Lucchese DeCavalcante
JF-Expert Member
- Jan 10, 2009
- 5,471
- 733
TIMU ya Soka ya Taifa (Taifa Stars) imepania kushinda mechi yake ya kirafiki na Timu ya Taifa ya Uganda ‘The Cranes' inayotarajiwa kutimua vumbi kesho kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini hapa.
Akizungumza jana katika Hoteli ya Isamilo ambako Stars imepiga kambi, Meneja wa Timu hiyo Leopold Mukebezi alisema kuwa kwenye mchezo huo Stars imeupa umuhimu wa pekee kwa madai kuwa The Cranes ni timu bora katika viwango ya Shirikisho la Soka Duniani (FIFA).
"Kucheza na The Cranes kwenye mechi ya keshokutwa ni faida kwetu kwa sababu ni timu iliyo katika kiwango bora kwa mujibu wa FIFA, na tuna imani Stars itafanya vizuri," alisema ingawa hakuwa tayari kuzungumzia masuala ya kiufundi kwa madai yeye anashughulikia zaidi mambo ya utawala.
Mukebezi alisema timu hiyo ya Uganda iko katika nafasi ya 80 kwenye viwango vya FIFA, na ikizingatiwa kuwa ndiyo bingwa wa Kombe la Chalenji.
Alisema baada ya mchezo huo na The Cranes, Stars inatarajia kukipiga tena na Timu ya Taifa ya Somali katika mchezo unaotarajiwa kufanyika mwanzoni mwa Aprili ambapo alidokeza kuwa endapo Stars itafanya vizuri kwenye mchezo yawezekana mchezo wake wa marudiano na timu hiyo ukafanyika jijini Mwanza.
"Stars ikicheza vizuri yawezekana mechi yake dhidi ya timu hiyo ya Somalia ikafanyikia huku Mwanza, ingawa hili jambo hatujalithibitisha," aliongeza. Mchezo wa Stars na Somalia ni wa kuwania kufuzu fainali za michuano ya Afrika kwa wachezaji wa ndani (Chan).
Juhudi za kumpata Kocha wa The Cranes Robert ‘Bobby' Williamson jana ziligonga mwamba kwani timu hiyo ambayo ilikuwa iwasili jijini Mwanza saa tano kwenye Uwanja wa ndege wa Mwanza ilikuwa haijawasili kutokana na uwanja huo kufungwa kwa muda baada ya ndege ya ATC kupasuka matairi na hivyo haikuruhusiwa ndege kubwa kutua.
Stars tangu juzi ilipowasili jijini imekuwa ikiendelea na mazoezi yake kwenye Uwanja wa CCM Kirumba ikiwa chini ya Kocha wake Mbrazili Marcio Maximo.
Hata hivyo Kocha huyo alipofuatwa jana kuzungumzia hali ya timu hiyo na gazeti hili, hakuwa tayari kuzungumzia chochote kile kwa madai kuwa mambo yote yatazungumzwa kwenye mkutano na waandishi wa habari uliotarajiwa kufanyika jana jioni.