindi kifupi kilichopita. Walipofika uwanjani, kwa haraka Victor akaanza kukimbia kuelekea katika jukwaa lile, bado damu zilikuwa mahali pale, alipofika katika eneo hilo, akajikuta akipiga magoti na kuanza kulia.
Wanachuo wote wakaanza kumwangalia, alionekana kuwa na majonzi kupita kawaida, kwa muonekano wake, kila mmoja akagundua kwamba mtu huyo alikuwa na undugu na marehemu Mickey lakini hawakujua kama alikuwa mtoto wake.
Wanachuo waliokuwa mbali wakaanza kumsogelea, walipomfikia, wakamzunguka na kuanza kumwangalia vizuri.
“Pole sana...” alijikuta akisema mwanachuo mmoja.
Victor hakuitikia kitu, alichokifanya, ni kuondoka mahali hapo huku akionekana kuwa na hasira mno.
Alichokifanya Victor ni kuwauliza wanachuo kuhusu tukio zima lilivyokuwa. Alipohadithiwa, akawaomba wampeleke katika hospitali aliyolazwa mama yake, baadhi ya wanachuo wakampeleka huko huku moyo wake ukiwa na machungu mno.
“Nitampata tu muuaji, nitampata tu,” alisema Victor huku akiuma meno yake kwa hasira.
****
“Ninahitaji kufahamu kitu kimoja, kuna wanafunzi wangapi kutoka nje ya nchi?” aliuliza Martin huku akimkazia macho rais wa chuo hicho, Ibrahim.
“Wapo wengi sana.”
“Wangapi?”
“Kwa kweli idadi yao kamili siifahamu.”
“Sawa. Kuna mwanafunzi mmoja namtafuta.”
“Yupi?”
“Mwanachuo anayependa kubeba begi jekundu na kupendelea kuvaa kofia nyeupe, unamfahamu?”
“Mhh! Wapo wengi wanaovaa hivyo.”
“Lakini bahati nzuri si kwa wenyeji.”
“Kivipi?”
“Kuna mgeni mmoja alikuwa akipendelea kubeba begi hilo na kuvaa kofia hiyo, haumfahamu?”
“Kiukweli simfahamu.”
“Sawa.”
Martin hakutaka kupoteza muda ndani ya ofisi ya rais huyo, alichokifanya ni kuaga na kuondoka. Kichwa chake kilikuwa na mawazo lukuki, alijua fika kwamba mbele yake kulikuwa na mtihani mkubwa lakini hakutaka kuona akikubali kushindwa kirahisi, alichokifanya kwa wakati huo ni kuwasiliana na mkuu wa TISS na kumwambia kile kilichokuwa kimeendelea.
“Rudi, kuna jambo jingine la maana tutalifanya, hili ni siri na hakuna mwanachuo yeyote anayelifahamu, muuaji tutampata tu,” alisema mkuu wa TISS, Bwana Godson Materu.
“Sawa.”
Martin akarudi mpaka ofisini kwake huku akiwa na ripoti kamili juu ya kile kilichokuwa kimeendelea. Hakujisikia furaha, hakufurahia kujiona akishindwa kazi aliyopewa na wakuu wake kuifanya, kutokumpata muuaji siku hiyo kulimhuzunisha kiasi kwamba hata kula hakuweza kula.
“Usijali, hii ni kazi kubwa, wewe ishia hapa, huku kulipobakia, tumuachie Mathias,” alisema bwana Materu.
“Mkuu!”
“Unasemaje?”
“Samahani kama nitakuwa nakuingilia kazi yako!”
“Usijali, kuna nini?”
“Nimeanza kuifanya hii kazi kwa kipindi kirefu mno, naomba unipe jukumu la kuianza kazi ya kumtafuta huyu muuaji, najua ni kazi ngumu lakini nakuahidi kwamba nitaikamilisha, haijalishi ni kipindi kirefu namna gani nitachukua,” alisema Martin.
“Una uhakika utaiweza?”
“Nakuahidi hilo. Huu ni mwanzo na ndiyo maana umekuwa mgumu sana kwangu, ila nakuahidi nitaiweza.”
“Sawa. Sisi tutakusaidia kuipata picha ya muuaji, baada ya hapo, kumtafuta na kumtia nguvuni itakuwa kazi yako!”
“Nitashukuru mkuu. Vipi kuhusu Wamarekani?’
“Hali imekuwa mbaya, wamechachamaa mno, sikuwahi kuwaona wakichachamaa kiasi hiki, mbaya zaidi, hata majasusi wao wa CIA wameingilia kati kwa kusema kwamba kama tumeshindwa kumpata muuaji kwa uzembe wetu, waje kuifanya kazi hiyo wao wenyewe.”
“Hakuna kitu kama hicho, hatujashindwa, wakiwaambieni tena, waambie kwamba kijana wenu yupo kazini, ndani ya kipindi kichache, muuaji atapatikana.”
“Nakuamini, ila kama ukishindwa?”
“Nakuahidi sitoshindwa, nitataka kuifanya kazi hii kwa uwezo mkubwa,” alisema Martin.
Hakutaka kuona kazi hiyo ikipotea bure huku akiwa ameshindwa kumpata muuaji huyo. Alikuwa tayari kufanya kitu chochote kile lakini mwisho wa siku muuaji huyo apatikane.
Alijua kwamba lilikuwa jambo gumu mno kupatikana lakini moyo wake ulimwambia kwamba alikuwa na uwezo mkubwa sana wa kumpata muuaji huyo hivyo asonge mbele zaidi.
Hiyo ikawa furaha kwake, aliuamini uwezo wake, alitaka kuikamilisha kazi hiyo kwa kipindi kifupi kijacho, ila kabla hajaingia kazini kwa kazi maalumu, akataka kuonana na mke wa marehemu, Elizaberth, hapo ndipo alipoona kufaa kuanzia, aliamini kupitia mwanamke huyo, angeweza kugundua mambo mengi.
“Huyu ndiye wa kwanza kuonana naye, ngoja nimfuate hospitalini,” alisema Martin huku akiwa amepania kuifanya kazi hiyo kwa uaminifu mkubwa.

Victor alibaki akiwa na majonzi tele, alifika hospitalini lakini akazuiliwa kuingia ndani kumuona mama yake ambaye aliambiwa kwamba alipoteza fahamu mara baada ya kifo cha mume wake. Moyo wake ulikuwa kwenye maumivu mazito yasiyoweza kusimulika.
Alibaki kitini huku akimuomba Mungu kwamba kila kitu kilichokuwa kikitokea kiwe ndoto na si maisha halisi aliyokuwa akiishi duniani. Hakuweza kubadilisha kitu, ukweli uliendelea kubaki palepale kwamba baba yake alikuwa ameuawa.
“Niambie nini kinaendelea,” Victor alimwambia daktari wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Dk. Kimario.
“Subiri kwanza.”
“Nitasubiri vipi na wakati sijajua hali anayoendelea nayo mama, niambie kwanza,” alisema Victor.
“Subiri, usiwe na presha.”
Ikambidi Victor awe mpole kitini. Kama kulia, alikuwa amelia kwa kipindi kirefu lakini hakukuwa na kitu chochote kilichobadilika, kuna wakati alimuomba Mungu kwamba ilikuwa ni bora na yeye amchukue kama amemchukua baba yake lakini kuna kipindi alimuomba Mungu kutokufanya hivyo mpaka atakapomkamata muuaji wa baba yake.
Aliendelea kubaki kitini pale mpaka ilipofika saa tatu usiku alipoambiwa kwamba alikuwa na mgeni aliyetaka kumuona na kuzungumza naye mawili matatu, hakupinga, akakubali kuonana naye.
Mgeni huyo alikuwa Martin, alifika hapo, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumpa pole kwa kila kitu kilichokuwa kimetokea, baada ya hapo akaanza kuzungumza naye.
“Ninataka kumuona mama yako,” alisema Martin.
“Bado hawaruhusu mtu yeyote kuingia ndani, wewe nani?” aliuliza Victor.
“Ninaitwa Martin.”
“Unahusika na nini na kwa nini unataka kumuona mama yangu?” aliuliza Victor.
“Ninahitaji kusaidia.”
“Kusaidia nini?”
“Kumkamata muuaji.”
“Hilo niachie mimi, nitamkamata tu.”
“Umkamate wewe?”
“Unanionaje? Acha, nitamkamata kwa mkono wangu, na nitamuua kama kisasi kwa baba yangu,:” alisema Victor.
“Naomba nikuulize swali moja.”
“Uliza.”
“Hivi unajua kwa nini baba yako aliuawa?”
“Hapana.”
“Nahisi kuna kitu, sijajua kimeanzia wapi ila nahisi kuna kitu.”
“Kitu gani?”
“Hapo ndipo upelelezi wangu utakapoanzia, tukifanikiwa kujua sababu, basi muuaji atapatikana, hatuwezi kumpata muuaji kabla ya kujua sababu iliyopelekea kifo chake,” alisema Martin.
Martin alijaribu kuzungumza na Victor na kumwambia mipango yake kabambe ambayo alikuwa njiani kuifanya. Hakutaka kumficha japokuwa hakuruhusiwa kufanya hivyo. Mtu pekee ambaye angewezesha kukamatwa kwa muuaji huyo alikuwa Victor na mama yake.
Kichwa chake kilimwambia kwamba kulikuwa na kitu ambacho kilipelekea kifo cha bwana Mickey kwani alimini kwamba hakukuwa na mtu ambaye angeamua kufanya mauaji tu bila kuwa na sababu.
Mbali na hivyo, akaanza kumfikiria bosi wake ambaye alimwambia kwamba angempa mwanzo wa kuanzia kazi yake. Ugumu mkubwa ulikuwa mbele yake, japokuwa alifika mahali hapo kwa ajili ya kuhitaji msaada lakini kuna kipindi alifikiria kwamba hiyo haikutosha, kulikuwa na sehemu nyingine ya kuanzia.
Waliendelea kusubiri mpaka bi Elizabeth aliposhtuka kutoka katika usingizi wa kifo. Akaanza kuangalia huku na kule, hakujua ni mahali gani alipokuwa lakini baada ya kuona dripu ya maji ikining’inia juu yake, akagundua kwamba mahali alipokuwa kulikuwa ni hospitali.
“Mickey!” alijikuta akiita.
Hapo ndipo kumbukumbu zake zilipoanza kurudi, akaanza kukumbuka kila kitu kilichokuwa kimetokea toka mume wake kipenzi alipopigwa risasi mbele ya macho yake na kufariki dunia.
Kila kitu kilichokuwa kikijirudia kichwani mwake kilikuwa kama filamu aliyokuwa akiitazama mbele yake, hakuamini kama mume wake ambaye alikuwa akimpenda, leo hii hakuwa naye, alikuwa ameuawa katika kifo kibaya cha kupigwa risasi.
Kikaanza kilio cha kwikwi na mwisho wa siku kulia kwa sauti kubwa. Maumivu ya moyo wake hayakupungua, kadiri muda ulivyozidi kwenda mbele na kukumbuka kile kilichokuwa kimetokea, aliendelea kuumia zaidi.
Baada ya dakika kadhaa, mlango ukafunguliwa na Dk. Kimario kuingia huku akiwa ametangulizana na watu wawili, mmoja alikuwa mtoto wake, Victor na mtu mwingine hakuwa akimfahamu. Alipomuona Victor tu, akaanza kulia.
Mtoto wake alimkumbusha marehemu mume wake, walifanana kwa kila kitu kiasi kwamba kadiri alivyokuwa akimtazama, alimkumbuka mume wake zaidi.
“Victor...bab...a ya...ko wam...emu...ua...” alisema bi Elizabeth huku akilia kama mtoto.
“Nyamaza mama, tutampata muuaji tu,” alisema Victor, naye machozi yakaanza kumtoka kwa mara nyingine tena.
Hakukuwa na wa kumbembeleza mwenzake, kila mmoja alikuwa akilia kwa uchungu mkubwa. Martin alibaki akiwaangalia, japokuwa alikuwa mwanaume shupavu mwenye moyo wa kikatili, naye akajikuta akibubujikwa na machozi, picha aliyokuwa akiiona ilimtia uchungu mno.
“Ni lazima nimpate muuaji,” alijisemea Martin.
Wala hakukaa sana mahali hapo, simu yake ya mkononi ikaanza kusikika ikiita, alichokifanya ni kutoka ndani ya chumba kile na kuelekea nje, mpigaji alikuwa bosi wake, bwana Godson ambaye akamtaka afike moja kwa moja mpaka ofisini kwake, hivyo akaaga na kuahidi atarudi kesho.
Hakuchukua muda mrefu, akafika ofisini hapo ambapo moja kwa moja akaanza kuelekea katika chumba cha bosi wake ambaye akamuweka kitini.
“Kila kitu tumekamilisha, muuaji amejulikana, kazi kwako kwenda kumkamata,” alisema bwana Godson.
“Mmmh! Muuaji amepatikana?”
“Ndiyo! Picha yake hii hapa,” alisema bwana Godson na kumpa picha ambayo Martin akaanza kuiangalia vizuri, akaonyesha mshtuko.
“Haiwezekani!”
“Ndiyo hivyo! Huyo ndiye muuaji wetu. Hakikisha anapatikana.”
“Lakini bosi, kweli Gideon anaweza kuwa muuaji?”
“Ndiyo! Hakikisha anapatikana.”
“Lakini unakumbuka kwamba huyu ni kipofu?”
“Najua hilo.”
“Sasa toka lini kipofu akaua tena kwa kumlenga mtu na bunduki akiwa mbali?”
“Hata sisi hatufahamu, cha msingi mtafute, kuna mengi ya kufahamu. Tunataka kujua zaidi huyu ni nani na kwa nini aliua. Usiuangalie upofu wake, kesho rudi chuoni ukamtafute, ukimkamata, mtie nguvuni,” alisema bwana Godson, Martin akaondoka huku akionekana kuchanganyikiwa, kumkamata kipofu na kumleta mbele ya chombo cha sheria, kwake ilionekana kuwa kitu kigumu, ila kwa sababu aliambiwa afanye hivyo, hakuwa na ubishi.
“Nitamkamata hiyo kesho, tena kwa sababu ni kipofu, hakuna tatizo,” alisema Martin huku akiondoka mahali hapo kurudi nyumbani kwake, kwani tayari ilikwishatimia saa teno usiku.

Wanachuo kutoka sehemu mbalimbali duniani walikuwa wakivutiwa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kutokana na elimu bora iliyokuwa ikitolewa. Sifa mbalimbali za chuo hicho kuanzia mandhari na vitu vingine ikiwepo elimu bora ndivyo vilivyowakusanya watu wengi kutoka sehemu mbalimbali na kuja kusoma katika chuo hicho.
Kulikuwa na wanachuo kutoka Afrika Kusini, Malawi, Msumbiji na sehemu nyingine, na si nchi hizo tu bali hata wanachuo kutoka katika baadhi ya nchi za Ulaya walikuwa wakija chuoni hapo kwa ajili ya kupokea elimu bora.
Kutokana na wingi mkubwa wa watu waliokuwa wakikusanyika chuoni hapo tena kutoka katika nchi mbalimbali, serikali ya Tanzania ikaanza kuhofia, ikaogopa kuingiliwa na kukifanya chuo hicho kuwa mlango wa ugaidi ambao ungeweza kutokea nchini hapa na hivyo kufanya uamuzi wa kuweka kamera ndogo zijulikanazo kama CCTV kwa ajili ya kuangalia kila kitu kilichokuwa kikiendelea chuoni hapo.
Kamera hizo za siri zilikuwa na kazi moja, kuangalia mandhari ya chuo hizo sehemu mbalimbali bila mtu yeyote kufahamu.
Kamera pekee zilizokuwa zikionekana zilikuwa zile zilizowekwa madarasani ambapo wanachuo wengi wakafikiri kwamba zilikuwa zikiwachunguza kila walipokuwa wakifanya mitihani kitu ambacho hakikuwa sahihi.
Katika sehemu kama kwenye miti, sehemu za kulia vyakula, vituoni na sehemu nyingine, kuliwekwa kamera ndogo zilizokuwa na nguvu ambazo hazikuwa zikionekana kwa wanachuo chuoni hapo na hata maprofesa hawakuwa wakikijua hicho.
Kamera zilifungwa usiku na asubuhi iliyofuata, kila kitu kilikuwa hewani. Picha zilizokuwa zikionekana chuoni hapo, zilikwenda moja kwa moja katika kompyuta za TISS zilizokuwa makao makuu na kuanza kukifuatilia chuo hicho na kuangalia mipango yote iliuyokuwa ikifanywa na wanachuo bila kujua.
Walifahamu mengi, kupitia kamera hizo, wakabaini wanachuo wengi waliokuwa wakifanya mapenzi porini na hata mabwenini, kila uchafu uliokuwa ukifanyika chuoni, walikuwa wakiuona lakini hawakutaka kujali, kile walichokuwa wakikitaka ni kuhakikisha kwamba ulinzi unakuwa wa kutosha.
Siku zikaendelea kukatika, wanachuo wengi kutoka katika nchi mbalimbali waliendelea kumiminika chuoni hapo. Baada ya kipindi cha muda mrefu toka kamera ziwekwe chuoni hapo kisiri, akahamia mwanachuo mmoja kutoka Malawi, mwanachuo aliyewachanganya watu wengi, mwanachuo wa kiume aliyekuwa kipofu, huyu aliitwa Gideon Mutinyama.
Watu wakaanza kujiuliza maswali mengi kuhusiana na kipofu huyo aliyekuwa na uwezo wa hali ya juu. Kila alipokuwa akikaa, pembeni kulikuwa na fimbo yake huku macho yake yakiwa yamefunikwa na miwani miyeusi ya jua.
Hakusoma vitabu vya kawaida, vitabu vyake vilikuwa ni vile vilivyokuwa vikitumiwa na vipofu ambavyo havikuandikwa kitu chochote zaidi ya kuwekwa nukta tu. Watu walimshangaa Gideon, hakuwa mtu wa kupiga stori na watu lakini baada ya kuishi kwa kipindi cha miezi minne, akajikuta akiwa rafiki wa watu wengi.
Uwezo wake wa darasani haukuwa mdogo, kila mwanachuo akagundua kwamba mwanafunzi huyu alikuwa genius kwani katika kila somo alilokuwa akisomea, ilikuwa ni lazima kupata alama A katika kila mtihani.
“Huyu Gideon ni mtu hatari sana, nasikia kakimbiza vibaya mpaka Professa Abdul ameona noma,” alisikika kijana mmoja.
“Acha masihara.”
“Ndiyo hivyo kaka.”
“Si ndiye huyu kipofu! Au kuna Gideon mwingine?”
“Ndiye huyohuyo.”
“Mmmh!”
“Yaani ni noma, kila mtu anashangaa, sasa angalia vitabu vyake, nukta, nukta, nukta, hakuna herufi hata moja, ni nukta nukta na nukta,” alisema jamaa huyo.
Bado uwezo wake ulikuwa gumzo chuoni, watu wengi wakawa wakifika chuoni hapo, kitu cha kwanza kilikuwa ni kuomba kukutana na kijana huyo aliyekuwa akimshangaza kila mtu.
Alishinda na miwani huku fimbo ikiwa mkononi mwake na hata mara mojamoja alipokuwa akivua miwani yake, macho yake yalionyesha wazi kwamba alikuwa kipofu jambo lililowafanya watu wengi kumuonea huruma kutokana na hali aliyokuwa nayo.
Gideon akajikuta akianza kupata umaarufu, upofu wake ukamfanya kuanza kujulikana, katika kila kona ndani ya Jiji la Dar es Salaam walikuwa wakimzungumzia, vyombo vya habari vikamtangaza sana huku watu wakitumia nguvu zao nyingi kuandika mambo mengi kuhusu yeye katika mitandao ya kijamii.
Siku ziliendelea kukatika, bado wanachuo hawakuweza kugundua kwamba chuo kizima kilikuwa kimewekwa kamera ndogo ambazo zilikuwa ngumu kuonekana kwa mtu yeyote yule.
Hakukuwa na mtu aliyekuwa akifahamu kuhusu uwepo wa kamera zile ndani ya chuo kile kwani hata professa Mitimingi ambaye alikuwa akikiongoza chuo hicho kwa wakati huo hakuwa akifahamu kitu chochote, yaani alikuwa kama wengine.
“Samahani....” ilisikika sauti ya msichana mmoja, kwa muonekano alikuwa binti mrembo ambaye sura yake ilipendezeshwa na tabasamu pana. Alikuwa akiongea na Gideon.
“Bila samahani...” alisema Gideon huku akiangalia juu, kwa mtazamo wake ulivyokuwa, ungegundua kwamba mtu huyo alikuwa kipofu.
“Naweza kukaa na wewe na kuzungumza pamoja?”
“Usijali, bila shaka wewe ni Juliet.
“Waooo! Umenijuaje?”
“Sauti yako haiwezi kunipotea.”
“Ila hatukuwahi kuongea hata siku moja!”
“Lakini huwa ninakusikia ukiongea na marafiki zako! Hongera kwa kupendeza,” alisema Gideon.
“Hahaha! Nimependeza! Sasa wewe kipofu umenionaje?”
“Huwa tunaishi kwa hisia, tunaweza kugundua kitu chochote kile kuanzia rangi, muonekano, minong’ono na vingine vingi,” alijibu Gideon huku akipapasa huku na kule kutafuta fimbo yake.
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa ukaribu wa watu hao wawili, Juliet akaanza kuwa na Gideon huku kila wakati akimshikia fimbo yake hasa kila alipotaka kumuongoza barabarani.
Wawili hawa wakazua gumzo, msichana Juliet alikuwa kila kitu kwa Gideon, siku ambayo kijana huyo hakuisikia sauti ya msichana huyo, hakuwa na raha, alipenda kila wakati awe karibu naye jambo lililoonekana kumfurahisha sana Juliet.
Kupitia Juliet, watu ndiyo wakajua historia ya maisha ya Gideon, historia iliyomhuzunisha kila mtu kwamba katika kipindi ambacho mvulana huyo alizaliwa, alikuwa akiona kama watu wengine lakini alipofikisha umri wa miaka kumi, akamwagiwa sumu kali machoni mwake na mwanamke aliyekuwa akiishi naye na kumuita mama wa kambo.
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa upofu wake, watu hawakuamini kama kweli kulikuwa na wanawake waliokuwa na roho mbaya kama alivyokuwa mwanamke huyo. Japokuwa alikuwa kipofu, baadae ikagundulika kwamba Gideon alikuwa na uwezo mkubwa wa kufikiria na kufanya maamuzi yake, au kwa kifupi aliitwa genius.
Shuleni akawa mwiba, watu waliutambua uwezo wake kwa kiasi kikubwa. Kila mwalimu aliyekuwa akimfundisha alifurahia kupata mwanafunzi kama huyo ambaye alikuwa msaada mkubwa hata kwa wanafunzi wengine.
“Ikawaje baada ya hapo?” aliuliza Juliet.
“Nikaamua kumchukia mama wa kambo, aliyabadilisha maisha yangu kwa kiasi kikubwa, sikuweza kumuona kwani ilikuwa ni lazima nimuue kwa kile alichonifanyia,” alisema Gideon.
Mambo yote hayo Juliet alikuwa amehadithiwa na kijana huyo aliyemwambia ilikuwa ni lazima iwe siri lakini Juliet hakuweza kukubali, kila alipokuwa akikaa, siri ile ilikuwa ikimfurukuta moyoni mwake na mwisho wa siku kujikuta akiizungumza kwa marafiki zake.
“Halafu eti mnasema nyie wanawake mna roho nzuri, si mmemsikia mwenzenu amemuharibia mtoto wa watu maisha yake, kumbe mimi kuwachukia nyie wapumbavu sawasawa tu,” alisema mwanachuo mmoja.
“Hiyo ni hulka ya mtu, haimaanishi kwamba wanawake wote wapo hivyo,” alisikika msichana mmoja.
Huyo ndiye alikuwa Gideon, kijana kipofu aliyemshangaza kila mtu chuoni hapo, kijana genius aliyekuwa akiongoza katika kila somo. Leo hii, bila kujua kitu chochote, mpelelezi Martin anaambiwa kwamba mtu aliyemuua mhamasishaji wa ujasiriamali kutoka Marekani, Potter Mickey kwa kumpiga risasi ya kichwa alikuwa Gideon.
Moyo wake haukuamini, alimfahamu Giodeon kuwa kama kijana kipofu, ilikuwaje ashike bunduki ya Rifle kwenye umbali wa mita zaidi ya hamsini na kisha kumlenga nayo mhamasishaji huyo wa ujasiriamali, kila alipofikiria, alikosa jibu, ila hakutaka kupuuzia, alitakiwa kufanya kama alivyoambiwa afanye, ilikuwa ni lazima arudi chuoni hapo na kumkamata Gideon.
“Sawa, ngoja niwaridhishe nirudi chuoni, ila, mmh! Sidhani kamaa kipofu yule aliweza kufanya mauaji hayo,” alisema Martin.

ITAENDELEA


CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA TATU

Kamera ndogo za CCTV ziliendelea kufanya kazi kila siku, wanachuo waliendelea kufanya yao pasipo kugundua kwamba asilimia tisini ya mambo waliyokuwa wakiyafanya chuoni serikali ilikuwa ikiyafuatilia.
Gideon, kijana aliyekuwa na akili kushinda wanachuo wote chuoni hapo hakujua kitu chochote kilichokuwa kikiendelea, ndani ya jengo kubwa la TISS, walikuwa wameweka umakini katika kukifuatilia chuo hicho kila siku.
“Mmm!”
“Nini?”
“Hivi huyu jamaa ni kipofu kweli?’
“Kwa nini umeuliza hivyo?”
“Kuna jambo lmetokea, nahisi kuna kitu.”
“Jambo gani?”
“Alikuwa akishuka ngazi vizuri bila kuweka fimbo yake, watu walipotokea, ghafla akabadilika na kuitanguliza fimbo yake.”
“Hahaha! Acha masihara bwana, huyu jamaa ni kipofu toka mwaka jana alipokuja ndani ya chuo hicho, halafu kingine, vipofu wote duniani huwa na hisia, anaweza akasikia sauti yako tu, akajua kwamba wewe mzuri au mbaya,”
Hayo yalikuwa mazungumzo yaliyokuwa yakiendelea ndani ya jengo hilo kubwa la upelelezi Tanzania. Mfuatiliaji aliyekuwa mbele ya kompyuta alikuwa akimwambia mwenzake aliyekuwa naye ndani ya chumba hicho juu ya Gideon aliyeonekana kufanya kitu cha tofauti.
Ilikuwa ni usiku na chuoni hakukuwa na watu wengi na hata wale waliokuwepo chuoni hapo, walikuwa bwenini mwao wamelala. Huo ndiyo muda ambao Gideon alionekana kuwa tofauti, wakati alipokuwa akishuka ngazi, alishuka ngazi kadhaa bila kutanguliza fimbo yake lakini mara baada ya kusikia wanachuo fulani wakija kule alipokuwa, akaichukua fimbo yake na kuendelea na mchezo wa kupapapasa.
Hilo lilimtia shaka mfuatiliaji mmoja, akalichukua suala hilo na kuwafikishia viongozi wa juu ambao nao wakaungana naye na kuanza kumchunguza Gideon.
Kwa muda wa mwezi mzima, waliendelea kumfuatilia kwa kumrekodi na kisha baadae kumtazama kwenye mikanda yao, lakini hawakuambulia kitu, dalili zote zilionyesha kwamba kijana huyo alikuwa kipofu.
“Au uliona vibaya?”
“Hapana, sikuona vibaya, nilikuwa makini.”
“Ilikuwa tarehe ngapi vile?”
“25 mwezi uliopita.”
“Hebu tafuta mkanda wa siku hiyo.”
Agizo likatolewa na Materu, mkanda wa siku hiyo ukatafutwa kwa lengo la kuangalia tukio lililotokea siku hiyo usiku. Kama alivyosema kijana yule, kilionekana kitu kilekile kwamba Gideon alifanya kama maelezo ya kijana yule yalivyosema.
“Inabidi tulichukulie suala hili kwa ukaribu zaidi,” alisema Materu.
Kumchunguza kwa mwezi mzima haukutosha, walichokifanya, wakawaandaa wanachuo wao na kuwapeleka chuoni hapo kwa ajili ya kuendelea na uchunguzi wao juu ya upofu wa Gideon.
Wanachuo hao walijitahidi kuwa karibu naye huku wakiwa makini kutokuweza kugundulika lakini mwisho wa siku, nao wakachemka na ripoti zao zikaonyesha kwamba Gideon alikuwa kipofu kwa asilimia mia moja.
“Basi tuseme kwamba siku ile Mungu alitaka kufanya muujiza wake, tuendeleeni na mambo yetu,” alisema Materu na maisha kuendelea kama kawaida.
Miezi ikaendelea kukatika, chuoni kukawa na amani, siku ambayo tangazo lilitolewa kwamba mjasiriamali mkubwa duniani, bwana Potter Mickey angekuja chuoni hapo kwa ajili ya kufundisha masomo ya ujasiriamali, hakukuwa na mtu aliyekuwa na wasiwasi kabisa.
Siku ya tukio hilo la mauaji lilipokuwa likitokea, kamera zao za CCTV zilimuonyesha Gideon akaelekea porini huku akiwa amevaa begi lake kubwa, kofia na fulana yake na huku mkononi akiwa na fimbo.
Wafuatiliaji wale waliokuwa kwenye kompyuta ndani ya jengo la TISS walibaki wakimwangalia, hawakujua porini kule alikuwa akienda kufanya kitu gani. Wala haikuchukua dakika nyingi, ghafla ukasikika mlio wa risasi, watu wakaanza kukimbia, Gideon ambaye aliingia porini, naye akatoka na kuanza kukimbia huku akiwa na begi lake mgongoni na alionekana kuwa na wasiwasi mwingi mno.
Hapo ndipo ilipogundulika kwamba Gideon ndiye aliyefanya mauaji yale, hakukuwa na mtu aliyefahamu sababu ya mtu huyo kumuua bwana Mickey. Maswali mengi yakaanza kumiminika vichwani mwao juu ya sababu ya Gideon kumuua mjasiriamali yule lakini hakukuwa na mtu aliyekuwa na jibu.
Mbali na kitu hicho, wakaanza kujiuliza maswali kuhusu upofu wa Gideon, waliwatuma watu wengi kumchunguza na majibu yakaonyesha kwamba alikuwa kipofu na hata wao walipojaribu kuchunguza kwa makini kupitia kamera zao, majibu yalikuwa yaleyale, Gideon alikuwa kipofu.
Kitu kilichobaki ambacho kilitakiwa kufanyika ni kumfuata Gideon chuoni, kumkamata kisha kumpeleka katika vyombo vya sheria ambapo huko, ukweli wote ungejulikana. Martin akatumwa kwa kazi hiyo.
****
Martin akafika chuoni hapo, moja kwa moja akaelekea katika ofisi ya Professa Mitimingi na kuomba kuzungumza naye kwani alikuwa na kitu muhimu alihitaji kukaa naye chini na kuongea.
Kwa sababu alikwishajitambulisha kipindi cha nyuma, hiyo wala haikuwa tatizo, akamkaribisha na kuanza kuzungumza. Alianzia mbali lakini mwisho wa siku akaamua kumwambia kile kilichokuwa kimemleta ofisini hapo.
“Ninataka kuonana na Gideon,” alisema Martin.
“Gideon yupi? Wapo wengi hapa,” aliuliza Professa.
“Gideon Mutinyama,” alisema Martin.
Hilo wala halikuwa tatizo, alichokifanya Professa ni kunyanyua simu yake na kisha kumpigia mtu wa upande wa pili na ndani ya dakika ishirini, mwanachuo mmoja akaanza kugonga mlango huo na kumruhusu kuingia.
“Gideon hayupo, hatujui amekwenda wapi,” alisema mwanachuo huyo.
“Mmejaribu kumwangalia sehemu zote?” aliuliza Martin.
“Ndiyo! Ila tumemkosa.”
“Hebu twende katika bweni lake,” alisema Martin.
Professa Mitimingi akahisi kwamba kulikuwa na tatizo limetokea japokuwa hakutaka kuwekwa wazi, alichokifanya, naye akainuka kutoka katika kiti chake na kuanza kuelekea huko pamoja nao.
Walikwenda mpaka katika bweni alilokuwa akiishi Gideon katika ghorofa ya tano, walipofika huko, waliangalia katika kila sehemu, hawakumuona. Hapo, Martin akapata uhakika kwamba kile kilichokuwa kimezungumziwa kilikuwa ukweli mtu kwamba Gideon alikuwa amehusika katika mauaji ya bwana Potter Mickey.
Wanachuo wengine wakabaki wakiwaangalia, halikuwa jambo rahisi kwa Professa mkuu kuingia katika mabweni kwa ajili ya kumtafuta mwanachuo fulani, walijua kulikuwa na tatizo.
Waliendelea kumtafuta ndani ya bweni hilo tena kwenye kila chumba lakini Gideon hakuwepo. Wakaamua kuwauliza wanafunzi wengine waliokuwa wakiishi ndani ya chumba hicho.
“Gideon yupo wapi?” aliuliza Professa Mitimingi.
“Sikumuona tangu jana, nahisi atakuwa amekwenda kuwatembelea ndugu zake,” alisema mwanachuo mmoja.
“Hakuna aliyemuona baada ya jana?”
“Mara ya mwisho kumuona ilikuwa juzi, baada ya hapo sikuona tena,” alisema mwanachuo mwingine.
Martin aliendelea kujipa uhakika kwamba ripoti iliyokuwa imetolewa kwamba Gideon alikuwa amehusika katika mauaji hayo ilikuwa sahihi kwani hakuwa akionekana katika kila kona, alipotea katika mazingira ya kutatanisha mno.
Hawakukata tamaa, waliendelea kumtafuta kwa kumuulizia lakini majibu yalikuwa ni yaleyale kwamba hakuonekana sehemu nyingine yoyote toka juzi.
“Mbona umekuja na kuanza kumtafuta Gideon, kuna nini?” aliuliza Professa Mitimingi.
“Hakuna kitu, subiri, tukimpata, utajua kila kitu,” alisema Martin, hakutaka kuendelea kubaki ofisini hapo, alichokifanya ni kuondoka.
Hapo kichwa chake kikaanza kugonga, hakuamini kama alikuwa ameshindwa kabisa kumpata Gideon, mwanafunzi aliyeaminika kuwa kipofu chuoni hapo. Aliingia ndani ya gari lake na kuanza kujifikiria, hakujua ni wapi alitakiwa kuanza, kitendo cha kumkosa mtu huyo kilimaanisha kwamba asingeweza kumpata tena.
Huku akiwa amekwishaliwasha gari lake kwa ajili ya kuondoka chuoni hapo, akaonekana kukumbuka kitu ambacho ilikuwa ni lazima kuulizia ili apate kujua ni wapi alitakiwa kuanzia.
Alichokifanya ni kuzima gari lake, akateremka na kuanza kurudi katika ofisi ya Professa Mitimingi, akagonga mlango, aliporuhusiwa, akaingia ndani.
“Ninataka kufahamu Gideon alitoka wapi,” alisema Martin.
“Alitoka nchini Malawi.”
“Una uhakika?”
“Nahisi nina uhakika kwa sababu nyaraka zake zote zilionyesha kwamba alitokea nchini humo.”
“Kuna kitu kingine kinachoweza kukupa uhakika kwamba alitokea nchini humo?”
“Hapana zaidi ya hizo nyaraka.”
“Ni nani aliyekuwa rafiki yake wa karibu hapa chuoni?”
“Kuna msichana anaitwa Juliet, huyu ndiye niliyekuwa nikisikia kwamba alikuwa karibu na kipofu yule,” alisema Professa Mitimingi.
“Ninahitaji kumuona pia.”
“Sawa.”
Walichokifanya ni kuondoka ndani ya ofisi hiyo, japokuwa Professa Mitimingi alitaka kupiga simu, akazuiliwa na hivyo kutakiwa kumuona ana kwa ana kwa sababu Martin alikuwa na maswali mengi yaliyotakiwa kujibiwa na msichana huyo.
Walipofika katika bweni alilokuwa akiishi Juliet, wakaomba kuonana naye, hilo halikuwa tatizo, baada ya dakika mbili, msichana huyo alikuwa mbele yao ambapo wakamchukua na kuelekea naye chini.
“Unamfahamu vipi Gideon?”
“Alikuwa rafiki yangu,” alijibu Juliet.
“Hakuwahi kuwa mpenzi wako?”
“Hapana, alikataa hilo.”
“Unahisi kwa nini alikataa?”
“Hata mimi sifahamu.”
“Si kwa sababu alikwambia wewe siyo mzuri?”
“Hapana. Kila siku alikuwa akinisifia kwamba mimi ni mzuri lakini kila nilipotaka kuwa na mahusiano naye ya kimapenzi, alikataa.”
“Unahisi kwa nini?”
“Sijajua kwa kweli.”
“Mara yako ya mwisho kumuona ilikuwa lini?”
“Toka juzi.”
“Ulijaribu kumtafuta simuni?”
“Nilifanya hivyo mara kadhaa lakini sikumpata.”
“Unaamini kwamba Gideon alikuwa kipofu?”
“Yaap! Naamini hilo.”
“Kipi kinachokufanya kuamini?”
“Macho yake, hakuna hii mboni nyeusi, jicho zima lilikuwa jeupe, pia matendo yake, alikuwa kipofu asilimia mia moja.”
“Sawa. Hivi ulishawahi kuishika hata simu yake?”
“Hapana! Alikuwa mgumu kukubali, na hata laptop yake alikuwa akiificha sana, hakutaka mtu mwingine yeyote aiwashe,” alisema Juliet.
“Sawa! Kwa hiyo unataka kuniambia haujui mahali alipo kwa sasa?”
“Ndiyo! Wala sifahamu!”
“Nashukuru!”
Siku hiyo, kila kitu alichokuwa akitaka kukifahamu, alikifahamu, alipoona kwamba ameridhika, akaondoka ofisini hapo huku akiwa na mipango mingi ya kufanya kuringana na maelezo yale aliyokuwa ameyasikia kutoka kwa watu wawili aliokuwa amezungumza nao.
Alipofika makao makuu, akaitwa katika chumba maalumu cha mikutano na kuulizwa kile kilichokuwa kimetokea, kwa maelezo waliyokuwa wameyatoa watu wale aliokwenda kuwahoji. Mbele yake kulikuwa na wakuu wake watano, akaanza kuelezea kila kitu kilichokuwa kimetokea.
“Kuna kitu hapa, nimeanza kuhisi kitu,” alisema Materu.
“Kitu gani?”
“Huyu mtu ametumwa!”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Nahisi tu, lakini subiri, ili hisia zetu zikamilike, nadhani tunatakiwa kumtafuta mpaka apatikane.”
“Atakuwa wapi sasa? Amerudi nchini kwake?”
“Inawezekana, lakini je, tunajua anapoishi? Tumesikia kwamba ni Malawi, kuna uhakika wowote kwamba nchini kwake ni Malawi?” aliuliza Ibrahim, mmoja wa wakuu katika Kitengo cha TISS.
“Hapo ndipo kwenye wakati mgumu, cha msingi tunapaswa kutuma watu wawili wa kufanya kazi hii, ni lazima wasafiri haraka iwezekanavyo kuelekea nchini Malawi, twende tukajaribu, nina uhakika tutampata tu,” alisema Ibrahim na kuendelea:
“Wa kwanza awe huyu Martin, wa pili nafikiri awe Mathias Jonathan, mnaonaje?” aliuliza Ibrahim.
“Haina tatizo. Tutawatuma waende huko, wahakikishe kwamba anapatikana,” alisema Materu.
“Na watakwenda kivipi?”
“Tutamfanya Martin awe kichaa, nafikiri ataweza hilo. Atakwenda katika Jiji la Lilongwe, huko atakuwa kichaa kwa muda wote mpaka Gideon atakapopatikana, wakati huohuo, Mathias atakuwa mfanyabaishara mkubwa wa madini, atakuwa akipenda sana starehe kuliko kitu kingine, kazi yake itakuwa ni kutumia fedha tu katika sehemu mbalimbali nchini humo.
“Kwa Martin, mara kwa mara tutakuwa tukimtuma mtu kwa ajili ya kumpelekea chakula pale alipokuwa, staili ya kumpa chakula ni kwamba kuna mfuko wa chakula utakuwa ukitupwa jalalani, atakuwa akiufuata na kukila chakula hicho, kila siku usiku itakuwa ni lazima kutoa ripoti amefikia wapi, kuna mengi yatajulikana, tuvuteni subira,” alisema Ibrahim, mmoja wa viongozi aliyekuwa na uwezo mkubwa wa kufikiria kuliko wengine.
Hilo wala halikuwa tatizo, taarifa zikasambazwa kwa watu wote ambao walitakiwa kujua ni kitu gani kilichokuwa kikitakiwa kufanyika, baada ya hapo, maandalizi yakawekwa tayari na watu waliotakiwa kufuatilia ishu hiyo, Martin na Mathias kuondoka nchini Tanzania kuelekea Malawi kwa ajili ya kuanza kazi yao mara moja. Japokuwa kwa mtazamo ilionekana kuwa kazi ngumu lakini kila mmoja alikuwa na uhakika kwamba iwe isiwe ni lazima Gideon apatikane na kufikishwa katika vyombo vya sheria.

