Hatimaye Filamu maalum ya kutangaza utalii wetu imezinduliwa rasmi. Mapokeo ya filamu hiyo miongoni mwa Watanzania wengi yamekuwa makubwa sana huku matarajio ya kupaa kwa utalii wetu yakipaa juu zaidi.
Mara ya kwanza nilipoona tangazo la filamu hii kwenye vyombo vya habari na mitandao ya kijamii niliona ni majibu ya kilio cha muda mrefu cha wadau mbalimbali wa utalii. Wadau waliopaza sauti zao kulilia jitihada zaidi za kutangaza vivutio vyetu vya utalii.
Baada ya kuitazama filamu ya Tanzania The Royal Tour nimeguswa sana na kazi nzuri iliyofanyika. Filamu inavutia,inahamasisha,imeonesha dunia vivutio vikubwa vya utalii vilivyomo nchini mwetu, utamaduni wetu, madhara ya kimazingira ya shughuli za kibinadamu kwenye mali asili zetu na mipango ya kusonga mbele zaidi kimaendeleo kama taifa.
Pamoja na kazi kubwa iliyofanyika kwenye filamu ya Tanzania The Royal Tour,kuna mambo machache ambayo kwa mtazamo wangu nimeona yangeweza kufanyika vizuri zaidi au tofauti.
Filamu nzima ya Tanzania The Royal Tour imechukua dakika 56 tu. Katika dakika hizo 56 kuna utangulizi, mahojiano kati ya Peter na mama Samia, historia fupi ya Mama samia na nchi,safari kwenda kutembelea visiwa vya Zanzibar, mlima Kilimanjaro, mgodi wa madini ya Tanzanite Mirerani-Arusha, Hifadhi za taifa za Ngorongoro na Serengeti. Mambo yote haya ndani ya dakika 56 tu.
Filamu inaweza kufikisha ujumbe tofauti na uliokusudiwa. Kwa mtu ambaye hajafika kabisa Tanzania kupitia filamu hii anaweza kupata picha madini pekee yaliopo Tanzania ni Tanzanite. Kwakuwa lengo la filamu ni kutangaza utalii na fursa zilizopo nchini,madini yote tuliyonayo yangemulikwa japo kwa ufupi na mkazo uliokusudiwa ungewekwa kwenye madini ya Tanzanite.
Filamu imeonesha hifadhi tatu tu,Hifadhi za Taifa za Serengeti, Ngorongoro na mlima Kilimanjaro. Hakuna maelezo japo kwa ufupi ya uwepo wa hifadhi nyingine nyingi za Taifa, hifadhi teule, hifadhi za mawindo na mapori ya akiba. Kwenye filamu hii ni kama vile Tanzania hakuna Mikumi, Saadani, Mkomazi, Gombe na hifadhi nyingine nyingi zilizopo sehemu mbalimbali za nchi yetu.
Ikiwa filamu imeonesha kwa uzuri historia iliyobebwa na visiwa vya Zanzibar,je haikufaa kitu kuonesha hata kwa ufupi sehemu nyingine za kihistoria ikiwemo Bagamoyo, Kilwa Kivinje, Kilwa kisiwani,makumbusho ya Taifa na sehemu zote zilizobeba historia nzuri ya nchi yetu.
Kwanini tutumie dakika 56 pekee kutangaza utalii wetu wakati iliwezekana kutengeneza filamu ya muda mrefu zaidi iliyoshiba?
Wakati namshirikisha jamaa yangu mmoja kuhusu mapungufu niliyoyaona kwenye filamu ya Tanzania The Royal Tour,aliniambia kitu kilichonifumbua macho zaidi. Kuna filamu nyingine za Royal Tour zilizoandaliwa na producer Peter Greenberg za mataifa ya Ecuador, Israel, Poland, Mexico na taifa moja lililonipa mshangao nilipoliona, Rwanda. Jamaa yangu hakutaka nikosoe filamu yetu akiamini walioandaa ni wataalam waliobobea. Lakini jicho langu liliguswa zaidi kuiona Rwanda kwenye hoja yake. Rwanda ametangaza nchi yake kwenye mfululizo wa filamu za The Royal Tour miaka minne kabla yetu,Rwanda ana nini cha kutangaza hata apate wazo miaka minne kabla yetu?
Filamu ya The Royal Tour ya Rwanda imetuumia dakika 56 kuonesha vivutio vyao vyote.Je dakika 56 hizo hizo zinatosha kuonesha vivutio vilivyopo Tanzania ambayo ukubwa wake kwa mujibu wa Peter Greenberg ni sawa na nchi za Ufaransa na Ujeruman zikiungana huku vivutio vyake vikitapakaa kila kona ya nchi?
Ikiwa utengenezaji wa Filamu hii unategemewa kuleta tija kwenye sekta ya utalii nchini, ni vizuri tukaangalia namna ya kutangaza utalii wetu katika kona tofauti tofauti. Hapa ndio akili yangu inaiwaza tena Rwanda ambayo haina lolote la maana katika utalii lakini imefanya The Royal Tour kabla yetu.
