MrFroasty
JF-Expert Member
- Jun 23, 2009
- 1,195
- 590
Joseph Mihangwa
MIAKA 46 tangu meli ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ing'oe nanga, Aprili 26, 1964 hadi sasa; bado inaendelea kuyumba kwa kusukwasukwa na mawimbi makali na kusababisha adha kubwa, kizunguzungu na kichefuchefu kwa wasafiri.
Na ingawa meli hii ilianza vyema safari yake, kwa kuzingatia dira thabiti, na kwa manahodha wake kusoma vyema ramani, yaelekea sasa imepoteza dira na kusuasua kuelekea kwenye ukungu wa hatari na wa kutisha.
Kama kuna mtu wa kulaumiwa kwa hilo, basi, manahodha wa meli hiyo hawawezi kukwepa lawana kwa kubeza dira na ramani. Na kama wahenga walivyosema: "Kwa nahodha asiyejua bandari aendayo, hakuna upepo ulio muafaka kwake". Hiyo ndiyo hali tuliyomo Watanzania kwa sasa ya kutojua hatima ya Muungano wetu.
Na kwa sababu tumeibeza ramani ya Muungano, mambo mengi yanakwenda kinyume kwa kishindo kikubwa. Baadhi ya hayo ambayo hapo kale yalionekana kama dhambi kwa Muungano, sasa yanaonekana na kukubalika kuwa si dhambi tena kutokana na uelewa wa abiria, baada ya kufichwa ukweli kwa muda mrefu.
Kwa mfano, hapo kale nani angekubali au kuamini kwamba Zanzibar inaweza kuwa na wimbo wake wa Taifa, ngao ya Taifa, bendera ya Taifa na Jeshi la Taifa?
Hapo kale, nani angeamini au kukubali kwamba Wazanzibari wanaweza kuhoji muundo wa Muungano bila kutiwa kizuizini; au Rais wa Zanzibar kukataa kauli za Chama tawala (CCM) kwa mambo yanayogusa Katiba ya Zanzibar kama vile suala la serikali ya mseto, kama alivyofanya hivi karibuni, Rais Abeid Amani Karume, kwa kubeza mapendekezo ya Tume ya Halmashauri Kuu ya CCM, ikiongozwa na Katibu Mkuu wake, Yusuf Makamba, na msimamo wa Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM, iliyoketi kijijini Butiama mwaka jana?
Kama hapo kale Rais wa Serikali ya awamu ya pili Visiwani, Mzee Aboud Jumbe Mwinyi, alivuliwa wadhifa huo na nyadhifa zote za Chama kwa kutumia haki yake ya kikatiba kuhoji muundo wa Muungano akidai kwamba unapashwa kuwa Shirikisho, iweje leo Rais wa sasa, Amani Abeid Karume na Wazanzibari kwa ujumla, wakiwamo kina Seif Sharif Hamad, wanaweza kufanya hivyo bila ya kuadabishwa wakati Katiba ya Muungano ni ile ile iliyomng'oa Jumbe?
Hapo kale nani angefikiria inawezekana kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano kuteua wapinzani (kutoka CUF), kuingia katika Bunge la Muungano; na kwa Rais wa Zanzibar vivyo hivyo?
Kama ambavyo hapo kale, Wakatoliki Walei (waumini wa kawaida), walikatazwa kumiliki au kusoma Biblia (neno la Mungu), kwa madai kwamba hawakuwa na uwezo na akili ya kutafsiri maandiko hayo kwa usahihi, na kwa hofu ya kuipotosha; ndivyo ilivyo kwamba, tangu kale, Watanzania walinyimwa fursa ya kuuona Mkataba, na hata Sheria ya Muungano ili kujua nini hasa kinasemwa au kinatakiwa kufuatwa chini ya Mkataba huo.
Matokeo yake, tafsiri ya Muungano na kwa yale yanayotakiwa na Muungano huo, wameachiwa wanasiasa kutafsiri wanavyotaka kwa manufaa yao binafsi kama tabaka la watawala, kama tutakavyoona katika makala haya.
