Tanga - Usiku Wa Manane

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,460
39,928
(Majina na matukio katika hadithi hii ni yakubuni. Mfanano wowote na watu, mahali au matukio halisi ni wa kinasibu na si kusudio la mwandishi. Haki zote za kunakili na kuchapisha zimehifadhiwa - Kijijini Productions Inc,)
___________________________________________________________
Mimi si mshirikina na mambo ya imani za jadi ziambatanazo na mambo ya kichawi kwangu ni kama hadithi za Hisopo na visa vya sungura na fisi. Katika pitapita yangu hapa yote hapa Bongo hata hivyo, nimekutana na watu wengi ambao wanaapa kwa majina ya wazazi wao na wengine hata wanaapia vifo cha watoto wao kuwa ati wamewahi kuona mambo ya kichawi au kushuhudia maluweluwe ya wataalam wa jadi. Hata nilipoenda masomoni kuanza kidato cha kwanza kule Ufipani watu walinishangaa na kuniasa niombe uhamisho kwani kule Sumbawanga "kwa wachawi ndio wenyewe". Maneno yao hayakunitisha wala kunikatisha tama. Nilienda na bila hofu yoyote ile nilianza na hatimaye kumaliza masomo ya sekondari pale Kaengesa Seminari. Kwa muda wote huo sikupata kujikuta nimechanjwa usiku au nywele zangu zimenyofolewa "kitaalam".

Bila shaka unajiuliza ni kwanini nimekuambia mimi si mshirikina. Nimesema hilo awali kabisa ili ujue kuwa nitakachokusimulia hapa ni ukweli, ukweli mtupu, na sikingine bali ukweli tu na hadi leo hii zaidi ya miaka kumi na tano baadaye sijapata maelezo ya kuniridhisha na yenye kunituliza akili yangu. Nimejaribu kwa kila namna kutafuta maelezo ya kisayansi ambayo yanaweza kuelezea kilichonisibu lakini hadi leo hii sijapata nadharia nzuri ambayo haivuji itakayoweza kuelezea kila kilichonitokea usiku ule ambao bado naukumbuka kama vile jana.

Baada ya kumaliza elimu ya sekondari kule Sumbawanga niliendelea na masomo ya kidato cha tano na sita pale Sangu ambako nilihitimu. Nilijikuta nimekubaliwa kuchukua mafunzo ya Ualimu kule Butimba Mwanza na baada ya miaka mitatu nilipata cheti changu cha ualimu ambacho nilijivunia sana. Tangu nilipokuwa mdogo nilipenda sana kufundisha, hivyo watu walipoanza kuniita "mwalimu Shija" nilijisikia fahari sana na kutiwa moyo. Kituo changu cha kwanza cha kazi kilikuwa ni Tanga, shule ya Msingi Mbuyuni iliyoko ndani ya kambi ya Kikosi cha Kutuliza Ghasia nje kidogo ya mji wa Tanga pembeni kidogo ya barabara iendayo Dar-es-Saalam.

Ulikuwa umepitwa mwezi mmoja tangu nihamie Tanga toka nyumbani Mwanza na baada ya kukaa hotelini kwa wiki moja nilijikuta nimepata chumba cha kupanga eneo la Majani Mapana karibu na Uwanja wa ndege. Umbali toka nyumbani hadi shule ni kama kilometa tano hivi na usafiri wangu hapo mwanzoni ulikuwa ni Baiskeli (kama hujafika Tanga basi hujui jinsi baiskeli zinavyotumiwa). Ilikuwa ni mwezi wa saba, wiki ya kwanza ya mwezi, siku ya Ijumaa nilienda Pongwe kuchukua gari ambalo Mzee wangu alininunulia kama zawadi ili linisaidie kwa usafiri katika mji huo wa watu wa pwani. Wakati huo Tanga hakukuwa na vidaladala kama ilivyokuwa katika miji mingine mikubwa. Lilikuwa ni gari kuku aina Vokswageni mgongo wa kobe lakini lililotunzwa vizuri na mapadre wa kirosmini wa pale Parokia ya Pongwe.