Kilikuwa ni kipindi cha baridi kali ndani ya Jiji la Lilongwe nchini Malawi, watu wote waliokuwa wakionekana mitaani, walikuwa na masweta au makoti makubwa kwa ajili ya kuzuia baridi hilo.
Hakikuwa kipindi kizuri kwa sababu wakazi wengi waliugua magonjwa mengi kama vichomi vilivyowapa wakati mgumu nyakati za usiku.
Wafanyabiashara ambao kwa Tanzania walijulikana kama Wamachinga, walikuwa wakiendelea na kutembeza bidhaa zao, kwa wakati huo hawakutembeza fulana nyepesinyepesi bali bidhaa kubwa waliyokuwa wakiitembeza ilikuwa ni makoti makubwa au masweta na huku wakati mwingine miamvuli, hasa pale walipoona kwa siku nzima manyunyu ya mvua yalikuwa yakidondoka.
Wakati wa mchana, hakukuwa na watu wengi mitaani, wengi walikuwa wakishinda ndani kutokana na baridi kali huku kwa nyakati za usiku, bila kuhofia kitu chochote kile, kila mtu alikuwa akiwasha moto nje ya nyumba yake na kisha kuanza kuota huku akiwa na shuka kubwa lililoufunika mwili wake.
Mishemishe ndani ya Jiji la Lilongwe zilipungua, si watu wengi waliokuwa wakizunguka huku na kule zaidi ya walevi waliokuwa wakirudi nyumbani kwao nyakati za usiku, walikuwa wakitembea kwa kuyumbayumba mpaka katika milango ya nyumba zao na kuingia ndani.
Katika kipindi hiki cha baridi kali, ndipo alipoanza kuonekana kichaa mmoja aliyekuwa akizurura hovyo ndani ya jiji hilo kiasi kwamba kila mtu akaanza kujiuliza juu ya kichaa huyo aliyeonekana kuwa na hasira kupita kawaida.
Kila wakati alikuwa na nguo zilizochakaa, mkononi alikuwa na fimbo huku nywele zake zikiwa timtim. Hakuonekana kuwa na masihara, kila mtu ambaye alipita karibu yake, alikuwa akimchapa kwa fimbo, na kama hakuwa na fimbo, alikuwa akikuvamia na kukupiga.
Watu wakaanza kumuogopa, hakuwa na makazi yoyote yale, kila siku alikuwa akilala barabarani huku muda wake mwingi wa mchana akitumia kushinda katika jalala kubwa lililokuwa pembezoni mwa Jiji la Lilongwe.
Kichaa huyo akaanza kupata umaarufu, alikuwa akizurura hovyo katika kila kona ya jiji hilo huku akiongea peke yake, kila wakati alikuwa akijikuna mwili wake uliokuwa ukiwasha mno na wakati mwingine kulala barabarani huku magari yakiendelea kupita.
Hakukuwa na mtu aliyejua historia kuhusu kichaa huyo ambaye kila siku alikuwa akikatiza huku na kule na makazi yake makubwa kuwa katika Jalala la Mabuya lililokuwa pembezoni kidogo mwa jiji hilo.
Upatikanaji wa kichaa huyo katika jiji hilo ikaonekana kuwa kero hivyo watu kuanza kuilalamikia Mamlaka ya Jiji kwa kuruhusu kichaa kama huyo kukaa mjini na wakati kulikuwa na wageni wengi waliokuwa wakifika kutoka nje ya nchi hasa Bara la Ulaya na Marekani.
Hapo ndipo mamlaka hiyo ilipoamua kuwakusanya vijana maalumu kwa ajili ya kazi moja ya kumkamata na kumpeleka katika hospitali iliyokuwa ikihifadhi vichaa wengine kama alivyokuwa yeye.
Kumkamata haikuwa kazi kubwa, japokuwa walikuwa vijana sita, lakini kila walipokuwa wakimsogelea, walichapwa fimbo na kupigwa ngumi. Alionekana kuwa kichaa lakini kwa jinsi alivyokuwa akipigana, ilionyesha kwamba kabla ya kuwa katika hali hiyo alipitia mafunzo ya mapigano.
Siku hiyo, wakashindwa kumkamata na hivyo kupanga siku nyingine. Siku iliyopangwa ilipofika, wakakusanyika tena, walikuwa zaidi ya watu kumi, walipomsogelea, kama kawaida walipokea mkong’oto na kuondoka.
Sifa za kichaa huyo zikaanza kutapakaa, asilimia kubwa ya wakazi waliokuwa wakikaa katika Jiji hilo lenye watu zaidi ya laki sita, walimfahamu kichaa huyo aliyekuwa na nguvu za ajabu zilizomuogopesha kila mtu.
Kila siku jioni, alikuwa akilisogelea jalala la Mabuya na kuokota chakula na kuanza kula. Hakukuwa na aliyejua kwamba yule kichaa waliyekuwa wakimwangalia, hakuwa kichaa kama walivyodhania bali alikuwa mpelelezi aliyekwenda kwa ajili ya kukamilisha kazi moja tu, kumkamata Gideon ambaye mara ya mwisho aliiona picha yake nchini Tanzania lakini bado aliendelea kumkumbuka vilivyo.
****
Bado watu hawakuwa wakiamini kile kilichokuwa kimetokea, hawakuamini kama mjasiriamali waliyekuwa wakimhusudu, Potter Mickey alikuwa ameuawa kwa kupigwa risasi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam nchini Tanzania.
Watu waliokuwa wakiyafuatilia mafundisho yake na hata wale waliokuwa wamepiga hatua baada ya kufundishwa namna ya kujiingizia kipato, kuibadilisha dola moja kuwa bilioni, hawakuweza kuvumilia, walijikuta wakianza kububujikwa na machozi, kile kilichotokea, kwao ilionekana kama ndoto.
Mwili wake ukasafirishwa na kupelekwa nchini Marekani katika Jiji la Florida alipokuwa akiishi. Katika mazishi hayo, watu waliohudhuria walikuwa wale waliopewa mualiko maalumu kama ilivyokuwa kwa masupastaa wengi nchini humo.
Walikuja viongozi mbalimbali wa serikali, matajiri kutoka nchi mbalimbali zikiwemo za Uarabuni na watu wengine maarufu kama wanamuziki walikuwa walikusanyika katika mazishi ya bwana Mickey.
Saa 10:30 jioni, magari matano ya kifahari yakaanza kuelekea katika Makaburi ya St. Andrew Square na mwili wake kuzikwa katika makaburi hayo.
"Pumzika kwa amani baba" alijisemea Victor huku machozi yakimbubujika mashavuni mwake.
Msiba huo ulipomalizika, Victor hakutaka kuendelea kukaa nchini Marekani, alichokifanya ni kuondoka na kuelekea nchini Uingereza katika Jiji la Liverpool kwa ajili ya kuonana na rafiki wa siku nyingi wa baba yake ambaye aliwahi kufanya kazi kama mpelelezi wa SIS (Secret Intelligence Service) kabla ya kustaafu, Edward Simpson.
Alipofika huko, kitu cha kwanza kabisa akataka kuonana naye faragha, hilo halikuwa tatizo, wakapanga siku ya kuonana na mahali, baada ya siku kadhaa, wakakutana katika Hoteli ya The Prince iliyokuwa katikati ya Jiji la Liverpool.
“Nikusaidie nini rafiki wangu wa siku nyingi?" aliuliza bwana Simpson.
“Baba yangu aliuawa wiki iliyopita" alisema Victor.
“Pole sana. Nilisoma magazetini, baba yako alikuwa mtu mwema, mcheshi, alikuwa baba mzuri na mtu wa karibu pia, polisi wamesemaje?" alisema na kuuliza bwana Simpson.
“Walituambia tusubiri, lakini huwa siziamini serikali za watu weusi, hasahasa serikali za kiafrika" alisema Victor.
“Kwa hiyo nikusaidie nini?"
“Nataka kufahamu ni nani aliyemuua baba yangu."
“Sawa! Nitakusaidia," alisema bwana Simpson.
Walizungumza mambo mengi siku hiyo, bwana Simpson alikuwa amestaafu kitambo kufanya kazi kama mpelelezi chini ya Shirika la Kijasusi la nchini Uingereza, SIS lakini kitendo cha Victor kumfuata na kumuomba msaada wa hali na mali, hakuwa na jinsi, alikubaliana naye.
Akamuahidi kwamba kila kitu kingefanyika na hata kama ilitakiwa kusafiri basi angesafiri na kwenda nchini Tanzania kwa ajili ya kuanza kazi yake na hatimae muuaji kupatikana ndani ya kipindi kifupi.
Victor akashukuru na hivyo kuagana naye na kumuahidi kwamba angemsaidia baada ya kumpa maelekezo ya kufika nchini humo kirahisi na pia kumwambia sehemu chuo hicho kilipo, kazi ingefanyika bila wasiwasi wowote ule.

“Huyu jamaa ana hela za kufa mtu.”
“Jamaa gani?”
“Bilionea Kijana.”
“Ndiye nani.”
“Kuna jamaa alikuja jana usiku, alinunulia pombe klabu yote.”
“Acha utani!”
“Kweli tena, yaani ni balaa aisee! Jana aliingia hapo Sweat Garden, akawanunulia pombe watu wote waliokuwa ndani ya klabu ile, akawaambia wanywe mpaka wasaze, yaani kila mtu akapigwa na butwaa.”
“Mmmh!”
“Unashangaa! Kwanza umeiona hiyo gari anayotembelea?”
“Hapana! Ipo vipi?”
“Lamboghin!”
“Unasemaje?”
“Anatumia Lamboghin yenye rangi nyekundu! Ni balaa. Ukiachana na usafiri huo, jamaa anapiga pamba za kufa mtu, yaani ni hatari, wenye mademu zetu wakali wenye tamaa, hapana, huyu jamaa anaweza akawachukua!”
“Kwani huyo jamaa yupo vipi?”
“Kwa mtazamo ni wa kawaida tu.”
“Katokea wapi sasa?”
“Hata sisi wenyewe hatujui, jana tu alivamia ghafla klabu na kuanza kutupiga pombe, ukisema katokea wapi, wala hatufahamu.”
“Na gari lake ulilionaje?”
“Si unajua sisi wapambe bhana! Tulitoka kuangalia usafiri wake, ni noma sana,”
Mathias alikuwa ameharibu hali ya hewa ndani ya Klabu ya Sweat Garden iliyokuwa katikati ya Jiji la Lilongwe, kitendo chake cha kuingia ndani ya klabu hiyo huku akiwapa watu ofa ya kunywa pombe kadiri walivyotaka, kiliwapagawisha walevi wote kiasi kwamba akaanza kuonekana muhimu katika ukumbi huo.
Usiku huyo, walevi walipombeka kupita kawaida, wale waliotaka kubeba, walipewa nafasi hiyo japokuwa hawakuweza kufanya hivyo. Mbali na kugawa pombe kwa kila mtu aliyekuwepo ndani klabu hiyo, wakati alipokuwa akiondoka, wapambe walioamua kumsindikiza huku wakiimba ‘Young Bilionaire...Young Bilionaire...” walipigwa na mshtuko baada ya kuona gari la kisasa aina ya Lamboghin yenye thamani ya shilingi milioni mia nane ikiwa imepaki, Mathias akaingia na kuondoka zake.
Hiyo ndiyo ilikuwa stori ya jiji, kila aliyekuwa ameona tukio la siku hiyo, aliisambaza taarifa hiyo kwa watu ambao hawakuwepo katika klabu hiyo usiku huo. Jina la Young Bilionaire likaanza kuvuma, wale ambao hawakuwepo ndani ya klabu hiyo usiku huo wakatamani masaa yarudi nyuma ili waweze kuwepo.
Mitandaoni, alitawala Young Bilionaire, kila mtu alitaka kumuona, maelezo yaliyokuwa yakitolewa kwamba jamaa alikuwa na pesa chafu yalimpagawisha kila mmoja jijini Lilongwe.
Mathias hakutaka kuishia hapo, kwa sababu alikwishaambiwa kwamba angetumia kiasi chochote cha fedha, alizitumia huku malengo yake yakiwa kwenye kufanikisha kile alichokuwa ametumwa, kumpata Gideon na kumfikisha katika vyombo vya sheria.
Kila siku usiku Mathias alikuwa akifika katika klabu hiyohiyo na kuanza kuzitumia, watu wote waliokuwa wakikusanyika katika klabu hiyo wakaanza kumpatia jina la Young Bilionaire na kuwa jina lake rasmi.
Wanawake hawakutaka kupitwa, kwa kuwa mbele yao alionekana mwanaume aliyekuwa na fedha za kumwaga, nao wakaanza kujilengesha kwa kutaka kula naye maisha.
Sifa za Young Bilionaire ziliendelea kusikika kila kona, hakuwa mchoyo, kila aliyetaka fedha alipewa bila kinyongo chochote kile. Kila alipoingia baa au klabu, alikuwa na kipaza sauti kidogo ambacho hakikuweza kuonekana, hicho alikuwa akikificha sana kwa ajili ya kurekodia mawasiliano yoyote ambayo angefanya na mtu yeyote yule.
Fedha zake ‘zilitisha’ kiasi kwamba watu wakaanza kufanya uchunguzi ili kuona hizo fedha zilitokea wapi, alizipata wapi mpaka kuanza kuzitumia pasipo kuzionea huruma. Walipochunguza, tena kwa kina, wakagundua kwamba Young Bilionaire alikuwa mfanyabiashara mkubwa wa madini, alikuwa akisafirisha madini ya Tanzanite kutoka Tanzania na kwenda sehemu nyingine barani Afrika.
“Utaendelea kujifanya mfanyabiashara wa madini, najua kuna mengi tutakuja kuyafahamu, wewe endelea kufuatilia,” ilisikika sauti ya bwana Materu simuni.
“Hakuna tatizo mkuu.”
“Na Martin unaonana naye?”
“Ndiyo! Huwa nipo naye karibu sana na ni mara chache ninapeana naye ishara za macho hasa mchana ambao watu hawagundui kwamba yule bilionea wa usiku ndiye mimi,” alisema Mathias.
“Safi sana! Acha nikuache upumzike, endeleeni kuchunguza, hata kama itawachukua miaka mitano, haina jinsi, pambaneni mpaka apatikane, na ninawahakikishia kwamba baada ya kufanikiwa, mtapata chochote mkitakacho,” alisema Materu.
“Hakuna tatizo bosi.”
Bado uchunguzi wa kimyakimya ulikuwa ukiendelea, hakukuwa na mtu yeyote aliyegundua kwamba yule kichaa aliyekuwa barabarani ambaye alishika sana hisia za watu na huyu mtumiaji mkubwa wa fedha katika klabu mbalimbali walikuwa watu wawili waliofahamiana ambao walifanya kazi kwa kificho huku wakiendelea kumtafuta mtu waliyetumwa kumtafuta.
Siku ziliendelea kukatika, jina la Young Bilionaire likawa kubwa katika Jiji lote la Lilongwe, matajiri waliokuwa wakitanua na fedha zao kwa kuchukua wanawake wazuri na kuwahonga wakawa wakimuogopa mno Mathias ambaye kama kawaida jina lake hilo la Young Bilionaire ndilo lililokuwa likijulikana zaidi.
“Unajua bosi mpaka sasa hivi sijajua unaitwa nani, mbali na hili la Young Bilionaire,” alisema jamaa mmoja, huyu aliitwa Oswald, kwa kipindi kirefu alijitahidi kujenga urafiki na Mathias, mwisho wa siku akafanikiwa na yeye kuanza kutumbua fedha ambazo hazikuwa na kikomo.
“Naitwa Kenneth Mutahaba, mimi ndiye mmiliki wa migodi zaidi ya mitano Tanzania,” alisema Mathias.
“Daaah! Unajua umewateka sana watu wa hapa mjini, kuna mtu nataka nikutambulishe kwake.”
“Mtu gani?”
“Dada mmoja hivi, hiyo ni mashine balaa, aliwahi kuwa Miss Malawi kabla ya kuanza kuwa muigizaji,” alisema Oswald.
“Yupo vipi?”
“Ni mkali sana, anaitwa Rebecca. Anavutia, wenye fedha wamejaribu kumfuata, mtoto kawakatalia.”
“Kweli?”
“Siwezi kukudanganya!”
“Basi sawa, wewe muite tu. Hela zipo ila watumiaji wamekosekana,” alisema Mathias.
Hilo halikuonekana kuwa tatizo hata mara moja, kwa kuwa yeye mwenyewe alijua kwamba angeweza kupata kitu chochote kile, akafanya mawasiliano na msichana huyo na kumuita katika nyumba aliyokuwa akiishi Mathias.
Baada ya masaa mawili, honi zilisikika nje ya nyumba hiyo na mlinzi alipofungua geti kuchungulia, macho yake yakatua katika gari la mrembo Rebecca. Kwa kuwa alikwishaambiwa kuhusu msichana huyo, akafungua geti na gari kuingizwa.
Maneno ya Oswald yalikuwa sahihi, muonekano wa msichana huyo ulikuwa balaa, alikuwa mrefu, hipsi zake zilionekana vema machoni mwa kila aliyemwangalia, alikuwa na mapaja manene huku ngozi yake nyeupe ikimpendezesha zaidi.
Mbali na umbo zuri alilokuwa nalo, Rebecca alikuwa amejaaliwa kuwa na sura nzuri, kila aliyemwangalia, sura yake ilimvutia kiasi kwamba akapewa jina la Barbie, ile midoli ya watoto inayoongoza kwa uzuri.
Kila alipokuwa, akitikisa, watu wengi walijaribu bahati zao kwa msichana huyo lakini hakukuwa na yeyote aliyepata bahati jambo lililomshangaza kila mtu. Hakuwa na fedha nyingi lakini aliwakataa watu wenye fedha hali iliyowafanya wasichana wengi kumshangaa.
Pamoja na uzuri wote aliokuwa nao, mvuto wote uliowapagawisha wanaume, aliposikia tu kuhusu Mtanzania aliyeitwa Young Billionaire, akaanza kuvutiwa naye, akahisi moyo wake ukianza kutekwa na mtu huyo hata kabla hajamuona.
Kitu pekee alichokuwa akikihitaji ni kuwa na mwanaume huyo huku kiu yake kubwa ikiwa ni kwenda nchini Tanzania na kukutana na msichana ambaye kila siku alimuona kuwa ‘Role Model’ wake, Wema Sepetu aliyekuwa akitikisa na filamu zake alizoigiza na Steven Kanumba ambazo zilitazamwa sana nchini Malawi.

ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA NNE

Macho ya Mathias yalipotua kwa Rebecca akaonyesha mshtuko wa waziwazi, hakuamini kama hapa Afrika angeweza kukutana na msichana mrembo kama alivyokuwa Rebecca, alibaki akimwangalia kwa umakini kana kwamba alikuwa akimchunguza.
Msichana huyo akatoa tabasamu pana lilioonyesha kila kitu kwamba alikuwa tayari kwa lolote na ni Mathias ndiye aliyekuwa akisubiriwa kuzungumza kitu chochote alichotaka kuzungumza.
Hakutaka kueendelea kukaa kochini na wakati aliingia msichana mrembo kama alivyokuwa Rebecca, akajikuta akisimama, akianza kupiga hatua kumsogelea, alipomfikia, huku akijifanya kuwa na heshima kubwa, akamsalimia kiustaarabu na tabasamu pana akiliachia usoni mwake.
“You are welcome,” (Karibu) alisema Mathias huku akiachia tabasamu.
“Thank you.” (Nashukuru)
“Make yourself at home,” (Jisikie upo nyumbani)
“Thank you.” (Nashukuru)
Akili ya Mathias haikutulia hata kidogo, mara alikuwa akifanya hili mara lile, kila alipokuwa akimwangalia msichana huyo, alipagawa kupita kawaida. Alichokifanya ni kusimama na kulifuata friji, aliporudi, alikuwa na chupa ya pombe ya Amarula na kuiweka katika glasi.
“Wewe ndiye Amanda Posh?” aliuliza Mathias huku akichia tabasamu.
“Mmmh! Ndiye nani?”
“Yule msichana aliyekuwa akitembea na na muigizaji wa Marekani, Brad Pitt!”
“Hahaha! Hapana!”
“Mbona umefanna naye sana!”
“Kweli?”
“Ndiyo! Hakika Mungu anajua kuumba. Mara ya kwanza niliposikia kuhusu wewe, sikuamini hata kidogo, nikajua kwamba Oswald ananidanganya, ila sasa hivi, nimeamini, u mrembo sana!” alisema Mathias.
“Hahah! Acha utani wako bwana!”
“Kweli tena! Haki ya Mungu wewe mzuri!”
“Hivi ushawahi kwenda Keremeyi?”
“Hapana! Ndiyo wapi huko?” aliuliza Mathias, Rebecca akamgeukia Oswald.
“Hujawahi kumpeleka Young Bilionea Keremeyi?” aliuliza Rebecca.
“Hapana ila nilitaka kufanya hivyo. Uliponiambia kuhusu huyu jamaa, nikaona hakuna jinsi, hakukuwa na haja ya kwenda huko,” alisema Oswald.
“Jamani! Mbona mnanitenga! Huko Keremeyi ndiyo wapi?”
“Ni hapahapa Malawi, sehemu iliyokuwa na wanawake wengi wazuri, huko ndiyo watu wakubwa na wenye fedha kama nyie wanapokwenda. Kama unaniona mimi mrembo, hebu nenda huko, kaa hata kwa wiki moja, ukirudi, naomba uniambie tena kwamba mimi ni mzuri, sidhani kama utaweza,” alisema Rebecca.
“Hakuna kitu kama hicho, Rebecca, nimewahi kuona wanawake wengi warembo, nimewahi kutumia pesa na wanawake wengi warembo, ila ninakiri kwamba sikuwahi kuwa na msichana mzuri na mrembo kama ulivyo, niamini, wewe ni mrembo mno,” alisema Mathias.
Siku nzima alikuwa na kazi ya kuusifia uzuri wa msichana huyo, kila alipomwangalia, macho yake hayakuridhika, alitamani kumtazama zaidi na zaidi na hata kulala naye usiku huohuo ili aendelee kuwa karibu naye.
Alijijua kwamba ni mzuri, alijijua kwamba alikuwa na umbo zuri na mapaja yaliyovutia, kila wakati, alikuwa akibadilisha mikao, mara akae hivi, mara akae vile, mara mguu uje kwa juu staili ya kukunja nne, mara akae vile, yaani kila staili aliyokuwa akikaa kochini pale, Mathias alibaki hoi.
“Nilisikia kwamba unataka kuniona!” aliuliza Mathias.
“Ndiyo!”
“Kuna nini tena?”
“Nilihitaji ukaribu na wewe!”
“Ukaribu upi?”
“Wa urafiki tu.”
“Mmmh!”
“Nini tena?”
“Nitaweza kuwa rafiki na msichana mrembo kama wewe?”
“Kwa nini usiweze?”
“Hapana! Nafikiri naweza kushawishika kula tunda, haiwezekani simba kuwa rafiki wa swala, si unajua kuna kipindi cha ukame porini!” alisema Mathias.
Alijisahau kama alikwenda nchini Malawi kwa ajili ya kupeleleza mahali alipokuwa Gideon na kisha kumkamata na kumpeleka katika vyombo vya sheria, msichana aliyekuwa mbele yake, alimchanganya mno, alikuwa tayari kufanya kitu chochote lakini si kumkosa msichana huyo mrembo.
Hapo ndipo maneno ya Oswald yalipoanza kujirudia kwamba msichana huyo aliwakataa wanaume wengi, wale wenye fedha na hata wale waliokuwa maarufu, hakujua ni kwa sababu gani msichana huyo aliamua kumfuata yeye, kwa upande mwingine, alijiona kuokota embe chini ya mbuyu.
Siku hiyo ilikuwa ni ya kula bata tu, muonekano wa Mathias ulimpagawisha hata Rebecca mwenyewe. Ingawa alikuwa na sababu zake, lakini ukweli mwingine ni kwamba aliwapenda Watanzania, walikuwa wanaume wa tofauti kabisa na Wamalawi.
Wanaume wa kule, walikuwa wanywaji wa pombe wakubwa lakini pia hawakuwa walaji, walikuwa wakiishi tofauti na Watanzania ambao mara nyingi huwa wanakunywa na kula sana nyama, ila kwa Malawi, wanaume walikuwa tofauti na hivyo kupelekea ufanyaji wao wa tendo kitandani kuwa mdogo tofauti na Watanzania.
Kila alipokuwa akimwangalia Mathias, moyoni mwake alijihisi kumpenda kwa mapenzi ya dhati. Pasipo kutegemea wala kupanga, siku hiyo wakajikuta wakilala pamoja na kufanya mapenzi. Mathias alichukulia kila kitu kuwa kawaida, hakujua kwamba kukutana na msichana huyo, ilikuwa njiamojawapo ya kukamilisha upelelezi wake.
Usiku ukawa wa burudani!
****
Saa 6:15 usiku, ndege ya kubwa ya Shirika la KLM ilikuwa ikitua ndani ya Uwanja wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere uliokuwa jijini Dar es Salaam. Mara baada ya ndege hiyo kusimama, abiria wakaanza kuteremka na miongoni mwa abiria hao alikuwepo bwana Simpson, mpelelezi aliyetumwa na Victor kwa ajili ya kumtafuta muuaji aliyemuua baba yake.
Alipoteremka, akaanza kuelekea katika sehemu ya kuchunguzia mizigo na kila kitu kilipokamilika, akachukua teksi ambayo ilimpeleka mpaka katika Hoteli ya Kilimanjaro.
Kichwa chake kilikuwa na mawazo, alijua fika kwamba mbele yake kulikuwa na kazi kubwa lakini pamoja na hayo yote, alihakikisha kwamba anaifanya kikamilifu kila hatua ili mwisho wa siku aje kufanikiwa kwani aliamini ilikuwa miongoni mwa kazi ngumu kuliko zote alizowahi kuzifanya maishani mwake.
Alipofika katika hoteli hiyo, akakabidhiwa chumba na maisha yake kuanza rasmi ndani ya hoteli hiyo. Japokuwa ilikuwa ni usiku sana, hakutaka kulala, alichokifanya ni kwenda kusimama dirishani na kisha kuanza kuangalia sehemu ya Jiji la Dar es Salaam.
Mandhari yake yalimfurahisha, aliporidhika, akaifuata brifukesi yake, akaifungua na kutoa laptop yake ndogo. Alichokuwa akitaka kukiona, ni baadhi ya kazi zake ambazo alizifanya katika kipindi cha nyuma.
Kompyuta ilikuwa na mafaili mengi, hasa ya kazi ambayo aliifanya kipindi cha nyuma alipotumwa nchini Iran, Syria na Libya, kote huko alikwenda kupeleleza na kazi yake ilipokamilika, alifanya mauaji yaliyomshangaza kila mtu pasipo kujua kwamba ni mpelelezi wa Uingereza ndiye aliyefanya hivyo.
Alijiamini kwa kila kitu, alijaribu kupitia faili moja baada ya jingine, alipomaliza, akachukua simu yake na kuanza kuyaingiza mafaili yake katika simu hiyo.
Alifika hapo huku akiwa hafahamu Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kipo upande gani. Simu yake ndiyo ilikuwa msaada mkubwa kwa siku iliyofuata ndiyo ambayo ilimuongoza mpaka chuoni hapo ambapo akaomba kuonana na mkuu wa chuo, Professa Mitimingi.
“Who are you?” (Wewe ni nani?) aliuliza Professa Mitimingi huku akimwangalia Simpson kwa umakini.
“My name is Simpson from SIS” (Nitaitwa Simpson kutoka SIS) alijibu Simpson.
“What is it?” (Ndiyo nini hiyo?)
“Secret Intelligence Service.
“From United Kingdom, right?” (Kutoka Muungano wa Kingereza, sawa?)
“Yes!” (Ndiyo)
“What can I help you Simpson?” (Nikusaidie nini Simpson?)
Simpson akaanza kumuuliza kuhusu na mauaji yaliyokuwa yametokea wiki chache zilizopita, alihitaji kufahamu kila kitu kwani kulikuwa na kazi kubwa ambayo alitaka kuifanya, kazi ambayo aliamini hakukuwa na nchi yoyote ya Kiafrika ingeweza kuifanya.
Alichokifanya Professa Mitimingi ni kumpeleka katika eneo lililofanyika tukio hilo la mauaji. Simpson akasimama mahali pale, alianza kuangalia huku na kule, alionekana kama mtu aliyekuwa akitafuta kitu fulani.
“Mlisikia mlio wa risasi, si ndiyo?” aliuliza Simpson.
“Ndiyo!”
“Mlio wake ulifanana vipi?”
“Kama mlio fulani wa bomu, ulitoka kwa sauti kubwa.”
“Sawasawa. Muuaji alikuwa nani?”
“Wala sifahamu kwa kweli.”
“Umesema mlio wake ulisikika kama bomu?”
“Ndiyo!”
“Sawa, subiri.”
Alichokifanya bwana Simpson ni kuchukua simu yake na kuanza kuangalia vitu ambavyo hata Mitimingi hakuweza kuvifahamu, alibaki akimwangalia mpelelezi huyo, kwa muonekano alikuwa mtu makini sana ambaye hakuwa na masihala hata kidogo.
Kila alipokuwa akibonyeza simu yake, kuna kipindi alikuwa akikunja sura, kuna wakati mwingine alikuwa akiachia tabasamu, wakati mwingine alikuwa akihuzunika, kila hali ambayo binadamu wa kawaida alikuwa akiionyesha wakati anatazama tukio fulani.
“Hiyo ni bunduki ya kisasa, inaitwa Rifle, imetengenezwa nchini Urusi, ni bunduki hatari inayotumiwa na watu wenye mafunzo makubwa, ina uwezo wa kulenga umbali mrefu na hutoa mlio mkubwa endapo haikuwekwa kiwambo cha kuzuia mlio wa risasi.
“Ukiachana na AK-47 yaani Avtomat Kalashnikov iliyotengenzwa mwaka 1947 na mwanajeshi aitwaye Mikhail Kalashnikov, hii ni bunduki nyingine inayoongoza kwa kuua watu wengi duniani, ni bunduki hatari sana,” alisema bwana Simpson.
Siku hiyo ilikuwa kama darasa kwa Mitimingi, kila neno alilokuwa akilizungumza mpelelezi yule, lilikuwa somo kubwa kwake. Alizungumza mambo mengi huku akisisitiza kwamba alitaka kumfahamu mtu aliyefanya mauaji hayo.
Professa hakumwambia ila alichojaribu kukifafanua ni kwamba kuna watu walikuja na walimuulizia mtu mmoja aitwaye Gideon ambaye alisoma ndani ya chuo hicho na alikuwa mwanachuo kipofu mwenye uwezo mkubwa darasani.
“Basi! Ishia hapohapo!”
“Kwa nini?”
“Umesema ni kipofu na alikuwa na uwezo mkubwa darasani, si ndiyo?”
“Ndiyo!”
“Sawa, nashukuru! Bila shaka anatokea nchini Msumbiji!”
“Hapana! Alikuwa akitokea Malawi!”
“Usibishe, anatokea Msumbiji.”
“Wewe unajuaje na wakati haumfahamu?”
“Ni kipofu, mwenye uwezo mkubwa, inatosha, nishajua ni kitu gani kimetokea, kuna sababu kubwa ya bwana Mickey kuuawa, ni sababu ambayo hakuna mtu anayeweza kuifahamu. Sidhani kama natakiwa kukaa sana hapa, naomba niondoke,” alisema bwana Simpson.
“Mmmh! Sawa, hakuna tatizo.”
Bwana Simpson hakutaka kuendelea kubaki mahali hapo, alionekana kufahamu kila kitu kilichokuwa kimetokea, alichokifanya ni kuondoka chuoni hapo na kuelekea hotelini. Alionekana kuwa mtu mwenye mawazo lukuki, kila alipokuwa akikaa, alisonya kwa hasira huku wakati mwingine akijipigapiga mapajani.
Alipofika hotelini, kitu cha kwanza kabisa ni kuwasiliana na Victor kwani kulikuwa na mambo mengi ya kumwambia.
“Unajua baba yako alikuwa nani?” aliuliza Simpson.
“Kivipi?”
“Wasifu wake!”
“Alikuwa Mjasiriamali?”
“Hilo tu?”
“Ndiyo!”
“Basi haukuwa ukimfahamu baba yako. Usijisumbue kumtafuta muuaji, sijamfahamu muuaji ila sifa zake zinanifanya kugundua alitumwa na nani,” alisema Simpson.
“Naomba uniambie, baba yangu alikuwa nani.”
“Huwezi kujua, na hata mama yako hawezi kujua. Baba yako alikuwa mpelelezi wa CIA,” alisema Simpson.
“Unasemaje?”
“Baba yako alikuwa CIA, alijifanya kuwa mjasiriamali kwa sababu alikuwa mpelelezi wa kimataifa, alisafiri nchi za Uarabuni si kwa sababu alikuwa mhamasishaji wa ujasiriamali, alisafiri kwenda huko kwa sababu alikuwa akifanya upelelezi kwani alikuwa chini ya CIA,” alisema Simpson.
“Mmmh!”
“Ndiyo hivyo! Na hata huyo mtu aliyemuua, alikuwa kama yeye.”
“Kivipi?”
“Na yeye ni mpelelezi kutoa CIA!”
“Unasemaje?”
“Ndiyo hivyo! Huyo jamaa anaitwa Jonathan Malumbu, mwanaume wa Kiafrika ambaye amekuwa akifanya oparesheni nyingi na kubwa, amekuwa akitumwa sehemu mbalimbali duniani, ni mwanaume mwerevu sana, mwenye nguvu na yupo makini katika utendaji wake.
“Kama upo nje ya kitengo, huwezi kumfahamu, ni mtu hatari sana. Alipokuja Tanzania, alikuwa akitumia jina la Gideon. Ni Mwafrika anayeishi Msumbiji, ila nilipoulizia hapa, niliambiwa kwamba ni kutoka Malawi, bila shaka hii kazi alipewa kwa kipindi kirefu, au kwa sababu baba yako pia alikuwa mtu makini kama alivyokuwa yeye na ndiyo maana kulikuwa na ugumu wa kumuua papo kwa papo, hivyo akaja huku kukaa kwa miaka kadhaa kwa ajili ya kumuua mzee wako,” alisema Simpson.
“Sasa kwa nini alimuua baba yangu?”
“Nitakuja kukwambia, hii ni siri kubwa ambayo hakuna anayeijua mbali na CIA, yote ni mambo ya kikazi, usijali, nitakwambia, na hili kukuthibitishia hili, nitakuletea ripoti kamili, nitakwenda Marekani na kuichukua.”
“Daaah! Sawa. Kwa hiyo hawezi kupatikana?”
“Anaweza, ila sitoweza kumuua, siwezi kumuua mtu ambaye sijapewa jukumu la kumuua.”
“Je kumkamata?”
“Naweza, ila kumfikisha kwako ni ngumu, ni mtu hatari mwenye uwezo wa kupambana na watu hata watano, mbali na hivyo, SIS kumkamata CIA ni jambo gumu na lisilokubalika kabisa, ni sawa na kumwandika mwandishi wa habari uovu alioufanya ukizingatia aandikwe na mwandishi mwenzake. Hii kazi haitowezekana,” alisema Simpson.
“Ooops! Haina tatizo!” alisema Victor.