Nayo Mahakama Maalumu ya Katiba, inayoanzishwa kwa mujibu wa ibara ya 125 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano, ambayo kazi yake pekee ni "kusikiliza shauri lililotolewa mbele yake, na kutoa uamuzi wa usuluhishi juu ya suala lolote kuhusu tafsiri au utekelezaji wake (iwapo) unabishaniwa kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Zanzibar", haijaanzishwa mpaka sasa, lakini si kwa sababu hakuna mashauri kuhusu kero za Muungano; bali ni kutokana na hofu kwamba, kama Mahakama hiyo itaachwa kufanya kazi ipasavyo, itaweza kutoa tafsiri sahihi juu ya muundo na mfumo sahihi wa Muungano na kuwaumbua wanasiasa.
Rais Jumbe alitaka kutumia ibara hiyo hiyo ya Katiba kuhoji Muungano, lakini akatunguliwa kwa kishindo kikubwa; na hakuna mwingine aliyethubutu kufanya hivyo baadaye. Ilikuwa dhambi hapo kale, lakini si dhambi leo, chini ya Mkataba wa Muungano huo huo!
Lazima kuna mtu au watu waliojiona yeye au wao ndio Muungano, na Muungano ndiye yeye au wao, lakini mambo sasa hayawezi kuwa hivyo tena kutokana na uelewa wa umma juu ya kinachotakiwa chini ya Muungano.
Mara nyingi njia ya mwongo ni fupi. Watanzania na Wazanzibari katika ujumla wao wanazidi na wataendelea kuhoji tafsiri sahihi ya Muungano wao, hata kama watawala wataendelea kuuficha Mkataba wa Muungano huo katika zama hizi za uelewa, demokrasia na haki za binadamu; hasa wanapoona mambo kadha wa kadha ambayo hayakutarajiwa, yakitendeka kwa mshangao wa wengi, kama nilivyoeleza hapo mwanzo.
Katika makala haya, tutaangalia baadhi ya mambo yaliyopotoshwa na wanasiasa na kuyumbisha Muungano. Niharakishe kutamka hapa kwamba, kero za Muungano si za kisiasa; bali ni za kikatiba.
Kwa hiyo, ni kosa kubwa kujaribu kutatua mgogoro wa kikatiba kwa njia za kisiasa kama zinavyofanya tume lukuki za CCM juu ya kero za Muungano. Kwa njia hiyo hakuna kitakachoweza kutatuliwa!
Wengi tunaamini kwa makosa kwamba Tanganyika na Zanzibar zilipoungana, Aprili 26, 1964, ziliunda Muungano wa nchi inayoitwa Tanzania. Ukweli ni kwamba, Muungano huo unajulikana kama "Muungano wa Tanganyika na Zanzibar", na sio Tanzania.
Hili ndilo jina la Muungano linaloonekana katika Mkataba (Hati) wa Muungano huo wa Kimataifa wa Aprili 22, 1964; na Sheria ya Muungano Namba 22 ya 1964 ya kuridhia Muungano kwa mabunge ya nchi hizo mbili. Je, jina "Tanzania" linatoka wapi?
Miezi mitatu baada ya Tanganyika na Zanzibar kuungana, lilitangazwa shindano la kubuni jina lenye kuwakilisha hadhi ya Muungano na zawadi ya pauni 10 za Uingereza kwa mshindi. Maombi yalipokelewa kutoka ndani na nje ya nchi, zikiwamo Urusi, Uingereza, Sweden, China, Ufaransa, Poland, Italia na Australia, ambapo jumla ya majina 1,534 yalipokelewa na kushindanishwa.
Kati ya majina manne yaliyochuana hadi mwisho, ni pamoja na "Tanzania", Tanzan, Tangibar na Zantan.
Akitangaza jina jipya Ikulu, mbele ya waandishi wa habari na namna ya kulitamka, Oktoba 29, 1964, Rais Julius Kambarage Nyerere alisema jina hilo lilipitishwa na Baraza la Mawaziri Oktoba 28, 1964, na litamkwe "Tan-zan-ia", sio "Tanzania".