Niliondoka Pongwe baada ya kula chakula cha jioni na Fr. John (aliyeniuzia gari) kwenye majira ya saa moja hivi. Giza lilikuwa limeshaanza kuingia katika mji huo uliotulia na uendao pole pole wa Tanga. Nilikuwa nimejawa na furaha sana kuwa na usafiri huo kwani nilijua sasa nitaufurahia mji wa Tanga kwa uhakika. Licha ya mshahara wangu, mzee wangu alikuwa akinitumia fedha kidogo za kunisaidia (yeye alikuwa ni Meneja wa Shirika la Mafuta la BP kule Mwanza). Nilipofika eneo la Maweni –ni kweli kuna mawe mengi sana- (karibu na lile gereza) nilimuona kwa mbali mtu akijaribu kuomba lifti na nilipokaribia niliweza kuona alikuwa ni mama na mtoto wake na vimizigo vyao. Kutokana na ukarimu niliopewa Tanga niliona nitakuwa ninafanya dhambi kumkatalia lift dada huyo, hivyo nilisimama baada ya kuwapita kwa mita chache hivi. Nilirudisha gari nyuma hadi walipokuwepo.

"Kaka habari yako" Alinisalimu dada huyo aliyekuwa amejitanda kanga ya vipande viwili huku kipande cha pili cha kanga kikiwa kimefunikwa kichwani na kuangukia mgongoni.

"Nzuri, mnakwenda wapi na usiku huu" Nilimuuliza huku lafudhi yangu ya kisukuma ikiwa ni dhahiri.

"Tunaenda Chumbageni" Alinijibu dada huyo huku akimvuta mkono binti mdogo wa kama miaka saba hivi.

"Haya ingieni" Nilimjibu huku nikitoka ndani ya gari langu na kuwasaidia kuweka mizigo yao kwenye boneti iliyo mbele ya mgongo huo wa kobe. Harufu ya manukato mazuri ilipenya ndani ya pua yangu, ilikuwa ni harufu ya yasmini. Haikuchukua muda tulianza safari ya kwenda Tanga mjini.

"Unaitwa nani" Nilimuuliza huku nikimuangalia kwa pembeni.

Kwa kumwangalia kwa karibu licha kigiza kilichokuwepo niliweza kutambua mara moja kuwa dada huyo alikuwa shombe, kwani licha ya ngozi yake kuonyesha kuchanganya damu, bali nywele zake zilikuwa ni za kiarabu (alikuwa ameiteremsha ile kanga aliyojitanda kichwani). Mashavu yake yalikuwa yameumuka sawia, huku macho yake yakiwa yamefunikwa kwa wanja. Midomo yake iliiva kwa rangi nyekundu ya mdomoni, na sikuweza kujizuia bali kukiri moyoni mwangu kuwa huyo dada alikuwa ni mzuri wa kuzaliwa.

"Naishwa Zainabu" Alinijibu.

"Mimi naitwa Mwl. Shija" Nilimjibu, huku nikiweka mkazo kwenye cheo cha ualimu na kujifanya mimi ni mtu miongoni mwa watu.

"Yaani wewe mwalimu? Mbona iko kazi basi" alisema huku akicheka kwa aibu.

"Mbona unacheka tena, kwani sifai kuwa mwalimu" nilimdodosa, huku nikijikuta nimefurahia kicheko chake cha kebehi.

"Si kwa ubaya, ila naona wewe ni kijana mdogo kujipachika cheo cha mwalimu" alifafanua huku kwa kutumia vidole vyake akiliweka neno "mwalimu" kwenye nukuu.

"Dada Zainabu, udogo si hoja" Nilimjibu. Nilimtaka anitambulishe huyo binti mdogo ambaye alikuwa ameanza kusinzia kwenye kiti cha nyuma.

"Huyo ni mtoto wa dadangu, tulienda kumuona baba yake pale Gerezani. Yuko kifungoni" Alinijibu na kunipa sababu ya wao kuwepo kule Maweni.

Aliniomba kama ingewezekana nimpeleke pale Masiwani na Kiwanda cha Chuma ili amrejeshe mtoto huyo kwa dadake, kasha nimpeleke Chumbageni. Kwa kweli sikuwa na haraka na nilifurahi kuwa na mtu wa kuzungumza naye kwani kwa karibu mwezi mzima nimekuwa nikizungumza zaidi na walimu wenzangu na wanafunzi. Haikuchukua muda mrefu hatimaye tulifika Masiwani, na Zainabu alimwamsha yule binti mdogo (anaitwa Saida) na kumpeleka ndani nyumbani kwa dadake. Miye nilisubiri nje na wala hakuchelewa kama nilivyohofia. Alipotoka nje dada yake alifuatana naye na alinipungia mkono kunisalimia na kuniasa.