Rwanda sio tu kwamba amefanya filamu hiyo bali pia ni mdhamini wa jezi za vilabu vya mpira vya PSG ya Ufaransa na Arsenal ya Uingereza. Katika udhamini huo wachezaji wa timu hizo watavaa jezi zao zikiwa na maandishi “VISIT RWANDA”. Katika hili kama taifa tuna jambo lingine la kujifunza na kuiga kutoka Rwanda.
Filamu ya Tanzania The Royal Tour ina tija bila shaka lakini filamu ile sio ya Hollywood na soko kubwa la filamu lipo Hollywood. Filamu za Hollywood ndio zina watazamaji wengi zaidi duniani. Wito wangu ni kutangaza zaidi vivutio vya utalii kwa kutumia filamu za Hollywood. Kwenye filamu ya Lara Croft Tomb Rider, mwanadada Angelina Jolie akiwa katika jukumu la kutafuta sanduku la Pandora anajikuta akiwa na wajibu wa kufika kwenye mlima Kilimanjaro,lakini kwenye sinema hiyo mlima Kilimanjaro haupo Tanzania na Angelina jolie anafika Kilimanjaro kupitia Kenya kwa msaada wa wazee wa Kikuyu.
Tanzania tuna kiwanda chetu cha filamu na filamu zetu zinaweza kutumika kutangaza utalii wetu .Ikiwa ubora wa filamu zetu kwenye soko la kimataifa ni jambo linalotia mashaka, ushirikishwaji wa makampuni ya kimataifa kutengeneza filamu zenye mazingira ya kitanzania zenye maudhui ya kutangaza utalii ni jambo linalopaswa kuangaliwa vizuri. Media For Development International wametengeneza filamu na tamthiliya za Kitanzania zenye viwango vya kimataifa zinazobeba jumbe mbalimbali ikiwemo magonjwa ya malaria na ukimwi,tohara kwa wanaume, rushwa na kilimo. Kona hiyo pia inaweza kutumika kutengeneza filamu za kwetu zenye viwango vya kimataifa zenye maudhui ya kutangaza utalii wetu na kuuza filamu hizo kwenye masoko ya kimataifa.
Ikiwa ni dhahiri kwamba serikali ya awamu ya sita imedhamiria kuweka nguvu za kutosha kwenye kukuza utalii wetu. Mafanikio ya filamu hii yawe chachu ya kutufunza kuwekeza nguvu zaidi kwenye mambo mengine yanayogusa uchumi wetu. Mwalimu Nyerere kwenye kitabu chake cha Ujamaa na Kujitegemea aliweka msisitizo kwa Watanzania kuingia kwenye vita vya kiuchumi tukiwa na silaha pekee tunayoifahamu vizuri,Kilimo.
Mara ya kwanza nilipoona tangazo la filamu hii kwenye vyombo vya habari na mitandao ya kijamii niliona ni majibu ya kilio cha muda mrefu cha wadau mbalimbali wa utalii. Wadau waliopaza sauti zao kulilia jitihada zaidi za kutangaza vivutio vyetu vya utalii.
Baada ya kuitazama filamu ya Tanzania The Royal Tour nimeguswa sana na kazi nzuri iliyofanyika. Filamu inavutia,inahamasisha,imeonesha dunia vivutio vikubwa vya utalii vilivyomo nchini mwetu, utamaduni wetu, madhara ya kimazingira ya shughuli za kibinadamu kwenye mali asili zetu na mipango ya kusonga mbele zaidi kimaendeleo kama taifa.
Pamoja na kazi kubwa iliyofanyika kwenye filamu ya Tanzania The Royal Tour,kuna mambo machache ambayo kwa mtazamo wangu nimeona yangeweza kufanyika vizuri zaidi au tofauti.
Filamu nzima ya Tanzania The Royal Tour imechukua dakika 56 tu. Katika dakika hizo 56 kuna utangulizi, mahojiano kati ya Peter na mama Samia, historia fupi ya Mama samia na nchi,safari kwenda kutembelea visiwa vya Zanzibar, mlima Kilimanjaro, mgodi wa madini ya Tanzanite Mirerani-Arusha, Hifadhi za taifa za Ngorongoro na Serengeti. Mambo yote haya ndani ya dakika 56 tu.
Filamu inaweza kufikisha ujumbe tofauti na uliokusudiwa. Kwa mtu ambaye hajafika kabisa Tanzania kupitia filamu hii anaweza kupata picha madini pekee yaliopo Tanzania ni Tanzanite. Kwakuwa lengo la filamu ni kutangaza utalii na fursa zilizopo nchini,madini yote tuliyonayo yangemulikwa japo kwa ufupi na mkazo uliokusudiwa ungewekwa kwenye madini ya Tanzanite.
Filamu imeonesha hifadhi tatu tu,Hifadhi za Taifa za Serengeti, Ngorongoro na mlima Kilimanjaro. Hakuna maelezo japo kwa ufupi ya uwepo wa hifadhi nyingine nyingi za Taifa, hifadhi teule, hifadhi za mawindo na mapori ya akiba. Kwenye filamu hii ni kama vile Tanzania hakuna Mikumi, Saadani, Mkomazi, Gombe na hifadhi nyingine nyingi zilizopo sehemu mbalimbali za nchi yetu.