Ni kusema kwamba, hadi Oktoba 28, 1964 hapakuwa na nchi iliyoitwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; bali kulikuwa na Jamhuri ya "Tanganyika na Zanzibar" kwa mujibu wa Mkataba wa Muungano. Wala hadi sasa hakuna nchi au sehemu ya Tanzania iliyosajiliwa kuitwa "Tanzania Bara" au "Tanzania Visiwani" kikatiba, bali kuna Tanzania na Zanzibar tu. Tutaona baadaye chimbuko la ubatili huu.
Wakati nchi mbili hizi zikiungana, hapakuwa na Katiba kwa ajili ya Jamhuri ya Muungano huo iliyoandaliwa. Kwa hiyo, ilikubaliwa chini ya Mkataba wa Muungano kwamba, Katiba ya Jamhuri ya Tanganyika (Tanganyika haikuuawa na Muungano) itumike pia kama Katiba ya mpito ya Muungano, kwa kufanyiwa marekebisho madogo kuingiza mambo yote 11 ya Muungano (Angalia Sheria ya Muungano ya 1964, kifungu cha 5).
Na kwa nini tunasema Tanganyika haikufa kufuatia Muungano? Katiba ilikuwa wazi kwa hilo, kwamba kwa mujibu wa kifungu cha 8, Sheria ya Muungano; na ibara ya 5, Mkataba (Hati) wa Muungano, "Kuanzia siku na baada ya siku ya Muungano, sheria za Tanganyika na zile za Zanzibar zitaendelea kuwa Sheria za Tanganyika na za Zanzibar kuwa za Zanzibar"; kila nchi kwa kadri ya mamlaka yake yasiyo ya Muungano.
Maana yake ni kwamba, Sheria za Tanganyika na zile za Zanzibar kwa mambo yasiyo ya Muungano, ziliendelea kuwa na nguvu katika nchi hizo; pia kwamba, Tanganyika na Zanzibar hazikuuawa na Muungano, bali zilibaki kama nchi ndani ya Serikali ya Muungano.
Chini ya ibara ya 8 ya Mkataba wa Muungano, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, kwa makubaliano na Rais wa Zanzibar, alitakiwa kuteua Tume ya Kupendekeza Katiba ya Jamhuri ya Muungano, na hatimaye kuitisha "Bunge la Katiba", likijumuisha wawakilishi kutoka Tanganyika (sio Tanzania wala Tanzania Bara) na kutoka Zanzibar, ndani ya mwaka mmoja kuanzia siku ya Muungano.
Shughuli ya Bunge la Katiba ikiwa ni kujadili na kupitisha Katiba ya Jamhuri ya Muungano; jambo ambalo halikufanyika hadi mwaka 1977 ilipoteuliwa Tume ya kupendekeza kuunganishwa kwa TANU na ASP kuunda CCM ambapo tume hiyo, baada ya kukamilisha kazi hiyo, ilijigeuza kwa makosa kuwa Tume ya Kupendekeza Katiba ya Jamhuri ya Muungano.
Kwa hilo, ninasema kwa kujiamini kabisa kwamba tume hiyo ilikuwa batili, kwa sababu uteuzi wake haukuzingatia matakwa ya Mkataba wa Muungano; licha ya kwamba muda wa mwaka mmoja wa Tume kama hiyo kuteuliwa chini ya Mkataba wa Muungano ulikuwa umepita.
Wala Bunge halikuwa na mamlaka kutunga Sheria (Machi 24, 1965) Namba 18 ya 1965 kuongeza muda wa kuteuliwa kwa Tume na kuitishwa kwa Bunge la Katiba kwa maelezo kwamba "hadi hapo itakapoonekana inafaa na vyema kufanya hivyo".
Hilo ndilo liliokuwa kosa hatari la kwanza na ukiukaji wa Mkataba wa Muungano uliofungua mlango kwa ukiukaji mwingine wa Mkataba kwa miaka iliyofuata.
Kuongezwa kwa muda wa kuitisha Bunge la Katiba kulimaanisha kuchelewa kupatikana kwa Katiba halali ya Jamhuri ya Muungano; na kwa sababu hiyo, Muungano uliendeshwa kwa vitimbwi na udikteta wa wanasiasa kadri walivyoona inafaa, na kwa njia ya amri (decrees) za Rais.