Kila mmoja alitekwa na penzi la mwenzake, kila walipokuwa wakiangalia, walibaki wakitabasamu bila sababu yoyote ile. Usiku wa siku huyo ambao walilala pamoja, kila mmoja alichanganyikiwa na mwenzake, hakukuwa na mtu aliyeboreka au kumkwaza mwenzake.
Mathias akajionyesha kwamba alikuwa Mtanzania aliyekamilika asiyekunywa pombe wala kutumia viagra, nguvu alizopewa na Mungu ndizo zilizompeleka puta Rebecca kiasi kwamba akajutia kuchelewa kwake kuwa na mwanaume huyo.
Kuanzia siku hiyo, mapenzi ya wawili yao yakatengenezwa na hatimae kila walipokuwa, walikuwa pamoja hali iliyowafanya wanaume wengine ambao walijaribu kila njia kumpata Rebecca kuanza kumchukia Mathias aliyeonekana kuokota embe dodo chini ya mlimao.
“Kuna kitu nataka nikwambie mpenzi,” alisema Rebecca.
“Kitu gani?”
“Kuwa na mimi si jambo jepesi, kuna watu wengi watajiinua na kuanza kukuchukia,” alisema Rebecca.
“Watu gani?”
“Walionitaka na kuwakatalia.”
“Unahisi wataweza kuyaharibu mapenzi yetu?”
“Hapana! Hawawezi lakini ni wakorofi.”
“Kivipi?”
“Hawaoni hatari kumtoa mtu roho kwa ajili ya wanawake, kuna watu wengi walinusurika kuuawa na wengine kuuawa kisa wanawake,” alisema Rebecca.
“Achana nao, mimi hawaniwezi, kama fujo nazijua vizuri tu,” alisema Mathias.
“Sawa! Ila kuwa makini, siyo Tanzania hapa, hii inaitwa Malawi!”
“Usijali!’
Hii ilikuwa mara ya kwanza kwa Rebecca kuwa na mwanaume mwenye pesa, hakukuwa na tatizo lolote lile, kila siku alijisikia kuwa na amani huku akitumia fedha kadiri alivyotaka.
Mathias ambaye alijulikana kama Young Bilionaire aliendelea kusikika masikioni mwa watu, wale ambao hawakuweza kumfahamu kabla, wakatamani kumfahamu japo jina lake.
Hakikujulikana ni kitu gani kilitokea, baada ya wiki kadhaa, hakukuwa na picha yake yoyote ambayo ilisambazwa katika mitandao, na hata zile zilizokuwa zimeenea, haijulikani ni kitu gani kilitokea, zilipotea zote.
Kwa sababu alikuwa nchini Malawi kwa kazi maalumu, Mathias akakabidhiwa miwani maalumu iliyokuwa na uwezo wa kuzuia picha yoyote isitoke endapo angepigwa. Hilo ndilo lililosaidia, watu ambao waliahidi kwamba picha za Young Bilionaire zingeonekana ili kwa wale wasiomfahamu wamfahamu, walishangazwa na picha walizokuwa wakizipiga, hazikuwa zikionyesha sura, miwani ile ambayo iliwekwa kifaa kidogo sana cha kuzuia picha kutoka ilimsaidia.
Upepelezi wa kumtafuta Gideon ulikuwa ukiendelea kila siku, Martin akazoeleka kwamba alikuwa kichaa, katika mji wote wa Lilongwe ulimfahamu kama kichaa mkorofi hali iliyopelekea kila siku watu kufika kwenye mji huo kwa ajili ya kumpiga picha.
Muonekano wake ilikuwa ni vigumu mno kumgundua kwamba hakuwa kichaa kama alivyokuwa akionekana, alikuwa akishinda jalalani huku akiongea peke yake na kuvichapa fimbo vitu visivyokuwa vikionekana.
Kila mtu alimpuuzia, hakukuwa na aliyejua kwamba yule kichaa mkorofi aliyekuwa akivuma hapo Malawi alikuwa mpelelezi mwenye ujuzi aliyetokea nchini Tanzania.
“Kuna chochote?” aliuliza Materu, ilikuwa saa sita usiku, alikuwa akizungumza na Martin usiku.
“Hapana! Ila bado tunaendelea. Hatujajua kama yule mtu yupo hapa Lilongwe au la!”
“Lakini kutakuwa na mafanikio? Miezi miwili ishapita!”
“Mafanikio yatakuwepo tu, subiri tuendelee. Hata kama nitakaa miaka kumi, nipo tayari lakini huyu mjinga apatikane tu.”
“Basi sawa, hakuna tatizo!”
Siku ziliendelea kuyoyoma kila siku lakini hakukuwa na mafanikio yoyote yale. Martin aliendelea kuwa chizi huku kila siku akiyaangalia mandhari ya jiji hilo huku akimtafuta Gideon lakini ilikuwa ngumu mno kumpata mwanaume huyo.
“Nitampata tu, au awe nchi nyingine, ila kama ni hapa, nitampata tu,” alijisemea Martin, hakuonekana kukata tamaa.
****
“Una samaki wazuri, huwa unawavua wapi?” ilisikika sauti ya msichana mrembo, mkononi alishika kapu huku mbele yake kukiwa na mwanaume aliyevaa nguo zilizolowana akiuza samaki.
“Nawavua ziwani hapahapa Malawi, umewapenda?” aliuliza muuzaji huyo.
“Yaaap! Ni wazuri, wakubwa na wanaonekana kuwa watamu sana,” alisema mwanamke huyo.
“Hahah! Huwa siuzi kitu kibaya, najua kuvua samaki wakubwa.”
“Sasa ukitoka hapa unakwenda kuwauza wapi?”
“Nitaanza kuuza kule Livingstone.”
“Mmmh! Mbona unakwenda kuuza kwa matajiri, kwa nini usije kuuza kwa walalahoi?”
“Sasa samaki kama hawa dada yangu ukienda kuuza uswahili utapata hela kweli?”
“Mmmh! Sawa, haina tatizo, nifungie wawili,” alisema mwanamke huyo huku akimkabidhi muuzaji huyo hela yake.
Mishemishe zilikuwa nyingi pembezoni mwa Ziwa Malawi, wauzaji wengi walikuwa wamejikusanya wakiuza samaki waliokuwa wakiwavua katika ziwa hilo. Kila mmoja alionekana kuwa bize mahali hapo ambapo kama ingekuwa Dar es Salaam basi tungepaita Feri.
Wauzaji kutoka sehemu nyingine, wote walikusanyika sehemu hiyo ambayo muda wote ilinuka shombo tu. Miongoni mwa wauzaji waliokuwa wakiuza samaki mahali hapo alikuwepo huyu kijana masikini ambaye kwa kumwangalia tu ungegundua kwamba alikuwa na maisha magumu, aliitwa Mutombo.
Mutombo alikuwa akitokea katika Mtaa wa Kipemalo uliokuwa hapohapo Lilongwe, huko, ndipo walipokuwa wakiishi watu masikini kama ilivyokuwa Tandale jijini Dar. Hakuwa na maisha mazuri, kila siku, alitegemea kujiingizia kipato kupitia biashara aliyokuwa akiifanya.
Samaki aliokuwa akiwavua, walikuwa wakubwa ambao kila siku walimfanya kuwavuta wateja wengi waliokuwa wakimiminika nyumbani kwake alipokuwa akiwakaanga.
Maisha yake hayo yalilowea uswahilini lakini baadae akaamua kuhama na kuhamia katika Mtaa wa Livingistone. Watu wengi wakalalamika kwamba ilikuwaje ahame na wakati walikuwa wakimhitaji.
Huko Livingstone alipata wateja wengi waliokuwa wakivutiwa na samaki wake, matajiri wa huko wakawa wakinunua samaki kwa bei kubwa kutoka kwake ambapo alitafuta kibanda kimoja na kuamua kuwauza mahali hapo.
Jina lake huko Livingstone likawa kubwa, akaendelea kufanya biashara hiyo huku akijiingizia kipato kikubwa. Hakuna aliyejua alipatwa na maswahibu gani, baada ya miezi miwili kufanya biashara yake, akatoweka.
Kila mmoja alisikitika, halikuwa jambo jepesi na rahisi kuamini kwamba Mutombo hakuwepo tena, waliokuwa wamemzoea walijaribu kumtafuta lakini walishindwa kumpata.
Baada ya kupotea kwa miaka miwili, akarudi tena na alipoulizwa alipokuwa, alisema kwamba alipotea ziwani na kwenda kwenye Kisiwa cha Abulegela kilichokuwa katikati ya Ziwa Malawi, huko, ndipo alipoishi kwa miaka hiyo na kuamua kurudi Jiji Lilongwe.
Biashara ikaanza upya katika mtaa wa kifahari wa Livingsone, bado watu waliendelea kumpenda na kununua samaki wake kama kawaida. Jina lake likarudi tena, watu wakaendelea kumiminika kiasi kwamba kuna wengine walikuwa radhi kusafiri umbali mrefu lakini mwisho wa siku wafike katika mtaa huo na kununua samaki wa Mutombo.
Siku zikaendelea kukatika, mbali na uuzaji huo wa samaki uliompa jina kubwa, hakukuwa na aliyejua kwamba muuzaji huyo samaki aliyeitwa Mutombo, alikuwa mpelelezi kutoka katika Shirika la Kipelelezi la nchini Msumbuji, na alikuwa Malawi kwa ajili ya kumpeleleza Bwana Timoth, tajiri mkubwa aliyemiliki fedha nyingi kupitia biashara ya madawa ya kulevya aliyokuwa akiifanya.
Kupotea kwake kwa miaka miwili, ni kwamba alitumwa na Shirika la Kijasusi la Marekani, CIA kwa ajili ya kumuua Mhamasishaji, Potter Mickey nchini Tanzania kwa kujifanya mwanachuo na kutumia jina la Gideon.
Mara baada ya kukamilisha kazi hiyo, akaamua kurudi Malawi kwa ajili ya kumalizia kazi aliyopewa na kisha kurudi Msumbiji na kuunganisha mpaka Marekani kwa ajili ya kuchukua pongezi zake.
Huku akiwa kwenye mipango ya kumkamata au kumuua Bwana Timoth, hakujua kama kulikuwa na Watanzania wawili ambao kila siku walikuwa wakimtafuta huku wakiwa na lengo la kumkamata au kumuua endapo akileta ubishi.
Hakulijua hilo, aliendelea kupeleleza huku akitumia kivuli cha kuuzia samaki. Maisha yake yalikuwa hatarini bila kujijua, mbali na hiyo, kila siku aliendelea kujinyakulia wateja wengi wa samaki huku kila mmoja akijua kwamba kijana huyo alikuwa masikini wa kutupwa, kumbe nyuma ya pazia alikuwa mpelelezi mwenye fedha aliyetembea chini ya kivuli cha CIA, huku uwepo wake wa kuwepo Livingstone si kwamba alitaka kuuza samaki, alikuwa na kazi moja ya kuua mzizi mkubwa wa usafirishaji wa madawa ya kulevya, bwana Timoth.

Ilianza mwaka 1972, mwaka ambao biashara ya madawa ya kulevya ilishika kasi nchini Malawi. Vijana wengi walioonekana kuwa na nguvu ya kuliendesha taifa hilo wakajiingiza katika usafirishaji wa madawa ya kulevya na mwisho wa siku kuingia katika utumiaji wa madawa hayo.
Hawakuwa vijana wengi waliokuwa wamejiingiza katika biashara hiyo lakini kadiri muda ulivyozidi kwenda mbele wakazidi kuongezeka hali ilionekana kuwa mbaya, wale watu waliokuwa wakiaminika ndiyo waliokumbwa na mkumbo wa utumiaji wa madawa hayo yaliyokuwa yakiwaharibu akili na miili yao kila siku.
Hapo ndipo kulipoanza kuwa na wafanyabiashara wakubwa ambao mbali na biashara nyingine walizokuwa wakizifanya, waliitegemea biashara hiyo ambayo iliendelea kukua kwa kasi kadiri siku zilivyoendelea kwenda mbele.
Hakukuwa na usafirishaji wa madawa hayo kwenda nje ya nchi, walikuwa wakiuziana ndani kwa ndani lakini ilipofika mwaka 1985, watu wakaanza kutoka na kwenda nchi za Kiarabu kama Qatar, Iran, Iraq, na nchi nyingine katika Bara la Asia kwa ajili ya kupeleka na kuchukua madawa ya kulevya, biashara ambayo ilianza kuwapatia fedha nyingi wale waliokuwa wakiifanya.
Ulipoingia mwaka 1992, wafanyabiashara wakubwa wakagundua kwamba mbali na ndege ambazo walikuwa wakizitumia, pia walikuwa na uwezo wa kutumia usafiri wa meli za mizigo kwa ajili ya kufikisha mizigo yao, hivyo mara moja usafirishaji wa madawa kwa kutumia usafiri huo ikaanza kufanyika.
Walifanikiwa kwa kiasi kikubwa kwa kuwa hakukuwa na polisi waliokuwa na uwezo wa kugundua ni meli gani ilikuwa imebeba mizigo ya madawa ya kulevya, na hata kama walikuwa wakigundua, kila walipoingia ndani ya meli hizo, walitafuta kila kona lakini mizigo haikuwa ikionekana.
Watu wakatajirika huku vijana wengi wakipotelea katika matumizi ya madawa hayo. Japokuwa nchini humo kulikuwa na wauzaji wengi wa madaya ya kulevya, lakini kulikuwa na mtu aliyekuwa akiifanya sana biashara hii, huyu alikuwa Timoth Makenzi.
Kwa kumwangalia, alikuwa kijana mdogo wa miaka thelathini lakini maisha aliyokuwa akiishi yalimshangaza kila mtu. Alimiliki kiasi kikubwa cha fedha kwa kuwa yeye ndiye alikuwa mzizi mkubwa wa kusafirisha madawa kutoka ndani ya nchi ya Malawi huku pia akiwa mpokeaji mkubwa wa madawa hayo ambayo mengi yalikuwa yakiletwa kutoka Pakistan.
Alitajirika, alikula raha, alitembelea fedha na kila alipokuwa, kichwa chake kilifikiria fedha tu. Alinunua magari mengi ya kifahari huku akijenga nyumba kubwa za thamani ambazo ziliwafanya watu wote kubaki midomo wazi.
Japokuwa tetesi zilisikika kwamba Timoth alikuwa akihusika na uuzaji wa madawa ya kulevya lakini hakukuwa na mtu aliyekuwa na uhakika. Polisi hawakutaka kuwa nyuma, walichokifanya ni kuanza kumfuatilia hatua kwa hatua, lakini mwisho wa siku, hawakufanikiwa kupata kitu zaidi ya kuona kwamba fedha za mtu huyo zilikuwa zikiingia kutokana na biashara ya magari aliyokuwa akiifanya.
“I’m not dealing with coccain, I’m dealing with selling and buyying cars from Japan,” (Sijihusishi na madawa ya kulevya, najihusisha na uuzaji na ununuaji wa magari kutoka Japan) alisema Timoth.
“Are you sure?” (Una uhakika?)
“One hundred percent,” (Asilimia mia moja)
Polisi hawakuishia hapo, waliendelea kusikia tetesi kwamba Timoth alikuwa akijihusisha na uuzaji wa madawa ya kulevya lakini kila walipokuwa wakimfuata na kupekua nyumba nzima, hawakufanikiwa kuona madawa yoyote yale kitu kilichowashangaza sana na kubaki na maswali mengi.
Kitendo cha polisi hao kuja mara kwa mara nyumbani kwake kikamkosesha amani, alichokifanya ni kuanza kutumia fedha zake tu. Aliziamini fedha, aliamini kwamba hakukuwa na mtu aliyekuwa na nguvu ya kukataa fedha, hivyo akaanza kuzilamisha kufanya kazi aliyotaka zifanye.
Kitu cha kwanza kabisa alichokifanya ni kuwakamata wakuu wa polisi, alimini hao ndiyo ambao walikuwa mstari wa mbele kuhakikisha kwamba wanafika nyumbani kwake kwa ajili ya kumpekua.
Kwa kuwa alikuwa na fedha, kwa kila mkuu wa kituo cha polisi akampa ofa ya dola za kimarekani elfu tano ambazo ni zaidi ya kwacha milioni kumi na tano kwa ajili ya kuwafunga midomo. Hicho, kwao kilikuwa kiwango kikubwa cha fedha, wakajikuta wakiingia mkenge na kusahau kufanya majukumu yao ya kila siku.
Timoth akawa huru, akatanua soko lake na kuwaongeza wafanyakazi wake wa ndani. Madawa yaliendelea kusambazwa sehemu mbalimbali, kupitia yeye, wakaongezeka wauzaji wengine na kuufanya mnyororo kuwa mkubwa.
Ulipofika mwaka 2001 ambapo polisi walianza kuwatumia mbwa katika viwanja vya ndege kwa ajili ya kuchunguza watu waliokuwa wakibeba madawa, soko lake likaanza kuporomoka kwa kuwa vijana wake wengi walikuwa wakikamatwa.
“What should we do?” (Tufanye nini?) aliuliza mmoja wa vijana wake.
“I don’t know, can you just let me think about it?” (Sijui, unaweza kuniacha nifikirie juu ya hili?)
“No problem” (Hakuna tatizo)
Usiku wa siku hiyo ulikuwa wa mawazo mengi, hakulala, hakupenda kuona biashara yake ikianguka kwa kiasi kikubwa kisa tu mbwa walikuwa wakimharibia shughuli uwanja wa ndege.
Alichukua masaa mengi kujifikiria na mwisho wa siku kuja na jibu kwamba ilikuwa ni lazima madawa yasafirishwe kupitia maiti. Hiyo ikawa njia nyepesi na rahisi, walichokifanya ni kuelekea hospitalini, wakaanza kuchukua maiti, wakazipasua na kuziwekea madawa na mwisho wa siku kuzisafirisha.
Njia hiyo aliyoigundua ikaonekana kuwa bora na ilifanikiwa kwa kiasi kikubwa sana, akaanza kupanda juu kisoko kama kawaida.
Iliendelea kukatika miaka mingi huku utajiri wake ukiwa mkubwa. Polisi wote waliokuwa wakifuatilia, waliitwa chemba na kupewa kitu kidogo kilichowafanya kunyamaza. Tamaa za polisi hao zikawafanya vijana wengi kupotea, watumiaji wa madawa ya kulevya wakaongezeka kwa kiasi kikubwa mno.
Baada ya biashara hiyo kuendelea kwa siri, hapo ndipo serikali ikaamua kuungana na kitengo cha kipelelezi na kuanza kumpeleleza bwana Timoth aliyewafunga midomo polisi wengi hapo Malawi.
Ilikuwa ni siri kubwa, hakukuwa na mtu mwingine nje ya kitengo hicho ambaye alitakiwa kufahamu kilichokuwa kikiendelea, walichokifanya ni kumwambia kijana kutoka nchini Msumbiji mwenye uwezo mkubwa wa kufanya kazi za kipelelezi, huyu aliitwa Jonathan Mulumbu.
Mara baada ya kuambiwa kile kilichokuwa kikiendelea, akapanda ndege na kwenda nchini Malawi na kisha kupewa maelekezo yote na kile alichotakiwa kukifanya, hapo ndipo alipoanza kujifanya kijana masikini aliyekuwa akifanya kazi ya uvuvi na kuuza samaki.
Hakukuwa na mtu aliyekuwa amegundua, ilikuwa ni siri kubwa, polisi waliendelea kula hela kutoka kwa bwana Timoth bila kujua kwamba karibu na nyumba ya mzee huyo, kulikuwa na kijana maarufu kwa kuuza samaki ambaye kazi yake kubwa ilikuwa ni kupeleleza kila kilichokuwa kikiendelea.
Chini ya meza yake alikuwa na bunduki ndogo iliyofungwa vilivyo, kiunoni mwake alikuwa na bunduki nyingine ambayo haikuweza kuonekana kwani muda wote shati lake lilikuwa likiificha bunduki hiyo, mbali na hayo yote, pembeni yake kulikuwa na miwani ya macho, ilionekana kuwa ya kawaida sana lakini kwa undani, miwani ile ilikuwa ni kamera iliyokuwa ikichukua kila kitu kilichokuwa kikiendelea ndani ya nyumba ile, ilikuwa na uwezo wa kuona hata kilichokuwa kikiendelea nyuma ya ukuta.
Aliona kila kitu, watu waliokuwa wakiingia na biashara kufanyika, picha zilizokuwa zikipigwa mahali hapo, zilipelekwa moja kwa moja mpaka mpaka katika makao makuu ya kipelelezi nchini hapo. Jonathan ambaye alitumia jina la Mutombo akaonekana kijana nuksi ambaye hakustahili hata kusogelewa.
Kila kilichofanyika, bado kiliendelea kuwa siri. Polisi wa Malawi waliendelea ‘kupiga mpunga’ bila kujua chochote kile.

Miongoni mwa watu waliowahi kuvutiwa Rebecca kutokana na uzuri aliokuwa nao alikuwa bwana Timoth, msichana huyo aliutikisa moyo wake, kila alipokuwa akimuona sehemu mbalimbali yakiwemo magazeti na televisheni, aliusikia moyo wake ukiingiwa na tamaa ya kutaka kulala na msichana huyo.
Alijiamini kwamba alikuwa na fedha, alijiamini kwamba hakukuwa na msichana yeyote ambaye angeweza kumkataa, hivyo akajipa uhakika kwamba hata kama angemfuata msichana huyo ilikuwa ni lazima amkubali.
Alichokiwaza ndicho alichokifanya, baada ya siku kadhaa, alisimama mbele ya msichana huyo katika Klabu ya Espanyol, klabu ya watu maarufu na matajiri hapo Lilongwe na kuanza kuzungumza na msichana huyo.
Kwa kuwa aliziamini sana fedha zake, alichokifanya siku hiyo ni kutumia fedha zake vilivyo, kila alipokuwa akiagiza kinywaji hiki na kile, vingine vilifuata huku akitumia muda wake mwingi kuwatuza wasichana waliokuwa wakicheza klabuni hapo.
Alikuwa na sifa, alijitengenezea CV iliyompa uhakika kwamba Rebecca asingeweza kumkataa. Mara baada ya kufanya vitu vingi klabuni hapo, akaamua kuanza kuzungumza na msichana huyo mrembo.
“Nimekuwa nikikutamani kwa muda mrefu sana, wewe ni msichana wa kipekee sana, najiona kuwa na bahati kukutana nawe,” alisema bwana Timoth huku akimwangalia msichana huyo usoni.
“Asante, nikusaidie nini?”
“Ninahitaji kuwa nawe usiku wa leo.”
“Unafikiri nipo hapa kwa ajili ya kujiuza?”
“Hapana, usinifikirie hivyo, nakuchukulia kuwa u miongoni mwa wasichana wanaojiheshimu na kujitambua,” alisema bwana Timoth.
“Sawa, naomba uniache,” alisema Rebecca na kutaka kuondoka mahali hapo, akashikwa mkono.
“Subiri kwanza,”
“Kuna nini?”
“Yaani unataka uniache kiholela kweli? Kweli umeamua kuniumiza namna hii? Subiri basi.”
“Hapana. Nimeamua tu, naomba uniache,” alisema Rebecca.
Bwana Timoth hakukubali kushindwa, alimhitaji sana msichana huyo kwa usiku wa siku hiyo, kitendo cha kumuona akiondoka hivihivi bila kufanya chochote kile kilimaanisha kwamba alishindwa, yaani fedha zake hazikusaidia kitu chochote kile.
“Rebecca!” alijikuta akiita.
Rebecca hakuitikia, akaanza kupiga hatua kuelekea nje ya klabu ile. Kitendo kile kilimaanisha kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho kwa mzee huyo kuzungumza na binti huyo kwa usiku huo.
Wasichana wengine waliokuwa wakiona kila kilichokuwa kikiendelea mahali hapo, walimlaumu Rebecca kwani alikuwa akipoteza bahati waliyokuwa wakiililia usiku na mchana.
Rebecca akatoka ndani ya ile klabu na kuelekea nje, bwana Timoth hakutaka kubaki ndani, huku kitambi chake kikichezacheza akaamua kutoka nje. Bado alikuwa aking’ng’ania kuzungumza na mrembo huyo na mwisho wa siku kulala naye kwa usiku huo.
Hilo lilikuwa gumu, bado Rebecca aliendelea kuwa king’ang’anizi zaidi.
Alimbembeleza kadiri alivyoweza, hakujali fedha zake, alimsihi sana kuwa naye huku akimuahidi vitu vingi lakini bado msichana huyo alikuwa mbishi kukubaliana naye.
“Sawa, nashukuru kwa kila kitu, ila chukua hii,” alisema bwana Timoth huku akiwa amekishika kibunda cha fedha, kwacha milioni tano.
“Sikuhitaji wewe wala sihitaji fedha zako,” alisema Rebecca kwa dharau huku akimwangalia mzee huyo kuanzia chini mpaka juu, akalifuata gari lake na kuondoka zake.
Hilo lilikuwa moja ya matukio yaliyomuumiza mno moyoni mwake, hakuamini msichana kama Rebeca angeweza kufanya kitu kama kile, alisikia maumivu makali, kitendo cha kukataliwa penzi tena huku akiwa ametoa kiasi kikubwa cha fedha, ilimuumiza mno.
Baada ya miezi tisa, akapata tetesi kwamba kijana aliyekuja kwa kasi kwa kutumbua fedha, kijana aliyesadikiwa kwamba alikuwa na fedha zaidi yake, Young Bilionaire alikuwa ameingia nchini Malawi na mwisho wa siku kumchukua msichana huyo ambaye kila siku alilala usiku kucha akimuota.
Moyo ulimuuma zaidi, kila alipofikiria jinsi alivyokuwa amekataliwa na msichana huyo na mwisho wa siku kuja kuchukuliwa na mtu mwingine, alijisikia uchungu moyoni mwake. Hakutaka kuliona hilo likiendelea kutokea, kwa sababu alidhamiria kumchukua msichana huyo kwa nguvu zote basi akajiona kuwa na jukumu zito la kufanya mbele yake, hilo lilikuwa ni kumuua huyo mtu aliyejiita Young Bilionaire.
“Ni lazima nimuue,” alisema bwana Timoth huku akionekana kuwa na hasira.
“Nani bosi?”
“Mna risasi za kutosha?”
“Ndiyo!”
“Mna vijana wa kutosha?”
“Ndiyo mkuu! Kuna nini?” aliuliza kijana mmoja, alikuwa na mwili uliojengeka kimazoezi, muda wote alikuwa akivaa fulana.
“Kuna mnyama fulani nataka kummalizia, kanidhalilisha sana.”
“Yupi bosi?”
“Young Bilionaire.”
“Hakuna tatizo, bila shaka kitendo chake cha kumchukua Rebecca ndicho kilichosababisha, nipo nawe kiongozi, hata mimi nimekasirika sana, mbaya zaidi, nasikia ni Mtanzania, haiwezekani, lazima tummalize,” alisema jamaa huyo.
“Ninataka kazi ifanyike mara moja. Umesikia?”
“Ndiyo mkuu! Mpaka saa tisa usiku, atakuwa marehemu!”
Japokuwa alikuwa ametoa amri kwamba mtu huyo ilikuwa ni lazima kuuawa lakini bado moyo wake ulikuwa na hasira mno, kila wakati alikuwa akiyauma meno yake kwa hasira, hakutaka kumuona mwanaume huyo akiendelea kuwa na Rebecca, kisa tu ni kwa sababu alikataliwa.
Mipango ikapangwa, kijana yule aliyejulikana kwa jina la Matata akawaita vijana wake na kuwapanga tayari kwa kufanya mauaji hayo.
“Ila ni tajiri, hawezi kuwa na walinzi?” aliuliza jamaa mmoja, alikuwa miongoni mwa vijana waliokusanywa na Matata kwa ajili ya kufanya kazi hiyo.
“Hatujui, ila kwangu, sijawahi kumuona akiwa na walinzi, au awe ameanza wiki hii kuwa na nao,” alisema jamaa mwingine.
“Basi sawa, jipangeni, mpaka saa tisa nataka kazi iwe imekamilika.”
“Sawa mkuu. Tumuue kwa kifo gani sasa?”
“Apigwe risasi, ila isiwe ndani ya nyumba yake, hakikisheni mnamchukua na kumpeleka porini,” alisema Matata.
“Hakuna tatizo bosi.”
Sehemu nzuri ambayo walikuwa wamepanga kumkamata mtu wao ilikuwa ni katika klabu nyakati za usiku. Walijua fika kwamba hakuna kitu ambacho Young Bilionaire alikuwa akikipenda kama kwenda klabu usiku.
Usiku wa siku hiyo wakaanza kupeleleza ni mahali gani Young Bilionaire alipokuwa. Wakapewa taarifa kwamba alionekana katika Klabu ya Boniventure, klabu iliyokuwa na wacheza kamari wengi, hivyo wakaenda huko.
Walipofika, hawakutaka kuteremka, wakabaki garini huku wakianza kumsubiri. Gari lake la Lamboghin lilikuwa nje kitu kilichowafanya kuwa na uhakika kwamba mtu wao alikuwa ndani ya klabu ile.
Waliendelea kusubiri zaidi, ilipofika saa 9:14 usiku, Mathias akaanza kutoka ndani ya klabu ile huku akiwa ameongozana na Rebecca. Baadhi ya watu walikuwa wakimpongeza kwa kumpigapiga mgongoni kwani fedha alizozimwaga siku hiyo ndani ya ukumbi ule ilikuwa balaa.
Wote wawili wakaingia ndani ya gari lao la kifahari na kuondoka mahali hapo. Walichokifanya wale vijana ni kuanza kulifuatilia gari hilo lililokuwa likiendeshwa kwa mwendo wa kawaida.
Walipofika katika katika makutano ya Barabara ya Ilukweza na St. Joseph, kwa mwendo wa kasi, dereva wa gari la vijana wale akalifuata pale lilipokuwa limesimama kwenye mataa na kwa haraka wakasimamisha gari lao kwa mbele na kuteremka garini.
Huku wakiwa na bunduki mikononi mwao, vijana wawili wakaanza kulifuata lile gari, walipolifikia, wakavunja kioo, wakatoa loki na kuufungua mlango.
Rebecca alikuwa akipiga kelele za kuomba msaada lakini vijana wale hawakutaka kuacha kufanya kile walichokuwa wamekikusudia, wakamtoa Mathias garini, hata kabla hajaongea kitu chochote kile, wakampiga vibao na mateke na kumpeleka katika gari lao na kuondoka naye.
Safari ya kwenda katika Msitu wa Mushibwara ikaanza huku kila mmoja akiwa na hamu ya kutekeleza kile walichokuwa wamekipanga.
Kwa Rebecca, hakunyamaza, bado alikuwa akiendelea kupiga kelele tu. Hakukuwa na mtu aliyetokea, ilikuwa ni usiku wa saa tisa, kila alipopiga kelele, zilionekana kuwa kazi bure.
Hakukuwa na gari upande wowote ule, baada ya dakika mbili kuona hakukuwa na msaada wowote aliokuwa ameupata, akakaa katika kiti cha dereva na kuliwasha gari lake, safari ya kuelekea kituo cha polisi ikianza, machozi yalikuwa yakimbubujika huku akionekana kama mtu aliyechanganyikiwa.
Hakuwafahamu watu waliomteka mpenzi wake, Mathias aliyemjua kwa jina la Kenneth, hakujua malengo yao yalikuwa nini na walitumwa na nani. Kila alipokuwa akilia zaidi, ni kama aliisikia sauti moyoni mwake ikimwambia kwamba huo ndiyo ulikuwa mwisho wa maisha ya mpenzi wake, alitakiwa kumsalia sala ya mwisho.
Rebecca akazidi kulia!

ITAENDELEA


CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA TANO


Bwana Timoth alikuwa amekaa kitini mwake, alionekana kuwa na mawazo mengi, kitendo cha binti mrembo, Rebecca kuchukuliwa na mwanaume mwingine kilimuumiza mno.
Kichwa chake kilimuuma, aliwatuma watu kwa ajili ya kumuua mtu aliyekuwa amemchukua msichana huyo, Mathias, lakini mpaka katika kipindi hicho, hakupata taarifa zozote kama mchakato mzima ulifanikiwa au la.
Aliambiwa kwamba mpaka saa tisa usiku kila kitu kingekuwa kimekamilika, yaani Mathias aliyejulikana kwa jina la Kenneth au Young Bilionaire angekuwa kashauawa.
Hiyo ilikuwa ni saa kumi na moja alfajiri. Kila alipokuwa akiangalia simu yake kuona kama kijana wake, Matata alikuwa akimpigia simu, alikuwa kimya, hakukuwa na simu yoyote iliyongia.
“Kuna nini? Mbona kimya?” alijiuliza pasipo kupata jibu.
Hakutaka kulala, alikesha usiku mzima kwa ajili ya kufuatilia kile kilichokuwa kikiendelea. Alijaribu kuchukua simu yake na kumpigia Matata, simu ilikuwa ikiita lakini haikupokelewa, baada ya saa chache, ikawa haipatikani.
Akashuka kutoka kitandani na kuelekea sebuleni, kwa muonekano aliokuwa nao tu ulionyeshea ni namna gani alikuwa na mawazo tele.
Sebuleni hapo, akalifuata kochi na kutulia. Akachukua simu yake na kuanza kupiga tena, simu haikuwa ikipatikana.
Kwa sababu alikuwa na mawazo tele, alichokifanya ni kuifuata televisheni na kuiwasha. Ilipofika saa moja kamili, taarifa ya habari ikaanza kusomwa katika Kituo cha Televisheni cha MBC (Malawi Broadcast Co-operation).
Taarifa ya kwanza kabisa kusikika ilikuwa ni ya mauaji yaliyotekea katika Msitu wa Mushibwaha alfajiri ya kuamkia siku hiyo. Hakuonekana kushtuka sana lakini mara baada ya picha za maiti kuonekana, bwana Timoth akapigwa na mshtuko mkubwa.
Hakuamini kama vijana wake aliowatuma kwa ajili ya kumuua Mathias walikuwa wameuawa kinyama huku miili yao ikiwa imetobolewa kwa risasi kadhaa.
Hakuamini kile alichokuwa anakiona, akainuka kutoka kochini na kuisogelea televisheni ile, kile alichokiona kwa mbali na kukihisi kwamba ndicho chenyewe, hakikubadilka, kilikuwa kilekile.
“Matata...” alijikuta akilisema kwa mshtuko.
Hapo, akachanganyikiwa zaidi, walikuwa ni vijana pekee aliokuwa akiwategemea kufanya kazi zake kipindi chote, katika kila kazi alizokuwa akiwatuma, walizifanya kwa mafanikio makubwa ambayo yalimjengea kuwaamini zaidi.
Leo hii, vijana hao aliokuwa akiwategemea, walikuwa wameuawa vibaya msituni mara baada ya kuwatuma kumuua mtu aliyemchukua msichana mrembo, Rebecca.
“Hapana! Haiwezekani vijana wangu kuuawa!” alisema bwana Timoth pasipo kujua alikuwa akitaka kumuua mtu wa aina gani. Japokuwa Mathias alikuwa mwanaume tajiri, lakini undani wa maisha yake, hakuwa tajiri kama alivyokuwa bali alikuwa mpelelezi mwenye ujuzi wa kutumia bunduki na uwezo mkubwa wa kupigana na watu hata kama walikuwa kumi.
****
Gari ya kifahari, Lamboghin ilikuwa ikiegeshwa katika sehemu ya maegesho ya Kituo Kikuu cha Polisi hapo Lilongwe. Polisi wote waliokuwa nje, wakabaki wakilishangaa gari lile kwani lilikuwa ni miongoni mwa magari ya kifahari yanayovuma duniani.
Mlango wa gari hilo ukafunguliwa na Rebecca kuteremka, polisi wote wakapigwa na mshangao, si kwamba hawakumfahamu msichana huyo, walimfahamu lakini siku hiyo alionekana kuwa mrembo haswa.
Japokuwa ilikuwa ni usiku sana lakini kulikuwa na baadhi ya polisi waliokuwa mahali hapo, kwa mwendo wa madaha lakini wenye haraka akaanza kupiga hatua kuelekea katika mlango wa kuingia ndani ya jengo la kituo hicho.
Polisi waliokuwa nje ya jengo la kituo kile, walibaki wakimwangalia kwa macho ya matamanio, Rebecca hakutaka kujali, hakuwasalimia zaidi ya kwenda mpaka kaunta ya kituo hicho.
“Kuna nini Rebecca, mbona harakaharaka huku ukihema kwa nguvu?”aliuliza mmoja wa polisi waliokuwa kaunta.
“Mpenzi wangu ametekwa,” alisema Rebecca huku akilia.
“Unasemaje?” aliuliza polisi mmoja huku akionekana kutokuamini alichokisikia.
“Kenneth ametekwa.....!!” alisema Rebecca na kuanza kulia kwa sauti kubwa.
“Hebu subiri kwanza, vuta pumzi,” alisema polisi mwingine.
Rebecca akatulia, japokuwa hakuongea kitu chochote lakini bado aliendelea kulia, kila alipokuwa akikumbuka namna ambavyo mpenzi wake, Mathias alivyokuwa ametekwa na watu wasiojulikana na kupelekwa pasipojulikana, aliumia kupita kawaida.
“Aya hebu tueleze, nani ametekwa?”
“Mpenzi wangu!”
“Nani? Bilionea?”
“Ndiyo!”
“Ilikuwaje?”
“Kuna watu walikuja kutuvamia.”
“Muda gani?”
“Dakika kadhaa zilizopita.”
“Hivi ilikuwaje mpaka watu hao wakaja kuwavamia? Tena bila sababu?” aliuliza polisi mwingine.
Hapo ndipo Rebecca alipoanza kusimulia kila kitu kilichokuwa kimetokea, toka walipoingia ndani ya klabu mpaka walipotoka na mpenzi wake kutekwa waliposimamisha gari katika Makutano ya Barabara za Ilukweza na St. Joseph kulipokuwa na mataa.
Kwa sababu polisi walijua kwamba mtu aliyekuwa ametekwa alikuwa tajiri mkubwa, alichokifanya ni kujikusanya, wakachukua bunduki zao, wakaingia ndani ya gari lao na kuondoka huku wakiwa na Rebecca garini humo.
Safari yao iliishia katika makutano ya barabara hizo, walibaki wakiangalia huku na kule kana kwamba waliambiwa watu hao walikuwa wamejificha mahali hapo.
“Walielekea wapi?”
“Walielekea kule,” alijibu Rebecca huku akiinyooshea barabara iliyokuwa ikielekea upande wa Kaskazini.
Walichokifanya ni kuelekea kule walipoambiwa kwamba watekaji wale walielekea. Barabara ilikuwa tupu, hakukuwa na magari yaliyokuwa yakipita, walijaribu kuangalia huku na kule, hawakufanikiwa kumuona mtu yeyote yule.
“Tunatoka nje ya mji sasa, kweli tunaweza kuwapata?” aliuliza mmoja wa polisi wale, mkononi akiwa na bunduki yake.
“Huku tunajipoteza, tukienda kule, tunatoka nje ya Lilongwe, nadhani ni vigumu kufuatilia, cha msingi itatubidi tuanze msako kesho asubuhi,” alishauri mkuu wa polisi wale.
Hakukuwa na aliyebisha, kwa sababu kiongozi wao ndiye aliyeshauri hayo, wengine wakabaki wakiuunga mkono ushauri wake. Wakarudi huku wakiamua kuanza msako rasmi kesho yake.
*****
Gari likuwa likiendeshwa kwa kasi kuelekea katika Msitu wa Mushibwaha uliokuwa kilometa mia sabini kutoka katika Jiji la Lilongwe. Ulikuwa msitu mkubwa ambao mara nyingi watu waliokuwa wakifanya mauaji walikwenda kutupa miili ndani ya msitu huo.
Hakukuwa na simba wala chui, wanyama wengi waliokuwa wakipatikana ndani ya msitu huo walikuwa wale wanaokula majani tu. Ukubwa wa msitu huo ulikuwa ni kilomita mia tatu, kulikuwa na idadi kubwa ya miti mirefu ambayo mara nyingi watu wanaohusika na utengenezaji mbao walifika msituni hapo na kukata miti kadhaa kwa ajili ya matumizi hayo ya kutengeneza mbao.
Kwa sababu mauaji yalikuwa yameshamiri sana ndani ya msitu huo, serikali ikaamua kuweka ulinzi mkubwa lakini wala haikusaidia kwani polisi waliokuwa wakipewa majukumu hayo, walikuwa wakihongwa fedha kidogo na kuwaruhusu wahuni au wauaji kuingia msituni humo.
Msitu ukachafuka, damu zikatapakaa, kulikuwa na sehemu nyingi zilizokuwa zikitoa harufu mbaya ya miili ya watu au damu. Watu wakakatazwa kungia msituni humo kwani hali haikuonekana kuwa ya amani hata kidogo.
Gari lile liliendeshwa kwa kasi mpaka kuingia ndani ya msitu huo, hakukuwa na mtu aliyewaona kwa sababu ilikuwa ni usiku sana. Garini, waliendelea kumpiga makofi Mathias hata kabla ya kumuua.
“Ni lazima tukuue, haiwezekani utoke Tanzania halafu uje hapa na urukie wanawake wa watu,” alisema jamaa mmoja.
“Kosa langu ni nini?” aliuliza Mathias, alikuwa akijiamini kupita kawaida.
“Kutembea na mke wa mtu!”
“Kwani Rebecca aliolewa?”
“Hebu fumba mdomo wako, maswali ya nini.”
“Paaaaaa...” lilisikika kofi moja, lilitua usoni mwa Mathias. Hakuugulia maumivu, alikuwa kimya ila sura yake ilionyesha kwamba alikuwa na hasira mno.
Walipofika sehemu ambayo waliiona kufaa, wakateremka na kumshusha. Walikuwa vijana watatu huku kila mmoja akiwa na bunduki yake mkononi, kila mmoja aliikoki tayari kwa kumyatulia risasi Mathias aliyekuwa mbele yao.
Hawakujua ni kitu gani kilitokea na wala hawakujua ni kasi ya aina gani aliyokuwa nayo Mathias, ghafla, jamaa mmoja akajikuta akipigwa teke kali la mbavuni, mmoja wa wale vijana wawili waliobaki akashtuka na kutaka kufyatua akishikwa mkono wake ulioshika bunduki na kupelekwa begani na kuvunjwa kwa staili ya aina yake.
“Aauugghh...!” alipiga kelele jamaa huyo.
Yule mmoja aliyebakia, akaona usalama wake ni kumfyatulia risasi Mathias lakini cha ajabu alipofyatua risasi zile, akajikuta akimpiga mwenzake kwani alifanywa kuwa kama kinga na Mathias.
Likatoka teke moja takatifu lililotua shingoni mwa yule jamaa, kama mzigo, akajikuta akianguka chini kwani alipigwa sehemu iliyokuwa na mishipa mingi ya damu iliyoaanza kuvilia kwa ndani.
Haikuwa kazi kubwa, alitumia muda wa dakika moja tu kuwaweka chini wote. Jamaa yule aliyekuwa amevunjwa mkono bado alikuwa akiugulia maumivu pale chini, alichokifanya Mathias, akachukua bunduki na kuwamiminia risasi za kifua, alipomaliza, akaingia garini na kuondoka zake huku akiiacha miili ile msituni pale.