Ikiwa filamu imeonesha kwa uzuri historia iliyobebwa na visiwa vya Zanzibar,je haikufaa kitu kuonesha hata kwa ufupi sehemu nyingine za kihistoria ikiwemo Bagamoyo, Kilwa Kivinje, Kilwa kisiwani,makumbusho ya Taifa na sehemu zote zilizobeba historia nzuri ya nchi yetu.
Kwanini tutumie dakika 56 pekee kutangaza utalii wetu wakati iliwezekana kutengeneza filamu ya muda mrefu zaidi iliyoshiba?
Wakati namshirikisha jamaa yangu mmoja kuhusu mapungufu niliyoyaona kwenye filamu ya Tanzania The Royal Tour,aliniambia kitu kilichonifumbua macho zaidi. Kuna filamu nyingine za Royal Tour zilizoandaliwa na producer Peter Greenberg za mataifa ya Ecuador, Israel, Poland, Mexico na taifa moja lililonipa mshangao nilipoliona, Rwanda. Jamaa yangu hakutaka nikosoe filamu yetu akiamini walioandaa ni wataalam waliobobea. Lakini jicho langu liliguswa zaidi kuiona Rwanda kwenye hoja yake. Rwanda ametangaza nchi yake kwenye mfululizo wa filamu za The Royal Tour miaka minne kabla yetu,Rwanda ana nini cha kutangaza hata apate wazo miaka minne kabla yetu?
Filamu ya The Royal Tour ya Rwanda imetuumia dakika 56 kuonesha vivutio vyao vyote.Je dakika 56 hizo hizo zinatosha kuonesha vivutio vilivyopo Tanzania ambayo ukubwa wake kwa mujibu wa Peter Greenberg ni sawa na nchi za Ufaransa na Ujeruman zikiungana huku vivutio vyake vikitapakaa kila kona ya nchi?
Ikiwa utengenezaji wa Filamu hii unategemewa kuleta tija kwenye sekta ya utalii nchini, ni vizuri tukaangalia namna ya kutangaza utalii wetu katika kona tofauti tofauti. Hapa ndio akili yangu inaiwaza tena Rwanda ambayo haina lolote la maana katika utalii lakini imefanya The Royal Tour kabla yetu.
Rwanda sio tu kwamba amefanya filamu hiyo bali pia ni mdhamini wa jezi za vilabu vya mpira vya PSG ya Ufaransa na Arsenal ya Uingereza. Katika udhamini huo wachezaji wa timu hizo watavaa jezi zao zikiwa na maandishi “VISIT RWANDA”. Katika hili kama taifa tuna jambo lingine la kujifunza na kuiga kutoka Rwanda.
Filamu ya Tanzania The Royal Tour ina tija bila shaka lakini filamu ile sio ya Hollywood na soko kubwa la filamu lipo Hollywood. Filamu za Hollywood ndio zina watazamaji wengi zaidi duniani. Wito wangu ni kutangaza zaidi vivutio vya utalii kwa kutumia filamu za Hollywood. Kwenye filamu ya Lara Croft Tomb Rider, mwanadada Angelina Jolie akiwa katika jukumu la kutafuta sanduku la Pandora anajikuta akiwa na wajibu wa kufika kwenye mlima Kilimanjaro,lakini kwenye sinema hiyo mlima Kilimanjaro haupo Tanzania na Angelina jolie anafika Kilimanjaro kupitia Kenya kwa msaada wa wazee wa Kikuyu.
Tanzania tuna kiwanda chetu cha filamu na filamu zetu zinaweza kutumika kutangaza utalii wetu .Ikiwa ubora wa filamu zetu kwenye soko la kimataifa ni jambo linalotia mashaka, ushirikishwaji wa makampuni ya kimataifa kutengeneza filamu zenye mazingira ya kitanzania zenye maudhui ya kutangaza utalii ni jambo linalopaswa kuangaliwa vizuri. Media For Development International wametengeneza filamu na tamthiliya za Kitanzania zenye viwango vya kimataifa zinazobeba jumbe mbalimbali ikiwemo magonjwa ya malaria na ukimwi,tohara kwa wanaume, rushwa na kilimo. Kona hiyo pia inaweza kutumika kutengeneza filamu za kwetu zenye viwango vya kimataifa zenye maudhui ya kutangaza utalii wetu na kuuza filamu hizo kwenye masoko ya kimataifa.
Ikiwa ni dhahiri kwamba serikali ya awamu ya sita imedhamiria kuweka nguvu za kutosha kwenye kukuza utalii wetu. Mafanikio ya filamu hii yawe chachu ya kutufunza kuwekeza nguvu zaidi kwenye mambo mengine yanayogusa uchumi wetu. Mwalimu Nyerere kwenye kitabu chake cha Ujamaa na Kujitegemea aliweka msisitizo kwa Watanzania kuingia kwenye vita vya kiuchumi tukiwa na silaha pekee tunayoifahamu vizuri,Kilimo.