"Uwe mwangalifu asikuzungushe usiku kucha huyo, mpeleke tu nyumbani" Alisema dada yake Zainabu kwa sauti ya kicheko. Nilimhakikishia kuwa hamna maneno na nitamfikisha salama mdogo wake huko kwake Chumbageni.
* * *

Tulikuwa tunakaribia eneo la Chuda karibu na kivuko cha reli ndipo vituko vya usiku huo viliponianzia. Kiza kilikuwa kimeshatanda na hakukuwa na mbalamwezi na mwanga wa pekee ulikuwa ni wa taa za rangu ya njano zilizokuwa kwenye milingoti mirefu pembeni ya barabara.

"Dada yako naona ni mtu mcheni kweli" Nilimwambia Zainab ambaye alikuwa amekaa kwenye kiti cha abiria huku akionekana mwenye fikara nyingi.

"Nakuambia, ana vituko sana Aisha" Alinijibu huku akinitajia jina la dada yake.

Tuliendelea kuzungumza kidogo hadi niliposikia honi ya treni ikiashiria kuwa treni ilikuwa karibu kufika mahali hapo. Niliamua kuongeza mwengo ili niweze kupita kabla ya treni kwani sikutaka kuzidi kuchelewa. Kwa bahati nzuri niliweza kufika pale kabla vya vyuma vya vizuizi kuteremka na kutenganisha barabara na reli. Hata hivyo kama vile nuksi, gari langu lilizimika katikati ya reli. Nilijaribu kuliwasha tena bila mafanikio kwani sauti ilikuwa ni ya betri iliyokuwa. Moyo ulianza kunienda kasi, kwa mbali niliweza kuona taa ile kubwa ya mbele ya kichwa cha treni ikiibuka toka viwanda vya sabuni, karibu na uwanja wa Saba Saba.

"Fungua mlango toka nje!" Nilimpigia kelele Zainabu aliyekuwa bado ameketi huku amekodoa macho yake kuangalia mbele.

Alikuwa kama amepigwa bumbuwazi wala hakunisikia wala kuonyesha dalili ya kufahamu hatari iliyokuwa inatukabili. Treni ilikuwa imeanza kukaribia huku ikipiga honi kwa nguvu zaidi. Nakajaribu kufungua mlango wangu nao uligoma, nikajaribu kufungua mlango wake huku nikimtingisha, bila ya mafanikio yoyote. Nilihisi kizunguzungu na akili kuniruka.

"Zainabu, Zainabu" Nilimuita kwa sauti kali huku jasho likinitoka.

Niliweza kulionga treni likiwa umbali wa kama mita mia moja hivi huku likiendelea kujaribu kufunga breki na kupiga honi yake kwa nguvu zaidi. Bila ya shaka dereva wa treni alituona na alijaribu kwa uwezo wake wote kutuashiria tutoke hapo relini. Haikuwezekana. Nilijaribu kwa kutumia ngumi kuvunja vioo vya gari bila ya mafanikio. Ama kweli, siku ya kufa nyani miti yote huteleza, nilijikuta nikijiambia. Nilimuangalia Zainabu aliyekuwa bado ametulia kwenye kiti chake akiwa bado anaangalia mbele bila ya hofu yoyote au kuonyesha tahadhari. Niliweza kuhisi mtingishiko na mtetemeko wa reli wakati treni imetukaribia huku mwanga wa taa yake kubwa ikitumulika. Niliamua kukata tama kwani nilijua huo ndo ulikuwa mwisho wa maisha yangu. Nilijalaumu moyoni kwanini nilimpa lifti binti huyo mkosi, kwani kama nisingempa lifti ningekuwa nimetulia zangu nyumbani mida hiyo na nisingekuwa kwenye hatari ya namna hiyo.

Treni ilikuwa imetukaribia kabisa kama mita kumi hivi toka tulipo na hakukuwa na jinsi ya kuikwepa au yenyewe kusimama. Zainabu alinigeukia kwa haraka utadhania yule "Mtambaaji wa Usiku (NightCrawler)" kwenye vitabu vya X-Men. Aliikunjua mikono yake kwa kasi ya mwanga na kunikumbatia kabla tu treni halijagonga Vokswageni yangu.

"Kash Kash" Alisema neno hilo haraka kwenye sikio langu, wakati treni ilipoligonga gari letu kwa nguvu zote.

