Taifa lilipotekwa Nyara, Usalama wa Taifa walikuwa wapi?

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,460
39,927
Makala hii imetoka kwenye gazeti la Tanzania Daima (hard copy) lakini kwenye mtandao haikuwekwa.

TAIFA LILIPOTEKWA NYARA, USALAMA WA TAIFA WALIKUWA WAPI?​
Na. M. M. Mwanakijiji

Ningependa kuungana na waandishi wengine wengi leo ambao wameandika kuhusu kikao cha NEC Butiama na maana yake kwa Taifa. Nikiwa mmoja wa waliofuatilia kwa karibu naomba nikwepe kufanya hivyo kwa sasa ili nipate muda wa kuchambua hasa kile kilichojiri. Nirudi kidogo kwenye suala la EPA na madai kuwa yawezekana Tanzania iko mikononi mwa maghaidi.

Uwezekano kuwa nchi yetu iko mikononi mwa maghaidi na kuwa vyombo vyetu vya usalama vinatambua hivyo, ni uwezekano ambao lazima umshtue Mtanzania yeyote yule kwani kama ni kweli, basi tunachopigania siyo hali yetu ya maisha ya kuwa huru na wenye kufanikiwa bali tunapigania uhai wetu kama Taifa.

Bila shaka umepigwa na butwaa unashangaa “hili limetoka wapi tena” hata hivyo kama umekuwa mfuatiliaji wa habari unajua kabisa nini niniachozungumzia. Mapema mwezi uliopita Inspekta Jenerali wa Polisi akizungumza na waandishi wa habari katika mkutano wa Kamati inayofuatilia wizi wa EPA alisema kuwa suala la wizi wa EPA linaweza kufananishwa na utekaji nyara wa ndege ambapo vyombo vya usalama vinalazimika kuzungumza na wateka nyara hao ili kunusuru maisha ya abiria.

Ni katika maelezo hayo na jinsi alivyotumia mfano huo ndipo leo ninajikuta najiuliza kama yumkini kuwa nchi yetu imetekwa nyara na maghaidi wa EPA na sasa tunafanya nao majadiliano ili wasitulipue? Kama kweli tumetekwa nyara basi tufanye nini tujinasue au tukubali tu yaishe na tusalimike?

Binafsi sitaki kuamini hata kidogo kuwa tumetekwa nyara; lakini dalili zote zinaonesha kuwa tumechukuliwa mateka na mafisadi wa EPA. Kwanza kabisa lazima tukumbuke kuwa hawa jamaa waliokwapua fedha za EPA ni kama majambazi ambayo yameingie Benki na kuchota fedha toka “Chumba Kikuu” na huku wakipepea mabomu na silaha zao wakatokomea mafichoni.

Na sasa baada ya polisi kujua ni kina nani walioiba benki wanagundua pia kuwa siyo walikwapua na vipande vya dhahabu na kuondoka na baadhi ya wafanyakazi kama bima y ao. Sasa polisi wanakabiliwa na swali wavamie nyumba kuokoa fedha na watu au wakae katika meza ya “majadiliano” na majambazi ili waokoe fedha na watu?

Kwa mujibu wa IGP Mwema uamuzi ni huu wa kukaa na majambazi na wateka nyara ili kupata suluhu wasije “wakailipua nchi”.

Sasa kama hili ni kweli lazima tujiulize kwanza, walinzi wa benki zetu walikuwa wapi hadi majambazi yakaingia hadi Benki Kuu na kuchota fedha na kutuchukua mateka? Wakati mafisadi wa EPA wanaingia mikataba ya wizi na kuunda makampuni ya geresha wale walinzi walioapa kuilinda nchi hii walikuwa wanalala wapi? Jibu siyo gumu.

Ndugu zangu, taifa letu limechukuliwa mateka kwa sababu walinzi wa Taifa hilo na hasa vyombo vilivyotakiwa kusimamia usalama wa Taifa hili wanadaiwa kuwa ni sehemu ya wezi hao. Kwamba, waliokula njama kuiibia nchi hii na kututeka mateka walifanya hivyo mbele ya vyombo vya usalama na vyombo hivyo havikufanya lolote kuzuia.

