Tanzania: Maridhiano ya Kijamii - Reconciliation and Social Justice

dudus

JF-Expert Member
Feb 28, 2011
22,121
49,368
Mh. Rais, Ikulu – Dar es Salaam;
Salaam.

Mh. Rais wetu, naomba nisipoteze muda mwingi badala yake niende moja kwa moja kwenye hoja. Katika kupitiapitia vyanzo mbalimbali nimekutana na mada fulani hapa:

Reconciliation and social justice | Public Eye Daily

ambayo ukiunganisha na HOTUBA YAKO YA UKWELI kwenye kilele cha Eid El Fitr hivi majuzi na ukipanua wigo kidogo wa kilichomo kwenye mada husika hapo juu na kukiwa na utashi wa kweli wa kisiasa tunaweza kuliponya taifa letu.

Mh. Rais, ulionya kabisa kwenye hotuba yako kwamba tuache ubinafsi na ushabiki hasa wa kidini kwenye mjadala tarajiwa wa KATIBA MPYA. Mh; UDINI ni tone tu kati ya hatari nyingi zinazoelekea kuikabili nchi yetu siku za usoni – yako mengi.

Nina wazo, hata kama ni la kipumbavu, tafadhali nisikilize kwani ndani ya upumbavu mwingi mwanadamu pia hujifunza. Wazo langu ni hili:

WATANZANIA TUMEJERUHIWA; KINAFSI, KISAIKOLOJIA, na hata KIMWILI. Nani kamjeruhi nani na lini, na tumefikaje hapa, hakika mie SIJUI; ila majeraha yapo. Kwa mujibu wa mtando huo hapo juu, kuna kitu kinaitwa "RECONCILIATION AND SOCIAL JUSTICE" au kwa tafsiri ya ki-maamuma "HAKI NA MARIDHIANO YA KIJAMII" - HAMAKI.

Mh; ikikupendeza, unaonaje kikaundwa chombo fulani cha kujaribu katafuta ufumbuzi wa mitafaruku hii inayoelekea kuinyemelea jamii yetu; tukapatana kisha tukasonga mbele. Naamini baada ya mapatano hata mchakato ujao wa Katiba Mpya utaenda vizuri pasi na mmoja kumshuku mwingine kama ambavyo hata wewe mwenyewe umeanza kutahadharisha. Chombo hiki kijitenge kabisa na itikadi ya aina yoyote ikiwezekana hata wajumbe si lazima wote wawe watanzania. Matokeo na ripoti viwe wazi na huru – aliyekosea aombe msamaha na anayeombwa msamaha sharti asamehe. Baada ya hapo tuingie kwenye mchakato wa Katiba Mpya tukiwa wamoja na wenye furaha na amani.

Chombo hicho kinaweza kuangalia angalau maeneo yafuatayo; wajumbe wengine kwenye jamvi hili (JF) wataongeza mengine; au ukipenda waweza kuita HADIDU ZA REJEA.

(i) SIASA: Je, ni kweli siasa yetu tangu uhuru kwa namna moja au nyingine imeleta majeraha katika jamii yetu na kwa kiwango gani? Rejea, Operesheni vijiji, wahujumu uchumi, utaifishaji wa majumba, mahospitali, shule, n.k. Ubinafsishaji; je watu wamejeruhiwa kiasi gani na kwa njia mbalimbali kama kuongezeka kwa ufukara, n.k.? Je, Muungano wetu?

(ii) MFUMO WA VYAMA VINGI: Je, kuna majeraha yoyote yaliyoletwa na mfumo huu? Rejea kejeli kama CCM itatawala milele, leteni wapinzani tuwachinje, n.k. Tume ya Uchaguzi, n.k. Na hata makundi hasimu ndani na nje ya vyama vya siasa.

(iii) UFISADI: Je, ufisadi una sehemu gani katika mitafuruku ya kijamii iliyopo sasa – umeongeza ufukara au vinginevyo?

(iv) RASILIMALI ZA TAIFA: Wakati mwingine rasilimali za taifa zaweza kuwa laana badala ya neema. Je, kwa taifa letu, mchango wake ni upi katika mitafaruku ya kijamii?

(v) JINSIA: Je, yawezekana jinsia za watanzania zikawa na michango katika mitafaruku ya kijamii na kwa kiwango gani? Kosa la nani? Ni mfumo au ilipangwa makusudi?

(vi) UKABILA: Ukabila unao sehemu yoyote ya mitafaruku ya kijamii? Ni kweli ukabila upo? Kwa kiwango gani? Umetokea by chance au ilipangwa?

(vii) UDINI: Ni kweli udini upo? Kama ndio, kwa bahati mbaya; kihistoria; au ilipangwa?

(viii) n.k. n.k. n.k.

Baada ya matokeo, hatua stahiki zichukuliwe pale inapowezekana/takiwa, tuombane msamaha, tuingie kwenye mchakato wa Katiba Mpya, halafu Uchaguzi Mkuu - 2015, kisha tusonge mbele. Naamini hata MAADILI yetu yatabadilika. Huko ndio KUTHUBUTU, KUJARIBU, na KUSONGA MBELE.

Asante na samahani kwa kukupotezea muda wako adhimu kwa utumishi wa Taifa letu.
 
Mawazo mazuri. Yafunge kwenye bahasha yapeleke kwa Rais pale jumba jeupe. Andika kwa jina lake na si cheo itamfikia.
 
Back
Top Bottom