Nilifumba macho yangu wakati wa mgongano. Sikusikia gari kutikikisika au sauti ya "bam"! Kulikuwa na ukimya wa ajabu nikiwa mikononi mwa Zainabu. Nilipofumbua macho yangu, tulikuwa bado tumekumbatiana ndani gari langu huku mabehewa ya treni yakipita ndani yatu kama vile tulikuwa ni mizuka. Niliweza kuona viti, watu, na kila kitu ndani ya treni huku treni ikiendelea kwenda kwa kasi. Sikuamini macho yangu, treni ilipita "ndani yetu" bila ya kutudhuru. Lilipofika behewa la mwisho, tulijikuta bado tuko katikati ya reli huku treni likiendelea mbele. Zainabu aliniachia na kurudi kitini na kuendelea kukodoa macho yake mbele. Nilitamani nipige kelele, sikuweza. Nilijaribu kuwasha gari tena na kwa jaribio moja tu, gari liliwaka na huku koo langu limenikauka kwa hofu nilianza kuendelea na safari.

"Zainabu, nini kimetokea pale" Nilimuuliza kwa sauti ya kutetemeka huku nikiegesha gari pembeni ya barabara ili kuvuta pumzi. Sikuamini kama nilikuwa bado hai, ndotoni, au ndo nshakufa na roho yangu bado inatangatanga.

"Unafanya nini?" Badala ya kujibu swali langu, alinirushia swali.

Nilimuambia siendi kokote hadi aniambie nini kimetokea pale, kwanini treni halikutugonga licha ya kwamba tulikuwa katikati kabisa ya njia yake. Niliegesha gari langu kama nilivyoadhimia huku vionjo vyangu vyote vikipiga kelele ya tahadhari. Nilitoka nje ya gari na kusimama pembeni huku nikihema kwa nguvu mikono yangu ikiwa imeagama kwenye dirisha la Zainabu ambaye hakutoka ndani ya gari. Aliendelea kuketi huku ameangalia mbele.

"Usitake kujua mengi Mwalimu Shija, hii Tanga" Aliniambia kwa sauti ya upole lakini iliyo thabiti.

Aliniambia si salama kuegesha hapo bali niendelee nimfikishe kwake Chumbageni na nihakikishe nimefika nyumbani kwangu kabla ya saa sita za usiku kwani anahisi kuna mabaya mengi yatatokea. Nilimwambia siendi kokote hadi anipe maelezo ya kutosha.

"Angalia nyuma yako!" Aliniambia kwa sauti ya kunitahadharisha na shari huku macho yake akiyaelekeza nyuma yangu ambapo na mimi sikuweza kujizuia bali kugeuka kufuatia alikoangalia.

Mwili ulinisisimka na nywele zikanisimama kwa ghafla utadhani paka aliyeona mbwa asiyemjua. Sikuweza kumuona mtu yeyote au kitu chochote bali nilihisi kama vile kuna mtu kasimama nyuma yangu. Kwenye kona ya jicho langu la kushoto nilihisi nimeona kivuli cha mtu au kitu kikinipitia karibu na kunitia kiza. Mwili ulipigwa na ubaridi wa ghafla na kwa sekunde chache sikujua nimeona nini au nimaluweluwe. Kabla sijamuuliza Zainabu "kulikoni" nilisikia kitu kizito kikinipiga kwenye kisogo na sikuwa na uwezo wa kukikwepa kitu hicho bali nilianguka chini kama gunia la mchanga.

Nilipozinduka nilikuwa nimeketi kwenye kiti cha dereva cha gari langu kana kwamba sikuwa nimeenda mahali popote. Gari lilikuwa limeegeshwa mbele ya nyumba kubwa ya rangi nyeupe ya "Msajili" – (hizo ni nyumba za NHC kule Tanga) na mara moja nikatambua mahali nilipo kwani upande wa kulia kwa mbali niliweza kuona nyumba maarufu za mbao za pale Chumbageni kwenye kijiji kilichojulikana kama "Kijiji cha Miaka 20". Zainabu alikuwa bado yupo pembeni yangu, na alikuwa akijiandaa kufungua mlango ili atoke.

"Mwl Shija asante sana" Alisema huku akitoka ndani ya gari hilo.

Sikuwa na kauli na ulimi ulikuwa umeganda kwenye taya la mdomo wangu. Nilijikuta nikimeza fundo kubwa la mate nikimuangalia Zainabu ambaye sasa alikuwa amezunguka mbele na kuja upande wa dirisha la dereva. Dirisha langu lilikuwa wazi. Aliinama kana kwamba alitaka kuniambia kitu. Kule kuinama kwake kulinipa nafasi ya kuangalia kifua chako na matiti yake yaliyokuwa yananing'inia kama embe bolibo; hakuwa amevaa sidiria. Alliegesha mikono yake kwenye ukingo wa mlango huku akiniangalia machoni, nilijifanya sikukiona kifua chake.