Polisi wakaanza kufanya upelelezi juu ya miili ile waliyoikuta katika msitu ule ikiwa imetobolewa na risasi kadhaa. Wakaanza kufanya msako ndani ya msitu huo kwa kuona kwamba wangeweza kuwaona watu waliowaua lakini waliambulia patupu, walichokifanya ni kuichukua na kuondoka nayo.
Uchunguzi wao haukuisha, kila walipoiangalia miili ile, ilikuwa ni ya watu waliokuwa wakiongoza kwa uharifu na fujo katika Jiji la Lulongwe. Walishukuru Mungu kuona watu ambao waliwashindwa kwa kipindi kirefu wakiwa wameuawa kwani wao walijaribu kufanya hivyo kwa miaka kadhaa lakini walishindwa.
Magazeti yalipotoa taarifa juu ya vifo vya watu hao akiwepo Matata aliyekuwa akiongoza kwa uharifu, watu wakanyoosha mikono yao juu kama ishara ya kumshukuru Mungu kwa kuona kwamba inawezekana ule uharifu uliokuwa ukifanyika mara kwa mara ungepungua.
Upande wa pili, usiku uliopita, Mathias alikuwa akitembea kuelekea nyumbani kwake. Hakuonekana kuwa na wasiwasi hata mara moja, japokuwa damu zilikuwa zimelichafua shati lake lakini hakutaka kujali, alichokuwa akikihitaji kwa wakati huo ni kufika nyumbani tu.
Alifika nyumbani baada ya saa moja, akaingia ndani na kutulia kochini. Alikaa mahali hapo kwa saa moja na ndipo mpenzi wake, Rebecca akaingia. Kitu cha kwanza, hakuamini kama yule aliyekuwa akimwangalia alikuwa mpenzi wake au la, akabaki akimshangaa.
Alimuacha katika makutano ya barabara alipokuwa ametekwa na watu asiowafahamu ambao waliondoka naye kuelekea pasipojulikana, sasa kwa nini katika kipindi hicho alikuwa mahali hapo? Kila alipokuwa akijiuliza, alikosa jibu.
“Kenneth! Is tha you?” (Kenneth! Ni wewe?) aliuliza Rebecca huku akionekana kutokuamini.
“It is me! Where have you been?” (Ni mimi! Ulikuwa wapi?) aliuliza Mathias.
“I went to police station, I had to report what happened, are you okey?” (Nilikwenda kituoni kutoa taarifa kilichotokea, upo salama?) alijibu Rebecca.
“I’m okey! Just give me a hug,” (Nipo salama, hebu nikumbatie) alisema Mathias.
Rebecca hakutaka kujivunga, alichokifanya ni kumsogelea Mathias na kumkumbatia. Moyo wake ulijawa na furaha tele lakini wakati mwingine alikuwa akijiuliza maswali mengi yaliyomfanya mpenzi wake kuwa nyumbani hapo na wakati alikuwa ametekwa na kupelekwa kusipojulikana.
Maswali hayakuishia hapo, kila alipokuwa akiziangalia damu zilizochafua shati lake, alibaki akitetemeka na kuhofia kwa kuona kwamba mpenzi wake huyo alikuwa amejeruhiwa na watu wale.
“Kuna mengi ya kukuuliza,” alisema Rebecca huku akijitoa kifuani mwa Mathias.
“Uliza tu.”
“Ilikuwaje? Mbona una damu halafu unasema hawakukujeruhi?”
“Ni habari ndefu, jua kwamba nilipambana nao!”
“Ulipambana nao?”
“Ndiyo! Huwa sipendi kupambana na watu, ila ilibidi iwe hivyo!”
“Mmmh! Una nguvu kweli?”
“Unanionaje? Mtoto wa mama?”
“Sidhani, nahisi kuna kingine, ukiniambia kwamba ulipambana nao, nahisi unanidanganya tu!” alisema Rebecca, kwa mbali tabasamu likaanza kujengeka usoni mwake.
Walikumbatiana kwa mara nyingine tena na kisha kuelekea chumbani. Hakukuwa na mtu aliyelala, kila mmoja alikuwa na hamu ya mwenzake hivyo wakabaki utupu huku wakikumbatiana na sauti ya kitanda tu kusikika usiku kucha.
Asubuhi iliyofuata, taarifa ya habari ilionyesha kwamba kulikuwa na vijana ambao waliuawa ndani ya Msitu wa Mushibwaha. Hapo ndipo Rebecca alipoamini kwamba mpenzi wake alikuwa nyuma ya kila kitu kwani baadhi ya vijana ambao waliuawa siku hiyo ambao aliwaona katika televisheni, aliwafahamu kwani ndiyo waliokuwa wakiongoza kwa vurugu na mauaji hapo Lilongwe.
****
Moyo wake uliendelea kumuuma, hakuamini kama vijana wake walikuwa wameuawa na mtu mmoja ambaye wala hakuufahamu uwezo wake. Hasira zake zikawaka, hakutaka kusikia kitu kingine chochote zaidi ya kummaliza Mathias kwa mkono wake.
Hakujua ni kwa jinsi gani angeanza kummaliza lakini alichokuwa akikiona, msichana Rebecca ndiye ambaye angemsaidia katika kukamilisha mauaji hayo aliyokuwa ameyapania.
Alichokifanya ni kuchukua simu yake na kuanza kuzungumza na msichana huyo, kitu cha kwanza kabisa alichokifanya ni kumuomba msamaha kwa kile kilichokuwa kimetokea miezi tisa iliyopita. Rebecca akawa muelewa, kwa kuwa mzee huyo alikuja kwa lengo la kumuomba msamaha, akakubaliana naye.
“Hakuna tatizo, nimekusamehe, na si kwamba nimekusamehe sasa hivi, toka kitambo tu,” alisema Rebecca.
“Nashukuru sana. Naomba nikukaribishe kwenye sherehe kesho,” alisema bwana Timoth.
“Sherehe gani?”
“Natimiza miaka sitini, ningependa uwe mgeni mwalika katika sherehe hiyo,” alisema mzee huyo.
“Sawa, hakuna tatizo, ila sitoweza kuja peke yangu.”
“Unataka kuja na nani?”
“Mpenzi wangu.”
“Sawa, usijali, uwepo wako ni muhimu zaidi.”
“Sawa, itafanyika saa ngapi?”
“Saa sita mchana.”
“Mmmh! Mbona mchana?”
“Mimi ni mzee, siwezi kufanya sherehe usiku, ninachoka mno,” alijitetea bwana Timoth.
“Sawa. Tutakuja.”
Furaha ya bwana Timoth ikawa kubwa, lengo lake la kumuua Mathias likaonekana kwenda kukamilika, kitu alichokifanya ni kuandaa mikakati ni kwa jinsi gani zoezi lake lingefanyika mchana wa siku inayofuata.
Kitu cha kwanza kilichomjia kichwani mwake ni kwamba ilikuwa lazima amuue Mathias kwa kumuwekea sumu kwenye juisi, sumu ambayo ingechukua siku mbili mwilini mwake na ndiyo imletee madhara makubwa na hatimae kumuua kabisa.
Akawaandaa vijana wake ambao walitakiwa kuwaleta watu kadhaa ambao hawakuwa wageni rasmi bali watu waliotakiwa kuonekana kama wageni katika sherehe hiyo. Kila kitu kilipokamilika, akaandaa vinywaji na kununua sumu iitwayo Sporthimus, sumu iliyoweza kuua baada ya siku tatu kuingia mwilini mwa binadamu.
“Itafaa, nitamuwekea kwenye kinywaji,” alisema bwana Timoth huku akionekana kuwa na furaha tele. Usiku huo ukawa wa raha kwake kwa kuona kwamba angekwenda kukamilisha kile alichokitaka kesho yake.

Saa 5:30 asubuhi, magari ya wageni bandia yakaanza kuonekana nje ya jengo la bwana Timoth, muda wote geti lilikuwa wazi hivyo kulifanya kila gari lililofika nje ya jengo hilo moja kwa moja kuingia ndani. Kila mgeni aliyeteremka, alikuwa amevalia suti kali huku pembeni akiwa na binti mrembo.
Kwa muonekano tu, kila mtu aliyekuwa akiingia ndani ya jumba hilo alionekana kuwa na pesa nyingi, hawakuwa na mionekano ya shida, walionekana kuwa watu wenye fedha na ilikuwa ngumu kugundua kwamba watu hao walipangwa kuingia ndani ya jumba hilo, lengo kubwa likiwa ni kuwazuga Rebecca na Mathias.
Saa 5:43 asubuhi, gari la kifahari, Lamboghin ilikuwa ikisimama nje ya jengo hilo, japokuwa mtaa wa Livingstone ulikuwa ukikaliwa na watu waliokuwa na fedha nyingi lakini hiyo haikutosha kutokuliangalia gari hilo kwa ukaribu zaidi.
Ilikuwa gari ndogo ya watu wawili tu ambapo milango yake ilikuwa ikifunguka kwa kwenda juu huku ikiwa imeshuka sana, kwa jinsi muundo wake ulivyokuwa, gari hiyo haikustahili kuendeshwa kwenye barabara za Tanzania kutokana na matuta yaliyokuwepo.
Mara baada ya milango kufunguliwa, Mathias na Rebecca wakaanza kuteremka, kila mmoja aliyekuwa ndani ya eneo la nyumba hiyo akabaki akiwaangalia tu, walionekana kupendeza kupita kawaida.
Mathias alikuwa amevalia suti nyeusi, huku ndani kukiwa na kikoi cheusi kulichokuwa nje ya shati jeupe lenye tai nyekundu, miguuni alikuwa amevalia moka nyeusi zilizopewa jina la ‘Four angle’
Kwa Rebecca, alivalia gauni lake refu la rangi ya pinki lililokuwa na mpasuko mpaka pajani na kulifanya paja lake jeupe kuonekana kwa ukaribu zaidi, paja lisilokuwa na doa hata moja, paja lililofananishwa na mwanamuziki mrembo kutoka nchini humo aliyejulikana kwa jina la Khadija ambaye alijipa jina la Dida.
Mbali na gauni hilo, chini alikuwa amevalia viatu vyake vilivyokuwa na kisigino kirefu vilivyokuwa na rangi ya pinki huku vikiwa na michirizi miyeusi kwa mbali, kichwani, alizifunga nywele zake vilivyo kama wanavyofunga wanawake wa Kiafrika waishio nchini Marekani.
Uso hakuuacha hivi hivi, aliupendezesha kwa miwani yake ya kike iliyokuwa na rangi ya pinki kwa mbali na masikio yake yaliwekewa hereni kubwa zilizomfanya kuvutia zaidi.
Ukiachana na mkoba wake wa bei mbaya, Rebecca alionekana kuvutia, kila mwanamke aliyekuwa ndani ya jumba lile alibaki akimshangaa, alionekana kuwa mwanamke wa kisasa.
Walitembea mpaka katika sehemu iliyokuwa na mkusanyiko wa wageni wengine na kuanza kumsalimia mmoja baada ya mwingine. Walikuwa wakinukia vizuri, manukato ya The Prince waliyokuwa wamejipulizia yalitoa harufu nzuri iliyopagawisha pua za watu wote mahali hapo.
“Tunavyoangaliwa, mpaka najisikia noma,” alisema Mathias huku akijifanya kusikia aibu.
“Hahaha! Hata wewe unasikia aibu?”
“Ndiyo! Ila umependeza sana, sijutii kuwa na msichana mzuri kama wewe,” alisema Mathias huku akionekana kuwa na furaha isiyo kifani.
“Asante mpezi, ila hata wewe umependeza mno, hakika sijuti kuwa na mtu kama wewe,” alisema Rebecca.
Mapenzi yaliwateka sana lakini kila siku Mathias alijitahidi kujificha, hakutaka kumuonyeshea msichana huyo kwamba alikuwa mpelelezi na aliletwa nchini humo kwa kuwa alikuwa katika kazi kubwa ya kumtafuta muuaji aliyefanya mauaji nchini Tanzania, Gideon.
Sherehe ikaanza huku kila mmoja akiwa na furaha, baada ya mhusika, bwana Timoth kuwakaribisha wageni, akaanza kuzungumza maneno kadhaa na baada ya kuridhika, akaruhusu vinywaji vipitishwe kwa watu ili waendelee kunywa huku yeye akiendelea kuzungumza.
Vijana walioonekana kuwa shapu, waliovalia mavazi yenye kuvutia, wakatokea mahali hapo huku wakiwa na vyombo vilivyokuwa na glasi zilizokuwa na juisi na kisha kuanza kuwapitishia watu.
Kijana ambaye alikuwa amepewa jukumu la kuwagawia juisi Mathias na Rebecca, akaanza kupiga hatua za harakaharaka kuwapelekea vinywaji vile, chombo chake kilikuwa na glasi mbili na hakutaka kumpa mtu yeyote glasi zile, aliendelea kupiga hatua mpaka alipowafikia, akawapa glasi zile, tena kwa nidhamu kubwa.
“Asante,” walisema kwa pamoja huku Mathias akishika ile glasi yenye sumu pasipo kujua kama juisi iliyokuwa ndani ya ile glasi, ilikuwa na sumu.
“Cheeers baby...!” alisema Mathias huku akiwa kwenye uso wenye tabasamu pana.
“Cheers...!” aliitikia Rebecca.
Wote wakaanza kuzipeleka glasi zile midomoni mwao.
****

ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA SITA


Bado Martin aliendelea kuigiza kama kichaa mitaani, watu waliendelea kumshangaa kila siku. Hakukuwa na mtu aliyemsogelea tena, bado alionekana kuwa kichaa mwenye hasira ambaye muda wowote ule alikuwa radhi kumchapa mtu yeyote kwa fimbo aliyokuwa akitembea nayo.
Katika kila sehemu aliyokuwepo, bunduki yake ilikuwa kiunoni mwake, alikuwa katika kazi nzito ambayo ingeweza kumchukua kipindi kirefu mpaka kukamilika.
Siku ziliendelea kwenda mbele huku kichaa huyo akiendelea kupata umaarufu kila siku. Alijulikana zaidi ya meya wa jiji hilo na makao yake makuu kama kawaida ilikuwa jalalani.
Aliendelea kufuatilia kila kitu kilichokuwa kikiendelea, japokuwa jeshi la polisi nchini Malawi lilikuwa na kitengo chao cha upelelezi lakini hakukuwa na mtu aliyeweza kugundua kama mtu waliyemuona kila siku kwamba ni kichaa, alikuwa mpelelezi kutoka nchini Tanzania.
Alizunguka kwa kipindi kirefu ndani ya jiji hilo, kila alipokuwa akiamka, alikuwa mjini lakini kuna kipindi akaamua kubadilisha mazingira, alitaka kutembea mitaani zaidi kwa kuamini kwamba huko angeweza kumuona Gideon.
Alianzia kwenye mitaa ya uswahili, alizunguka sana na hata wakati mwingine watoto kumuimba kama kichaa, hakujali, alijifanya kichaa mwenye hasira.
Katika kila sehemu aliyokuwa akipita, alikuwa akiangalia vizuri. Alizunguka kwa zaidi ya mitaa mitano ya uswahilini lakini hakuambulia kitu. Baada ya kuona kwamba hakuweza kufanikiwa, alichokifanya ni kuanza kuelekea katika mitaa ya uzunguni.
Huko, mitaa ilikuwa kimya sana, majengo makubwa na ya kifahari yalikuwa kwa wingi. Alizunguka katika mitaa mingi na mwisho wa siku akajikuta akiwa katika Mtaa wa Livingstone.
Mtaa huu ulionekana kuwa tofauti, kulikuwa na msururu wa magari yaliyokuwa yakiingia katika jumba moja la kifahari, hakujua jumba lile lilikuwa la nani kwani magari yote yaliyokuwa yakiingia, yalikuwa ya kifahari mno.
Huku akiendelea kuyaangalia magari yale, ghafla akaliona gari alilokuwa akilifahamu kabisa, ilikuwa Lamboghin ya rangi ya nyekundu ambayo alipewa Mathias kwa ajili ya kufanikisha kazi zake.
Hakutaka kufuatilia sana kwani alijua kwamba mwenzake naye alikuwa kwenye mchakato wa kuhakikisha kwamba kazi waliyokuwa wamepewa inafanikiwa kwa asilimia mia moja.
Aliendelea kusonga mbele, wakati amekata kona na kuingia katiba barabara nyingine ya vumbi iliyokuwa imezungukwa na majumba ya kifahari, akakutana na kundi la wanawake waliokuwa wamekusanyika sehemu moja huku wakionekana kama wamekizunguka kitu.
Alitamani kuuliza ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea mahali hapo lakini haikuwezekana kuwa hivyo kwani bado alijulikana kama mwanaume kichaa.
Hapo, shombo kali ya samaki ikaanza kuzisumbua pua zake na kupata jibu la moja kwa moja kwamba kundi lile la watu waliokuwa wamesimama mbele ya meza hiyo walikuwa wakichagua samaki kwa ajili ya matumizi nyumbani kwao.
“Jamani kichaa anakuja, atatuchapa,” alisema mwanamke mmoja, alionekana kuwa na hofu moyoni mwake.
Sauti ya mwanamke huyo ikawashtua wengine, walipogeuka, macho yao yakagongana na macho ya kichaa yule aliyekuwa akija huku fimbo ikiwa mkononi mwake.
Mmoja baada ya mwingine wakaanza kuondoka mahali hapo, walimfahamu kichaa huyo, alikuwa mkorofi ambaye angeweza kukuchapa fimbo wakati wowote ule tena pasipo kumfanya kitu chochote, wakaanza kutawanyika.
Ndani ya sekunde thelathini, hakukuwa na mnunuaji yeyote mbele ya meza ile zaidi ya muuza samaki aliyejulikana kwa jina la Mutombo tu. Macho ya Martin yalipotua usoni kwa Gideon, kwanza akashtuka, akaanza kumwangalia vizuri usoni.
Japokuwa aliiangalia sura hiyo siku moja tu tena katika kipindi ambacho alikuwa akitaka kuja nchini Malawi, lakini aliikumbuka vizuri sura ile, ilikuwa ni ya yule mtu aliyejitambulisha kwa jina la Gideon ambaye alijifanya kipofu na kumuua mjasiriamali, Potter Mickey nchini Tanzania.
Kwa jinsi alivyokuwa amemkodolea macho, kwa kiasi fulani Gideon akaonekana kushtuka, akaanza kuwa na wasiwasi juu ya kichaa yule aliyekuwa akimwangalia, akajiandaa kuchukua bunduki yake iliyokuwa chini ya meza.
Alichokifanya Martin ni kuanza kumsogelea Gideon kwa mwendo ambao ulizidi kumtia mashaka, alipoifikia meza ile huku mkono wa Gideon ukiwa chini ya meza tayari kwa kuchukua bunduki yake, Martin akachukua samaki mmoja na kuanza kukimbia naye, yote hiyo ilikuwa ni kucheza na akili ya Gideon ili aone kwamba alikuwa kichaa kweli.
Kwa kitendo kile alichokuwa amekifanya, Gideon akashusha pumzi, akajiona mjinga kwa kutaka kuchomoa bunduki yake chini ya meza na wakati mtu mwenyewe alikuwa kichaa na alimsogelea kwa ajili ya kuchukua samaki tu.
Martin aliendelea kwenda mbele huku mkononi akiwa na samaki yule, wanawake mbalimbali walikuwa wakimwangalia huku kila mmoja akimshangaa.
Martin alitembea mpaka katika geti la kuingilia katika jumba la kifahari la bwana Timoth na kuanza kugonga kifujofujo, lengo lake kubwa likiwa ni kutaka kuonana na Mathias ambaye alikuwa ndani ya jumba hilo, alitaka kumpa taarifa kwamba mtu waliyekuwa wakimtafuta kwa kipindi kirefu alikuwa katika mtaa huo, hivyo walitakiwa kumkamata.
“Ngoo..ngoo..ngoo..” aliendelea kuligonga geti lile, kila mtu aliyesikia, akazichukia kelele zile kwani ndiyo kwanza sherehe ilikuwa imeanza ndani ya jengo lile la kifahari.

Kelele za mlango ule ndizo zilizowashtua watu waliokuwa ndani ya eneo la jumba lile la kifahari la bwana Timoth ambao walikuwa wakiendelea na sherehe kama kawaida yao.
Kitendo cha Mathias kupeleka glasi yake mdomoni, hata kabla hajainywa juisi ile, mlango ukaanza kugongwa kwa fujo, kelele zikawa nyingi kutoka getini na kumfanya kusitisha zoezi lake la kunywa juisi ile.
Alichokifanya mmoja wa walinzi akaelekea getini pale, akalifungua geti ili kuona ni nani alikuwa akiugonga mlango huo kwa fujo, ghafla, akajikuta akivamiwa na Martin kichaa, akaingia ndani.
Kila mmoja akabaki na mshangao, hawakuamini kama yule kichaa aliyepata umaarufu kwa kipindi kirefu alikuwa ameingia ndani ya jumba lile, wanawake wakaanza kukimbia kwani kila mmoja alimuogopa.
Japokuwa alikuwa akimfahamu Martin, alichokifanya Mathias, naye akajifanya kumuogopa, akaanza kurudi nyuma kwa lengo la kutaka kujificha. Alipoyagonganisha macho yake na Martin, akapewa ishara moja ambayo hakukuwa na mtu aliyeweza kuiona mahali pale, ishara iliyomwambia kwamba asimame kwa kuwa kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea.
“Ameonekana?” hilo lilikuwa swali la kwanza alilojiuliza.
Martin akawa anaichezesha fimbo yake mkononi, akaanza kumsogelea Mathias mahali pale aliposimama na kuwafanya watu wote kuogopa kwamba angeweza kuchapwa na kichaa yule.
Huku akiwa amesogelewa, Martin akatoa ishara nyingine, ishara za siri ambazo hakukuwa na mtu yeyote aliyeelewa zaidi ya watu wa usalama wa taifa, ishara iliyomwambia kwamba ilikuwa ni lazima amkimbize.
Huku akiwa amemuelewa kabisa, Martin akachukua ile fimbo yake na kumchapa Mathias na kisha kuanza kukimbia kutoka nje. Mathias akajifanya kuwa na hasira, akatoka mbio na kuanza kumkimbiza Martin, hakukuwa na mtu yeyote aliyeelewa, naye Mathias akaonekana kama kichaa kwa kuwa alikuwa akimkimbiza kichaa.
“Kenneth...Kenneth....” aliita Rebecca lakini alikuwa amekwishachelewa, tayari wawili hao walitoka nje ya jengo hilo huku Mathias akiwa nyuma akimkimbiza Martin.
Kelele alizokuwa akizipiga Martin ndizo zilizowafanya watu wengi washangae, walikuwa wakijiuliza sababu ya Martin kukimbizwa na Mathias lakini hawakupata jibu, nao wakamchukulia kama Mathias alikuwa kichaa, na kama hakuwa kichaa, basi alikuwa amechokozwa na kichaa yule.
Mbio zao walikuwa wakielekea kule kulipokuwa na meza ile ya samaki ya Gideon ambaye alikuwa akiendelea kuuza samaki wake. Wakati wakiwa njiani, wanawake waliokuwa wamezunguka meza ile wakaanza kukimbia huku kila mmoja akimshangaa Mathias kwa kitendo chake cha kumkimbiza Martin kichaa.
Gideon hakuelewa kilichokuwa kikiendelea, alibaki akiwashangaa tu huku naye akiwa na swali kwamba ilikuwaje Mathias amkimbize kichaa yule lakini kitu alichokielewa, ni kwa sababu kichaa yule alikuwa mtata, basi ilikuwa ni lazima alimchokoza mtu huyo na ndiyo maana alikuwa akikimbizwa.
“Tutakimbia mpaka wapi? Mbona bado sijaelewa kinachoendelea? Huyo mtu mwenyewe yupo wapi?’ Mathias alikuwa akijiuliza maswali mfululizo pasipo kupata jibu.
Huku wakiwa wamefika karibu na ile meza ya samaki, Martin akaifuata na kuivamia, Gideon alitaka kuizuia lakini akashindwa, meza ikaanguka, samaki wote wakawa chini.
Hata kabla hajajua nini cha kufanya, akashtuka kuona mdomo wa bunduki iliyoshikwa na Martin kichaa ukimwangalia. Kuona hivyo, naye Mathias akatoa bunduki yake na kumnyooshea Gideon, kila mtu aliyekuwa akiliangalia tukio lile, akapigwa na mshangao.
Kichaa Martin kuwa na bunduki! Watu wote waliokuwa wakilishuhudia tukio hilo, wakapigwa na butwaa!

Gideon alibaki kimya, alikuwa akiwaangalia watu waliomzunguka, aliwagundua kwamba hawakuwa watu wa mchezo hata mara moja na walionekana kuwa na nguvu, ujanja, kujua mapigano hata zaidi yake, alichokifanya ni kuwa mpole tu.
Bado watu walikuwa wakiwaangalia, hawakuwa wakiwaelewa wale walikuwa wakina nani na walihitaji nini mpaka kumnyooshea bunduki muuza samaki.
Kitu ambacho kiliwashangaza watu zaidi ni kichaa Martin kushika bunduki na kumnyooshea Gideon. Wala hazikupita sekunde nyingi, Rebecca na watu wengine ambao walikuwa katika sherehe ile wakafika mahali hapo, hata wao walionekana kushangaa.
“Kuna nini mpenzi?” aliuliza Rebecca huku akimsogelea mpenzi wake, Mathias.
“Usinisogelee, baki hukohuko,” alisema Mathias huku akionekana kumaanisha kile alichokuwa akikizungumza.
Hakuwa na sura ya upole kama ile iliyozoeleka kila siku, leo hii, tena katika tukio kama hili, Mathias alionekana kuwa tofauti kabisa, hakuonekana kuwa na utani hata mara moja.
Kivutio zaidi mahali hapo kilikuwa ni Martin, yule kichaa aliyekuwa akivuma nchini Malawi, kitendo chake cha kushika bunduki bado kilizua maswali mengi.
Alichokifanya Martin, akamsogela Gideon huku Mathias akiwa na bunduki mkononi na kisha kumfunga pingu mkono mmoja huku mwingine akijifunga yeye na kuondoka mahali hapo.
Simu zikapigwa nchini Tanzania na kuwaambia kuhusu mafanikio makubwa yaliyokuwa yamepatikana katika ukamatwaji wa Gideon nchini Malawi, kwa haraka sana, ndege ya kijeshi ikatumwa mpaka nchini Malawi na kisha kupandishwa na kupelekwa nchini Tanzania.
Walipofika, hawakutaka kupoteza muda, moja kwa moja akapelekwa sehemu husika kwa ajili ya kuhojiwa kabla ya kufikishwa mahakamani kujibu mashtaka ya mauaji yaliyokuwa yakimkabili.
Usiku wa siku hiyo, taarifa zikaanza kutangazwa kwamba yule mwanaume aliyemuua bwana Mickey chuoni zikaanza kutangazwa katika vyombo mbalimbali vya habari hasa redio na televisheni.
Kutokana na maendeleo makubwa ya teknolojia, watu walizipata taarifa hizo kwa haraka sana, kila mtu aliijua taarifa hiyo kuhusu kukamatwa kwa muuaji huyo aliyekuwa akitafutwa kimyakimya.
“Kuna barua pepe nimetumiwa kutoka nchini Marekani,” alisema Materu, mkuu wa kitengo cha Usalama wa Taifa.
“Inasemaje?”
“Wamekiri kwamba wao ndiye waliyemtuma kijana huyo kumuua bwana Mickey!”
“Mmmh! Kwa nini sasa?”
“Hatujui!”
“Sawa. Kisha wamesemaje?”
“Kwamba tumuachie huru kwani huyo ni mtu wao!”
“Kivipi? Yaani naye ni jasusi?”
“Ndiyo!”
“Hapana! Haiwezekani kuwa kirahisi namna hiyo,”
Kila mmoja alibaki katika hali ya sintofahamu, barua pepe iliyotumwa kutoka nchini Marekani tena ndani ya Shirika la Kijasusi la CIA iliwashtua mno.
Hawakuamini kama kwa kipindi chote hicho walikuwa wakifanya kazi ya kumtafuta muuaji ambaye naye alikuwa jasusi kama jinsi walivyokuwa. Walipokea maombi yote ya Marekani lakini kumuachia Gideon huru likaonekana kuwa jambo gumu sana, hawakutaka kukubaliana nalo.
Waliendelea kumshikilia mpaka pale ambapo CIA ilipotuma mwakilishi wake nchini Tanzania kwa ajili ya kulizungumzia jambo hilo.
Bwana Mendez, mwakilishi kutoka nchini Marekani katika Shirika la Ujasusi la CIA akafika nchini Tanzania na moja kwa moja kwenda katika Jengo la Usalama wa Taifa kwa ajili ya kulizungumzia suala lao.
Huko, aliwaambia kila kitu kilichokuwa kikiendelea na hata mauaji ambayo yalifanyika, yalitakiwa kufanyika miaka mitatu nyuma lakini kutokana na uzoefu aliokuwa nao bwana Mickey, hakuweza kuuawa kipindi hicho.
“Kwa hiyo mkaamua kumleta mtu wenu nchini Tanzania katika chuo kikuu ili kukamilisha kazi yenu?” aliuliza bwana Materu, walikuwa wamekaa katika chumba kikubwa cha kukutania kwa ajili ya mikutano, walikuwepo na viongozi wengine.
“Ndiyo! Hiyo ni sababu iliyotufanya tumtume mtu ili asigundue.”
“Sawa. Sasa mlijua vipi kama angekuja nchini Tanzania? Na kwa nini iwe Tanzania na isiwe uarabuni?” aliuliza bwana Materu.
“Tofauti na Afrika, angeshtukia na lingekuwa suala gumu sana. Mickey hakuwa mtu wa kawaida, alikuwa mtu wa juu mwenye uwezo mkubwa sana, akili nyingi, bila kufanya hivi, angeweza kutuletea balaa hapo baadae kwani alivunja sharti letu kubwa, hivyo alitakiwa kuuawa,” alisema bwana Mendez.
“Tumekuelewa, ila ni kwa nini mlimuua bwana Mickey?” aliuliza Materu.
Bwana Mendez akakaa kimya kwa muda, akaanza kumwangalia kila mtu aliyesimama mahali pale, alionekana kama alikuwa akiwachunguza, aliporidhika, akayahamisha macho yake na kuiangalia saa yake aliyoivaa.
Swali hilo likaanza kuyarudisha mawazo yake nyuma kabisa, toka alipoanza kazi katika shirika hilo la kijasusi na mpaka alipokutana na bwana Mickey ambaye kwa kipindi hicho alikuwa kijana mdogo.
Alikumbuka mengi, mwisho wa siku, akashusha pumzi ndefu.
“Unaweza kutuambia sababu ya nyie kumuua bwana Mickey? Hata kama kuna vizuizi vya wewe kutuambiwa, hebu tuweke wazi,” alisema bwana Materu.
Mendez hakuzungumza kitu, alibaki kimya huku akionekana kama mtu aliyekuwa akifikiria jambo fulani. Alikaa katika hali hiyo kwa sekunde kadhaa kisha kushusha pumzi ndefu na kuachia tabasamu la mbali lililoonekana kuwa na mashaka.
Aliwaangalia watu waliokuwa ndani ya chumba kile, walionekana kuwa watu makini sana lakini kwa jinsi alivyokuwa akijiamini, kuna kipindi kingine aliwaona kuwa watu wa kawaida mno, alichokifanya, akaipeleka mikono yake mezani, mkono wake mmoja ulikuwa na tattoo kubwa iliyosomeka ‘Merciless’ (Isiyo na huruma)
“Historia ya maisha ya bwana Mickey inaanzia mbali sana,” alisema Mendez.
“Tunajua, unaweza kutuambia yote kisha na sisi tutafanya uamuzi wetu,” alisema Materu.
“Hakuna tatizo, historia yenyewe ipo hivi…..” alisema bwana Mendez na kuanza kusimulia historia ndefu ya bwana Mickey, mengi yaliyokuwa yametokea huko nyuma mpaka Marekani kuamua kumtuma mtu amuue. Kila mtu alikuwa kimya akimsikiliza.