Hapo ndipo kuyumba kwa meli ya Muungano kulipoanzia, na kwa manahodha kulewa madaraka wakidai Muungano hauhojiki; na kwamba kufanya hivyo ilikuwa sawa na uhaini.
Kutoteuliwa kwa Tume, na kutoitishwa kwa Bunge la Katiba kwa mujibu wa Mkataba na Sheria ya Muungano, kulitokana na mifarakano ya dhahiri kati ya manahodha wawili wa meli ya Muungano - Mwalimu Nyerere na Abeid Amani Karume, baada ya kugunduana kwamba wasingeweza kupikwa chungu kimoja wakaiva.
Kuna wakati Karume alitamka wazi kwamba alikuwa amedanganywa juu ya Muundo wa Muungano; na katika hali ya kukata tamaa, alidai kuwa Muungano huo si kitu, akaufananisha na koti ambalo mtu likimbana aweza kulivua wakati wowote.
Kauli hii imerudiwa na Katibu Mkuu wa CUF, Seif Sharif Hamad hivi karibuni alipokuwa akiwahutubia wananchi katika viwanja vya Kibanda Maiti, Zanzibar, Desemba 2009.
Ni kauli ambayo pia mwanasiasa mwingine wa CUF, Juma Haji Duni, imempa sifa ya kuteuliwa kuwa Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi hivi karibuni: Kwa nini? Ni kwa sababu Wazanzibari wameanza kufuta tofauti zao za kiitikadi na kuungana kuonyesha kukerwa kwao na kero za Muungano, wakielewa au kuelimishana kuhusu ukweli juu ya kinachotakiwa kufanyika chini ya Mkataba halisi wa Muungano.
Kama hivyo ndivyo, nasi hatuna budi kusoma alama za nyakati kwa makini ili kuusalimisha Muungano wetu.
Julai 10, 1965, Bunge lilipitisha Katiba ya Muda (Sheria Na 43 ya 1965) ya Tanzania iliyotambua kwa mara ya kwanza kuwa, "Tanzania ni Jamhuri ya Muungano" (ibara ya 1) inayoundwa na Tanganyika na Zanzibar (ibara ya 2), na kwamba kutakuwa na chama kimoja cha Siasa Tanzania (ibara ya 3); "lakini, hadi hapo TANU na ASP vitakapoungana, Chama cha Siasa kwa Tanganyika kitaendelea kuwa TANU, na kwa Zanzibar kitakuwa ASP".
Katiba hii, kama tunavyosoma, bado iliendelea kutambua kuwapo kwa Tanganyika na Zanzibar kama nchi mbili wabia wa Muungano.
Hata hivyo, Katiba hii ilivuka mipaka kwa kuingiza mambo ya vyama vya siasa ambayo hayakuwa moja au sehemu ya mambo ya Muungano katika Mkataba wa Muungano. Na kuanzia hapo, siasa ilichukua kiti cha mbele badala ya Katiba katika kuongoza Muungano; na kwamba, badala ya kero za Muungano kutatuliwa kwa mujibu wa Katiba, suluhisho lilitafutwa au kufanyika kwa hisia za kisiasa chini ya dhana ya "Chama kushika hatamu" za uongozi.
Ni maoni yangu kwamba, hatua ya kuingiza mamlaka ya vyama vya siasa katika Muungano ilikuwa ya ukiukaji wa Mkataba wa Muungano na Sheria ya Muungano, kwa sababu vyama vya siasa halikuwa jambo au suala la Muungano tangu mwanzo.
Ikumbukwe pia kwamba wakati wakitia sahihi Mkataba wa Muungano na Miswada ya Sheria za Muungano, waasisi wa Muungano, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Tanganyika) na Rais Abeid Amani Karume (Zanzibar), walifanya hivyo kama marais wa Tanganyika na Zanzibar huru, na si kwa niaba ya vyama vyao vya siasa, TANU na ASP.
Wasingeweza kutia sahihi Mkataba wa Muungano kwa niaba ya vyama vya siasa kwa sababu hawakuwa na mamlaka (mandate) hayo, isipokuwa kama marais pekee wa nchi zao.
