Tanzania ilianza vibaya inaelekea pabaya

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,315
33,109
Tanzania ilianza vibaya ndiyo maana inaelekea pabaya. Kuanzia wakoloni na Nyerere waliotutawala, Wote waliifanya Tanzania kuanza vibaya. Lazima tuanze upya vizuri, ili tuelekee pazuri. Watanzania tumechoshwa na sera za kwenye vitabu, lakini kwenye maisha yetu hazitekelezeki. Tumepotezewa muda mrefu ambao tungeutumia vizuri leo hii hali yetu kimaisha ingekuwa tofauti na ilivyo sasa.

Lakini yote hayajapotea kwani tuna muda wa kuanza upya. Hatutakuwa na muda wa kupoteza kwani tayari tumepitwa na wakati. Tutaanzia tutakapoikuta nchi yetu na tuendelee mbele. Muhimu hatutarudia makosa ya zamani. Tutarekebisha yanayoweza kurekebishwa haraka ili angalau tupumue hewa yenye mabadiliko.

Tutaanza na kodi. Wananchi watapunguziwa mzigo wa kodi, na tutabadili mfumo wa kuikusanya. Tofauti na ilivyo sasa kodi kidogo sana itatozwa katika bidhaa muhimu, na nyingine hazitatozwa kodi kabisa. Badala ya kuwafanya wananchi wa kawaida masikini kwa kuwatoza kodi nyingi, tutaruhusu watu watoe michango ya hiari kusaidia taasisi za umma. Serikali na wananchi pamoja tutalijenga taifa letu kwa moyo wa kizalendo.

Kupigana na RUSHWA tutaimarisha taasisi za sheria nchini kwa kuinua kiwango cha mishahara kwa watumishi katika taasisi zote za kisheria. Polisi hali yao ya maisha itainuliwa na nyumba wanazoishi kufanyiwa ukarabati na mpya kujengwa haraka kukithi mahitaji yao ya nyumba. Suala la familia mbili au tatu kushiriki chumba kimoja litakuwa historia katika kikosi cha polisi.

Majeshi yetu yatarekebishwa kutoka yale yanayongojea vita mpaka kuwa mahali pa kufikiri na kugundua vitu kwa ajili ya ujenzi wa Taifa. Pia mishahara yao itarekebishwa ili ikithi mahitaji yao ya kila siku. Majaji nao wataongezewa mishahara ili iwe vigumu wao kupokea rushwa na kupindisha ukweli mahakamani. Tunajua hakuna kiasi cha pesa kinachotosha mwanadamu akose vishawishi, lakini kwa kiasi kikubwa tutapunguza rushwa katika taasisi zetu za kisheria.

Mipango yetu itakuwa ya kudumu na hakutakuwepo na oparesheni za kushitukiza ambazo ni sawa na kuhamisha rushwa kutoka taasisi moja kwenda nyingine. Pia wote watahesabiwa ni wananchi wa Tanzania bila kujali walihusika vipi katika serikali ya CCM iliyokuwepo madarakani. Kifupi hatutapoteza muda kwa yaliyopita bali tutakaza mwendo kwa yaliyo mbele yetu.

Tunajua kuna watu wenye majumba makubwa waliyojenga kwa pesa za rushwa walipokuwa madarakani, Lakini serikali yetu haitawabomolea watu hao majumba kwa kisingizio kwamba zilijengwa kwenye sehemu za barabara, Badala yake tutawaonyesha jinsi mtu anavyoweza kuwa tajiri kihalali bila rushwa au kuwathulumu wengine. Kwao hilo litakuwa somo kubwa maishani kujifunza. Kwa hiyo badala ya kuanza kukimbiza pesa zao nje wakidhani serikali yetu itawanyanganya kama walivyonyanganya, Watulize roho.

Pesa ni za watanzania. Wakizitumia Tanzania ni bora zaidi kuliko wakizipeleka nje ya Tanzania. Hapo washike neno langu. Mimi siyo mtu wa kuyatafuna niliyokwisha sema.