Kilikuwa ni kipindi cha baridi kali jijini New York, theluji zilitapakaa katika kila kona ndani ya jiji hilo hali iliyopelekea barabara zote za lami kutokuonekana kabisa kitu kilichopelekea halmashauri ya Jiji hilo kuleta magari kadhaa kwa ajili ya kuziondoa theluji hizo barabarani.
Mazingira yalikuwa mabovu, viwanja vya mpira, tenesi, NFL na vinginevyo vikatawaliwa na theluji hiyo iliyoonekana kila kona. Watu wakavaa makoti makubwa huku baadhi yao wakiwa na miamvuli kwani theluji iliyokuwa ikiendelea kudondoka, ilimkera kila mtu.
Huo ulikuwa mwezi wa saba, kipindi ambacho huwa na baridi kali nchini Marekani, waliokuwa wakicheza michezo ya kuteleza katika barafu, hicho kilikuwa kipindi chao na mashindano kadhaa kuanzishwa.
Mtoto wa miaka kumi na tano alikuwa amejikunyata karibu na pipa la takataka lililokuwa likiwaka moto, alikuwa akisikia baridi kali, koti kubwa alilokuwa amelivaa lililokuwa limechakaa mno, likaonekana kutoumsaidia kabisa.
Meno yake yalikuwa yakigongana, kila alipokuwa akizungumza au kupumua, moshi fulani ulitoka mdomoni mwake kwani kulikuwa na baridi kali mno.
Hakukuwa na mtu aliyemjali, wapitanjia wengi waliokuwa wakipita mahali alipokuwa, walikuwa wakimwangalia na kumpuuza, japokuwa alikuwa ameweka chombo kidogo mbele yake kwa ajili ya kupata msaada wa fedha kama ambavyo anafanya kila siku, siku hiyo ikaonekana kuwa gundu kwake.
Aliyatamani maisha mazuri, hakutaka kuendelea kuishi katika maisha hayo hata siku moja, alihitaji kuwa na magari ya kifahari, kuwa na nyumba kubwa na nzuri, kuwa na kiasi kikubwa cha fedha katika akaunti yake, lakini kwa jinsi hali aliyokuwa nayo, kila kitu kikaonekana kuwa ndoto ya mchana.
Kila alipokuwa akiyaona magari yaliyokuwa yakipita katika barabara nyingi ikiwepo St. Joseph Hill 34W, moyoni alijisikia kuwa na maumivu makali kiasi kwamba kuna wakati alimlaumu Mungu, aliona kama amemtenga na kuwapendelea watu wengine.
Baba yake alifariki kwa ugonjwa wa kansa ya damu miaka miwili iliyopita katika Hospitali ya Lauren Medical Center iliyokuwa jijini Washington DC huku mama yake akimkimbia kwa sababu tu hakuwa na maisha mazuri hata kidogo na aliogopa kuwa na majukumu mengi lakini mbali na hilo, ukweli ni kwamba alipata mwanaume mwingine na kumwambia kwamba hakuolewa na wala hakuwa na mtoto yeyote yule.
Hakujua wapi pa kwenda, baada ya kukaa kwa kipindi cha miezi kadhaa huku akila na kulala mitaani, hapo ndipo alipoamua kujiunga rasmi na kundi la watoto wa mitaani jijini New York waliojipa jina la Outcast (Watengwa).
Hilo lilikuwa kundi kubwa la watoto wa mitaani na wa watu wasiojiweza ambao waliishi ndani ya jiji hilo huku muda wao mwingi wakiutumia kushinda karibu na mapipa yao machafu huku wakiwa wameyawasha moto kutafuta joto.
Hakukuwa na mtu aliyekuwa akipita mitaa hiyo kwani pamoja na kuwaomba watu fedha lakini kundi hilo la watoto hao ndilo lililoongoza kwa unyang’anyi mkubwa.
Kutembea na visu viunoni lilikuwa jambo la kawaida mno, kutokana na upatikanaji bunduki kuwa mwepesi nchini Marekani, baada ya muda nao wakajikuta wakimiliki bunduki.
Maisha hayo ndiyo aliyoamua kuishi, hakutaka kuondoka jijini humo kwani ndiyo sehemu pekee iliyokuwa ikimpa chakula na kiasi fulani cha fedha kwa ajili ya kuyaendesha maisha yake.
Hakuwa msafi wala hakuwa na fedha lakini kijana huyo alionekana kuwa tofauti na wengine katika kundi hilo. Uwezo wake kichwani wa kufafanua vitu na hata kutoa njia mbalimbali ambazo zingewawezesha kupata fedha zilikuwa kubwa kiasi kwamba kila mmoja alionekana kumshangaa.
Kwa hilo, akajikuta akipendwa na kila mtu, kila aliyetaka ushauri, alimpatia huku akiwasisitizia vijana wenzake wa kundi hilo kufanya jambo jingine zuri mbali na kuiba na kutumia fedha shaghalabaghala.
Ili kuonyesha mfano kwa wengine, kiasi kidogo cha fedha alizokuwa akigaiwa mara baada ya kuomba mitaani au hata kupora, alikuwa akizifungulia biashara lakini ugumu ulikuja pale alipokuwa akizihifadhi, wenzake walikuwa wakimuibia na hivyo biashara zake ndogondogo kufa.
“Do you see these New Yorkers?” (Unawaona hawa Wa New Yorkers?) aliuliza kijana huyo, alikuwa akiwazungumzia watu waliokuwa wakiishi jijini New York.
“Yes! What the hell with them?” (Ndiyo! Wana nini?)
“They have got lot of money, so, we have to take it from them,” (Wana fedha nyingi mno, kwa hiyo tunatakiwa kuzichukua kutoka kwao)
“How can we rob them? We are only two people, can we be able to take it from them? What if they have guns! Don’t you see they will shoot us down?” (Tutaweza vipi kuwapora? Tupo wawili tu, tutaweza kuzichukua kutoka kwao kweli? Je kama wana bunduki! Hauoni kama wanaweza kutufyatulia risasi?) aliuliza Sam, mmoja wa watoto wa mitaani.
Hapo ndipo kijana huyo alipoanza kufafanua kwamba maana yake haikuwa kushika bunduki au kisu na kuwavamia bali walitakiwa kufanya jambo ambalo lingewafanya watu hao wote kutoa fedha mifukoni mwao na kuwagawia kwa kununua vitu watakavyokuwa wakiviuza.
Hiyo ikaonekana kuwa akili nzuri lakini ilihitaji fedha kwa ajili ya kuanzisha biashara hizo. Walikuwa na umri mdogo hivyo upatikanaji wa fedha haukuwa rahisi kama kwa watu wengine.
Walichokifanya ni kujaribu kwenda katika hoteli kubwa mbalimbali kwa ajili ya kuomba kazi ili waweze kupata fedha za kufanya biashara ambazo walikuwa wamezipanga.
Siku ya kwenda huko, wote wawili, kijana huyo na rafiki yake Sam wakaamua kuvalia vizuri na kwenda katika Mghahawa wa McDonald uliokuwa katikati ya Jiji la New York, walipofika huko, waliomba kazi ndogondogo za kufagia na kusafisha vioo lakini hawakuweza kukubaliwa kwani hawakuwa wamefuata utaratibu wa kuomba kazi.
“Kwanza kaandikeni barua,” ilisikika sauti ya bosi wa mghahawa huo.
“Ila kazi zipo?” aliuliza kijana huyo.
“Bado sijajua, ila mkituma barua, siku zikitokea tutawashtua,” alisema bosi huyo.
Hakukuwa na muda wa kuendelea kubaki mahali hapo, walichokifanya, tena huku baridi likiendelea kuwapiga ni kuondoka mahali hapo na kurudi mitaani. Nguo safi walizozivaa siku hiyo zikaonekana kutokuwasaidia kabisa.
Hayo ndiyo yalikuwa maisha yao mitaani, kila siku walikuwa wakijaribu kwenda sehemu mbalimbali kutafuta kazi lakini hawakuweza kufanikiwa. Siku zikaendelea kukatika mpaka mtoto huyo alipokuja kukutana na msichana mzuri, msichana mrembo ambaye kwa kumwangalia, hata kama alikuwa mdogo lakini alionekana kuvutia sana, huyu aliitwa Elizabeth Kenz, binti mrembo aliyekuwa na asili ya Ujerumani.
“What is your name?” (Unaitwa nani?) aliuliza Elizabeth.
“My name is Potter Mickey from Harlem,” (Naitwa Potter Mickey kutoka Harlem) alisema Mickey huku akiutaja mtaa waliokuwa wakiishi watu masikini hapo New York.
“Harlem! Ooh My God! I’ve never expected to meet someone from Harlem, you look handsome,” (Harlem! Ooh Mungu wangu! Sikutegemea kukutana na mtu anayetokea Harlem, unaonekana mzuri mno) alisema Elizabeth huku akionyesha tabasamu pana.
Huo ndiyo ukawa mwanzo wa wawili hao kukutana. Japokuwa walikuwa na umri chini ya miaka kumi na nane lakini bado walionyeshana mapenzi ya dhati. Kila mmoja akatokea kumpenda mwenzake, walithaminiana lakini hakukuwa na mtu aliyekuwa radhi kumwambia mwenzake jinsi alivyokuwa akijisikia moyoni mwake.
Elizabeth alitoka katika familia ya kitajiri, alikutana na Mickey katika kipindi alichokuwa amekwenda maktaba na baba yake. Kwa kumtazama tu, hakuonekana kuwa na fedha, alionekana kujaa shida kwani hata muonekano wake, ulikuwa ni wa kimasikini sana.
Kila mmoja akaanza kumuonea aibu mwenzake, hakukuwa na aliyekuwa na uwezo wa kumwangalia mwenzake machoni kwa zaidi ya dakika moja, wote wawili walikuwa wakijisikia aibu.
Wazazi wa Elizabeth wakamfahamu Mickey kama rafiki wa binti yao hivyo wakati mwingine walikuwa wakimpa nafasi ya kuja nyumbani hapo, kukaa na binti yao na kisha usiku kuondoka, alipokuwa akiondoka, hakukuwa na mtu aliyegundua kwamba Mickey alikwenda mitaani, kulala karibu na mapipa yaliyowashwa moto, maumivu yote hayo ya maisha yalibaki kuwa siri yake, hata Elizabeth, hakutaka kumwambia. Umasikini ulimtesa mno!

ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
Hii ni sawa kweli, kichwa cha hadithi kwa kiingereza halafu ndani hadithi kwa kiswahili?
Book's title gets completely changed in order to sound better in a new language.

Books are often released under different titles in different countries, based on what the publisher thinks their readers will be drawn to.

Labda unisaidie mkuu, kitabu hiki kwa kiswahili ungekiitaje?
 
SEHEMU YA SABA

“Stop Elizabeth! Stop! Please don’t come closer, your father will find out,” (Acha Elizabeth! Acha! Tafadhali usisogee karibu, baba yako atajua) alisikika Mickey akimwambia Elizabeth kwa sauti ya chini ambayo alihakikisha isingeweza kusikika mpaka chumbani kwa wazazi wa binti huyo.
“Are you going to tell him?” (Utamwambia?)
“No! But he will find out, please! Stop,” (Hapana! Lakini atajua tu, tafadhali, acha) alisema Mickey huku akionekana kuwa na hofu.
Wawili hao walikuwa wamekaa sebuleni, giza lilikuwa limeingia huku saa ya ukutani ikionyesha kwamba tayari ilikwishatimia saa moja usiku. Mickey hakutaka kubaki nyumbani hapo, siku nyingine, muda kama huo tayari alikuwa amekwishaondoka lakini siku hiyo hali ilikuwa tofauti kabisa.
Elizabeth hakutaka kuona Mickey akiondoka, alitaka kumuona akikaa mpaka asubuhi. Walitulia sebuleni huku wakiangaliana tu, macho ya Mickey yalionyesha wasiwasi mwingi kwani kila alipokuwa akimwangalia Elizabeth, aliyasoma macho yake na kugundua ni kitu gani msichana huyo alitaka kukifanya.
Hata kabla hajafanya chochote kile, msichana huyo akaanza kumsogelea kochini pale huku akiuandaa mdomo wake kukutana na mdomo wa Mickey kitu kilichomuongezea hofu kubwa kijana huyo.
Alimheshimu mzee Kenz, alimchukulia kama baba yake, kila alipokuwa akimwangalia msichana huyo na kile alichotaka kukifanya, kichwa chake kilimkumbuka mzee huyo siku ambayo alimkaribisha ndani ya nyumba hiyo na kumuonya kuhusu tabia mbaya ambayo angejaribu kuifanya kwa binti yake, basi angeweza kumuua.
Bado alimkataza Elizabeth kufanya kile alichokusudia kukifanya, kwa msichana huyo, hilo lilikuwa jambo gumu, tayari mwili wake ulipata mhemko wa hali ya juu, hakuwa radhi kumuona Mickey akiondoka nyumbani kwao pasipo kumnyonya mdomo.
Alikuwa binti mdogo lakini hakuweza kuwa msiri, hisia zake za mapenzi zilikuwa wazi na alikuwa tayari kumuonyeshea mvulana huyo kwamba alikuwa akimpenda na hakutaka kumpoteza.
Huku akiogopaogopa, ghafla akajikuta mdomo wake ukikutana na mdomo wa Elizabeth, na pasipo kutarajia, wakaanza kubadilishana mate.
Alikataa kwa kuwa alijua kwamba angejisikia vibaya lakini baada ya kitendo kile kutokea, akajikuta akivikunjakunja vidole vyake kwa raha aliyokuwa akiisikia, pasipo kupenda, akaikuta mikono yake ikienda kifuani mwa Elizabeth na kuanza kukipapasa.
Huo ukawa mwanzo wa mchezo wao mchafu, ratiba ya Mickey kuondoka ndani ya nyumba hiyo ikabadilika, hakuwa akiondoka jioni, alisubiri mpaka giza liingie ndiyo aondoke nyumbani hapo.
“Itakuwaje baba yako akijua?” aliuliza Mickey, katika kipindi chote walichokuwa wakifanya mchezo huo, siku zote alikuwa akisikia hofu moyoni mwake.
“Hatofanya kitu.”
“Mhh!”
“Ndiyo! Kwanza atajuaje? Unafikiri nitamwambia, hawezi kujua, niamini.”
“Sawa! Lakini sisi bado wadogo, hukumsikia mama alivyosema siku ile kwamba mpaka tukue?”
“Hapana! Mama alitudanganya kwa kuwa hakutaka tuwe karibu. Nimekwishakua, si unaona kifua changu kilivyokuwa kikubwa!”
“Elizabeth! Lakini mbona tunawahi sana kufanya mchezo huu, unajua namuogopa sana baba yako!”
“Usimuogope, hawezi kufanya kitu.”
“Una uhakika?”
“Ndiyo! Hebu sogea karibu yangu!”
“Hapana, sogea wewe.”
“Sawa.”
Japokuwa hawakuwahi kufanya mapenzi, lakini usiku huo ulikuwa ni wa burudani kwao wote, walikumbatiana na kupapasana hapa na pale, miili yao ilishikwa na mihemko lakini kila mmoja aliogopa kuvua nguo zake, hivyo wakabaki wakipapasana tu kochini.
Hakukuwa na mtu yeyote ndani ya nyumba hiyo zaidi yao na wafanyakazi ambao muda wote walikuwa jikoni na sehemu nyingine.
Waliendelea kupapasana sebuleni pale na mwisho wa siku, hali hiyo ikaonekana kuwashinda, walichokifanya ni kuanza kuvuana nguo. Kwa wakati huo, kila mmoja alikuwa akiwaza lake, hofu aliyokuwa nayo Mickey ikamtoka kabisa, hakufikiria tatizo ambalo angelipata, kitu pekee alichokuwa akikifikiria kwa wakati huo ni kuuridhisha mwili wake tu.
“Siku ukileta ujinga wako kwa binti yangu! Nitakuua na mwili wako kuutupa porini uwe chakula cha ndege na wanyama,” aliisikia sauti ya bwana Kenz kichwani mwake, maneno hayo yalikuwa yakijirudia mara kwa mara kiasi kwamba nguvu za kufanya mapenzi zikaanza kumtoka.
“Subiri kwanza....” alisema Mickey! Wote walikuwa watupu.
“Ku..na ni..n..i mp..en...zi...?” aliuliza Elizabeth, tayari alikuwa katika ulimwengu mwingine wa kimahaba.
“Baba yako ataniua”
“Haw..e...zi...” alisema Elizabeth na kuendelea kumpapasa Mickey.
Kwa sababu Elizabeth alikuwa amekwishaamua, Mickey hakuwa na jinsi, alichokifanya ni kukubaliana naye.
Waliendelea kwa dakika zaidi ya kumi huku Eizabeth akijaribu kufanya kila alichoweza kuhakikisha kwamba anamdatisha Mickey. Hakuwa na uwezo kabisa lakini alijaribu kufanya kile alichokuwa akikijua. Waliendelea zaidi lakini ghafla, katika hali ambayo hawakuitarajia, mara mlio wa gari ukaanza kusikika nje ya eneo la nyumba hiyo getini.
Kama watu walioshtushwa na jambo fulani, wakasimama na kuanza kuangalia nje, geti la umeme likaanza kujifungua na gari kuingizwa kwa kasi kana kwamba dereva alikuwa akiwahi kitu fulani.
Walipoliangalia gari, lilikuwa ni la mzee Kenz, baba yake Elizabeth. Huku wakiwa hawajui wafanye nini, mlango wa gari ukafunguliwa na mzee huyo kuteremka huku akiwa na bunduki mkononi, akaanza kutembea kwa harakaharaka kuufuata mlango wakuingilia sebuleni.
Wala hazikupita sekunde nyingi, mlango wa upande wa pili ukafunguliwa na mke wake kuteremka, akaanza kumkimbilia mume wake huku akionekana kuwa na hofu.
“Kenz...usimuue, naombe usimuue...” alisikika mama yake Elizabeth maneno yaliyowashtua wote wawili pale sebuleni walipokuwa. Bwana Kenz alifura kwa hasira, kijasho kilikuwa kikimtoka na mwili kumtetemeka!
“Elizabeth! Tumekufa, baba yako amerudi,” alisema Mickey huku akivaa nguo zake kwa haraka sana.
“Kimbia Mickey! Kimbia baba atakuua,” alisema Elizabeth, hata naye alionekana kuchanganyikiwa.
“Siwezi! Miguu haina nguvu!”
“Baba atakuua...Mickey! Kimbia,” alisema Elizabeth huku akionekana kuchanganyikiwa, Mickey akashindwa kukimbia, kila alipotaka kuiinua miguu yake, aliiona kuwa mizito kana kwamba ilifungwa mzigo mkubwa wa mawe, akashindwa kabisa kuondoka, akabaki akitetemeka huku akiwa na hofu kubwa moyoni mwake.

Bwana Kenz alikuwa mwanaume tajiri aliyekulia nchini Marekani ila alizaliwa nchini Ujerumani na kumfanya kuwa Mjerumani hasa. Mara baada ya maisha kumpiga ndani ya Jiji la Berlin, hapo ndipo alipoamua kwenda nchini Marekani.
Huko, maisha hayakuwa mepesi kama alivyosikia, ili upate kula kila siku basi haukuwa na budi kufanya kazi kwa bidii sana. Kwake, kwa kiasi fulani maisha yalionekana kuwa mateso makubwa, kuingiza kipato cha dola ishirini kwa siku na kutumia dola kumi kwa ajili ya chakula cha siku nzima, hakika ilimuuma mno.
Alitambua kwamba alifika nchini Marekani kwa kuwa alikuwa mtafutaji, hakutaka kurudi nchini Ujerumani huku akiwa masikini kama alivyokuwa, alitamani kurudi tena nchini humo huku akiwa na utajiri wa kutosha.
Alichokifanya ni kuanza kuuza baga za Mc Donald karibu kabisa na viwanja wa timu zilizokuwa zikicheza mchezo wa NFL. Maisha yalikuwa magumu lakini kutokana na kuipenda sana biashara hiyo, akajikuta akianza kufanikiwa na kuwa muuzaji aliyejijengea jina kubwa kwa watu waliokuwa wakifika katika viwanja hivyo kwa ajili ya kuangalia mchezo huo.
Siku zilivyoendelea kwenda mbele, alipoona kwamba jina lake limekuwa kubwa zaidi, hakutaka kuendelea kuwa mfanyakazi wa kampuni hiyo bali alichokifanya ni kuanzisha baga zake mwenyewe. Alijua kwamba angeweza, hivyo kitu alichokifanya ni kumuita rafiki yake kutoka nchini Ujerumani, rafiki aliyekuwa mtaalamu wa kutengeneza baga, huyu alikuwa Hamman, ambaye baada ya kufika, wakaanza kutengeneza na kuuza.
Hayo ndiyo yalikuwa mafanikio makubwa yaliyowapatia kiasi kikubwa cha fedha na mwisho wa siku kujikuta wakifungua biashara nyingine nyingi.
Hapo ndipo mafanikio yalipoanzia, japokuwa walipata kiasi kikubwa cha fedha huku akichangia na rafiki yake, mtaalamu wa kutengeneza baga, Hamman lakini halikuwa jambo rahisi, walipambana mpaka kuhakikisha wanatoka na kufanikiwa.
Baada ya miaka miwili ya mafanikio makubwa ndipo alipoamua kumuoa mwanamke wa Kimarekani, huyu aliitwa Patricia. Alikuwa mwanamke mzuri kwa kumwangalia, upole wake, roho yake ya huruma ndivyo vitu vilivyowavutia watu zaidi.
Baada ya kuingiza zaidi ya dola bilioni nane kupitia biashara zao, wakaamua kugawana nusu kwa nusu na Hamman. Kutokana na uzoefu mkubwa wa biashara aliokuwa nao, Kenz akafanikiwa zaidi lakini kwa Hamman, fedha zake zikaishia katika michezo ya kamari tu jijini Las Vegas.
Baada ya kuishi miaka miwili na mkewe, ndipo walipopata mtoto wa kike na kumpa jina la Elizabeth. Walimpenda mtoto wao kiasi kwamba wakamuwekea ulinzi mkali ili asitekwe na watekaji na kisha kuhitaji kiasi kikubwa cha fedha.
Baada ya miaka kumi na moja, wakati binti yao akivunja ungo, bwana Kenz akaamua kufunga kamera ndogo za CCTV ndani ya nyumba yake kwani hata wafanyakazi wake hakuwa akiwaamini.
Kila kitu kilikuwa salama lakini baada ya kuanza kumruhusu Mickey ndani ya nyumba hiyo, kukaanza kuonekana mabadiliko makubwa hali iliyomtia wasiwasi na hivyo kuanza kufuatilia kilichokuwa kikiendelea katika kipindi alichokuwa kazini na binti yake kuwa nyumbani na Mickey.
Kupitia kompyuta zake za ofisini zilizounganishwa na kamera zile, akaanza kugundua michezo waliyokuwa wakiifanya wawili hao jambo ambalo lilimpa hasira kupita kawaida.
Kwa kuwa hakutaka kufanya mambo yake pasipo kumshirikisha mkewe, akaamua kumuita na kuanza kufuatilia pamoja kile kilichokuwa kikitokea kwani ulikuwa mchezo wa mara kwa mara.
Waligundua kwamba Mickey hakuwa na kosa ila binti yao, Elizabeth ndiye aliyekuwa akilazimisha wafanye mapenzi jambo ambalo kwa Mickey lilikuwa gumu kukubalika.
Siku ya tukio hilo lililomtia hasira, bwana Kenz alikuwa ofisini kwake na mke wake, hakutaka kuondoka mapema, alimuita mke wake ili kushuhudia upumbavu uliokuwa ukifanyika ndani ya nyumba yake.
Waliangalia kila kitu kilichokuwa kikiendelea sebuleni, kitendo cha kuwaona wawili hao wakipapasana, kiliwatia hasira wote, pasipo kutarajia, bwana Kenz akafungua droo yake na kuchukua bunduki yake.
“Twende nyumbani....!” alimwambia mkewe huku akionekana kuwa na hasira.
“Bunduki ya nini sasa?”
“Twende nyumbani...!” alisema bwana Kenz kwa hasira.
Safari ya kwenda nyumbani ikaanza.
****
Kila mmoja ndani ya nyumba alikuwa akitetemeka, mioyo yao ilijawa na hofu kubwa, kitendo cha kumuona mzee Kenz akija huku akionekana kubadilika kilimtisha kila mmoja.
Mkononi mwake alikuwa na bunduki ndogo, mwendo wake tu, ulitosha kukwambia kwamba kwa wakati huo mzee huyo alikuwa na hasira zaidi ya siku zote zile. Mickey alitamani kukimbia, lakini kitu cha ajabu, kila alipotaka kufanya hivyo, alishindwa kabisa.
Bado Elizabeth aliendelea kumsisitiza Mickey kukimbia kwani alijua fika kwamba baba yake alikuwa na hasira kali hivyo kama angemkuta ndani ya nyumba hiyo, ilikuwa ni lazima amuue.
“Mickey! My dad is coming to kill you, run away,” (Mickey! Baba yangu anakuja kukua, kimbia zako) alisema Elizabeth huku akimpiga kibao Mickey.
Kibao hicho kikawa kama kimemshtua kutoka katika bumbuwazi alilokuwa nalo, akaangalia vizuri nje, bado mzee huyo alikuwa akipiga hatua za harakahara kuusogelea mlango wa kuingia ndani ya nyumba hiyo.
Hakukuwa na cha kuchelewa, tayari alikiona kifo kuwa mlangoni, alichokifanya ni kuondoka kwa kupitia mlango wa nyuma, akaanza kukimbia kwenye majani mafupimafupi kuelekea nje.
Mzee Kenz akaufungua mlango na kuingia sebuleni, mwili wake ulikuwa ukitetemeka kwa hasira, kijasho kilikuwa kikimtoka. Eizabeth ambaye alibaki sebuleni pale, alibaki akiomba msamaha tu huku akimsisitiza baba yake asimuue Mickey kwani ni yeye ndiye alikuwa chanzo.
“I will kill him! where is he?” (Nitamuua! Yupo wapi?) aliuliza mzee Mickey.
“Please dad, don’t kill him,” (Tafadhali baba, usimuue) alisema Elizabeth huku akilia.
Kilio hicho hakikusaidia, bwana Mickey hakutaka kujali, hasira zake zilimkaba kooni, kichwa chake kilivurugika kwani kitendo alichokuwa akikifanya Mickey kilimkasirisha mno.
Alijaribu kumtafuta katika kila kona sebeuleni pale, Mickey hakuwepo jambo lilimkasirisha mno. Hakutaka kubaki mahali hapo, kwa kuwa mlango wa kwenda nyuma ulikuwa wazi, akajua kwamba kwa namna moja au nyingine Mickey alikuwa ametoka nje kupitia mlango huo, alichokifanya ni kuelekea nje kwa kupitia mlango ule.
Hakukuwa na giza, kulikuwa na mwanga mwingi na wa kutosha kabisa, kelele za mbwa kutoka kwa majirani zilikuwa zikisikika kila wakati kuonyesha kwamba kulikuwa na mtu aliyekuwa akikatiza huko.
Bwana Kenz hakutaka kuishia hapo, alijaribu kuyapeleka macho yake huku na kule lakini hakuweza kumuona Mickey, moyoni mwake aliumia mno, hakutaka kubaki hapohapo mlangoni bali alichokifanya ni kuanza kumtafuta sehemu mbalimbali ndani ya eneo la nyumba hiyo kwa kuamini kwamba kulikuwa na sehemu aliyokuwa amejificha.
Alimtafuta sehemu zote kuanzia kwenye eneo la maegesho ya magari mpaka kwenye bustani lakini kote huko, Mickey hakuwepo jambo lililomuongezea hasira mzee huyo.
Kwa harakaharaka akarudi ndani na moja kwa moja kumfuata Elizabeth, kwa jinsi alivyoonekana kipindi hicho, hakuonekana kuwa na utani hata kidogo, alikuwa amefura kwa hasira na hakutaka kuambiwa kitu chochote kile, alichokuwa akikitaka ni kumwaga damu tu.
“Where is your nigger?” (Mniga wako yupo wapi?) aliuliza bwana Kenz, alilitumia jina ambalo kwa Mzungu hakutakiwa kulitamka kwa kuwa lilionekana kuwa tusi.
“I don’t know, please dad, don’t kill him,” (Sifahamu tafadhali baba, usimuue) alisema Elizabeth huku akilia.
Huku akimwangalia binti yake kwa hasira, ghafla wakasikia alamu ya mlangoni ikianza kulia kumaanisha kwamba kulikuwa na mtu aliyekuwa ameligusa geti.
Kwa kasi ya ajabu, bwana Kenz akatoka sebuleni hapo na kuanza kuelekea kule getini. Kama ilivyokuwa kwake, hata mke wake na Elizabeth nao wakachomoka na kuelekea huko.
Kila mmoja alikuwa na uhakika kwamba mtu aliyekuwa ameligusa geti hilo alikuwa Mickey hivyo walikwenda huko ili waweze kumnusuru kutoka katika mikono ya bwana Kenz aliyeonekana kuwa na hasira kali.
“Stop! Don’t move, I wil shoot you down!” (Simama! Usisogee, nitakupiga risasi) alisema bwana Kenz, mbele yake kulikuwa na mtu, alipozidi kusogea zaidi, alikuwa Mickey ambaye alilishika geti kwa lengo la kulifungua, alipoisikia sauti hiyo tu, akaanza kulia na kuanza kuomba msamaha, bwana Kenz hakutaka kujali, ndiyo kwanza akakikoki bunduki yake.

Bwana Kenz alionekana kuwa na hasira mno, kila alipomwangalia Mickey getini pale, alitamani kumpiga risasi mfululizo. Tayari alikuwa ameikoki bunduki yake, kilichofuatia mara baada ya kumnyooshea bunduki kijana huyo ni kuifyatua risasi.
“Aagghh…” kilisikika kilio kutoka kwa Mickey, alikuwa chini huku akiushika mguu wake wa kulia, damu zilimtoka mfululizo, risasi ile ilipenya kwenye mguu wake wa kushoto.
“What have you done?”(Umefanya nini?) aliuliza bi Patricia, alionekana kuchanganyikiwa, akamsogelea mume wake na kumpokonya bunduki ile.
Pamoja na hasira zote alizokuwa nazo, mara baada ya risasi ile kupenya mguuni mwa Mickey, bwana Kenz akaanza kujuta, hasira zikapotea na hofu kuanza kumuingia, hakuamini kama alikibonyeza kitufe cha bunduki ile na risasi kutoka.
Kilio cha sauti kubwa kilisikika kutoka kwa Elizabeth, hakuamini kile alichokuwa akikiona kwamba mpenzi wake, Mickey alipigwa risasi na baba yake.
Akamsogelea Mickey pale alipokuwa, bado alikuwa akilia kwa maumivu makali, akamshika huku akimpoza asilie kwa maumivu lakini bado kijana huyo aliendelea kulia.
Maumivu aliyokuwa akiyasikia mahali hapo yalikuwa makubwa mno, aliusikia mguu ukivuta huku akiwa na wasiwasi kwamba mguu wake ulikuwa umetobolewa na risasi ile.
Pasipo kutarajia, bwana Kenz akaondoka, akalifuata gari lake na kisha kurudi mahali hapo, kilichofuatia, ni kumbeba Mickey na kuanza kumpeleka hospitalini.
“Dad! Why did you shoot him down?” (Baba! Kwa nini umempiga risasi?) aliuliza Elizabeth huku akilia kwa uchungu.
“I’m sorry, forgive me!” (Samahani! Nisamehe) alisema bwana Kenz huku akiendesha gari, kijasho chembamba kilikuwa kikimtoka.
Aliendesha gari huku akiwa amechanganyikiwa, kitendo cha kumpiga risasi Mickey kilimchanganya mno. Kwa wakati huo, moyo wake ukaanza kuwa na majuto kwa kile alichokuwa amekifanya, kila wakati alijikuta akiwa na hamu ya kuomba msamaha kwani uamuzi aliokuwa ameuchukua ulionekana kuwa mzito mno.
Kilio cha mtoto wake, Elizabeth ndicho kilichomtisha zaidi na kuona kwamba Mickey aliumia mno. Alitamani kumwambia anyamaze lakini hakuwa na nguvu za kufanya hivyo, akabaki akiliendesha gari kwa kasi kubwa lengo likiwa ni kumuwahisha Mickey hospitalini.
Hawakuchukua muda mrefu, wakafika katika Hospitali ya Maimonides Medical Centre iliyokuwa katikakati ya Jimbo la New York, jijini Brooklyn. Gari hilo lilipokuwa likiingia ndani ya eneo hilo tu, machela moja ikaletwa mahali hapo huku ikisukumwa na manesi wawili walioonekana kuwa shapu.
Gari liliposimamishwa, mlango ukafunguliwa na Mickey kuteremshwa kisha kupakizwa juu ya machela hiyo na kuanza kusukumwa kuelekea ndani ya jengo la hospitali hiyo.
Elizabeth hakutaka kumuacha mpenzi wake, aliendelea kuwa naye karibu huku akiambatana naye na machozi yakimbubujika mashavuni mwake, bado moyo wake uliendelea kumuuma huku muda wote akimlaumu baba yake kwa kile alichokuwa amekifanya.
“Elizabeth! Your dad has shot me down,” (Elizabeth! Baba yako amenipiga risasi) alisema Mickey huku akilia kwa maumivu makali.
“I’m sorry baby! Please forgive him,” (Samahani mpenzi! Tafadhali msamehe) alisema Elizabeth huku akiendelea kulia.
Machela iliendelea kusukumwa mpaka katika chumba cha upasuaji kilichokuwa na mlango ulioandikwa I.C.U (Intensive Care Unit) na kisha kuingizwa ndani huku Elizabeth akitakiwa kubaki nje ya chumba kile.
Elizabeth hakunyamaza, bado aliendelea kulia kwa uchungu. Lawama zake zote zilikuwa kwa baba yake, kitendo alichokuwa amekifanya kilimuumiza mno. Alibaki kitini huku akilia tu, hata wazazi wake walipokuja na kuanza kumfariji, hakufarijika zaidi ya kuendelea kulia zaidi.
Madaktari walikuwa wakipokezana kuingia ndani ya chumba hicho huku kila mtu akionekana kuwa na haraka, kila walipotaka kumsimamisha daktari mmoja ili kumuuliza juu ya kilichokuwa kikiendelea ndani ya chumba kile, hakukuwa na daktari yeyote aliyesimama.
Bwana Kenz alikuwa na kazi kubwa ya kumuomba msamaha binti yake kwa kile alichokuwa amekifanya, kilimuumiza na kumuwekea majuto makubwa moyoni mwake. Japokuwa aliona kupitia kamera zilizokuwa ndani kwamba binti yake alitaka kufanya mapenzi na Mickey, lakini hiyo haikuwa sababu ya kujitosheleza kumpiga risasi Mickey.
“Mwambie anisamehe! Sikukusudia kufanya vile, ni hasira tu,” alisema bwana Kenz.
“Baba! Lakini kwa nini? Kwa nini umeamua kufanya hivi?” aliuliza Elizabeth huku akilia.
“Ni hasira tu. Nilichanganyikiwa!”
“Sikupendi baba! Ninakuchukia, sikupendi baba!” alisema Elizabeth huku akionekana kuwa na hasira.
“Nisamehe binti yangu!”
“Siwezi kukusamehe! Siwezi kukusamehe baba....!” alisema Elizabeth huku akilia.
Hakutaka kubaki mahali hapo, alichokifanya ni kukimbia na kuelekea nje huku akilia tu. Kila mmoja akayahofia maisha ya Elizabeth, walichokifanya ni kuanza kumfuata huku nao wakikimbia.
Alipofika nje ya hospitali hiyo, akaendelea mbele kuelekea upande mwingine wa barabara. Japokuwa kulikuwa na magari mengi yaliyokuwa yakipita, Elizabeth hakuogopa, alizidi kusonga mbele huku akiendelea kupiga hatua kwenda mbele zaidi.
Bwana Kenz na mkewe, Patricia wakafika mpaka katika barabara ile, wakaanza kuangalia huku na kule, hawakuweza kumuona Elizabeth. Kila mmoja akabaki na mshtuko, hawakuamini kwamba kwa kitendo kile kilichokuwa kimetokea, binti yao angeamua kukimbia na kuelekea pasipojulikana.
“Amekwenda wapi?” aliuliza bwana Kenz.
“Sijui, labda kule, twende tukamwangalie,” alisema bi Patricia, bila kupoteza muda, wakaanza kuelekea huko.
Walijitahidi kumtafuta kadiri walivyoweza lakini hawakuweza kumuona, kila mmoja akaonekana kuchanganyikiwa kwani halikuwa jambo jepesi kwa binti yao kuchukua uamuzi mbaya na wa haraka kama ule.
Walimtafuta zaidi lakini matokeo yakawa vilevile, walipoona kwamba wameshindwa kabisa, wakaamua kurudi nyumbani huku wakiamini kwamba binti yao alikuwa ameelekea huko.
Walipofika, kitu cha kwanza kabisa ni kwenda chumbani kwake, Elizabeth hakuwepo, baada ya hapo wakaanza kumtafuta na sehemu nyingine za nyumba hiyo lakini majibu yalikuwa yaleyale, binti yao hakuwepo.
Walichanganyikiwa, usiku ulikuwa umekwenda sana huku ikiwa imekwishafika saa tatu, lakini hakukuwa na dalili za kuwepo kwa binti yao.
Waliendelea kusibiri huku wakimuomba Mungu amlete binti yao nyumbani hapo. Dakika zikakatika huku masaa yakisonga mbele, mpaka inatimia saa sita usiku, bado Elizabeth hakutokea nyumbani hapo jambo lililowahuzunisha wote wawili.
“Nini kimetokea?” alijiuliza bi Patricia huku akiwa na wasiwasi mwingi.
“Bila shaka atakuwa amekufa,” ilisikika sauti kichwani mwake, hakujua kama ni sauti ya Mungu, yake au ya shetani, ikamtia hofu zaidi.