…Itaendelea wiki ijayo.
MIAKA 46 tangu meli ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ing'oe nanga, Aprili 26, 1964 hadi sasa; bado inaendelea kuyumba kwa kusukwasukwa na mawimbi makali na kusababisha adha kubwa, kizunguzungu na kichefuchefu kwa wasafiri.
Na ingawa meli hii ilianza vyema safari yake, kwa kuzingatia dira thabiti, na kwa manahodha wake kusoma vyema ramani, yaelekea sasa imepoteza dira na kusuasua kuelekea kwenye ukungu wa hatari na wa kutisha.
Kama kuna mtu wa kulaumiwa kwa hilo, basi, manahodha wa meli hiyo hawawezi kukwepa lawana kwa kubeza dira na ramani. Na kama wahenga walivyosema: "Kwa nahodha asiyejua bandari aendayo, hakuna upepo ulio muafaka kwake". Hiyo ndiyo hali tuliyomo Watanzania kwa sasa ya kutojua hatima ya Muungano wetu.
Na kwa sababu tumeibeza ramani ya Muungano, mambo mengi yanakwenda kinyume kwa kishindo kikubwa. Baadhi ya hayo ambayo hapo kale yalionekana kama dhambi kwa Muungano, sasa yanaonekana na kukubalika kuwa si dhambi tena kutokana na uelewa wa abiria, baada ya kufichwa ukweli kwa muda mrefu.
Kwa mfano, hapo kale nani angekubali au kuamini kwamba Zanzibar inaweza kuwa na wimbo wake wa Taifa, ngao ya Taifa, bendera ya Taifa na Jeshi la Taifa?
Hapo kale, nani angeamini au kukubali kwamba Wazanzibari wanaweza kuhoji muundo wa Muungano bila kutiwa kizuizini; au Rais wa Zanzibar kukataa kauli za Chama tawala (CCM) kwa mambo yanayogusa Katiba ya Zanzibar kama vile suala la serikali ya mseto, kama alivyofanya hivi karibuni, Rais Abeid Amani Karume, kwa kubeza mapendekezo ya Tume ya Halmashauri Kuu ya CCM, ikiongozwa na Katibu Mkuu wake, Yusuf Makamba, na msimamo wa Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM, iliyoketi kijijini Butiama mwaka jana?
Kama hapo kale Rais wa Serikali ya awamu ya pili Visiwani, Mzee Aboud Jumbe Mwinyi, alivuliwa wadhifa huo na nyadhifa zote za Chama kwa kutumia haki yake ya kikatiba kuhoji muundo wa Muungano akidai kwamba unapashwa kuwa Shirikisho, iweje leo Rais wa sasa, Amani Abeid Karume na Wazanzibari kwa ujumla, wakiwamo kina Seif Sharif Hamad, wanaweza kufanya hivyo bila ya kuadabishwa wakati Katiba ya Muungano ni ile ile iliyomng'oa Jumbe?
Hapo kale nani angefikiria inawezekana kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano kuteua wapinzani (kutoka CUF), kuingia katika Bunge la Muungano; na kwa Rais wa Zanzibar vivyo hivyo?
Kama ambavyo hapo kale, Wakatoliki Walei (waumini wa kawaida), walikatazwa kumiliki au kusoma Biblia (neno la Mungu), kwa madai kwamba hawakuwa na uwezo na akili ya kutafsiri maandiko hayo kwa usahihi, na kwa hofu ya kuipotosha; ndivyo ilivyo kwamba, tangu kale, Watanzania walinyimwa fursa ya kuuona Mkataba, na hata Sheria ya Muungano ili kujua nini hasa kinasemwa au kinatakiwa kufuatwa chini ya Mkataba huo.
Matokeo yake, tafsiri ya Muungano na kwa yale yanayotakiwa na Muungano huo, wameachiwa wanasiasa kutafsiri wanavyotaka kwa manufaa yao binafsi kama tabaka la watawala, kama tutakavyoona katika makala haya.