"Tutaonana baadaye" Alisema na kunyanyuka kuelekea iliko nyumba.

Sikuelewa alimaanisha nini aliponiambia "tutaonana baadaye" Nilimwomba Mungu kusiwe na baadaye. Alipoanza kukatisha kwenye baraza la nyumba hiyo niliweza kusikia mlio wa ‘ko ko ko' kama vile mtu aliyevaa viatu vya mchuchumio. Nina uhakika moyoni mwangu Zainabu hakuwa amevaa viatu hivyo kwani alikuwa amevaa viatu vya wazi. Nilitazama miguu yake nione alivaa viatu gani vyenye kutoa mlio utadhani mbao ikigonga sakafu. Moyo ulinipasuka kwani sikuyaamini macho yangu. Zainabu hakuwa amevaa viatu vya mchuchumio bali miguu yake ilikuwa ya kwato za ng'ombe. Sikutaka ushahidi wa ziada. Niliingiza gia na kukanyaga mafuta sikutaka kuangalia nyuma wala nini na kuondoka eneo hilo kwa mwendo wa kasi kuelekea nyumbani Majani Mapana. Moyoni, nilijikuta nikianza kusali sala ya "Baba Yetu" na ile ya "Salamu Maria". Nilijikuta najifunza "Kukemea" kama walokole huku nikirudia maneno ya "Ushindwe katika Jina la Yesu". Sikujua kama usiku huo ndio utakuwa wa mwisho kwangu duniani au kama nitaamka na kuiona Jumamosi. Sikujali sheria za usalama barabarani wala hofu ya ajali, kwani nilitaka kufika kwenye chumba changu ambako ningejihisi niko salama.

Kutoka eneo la kijiji cha miaka ishirini nilichukua barabara ya Pangani hadi karibu na stesheni ya treni ambako nilikata kona kulia na kuchukua barabara ya Morogoro na bila kufanya ajizi, nilikaza mwendo na kukanyaga mafuta kama nimepagawa kuelekea nyumbani. Ilikuwa nimekaribia lile eneo ambalo "nusura nipate ajali" pale Chuda, karibu kabisa na kituo cha mafuta cha BP. Kwa sababu fulani sikutaka kuangalia pale relini, macho yangu niliyakaza mbele. Nilipopita tu pale kiwanda cha sabuni, nilihisi kaubaridi kakinipuliza shingoni kwangu. Nilidhania nimeacha mojawapo ya madirisha ya gari wazi, na kwa haraka nikaangalia pembeni, na kukuta madirisha yote yamefungwa. Nywele zilinisimama tena, na mara moja nikajua kuna tatizo.

"Mwalimu Shija" Iliniita sauti ndogo ya kike, iliyonishtua utadhania nimeona mzimu wa Sokoine!

Nilijikuta nafunga breki ghafla huku gari likiserereka upande wa kushoto wa barabara. Ilikuwa inakaribia saa nne nusu za usiku wakati tukio hilo liliponikuta. Niliangalia kwenye kiti cha nyuma na kumkuta bindi mdogo Saida akiwa amekaa upande ule ule wa gari kama vile alivyokuwa ameketi wakati tunatoka Maweni. Nina uhakika Saida tulimshusha kula Masiwani kwa mama yake, na ninaapa mbele ya Mungu kuwa tulipoondoka Masiwani ilikuwa ni mimi na Zainabu tu. Jinsi gani Saida aliingia ndani ya gari sijui na sitaki kujua. Nilifumba macho yangu huku nikiyafikicha. Nilipoyafumbua tena na kuangalia ndani ya gari, Saida alikuwa ametoweka jinsi ile ile alivyoingia ndani ya gari. Sasa nilijua kuwa aidha nimeanza kurukwa na akili au ndo nimefanywa ndondocha.