ITAENDELEA


CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA NANE

Elizabeth alikuwa akilia tu, moyo wake ulikuwa kwenye maumivu makali mno, alimchukia baba yake kisa tu alimpiga risasi mvulana aliyekuwa akimpenda na kumthamini kuliko wote. Kadiri alivyokuwa akitembea ndivyo alivyokuwa akiumia zaidi na machozi kumbubujika.
Kichwa chake kilimfikiria Mickey tu, hakuwa radhi kuona mvulana yule akiendelea kupata mateso na wakati alikuwepo. Hakutaka kurudi nyumbani, kwa kuwa alimwambia baba yake kwamba alikuwa akimchukia, hivyo hata kurudi nyumbani hakutaka.
Kila alipokuwa akipita, macho yake yalikuwa yakiangalia huku na kule, alikuwa na hofu moyoni mwake, mazingira ya usiku yalivyoonekana, yalimuogopesha.
Aliendelea kutembea kusonga mbele, bado moyo wake ulijawa hofu kwa kuwa hakutaka kuonwa na wahuni wowote ambao walikuwa na tabia ya ubakaji. Alipiga hatua mpaka alipoona sehemu ambayo kulikuwa na nyumba moja kubwa ya ghorofa, moja ya nyumba zilizokuwa zikipangishwa na kisha kupanda ngazi mpaka juu na kutulia karibu kabisa na mlango.
Hakutaka kuondoka mahali hapo, alibaki akijiinamia huku akiendelea kulia. Muda huo ndiyo alipoanza kufikiria kila kitu kilichokuwa kimetokea kati yake na Mickey, aliikumbuka siku ya kwanza alipokutana naye nje ya maktaba hapohapo New York, alipoanza kuzoeana naye na mwisho wa siku mvulana yule kuanza kuja kwao.
Kila kitu alichokifikiria wakati huo kikamuumiza, mapenzi aliyokuwa nayo juu ya kijana huyo yalikuwa makubwa mno. Hakuacha kumlalamikia baba yake, kadiri alivyokuwa akimfikiria na ndivyo alivyozidi kumchukia kwa kusababisha kidonda kikubwa moyoni mwake kwa kitendo kile cha kumpiga risasi Mickey.
“Nitamchukia baba, sitokuja kumpenda maishani mwangu,” alijisemea Elizabeth huku akiendelea kulia.
Usiku mzima alishinda mahali hapo, hakutaka kwenda sehemu yoyote ile, hakutaka kurudi nyumbani, alikuwa radhi kukaa sehemu yoyote ile lakini si kurudi katika nyumba aliyokuwa akiishi mbaya wake.
Hakuendelea kubaki macho, japokuwa alikuwa na mawazo mengi lakini kutokana na mchoko aliokuwa nao, akajikuta akichoka na kulala mahali hapo.
Asubuhi ilipofika, aliamshwa na kelele za watu waliokuwa wameamka ndani ya nyumba hiyo. Kutokana na kelele za kujiandaa kwa ajili ya kwenda kazini, akajikuta akiamka na kuanza kuangalia huku na kule.
Hakuonekana kuwa tofauti na watoto wa mitaani, alionekana kufanana nao kwani hata watu wengi waliokuwa wakipita karibu na nyumba hiyo, walipomuona Elizabeth, walimchukulia kama mtoto wa mitaani asiyekuwa na makazi, hivyo angeweza kulala popote pale.
“What the hell are doing here?” (Unafanya nini hapa?) aliuliza mwanaume mmoja, alikuwa ametoka nje tayari kwa kuelekea kazini. Alipoufungua mlango mkuu tu, akakutana na Elizabeth.
“I’m sorry sir,” (Samahani mkuu) alisema Elizabeth, akaanza kuinuka na kuondoka mahali hapo.
Alikuwa na uchovu mwingi mno, njaa ilikuwa ikimuuma na hakujua ni wapi alitakiwa kwenda. Bado moyo wake haukuwa radhi kurudi nyumbani kwani hakutaka kukutana na baba yake ambaye bado alimuona kuwa mwanaume katili hata zaidi ya Adolf Hitler.
Kitu kilichomjia kichwani mwake, tena kwa haraka sana ni kwenda hospitalini kwa ajili ya kumuona mpenzi wake aliyepelekwa usiku uliopita mara baada ya kupigwa risasi na baba yake.
Alipofika hospitalini hapo, akapitiliza mpaka karibu na kile chumba cha wagonjwa mahututi, akakaa kitini na kukiinamisha kichwa chake katikati ya mapaja yake na kuanza kulia tena.
“Wewe binti...” alisikia sauti ikimuita, kwa harakaharaka akauinua uso wake, alikuwa daktari aliyevaa koti kubwa jeupe huku shingoni akiwa na mashine ya kusikilizia mapigo ya moyo.
“Unasubiri nini hapa?” aliuliza dokta huyo.
“Nimekuja kumuona kaka yangu.”
“Nani?”
“Anaitwa Mickey!”
“Alikuwa wapi?”
“Ndani ya chumba hiki toka jana.”
“Hapana! Ndani hakuna mtu, atakuwa ametolewa na kupelekwa chumba kingine kwa ajii ya mapumziko. Humu hakuna mtu,” alisema dokta yule.
“Chumba kipi?”
“Hebu jaribu kule.”
Elizabeth hakutaka kuendelea kusubiri, alichokifanya ni kuinuka na kuanza kuelekea kule alipoelekezwa, sehemu iiyokuwa na vyumba kadhaa vya wagonjwa waliopewa muda wa kupumzika mara baada ya kufanyiwa upasuaji.
Alipoufikia moja ya milango ya vyumba hivyo, akaingia ndani na kuanza kumtafuta mpenzi wake. Hakukuwa na wagonjwa wengi, vitanda havikuwa vingi lakini watu hao wachache waliokuwemo humo, walionekana kuwa na mateso makali.
Wapo waliokuwa wamening’inizwa miguu juu, wapo waliokuwa wakipumulia mashinde za hewa safi na pia kulikuwepo na wengine walioonekana kukata tamaa ya kuendelea kuishi.
Madaktari hawakutulia, waliendelea kuwahudumia wagonjwa kwa kuwapa dawa na hata kuwawekea dripu za maji na damu. Elizabeth alitembea ndani ya chumba kile huku akimwangalia kila mgonjwa, bahati mbaya kwake, hakuweza kumuona Mickey.
Hakutaka kukata tamaa au kurudi alipotoka, alichokifanya akaenda katika vyumba vingine vilivyokuwa na wagonjwa waliopewa mapumziko, baada ya kuzunguka sana, akafanikiwa kumuona mpenzi wake, huku akiwa na moyo wenye furaha, akaanza kumfuata pale kitandani.
“Mickey mpenzi wangu!” aliita Elizabeth kwa sauti ya chini, sauti yenye upendo wa kutosha, Mickey akayafumbua macho yake, alipomuona Elizabeth, uso wake ukajawa na tabasamu pana.
“Mbona unaonekana hivyo?” aliuliza Mickey kwa sauti ya chini.
“Naonekanaje?”
“Umechoka mno, halafu si nadhifu kama unavyokuwa kila siku.”
“Kawaida tu.”
“Hapana, si kawaida yako, hebu niambie,”
“Sikulala nyumbani!”
“Unasemaje?”
“Sikulala nyumbani!”
“Ulilala wapi?”
“Barabarani, nje ya nyumba moja hivi.”
“Elizabeth! Kwa nini?”
“Nisingeweza kurudi nyumbani, ninamchukia baba yangu, sikutegemea kama angekupiga risasi, na sikutegemea kama kuna siku ningemchukia kama ninavyomchukia” alisema Elizabeth.
Mickey akabaki kimya, akamwangalia Elizabeth usoni, maneno yake yalifanana na mtazamo aliokuwa akiutumia kumwangalia. Mapenzi yalionekana machoni mwake, Mickey akaonekana kuogopa, Elizabeth alionekana kumaanisha kile alichokuwa akikisema kwamba alimpenda mno.
Wakabaki wakipiga stori huku msichana huyo akiendelea kusisitiza kwamba alikuwa akimpenda na hakuwa radhi kumuacha maneno ambayo yalimfariji mno Mickey.
Wala hazikupita dakika nyingi, bwana Kenz, mkewe na polisi wawili wakafika mahali hapo. Elizabeth akakunja sura yake, kitendo cha kumuona baba yake kikamfanya kukasirika zaidi kwani tukio lile la kumpiga risasi mpenzi wake lilikuwa likijirudia kichwani mwake.
Akajikuta akianza kurudi nyuma huku akikataa baba yake kumsogelea. Bwana Kenz hakutaka kujali, kwa sababu alijua fika kwamba alifanya kosa kubwa kumpiga risasi Mickey, hapohapo akapiga magoti na kuanza kumsogelea binti yake kwa kutembea na magoti, alikuwa akimuomba msamaha binti yake na mwisho wa siku arudi nyumbani.
“Forgive me my daughter! Please, forgive me and come back home,” (Nisamehe binti yangu! Tafadhali nisamehe na urudi nyumbani,” alisema bwana Kenz, alikuwa tayari kuonekana mjinga lakini si kumuona mtoto wake akiondoka nyumbani na kulala sehemu nyingine bila wao kujua yupo wapi.
“I can’t forgive you, you are a devil....” (Siwezi kukusamehe, wewe ni shetani....) Elizabeth alimwambia baba yake na kuanza kulia tena.
Kila mmoja akashangaa!

Hakukuwa na aliyeamini kama maneno yale aliyosema Elizabeth yalitoka mdomoni mwake, kitendo cha kumuita baba yake kwamba ni shetani kilimshangaza kila mtu. Wote wakabaki mdomo wazi, si wao tu, bali hata Mickey mwenyewe alimshangaa mpenzi wake.
Moyoni aliumia, hakuweza kuzificha hasira zake kwamba alimchukia mno baba yake, alikuwa radhi kuongea kitu chochote kile kwa sababu chuki yake dhidi ya baba yake ilikuwa kubwa.
Alikuwa na miaka kumi na tatu, lakini tayari hakuwa radhi kumuona mtu akimuingilia katika mapenzi ya dhati aliyokuwa nayo kwa Mickey. Mashavuni alikuwa akibubujikwa na machozi, alishikwa na hasira kali na bado alitamani kuongea maneno mengi ya chuki dhidi ya baba yake ili kumuonyeshea kwamba alikuwa amekasirika.
Bwana Kenz hakutaka kujali sana, alimpenda mno binti yake na aligundua kwamba alifanya kosa hivyo aliona kwamba huo ulikuwa muda wake wa kuomba msamaha.
“Naomba unisamehe binti yangu,” alisema bwana Kenz huku akisisitiza kwamba aligundua kuwa alifanya kosa na hivyo alihitaji msamaha kutoka kwa Elizabeth.
Wagonjwa wote waliokuwa ndani ya chumba kile kikubwa, wakabaki wakimshangaa mzee huyo ambaye hakuonyesha hata tone la aibu mahali hapo. Polisi aliokuja nao walionekana kumshangaa, hawakujua ni kitu gani kilichokuwa kimetokea mpaka mzee huyo kumuomba msamaha binti yake.
Bi Patricia akamsogelea binti yake na kumsihi amsamehe baba yake, alipoona kwamba msichana huyo ameweka msimamo kwamba asingeweza kumsamehe baba yake, alichokifanya ni kumsogelea na kisha kumkumbatia.
“Msamehe baba yako! Binti yangu! Msamehe baba yako,” alisema bi Patricia.
Ilikuwa ni ngumu mno kwa Elizabeth kumsamehe baba yake, kila alipokuwa akimwangalia Mickey kitandani pale, moyo wake ulimuuma mno na kuona kwamba baba yake hakutakiwa kusamehewa hata mara moja.
Bi Patricia hakunyamaza, kila wakati alimwambia binti yake kwamba alitakiwa kumsamehe baba yake lakini msimamo wa Elizabeth ulikuwa uleule kwamba hakutaka kumsamehe. Hali ilipoendelea hivyo, ndipo mama huyo akamuomba Mickey kwamba amwambie Elizabeth amsamehe baba yake, hivyo kijana huyo kuanza kumuombea mzee huyo msamaha.
“Msamehe baba yako mpenzi, naomba umsamehe,” alisema Mickey kwa sauti ya chini huku akimwangalia Elizabeth.
“Lakini amekuumiza Mickey!”
“Najua, naomba umsamehe tu.”
“Ila ninamchukia!”
“Hapana! Hautakiwi kumchukia baba yako, naomba umsamehe mpenzi!” alisema Mickey.
Maneno ya mpenzi wake yakamuingia na hatimae mwisho wa siku kujikuta akimsamehe baba yake kwa kitendo kile alichokuwa amekifanya.
Kuanzia siku hiyo, hata baada ya kutoka hospitali, Mickey aliendelea kuwa karibu na binti huyo, walifanya mambo mengi lakini hakukuwa na mtu aliyekuwa tayari kufanya mapenzi mpaka pale watakapofunga ndoa na kuishi pamoja.
Kwa sababu alikuwa kijana wa mitaani asiyekuwa na elimu yoyote ile, mzee Kenz akaamua kumuanzisha shule Mickey na kuanza masomo yake katika moja ya shule bora kabisa nchini Marekani, Lincoln School iliyokuwa pembezoni mwa jiji la Washington.
Ukaribu wa watu hao wawili ukaendelea zaidi, mpaka Mickey anafikisha umri wa miaka ishirini huku Elizabeth akifikisha miaka kumi na nane, tayari walifanya mambo mengi kama wapenzi likiwepo suala la kufanya mapenzi kwani kusubiri mpaka ndoa, waliona ni kipindi kirefu mno.
****
Kati ya wanafunzi waliokuwa na akili nyingi katika Shule ya Brighton High School, Mickey alikuwa mmoja wao. Alikuwa kijana mkimya ambaye kila wakati alikuwa akifikiria mambo yake, hakujihusisha kabisa na mambo ya kusoma, kumuona akiwa amekaa sehemu na kujisomea, hilo lilikuwa jambo gumu.
Darasani alikuwa tofauti, kila alipokuwa akifanya mtihani, aliwaongoza wanafunzi wengine jambo lililomtengenezea heshima kubwa na wengi kumuogopa. Hakuwa akisomea masomo ya sanaa au sayansi, masomo yake yalikuwa ni ya biashara ambapo kila wakati alikuwa akisoma vitabu mbalimbali vilivyowahusu watu walioanzia maisha ya kimasikini na baadae kutajirika kupitia biashara mbalimbali.
“Jamaa ana akili sana, toka alipokuwa Lincoln alikuwa hivihivi, jamaa ni hatari,” alisema jamaa mmoja aliyekuwa akisoma katika shule hiyo.
Huo ulikuwa ni mwanzo tu na bado Mickey aliendelea kuonyesha maajabu makubwa. Akawa gumzo shuleni hapo, wanafunzi wengi wakaanza kumsumbua kwa kumtaka wafundishwe mengi kuhusu biashara.
Mickey hakuwa mchoyo, japokuwa hakuwahi kuwa mfanyabiashara lakini alifanikiwa kuwafundisha watu wengi kuhusu biashara walizokuwa wakizifanya kwa kuwapa mikakati mingi ya kufanikiwa katika biashara zao.
Mickey akawa genius, hakuwa mfanyabiashara lakini uwezo wake wa kuwafundisha watu kupata fedha ukawa mkubwa. Alikuwa na miaka ishirini lakini uwezo wa kufafanua mambo kuhusu biashara ulimfanya kuonekana kama alikuwa na miaka hamsini.
Alianzia shuleni hapo lakini kadiri siku zilivyozidi kwenda mbele, akajikuta akialikwa sehemu mbalimbali kwa ajili ya kutoa semina kuhusu biashara. Watu wengi waliokuwa wakishiriki katika semina zake walikuwa vijana wadogo lakini mara baada ya watu wengi kusikia uwezo wake, watu wazima, tena waliokuwa wafanyabiashara wakubwa nao wakaanza kukusanyika kwa ajili ya kumsikiliza Mickey.
“Kuna watu wanakuhitaji,” alisema mwanafunzi mmoja, zilikuwa siku chache kabla ya kumaliza elimu ya sekondari na kuingia chuoni.
“Wakina nani?”
“Sijajua, wamekuja na kukuuliza hivyo nimeambiwa nije nikuite.”
“Sawa.”
Alichokifanya Mickey ni kuelekea huko ofisini ili kukutana na watu waliokuwa wamemuulizia, alipofika katika ofisi ya mkuu wa shule, macho yake yakatua kwa watu wawili waliokuwa wamevaa suti nyeusi ambapo baada ya kumuona, wakainuka na kumsalimia.
Watu hao walikuwa wageni kwake, kila alipokuwa akivuta kumbukumbu ilikuwa kukumbuka ni mahali gani aliwahi kuwaona watu hao, hakukumbuka kitu chochote kile, akabaki akiwaangalia tu.
“Tunamuhitaji mara moja,” alisema mwanaume mmoja, alikuwa akimwambia mkuu wa shule.
Hakukataa, aliwakubalia kirahisi kitu kilichomshangaza hata Mickey mwenyewe. Aliondoka na watu wale hadi ndani ya gari lao kubwa na kuanza kuongea naye. Walionekana kuwa watu wenye uwezo mkubwa wa kuongea, katika kila neno walilokuwa wakiongea huku wakiuliza maswali, Mickey aligundua kwamba watu waliokuwa mbele yao hawakuwa watu wa kawaida hata kidogo.
“Wewe ni genius,” alisema jamaa mmoja.
“Hapana! Watu wanasema hivyo, ila sidhani kama ni kweli,” alisema Mickey.
“Unafahamu nini juu ya Iraq?”
“Iraq! Ni nchi ya Kiarabu iliyo chini ya mtawala Saddam Hussein, kuna jingine?” aliuliza Mickey.
“Unawafahamu wanajeshi waliokwenda huko kupigana?”
“Siwafahamu, ila ninajua kuna wanajeshi wamekwenda huko.”
“Unauonaje uwepo wao ndani ya nchi ile, ni sehemu sahihi kuwepo kule kwa kipindi hiki?” aliuliza mwanaume mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Paul.
“Labda naweza kuonekana tofauti, uwepo wao ndani ya nchi ile, si sahihi kabisa. Siwaangalii wanajeshi wale, najaribu kuziangalia familia zao. Kama hakuna umuhimu wa kuwepo kule, kwa nini wawepo? Kuna mengi ya kuzungumza lakini kama nitakutana na rais wetu, George Bush, nitazungumza naye mengi,” alisema Mickey, katika kipindi hicho, nchi hiyo ilikuwa ikiongozwa na aliyekuwa baba wa rais wa baadae wa Marekani, George Bush aliyeitwa George Herbert Bush.
Walizungumza na Mickey kwa kipindi cha dakika ishirini, waliporidhika, wakaagana naye huku wakiahidi kumtafuta baada ya siku chache. Mickey akabaki na mawazo, suala la kuambiwa na watu wale kwamba wangeweza kumuona baada ya siku chache lilimchanganya mno, hakufahamu watu wale walikuwa wakina nani na walihitaji nini kutoka kwake.
“Mpenzi!” alimuita Elizabeth simuni.
“Nipo mpenzi!”
“Kuna watu walinifuata shuleni leo!”
“Wakina nani?”
“Siwafahamu!”
“Walihitaji nini?”
“Kiukweli sifahamu. Wamekuja na kuniulizauliza maswali ya kawaida kisha wakaondoka,” alisema Mickey.
“Maswali gani?”
“Ya kawaida tu, lakini yaliyohitaji umakini kwenye kujibu.”
“Kwa hiyo huwafahamu?”
“Hata kidogo, simfahamu yeyote yule.”
“Unadhani watakuwa watu salama?”
“Kimuonekano, ni watu salama, lakini sijajua roho zao kwani naamini wakati mwingine naye shetani hujifanya malaika wa nuru,” alisema Mickey na wote kuanza kucheka.
“Ila kuwa nao makini, hautakiwi kumuamini mtu yeyote yule,” alisema Elizabeth.
“Usijali mpenzi.”
Wala hazikupita siku nyingi, wale watu wakarudi tena shuleni pale na kumuhitaji Mickey kwa mara nyingine. Kwa kuwa hakuwa na wasiwasi nao tena, hata alipoambiwa kwamba aongozane nao kwenda ndani ya gari lao, alikubaliana nao.
Walipofika huko, kama kawaida yao wakaanza kumhoji maswali kadhaa. Kila mmoja akaonekana kufurahia kwani kwa kiasi fulani tayari walikuwa wamejenga urafiki na kuwa karibu zaidi.
Hakunywa wala kunywa kitu chochote kile garini, hakuchomwa sindano yoyote lakini ghafla, huku akiwa ndani ya gari lile, akahisi macho yake yakiwa mazito, nguvu zikaanza kumuisha huku akijiona kubadilika na kuanza kuhisi usingizi mzito.
Hakujua ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea, wanaume wale wawili waliendelea kuzungumza naye kwa furaha, hakukuonekana hata mtu mmoja aliyeonekana kuwa na wasiwasi wowote ule.
Ghafla, kizunguzungu kikaanza kumpata na hatimae akaanza kuona giza ambalo lilizidi kuongezeka kadiri sekunde zilivyozidi kwenda mbele, baada ya dakika mbili, akashindwa kuwa kama alivyokuwa, ghafla, akafumba macho, mwili wake ukalegea na hakujua ni kitu gani kikiendelea mahali hapo.

Alipata fahamu na kujikuta akiwa ndani ya chumba kimoja kikubwa. Kitu cha kwanza kabisa akaanza kujiuliza juu ya mahali alipokuwa, kilikuwa chumba kigeni kabisa ambacho hakuwa akijua kilikuwa katika nyumba ipi.
Kichwa chake kilijaa maswali juu ya mara ya mwisho kabla ya kupatwa na tatizo lile. Alikumbuka vyema kwamba mara ya mwisho alikuwa ndani ya gari na watu wawili ambao aliwafahamu kama marafiki zake wa muda mfupi ambao walikuwa na maswali ya utata sana, baada ya hapo, aliona kizunguzungu na mwisho wa siku kutokujua kile kilichokuwa kimeendelea.
Akainuka kitandani pale, alikuwa huru kabisa, akaanza kuzunguka huku na kule huku lengo lake likiwa ni kukizoea chumba kile. Alizunguka kwa sekunde kadhaa kisha akarudi kitandani na kutulia.
Mawazo hayakumuisha, kila wakati alikuwa akifikiria mambo mengi yaliyopelekea kuwa mahali hapo lakini hakupata jibu. Maswali mengi yakamiminika lakini kila alilokuwa akijiuliza, alikosa kujua sababu iliyomfanya kuwa mahali hapo.
Baada ya dakika kadhaa, mlango ukafunguliwa na msichana mmoja kuingia ndani. Alikuwa msichana mrembo aliyevalia sketi fupi iliyoishia magotini, blauzi nyepesi aliyokuwa ameivaa iliyafanya matiti yake kuonekana kitu kilichoonekana kuwaweka katika wakati mgumu wanaume rijali.
“Hapa ni wapi?” lilikuwa swali la kwanza alilouliza Mickey.
“Kunywa maji kwanza,” alisema msichana yule.
“Hapana! Niambie hapa ni wapi,” alisema Mickey.
“Nitakwambia, kwanza kunywa maji uwe sawa.”
Mickey hakutaka kunywa maji yale, kitu alichokuwa akitaka kufahamu kwa wakati huo ni kujua alikuwa wapi. Bado kumbukumbu zake zilimwambia kwamba mara ya mwisho alikuwa ndani ya gari,
Msichana yule hakutaka kukaa ndani ya chumba kile kwa muda mrefu, alichokifanya ni kugeuka nyuma, akaufungua mlango na kuondoka zake.
Wala haukupita muda mrefu, mlango ukafunguliwa na wanaume wawili kuingia ndani, alipowaangalia, walikuwa wanaume walewale aliokuwa nao ndani ya gari lile. Hasira zikamkaba kooni, akaanza kuwaangalia kwa macho ya hasira huku akianza kukunja ngumi.
“Usihofu Mickey! Sisi si watu wabaya, kama tungekuwa wabaya, tungekuua na kukuweka katika chumba kibaya na si kizuri kama hiki,” alisema Paul huku akimwangalia Mickey.
“Na kama mngekuwa watu wazuri, msingenilevya kwa madawa yenu,” alisema Mickey.
“Hatukukulevya Mickey.”
“Kumbe mlifanyaje?”
“Hata sisi hatujui, kwani ulikunywa kitu chochote?”
“Hapana.”
“Ulikula kitu chochote?”
“Hapana.”
“Ulichomwa na kitu chochote?”
“Hapana.”
“Sasa kwa nini unasema tulikulevya?”
Mickey akabaki kimya, maswali yaliyoulizwa yalikuwa ya msingi sana, hakuwa na la kujibu zaidi ya kuwaangalia tu. Alikuwa na uhakika kwamba alilevya lakini kila alipotaka kufahamu alilevywa vipi, alikosa jibu.
“Nyie ni wakina nani na mnataka nini?” aliuliza Mickey.
“Hilo ndilo swali la msingi ulilokuwa umeliacha, tunahitaji ufanye kitu kimoja,” alisema Paul.
“Kitu gani?”
“Kafungue kabati, utakuta suti, chukua, kaoge kisha zivae, ukimaliza, njoo katika chumba kilichoandikwa unit hapo nje,” alisema Paul.
“Mmmh! Sawa!”
“Tunatumaini hautochukua zaidi ya dakika kumi.”
“Sawa.”
Paul na mwenzake, Nick wakatoka ndani ya chumba kile na kuelekea katika chumba kingine, alichokifanya Mickey ni kuelekea bafuni, akaoga harakaharaka kisha kurudi chumbani na kuvalia, kisha kuelekea katika chumba hicho.
Chumba kilikuwa kikubwa, kulikuwa na watu zaidi ya kumi waliokuwa wamekaa mbele ya meza kubwa. Juu ya meza ile, kulikuwa na maneno yaliyoandikwa kwa ukubwa ambayo yalisomeka vizuri mno, yaliandikwa C.I.A.
Mickey akashtuka, hakuamini kile alichokuwa akikiona mbele yake, kuwa mbele ya watu waliotambulika kiserikali kwamba ni majasusi kilimshtua mno.
Alijua ugumu uliokuwepo mpaka mtu kuwa katika kitengo hicho cha kijasusi, kulikuwa na Wamarekani wengi waliotamani hata siku moja kuitwa lakini hawakuweza kupata bahati hiyo, kwake, hiyo ilikuwa ni sawa na kuokota dodo chini ya mlimao.
“Karibu,” alikaribishwa katika kikao hicho cha muda na hivyo kupewa maelekezo juu ya kile alichotakiwa kukifanya.
****
C.I.A (Central Intelligence Agency) lilikuwa shirika kubwa la kijasusi nchini Marekani. Mbali na mashirika mengi yaliyopo katika nchi nyingine, shirika hili ndilo lililoendesha mikakati mingi ya kuweza kuzipeleleza nchi nyingi za kiarabu na mwisho wa siku kuzishambulia.
Idadi kubwa ya Wamarekani walikuwa wakitamani kuingia katika shirika hilo lakini nafasi yake kupatikana ilikuwa ngumu kwa sababu watu wengi waliokuwa wakichukuliwa ni wale wenye uwezo mkubwa kufikiria na pia wale waliokuwa wakiishi katika umati mkubwa wa watu huku wakiwa viongozi kama walimu, waandishi na watu wengine.
Watu hao wenye akili kubwa ya kufikiria ndiyo walioleta changamoto ndani ya shirika hilo, wao ndiyo waliopendekezwa namna ya kuwashambulia vizuri Waarabu hasa kwa kulilipua jengo lao kubwa lenye ghorofa hamsini lililokuwa na ofisi nyingi na mwisho wa siku kusema kwamba Waarabu ndiyo walikuwa wamehusika na hivyo kuanza kuwashambulia.
Bado Saddam Hussein alivisumbua vichwa vyao. Kila siku walitamani mtu huyo afe na ndiyo maana walifanya kila liwezekanalo kumuangamiza lakini bado walionekana kuwa na mtihani mkubwa mbele yao kwani haikuwa rahisi nchi ya Kiarabu kama Iraq, Mmarekani kuingia na kufanya kile walichokuwa wakikitaka kifanyike.
Bado hawakujua wafanye nini, walijaribu kila njia ili wafanikiwe lakini kila kilichokuwa kikifanyika, kitu cha ajabu Saddam alijua kila kitu kilichokuwa kikiendelea.
Siku zikakatika, waliendelea kuziwekea vikwazo nchi za Kiarabu kutumia mabomu ya nyuklia, mioyo yao ilikuwa na hofu kwa kuhofia kwamba ingetokea siku mabomu hayo yangeweza kutumika kuwaangamiza.
Hapo ndipo walipoamua kuwatumia watu wao kwa ajili ya kwenda katika nchi zote za Kiarabu kwa ajili ya kufanya kile walichotaka kukifanya, kujua sehemu zote zilizokuwa zikitumika kutengeneza mabomu ya nyuklia na kupeleleza zaidi nchi hizo ili wajue kila kitu kilichokuwa kikiendelea na hata siku watakayoamua kuzivamia nchi hizo, wajue ni wapi pa kuanzia.
“Tumtumie nani sasa?” lilikuwa swali moja muhimu.
Hawakuwa na jibu lolote lile, kila uamuzi walioufanya haukuonekana kuwa sahihi, mwisho wa siku, wakaamua kuwatumia watu wengine kabisa, vijana wenye ari mpya kwa ajili ya kufanya mchakato mzima hasa mara baada ya kuwapa mafunzo ya kutosha.
Katika pitapita zao, ndipo waliposikia uwezo mkubwa aliokuwa nayo Mickey. Japokuwa alikuwa kijana mdogo, lakini alikuwa na akili nyingi, uwezo wa kuwashawishi watu wengine wafanye kile alichotaka kukifanya.
Hawakutaka kulaza damu, walichokifanya, tena kwa haraka zaidi ni kumchukua kijana huyo kwa lengo la kuwafanikishia kile walichotaka kukifanya kwani uwezo wake haukuwa wa kawaida na alikuwa na sifa zote ambazo watu waliotakiwa kuwa ndani ya shirika hilo walitakiwa kuwa nao.
Wakawatuma vijana wawili, wakafika shuleni huko na moja kwa moja kufanya mipango ya kumchukua kijana huyo. Siku ambayo walipanga kumchukua, wakanywa vidonge viitwavyo anti psyprominium, vilikuwa vidonge maalumu vya kuzuia sumu ya psyprominium isiweze kumuathiri mtu ambaye angeivuta hewa iliyokuwa na sumu hiyo ambayo waliamua kuipulizia ndani ya gari na kisha kumuita Mickey.
Mickey alivyoingia garini, alipovuta hewa hiyo iliyokuwa na mchanganyiko wa sumu hiyo, ghafla hali ikaanza kubadilika na mwisho wa siku kuhisi kizunguzungu na baada ya muda kuona giza pasipo kujua ni kitu gani kiliendelea baada ya hapo.
Wakafanikiwa kumpata kijana huyo kwa ajili ya kuwafanyia kazi maalumu ya kwenda katika nchi za Kiarabu.

ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA TISA

Mickey hakuweza kukataa, kwa sababu naye alikuwa akitamani kufanya kazi katika shirika hilo, akakubaliana nao kwamba ilikuwa ni lazima afanye nao kazi na kuyafanya yale yote waliyotaka ayafanye sehemu yoyote ile.
Siku iliyofuata, akachukuliwa kwa gari na kupelekwa katika Jiji la Texas, huko ndipo kulipokuwa na kambi maalum ya kufanyia mazoezi ya kijeshi na mambo mengi ya kijasusi.
Sehemu hiyo haikuonekana kuwa na jengo hata moja, walipofika, kulikuwa na uzio mkubwa, walipoingia ndani ya uzio huo, Mickey alibaki akishangaa tu kwani hakuamini kama hiyo ndiyo sehemu aliyotakiwa kufanya mazoezi ya kijeshi.
Kwa sababu sehemu kubwa ya jiji hilo ilikuwa ni jangwa huku ikiwa karibu sana na mpaka wa Ciudad Juarez, mpaka wa kuingilia nchini Mexico kutokea nchini Marekani, hata sehemu hiyo ilionekana kuwa kama jangwa na ilionekana kutelekezwa.
“Hapa ni wapi? Ndipo tutakapofanya hayo mazoezi?” aliuliza Mickey huku akionekana kushangaa.
“Ndiyo! Subiri!” alisema Paul.
Mickey hakujua ni kitu gani kilitokea, ghafla, sehemu ya ardhi ikaanza kupanda juu na ngazi za kushuka chini kuanza kuonekana, wakazifuata na kuanza kupiga hatua kuingia ndani ardhini, sehemu hiyo ilionekana kuwa kama handaki fulani.
Kwa Mickey, hiyo ilionekana kuwa ajabu, walikuwa wamefika chini lakini muonekano wake haukuweza kukufanya kugundua kwamba huko kulikuwa ni chini ya ardhi. Kulikuwa na vitu vyote vilivyokuwa vikipatikana juu, kulikuwa na hewa ya kutosha kwani viyoyozi vilivyokuwa vimefungwa viliwasaidia kuwaletea hewa safi kule walipokuwa.
Mbali na hayo, kulikuwa na magari ya kijeshi, magari ya kawaida, barabara, majengo, kompyuta na kila kitu ambacho kilitakiwa kitumike katika mafunzo. Ukiachana na hayo, kulikuwa na sehemu iliyokuwa na msitu wa kutengeneza ambapo kuliwekwa wanyama wadogowadogo wasiong’ata.
Mickey alipigwa na mshangao, kila kitu alichokuwa akikiona kilimshangaza. Idadi ya watu ilikuwa kubwa, wapo wengine waliokuwa wakifanya mazoezi magumu na hata yale mepesimepesi ya kuwaweka sawa.
Wakaanza kupiga hatua kuelekea katika jengo moja lililokuwa na mlango mkubwa ulioandikwa C.I.A, ulikuwa mlango mkubwa wa chuma huku madirisha yake yakiwa na vioo visivyoruhusu risasi kupenya.
Walipoufikia, Paul akabonyeza kitufe na kuingia ndani. Kama zilivyokuwa ofisi nyingine, napo ndani ya jengo hilo kulikuwa na meza, viti, makabati na vitu vingine vingi.
Kuanzia siku hiyo, Mickey alitakiwa kuishi huko, alikabidhiwa chumba alichokuwa akikitumia na jamaa ambaye alikuja kuwa rafiki yake mkubwa, huyu aliitwa Denis.
Kila siku asubuhi walikuwa wakiamka na kuanza mazoezi yakiwepo ya mapigano, kutengeneza bunduki, huku wakati mwingine wakiingia darasani kujifunza lugha mbalimbali hasa Kiarabu.
“Tutaishi huku kwa muda gani?” aliuliza Mickey.
“Sijajua, mimi nililetwa toka wiki iliyopita,” alijibu Denis.
“Kulikuwa na kitu gani kilichowavutia mpaka kukuchukua?”
“Sijajua, ila waliponiita kwa mara ya kwanza, waliniambia kwamba mimi ni genius wa kompyuta,” alijibu Denis.
“Kwa hiyo unaijua vizuri kompyuta?”
“Ndiyo! Ninaijua sana tu, tangu nilipokuwa mdogo,” alijibu Denis.
Wawili hao wakatokea kuwa marafiki wakubwa, kila siku walikuwa wakitoka pamoja na kuingia pamoja, walipokwenda darasani, walikuwa karibu na hata walipofanya mazoezi mengine, bado ukaribu wao ulikuwa mkubwa.
Hawakuwa wakiruhusiwa kuwasiliana na watu waliokuwa nje ya jengo hilo, waliporwa simu zao, kila kitu kilichokuwa kikiendelea huko, kilitakiwa kuwa siri na hakukutakiwa mtu yeyote aliyekuwa nje kufahamu kile kilichokuwa kikiendelea.
Mickey hakuacha kumkumbuka Elizabeth, alikuwa msichana pekee aliyekuwa akimpenda, alimthamini na kumuhitaji maishani mwake. Kila alipokuwa akipata muda wa kukaa peke yake, mawazo juu ya msichana huyo yalimtesa sana.
Hakuonekana kuwa na raha, kuna wakati alijihisi kuwa na huzuni ambapo kila aliyekuwa akimwangalia, aliligundua hilo lakini hakukuwa na mtu aliyejali. Kila siku, kazi yake kubwa ilikuwa ni kutafuta njia ya kuwasiliana na Elizabeth, kwanza apate simu na kuongea na msichana huyo, ajue anaendeleaje na pia kumpa taarifa juu ya mahali alipokuwa.
“Ninahitaji simu,” alisema Mickey.
“Ya nini?” aliuliza Dennis.
“Nataka kuwasiliana na Elizabeth.”
“Mmmh! Kuhusu simu, itakuwa ngumu kuipata.”
“Lakini si tunaweza kuungana mpaka tukaipata?”
“Haiwezekani, toka jengo hili limejengwa, hakuna aliyewahi kutumia simu, kwanza hazitoki.”
“Kwa nini?”
“Wamezifunga.”
“Hata kama, hivi haujamkumbuka Victoria?”
“Nimemkumbuka sana, sasa unafikiri nitafanya nini.”
“Hapana, kama wanaamini kuwa waliotuchukua ni magenius, inabidi tulidhihirishe hilo, tuwaonyeshee ugenius wetu, pale pasipotumika simu, patumike,” alisema Mickey.
“Mmmh!”
“Usishangae, kwanza wewe si mtaalamu wa kompyuta?”
“Ndiyo!”
“Basi haina noma, kama vipi tutumie uwezo wetu mpaka tuwasiliane na watu wetu,” alisema Mickey.
“Tutajaribu.”
Huo ulikuwa ni mwezi wa sita tangu waingie ndani ya jengo hilo. Hawakuwasiliana na watu wa ulimwengu wa juu, walitakiwa kubaki wao kama wao. Kila siku waliendelea kufanya ratiba zao za kila siku zikiwepo za kuingia msituni, mazoezi ya kijeshi na hata utengenezaji wa bunduki.
Wawili hao hawakutulia, kila siku walikuwa wakifanya hili na lile kuhakikisha kwamba simu inapatikana na hatimae waweze kuwasiliana na wapenzi wao. Halikuwa jambo jepesi hata kidogo, sehemu nyingi zilikuwa na kamera ndogo za CCTV zilizowafanya kuhofia kwamba walikuwa wakionekana kila sehemu.
Kamera zile ziliwapa hofu, hawakutaka kufanya kitu chochote kibaya kwa kuwa tu waligundua kwamba kila walichokuwa wakikifanya walionekana. Kamera zile zilifungwa kila sehemu, kuanzia vyumba vya mazoezi, msituni, vyooni na hata bafuni, kila sehemu, kamera zile zilifungwa.
Baada ya kukaa kwa miezi saba, watu wote wakaitwa kwa ajili ya kugaiwa majukumu waliyotakiwa kuyafanya. Kitu cha kwanza, wote walitakiwa kuoga na kuvaa suti zao tayari kwa kuanza kazi watakayopewa, wakagaiwa bunduki ndogo na kutakiwa kwenda katika chumba maalumu kwa ajili ya kupewa maelekezo juu ya kile walichotakiwa kukifanya.
“Nimesikia tetesi,” alisema Denis.
“Tetesi gani?”
“Tunakwenda kuua.”
“Kuua?”
“Ndiyo! Huwa ni kazi ya kwanza watu wanayopewa watu wakiingia humu.”
“Una uhakika?”
“Ndiyo maana nimesema tetesi.”
“Mmmh! Sawa, ngoja tusubiri!”
Wakaingia ndani ya chumba hicho, wakapewa risasi ambazo wakaziingiza ndani ya bunduki zao na kuzikoki, walipomaliza, wakapewa vyombo maalumu vya kuzuia milio ya risasi mara inapopigwa, baada ya hapo, wakatakiwa kujiandaa vilivyo kwa kuwa kuna kazi maalumu ilikuwa ikienda kufanyika.
“Kazi gani?” aliuliza Mickey.
“Mmekaa kwa kipindi kirefu na huu ndiyo mwanzo wa kazi yetu. Leo, mtasafiri watu wawiliwawili kwenda sehemu tofautitofauti, huko, kuna kazi mnakwenda kuifanya, mkifanikiwa, mtapongezwa,” alisema Paul, mwanaume aliyeonekana kuwa kiongozi wao. Mbele yake kulikuwa na watu kumi na saba.
“Kazi gani?”
“Kuua.”
“Kuua?” aliuliza Mickey kwa mshtuko.
“Ndiyo. Kuna watu wanatakiwa kufa, kuanzia wao na familia zao. Kumbuka kile tulichowaambia, hakuna huruma katika kazi hii. Ukiambiwa ua, wewe ua, ukiambiwa fanya hivi, fanya,” alisema Paul.
Kila mmoja akashikwa na hofu. Kwao, kuua halikuonekana kuwa jambo jepesi kwao!
****
Walitakiwa kusafirishwa kutoka hapo walipokuwa na kwenda sehemu mbalimbali kwa ajili ya kufanya mauaji. Kulikuwa na watu wengi ambao walikuwa maadui zao, watu waliokuwa wakisafirisha madawa ya kulevya kutoka Mexico na kuyaingiza ndani ya nchi hiyo, hao wote, walikuwa maadui zao ambao hawakutakiwa kuishi, walitaka kuwamaliza nao na kizazi chao chote.
Waliambiwa kwamba wangepelekwa sehemu mbalimbali hapo nchini Marekani, wakaanza kugaiwa majukumu, kwa kila mtu aliyekuwa akiambiwa kwenda kwa mtu fulani kumfanyia mauaji yeye na familia yake, walipewa maelekezo yote, nyumba ilipokuwa, haukupewa njia ya kuingia ndani, wao ndiyo wangeweza kufanya kila liwezekanalo mpaka kuingia ndani ya kufanya mauaji.
Mickey na Denis wakapewa kazi ya kukamilisha mauaji ya mzee tajiri, aliyejilimbikizia mali kutokana na biashara yake kubwa ya madawa ya kulevya aliyokuwa akiifanya kipindi hicho. Mzee huyo aliitwa Sanchez na alitokea nchini Mexico.
Walipopewa maelekezo yote, wakatakiwa kuondoka kuelekea Washington kwa ajili ya kuanza kazi waliyokuwa wamepewa. Kwao, ilionekana kuwa kazi ngumu lakini hawakuwa na jinsi, ilikuwa ni lazima ifanyike ili waweze kujitengenezea sifa kubwa. Kwa sababu kazi ilionekana kuwa ngumu, walipewa wiki nzima ili kukamilisha kabla ya kuanza kazi nyingine, yaani kulikuwa na msururu wa kazi za mauaji, hivyo ndivyo C.I.A walivyofanya.
Walipewa kila kitu kilichotakiwa kupewa, walipokuwa navyo, wakaanza safari ya kuelekea huko. Kutoka Texas mpaka Washington, kwa kutumia ndege, walitumia masaa saba, wakaingia ndani ya Jiji hilo kubwa na kuchukua vyumba katika hoteli kubwa ya Caspians Hill iliyokuwa pembezoni mwa jiji hilo.
“Ni lazima tufahamu mengi kabla ya kwenda huko, kuna chochote walichotuambia ambacho kinaweza kutusaidia?” aliuliza Mickey.
“Hapana! Hakuna chochote zaidi ya kutueleza mahali nyumba ilipo.”
“Kwa hiyo tuanze vipi?”
“Ni lazima tuanze kufuatilia kwa karibu kile kinachoendelea ndani ya nyumba ile,”
Walichokifanya, siku iliyofuata ni kwenda katika mtaa uliokuwepo nyumba hiyo, ulikuwa moja ya mitaa iliyokaliwa na watu wenye fedha zao. Hakukuwa na kelele nyingi, mtaa ulikuwa umepoa sana na hata idadi ya watu waliokuwa wakionekana mitaani, wengi walikuwa Wazungu.
Walifuatilia siku ya kwanza kwa kuanza kuyazoea mazingira, kwa sababu nyumba hiyo ilizungushiwa ukuta mkubwa, hawakuweza kuona ndani. Hiyo ndiyo ilikuwa ratiba yao kila siku, mara kwa mara walifika mahali hapo na kuangalia kipi kilichokuwa kikiendelea, walipoona kwamba kulikuwa na chochote walichotakiwa kufanya, walifanya huku wakijiamini kwamba kila kitu kingekwenda kama kinavyotakiwa.
Ndani ya siku tatu nzima, kila ilipofika saa mbili asubuhi, gari la McDonald lilikuwa likifika nyumbani hapo na kuleta kuleta pizza kwa ajili ya familia nzima na ice cream kwa ajili ya mtoto aliyekuwa ndani ya nyumba hiyo.
Hilo likaonekana kuwa jambo la msingi sana, kitendo cha gari hilo kufika hapo kila asubuhi wakaona kwamba lingekuwa jambo zuri kuitumia nafasi hiyo kwa ajili ya kutekeleza kile walichokuwa wameambiwa wakitekeleze.
Walichokifanya, wakalipiga picha gari lile kisha kuondoka mpaka katika jengo lililokuwa likitumika kama Tawi la Shirika la C.I.A ambapo huko wakaomba kupewa gari kama lile pia liwekwe stika zinazofanana na gari lile la kubebea pizza na ice cream kutoka McDonald.
Kwa kuwa hakukuwa na kitu kilichokuwa kikiwasumbua, mchakato huo ukakamilika ndani ya siku mbili tu, wakapewa gari hilo. Kwa kuliangalia, usingeweza kugundua kama lilikuwa tofauti na magari yale ya McDonald na hata walipohitaji kutengenezewa vitambulisho, wakatengenezewa vyao kwa kuwa ndani ya shirika hilo, kulikuwa na kopi za vitambulisho vya makampuni yote nchini Marekani.
“So, my name is Edward Konn?” (Kwa hiyo naitwa Edward Konn?) aliuliza Mickey.
“Yes! Denis, you will be Andrew Adrian,” (Ndiyo! Na Denis utakuwa Andrew Adrian) alisema mkuu wa shirika hilo hapo Washington.
Huo haukuwa mwisho, walitaka kupata ratiba kamili ya gari hilo, lilikuwa likiondoka makao makuu muda gani, walitumia dakika ngapi mpaka kufika katika jengo lile. Walichokifanya, siku iliyofuata, asubuhi sana walikuwa nje ya jengo la makao makuu ya McDonald ambapo hapo wakatulia kwa nje huku wakiwa ndani ya gari lao la kawaida, walipoliona gari lile likianza kutoka, wakaanza kulifuatilia.
Walitembea kwa mwendo wa taratibu, kila gari lile liliposimama na kuwauzia watoto pizza na ice cream, nao walisimama na walipokuwa wakiendelea na safari, nao waliendelea.
Zoezi hilo ndilo walilokuwa wakiendelea nalo siku hiyo. Walitaka kukamilisha mchakato waliopewa kwa haraka sana na kisha kupeleka ripoti iliyokamilika kwamba kila kitu kilifanyika pasipo tatizo lolote lile.
Mpaka gari lile linafika nje ya jengo la nyumba ile, ilikuwa imetimia saa 2:20 asubuhi, hapo wakauandika muda ule.
Kesho ilipofika, kama kawaida wakaanza kufanya kilekile walichokuwa wamekifanya siku iliyopita, walitaka kufahamu ni muda gani ungetumiwa pia. Walianza kulifuatilia gari lile, baadae, likafika katika nyumba ile ikiwa ni saa 2: 27.
Hapo wakajua kwamba muda rasmi wa kufika ndani ya nyumba ile ilikuwa saa mbili asubuhi hivyo hata watakapoanza kazi yao, ilikuwa ni lazima ndani ya muda huo wawe katika nyumba ile.
“Leo si ndiyo tunafanya kazi?”
“Ndiyo!”
“Tuandae kila kitu, tusisahau sare zao.”
Walikuwa wamejiandaa kwa kila kitu. Walikuwa na sare zile alizovaa dereva na muuzaji wake, walipoona kwamba kila kitu kipo tayari, wakaanza kuelekea huko huku wakiwa wamewasiliana na majasusi wengine wa C.I.A ambao walijifanya kuwa maaskari wa barabari (trafki) kwa ajili ya kulizuia gari lile la kusambaza pizza na ice cream.
Njiani ilikuwa kero, kila walipopita, watoto walikuwa wakishangilia huku wakijaribu kuwasimamisha lakini hawakutaka kusimama, safari yao ilikuwa moja tu, kwenda ndani ya nyumba ile na kufanya mauaji.
Huku wakiwa njiani, wakapewa taarifa kwamba lile gari la McDonald lililokuwa na jukumu la kusambaza vyakula hivyo lilikuwa limesimamishwa njiani na askari wa barabarani ili wao waweze kufanya vitu vyao kisha wawaruhusu.
Hiyo ilikuwa nafuu kwao, hawakuchukua muda mrefu, wakafika nje ya jengo hilo, tayari saa zao zilisoma kwamba ilikuwa imetimia saa 2:00 asubuhi. Walipopiga honi, geti likafunguliwa na kuingia ndani.
Zaidi ya watu kumi waliokuwa na bunduki mikononi mwao walionekana ndani ya jumba lile la kifahari. Ulinzi ulikuwa umeimarishwa kila sehemu, kamera ndogo za CCTV zilikuwa zimepachikwa katika kila kona.
Walipolisimamisha gari lile katika eneo husika, walinzi wawili wakawafikia na kuwataka kuteremka, wote wakateremka huku wakiwa na maboksi ya pizza na ice cream.
“Nyie ni wakina nani?” aliuliza jamaa mmoja, watu waliofika siku hiyo walikuwa tofauti na wale waliowazoea.
“Wafanyakazi wa McDonald.”
“Mbona mmekuja wengine?”
“Wale wengine wamebadilishwa maeneo ya kazi mkuu,” alijibu Mickey huku Denis akijifanya kuwa bize kutoa maboksi ya pizza na ice cream kutoka garini.
“Na mbona mmewahi sana?”
“Hakukuwa na wateja wengi njiani. Tuiweke wapi hii mizigo?” aliuliza Mickey.
“Subirini kwanza, msiwe na haraka,” alisema mlinzi yule.
Mickey akashikwa na wasiwasi, tayari kichwa chake kilikwishamwambia kwamba walikuwa wamegunduliwa. Mlinzi yule aliwaangalia vizuri, hakuridhika, alichokifanya ni kuwaita wenzake ambao wakafika hapo huku wakiwa na bunduki.
Walipofika, akawaambia kwamba waletaji wa vyakula hivyo walibadilishwa pasipo kupewa taarifa. Walichokisema wale wengine ni kuhitaji viatambulisho, wakapewa na kuanza kuviangalia.
Havikuwa tofauti, vilifanana na vitambulisho halali vya wafanyakazi kutoka McDonald, waliporidhika wakawarudishia na kuwaamuru waweke mikono juu na kutaka kuwapekua.
“Mnasemaje?” aliuliza Mickey.
“Weka mikono juu,” alisema mlinzi yule.
Hawakutaka kuwaruhusu kuingia ndani ya mjengo ule, walionekana kuwa na wasiwasi nao. Kitu walichotaka kukifanya ni kuwapekua watu hao kuona kama walikuwa na bunduki au la.
Hofu waliyokuwa nayo walikuwa sahihi kabisa, hao hawakuwa wauzaji wa pizza na ice cream, walikuwa ni majasusi waliokuja mahali hapo kwa kukamilisha ‘mission’ waliyokuwa wamepewa. Kama walivyosema kwamba walihisi kwamba watu hao walikuwa na bunduki, kweli, waliingia mahali hapo na bunduki.
Hivyo wakawaamuru kunyoosha mikono juu kwa ajili ya kuwapekua, walinzi wote walikuwa wamekwishakoki bunduki zao. Si hao wa karibu tu, bali hata wale waliosimama mbali, nao waliwanyooshea bunduki, hali ikaonekana kuchafuka mahali hapo.

Huo haukuwa utaratibu wao, hakukuwa na sheria zilizokuwa zikiruhusu wauzaji wa bidhaa kama vyakula kupekuliwa eti kisa walihisiwa kuwa na kitu fulani. Walizijua sheria za Marekani lakini hawakutaka kubisha, walichokifanya ni kukubaliana nao.
Wakaweka mikono juu na kuanza kupekuliwa, kila walipopekuliwa, kwenye kila maeneo lakini hawakuweza kupatikana na silaha yoyote ile. Walinzi wale hawakuridhika, wakachukua yale maboksi ya pizza na ice cream na kuanza kuangalia ndani, walikuta patupu.
“Angalieni garini,” alisema jamaa mmoja na wenzake kufanya hivyo lakini matokeo yalikuwa ni yaleyale kwamba hakukuwa na silaha yoyote iliyopatikana.
Waliridhika kwamba watu hao hawakuwa na silaha yoyote ile hivyo wakawaruhusu kuingia ndani ya nyumba hiyo. Mickey na Denis wakachukua maboksi yao na kuelekea ndani, walipofika, wakakaribishwa sebuleni na baada ya dakika kadhaa, mzee Sanchez na familia yake wakafika mahali hapo, hiyo ndiyo ilikuwa kawaida yao, kila siku wauzaji wa pizza walipokuwa wakifika, ilikuwa ni lazima wote waende sebuleni, wachukue mizgo yao na kuiweka jikoni.
“Nyie ni wakina nani?” aliuliza bwana Sanchez, alionekana kuwashangaa.
“Wauzaji kutoka McDobald.”
“Wale wengine wapo wapi?”
“Wamekwenda seheumu nyingine, tumebadilishana majukumu kwa wiki hii,” alisema Mickey.
“Sawa. Hebu nizione pizza za leo,” alisema mzee Sanchez.
Mtoto wake na mke wake walikuwepo mahali hapo pamoja. Ingawa alikuwa mwanaume katili, asiyekuwa na huruma hasa anaposhika bunduki lakini kwa familia yake, mzee huyo alikuwa mpole na aliwapenda wote.
Huyo ndiye mtu waliyekuwa wakimtaka, alikuwa ni ‘mission’ ya kwanza waliyopewa kuifanya na kisha kusubiria ni kipi kilitakiwa kufanywa baada ya hicho. Wakampa boksi moja la pizza na kuanza kuliangalia, aliporidhika, akahitaji mke wake na mtoto wake wazichukue na kuzipeleka jikoni. Wakazipeleka.
Ilikuwa ni nafasi waliyokuwa wakiitaka, kwa sababu mchakato wa kuendelea kupeleka pizza jikoni ilikuwa ukiendelea, wakachukua boksi moja lililokuwa na bunduki zao na kisha kuzitoa na kumnyooshea mzee huyo.
Hiyo ndiyo mbinu waliyokuwa wameitumia, walizificha bunduki zao katika maboksi ya pizza, tena katikati ya pizza kubwa kiasi kwamba hata wale walinzi walipokuwa wakiwapekua, hawakuweza kuziona kwani zilijificha mno.
Hakukuwa na cha kupoteza mahali hapo, kwa sababu mzee huyo na familia yake ndiyo waliokuwa wahusika na ndiyo ‘mission’ yenyewe, kwa kutumia bunduki zao zilizokuwa na viwambo vya kuzuia mlio wa risasi, wakamfyatulia, damu zikatapakaa na mzee huyo kudondoka chini pasipo kuzungumza chochote.
Mke na mtoto wake walipokuja sebuleni, wakapigwa na mshtuko, kitendo cha kumuona mzee Sanchez akiwa chini huku damu zikimtoka, ziliwatia hofu, wakajikuta wakipiga kelele ambazo hazikuweza kufika nje kutokana na sehemu kubwa ya nyumba hiyo kujengwa kwa vioo.
Denis hakutaka kuchelewa, alichokifanya, akamnyooshea bunduki yake mke wa mzee huyo, hakutaka kusikia kitu chochote, kitu pekee kilichokuwa kikimwambia kichwani ni kwamba ilikuwa ni lazima wakamilishe mission ile waliyokuwa wamepewa, hapohapo akaanza kummiminia risasi mfululizo mwanamke yule.
“Kill his daughter,” (Muue binti yake) alisema Denis.
“What?” (Nini?)
“Kill his daughter! We have to leave,” (Muue binti yake, tunatakiwa kuondoka) alisema Denis, alikuwa akimwambia Mickey aliyeonekana kutetemeka.
Alikosa nguvu, kila alipokuwa akimwangalia binti yule mwenye umri wa miaka mitano, alimuonea huruma, hakuwa na nguvu za kumfyatulia risasi kama alivyoelekeza. Alijua kwamba kumuua kila mtu ndani ya nyumba hiyo ndiyo ilikuwa mission yao lakini akajikuta akikosa nguvu za kufanya hivyo, akabaki akimwangalia tu yule mtoto.
“Kill her,” (Muue,) alisema Denis lakini bado Mickey alikuwa akisitasita.
Ulisikika mlio wa risasi uliosikika kwa sauti ya chini mno, kwanza Mickey alidhani kwamba bunduki yake ndiyo iliyofyatua risasi hiyo, alipoangalia vizuri, hakuwa ameboyeza kitufe cha bunduki ile.
Alipoangalia mbele, binti yule mdogo alikuwa chini huku damu zikimtoka kifuani, alipoyageuza macho yake kumwangalia Denis, bado alikuwa ameinyoosha bunduki ile kwa mtoto yule, akamsogelea na kumpiga risasi nyingine mbili, Mickey akatetemeka mno, kijasho chembamba kikaanza kumtoka.
We’ve to complete the mission, don’t be scared, if we ain’t complete it, we gonna die my friend,” (Tunatakiwa kukamilisha misheni, usiogope, kama tusipokamilisha, tutakufa) alisema Denis kwa Kingereza cha mitaani.
Hawakutaka kuendelea kubaki mahali hapo, kwa kuwa walikwishakamilisha kile walichotaka kukifanya, wakaziweka bunduki zao viunoni na kutoka nje.
Hakukuwa na mlinzi yeyote alijua kile kilichokuwa kimeendelea ndani ya nyumba ile, wakaagana na wauzaji hao na kuondoka,
Hiyo ndiyo ilikuwa kazi ya kwanza kabisa Mickey kupewa, yalikuwa ni mauaji ya kwanza kuyafanya toka apewe mafunzo makali ya kijeshi kule alipopelekwa huku kukiwa na mafunzo mengine ya kuficha bunduki, kuunganisha vipande vya bunduki na kuwa bunduki kamili pamoja na kufundishwa lugha mbalimbali kwani kutokana na kazi yake kubwa, pia alitakiwa kwenda nchi mbalimbali kwa ajili ya kukamilisha mauaji aliyokuwa akipewa.
Mwaka huo ulipokatika na mwaka mwingine kuingia, Mickey alikuwa hashikiki, hakuwa yule Mickey wa kipindi cha nyuma, huyu, alikuwa tofauti kabisa. Alionekana mwanaume jasiri, mwenye sura ya upole lakini moyo wake ulikuwa na mambo makubwa kupita kawaida.
Hakuwa na huruma, kila kazi aliyokuwa amepewa aliifanikisha na kuonekana mfanyakazi bora asiyekuwa na huruma hata kidogo. Huyo ndiye mtu ambaye C.I.A walikuwa wakimhitaji, walijua kwamba walikuwa kwenye vita vikali na Waarabu hivyo walitaka kuwa na mtu atakayeifanya kazi kwa ufasaha kabisa.
Walichokifanya C.I.A ni kumfundisha Mickey kuhusu ujasiriamali, walitaka kumpa mafunzo ya kutosha na kisha kumpa kazi kubwa ya kuelekea nchi za Kiarabu kwa ajili ya kufanya mauaji tu, hasa kwa maadui zao.
Masomo yalikuwa ni ya kawaida, na wakati yupo katika Chuo cha San Diego State kilichokuwa katika Jiji la California alikuwa akitenga muda maalumu wa kuonana na msichana wake wa siku nyingi, Elizabeth.
Bado alikuwa na mapenzi makubwa, alimpenda msichana huyo kupita mtu yeyote katika dunia hii. Alijua fika kwamba alipendwa na msichana huyo, si kwamba kwa kipindi hicho alikuwa na fedha, alipendwa toka katika siku ambazo hakuwa na kitu.
Alijiahidi kumpenda msichana huyo lakini suala la kuwa jasusi wa C.I.A lilikuwa siri kubwa, hakutakiwa kumwambia mtu kwani hiyo ndiyo ilikuwa sheria moja muhimu ndani ya shirika hilo, kuwa ndani ya kitengo hicho, hasa kile kilichokuwa kikihusika na mission nyingi za mauaji, hakutakiwa mtu yeyote kufahamu.
“Siku mtu yeyote akijua kwamba wewe ni jasusi wa C.I.A, adhabu yetu ni kukuua tu,” aliyakumbuka maneno aliyoambiwa na kiongozi wao katika makao makuu ya C.I.A
Kwa wengine, kujulikana lilikuwa jambo la kawaida lakini kuna wale waliokuwa wakihusika katika mauaji, au wale waliokuwa wakihakikisha rais anapata ulinzi wa kutosha popote aendapo, hivyo hutangulia kabla ya mwezi mmoja na kukamilisha ulinzi wao.
“Unataka kuwa mjasiriamali?” aliuliza Elizabeth, walikuwa kitandani huku wakiwa watupu.
“Yaaap! Nina hamu ya kuwahamasisha wengine wafanye biashara na kuwa matajiri wakubwa,” alisema Mickey.
“Safi sana. Hivi ni nini siri ya mafanikio yako? Nashangaa nilipotezana nawe kwa mwaka mzima, baadae, ukaibuka na kuwa tofauti sana mpenzi, ulikuwa wapi?”
“Nilikuwa natafuta. Unakumbuka siku zile nilizokuwa sina kitu? Nilipokuwa nadharaulika kwa kuwa sikuwa na fedha?” aliuliza Mickey.
“Nakumbuka.”
“Sikutaka kuishi katika hali ile, nilitamani nibadilike na kuwabadilisha watu wengi, hatimae nikafanikiwa,” alisema Mickey.
Elizabeth hakuwahi kuhisi kama mpenzi wake alikuwa jasusi wa C.I.A, mtu aliyetakiwa kuogopwa kutokana na umafia waliokuwa wakiufanya hasa katika kuhakikisha kwamba wanaua pale wanapoambiwa waue.
Aliendelea kusoma ndani ya chuo hicho kwa miaka mitatu, katika kipindi chote hicho, alikuwa akiwafundisha wanachuo wengine namna ya kuwa wafanyabiashara wakubwa na hatimae baadae kufanikiwa.
Hapo ndipo alipoanza kupata jina, watu wakaanza kumfahamu kama mhamasishaji wa ujasiriamali ambapo kama ukijaribu kukaa chini na kusikiliza kile alichokuwa akikiongea, basi ulikuwa ukiuona utajiri ukiwa mlangoni.
Sifa za mafundisho yake zikaanza kutapakaa hapo California, watu wakubwa, wenye fedha zao walikuwa wakimtafuta Mickey kwa ajili ya kushauriwa jinsi ya kuziendesha biashara zao na kufanikiwa zaidi.
Hicho ndicho ambacho C.I.A walichokuwa wakikitaka. Kupitia serikali, nao wakaanza kumtangaza Mickey kwamba alikuwa mhamasishaji mkubwa aliye na uwezo mkubwa wa kuwafanya wale masikini kupata fedha na kuwa wafanyabiashara wakubwa.
Mafundisho yake hayakuishia California tu, watu mbalimbali wakaanza kumuita kutoka katika majiji mengine nchini Marekani, kila alipokwenda, alipoondoka, aliacha sifa kubwa ya kumfanya kutafutwa na watu wengine.
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa kila kitu, hakukuwa na mtu aliyejuta kuwa naye, alipendwa na kuonekana kuwa mtu sahihi ambaye hakutakiwa kuachwa hivihivi, watu wakaomba ulinzi zaidi kwake kwa kuhofia kwamba watu wabaya wasiokuwa na mapenzi makubwa kwa Wamarekani wangeweza kumuua mtu huyo.
Magazetini, jina lake likaandikwa sana, kwenye majarida makubwa kama Forbes, Fantastic na majarida mengine, picha yake ilikuwa ikitokea katika ukurasa wa mbele kabisa, alikuwa amevaa suti yake na miwani machoni.
“Huyu jamaa ni balaa, natamani atoe vitabu,” alisema jamaa mmoja, alikuwa akinunua Jarida la Forbes baada ya kuiona picha ya Mickey mbele kabisa.
“Halafu nasikia alikuwa masikini tu,” alisema jamaa mwingine.
“Nani kasema?”
“Alihojiwa kwenye Kituo cha Televisheni cha Smash, yaani alivyokuwa akihadithia, unatamani kulia,” alisema jamaa huyo.
“Acha utani bwana, haiwezekani kuwa hivyo.”
“Kweli tena. Yaani mpaka sikuamini kabisa.”
“Mmmh! Basi kweli nimeamini hapa duniani hakuna masikini, ukiitumia vizuri akili yako, utatajirika tu,” alisema jamaa mwingine.
Mickey akawa gumzo, kwa sababu C.I.A kwa kupitia serikali walivyozidi kumtangaza na ndivyo jina lake lilikuwa likitangazwa sana. Kila alipokuwa akiandaa semina, watu walikusanyika kwa wingi na kutaka kusikiliza kile alichokuwa akikizungumza.
Mwaka mmoja baadae, akaamua kutoa kitabu chake cha kwanza alichokipa jina la Think Like A Businessman (Fikiri Kama Mfanyabishara). Kilikuwa kitabu chenye msisimko mkubwa, watu wengi wakakinunua, kilikuwa moja ya vitabu vilivyovunja rekodi ya mauzo duniani.
Ndani ya wiki ya kwanza, tayari kopi milioni themanini zilikuwa zimekwishauzwa. Kila mtu alikitaka kitabu hicho kilichokuwa kikitangazwa kila siku. Jina lake likawa kubwa, watu wakamuheshimu Mickey na kumuona kuwa mtu muhimu katika ulimwengu wa sasa uliojaza masikini wengi kuliko matajiri.
Bado C.I.A waliendelea kumtangaza Mickey, alikuwa mtu pekee waliyemtegemea kwa kufanya mission zao zote katika nchi za Waarabu. Walijua fika kwamba watu hao walikuwa hatari sana, walikuwa wakitengeneza mabomu ya nyuklia, japokuwa waliwashutumu sana lakini hakukuwa na mtu aliyelikubali hilo.
Baada ya miaka miwili ya kumtangaza na kujulikana zaidi dunia nzima, wao wenyewe, C.I.A wakaanza kumtafutia semina za kwenda kufanya katika nchi za Kiarabu na nchi ya kwanza kuifikiria ilikuwa Iran.
Japokuwa mara ya kwanza kulitokea malumbano nchini humo kwamba haikuwezekana Mmarekani kuja nchini mwao na kufanya semina jinsi ya kutengeneza fedha, lakini mwisho wa malumbano hayo, Mickey alitakiwa kwenda huko kwa ajili ya kufanya semina ya siku tatu.
Si Waarabu wote waliungana bali kulikuwa na wengine waliotumika kama vibaraka vya Wamarekani ambao waliwarahisishia mambo yao kufanyika kwa wepesi zaidi.
“Utaondoka lini?” aliuliza Elizabeth.
“Keshokutwa!”
“Nitakukumbuka mpenzi, na vipi kuhusu lile suala?”
“Lipi? Kuoana?”
“Jamani, kwani umesahau?”
“Tutaoana tu, nikirudi, nitafanikisha hilo, cha msingi fanya mipango yote, kuwapa watu taarifa na mambo mengine,” alisema Mickey.
“Sawa. Nitafanya hivyo.”
Wakakumbatiana usiku mzima, bado mapenzi yao yaliendelea kukua. Japokuwa kulikuwa na wanawake wengi waliomfuata Mickey na kumwambia kwamba walikuwa wakimpenda na hivyo kutaka kuwa naye, lakini kijana huyo hakutaka kukubaliana nao kabisa.
Alikuwa na miaka ishirini na nne lakini akili yake, maarifa yake yaliuzidi umri wake. Alikuwa amekwishaandaliwa tayari kwa kuanza mission nyingine uarabuni.
Mwezi mmoja kabla, tayari mazingira yalikuwa yamekwishaandaliwa, ulinzi wa kutosha ulikuwa umekwishawekwa hivyo kwa Mickey, siku hizo mbili zilizobaki hazikuonekana kuwa tatizo kwani kila kitu kilikuwa tayari.
Siku ya safari ilipofika, akaondoka na kwenda uwanja wa ndege. Hakutaka mpenzi wake afahamu kama alikuwa jasusi kutoka C.I.A, kila kitu alichokuwa akikifanya, alikifanya kwa umakini pasipo kugundulika.
Uwanjani, alisindikizwa na mpenzi wake, Elizabeth na watu wengine ambao aliwatambulisha kama marafiki zake aliosoma nao na wakati ukweli ni kwamba walikuwa majasusi wenzake waliokuwa wakihakikisha kila kitu kinakaa sawa.
Kwa wakati huo, majasusi wote wa C.I.A walimtegemea Mickey, hata rais wa nchi hiyo, Bush alikuwa akifahamu kila kilichokuwa kikiendelea. Alimheshimu Mickey kwa kuwa alijua kwamba huyo ndiye ambaye angewaziba mdomo Waarabu pasipo kufahamu chochote kile.
“Nakupenda mpenzi!” alisema Elizabeth huku akiwa amemkumbatia Mickey.
“Nakupenda pia.”
Wakakumbatiana na kuagana. Alipoingia ndani ya ndege, kila mtu alitaka kupiga naye picha. Mickey alikuwa mtu maarufu, kitendo cha kupanda ndege na abiria wa kawaida kilimshangaza kila mtu.
Aliyekuwa na simu, kamera, alitaka kupiga naye picha kwani kumuona Mickey katika sehemu za mkusanyiko wa watu kama hiyo ilikuwa vigumu kutokea.
“Ninaitwa Stacie,” alijitambulisha msichana aliyekuwa amekaa naye.
“Nashukuru kukufahamu. Unakwenda wapi?” aliuliza Mickey.
“Uholanzi!”
“Kuna nini?”
“Nakwenda kusoma.”
“Unasomea nini?”
“Uandishi wa Habari.”
“Mmmh! Safi sana. Nakuombea Mungu uwe kama Larry King!”
“Nashukuru. Natumaini nitafanikiwa.”
Huo ndiyo ukawa mwanzo wa kufahamiana na msichana huyo mrembo, walikuwa wakiongea mengi, walizoeana kwa kipindi kifupo mno, hakukuwa na mtu aliyetaka kulala, kila mmoja alitaka kuuonyesha umahiri wake katika kuzungumza.
Ndege ilikata mawingu kama kawaida. Ilichukua masaa tisa kuivuka Bahari ya Atlantiki, ikaanza kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Hearthrow jijini London nchini Uingereza.
Wote wakateremka, baada ya saa moja, wakaendelea na safari kuelekea nchini Uholanzi ambapo huko, kwa Mickey alitakiwa kubadilisha ndege na kuelekea katika nchi iliyokuwa kwenye Umoja wa Emirates, Qatar, ambapo hapo angechukua ndege nyingine itakayompeleka mpaka Iran, nchi jirani ya adui wao, Saddam Hussein.
“Huu ndiyo mwisho wa safari yangu! Mungu akipenda tutaonana,” alisema msichana huyo huku akimwangalia Mickey usoni, tayari ndege ilikuwa ikitua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Amsterdam nchini Uholanzi.
“Mmmh!”
“Kuna nini tena?”
“Hapana. Hakuna kitu.”
“Mbona umeguna?”
“Nahisi huu si mwisho wa kuonana nawe!”
“Sidhani. Unaweza usinione tena!”
“Una uhakika?”
“Ndiyo! Nitakuwa bize masomoni, halafu nikimaliza, sitorudi nchini Marekani, nitakwenda kuanza maisha ya uandishi Ukraine,” alisema Stacie.
“Sawa, ila utaliweza baridi la huko? Si unajua yote Urusi hiyo,” alisema Mickey huku akionekana kutokuwa sawa.
“Nitaliweza tu, hakuna tatizo.”
Stacie aliigundua hali hiyo lakini hakutaka kuuliza sana, alichokifanya mara baada ya ndege kusimama, akateremka na kuanza kutembea kwa mwendo wa harakaharaka kuelekea katika jengo la uwanja huo. Alionekana kama mtu aliyejishtukia.