Tumetekwa mateka kwa sababu Jeshi la Polisi na vitengo vyake vyote ambavyo vimepewa jukumu la kulinda “raia na mali zao” walishindwa kufanya hivyo. Kama Jeshi la Polisi lilishindwa kuanzisha uchunguzi wa kihalifu muda wote wa tuhuma za wizi wa EPA kwanini leo walalamike kuwa tumetekwa mateka?

Kama Jeshi la Polisi ambalo lina maofisa wenye nyota nyota, magari ya ving’ora na mbwa wa kunusa walishindwa kuzuia wizi wa Benki Kuu mchana kweupe ni jinsi gani tunaweza kulalamika kuwa tumechukuliwa mateka? Lakini binafsi siwapi mzigo mzito wa lawama polisi isipokuwa chombo kimoja ambacho kwa hakika siyo tu hakina budi kupanguliwa lakini viongozi wake kuwajibishwa kwa kuacha nchi yetu itekwe nyara na mafisadi

Chombo hicho ni idara ya Usalama wa Taifa ya Tanzania. Kama kuna chombo ambacho siyo tu kimeliangusha Taifa letu bali pia kimeonesha udhaifu mkubwa wa kuwajibika ni idara hii ya Usalama wa Taifa ambayo imekaa kana kwamba inafanya kazi wakati wa vita baridi.

Kwa mujibu wa sheria iliyounda idara hiyo ina majukumu makubwa manne ambayo yote yanahusiana na mambo ya usalama wa Taifa na kukusanya habari za kijasusi na kutoa taarifa kwa vyombo husika. Katika kufanya hivyo idara hiyo inajukumu la kuangalia mambo ya wizi wa siri za serikali kupeleka kwa adui, habari za kighaidi, kuvuruga vitu, na pia mambo mengine kama hayo.

Idara hiyo inakatazwa kisheria kusimamia usalama moja kwa moja na pia inakatazwa kuanzisha uchunguzi au ujasusi dhidi ya mwananchi yeyote wa Tanzania kwa sababu ya shughuli halali za mtu huyo kupinga au kutokubali maamuzi fulani ya serikali akitelekeza haki zake za kikatiba.

Idara hii ilitakiwa kuhakikisha kuwa inakusanya taarifa zote za kijasusi ambazo zinaweza kusaidia kuwa hakuna ghaidi ambaye anaweza kupenya na kufanya uovu na hivyo ni jukumu la idara hiyo kutoa taarifa kwa vyombo husika ili vichukue hatua madhubuti. Kwa maneno mengine, Usalama wa Taifa wanatakiwa kushughulikia ukusanyaji wa taarifa za kijasusi na siyo ulinzi wa viongozi au mipango ya viongozi.

Yawezekana kuna sababu ya Usalama wa Taifa kuonekana wanashughulikia “ulinzi wa viongozi” lakini kisheria jukumu hilo naamini halipo mikononi mwao; wao jukumu lao ni kushughulikia mambo ya kijasusi.

Ni kwa sababu hiyo basi naweza kusema pasipo shaka kuwa wizi uliotokea Benki Kuu kuanzia huu wa EPA, na ndugu zake wa Deep Green, Meremeta, Tangold, na Mwananchi Gold yote yametokea kwa sababu TISS ilishindwa vibaya kabisa kukusanya taarifa za kijasusi. Hii ni aibu kwa taifa hili.

Kama watu wanaolipwa kukusanya habari za kijasusi walishindwa kugundua kuwa kuna fedha zimeibwa toka Benki Kuu ni nani basi tunaweza kumuamini? Lakini swali jingine ni kuwa je yawezekana kuwa TISS haikushindwa lakini ilikuwa ni sehemu ya uchafu na ufisadi huo?