Nayo Mahakama Maalumu ya Katiba, inayoanzishwa kwa mujibu wa ibara ya 125 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano, ambayo kazi yake pekee ni "kusikiliza shauri lililotolewa mbele yake, na kutoa uamuzi wa usuluhishi juu ya suala lolote kuhusu tafsiri au utekelezaji wake (iwapo) unabishaniwa kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Zanzibar", haijaanzishwa mpaka sasa, lakini si kwa sababu hakuna mashauri kuhusu kero za Muungano; bali ni kutokana na hofu kwamba, kama Mahakama hiyo itaachwa kufanya kazi ipasavyo, itaweza kutoa tafsiri sahihi juu ya muundo na mfumo sahihi wa Muungano na kuwaumbua wanasiasa.
Rais Jumbe alitaka kutumia ibara hiyo hiyo ya Katiba kuhoji Muungano, lakini akatunguliwa kwa kishindo kikubwa; na hakuna mwingine aliyethubutu kufanya hivyo baadaye. Ilikuwa dhambi hapo kale, lakini si dhambi leo, chini ya Mkataba wa Muungano huo huo!
Lazima kuna mtu au watu waliojiona yeye au wao ndio Muungano, na Muungano ndiye yeye au wao, lakini mambo sasa hayawezi kuwa hivyo tena kutokana na uelewa wa umma juu ya kinachotakiwa chini ya Muungano.
Mara nyingi njia ya mwongo ni fupi. Watanzania na Wazanzibari katika ujumla wao wanazidi na wataendelea kuhoji tafsiri sahihi ya Muungano wao, hata kama watawala wataendelea kuuficha Mkataba wa Muungano huo katika zama hizi za uelewa, demokrasia na haki za binadamu; hasa wanapoona mambo kadha wa kadha ambayo hayakutarajiwa, yakitendeka kwa mshangao wa wengi, kama nilivyoeleza hapo mwanzo.
Katika makala haya, tutaangalia baadhi ya mambo yaliyopotoshwa na wanasiasa na kuyumbisha Muungano. Niharakishe kutamka hapa kwamba, kero za Muungano si za kisiasa; bali ni za kikatiba.
Kwa hiyo, ni kosa kubwa kujaribu kutatua mgogoro wa kikatiba kwa njia za kisiasa kama zinavyofanya tume lukuki za CCM juu ya kero za Muungano. Kwa njia hiyo hakuna kitakachoweza kutatuliwa!
Wengi tunaamini kwa makosa kwamba Tanganyika na Zanzibar zilipoungana, Aprili 26, 1964, ziliunda Muungano wa nchi inayoitwa Tanzania. Ukweli ni kwamba, Muungano huo unajulikana kama "Muungano wa Tanganyika na Zanzibar", na sio Tanzania.
Hili ndilo jina la Muungano linaloonekana katika Mkataba (Hati) wa Muungano huo wa Kimataifa wa Aprili 22, 1964; na Sheria ya Muungano Namba 22 ya 1964 ya kuridhia Muungano kwa mabunge ya nchi hizo mbili. Je, jina "Tanzania" linatoka wapi?
Miezi mitatu baada ya Tanganyika na Zanzibar kuungana, lilitangazwa shindano la kubuni jina lenye kuwakilisha hadhi ya Muungano na zawadi ya pauni 10 za Uingereza kwa mshindi. Maombi yalipokelewa kutoka ndani na nje ya nchi, zikiwamo Urusi, Uingereza, Sweden, China, Ufaransa, Poland, Italia na Australia, ambapo jumla ya majina 1,534 yalipokelewa na kushindanishwa.
Kati ya majina manne yaliyochuana hadi mwisho, ni pamoja na "Tanzania", Tanzan, Tangibar na Zantan.
Akitangaza jina jipya Ikulu, mbele ya waandishi wa habari na namna ya kulitamka, Oktoba 29, 1964, Rais Julius Kambarage Nyerere alisema jina hilo lilipitishwa na Baraza la Mawaziri Oktoba 28, 1964, na litamkwe "Tan-zan-ia", sio "Tanzania".
