BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,792
- 287,994
Date::2/26/2009
Taifa Stars waliwatoroka polisi Abidjan kimya kimya
Na Saleh Ally, Abidjan
Mwananchi
Taifa Stars waliwatoroka polisi Abidjan kimya kimya
Na Saleh Ally, Abidjan
Mwananchi
UAMUZI wa kikosi cha Taifa Stars kuamua kutokula chakula kwenye hoteli ya Golf ya mjini hapa ili kukwepa hujuma, kulizua tafrani kubwa baada ya askari Polisi aliyepewa dhamana ya kuwalinda kutaka kuwalazimisha kupanda kwenye basi kwa nguvu.
Stars juzi iliibuka na ushindi wake wa kwanza wa mashindano ya CHAN kwa kuwachapa wenyeji Ivory Coast kwa bao 1-0 lililofungwa na Mrisho Ngassa kwa kichwa cha kuchupa.
Kamati maalum iliyo jijini hapa ilichukua uamuzi wa kuhakikisha Stars hawali chakula cha hotelini hapo na maandalizi yakafanyika kwenda kula mafichoni ili kuepuka hujuma hasa suala la kuwekewa 'vitu' mbalimbali kwenye chakula.
Lakini ilibidi ifanyike kazi ya ziada kuwatoroka walinzi ambao wamekuwa wakitembea na timu hiyo tangu imewasili jijini hapa, wakiwamo askari Polisi wawili wa usalama barabarani wenye mbwembwe za kila namna.
Wachezaji Stars walitoroka kimya kimya kutoka hoteli ya Golf ndani ya Taxi sita kwenda kula huko walikopangiwa, baada ya hapo walinzi hao walianza kuwasaka kila kona ya jiji na mwisho walifanikiwa kuwapata pale walipokuwa kitu ambacho kilimshangaza kila mmoja.
'Kila mtu alishangaa jamaa wamepajua vipi, tulibaki tumepigwa na butwaa na mara moja wakaanza kutulazimisha kupanda kwenye gari, lile basi tunalotumia lakini viongozi pamoja na (Crescentius ) Magori na Teddy Mapunda wakazuia. Hatukupanda.
'Walitaka kuanza kutumia nguvu na sisi tukagoma, ikawa mshike mshike, lakini mwisho jamaa wakakubali kufuatana na sisi. Tukaingia kwenye zile taxi na kuanza kurudi hotelini huku wakitusindikiza kwa ving'ora na basi likiwa tupu,' anaeleza mmoja wa wachezaji wa Stars.
Lakini hali ya kuwalazimisha wachezaji kupanda kwenye basi hilo tayari ilionyesha kulikuwa na walakini na askari mmoja aliiambia Mwananchi kwamba ule ni utaratibu ingawa mmoja alikiri kwamba ilikuwa ni amri kutoka ngazi za juu zinazoshughulikia masuala ya usalama katika michuano ya CHAN ambao walitaka kuona lazima wachezaji wa Stars wapande basi hilo.
Kumekuwa na hujuma katika mechi nyingi hasa katika nchi za Afrika kitu ambacho kimeifanya Stars kuongeza umakini hasa inapokua mbali na nyumbani.
Hali hiyo pia ilijitokeza wakati wa mechi yake ya mwisho kufuzu katika michuano ya CHAN dhidi ya Sudan mjini Kharthoum ambako wenyeji walilala kwa mabao 2-1.
Imeelezwa kumekua na tabia ya kupulizia dawa kwenye vyumba au kwenye chakula na wachezaji baada ya muda mfupi wanachoka hivyo kuwafanya washindwe kucheza kwenye viwango vyao. Ingawa Caf imeshindwa kuthibitisha hilo hadharani lakini imekua hali inayojitokeza mara kwa mara.