TBS yaamka usingizini

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,790
288,005
TBS yaamka usingizini
Wednesday, 20 June 2012 21:06

Fidelis Butahe
Mwananchi

SIKU chache baada ya Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Abdallah Kigoda kuiagiza Bodi ya Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kumsimamisha kazi Mkurugenzi wake Charles Ekelege, shirika hilo limetangaza kampuni zilizopewa kazi ya kukagua magari yanayotoka nje ya nchi.

Mapema mwezi uliopita Dk Kigoda alitoa agizo hilo la kumsimamisha kazi Ekerege ili kupisha taratibu za kisheria ikiwamo uchunguzi kufanyika dhidi yake kutokana na madai ya TBS kuwa na ofisi hewa za ukaguzi wa magari nje ya nchi.

Sakata la Ekelege liliibuliwa mwanzoni mwa mwaka huu, ambapo Kamati ya Bunge ya Mashirika ya Umma (POAC), chini ya Makamu Mwenyekiti wake, Deo Filikunjombe ilimtuhumu mkurugenzi huyo baada ya kubaini kuwepo kwa udanganyifu kwenye mpango wa TBS wa kukagua bidhaa nje ya nchi. Filikunjombe alieleza kuwa waligundua madudu baada ya kutembelea vituo vya ukaguzi wa magari nchini Singapore na mjini Hong Kong, China ambapo walikuta vituo hewa vya ukaguzi wa magari.

Lakini jana, shirika hilo kupitia gazeti hili lilitoa tangazo lililotolewa na Kaimu Mkurugenzi wake mkuu, linataja kampuni zilizopewa na zilizopokonywa kazi ya kukagua magari.

Tangazo hilo limeeleza kuwa tangu Juni 18 mwaka huu TBS imefuta leseni Na 0656 ya ukaguzi wa magari iliyokuwa ikifanywa na gereji ya Jaffar Mohammed Ali iliyopo Dubai ambayo ilikuwa ikikagua magari yanayoingizwa nchini kutoka nchi hiyo.

“Kutokana na tangazo hili wote wanaoingiza magari kutoka Dubai wanashauriwa kupeleka magari yao kukaguliwa na kampuni ya Jabal Kilimanjaro Auto Elect Mechanical, magari ambayo yataingizwa nchini bila kukaguliwa na kampuni hii hayataruhusiwa kuingizwa katika soko la Tanzania,” lilieleza tangazo hilo.

Pia, lilieleza kuwa limefuta leseni Na 0655 ya kampuni ya WTM Utility Services ya nchini Uingereza kujihusisha na ukaguzi wa magari na badala yake magari yote kutoka nchini humo yanatakiwa kukaguliwa na kampuni ya Vehicle Operator Services Agency (VOSA).

“Magari yatakayoingizwa nchini kutokea Uingereza bila kukaguliwa na kampuni hii ya VOSA hayataruhusiwa kuingia katika soko la Tanzania” lilieleza tangazo hilo.

 
Back
Top Bottom