Mpendwa msomaji kama unakumbuka utaona kuwa wakati Bi. Meghji ameidhinisha fedha za kuilipa kampuni ya Kagoda aliambiwa na Balali kuwa fedha hizo zilikuwa ni kwa ajili ya shughuli za “Usalama”. Hadi leo hii, hakuna chombo cha usalama ambacho kimekana kuhusika na wizi wa fedha hizo. Siyo Polisi, JWTZ au Usalama wa Taifa ambao wamesimama na kusema hawakuhusika na wizi huo au kutoa baraka zao kama ilivyodaiwa kitu ambacho mwenye fikra anaweza kujua ina maana gani. Wakati mwingine ukimya una maana ya kukubali.

Usalama wa Taifa hawakushindwa wajibu wao kwenye suala la EPA tu bali pia kwenye suala jingine la Richmond. Hivi hadi Watanzania tunaingia kwenye mkataba huu wao Usalama wa Taifa (TISS) walikuwa wapi? Hivi ni kitu gani ambacho kinahatarisha nchi kama suala la nishati kuchezewa?

Wakati tumepata dharura ya nishati ilihitajika uangalizi mkubwa wa nini tunafanya tusije kukurupuka kualika wasiotutakia mema kuja kutuletea umeme. Mara baada ya tetesi kuwa Richmond ni kampuni feki zimeanza (na zilianza zamani) TISS walifanya nini kuhakikisha kuwa usalama wa nchi yetu hauwi mikononi mwa kikundi cha watu wachache? Hakuna.

Katika ripoti ya Kamati ya Bunge iliyoongozwa na Dr. Mwakyembe hatuoni ni jinsi gani watu wa Usalama wa Taifa walishiriki katika kuhakikisha kuwa Richmond haipewi tenda hiyo. Kwa mujibu wa sheria iliyounda taasisi hiyo nina uhakika wanazo nguvu za kuangalia habari za kijasusi ambazo zinaweza kutishia usalama wa nchi yetu. Ninaamini TISS ingeweza kutumia nguvu walizonazo katika ibara ya 5(b) ya sheria hiyo ya Idara hiyo. Hawakufanya hivyo.

Sasa hivi kuna suala zima la fedha za dola zilizokosewa karibu miaka nane iliyopita karibu dola milioni tatu; fedha zile ziliishia wapi baada ya kukataliwa? Hakuna anayejua na hakuna taarifa iliyotolewa lakini wakusanya habari za kijasusi wetu wanaendelea na maisha yao wakiombea kuwa Tanzania iko salama.

Idara hii inahitaji kufanyiwa mabadiliko ya haraka na ya lazima ili kuinusuru na kuipa nguvu ya kulinda maslahi ya Taifa hili. Ndugu zangu, roho ya usalama wan chi yetu iko mikononi mwa taasisi hii na inaposhindwa kutimiza wajibu wake siyo tu viongozi wake wanahitaji kuwajibika lakini wao wenyewe wakiwa waungwana wangeweza kuwajibika.

Hivi Mkurugenzi wa Idara hiyo anaweza vipi kupata usingizi huku akijua kuwa taasisi yake imeshindwa kazi ya kukusanya habari za kijasusi? Na hapa simaanishi kutafuta nani ni nani wa Jambo forums! Nina maana kukusanya habari ambazo zingesaidia kuzuia Taifa kutekwa nyara na mafisadi? Yeye na waziri wake (sijui waziri wa Usalama wa Taifa ni nani.) wanaweza vipi kunywa chai, na kula kuku kwa mrija wakati wahuni wachache wanatuingiza mjini na kampuni hewa hadi Taifa linaadhirika kwa kujiuzulu waziri Mkuu?

Tunaweza kuchezea mambo mengine lakini hili la usalama wa Taifa letu siyo jambo la kuchezea hata kidogo au kuchukulia kwa wepesi. Idara inayotengewa mabilioni ya shilingi inaposhindwa kugundua ufujaji mkubwa benki kuu siyo tu imeshindwa kazi bali pia imeihatarisha nchi na kwa hakika viongozi wake lazima wawajibishwe.

