Tanganyika Law Society
Member
- Oct 15, 2018
- 17
- 153
TAARIFA KWA UMMA
TAMKO LA TANGANYIKA LAW SOCIETY (TLS) JUU YA UAMUZI WA KAMATI YA MAWAKILI KUMUONDOA BI. FATMA AMANI KARUME KATIKA REJISTA YA MAWAKILI TANZANIA BARA NA UAMUZI WA WAKILI FATMA AMANI KARUME KUKATA RUFANI
TAMKO LA TANGANYIKA LAW SOCIETY (TLS) JUU YA UAMUZI WA KAMATI YA MAWAKILI KUMUONDOA BI. FATMA AMANI KARUME KATIKA REJISTA YA MAWAKILI TANZANIA BARA NA UAMUZI WA WAKILI FATMA AMANI KARUME KUKATA RUFANI
Mnamo tarehe 2 Oktoba 2020 Baraza la Uongozi la Tanganyika Law Society (TLS) baada ya kuupokea na kusoma kwa makini Uamuzi wa Kamati ya Mawakili katika Maombi Namba 19 ya Mwaka 2019 baina ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Fatma Amani Karume, lilikaa na kuujadili. Baraza la Uongozi liliziona sababu zilizoifanya Kamati ya Mawakili kumkuta Wakili Fatma Amani Karume na hatia ya ukiukwaji mkubwa wa maadili ya taaluma ya sheria na kuamuru kuondolewa kwake katika Rejista ya Mawakili nchini.
Licha ya mambo mengi yanajitokeza mtu anapousoma uamuzi huo, Baraza la Uongozi liliguswa sana na mambo yafuatayo:
a. Namna ambavyo Mwanasheria Mkuu aliwasilisha upya malalamiko yake kwa Kamati ya Mawakili kinyume na amri na maelekezo ya Jaji Kiongozi Dr. Eliezer Mbuki Feleshi aliyoyatoa katika uamuzi wake katika kesi Ado Shaibu v. John Joseph Pombe Magufuli (The President of the United Republic of Tanzania) & wengine wawili (Misc. Civil Cause No 29 of 2018) ya kumuagiza Msajili wa Mahakama Kuu “ kuwasilisha madai ya kukiuka maadili ya kitaaluma yaliyomo katika mawasilisho ya mleta maombi na majibu ya mwisho ya mlalamikiwa pamoja na uamuzi huu kwenye Kamati ya Nidhamu ya Mawakili ili yaamuriwe.”
b. Muundo wa Kamati hiyo ya Mawakili kusikiliza lalamiko lililowasilishwa kwake na Mwanasheria Mkuu dhidi ya Bi. Fatma Amani Karume na uwezekano mkubwa wa kuwepo upendeleo au muonekano wa upendeleo;
c. Kupokelewa kwa ushahidi wa kieletroniki wakati shauri linaendelea ambao haukuambatanishwa kwenye lalamiko au katika Orodha ya Nyaraka zitakazotumiwa (kama ilikuwepo);
d. Ukubwa na ukali wa adhabu; na
e. Taathira ya uamuzi huo kwa uwakili/utetezi na uhuru wa mawakili Tanzania Bara.
Baraza la Uongozi, kupitia kwa Raisi wa TLS, liliwasiliana na Wakili Fatma Amani Karume ambaye alisema hakubaliani kabisa na uamuzi huo na yu tayari kukata rufani. Na hivyo basi, Baraza la Uongozi likizingatia wajibu wake mkubwa iliopewa na kifungu cha 4(1)(d) cha Sheria ya Chama cha Mawakili Tanganyika (Tanganyika Law Society Act Cap 307 R.E. 2002) unaoitaka TLS “kuwawakilisha, kuwalinda, na kuwasaidia wana taaluma wa sheria nchini Tanzania kuhusu hali ya utendaji kazi za sheria au vinginevyo” liliazimia kwa kauli moja kutoa msaada wake kwa mwanachama wake, Fatma Amani Karume, kukata rufani dhidi ya uamuzi wote huo na Amri Andikwa ya Kamati ya Mawakili, na litampa msaada wote wa kisheria litakaloweza katika rufani yake kwa Jopo la Majaji Watatu wa Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania.
Limetolewa Jijini Dar es Salaam kwa Amri ya Baraza la Uongozi leo tarehe 6 Octoba 2020.
………………………………………
Dkt. Rugemeleza A.K. Nshala
Rais
Dkt. Rugemeleza A.K. Nshala
Rais