Kuhusu ELIMU tayari watanzania mlizoea elimu ya bure ambayo ilizalisha wasomi duni. Serikali yetu itaruhusu ushindani katika sekta ya elimu ili ubora wa elimu udumishwe. Taasisi za kidini na zile za watu binafsi zitaruhusiwa kuendesha mashule lakini kwa utaratibu urtakaowekwa na serikali yetu. Moyo wa kujitolea kutoka kwa wananchi pamoja na serikali, utahakikisha kwamba hakuna mwanafunzi wa Tanzania anayekosa elimu kwa sababu tu wazazi ni masikini hawawezi kulipa gharama za shule. Huo utaitwa moyo wa ENZI MPYA.

MATIBABU nayo yatakuwa sawa na elimu. Lakini kila juhudi zitafanywa kuhakikisha hakuna anayefukuzwa kwenye hospitali kwa kisingizio cha kukosa malpo ya hospitali. Serikali itakuwa bega kwa bega na taasisi za kibinafsi pamoja na zile za kidini. kuwahudumia wananchi wa Tanzania kiafya na kielimu. Mahospitali yaliyoko yataimarishwa na mengine mapya kujengwa. Pia vifaa vya kiafya vitaboreshwa kuyafanya mahospitali yetu yaweze kuwahudumia watu wa aina zote.

Hali ilivyo sasa mahospitali yetu yameachwa kiholela kwani wakubwa hutibiwa hata mafua nje ya nchi. Mamilioni yanayotumika kuwatibu viongozi nje ya nchi yanaweza kabisa kutumika kuyaboresha mahospitali yetu , Na hata kujenga mengine mapya.

Kwa mfano matibabu ya Mheshimiwa Mkapa hivi karibuni, Yameligharimu Taifa mamilioni ya shilingi kama siyo mabilioni. Hawatasema gharama halisi kuogopa aibu, Lakini watafiti wanasema ni kitita cha pesa.

Ajabu ni kwamba aliyofanyiwa huko, yangewezekana kabisa kufanyika nchini pamoja na hali duni za hospitali zetu. Mimi siyo muuguzi, lakini najua upasuaji unahitaji dawa ya kumfanya mtu alale ili kisu kiingie bila mgonjwa kusikia. Je dawa hiyo hapa nchini hakuna? Na kisu je, hata hicho hatuna?

Wengine wanasema Mkapa ni BONGE LA JITU Tena mtumiaji mzuri wa vileo kwa hiyo pengine dawa zetu za kumfanya alale zisingefua dafu. Sawa. Kama tunaweza kumfanya Tembo mzima alale na ahamishwe kutoka Ziwa Manyara hadi Ngorongoro, Je hata hiyo Mkapa angewekewa dozi moja asingelala?

Wengine wanasema hatuna madaktari bingwa wa kuweza kumhudumia RAIS. Mbona basi aliandamana nao huko alikotibiwa? Au walienda kufanya nini? Kuwatizama mabingwa wenzao wa nchi za nje wakimhudumia rais wao? Kuna malalamiko kutoka baadhi ya madaktari bingwa nchini kwamba viongozi wanawapuuza wakati wana elimu sawa na ya wenzao wa nchi za nje.

Wanadai kwamba elimu ya udaktari haina njia fupi kwa daktari wa Amerika na yule wa Tanzania. Wote inabidi wapitie mafunzo mamoja na kuhitimu kumoja. Tatizo ni kwamba wenzetu wana nyenzo za kisasa wakati Tanzania tunatumia nyenzo za kizamani.

Lakini pia wanaliona hilo siyo tatizo kubwa kushindwa kulishughulikia tatizo kama la Mheshimiwa Mkapa nchini. Japo hawakutaka kutajwa, walijigamba kwamba wakati wa ajali ya TRENI Dodoma, walihusika katika kuwahudumia majeruhi waliokuwa katika hali mbaya mara kumi ya Mkapa na wakapona kabisa.

Hawaoni sababu yeyote ya Rais kutumia pesa za walipa kodi nyingi kiasi hicho kufanyiwa kile ambacho wenyewe wangeweza kukifanyia hapa nchini kwa gharama ndogo. Kuongezea uzito hoja yao wanasema, mbali na vyombo vya kisasa, dawa za kutuliza maumivu ni zile zile walizo nazo hapa nchini. Hata zile za kuzuia INFECTION nazo hazina tofauti na zile walizo nazo Tanzania.