Mabadiliko makubwa yanahitajika katika kuiboroesha idara hii. Kwanza kabisa ni kubadilisha sheria ya TISS ili kukipa chombo hicho jukumu la wazi la kufuatilia habari za kijasusi katika utendaji kazi wa idara na wizara mbalimbali za serikali na kuhakikisha kuwa habari hizo zinafanyiwa kazi aidha kwa kutoa taarifa za ndani au kutoa taarifa kwa Kamati ya Usalama ya Bunge na kwa Rais (yaani Rais asitaarifiwe bila Kamati ya Bunge nayo kupatiwa taarifa).

Jingine ambalo naamini linaweza kutusaidia huko mbeleni ni kuhakikisha kuwa idara hiyo haijajaa ndugu, jamaa, na marafiki wa familia za viongozi kwani siyo tu ni hatari lakini maslahi ya watu yanaweza kupiku maslahi ya Taifa. Sijui sasa hivi idara ilivyo lakini kama kuna dalili yoyote ya undugunization basi ni chumvi inayokoleza kushindwa kwa taasisi hiyo kugundua maovu (itaweza vipi kuchimba ofisi anayosimamia baba au mama)!? Hivyo, idara hii irudi kwenye uwezo na uwezo pekee na ianze tena kutafuta watumishi wake hata nje ya jamaa, ndugu, na marafiki. Ninasema hili nikiwa najua mambo fulani jinsi ya watu walivyopata kazi kwenye idara hiyo nyeti.

Pamoja na hayo, idara hii lazima ipewe uwezo wa kujipenyeza katika taasisi mbalimbali kama ilivyokuwa miaka ile ambapo wale watumishi waliipenda nchi kuliko. Leo hii hata waliojipenyeza wengi wanajulikana na siyo siri kama ilivyokuwa zamani. Kama tungekuwa na watu waliojipenyeza Benki Kuu na wanajua jukumu lao sijui kama kina Kagoda wangeweza kuiba na kututeka nyara! Kama tungekuwa na watu wa Usalama Idara ya Madini sijui kama leo tungekuwa na vibangusilo vinavyolia lia!

Hapa simaanishi kujaza watu wa usalama kila kona na kuanza kulifanya Taifa liishi kwenye hali ya wasiwasi bali kuhakikisha kuwa wale wote wanaofanya kazi na serikali au kuingia mikataba na serikali wajue kuna hatari ya kutiwa pingu. Hivyo, watu hao wa Usalama naamini wakati umefika wapewe nguvu ya kupekua na kukamata (search and seizure) ili katika mazingira fulani basi wawe na uwezo wa kutia mbaroni wahujumu wa uchumi wetu kabla hawajatoroka.

La mwisho ambalo naamini linaweza kusaidia idara hii ni mahusiano yake na wananchi wa kawaida katika kukusanya taarifa nyeti. Idara hii lazima ihakikishe inafanya kazi na wananchi kwa ukaribu hata kama kwa siri ili iweze kupata habari nyeti. Suala la Richmond na suala la EPA ni uthibitisho kuwa idara hii iko mbali na wananchi.

Ni nani basi atawaambia wana Usalama wetu kuwa kuna tatizo na wafanye uchunguzi? Hivi IGP Mwema na Mkurugenzi Rashid Othman wanaweza kufanya uchunguzi kuhusu makampuni hayo bila kuomba kibali ikulu? Hivi tulipotekwa mateka wao walifanya nini? Kama Rais asingeamuru wafanye uchunguzi huo wao wangefanya nini? Ni wazi kuwa hawawezi kufanya au kuanzisha uchungu wao wenyewe isipokuwa hadi wapate baraka toka Ikulu ndio maana leo tumetekwa nyara na wao hawana cha kufanya isipokuwa kupiga magoti katika altare ya mafisadi na kujaribu kujitoa mhanga kama bangusilo wa mafisadi. Usalama uamka na kuwa kweli usalama wa Taifa, tusije kuwa na taasisi ya usalama ambayo yenyewe si salama.

