TCCIA Manyara watoa ushauri TRA kufuatia Malalamiko ya wafanyabiashara

mkiluvya

JF-Expert Member
May 23, 2019
802
725
Baadhi ya wafanyabiashara mjini Babati mkoa wa Manyara wakitoa maoni yao juu ya utendaji wa mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) mkoani hapo,wameonyesha kutoridhishwa na namna wanavyohudumiwa. Wakizungumza na kituo hiki bila kutaja majin yao, wamesema kuwa baadhi ya watumishi katika mamlaka hiyo wamekuwa na tabia ya kukadiria mapato makubwa kwa wafanyabiashara ili kutengeneza meza ya mazungumzo, hatua inayopelekea kutengeneza mazingira ya Rushwa.

Wameipongeza TAKUKURU mkoa wa Manyara kwa kuanza kufuatilia utendaji wa Mamlaka ya Mapato (TRA) huku wakiomba viongozi wa ngazi mbalimbali za serikali, kuwa na utaratibu wa kusikiliza kero zinazowakabili wafanyabiashara. Katibu wa chama cha wafanyabiashara,wakulima na wenye viwanda (TCCIA) Mkoa wa Manyara Mwanahamisi Hussein amesema ni muda mrefu wafanyabiashara wamekuwa wakiilalamikia mamlaka hiyo.

Katibu huyo ameiomba mamlaka hiyo kuwa na tabia ya kuwatembea wafanyabiashara mara kwa mara na kufuatilia mienendo ya watendaji wao wanaowatuma akieleza kuwa hatua hiyo itasaidia kupunguza kero za muda mrefu za kodi ambazo zimekuwa kikwazo katika ukuaji wa shughuli za biashara nchini.

Katika hatua nyingine Mwanahamisi ameeleza kuwa wameandaa utaratibu maalum wa kusikiliza kero mbalimbali za wafanyabiashara mkoani hapo na kuwapatia ushauri,ambapo huwashirikisha pia Mamlaka ya Mapato Manyara. Kwa madai ya kusumbuliwa na Mamlaka hiyo taarifa zinaeleza kuwa imepelekea wengine kupata shinikizo la damu huku baadhi wakifunga biashara zao.

Mkuu wa Taasisi ya kuzuia na kupambana na Rushwa mkoa wa Manyara (TAKUKURU) Holle Mkungu, mwezi Mei,2020 waliwafikisha katika Mahakama ya hakimu mkazi Manyara maafisa wawili wa TRA kwa makosa ya kudai na kupokea Rushwa ya shilingi Milioni kumi. Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Subilaga Mwangama na Ojungu Mollel, na kwamba walifanya makosa hayo kinyume cha kifungu cha 15 cha sheria ya kuzuia na kupambana na Rushwa namba 11/2007.

Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango akizungumza bungeni Juni 13, 2019 wakati akiwasilisha bajeti ya Serikali Kuu kwa mwaka 2019/2020, alisema ili kupunguza malalamiko ya wafanyabiashara, Serikali imeamua kuanzisha kitengo huru cha kupokea malalamiko ya taarifa za kodi dhidi ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na kusimamiwa na kuratibiwa na wizara yake ili kuhakikisha kinakuwa na ufanisi wa kushughulikia kero za wafanyabiashara. Alisema majukumu ya kitengo hicho ni kupokea malalamiko ya rushwa dhidi ya watumishi wa TRA ambao wamekuwa wakijipatia fedha kinyume na sheria na kuwakandamiza wafanyabiashara.

Aidha, kitengo hicho kinahusika kupokea malalamiko ya ukadiriaji wa kodi na uthaminishaji wa bidhaa husika pasipo kufuata taratibu zilizowekwa na malalamiko ya matumizi ya nguvu katika ukusanyaji wa kodi dhidi ya TRA.
 
Back
Top Bottom