Tofauti ni kwamba kwa sababu Mkapa ameziacha dawa hizo Tanzania, Amekwenda kulipa mamilioni kununua kile ambacho angeweza kukipata kiurahisi Tanzania.

Mwisho walimalizia kwa kusema kwamba haijalishi ni dawa gani utakazotumia. Kama nguvu ya mwili kupambana na madadhi imekufa, madaktari wanaweza kufanya sufuri kumfanya mgojwa apone.

Walisisitiza kwamba dawa husaidiana na mwili kupambana na maradhi. Walidokeza kwamba watu wengi wanakufa kwa magojwa yanayotibika kwa sababu uwezo wa kupambana na maradhi mwilini umekufa. Walitumia lugha ya kitaalamu na kusema Upungufu wa Kinga Mwilini {UKIMWI} unawamaliza wengi japo dawa na mashine za kisasa wanazo.

Walionya kwamba viongozi wetu wanatakiwa waige mfano wa Rais wa Kwanza Kenya Mzee Jomo Kenyatta ambaye asliwaamini madaktari wa nchi yake na hakwenda ngambo kutibiwa. Alikufa usingizini Mombasa alipokuwa amekwenda kusheherekea sikukuu ya Krismasi na mwaka mpya. Alikufa kishujaa nchini mwake chini ya uangalizai wa madaktari wazalendo wa Kenya.

Tanzania inawadhalilisha madaktari wake na kuonekana duni mbele ya wenzao wa ULAYA, lakini bado viongozi wetu wanakufa wakiwa mikononi mwa mabingwa hao. Walitoa mfano wa Nyerere kama kiongozi wa Tanzania aliyewahikufa mikononi mwa madaktari bingwa wa nchi za nje. Wanadai kwamba hata kama wanatoa mawazo wakati mgonjwa yuko nje ya nchi, Mawazo yao hayasikilizwa, jambo linaloleta lawama baadaye kwamba kama wangesikilizwa pengine Nyerere angekuwa hai leo.

Mambo hayatakuwa hivyo katika serikali ya ENZI MPYA. Tutaheshimu madakrari wetu, na watapewa kila motisha kuyaokoa maisha ya watanzania na viongozi wake wa ngazi zote. Hakuna sababu ya kutumia pesa za walipa kodi kuwaelimisha madaktari ambao kazi zao hazithaminiwi na viongozi.

Ndio maana wengi wa madaktari kutoka Tanzania wamehamia huko wanakokimbilia viongozi kwa matibabu. Inaelekea siku moja watakutana nao huko kama madaktari bingwa kumbe ni wale wale kutoka Tanzania na elimu ile ile waliyoidharau viongozi wetu.

Kuna wengine wanaohoji kwamba viongozi ni watu muhimu katika taifa na ni lazima kila hatua zichukuliwe kuchunguza afya zao. Hatuipingi hoja hiyo, ila tunasema yote hayo yafanyike Tanzania..

Wanataaluma hiyo wapo. Kwa nini viongozi waharibu pesa tunazozihitaji zaidi kwa yale yanayowezekana hapa? Kama ni ajali na iwe kiongozi kapoteza sehemu ya ubongo, halafu wajaribu kurudisha waliouokoteza chini zoezi hilo liwashinde, Hapo itaeleweka watakapotumia ndege yeyote hata kama ni ya jeshi kumkimbiza kiongozi husika kunakoweza kupatikana msaada wa haraka.

Lakini suala la Mkapa ni tofauti kabisa. Hata kama angehitaji vipimo vya mifupa vifanyiwe nje ya nchi, ilikuwa rahisi.Upasuaji ungefanyiwa Tanzania, na sehemu ya mfupa ipelekwe nje ya nchi kwa ucvhunguzi zaidi na majibu yangekuja mapema. Bado Rais angekuwa Nyumbani, angekunywa uji wa mbege kusaidia kujenga mifupa, na watu wangemuona kirahisi MUHIMBILI au IKULU kumtakia dua apone haraka.

Yale aliyokataa kuyafanya ndiyo anayoyafanya sasa. Bado inasemekana hajapona kabisa, na dawa bado anatumia tena kwa wingi. Nitashangaa zaidi nikisikia kwamba bado dawa anaagiza ngambo wakati zipo hapa TZ.

Imeandikwa na Mchungaji Munishi
 
Back
Top Bottom