Kama tunataka kweli kulinda rasilimali zetu hatuna budi kuimarisha usalama wa Taifa ili usiwe usalama wa wenye matumbo ya Taifa bali usalama wa hazina, mali, na raslimali za Taifa. Kama wale waliodhaminiwa kusimamia usalama wa taifa hili wameshindwa kufanya hivyo, kama waliopo katika safu za usalama wa taifa weshindwa kulinda usalama wa Taifa na badala yake wanahangaika na kutafuta watu wasiowahusu na kushiriki kwenye michezo michafu ya kisiasa basi waachie ngazi tu ili tukodi watu wengine waje watulindie usalama wetu kwani ndugu zetu wenyewe wametuuza!

Vinginevyo, tunapofanya majadiliano na hawa mafisadi waliotuteka ni nani ana nguvu basi? Ni wazi nguvu ya mjadala haiko na timu ya Mwanyika bali na wateka nyara maana katika utekaji nyara mwenye nguvu ni aliyeshika silaha.

Swali ambalo naogopa jibu lake ni kuwa hawa walioiteka nchi na kututishia kuwa tukipega kelele “watailipua” wameshika kitu gani cha thamani kiasi kwamba tunashindwa kuwatia pingu na kufanya majadiliano nao?

Hoja yangu nimejenga, kaditamati natama,
Kwa maneno nilopanga, inahusu usalama,
Mwenye kutaka kupinga, namruhusu kusema,
Usalama wa taifa, mbona kama wa fisadi.

Niandikie: mwanakijiji@klhnews.com
Ujumbe: 248 686 2010
 
Makala hii imetoka kwenye gazeti la Tanzania Daima (hard copy) lakini kwenye mtandao haikuwekwa.

Sasa umeamua kuwafuata watu wa Usalama wa Taifa? Hawa hawaguswi na hawagusiki, walioliteka taifa siyo mafisadi wa EPA.. tumia akili kchwani...Nusura upatie...

asante.
 
Tatizo linabaki pale pale mwanakijiji, hakuna mwanausalama atakayejitokeza na kukuambia kuwa wao waliona uovu huo (kama waliuona), na walishauri na akina EL hawakuwasikiliza......na hatimaye wananchi tukayaona hayo matatizo...........lets say hata wewe mwanakijiji leo hii upewe kazi kulinda kwa kuishauri JF Admin........wasipofuata ushauri wako na kesho yake ukakuta JF imekuwa hacked.........utajisikiaje Ogah akikulaumu kuwa hufanyi kazi yako.........huku mkataba wako unakuambia mawasiliano ni kati ya wewe na JF Admin tu

pili, ukiangalia act yao utagundua kuwa hawana meno, kwa hiyo modification ya ile act ni muhimu ili kuwapa hawa jamaa angalau nguvu za kipolisi pia

tatu, restructuring ni muhimu ili kupunguza undugunization kama ulivyo-point out, kui-modernise na ku-recruit watu walio na good (if not best) qualifications....................na ili kufanikisha ili inabidi kuwachanganya (piga bogi kama JKT vile) i.e. aliyeko polisi mpeleke UWT/PCCB aliye UWT mpeleke PCCB/Polisi na aliyeko PCCB mpeleke UWT/polisi.....wachanganywe na JWTZ pia..........hii itasaidia hata kiutendaji.....asiye-perform atupwe uraiani ktk kazi za kawaida.

Uzuri wa wenzetu kama US, UK....kama CIA/MI6/MI5 walitoa taarifa feki e.g kuhusu Iraq na nuclear weapons.........Bush, Powel walikiri kuwa intelligence waliyopewa haikuwa sahihi kuhusu Iraq

Kuhusu Mwakyembe na kama ti yake kutoonyesha uhusikaji wa TISS.........easy.........wee huoni hata baadhi ya information walinyimwa wasizione....