Ni kusema kwamba, hadi Oktoba 28, 1964 hapakuwa na nchi iliyoitwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; bali kulikuwa na Jamhuri ya "Tanganyika na Zanzibar" kwa mujibu wa Mkataba wa Muungano. Wala hadi sasa hakuna nchi au sehemu ya Tanzania iliyosajiliwa kuitwa "Tanzania Bara" au "Tanzania Visiwani" kikatiba, bali kuna Tanzania na Zanzibar tu. Tutaona baadaye chimbuko la ubatili huu.
Wakati nchi mbili hizi zikiungana, hapakuwa na Katiba kwa ajili ya Jamhuri ya Muungano huo iliyoandaliwa. Kwa hiyo, ilikubaliwa chini ya Mkataba wa Muungano kwamba, Katiba ya Jamhuri ya Tanganyika (Tanganyika haikuuawa na Muungano) itumike pia kama Katiba ya mpito ya Muungano, kwa kufanyiwa marekebisho madogo kuingiza mambo yote 11 ya Muungano (Angalia Sheria ya Muungano ya 1964, kifungu cha 5).
Na kwa nini tunasema Tanganyika haikufa kufuatia Muungano? Katiba ilikuwa wazi kwa hilo, kwamba kwa mujibu wa kifungu cha 8, Sheria ya Muungano; na ibara ya 5, Mkataba (Hati) wa Muungano, "Kuanzia siku na baada ya siku ya Muungano, sheria za Tanganyika na zile za Zanzibar zitaendelea kuwa Sheria za Tanganyika na za Zanzibar kuwa za Zanzibar"; kila nchi kwa kadri ya mamlaka yake yasiyo ya Muungano.
Maana yake ni kwamba, Sheria za Tanganyika na zile za Zanzibar kwa mambo yasiyo ya Muungano, ziliendelea kuwa na nguvu katika nchi hizo; pia kwamba, Tanganyika na Zanzibar hazikuuawa na Muungano, bali zilibaki kama nchi ndani ya Serikali ya Muungano.
Chini ya ibara ya 8 ya Mkataba wa Muungano, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, kwa makubaliano na Rais wa Zanzibar, alitakiwa kuteua Tume ya Kupendekeza Katiba ya Jamhuri ya Muungano, na hatimaye kuitisha "Bunge la Katiba", likijumuisha wawakilishi kutoka Tanganyika (sio Tanzania wala Tanzania Bara) na kutoka Zanzibar, ndani ya mwaka mmoja kuanzia siku ya Muungano.
Shughuli ya Bunge la Katiba ikiwa ni kujadili na kupitisha Katiba ya Jamhuri ya Muungano; jambo ambalo halikufanyika hadi mwaka 1977 ilipoteuliwa Tume ya kupendekeza kuunganishwa kwa TANU na ASP kuunda CCM ambapo tume hiyo, baada ya kukamilisha kazi hiyo, ilijigeuza kwa makosa kuwa Tume ya Kupendekeza Katiba ya Jamhuri ya Muungano.
Kwa hilo, ninasema kwa kujiamini kabisa kwamba tume hiyo ilikuwa batili, kwa sababu uteuzi wake haukuzingatia matakwa ya Mkataba wa Muungano; licha ya kwamba muda wa mwaka mmoja wa Tume kama hiyo kuteuliwa chini ya Mkataba wa Muungano ulikuwa umepita.
Wala Bunge halikuwa na mamlaka kutunga Sheria (Machi 24, 1965) Namba 18 ya 1965 kuongeza muda wa kuteuliwa kwa Tume na kuitishwa kwa Bunge la Katiba kwa maelezo kwamba "hadi hapo itakapoonekana inafaa na vyema kufanya hivyo".
Hilo ndilo liliokuwa kosa hatari la kwanza na ukiukaji wa Mkataba wa Muungano uliofungua mlango kwa ukiukaji mwingine wa Mkataba kwa miaka iliyofuata.
Kuongezwa kwa muda wa kuitisha Bunge la Katiba kulimaanisha kuchelewa kupatikana kwa Katiba halali ya Jamhuri ya Muungano; na kwa sababu hiyo, Muungano uliendeshwa kwa vitimbwi na udikteta wa wanasiasa kadri walivyoona inafaa, na kwa njia ya amri (decrees) za Rais.