Kulikuwa na watu kadhaa waliolikaribia gari langu kuangalia ni tatizo gani. Waliniuliza kama kila kitu kiko sawa au nahitaji msaada, niliwaangalia nikitamani niwaeleze yaliyonisibu na kuwaomba msaada. Kwa kiburi changu cha Kisukuma sikuweza. Niliwaambia tu kuwa nilikuwa nimesinzia kidogo kwenye usukani nilitaka nipate upepo kidogo kwani nina safari ndefu ya kwenda Korogwe usiku huo. Waliniponiacha nilivuta pumzi kidogo na niliangalia tena ndani ya gari kuhakikisha hakukuwa na mauzauza mengine. Nilipohakikisha kuwa hakuna kitu nilianza tena msafara wa kuelekea nyumbani Majani Mapana. Moyoni nilimuomba Mungu anisaidie nifike salama, na akinifikisha salama basi Jumapili iliyofuata nitaenda Kanisani.
* * *

Ilikuwa ni saa nne na nusu za usiku nilipojikuta nafungua mlango wa chumba changu kilichokuwa uwani kwenye nyumba ya Mzee Sudi karibu na duka la Mpemba pale Majani mapana. Niliingia ndani na mara moja nilienda kujitochea maji ya kunywa na kukata kiu cha muda mrefu kilichokuwa kimenikaba. Kwa sababu fulani, niliingia sebuleni, na chumbani, kuangalia kuwa hakukuwa na kitu chochote cha ajabu. Dari langu halikuwa na tundu wala nini. Kwa mara ya kwanza kwa muda wa masaa karibu matano nilijikuta najihisi niko salama. Nilivuta pumzi na kujisemea kwa kimombo "what a day?"!

Nilikuwa na njaa ile mbaya, na sikutaka hata nikae chini. Niliondoka mara moja kwa mguu kwenda kwenye duka la Mpemba kwani pembeni ya duka hilo kulikuwa na msururu wa kina mama na vijana kadhaa waliokuwa wakifanya biashara mbalimbali za vyakula. Meza zilipangwa kiustaarabu huku koroboi zikitoa mwanga hafifu kwenye genge hilo. Niliagiza samaki wa kukaanga, wali wa nazi na maharage ya nazi. Nilikaa pembeni chini ya taa iliyokuwa ikizungukwa na vijidudu na kula chakula changu huku akili yangu ikinizunguka utadhani gurudumu lililochomoka kwenye baiskeli. Nilihisi kichwa kikianza kuniuma. Nilitingisha kichwa changu na kujisemea tena "what a day". Baada ya kula kwa haraka haraka nilianza kujikongoja taratibu kuelekea nyumbani ili nipumzike maana ilitosha kwa siku moja kupata msisimko wote huo.

Saa tano na robo hivi, nilijikuta nikijilaza kitandani kwangu huku moyo wangu ukianza kutulia. Kwa sababu fulani nilijikuta nashindwa kupata usingizi kwani akili yangu ilikuwa inajaribu kutafuta maelezo ya kina ya kile kilichonitokea jioni hiyo. Licha ya jitihada zangu kutaruta maelezo ya kujiridhisha nilijikuta nagonga mwamba. Niliendelea kujigeuza geuza hapo kitandani kwa karibu saa nzima. Ilikuwa ni majira ya karibu saa sita na nusu za usiku, nilihisi harufu ya yasmin ikiingia chumbani mwangu. Ilikuwa ni harufu ya manukato aliyokuwa amejipaka Zainabu. Nilijaribu kufumbua macho yangu katika giza la chumba changu bila ya mafanikio Nilijitahidi kuamka sikuweza. Nilijaribu kujitingisha kidogo, mwili wangu uligoma. Nilikuwa nimepigwa ganzi.

"Kash Kash!" Sauti ya kike ilisema kwa upole na kwa ulaini, na kabla sijasema au kufanya chochote usingizi mzito uliniingia.

Haikunichukua muda nilijikuta nimeanza kuota. Sikutarajia ndoto hiyo, kwani niliota mimi na Zainab tuko kwenye ghorofa kubwa na ndefu, lililokuwepo pembeni ya bahari ya Hindi, huku tukiwa tumekumbatiana kimapenzi kwenye kitanda cha sufi chenye mashuka ya hariri. Nilikuwa nimelala chali bila nguo yoyote ile huku Zainab naye akiwa uchi wa mnyama amelala pembeni yangu kuangalia upande wa bahari. Mwili wake ulikuwa ni laini na ngozi yake nyororo. Shingoni alikuwa amevaa mkufu wa dhahabu ulioendana na hereni zake, na bangili alizokuwa amevaa mkono wa kushoto. Kwa kweli alikuwa ni malkia wa malkia wote. Nililala nyuma yake huku ****** yake yakiwa yamejibamiza mbele ya kiuno changu. Joto lake lilinipa ashki kupita kiasi na nilijikuta mzee akisimama na kupiga saluti.