ITAENDELEA

CHANZO :BURE SERIES
 
SEHEMU YA KUMI ...... MWISHO

Mickey akapigwa na mshangao, kila alivyokuwa akimwangalia Stacie alishindwa kuelewa sababu iliyomfanya msichana huyo kuwa hivyo. Wakati mwingine akahisi vibaya kwamba msichana huyo alikuwa gaidi na hivyo alitaka kuulipua uwanja huo lakini wakati mwingine, alilitupilia mbali wazo lake na kuendelea na mambo yake.
Kwa kuwa alikuwa maarufu duniani kote, hata hapo nchini Uholanzi ilikuwa kero kwake, kila aliyemuona, alimfuata na kutaka kupiga naye picha huku wengine wakitaka kupewa ushauri juu ya biashara walizokuwa nazo, kwa kifupi, Mickey alichukia kuwa maarufu.
“Can you help me?” (Unaweza kunisaidia?) ilisikika sauti ya msichana mmoja, kimuonekano, alionekana kuwa miongoni mwa watu waliokuwa na mafanikio, wale waliopitia njia mbalimbali na ngumu mpaka kufanikiwa.
“What can I help you?” (Naweza kukusaidia nini?)
“My name is Candy, I’m enterprenuer, I have been passing through many problems in my business,” (Ninaitwa Candy, mimi ni mjasiriamali, ninimepitia matatizo mengi katika biashara zangu) alisema msichana yule.
Akabaki akizungumza na yule mwanamke. Alimueleza ukweli kwamba alikuwa na biashara nyingi na kubwa lakini kwa kipindi kirefu amekuwa akipata hasara kwani hakujua ni kwa namna gani angeweza kuzizuia fedha zake kutumika kwa kiwango kikubwa kama ilivyokuwa.
Kwa kuwa alikuwa mtu aliye na kiu ya kuwasaidia watu ili wanufaike na kile kiasi walichokuwa wakikipata, Mickey akaanza kumshauri mwanamke yule mpaka alipohakikisha kwamba alielewa kila kitu.
Hawakukaa sana hapo Uholanzi, baadae wakatakiwa kupanda ndege ya Shirika la Ndege la Qatar Airways kwa ajili ya kuendelea na safari yao mpaka Qatar. Kutoka hapo mpaka Qatar, walichukua masaa kumi, ndege ikaanza kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Hamad uliopo nchini humo katika Jiji la Doha na kisha kuchukuliwa na kupelekwa katika hoteli moja ya nyota tano.
Mickey alibaki akiyaangalia mandhari ya jiji hilo. Idadi ya watu haikuwa kubwa lakini ulikuwa moja ya mji uliokuwa safi huku kukiwa na majengo makubwa yalioufanya kupendaza na kuvutia mno.
Walipofika katika Hoteli ya Sultan Adesh, akateremka na kupelekwa katika chumba alichotakiwa kukaa. Mickey hakutulia, kila muda alikuwa kazini, kitu cha kwanza kabisa kukifanya kilikuwa ni kuchukua kompyuta yake ya mapajani na kuiunganisha na internet na kuanza kuangalia vitu alivyotaka kuviangalia muda huo.
Hakuchukua muda mrefu kuangalia vitu hivyo, akapitiwa na usingizi kwani tayari muda ulisomeka kwamba ni saa saba usiku.
****
Waarabu walitumia wiki nzima kumtangaza Mickey kwamba angeweza kufika nchini Qatar kwa ajili ya kutoa semina kubwa iliyohusu ujasiriamali. Walimjua, waliufahamu uwezo wake kwani hata kile kitabu alichokuwa amekitoa, walikinunua na kilionekana kuyabadilisha maisha yao kibiashara.
Kitendo cha kusema kwamba mtu huyo angeweza kufika Qatar, kiliwafanya matajiri wengi kutamani kuhudhuria huku kiingilio kikiwa kikubwa, zaidi ya riyal milioni moja ambayo ilikuwa ni sawa na milioni tano za Kitanzania.
Tiketi za kutosha zaidi ya elfu mbili zikaandaliwa na ndani ya siku mbili, tiketi zote zikawa zimekwisha huku watu wengine wakilalamikia kukosa, Hakukuwa na cha kufanya, kwa sababu mtu huyo angeweza kwenda mpaka Dubai, wale waliokosa tiketi basi wangekuwa na fursa ya kwenda huko kwa ajili ya kumsikiliza mhamasishaji huyo.
“What if Qaar Shalbaab come?” (Itakuwaje Qaar Shabaab wakija?) aliuliza jamaa mmoja.
“Impossible, we have enough security in here,” (Haiwezekani, tuna ulinzi wa kutosha mahali hapa) alisema jamaa mwingine.
Qaar Shalbaab lilikuwa moja ya makundi ya kigaidi yaliyokuwa yakiogopwa sana duniani. Kundi hili lililokuwa nchini Afghanistan, lilikuwa miongoni mwa yale makundi yaliyokuwa yakishambulia sehemu mbalimbali katika nchi za kiarabu kwa kutumia mabomu na hata kujitoa mhanga kwa kujilipua na mabomu waliyokuwa wakiyavaa miilini mwao.
Hawakuwa watu wazuri, kundi hili la kigaidi lililojificha katika Milima ya Tora Bola nchini humo lilikuwa likiongozwa na mtu aliyesadikiwa kuwa na roho mbaya kuliko watu wote duniani, huyu aliitwa Tawfaq Majid.
Wanawake wengi wa Kiarabu walikuwa wakivamiwa katika makazi yao na kubakwa huku wengine wakiteswa kwa kufanyiwa mambo ya kikatili. Wasichana wadogo wakaogopa kwenda shuleni kwani shule nyingi zilikuwa zikivamiwa na watoto wa kike kupigwa huku sheria kuu ya kundi hilo ikisema kwamba mtoto wa kike hakutakiwa kupata elimu.
Japokuwa sheria za nchi za Kiarabu kuwa ngumu, lakini kundi hilo lilizifanya sheria hizo kuwa ngumu zaidi. Kila siku msimamo wao ulikuwa mmoja kwamba nchi za Kiarabu zilitakiwa kukaliwa na Waarabu tu na hakutakiwa kuingia Mzungu yeyote ndani ya nchi hizo.
Mauaji hayakukoma katika nchi nyingi za Kiarabu, Wazungu wengi walikuwa wakiuawa kwa kuchinjwa hadharani jambo lililowafanya Wamarekani kuwa na chuki kubwa na kiongozi wa kundi hilo, Tawfaq Majid.
Huyo ndiye mtu aliyekuwa akitafutwa kipindi hicho, kichwa chake kilikuwa na thamani ya zaidi ya dola milioni mbili, zaidi ya shilingi bilioni nne za Kitanzania. Hakukuwa na mtu aliyekuwa akifahamu kama mtu huyo alikuwa akipatikana katika milima hiyo.
Mashirika mbalimbali ya kijasusi duniani likiwepo shirika la kijasusi lenye uwezo mkubwa dunia, ISI (Inter Services Intelligence) kutoka nchini Pakistan, yalifanya kila liwezekanalo kumpata kiongozi huyo au hata watu waliotoka katika kundi hilo lakini hawakufanikiwa.
Kila siku watu walizidi kuuawa, idadi ya watu waliokuwa wakijitoa mhanga ilizidi kuongezeka jambo lililozua hofu kubwa duniani. Hakukuonekana kuwa watu waliokuwa na nguvu za kuwatafuta watu hao ambao walizidi kuwa hatari kadiri siku zilivyozidi kwenda mbele.
Mataifa yote ya Kiarabu yalilichukia kundi hili lililoshikilia msimamo wake kwamba watoto wa kike hawakutakiwa kwenda shule na wala nchi za Kiarabu hazikuwa kambi za Wazungu.
“Nina wasiwasi nao,” alisikika jamaa mmoja.
“Kwa nini?”
“Wanaweza kuja kuanzisha vurugu, inabidi kuwe na ulinzi mkali hapa,” alisema jamaa huyo.
Hicho ndicho kilichofanyika, kwa sababu ndani ya ukumbi huo kulitarajiwa kuwa na watu wenye fedha zao, tena wengine wakiwa viongozi wa nchi, ulinzi mkubwa ukaimarishwa, hakukuwa na mtu yeyote aliyeruhusiwa kuingia na aina yoyote ile ya chuma huku wanawake waliokuwa wakivaa majuba wakichunguzwa kwa umakini kwa kuvuliwa nguo hizo katika vyumba maalum ili kuwaepuka wale waliojivisha mabomu kwa ajili ya kujilipua.
Siku ambayo semina hiyo ilitakiwa kuanza, ndiyo ambapo kundi hilo lililokuwa chini ya Tawfaq lilihisiwa kufanya shambulio ndani ya ukumbi huo huku lengo lao likiwa ni kumuua Mickey aliyekuja kwa ajili ya kazi ya upelelezi huku akitumia kivuli cha ujasiriamali.
Saa 4:05 asubuhi siku ya semina hiyo, tayari Mickey alikuwa amesimama mbele ya ukumbi huo, watu wengi walikuwa mbele yake kwa ajili ya kumsikiliza. Hakuonekana kuwa na wasiwasi, alizungumza huku akionekana kujiamini kwa kila neno alilokuwa akilitamka.
Watu walikuwa makini kumsikiliza, kila neno alilokuwa akilizungumza, lilionekana kuwa ‘nondo’ vichwani mwa watu, wengi wakajikuta wakitingisha vichwa vyao kutoka juu kwenda chini.
Ilipofika saa sita mchana, watu wakapata muda wa mapumziko, hapo, walikunywa na kula, kila kona, walikuwa wakimzungumzia Mickey, alionekana kuwa na uwezo mkubwa wa kuyafafanua yale aliyokuwa akiyazungumza, baada ya nusu saa, semina ikaendelea kama kawaida.
“Mbona nasikia kelele, kuna nini?” aliuliza jamaa mmoja, alikuwa karibu na mlango wa kuingilia ukumbini humo.
“Kuna mwanamke anataka kuingia, hebu njoo kwanza,” alisema jamaa mwingine, alitoka huko mlangoni na kuja kuwaita wenzake.
Malumbano yalikuwa yakiendelea baina ya walinzi hapo mlangoni na mwanamke aliyefika mahali hapo huku akiwa amevaa juba jeusi jeusi na hijabu kichwani. Alitaka kuingia kinguvu, japokuwa walinzi walikuwa wakimzuia, lakini alikuwa akilazimisha jambo lililozua hofu kubwa kwa kila mtu aliyekuwa hapo mlangoni.
“Twende kule...” alisema mlinzi mmoja.
“Wapi?” aliuliza mwanamke yule.
“Kwenye chumba maalum.”
“Kufanya nini?”
“Kukupekua, hivyo ndivyo tunavyofanya kwa kila mwanamke anayetaka kuingia ndani.”
“Haiwezekani.”
“Haiwezekani nini?”
“Kwenda huko.”
“Basi napo hautakiwi kuingia humu,” alisema mlinzi.
“Hapana! Nitaingia tu.”
Bado mwanamke yule alikuwa aking’ang’ania kuingia ndani ya ukumbi ule pasipo kukaguliwa. Hawakujua sababu iliyomfanya kukataa lakini kosa kubwa walilolifanya, mashine ya kuchunguzia kama mtu alikuwa na kitu cha chuma au silaha yoyote ilikuwa ndani ya jengo lile, umbali kadhaa kutoka katika chumba kile kikubwa kilichokuwa kikifanyikia semina ile.
Walinzi walijitahidi kumzuia mwanamke yule lakini naye alikuwa mbishi, hakutaka kukubaliana nao, aliendelea kubishana nao, lakini huku kila mmoja akiwa hajui ni kitu gani kilichotokea, ghafla, mwanamke yule akaanguka chini, kichwa chake kilikuwa kimefumiliwa kwa risasi, damu zilizokuwa zikimtoka kichwani, zikaanza kutapakaa katika sakafu, kila mmoja akaogopa, walipoangalia huku na kule, hakukuwa na mtu aliyeshika bunduki, kila mmoja akachanganyikiwa!
Hawakujua ni nani aliyekuwa amempiga risasi, wao walishtukia akiwa chini huku damu zikiendelea kumtoka, tukio hilo, liliwashangaza mno!
****
Wamarekani waliamua kutilia umakini katika kumlinda mtu wao, alikuwa mtu maalum ambaye walihakikisha kwamba angekamilisha kazi zote walizokuwa wamemuagiza katika nchi za Uarabuni.
Kila alipokuwepo, tayari ulinzi mkubwa ulikuwa umekwishawekwa hivyo alitakiwa kufanya kila kitu kwa kujiaminisha lakini mwisho wa siku walitaka kupata kile walichokuwa wakikitata.
Kitendo cha kuwa ndani ya ukumbi ule wa semina, tayari Wamarekani walikwishadumisha ulinzi wao kwa kutamani kumlinda mtu huyo kwa kitu chochote kibaya ambacho kingeweza kumtokea.
Nje ya hoteli hiyo, sehemu mbalimbali hasa maghorofani na hata kwenye vioo vya hoteli zilizokuwa karibu na eneo hilo, Wamarekani kutoka C.I.A walikuwa wamejaza titi madirishani huku wakiwa na bunduki zao zilizowekwa vyombo vya kuzuia mlio wa risasi, bunduki zenye nguvu zijulikanazo kama Riffle, bunduki maalumu zilizokuwa zikitumika na wadunguaji (snipers)
Mara baada ya kumuona mwanamke wa Kiarabu aliyevaa juba jeusi akizozana na walinzi waliokuwepo mlangoni, wakahisi kwamba kulikuwa na tatizo lililokuwa limetokea. Walichokifanya ni kuziweka vizuri ‘earphone’ zao ili kusikika mwanamke yule alikuwa akizungumza nini.
“Who is she?” (Ni nani?) aliuliza jamaa mmoja, alikuwa ameiweka vizuri bunduki yake huku akiwa amekwishamlenga mwanamke yule, alikuwa akizungumza na mwenzake aliyekuwa ghorofa nyingine.
“I don’t know,” (Sijui)
“Should I shoot her down?” (Nimpige risasi?)
“No! Just wait,” (Hapana! Subiri kwanza)
Bado walinzi waliendelea kuzozana na mwanamke yule kwamba ilikuwa ni lazima aende katika chumba maalum kwa ajili ya kupekuliwa ili aonekane kama alikuwa mtu salama au la, yeye hakutaka, aliendelea kusisitiza kwamba ilikuwa ni lazima kupita pasipo kukaguliwa.
“Just shoot her down,” (Mpige risadi tu)
Ulikuwa ni uamuzi ulioonekana kuwa sahihi, alichokifanya mwanajeshi yule wa Kimarekani ni kumpiga risasi mwanamke yule, risasi ya kichwa ilimpiga na kumwangusha chini na hapohapo kupoteza maisha hapohapo. Walinzi wale walipomwangalia vizuri kwa ndani, alikuwa amevalia kikoi kilichokuwa na mabomu kadhaa ya kujitoa mhanga.

Mickey aliendelea kutoa masomo ya ujasiriamali katika sehemu mbalimbali katika nchi za Kiarabu, tofauti na Wamarekani wengine, Mickey akatokea kupendwa na kuaminika zaidi ya mtu yeyote kitu kilichowapelekea Waarabu wengi kutaka mtu huyo aendelee kuishi nchini mwao.
Japokuwa alionekana mtu mwenye busara ambaye alizungumza taratibu mpaka kumuelewa, lakini hakukuwa na aliyegundua kwamba huyo Mickey alikuwa miongoni mwa watu wenye roho mbaya waliowahi kutokea katika Shirika la Kijasusi la C.I.A.
Hiyo ilikuwa ni safari yake ya kwanza, baada ya kumaliza semina yake iliyomchukua wiki nne, akarudi nchini Marekani ambapo moja kwa moja akaamua kumuoa msichana wake wa siku nyingi, Elizabeth Kenz na kuanza kuishi pamoja ambapo baada ya mwaka mmoja, wakapata mtoto wa kiume waliyemuita kwa jina la Victor.
Maisha yalikuwa mazuri, japokuwa aliishi na mume wake lakini hakuna hata siku moja Elizabeth aligundua au kuhisi kwamba mume wake, Mickey alikuwa jasusi wa Kimarekani aliyekuwa akiua watu kadiri alivyoagizwa.
Ilipofika mwaka 1993, Mickey akatumwa tena kwenda nchini Iran, lengo kubwa la kutumwa nchini humo lilikuwa ni kupeleleza ni kwa namna gani jeshi la Marekani lingeweza kupenya na kuingia katika nchi mbili, Iraq na Syria.
Hilo, kwake wala halikuwa tatizo, kwa sababu alikuwa mtu makini kwa kila alichokuwa akikifanya, akaelekea huko. Kitu cha kwanza kabisa alichokifanya mara baada ya kuwasili nchini humo ni kwenda katika kambi ya Wamarekani iliyokuwepo katika Mji wa Badhiir, pembezoni mwa nchi ya Iran upande wa Mashariki, sehemu ambayo iliaminika kama imelaaniwa kutokana na ardhi yake kuwa kavu kila wakati.
Alipofika huko, akakaribishwa na kuambiwa kwamba baada ya wiki moja kazi ilitakiwa ifanikiwe na hivyo kurudisha majibu mazuri nchini Marekani. Kwa kuwa alijiamini sana, siku iliyofuata, akaanza zoezi lake la kusafiri kwa kutumia ngamia jangwani ili aweze kufahamu ni sehemu gani jeshi lao lingeweza kupita ili kuingia katika nchi hizo.
Safari haikuwa nzuri, ilikuwa yenye kuchosha, alipita jangwa kwa jangwa, jua lilikuwa kali lakini yote hayo alivumilia kwa kuwa aliamini kwamba anafanya kazi kwa ajili ya nchi yake. Alitembea na ngamia yule mpaka alipofika katika sehemu iliyokuwa na mahema kadhaa, hapo, wakatokea Waarabu wawili waliokuwa na bunduki na kuanza kumsogelea.
“You American?” (Wewe ni Mmarekani?) aliuliza Mwarabu mmoja aliyetumia Kingereza cha kujifunza.
“Yes! Where Am I?” (Ndiyo! Nipo wapi hapa?) aliuliza Mickey.
Waarabu hao waliposikia kwamba mtu aliyesimama mbele yao alikuwa Mmarekani, miongoni mwa watu waliokuwa wakiwachukia, wakamuweka chini ya ulinzi na kumuingiza ndani. Mickey hakuonekana kuwa na wasiwasi, zaidi ya Waarabu kumi walisimama mbele yake na kuanza kuzungumza nao kwa kutumia Lugha ya Kiarabu aliyokuwa akiifahamu vizuri kitu kilichowafanya Waarabu wale kujiona kuwa na thamani, kitendo cha Mmarekani kuzungumza Kiarabu, wakajiona kuwa juu.
Mickey akaanza kuwaelezea kwamba alifika mahali hapo kwa kuwa alikuwa safarini kuelekea nchini Iraq hivyo hakujua ni njia ipi angeweza kupitia, njia ingemfanya kuwa nyepesi kuingia nchini humo pasipo kugundulika.
Alipoulizwa sababu zaidi, aliwaambia kwamba alikuwa mjasiriamali aliyekatazwa kuingia nchini humo ila kwa sababu asilimia kubwa ya watu waliokuwa wakiishi Iraq walikuwa masikini, alitaka kuzungumza nao na kuwaambia namna ambavyo wangeweza kufanya na hatimae kupata utajiri na kuwa wafanyabiashara wakubwa.
Maneno yake, sura yake ya huruma, tabasamu lake likawafanya Waarabu wale wamuamini kwa asilimia mia moja kwani hakuwa mgeni kwao hivyo kumwambia njia za panya zote ambazo zilikuwa zikitumika, alitakiwa kuzitumia hizo kwa ajili ya kufika nchini humo.
“Nashukuru, natakiwa kurudi sasa,” aliwaambia Waarabu gao.
“Kurudi wapi?”
“Mjini.”
“Hauendi Iraq?”
“Nilitaka nifahamu kwanza, nina semina na Wairan, baada ya hapo ndiyo nitaondoka. Mmebarikiwa kuwa na mafuta mengi, ila bado hamjajua ni kwa jinsi gani mnaweza kufanikiwa kupitia mafuta hayo,” alisema Mickey.
Kwa muda wa masaa matano ambayo alikaa nao tayari akaonekana kuwa rafiki yao, wakaanza kucheka naye huku wakimwambia mambo mengi kuhusu nchi nyingi za Kiarabu.
Mickey hakutaka kukaa sana, alichokifanya ni kuondoka na kurudi Badhiir ilipokuwa kambi ya Wamarekani. Alipofika huko, akawaambia kila kitu kilichokuwa kimetokea, mpaka njia ambayo walitakiwa kuitumia jambo lililoonekana kuwa rahisi kufanyika, hivyo Mickey alionekana kuwa msaada kwao.
“You are the man......You are the man,” (Wewe mwanaume...Wewe mwanaume) alisema mwanajeshi mmoja huku akitumia msemo uliomaanisha kumpa sifa mtu, msemo uliotumika sana nchini Marekani hasa kwa vijana wa mtaani.
Usiku wa siku hiyo, Mickey akaanza kupanga mipango yake ya kusonga mbele, alitaka kuelekea upande uliokuwa na nchi ya Syria kwa ajili ya kukamilisha kazi zake alizokuwa amepangia.
Kitu kilichomshtua kutoka katika lindi la mawazo ya mipango yake, ni pale alipoanza kusikia kelele za wanawake zikitokea sehemu kulipokuwa na mahema yaliyotengwa.
Kwanza akashtuka, hiyo ilikuwa ni kambi pekee ya Wamarekani nchini Uarabuni ambayo haikuwa na mwanamke yeyote yule, sasa hizo sauti za wanawake zilikuwa ni za wakina nani.
Hakutaka kubaki hapo, alichokifanya, akachukua bunduki zake na kwenda kule kulipokuwa na mahema yale. Sauti za wanawake waleziliendelea kusikika kwa ukaribu zaidi, alipolifungua hema lile, akapigwa na mshtuko, zaidi ya wanawake kumi wa Kiarabu walilazwa chini na wanajeshi wa Kimarekani waliokuwa na kazi moja tu, kuwabaka kwa zamu huku wanajeshi wengine wakiwa pembeni na bunduki zao, kwa kila kilichokuwa kikiendelea, walikishangangilia.
Moyo wa Mickey ukabadilika, hasira kali zikamkaba kooni, hakuamini kile alichokuwa akikiona mbele yake. Ni kweli alikuwa mwanaume mwenye roho mbaya hasa linapokuja suala la kuua lakini kitendo cha kushuhudia wanawake wakibakwa, kilimkera moyoni mwake. Akageuka na kutaka kuondoka.
“Hey man! Where are going? Come and https://jamii.app/JFUserGuide these young slut girls,” (Hey mwanaume! Unakwenda wapi? Njoo ufanye mapenzi na wanawake hawa wadogo na wachafu) alisema mwanajeshi mmoja huku akimvuta Mickey.
“Let me go,” (Niache niondoke) alisema Mickey huku sauti yake ikisikika kama ya mtu mwenye hasira kali.
Mwanajeshi yule akamuachia Mickey ambaye akaanza kupiga hatua mpaka kwenye hema lile, alipofika, akajilaza kitandani.
Kadiri alivyokuwa akizisikia kelele za wanawake wale, hasira zilizidi kumpanda, akajikuta akianza kuwachukia wanajeshi wale. Ilipofika saa saba usiku, tena kelele zile zikizidi kuongezeka, alichokifanya ni kuchukua bunduki zake zilizokuwa ndani ya begi na kuanza kurudi kule kulipokuwa na mahema yale. Hakukuwa na kitu kingine alichokuwa akikifikiria zaidi ya kuwaua wanajeshi wote, kitendo cha kubakwa kwa wanawake wale, alikichukia kwani alijua haikuwa kazi ambayo iliwapelekea wanajeshi wale kupelekwa katika nchi za Kiarabu.
Alipolifikia hema lile kubwa, akaingia ndani, bunduki zilikuwa mikononi. Hakuwa Mickey yule aliyekuja kipindi cha nyuma, alikuwa amebadilika, hasira kali ilimkaba kooni, alichokuwa akikitaka ni kuwaua wanajeshi wote waliokuwa mule ndani ya lile hema, aliwahesabu harakaharaka, walikuwa kumi na tano.

Aliyesimama mbele yao alikuwa Mickey, yuleyule jasusi kutoka C.I.A, jasusi aliyejulikana zaidi kwa mauaji makubwa aliyokuwa akiyafanya kila alipoambiwa kwamba mtu fulani alitakiwa kuuawa.
Aliwaangalia wanajeshi, kelele za wanawake wale zilimfanya kushikwa na hasira zaidi, paji lake la uso lilitawaliwa na ndita, hakutaka kusikia kitu chochote kwa wakati huo, kile alichokuwa akikitaka ni kuwapiga risasi tu.
Hawakujua kwamba huyu Mickey aliyeingia alikuwa tofauti na yule wa kipindi kilichopita, sasa hivi, alikuwa na hasira mithiri ya mbwa mwitu aliyechokozwa hivyo hakutaka kusikia kitu chochote kile. Akazikoki bunduki zile na kuwanyooshea.
“Paaa...paaaa....” ilisikika milio kadhaa ya risasi ndani ya hema lile, wanajeshi wote kumi na tano wakaanguka chini na kufa hapohapo.
Hali ilionekana kuwa ya hatari mahali hapo, damu zilitapakaa katika kila eneo ndani ya hema lile, wanawake wale wa Kiarabu wakabaki wakilia, hawakuamini kama mtu yule angeweza kuwaua wanajeshi wale na kuwaacha hai wao.
“You are free, you can go home now,” (Mpo huru, mnaweza kwenda nyumbani sasa) alisema Mickey na kutoka hemani mule.
Moyo wake ukaridhika, alichokifanya ni kuondoka mahali hapo huku akijiandaa kutoa ripoti ya uongo juu ya kilichokuwa kimetokea hapo Badhiir.
****
‘Fifteen soldiers were killed in Iran’ (Wanajeshi kumi na tano wauawa Iran) kilikuwa kichwa cha habari kilichopita katika Kituo cha Televisheni cha CNN cha nchini Marekani. Ilikuwa moja ya taarifa iliyomsisimua kila Mmarekani huku wengi wao wakiwa hawaamini kama waliweza kuwapoteza wanajeshi wengi namna hiyo tena kwa wakati mmoja.
Maswali mengi yakaanza kumiminika vichwani mwa watu kwamba ilikuwaje wanajeshi hao wauawe kwa pamoja tena ndani ya hema huku wakiwa wamekaa karibukaribu namna ile.
Swali hilo na maswali mengine yaliyokuwa yakiulizwa na watu yakakosa majibu. Walichokifanya C.I.A ni kuwasiliana na Mickey ili kutaka kufahamu ni kitu gani kilichokuwa kimetokea mpaka wanajeshi hao kuuawa katika kambi waliyomwambia aende huko.
Hawakutaka kupewa majibu kupitia simu, walichomwambia ni kwamba alitakiwa kwenda nchini Marekani ambapo huko, wakamuweka chini na kuanza kuzungumza naye huku ndani ya chumba hicho kukiwa na watu zaidi ya ishirini.
“Nini kilitokea?” aliuliza kiongozi wa shirika hilo, bwana Powell.
“Sifahamu. Siku ya tukio, sikuwa hapo Badhiir, nilikwenda kukamilisha majukumu yangu, na bahati nzuri nikakamilisha kila kitu, tena kwa mafanikio makubwa,” alisema Mickey.
“Ulipoondoka, uliiacha kambi katika hali nzuri?”
“Naweza kusema hivyo kwani hakukuwa na dalili za kutokea kwa adui yeyote yule,” alisema Mickey.
“Kipi unahisi kinaweza kuwa chanzo cha watu hawa kuuawa?”
“Sijajua, ila nilipowaacha, kulikuwa na kundi la wanawake kambini, nahisi, hao ndiyo waliosababisha kila kitu,” alisema Mickey.
Kilichofanyika, upelelezi ulitakiwa kufanyika zaidi ili kujua ni kitu gani kilichokuwa kimetokea. Watu makini walioaminika katika kufanya upelelezi wakaelekea huko, wakaingia mpaka kwenye kambi hiyo na kukaa huko kwa muda wa wiki moja lakini hawakufanikiwa kupata chochote kile.
Siku iliyofuata, zaidi ya Wamarekani mia tatu walikuwa barabarani huku wakiwa na mabango yaliyosema kwamba ilitakiwa wanajeshi wote waliokuwepo katika nchi za Uarabuni warudishwe nchini kwani kuwepo huko kulimaanisha kwamba wanajeshi wengi wangeendelea kuuawa.
Alichokifanya Bush baba ni kuongeza jeshi zaidi nchini humo, hakutaka kusikia kitu chochote kile kuhusu kuwarudisha wanajeshi wake nchini Marekani. Alikuwa na hasira mno na Waarabu, hakutaka watu hao waendelee kuishi, kuna wakati alitamani awe Mungu ili awapoteze wote kwani uwepo wao mbele ya macho yake ilikuwa chukizo kubwa kwake.
Wamarekani walipiga kelele lakini hakukuwa na kilichobadilika, waliandamana mno tena katika majimbo yote nchini humo lakini hakukuwa na utekelezaji wowote ule, msimamo wa rais huyo ulikuwa mmoja tu kwamba ilikuwa ni lazima wanajeshi waongezwe nchini humo kwa ajili ya kuongeza nguvu.
“Kwa nini wasiwaruhusu wanajeshi wetu warudi? Haya mambo ya kivita, huwa siyapendi sana,” alisema Elizabeth huku akionekana kuumizwa na kile kilichokuwa kikiendelea.
“Sijajua ila kama ningekuwa mwanajeshi, nisingeweza kwenda, sisi wengine ambao hata hatujui kushika bunduki, tunaweza kufa kwa presha,” alisema Mickey.
“Hata kule mitaani haukuwahi kushika bunduki?”
“Hapana! Nilikwishawahi kuziona wakiwa nazo watoto wenzangu, lakini sikuwahi kushika hata siku moja, ninazihofia mno,” alisema Mickey huku akijifanya kuogopa kushika bunduki.
Elizabeth aliendelea kupigwa upofu, hakujua kama mume wake ndiye alikuwa nyuma ya kila kitu kwa kuwaua wanajeshi wale. Alipoambiwa kwamba alikuwa muoga kushika bunduki, akayaamini maneno hayo kwani hakuwahi kumuona mume wake akishika bunduki na hata alipomshauri kwamba amiliki bunduki kutokana na umaarufu wake, alimkatalia.
Miongoni mwa watu ambao Elizabeth alikuwa akiwaona kwamba ni waoga namba moja duniani, wa kwanza alikuwa mume wake. Wakati mwingine alijifanya kuogopa mpaka kutazama filamu za kutisha au kila alipokuwa akiangalia filamu zilizojaa mauaji makubwa, alikuwa akikunja sura yake kama mtu aliyeumizwa mno.
Siku zikaendelea kukatika. Kadiri Mickey alipotumwa nchini Marekani, aliendelea kuua kificho hasa pale alipowaona wanajeshi wenzake wakiendelea kuwabaka wanawake wa Kiarabu.
Mwaka 2009 wakati Barack Obama alipokuwa akichukua ofisi na kuwa rais wa Marekani, ndicho kilikuwa kipindi Mickey alitumwa nchini Iran kwa ajili ya kuhakikisha kwamba anawachonganisha watu wa taifa hilo na Iraq kutokana na mtafaruku mkubwa wa mafuta uliokuwa ukiendelea.
Alipofika huko, kama kawaida, tabia za wanajeshi kubaka wanawake wa Kiarabu ilikuwa ikiendelea na hakuacha kuua, aliendelea kuwamaliza wanajeshi wa Marekani kwani kwake, kitendo cha kubakwa kwa mwanamke kilionekana chukizo kubwa kuliko hata kuua.
Ilipofika mwaka 2010, hapo ndipo tetesi zilipoanza kusikika kwamba Mickey, jasusi aliyekuwa akitumainiwa kwa kupewa ‘mission’ nyingi ndiye aliyehusika katika kuwamaliza wanajeshi wengi wa Kimarekani kwa kuwaua kwa sababu tu walikuwa na tabia ya kuwabaka wanawake wa Kiarabu, wakuu wa C.I.A wakakasirika, hasira zao zikawaka dhidi ya Mickey.
Nao wakataka kumuua, yaani ni sawa na kuukata mti ulioupanda mwenyewe na kuumwagilia kila siku. Japokuwa alikuwa mtu muhimu, hawakuwa na jinsi, ili kuokoa maelfu ya wanajeshi wa Kimarekani, ilikuwa ni lazima kumuua Mickey. Ripoti ya ombi la kuuawa, likapitishwa na bwana Powell kusaini. Kilichosubiriwa ni kazi tu kufanyika.

Zoezi la kumuua Mickey halikuwa jepesi hata mara moja, alifanya kazi kama jasusi wa C.I.A kwa kipindi kirefu mno hivyo mbinu zote walizokuwa wakizitumia majasusi alikuwa akizifahamu.
Kuna kipindi walitaka kumuua hotelini huku mmoja wa majasusi akijifanya mfanyakazi wa hoteli hiyo ambaye alikuwa bize akikihudumia chumba chake, kitu cha ajabu, siku ambayo alitaka kummaliza, hakuweza kumuona tena, alikuwa amekwishaondoka zake hotelini hapo.
C.I.A hawakuchoka, bado waliendelea kusisitiza kwamba Mickey alitakiwa kuuawa haraka iwezekanavyo. Kila kitu walichokuwa wakikifanya, alikigundua hivyo walipata wakati mgumu mno.
Mpaka nchi ya Marekani inaweka historia ya kutawaliwa na mtu mweusi, Barack Obama, bado walikuwa wakiendelea kumtafuta Mickey ili wamuue lakini ikashindikana kabisa.
“Nataka tufanye kitu,” alisema Mickey, alikuwa akizungumza na mwanaume mmoja aliyeonekana kufanana naye kuanzia umbo, yaani urefu na mwili.
“Kitu gani?”
“Nitakulipia dola milioni tano endapo tu utakubali kufanya kile ninachokitaka,” alisema Mickey.
“Kitu gani?”
“Nataka uwe mimi.”
“Niwe wewe? Kivipi?”
Mickey akaanza kumfafanulia kwamba alitaka kutengeneza sura ya bandia inayofanana na yeye na kisha kumgawia jamaa huyo ambaye angekuwa mbadala wake na angeshughulika katika kila kitu alichokuwa akikifanya, yaani aonekane kama Mickey.
Japokuwa ilikuwa kazi kubwa lakini malipo yake yakamfanya kuvutiwa na kutaka kuifanya kazi hiyo. Kiasi cha dola milioni tano ambazo zilikuwa ni zaidi ya shilingi bilioni kumi, kilimpagawisha mwanaume huyo aliyeitwa Stefan.
Baada ya kukubaliana kwa kila kitu, Mickey akaanza kufanya mawasiliano na mtaalamu wa kutengeneza sura za bandia, Chung Lu, mwanaume kutoka nchini China. Akafika nchini Marekani na kuonana na Mickey ambapo akapewa maelezo juu ya nini kilitakiwa kufanyika.
Baada ya kupewa maelekezo yote, siku iliyofuata, wote watatu wakawa ndani ya chumba maalumu ambapo humo ndipo kulipofanyika mchakato wa kutaka kutengeneza sura ya bandia na kuvishwa Stefan.
Mchakato mzima ulichukua masaa nane, sura iliyofanana na Mickey ikatengenezwa na kisha kuvarishwa Stefan huku sura nyingine ya Stefan ikitengenezwa na kuvarishwa Mickey. Huo ndiyo ulikuwa mchezo alioamua kuucheza na hakutaka kujali kuhusu chochote kile.
Kesho yake, akachukua kila kilichokuwa chake, kuanzia simu yake, kadi zake zote zikiwepo za benki, magari yake na kumuachia.
Hata Stefan alipoanza kuishi na Elizabeth, mwanamke huyo hakuweza kugundua kitu chochote kile. Kuanzia sauti, muonekano mpaka baadhi ya tabia bado mwanaume huyo alionekana kuwa kama Mickey.
Mara kwa mara Mickey alikuwa akiendelea kufika nyumbani hapo na kujifanya kuwa rafiki mkubwa wa Stefan. Japokuwa kila alipokuwa akimwangalia mke wake akiwa amekumbatiana na Stefan alijisikia wivu lakini hakuwa na jinsi, alijua alichokuwa akikifanya hivyo alivumilia kwa kila kitu.
Katika kipindi ambacho Mickey alitakiwa kwenda nchini Tanzania, tayari C.I.A walikuwa wamekwishaandaa mpango mkubwa wa kumuua hivyo walijiandaa vilivyo. Siku ambayo Stefan alipokuwa akielekea huko huku akiwa na muonekano wa Mickey, hakugundua kwamba kulikuwa na mpango kabambe wa kumuua.
Mickey mwenyewe hakutaka kubaki nchini Marekani, alitaka kufuatilia kila kitu kilichokuwa kikiendelea. Mpaka kipindi ambacho Stefan alipigwa risasi, Mickey alikuwa uwanjani hapo akishuhudia na kuona kwamba hiyo ilikuwa nafasi yake ya kuuawa kama ilivyokuwa imepangwa.
Dunia nzima ikaingiwa na majonzi, kila mtu akalaumu kwa nini Mickey alikuwa ameuawa na wakati alikuwa mhamasishaji mkubwa duniani na alifanya kila kitu alichoweza kuwakwamua watu kutoka katika umasikini mkubwa waliokuwa nao.
C.I.A wakafurahia pasipo kufahamu kwamba mtu waliyekuwa wamemuua hakuwa Mickey bali alikuwa Stefan aliyevaa sura ya bandia ya Mickey.
Elizabeth alilia usiku na mchana, kifo cha mumewe kilimuuma mno, hakula wala hakulala, kila alipokuwa akikaa na kumfikiria mume wake, alizidi kuumia moyoni wake.
“I will avenge, I will kili a person who murded my father,” (Nitalipa kisasi, nitamuua yule aliyemuua baba yangu) alisema Victor huku akionekana kuwa na hasira.
Mwaka mmoja baadae, Mickey akajitokeza kwa mke wake huku akiwa na muonekano wa Stefan. Elizabeth alipomuona, hakujua kama ni mume wake bali alijua kwamba ni rafiki mkubwa wa marehemu mume wake.
“Kuna siri nzito nataka kuongea nawe,” alisema Mickey huku sauti yake ikiwa imebadilika kabisa.
“Siri gani?”
“Kuhusu mume wako,” alisema Mickey, hapohapo Elizabeth akaanza kububujikwa na machozi kwani picha ya mume wake ikaanza kumrudia tena.
“Amefanyaje?”
“Naomba tukaongelee chumbani, hii ni siri nzito mno,” alisema Mickey.
“Kuongelea chumbani?”
“Ndiyo!”
“Hapana. Hakuna mtu anayeruhusiwa kuingia chumbani kwangu, haiwezekani!”
“Lakini hili ni muhimu kwako.”
“Hapana. Nimesema haiwezekani, tena naomba uondoke,” alisema Elizabeth huku akiwa amekwishabadilika, tayari machozi yale yalikuwa yamekwishaloanisha mashavu yake. Taswira ya mume wake ilijirudia vema kichwani mwake.
****
Ilionekana kuwa ngumu sana kwa Mickey kuzungumza na mkewe kuhusu kile kilichokuwa kimetokea mpaka kufikia siku hiyo. Muda wote Elizabeth alikuwa akilia tu kwani kwa jinsi alivyokuwa akimpenda mume wake, na vile ambavyo Mickey mwenye sura ya Stefan alivyomkumbusha, aliumia mno.
Alitamani kumwambia hapohapo kwamba yeye ndiye alikuwa mume wake lakini hakuona aanzie wapi, alichokifanya ni kuondoka huku akimuachana mke wake katika hali hiyo.
Huko, kitu cha kwanza kabisa alichokifanya ni kuwasiliana na mtoto wake, Victor na kuomba kukutana naye kwa kuwa alikuwa na mambo mengi aliyotaka kumwambia kuhusu baba yake, yaani yeye mwenyewe.
Kwa kuwa kijana huyo alikuwa nchini Ujerumani, akaomba kukutana naye baada ya wiki moja, kweli, baada ya wiki moja, Victor alikuwa mbele yake, akaanza kuzungumza naye.
Victor alibaki kimya akimsikiliza Mickey, hakugundua kama alikuwa baba yake, alichokifahamu ni kwamba mtu huyo alikuwa rafiki mikubwa wa baba yake.
Kitu alichokifanya Mickey ni kumuhadithia Victor tangu siku ile alipokuwa amezaliwa, vitu alivyokuwa akivifanya kama mtoto na kumuonyeshea picha nyingi za kipindi hicho. Victor akapigwa na mshangao, alijiuliza kwamba ilikuwaje rafiki wa baba yake awe na vitu vingi namna hiyo na wakati hata baba yake hakuwa navyo? Kila alichojiuliza, alikosa majibu.
“Where did you get them?” (Umevipata wapi?) aliuliza Victor.
“I had them since you were a baby boy,” (Nilikuwa navyo tangu ulipokuwa mtoto mdogo) alisema Mickey.
“My dad has never shown me all of these,” (Baba hakuwahi kunionyeshea hivi vyote) alisema Victor huku akichukua simu ile na kuanza kuziangalia picha zile.
“I know! But let me tell you the truth,” (Najua! Ila acha nikwambie ukweli)
“What truth?” (Ukweli upi?)
“I am your father,” (Mimi ni baba yako)
“What?” (Nini?)
“Shiiiii”
Mickey akamtuliza Victor, alionekana kama mtu aliyeshtuka sana hivyo akamwambia atulie na kisha angemwambia kila kitu kilichokuwa kimeendelea. Kwanza Victor hakuonekana kuamini, ilikuwaje mwanaume huyo aseme kwamba alikuwa baba yake na wakati alifahamu fika kwamba baba yake alikuwa Mickey.
Aliendelea kujiuliza zaidi labda mama yake alikuwa ametembea nje ya ndoa na mwisho wa siku mwanaume huyo kumpa mimba na hivyo kupata mtoto ambaye ndiye yeye, kila alichokuwa akijiuliza, alikosa jibu.
“Haiwezekani, baba yangu ninamjuua, mama hawezi kumsaliti baba na kutembea na wewe,” alisema Victor huku akionekana kuchanganyikiwa.
“Mimi ni nani?”
“Nakujua wewe kama rafiki yake baba yangu.”
“Sawa. Twende tukatembee, nitakwambia kila kitu.”
Walichokifanya ni kutoka hapo mgahawani walipokuwa na kwenda kutembea katika eneo kubwa la Bustani ya Livingston iliyokuwa hapo New York, pembezoni mwa Mghahawa wa KFC.
Huku, Mickey akaanza kumuhadithia mtoto wake kila kitu kilichokuwa kimetokea katika maisha yake tangu siku ya kwanza alipojiunga na CIA, wanajeshi walipowabaka wasichana wa Kiarabu na kuamua kuwaua mpaka mpango mzima uliofanywa kwa ajili ya kummaliza.
Victor alibaki akishangaa, hakuamini kile alichokuwa amekisikia kutoka kwa baba yake, hapohapo, akajikuta akimkumbatia kwa furaha kwani baada ya kuumia kwa kipindi kirefu kwa kudhani kwamba baba yake alikuwa ameuawa nchini Tanzania na C.I.A, mwisho wa siku akakutana naye tena na kumwambia kwamba alikuwa mzima na aliyeuawa hakuwa yeye.
Siku hiyohiyo wakaelekea nyumbani, huko, akamwambia mama yake kile kilichotokea, bi Elizabeth akajikuta akibubujikwa na machozi na hata Mickey alipoamua kuwatembelea tena, akajikuta akimkumbatia kwa furaha.
Hawakutaka kuchelewa, baada ya miezi miwili, Elizabeth akatangaza kwamba alitaka kuolewa na rafiki wa mume wake, Stefan pasipo dunia kujua kwamba huyo bwana harusi ndiye alikuwa mume wake wa ndoa.
Mickey akamuoa tena Elizabeth na maisha kuanza tena. Akaachana na C.I.A, akawa mwanaume huru aliyeanzisha biashara nyingi na kuuendelezea ubilionea aliokuwa nao.
Kwa nchini Tanzania, mara baada ya kupewa maelezo juu ya mauaji yaliyokuwa yametokea kwamba yalikuwa chini ya Marekani, Gideon akaachiwa huru na kurudi nchini Malawi ambapo huko akaendeleza upelelezi wake mpaka kumtia mikononi bwana Timoth.
Mpaka ilipofikia mwaka 2013, bwana Mickey, huku akiwa chini ya jina la Stefan, akafanikiwa kupata mtoto wake wa pili wa kike aliyempa jina la Lindsey.

MWISHO
TOA MAONI YAKO


CHANZO : BURE SERIES
 

Similar Discussions

5 Reactions
Reply
Back
Top Bottom