Mama Amon
JF-Expert Member
- Mar 30, 2018
- 2,021
- 2,478
Tundu Lissu (Mgombea Urais wa Chadema) na Job Ndugai (Spika)
Kuna mdau kanitumia kitabu cha Gene Sharp (2012), kiitwacho "From Dictatorship to Democracy: A Conceptual Framework for Liberation."
Yaani, "Safari ya Kutoka Kwenye HImaya ya Kidikteta Kuelekea Kwenye HImaya ya Kidemokrasia: Mawazo Ambayo ni Msingi wa Hoja za Kuendeleza Mapambano ya Ukombozi." (Tafsiri yangu).
Mdau huyu amenitaka nikisome na kisha nijibu swali hili: Kama wabunge wa viti maalum wanatokana na kura za mgombea urais, na kama kura za mgombea urais wa CHADEMA zilizotangazwa na tume ni sehemu ya kura zote ambazo Chadema wanadai kwamba walipata, uamuzi wa kukataa kuteua wabunge wa viti maalum wa Chadema ili waende Bungeni kula kiapo na kuchapa kazi ya ubunge unachangia vipi katika kuimarisha demokrasia nchini Tanzania?
Nimekisoma kitabu na kukimaliza. Kina kurasa 100, na kimeandikwa kwa Kingereza chepesi. Ninaelewa mengi yaliyojiri katika siku zote za uchaguzi mkuu wa 2020. Pia najua malalamiko kadhaa ya vyama vya upinzani. Baada tafakari nimefikiria kama ifuatavyo:
Mosi, kama mgombea urais wa Chadema (Lissu) alipata kura X, na NEC ikatangaza kwamba Lissu kapata kura Y, ni wazi kwamba kura X ni kubwa kuliko kura Y, yaani X>Y.
Pili, Tofauti kati ya kura X na kura Y, tuseme kura Z, ndizo kura zinazobishaniwa. Chadema wanapinga kutotangazwa kwa kura Z. Yaani, Chadema wanapinga kutangazwa kwa kura Y pekee bila kujumlisha kura Z.
Tatu, kura Y zilizotangawa na NEC ni sehemu ya kura X zinazotamkwa na viongozi wa Chadema.
Nne, wabunge wa viti maalum wa Chadema wanatokana na kura Y, ambazo ni kura halali.
Kwa hiyo, idadi ya wabunge wa viti maalum kupitia Chadema iliyotangazwa na NEC ni idadi ya wabunge iliyotokana na kura halali.
Lakini, kama Chadema wanasema kuwa LIssu alipata kura ambazo ni ndogo kuliko zile zilizotangazwa na NEC, basi hitimisho langu linaporomoka hadi kuwa kifusi; na nitaungana nao katika msimamo wa kukataa kuteua wabunge wa viti maalum.
Nitatoa mifano miwili ili kufafanua hitimisho langu hili.
Mfano wa kwanza, ni mfano wa mtu aliyefukuzwa kazi, akamshitaki mwajiri kwenye Mahakama ya Kazi, Makahaka ikaamuru alippwe Milioni 10 kama fidia. Ikiwa mwajiri atamlipa milioni 3 pekee, anazipokea na kuzitumia kama gharama za kuweka wakili ili ambane mwajiri kwa hoja kwamba malipo ya milioni tatu "pekee" hayatoshi, lakini baada ya kuchukua milioni tatu.
Na mfano wa pili ni wa kifalsafa zaidi. Tunapotaja fasili ya umbo linaloitwa pembetatu tunasema hivi: "Pembetatu ni umbo lenye kona tatu pekee na pande tatu pekee."
Katika fasili hii neno "pekee" ni muhimu sana, kwani hata mraba unazo pembe tatu na kona tatu pia. Lakini mraba hauna pembe tatu "pekee" wala pande tatu "pekee."
Kwa mujibu wa mifano hii miwili, sasa nahitimisha hoja yangu. Katika kura za mgombea urais, Tundu Lissu, Chadema hawadai kura Y pekee, kama ilivyotangazwa na NEC. Wanadai kura Y na kura Z, ambapo tayari wamekwishapatiwa kura Y, lakini bado kupatiwa kura Z, kama watathibitisha kwamba zipo.
Hivyo, Chadema wanaweza, na wanapaswa kupokea kura Y na kuendelea kudai kura Z, kwa kuweka bayana hoja isiyoruhusu hewa wala maji kupenya.
Kwa mantiki hii, Chadema hawapaswi kuona shida kuteua wabunge wa viti maalum ili waende Bungeni kuapa. Nashauri wafanye hivyo leo.
Hapa nimejaribu kufikiri kwa sauti kwa kuzingatia hoja zilizojengwa na Gene Sharp (2012) katika kitabu chake kiitwacho "From Dictatorship to Democracy: A Conceptual Framework for Liberation."
Kwa mujibu wa kitabu hiki, kukataa kuteua wabunge wa viti maalum, kama wanavyofanya Chadema kwa sasa, ni aina mojawapo ya udikteta; na majadiliano ya maana hufanyika kati ta "mdikteta" na "mdemokrasia."
Yaani, Chadema inabidi waonyeshe kwa mawazo, maneno na vitendo kwamba wao ni "wademokrasia" ili wapate uhalali wa kumkabili yule anayeitwa "mdikteta."
Nimeambatanisha kitabu hicho hapa chini, kwa ajili ya wale wenye utayari wa kujisomea.
Huu ni mtazamo wangu, na ninawajibika kikamilifu kusanifu hoja hii yenye kutetea mtazamo huu.
Mama Amon,
Sumbawanga Kusini.