Pole pole nilimgeuza na kumlaza chali huku nikitumia miguu yangu kumpanua. Zainab hakukaidi bali aliinyanyua mikono yake kunikaribisha kwa kunikumbatia. Alikuwa amelowa ile mbaya, na nilipojaribu kuingia, niliteleza kama vile sime inavyochomekwa kwenye ala. Sikuweza kujizuia nilianza kumkatikia, na binti huyo wa damu iliyochanganya hakuwa mwanafunzi. Kwa mahaba makubwa tulipeana mapenzi huku harufu ya maji ya chumvi ikijaza chumba chetu. Moyoni nilisahau yote yaliyonisibu na wala sikuwa na kumbukumbu nayo. Zainabu alibana miguu yake kiunoni kwangu huku akijiviringisha kunileta miye chali. Na mimi sikukaidi kwani napenda mwanamke akiwa juu yangu na kama anajua kutumia alichojaliwa na mama yake. Zainabu alikuwa ni mwanamke wa jinsi hiyo. Alianza kunipa mavitu hadi nusura nipige kelele za furaha. Nilifumba macho yangu kufurahia penzi hilo la mtoto wa Kitanga.

Mikono yangu iliendelea kuchezea matiti ya binti huyo wakati yeye akiendelea na "vitu vyake". Nilizungusha mikono yangu mgongoni mwake ili niendelee kumpapasa kwa raha. Viganja vyangu vilihisi vitu kama magamba mgongoni mwake. Nilijaribu tena na kugundua kuwa binti huyo alikuwa na magamba mgongoni. Mara moja nikahisi mwili wa binti yule umepoteza joto lote na umekuwa baridi kama barafu. Yeye alikuwa hajali aliendelea na shughuli. Sikuweza kuendele niliacha kumchezea mgongo na kufumbua macho yangu. Naapa maajabu haya mwanadamu hapaswi kuona na baadaye kusimulia.

"Kash Kash" Alisema tena.

Na mara hiyo chumba kizima kilijazwa na mwanga uliotoka ndani ya mwili wa binti huyo. Ulikuwa ni mwanga wenye rangi ya mbalamwezi angavu. Nilipomuangalia usoni, ndipo nilipojikuta roho ikinitoka. Zainabu alikuwa na jicho moja kwenye paji la uso wake, huku mwili wake ukiwa nusu toka juu hadi chini. Titi moja, mkono mmoja, mguu mmoja, nusu ya kila kitu. Nilimsukuma kwa nguvu na kumuondoa kifuani mwangu. Sikuweza tena kujizuia bali nilipiga ukelele kama mtoto mdogo, kuomba msaada.

Nilizinduka usingizini huku nikihisi mwili wangu wote ukipigwa na upepo mkali, na niliweza kuona kuwa jua limeanza kutoka kwani ilikuwa ni asubuhi ya siku ya Jumamosi. Nilipoangalia vizuri niligundua kuwa sikuwa chumbani kwangu, wala ndani ya nyumba, wala ndani ya hoteli. Mwenzenu nilijikuta juu ya mti wa Mbuyu huku nguo zangu zikiwa zinaning'inia kwenye matawi yake. Chini ya mti huo kulikuwa na kikundi cha watu wamezunguka wananiangalia na bila ya shaka walikuwepo hapo kwa muda mrefu.

"Baba karibu Tanga" Sauti ya mzee mmoja ilisema kwa sauti.

"Naomba msaada jamani, mniokoe" Niliomba kwa sauti ya kimasikini na nisiye na uhakika kama wanaweza kunisaidia.

Haikuchukua muda mrefu wasamaria wema hao walinisaidia kuteremka kwenye mti huo mkubwa. Sikuhitaji kuambiwa nilikuwa wapi kwani niliweza kuona wachuuzi wakianza kuleta mazao yao kwenye soko maarufu la matunda mjini Tanga. Nilikuwa pembeni kidogo ya soko la Makorola karibu kilometa kumi na tano toka nyumbani Majani Mapana. Walinipa shuka nikajisitiri. Yule mzee aliyenikaribisha Tanga alinichukua chemba na kuniuliza yaliyonisibu. Nilimweleza tangu mwanzo wa mkasa hadi dakika ile. Muda wote huo mzee hakuonyesha kushtushwa au kushangazwa. Nilipomaliza nilimsikiliza alichonacho. Mzee huyo aliniambia kuwa kilichonisibu ni shetani wa Mahaba aliyewahi kuwa mke wa Jini la Kiarabu la Kash Kash. Sikuwa wa kwanza kukutwa na masahibu kama hayo.