Hapo ndipo kuyumba kwa meli ya Muungano kulipoanzia, na kwa manahodha kulewa madaraka wakidai Muungano hauhojiki; na kwamba kufanya hivyo ilikuwa sawa na uhaini.
Kutoteuliwa kwa Tume, na kutoitishwa kwa Bunge la Katiba kwa mujibu wa Mkataba na Sheria ya Muungano, kulitokana na mifarakano ya dhahiri kati ya manahodha wawili wa meli ya Muungano - Mwalimu Nyerere na Abeid Amani Karume, baada ya kugunduana kwamba wasingeweza kupikwa chungu kimoja wakaiva.
Kuna wakati Karume alitamka wazi kwamba alikuwa amedanganywa juu ya Muundo wa Muungano; na katika hali ya kukata tamaa, alidai kuwa Muungano huo si kitu, akaufananisha na koti ambalo mtu likimbana aweza kulivua wakati wowote.
Kauli hii imerudiwa na Katibu Mkuu wa CUF, Seif Sharif Hamad hivi karibuni alipokuwa akiwahutubia wananchi katika viwanja vya Kibanda Maiti, Zanzibar, Desemba 2009.
Ni kauli ambayo pia mwanasiasa mwingine wa CUF, Juma Haji Duni, imempa sifa ya kuteuliwa kuwa Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi hivi karibuni: Kwa nini? Ni kwa sababu Wazanzibari wameanza kufuta tofauti zao za kiitikadi na kuungana kuonyesha kukerwa kwao na kero za Muungano, wakielewa au kuelimishana kuhusu ukweli juu ya kinachotakiwa kufanyika chini ya Mkataba halisi wa Muungano.
Kama hivyo ndivyo, nasi hatuna budi kusoma alama za nyakati kwa makini ili kuusalimisha Muungano wetu.
Julai 10, 1965, Bunge lilipitisha Katiba ya Muda (Sheria Na 43 ya 1965) ya Tanzania iliyotambua kwa mara ya kwanza kuwa, "Tanzania ni Jamhuri ya Muungano" (ibara ya 1) inayoundwa na Tanganyika na Zanzibar (ibara ya 2), na kwamba kutakuwa na chama kimoja cha Siasa Tanzania (ibara ya 3); "lakini, hadi hapo TANU na ASP vitakapoungana, Chama cha Siasa kwa Tanganyika kitaendelea kuwa TANU, na kwa Zanzibar kitakuwa ASP".
Katiba hii, kama tunavyosoma, bado iliendelea kutambua kuwapo kwa Tanganyika na Zanzibar kama nchi mbili wabia wa Muungano.
Hata hivyo, Katiba hii ilivuka mipaka kwa kuingiza mambo ya vyama vya siasa ambayo hayakuwa moja au sehemu ya mambo ya Muungano katika Mkataba wa Muungano. Na kuanzia hapo, siasa ilichukua kiti cha mbele badala ya Katiba katika kuongoza Muungano; na kwamba, badala ya kero za Muungano kutatuliwa kwa mujibu wa Katiba, suluhisho lilitafutwa au kufanyika kwa hisia za kisiasa chini ya dhana ya "Chama kushika hatamu" za uongozi.
Ni maoni yangu kwamba, hatua ya kuingiza mamlaka ya vyama vya siasa katika Muungano ilikuwa ya ukiukaji wa Mkataba wa Muungano na Sheria ya Muungano, kwa sababu vyama vya siasa halikuwa jambo au suala la Muungano tangu mwanzo.
Ikumbukwe pia kwamba wakati wakitia sahihi Mkataba wa Muungano na Miswada ya Sheria za Muungano, waasisi wa Muungano, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Tanganyika) na Rais Abeid Amani Karume (Zanzibar), walifanya hivyo kama marais wa Tanganyika na Zanzibar huru, na si kwa niaba ya vyama vyao vya siasa, TANU na ASP.
Wasingeweza kutia sahihi Mkataba wa Muungano kwa niaba ya vyama vya siasa kwa sababu hawakuwa na mamlaka (mandate) hayo, isipokuwa kama marais pekee wa nchi zao.
…Itaendelea wiki ijayo.