Changamoto za Upungufu wa umeme Kupatiwa Ufumbuzi
Mkurugenzi mkuu wa TANESCO Bw. Maharage Chande akizungumza na waandishi wa habari leo December 2, 2022 kuhusu hatua za muda mfupi na muda mrefu kumaliza upungufu wa umeme .
Mkurugenzi ameongeza kuwa mvua zinazonyesha muda huu nchini bado hazijaweza kutiririka katika mito ya maji inayoingia katika mabwawa ya umeme.
Hivyo juhudi zimeelekezwa mitambo ya gesi na kukarabati mitambo huku mvua zinazoendelea kunyesha hatimaye kujaza mito inayotiririsha maji katika mabwawa ya umeme.
---
Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) ameelezea mikakati yao wanayoendelea nayo pamoja na changamoto wanazokutana nazo katika harakati zao za kurejesha huduma ya umeme.
Amesema “Tayari tumeshakamilisha matengenezo ya mtambo mmoja wa LM6000 katika kituo cha Ubungo namba III na umeshaanza kuingiza megawati 35 za umeme katika Gridi ya Taifa kuanzia tarehe 25 Novemba 2022 kama tulivyoeleza hapo awali.
“Tayari tumeshakamilisha matengenezo ya mtambo mmoja wa kituo cha Kidatu na umeshaanza kuzalisha megawati 50 za umeme katika Gridi ya Taifa kuanzia tarehe 30 Novemba 2022.
“Matengenezo ya mtambo mmoja katika kituo cha Kinyerezi namba II yameshakamilika na tayari umeshaanza kuzalisha megawati 215 za umeme kuanzia tarehe 24 Novemba 2022.”
Kuhusu juhudi zao za muda mfupi, amesema majaribio ya mitambo miwili katika kituo cha upanuzi cha Kinyerezi namba I yanaendelea, na kwa sasa mitambo hiyo inaingiza jumla ya megawati 65 za umeme katika Gridi ya Taifa. Pia wanategemea hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Disemba 2022, mitambo hii itakuwa inazalisha jumla ya megawati 90 kama tulivyoeleza hapo awali;
Ameongeza kuwa bado wanaendelea na kazi za matengenezo ya mitambo miwili ya Ubungo namba III ambapo baada ya kukamilika mwishoni mwa Disemba 2022, itazalisha jumla ya megawati 40 za umeme.
JITIHADA ZA MUDA WA KATI ZINAZOENDELEA KUFANYIKA
Ameseme “Tunategemea mitambo mingine miwili kuanza kufanya kazi katika kituo cha upanuzi cha Kinyerezi namba I kuanzia mwezi Februari 2023 ili kuingiza megawati 90 za umeme katika Gridi ya Taifa.
“Iwapo mvua zitaendelea kunyesha katika mabwawa yote ya kufua umeme na matengenezo yaliyobakia kukamilika kama yalivyopangwa, basi tunategemea hali ya umeme itaendelea kuimarika na hivyo tunatarajia kiasi cha upungufu wa umeme kwa siku kuendelea kupungua kutoka wastani wa kati ya megawati 300 hadi 350 wiki iliyopita hadi kufikia megawati 215 za umeme wiki hii.”