Nilimuuliza kama kuna dawa au madhara yoyote yaliyonipata baada ya kukutana na jini lile. Kwanza kabla ya kunijibu alitaka kujua kama nilifanya mapenzi na jini hilo kwenye ndoto. Nilimjibu ndiyo. Alisikitika sana. Aliniambia kuwa "nimeteuliwa" na jini hilo, na kwa sababu hiyo Kash Kash hataniacha nilale na mwanamke mwingine yoyote yule hadi kifo. Kwa vile nimelala na mke wake (Zainabu) basi jini hilo limeweka dai kuwa nisioe au kulala na mwanamke mwingine yoyote yule. Nilimuuliza mzee huyo kama kuna kitu chochote ninachoweza kufanya kujikinga au kujiondoa na laana hiyo.Aliniambia kuwa njia pekee ni kwenda Mabokweni kwa Sheikh Hamza Hamdani anayeweza kunipa dawa na kuniagua.

Nilifunga safari siku hiyo hiyo kwenda Mabokweni, kijiji kilichoko nje kidogo ya mji wa Tanga kwenye barabara ya kwenda Mombasa. Nilipewa masharti kadhaa ambayo ilinichukua karibu miaka mitatu kutimiza, na hatimaye ile laana ilivunjwa baada ya mimi na mimi kumtafuta mtu mgeni wa Tanga na kumtupia jini hilo. Leo hii niko salama, kwani mara tu ya kukamilisha matakwa hayo ya kijadi, niliamkua kuondoka mji wa Tanga na kurudi kwetu Mwanza. Leo hii nimeoa na nina mtoto mmoja. Anaitwa Shida. Mke wangu anaitwa Zabibu.

H A P P Y H A L L O W E E N !!
 
Mwanakijiji, haya matukio yalikutokea wewe binafsi ama umeletewa na mtu ambaye yalimsibu? Ufafanuzi kidogo tafadhali.
Najua tarishi hauwawi
 
Majina na matukio katika hadithi hii ni yakubuni. Mfanano wowote na watu, mahali au matukio halisi ni wa kinasibu na si kusudio la mwandishi. Haki zote za kunakili na kuchapisha zimehifadhiwa - Kijijini Productions Inc,)

Jamani mmesoma huu mstari,tushaambiwa amebuni. Na hiyostory ni spesho kwa haloween.

Good job mtunzi.
 
mh???!!! nahisi wakati yunaishi huyo jini alishapotea
ila kwa kuwa ni stori ya kubuni haina shida japo ni aina ya hadithi utakazoambiwa na ndugu zako au jamaa zako kuwa ukienda tanga utakutana na hayo,
kama yalikuwapo basi ni zamani sana kwani hata wagosi waliimba tanga jamani paleee mbona kila kitu kimekwisha?so mambo hayo jamani yamekwisha tanga ni bonge ya mji kuishi,i miss it very much

dr remmy aliimba mwanza nitarudi mwanza wacha mimi niimbe tanga nitarudi tanga
 
SASA HIVI UTAKUTA SOKONI SINEMA YA KISWAHILI YENYE JINA LA KIINGEREZAIKIWA NA MTIRlRIKO HUU.
UNAWAUZIA KINA KANUMBA MA IDEA BILA YA WEWE KUFAHAMU.

lakini watakuwa wazembe.. maana ningeweza kuwatungia kisa cha movie ambacho kingemuondoa Kanumba katika "ze ugreat" na kuwa Kanumba the actor!
 
Duh! MM imekaa pouwa nimeichukua nitaenda kumsomea mwadada wangu. Asandi
 
dah mkuu hii imetulia sana,mi ni msomi sana wa riwaya na hadithi za namna hii ni nyingi mno mpaka niliamua kwenda tanga mapumziko nione tu watu wake kwa hadithi nilizowahi kusikia,lakini mengi yana ukweli ndani yake,maana ukifika tanga lazima uaguliwe,we waweza jiona mzima waganga wakikuagua watakwambia mlolongo wa mambo mpaka utasikia kizunguzungu.
 
dah mkuu hii imetulia sana,mi ni msomi sana wa riwaya na hadithi za namna hii ni nyingi mno mpaka niliamua kwenda tanga mapumziko nione tu watu wake kwa hadithi nilizowahi kusikia,lakini mengi yana ukweli ndani yake,maana ukifika tanga lazima uaguliwe,we waweza jiona mzima waganga wakikuagua watakwambia mlolongo wa mambo mpaka utasikia kizunguzungu.

wewe uliganguliwa ?
 

Similar Discussions

4 Reactions
Reply
Back
Top Bottom