JamiiForums
JF Official Account
- Nov 9, 2006
- 6,202
- 5,012
Jamii Media Limited inasikitika kutangaza kuondokewa na mmoja wa wafanyakazi wake, Mwandishi Mkuu wa FikraPevu.com, Dotto J. Mnzava aliyefariki leo, Disemba 14, 2015 kufuatia ajali iliyohusisha pikipiki na gari iliyotokea maeneo ya Victoria, Mwananyamala jijini Dar es Salaam.
Mnzava alikuwa mwandishi wa Habari akiiandikia mitandao ya JamiiForums.com na FikraPevu.com na alijiunga na Jamii Media mapema mwaka jana, 2014.
Mipango ya mazishi na kusafirisha mwili wa marehemu kuelekea kwao Same kwa ajili ya maziko inaendelea kufanyika na kwa sasa mwili umehifadhiwa katika Hospitali ya Mwananyamala. Kuaga mwili kwa wakazi wa Dar kutafanyika Disemba 16, 2015 katika Kanisa la Waadventista Wasabato, Manzese (ulipo uwanja wa Tippi).
Tunatoa pole za dhati kwa ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu Dotto J. Mnzava.
Mungu amjalie pumziko la amani!
Amina
===================
Habari toka vyanzo vingine zaidi:
HABARI
Nimepokea taarifa za kushtua na zenye simanzi ambayo ni ngumu kufutika kichwani, tumempoteza kipenzi chetu, mwenzetu na rafiki yetu Dotto Mnzava. Dotto ni mwandishi wa habari na alikuwa anaenda kwenye mishe zake za kikazi, kutokana na foleni za Dar ikabidi achukue bodaboda (usafiri wa pikipiki).
Akiwa eneo la Victoria, pikipiki aliokuwa akisafiria ilipata ajali na yeye alianguka barabarani ndipo gari ikampitia kichwani na kusababisha mauti yake. Mwili wa marehemu umehifadhiwa hospitali ya Mwananyamala kusubiri taratibu za mazishi.
BWANA AMETOA NAYE AMETWAA JINA LAKE LIHIMIDIWE
BLOGGER chipukizi nchini Dotto Mzava, amefariki Dunia katika ajali ya barabarani Desemba 14, 2015 hapa jijini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa taarifa ya Mwenyekiti wa Mtandao wa Bloggers Nchini, (TBN), ambao marehemu alikuwa ni mwanachama wake, Bw. Joackim Mushi amesema Dotto ambaye alikuwa akifanyia kazi Jamii Media (Wamiliki wa mtandao wa JamiiForums na Fikra Pevu, amefariki kwa ajali ya pikipiki ingawa haikuelezwa ajali hiyo imetokea maeneo gani hasa ya jiji la Dar es Salaam.
Bwana ametoa na Bwana ametwaa Jina lake Lihimidiwe Amin.
SOURCE: MICHUZI MEDIA
===================
UPDATE:
Habari za jioni WanaJamiiForums,
Mwili wa ndugu yetu Dotto Mnzava tayari umeagwa rasmi kwa hapa Dar-es-Salaam katika Kanisa la Waadventista Wasabato Manzese karibia na uwanja wa TIPPI.
Mwili wake uko njiani unasafirishwa kuelekea nyumbani kwao Same Kilimanjaro kwa ajili ya kupumzishwa kwenye nyumba yake ya milele.
Tunaendelea kuwakaribisha rafiki na ndugu wote wa Dotto Mnzava tuungane tukielekea kumpumzisha kwenye nyumba yake ya milele.
Kwa maelezo zaidi piga namba: 0767 137 137
=====================
Jeneza lenye Mwili wa Marehemu Dotto Mzava likishushwa Kwenye gari maalum mara baada ya kuwasili katika kanisa la Wasabato Manzese uzuri kwaajili ya sala ya kuombea kabla ya Mwili kusafirishwa kuelekea Wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro.
Mchungaji wa kanisa la Adventist wasabato akiendelea na ibada wakati wa ibada ya kumuombea marehemu kabla ya kusafirishwa kuelekea Same Kilimanjaro
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Jamii Media Maxence Mello akitoa historia fupi ya Marehemu Dotto Mzava ambae pia alikua mmoja wa watumishi katika kampuni hiyo.
Baba Mkubwa wa marehemu Dotto Mzava akitoa maneno ya shukrani katika kanisa la Kisabato la Manzese Uzuri mara baada ya zoezi la misa kumalizika.
Heshima za Mwisho zikiendelea kutolewa
Majonzi na simanzi kwa ndugu wa marehemu
Mmiliki wa Fullshangwe Blog, John Bukuku akitoa heshima za mwisho
Heshima za mwisho zikiendelea kutolewa kwa mwili wa marehemu Dotto Mzava kabla haujasafirishwa kuelekea Same Kilimanjaro kwaajili ya mazishi
Mbunge wa Jimbo la Kibamba, John Mnyika akitoa heshima zake za mwisho kwa mwili wa marehemu Dotto Mzava kabla ya Kusafirishwa kuelekea Same Kilimanjaro kwa mazishi yanayotarjiwa kufanyika kesho
Mkurugenzi mtendaji wa Jamii Media akitoa heshima za mwisho kabla ya mwili wa marehemu kusafirishwa Same Mkoani Kilimanjaro mapema leo.
Ibada ikiendelea
Jeneza lenye mwili wa marehemu Dotto Mzava likipandishwa ndani ya gari tayari kwa safari ya kuelekea Same Mkoa wa Kilimanjaro leo kwaajili ya mazishi yanayotarajiwa kufanyika kesho