Sasa leo JK au EL wajitokeze waseme kuwa TISS hawakuwashauri kuhusu UFISADI........then makala yako itakuwa ime-hit right on spot
 
Mkuu nakubaliana na wewe kabisa,
Tulishasema hapo awali kuwa Usalama wa Taifa umeshindwa majumukumu yake na hivyo uvunjwe mara moja na kiundwe chombo kingine chenye machungu na Taifa letu.Usalama wa Taifa si kwamba nao wamekuwa mashabiki wa ufisadi pia nao inaelekea wanaikubali na kunufaika kwa namna moja au nyingine na uwizi wa rasilimali za Taifa letu kipenzi.
Maana tukijiuliza tu kwa haraka haraka kuwa hawa mabwana walikuwa wapi wakati pesa zote zile zikitafunwa pale BOT au ile mikataba ya madini ikisainiwa kule hotelini uingereza au wakati Mkapa na Sumaye wakijipa share kubwa kwenye mradi wa kuzalisha makaa ya mawe ya Kiwira utaona wazi kuwa hawa si Usalama wa Taifa bali ni Usalama wa mafisadi.
Hiki chombo kinafanya kazi tu pale wapinzani wanapofanya maandamano au kwenye chaguzi mbalimbali au wanafunzi pale chuo kikuu wanapogoma au waislamu wanapoandamana!!! Lakini ikija kwenye kufichua uwizi au mipango ya kuhujumu uchumi wa Taifa letu wanakuwa wamelala usingizi wa pono au wanakuwa waoga kama mbweha!!
Nadhani sasa wakati umefika wa kuunda chombo kinachoundwa na watu wenye machungu na Taifa letu,watu wasioogopa kufichua rushwa,uwizi,ubadhirifu wa mali ya umma,chombo chenye kufanya kazi bila ya kuogopa mtu hata kama mtu huyo ni kiongozi au waziri.

-Wembe
 
bahati mbaya sana wakati niko sekondari somo la Historia lilichukuliwa kama ni somo la wanawake.lakini kwa sasa naona kila mtu anapaswa kujikita kwenye historia ya nchi yetu ili kujikwamua hapa tulipokwama!

Mkjj hoja yako ni nzito na yenye kugusa mambo mengi sana ya hatima ya nchi yetu. Usalama wa taifa kwa bahati mbaya walitokana kwanza na vijana wa TANU (TANU Youth League) hao waliwekwa pale kwa kuilinda TANU na viongozi wake dhidi ya wananchi na wenye fikra zinazopingana na TANU

Hata sasa mfumo wa kuchagua wa kujiunga na TISS haujabadilika na mkazo unatiwa kwenye uwezo wa recruits kulinda maslhai ya CCM mtoto wa TANU. kwa hiyo hata kama Taifa likitekwa lakini viongozi wa CCM wakiwa ndiyo watekaji wenyewe au mawakala wa watekaji hakuna kitu TISS watafanya!
 
hata mimi ninaogopa na huu uchambuzi. ni wa kina ila sasa tunaowaambia wanamasikio ila hawasikii.
 
Mzee wa kijijini
Hawa wana intelligisia wameonyesha udhaifu wa hali ya juu sana.
Huyu bosi mpya RO alikuwepo siku nyingi haoni mahali pa kuanzia kuukoa hili taifa?au kwa kuwa aliteuliwa na Rais sasa nchi ni bora liende?Nahisi bado wapo ktk mawazo yale ya zamani ya sheria ya mwaka 1970 wakati tuna chama kimoja na itikadi moja.Pamoja na mifumo ya dunia kubadilika badilika na mingine kuboreshwa kwa maslahi ya Taifa,hawa bado wako sisiem ndo maana kila Msalama wa Mkoa ana kinafasi chake kila mwaka cha kumchukua nduguye au rafiki ajiunge waendelee kunyonga wadanganyika.

Mashushushu badilikeni,mtatumbukiza nchi hii Jehanamu.Mtu akipinga hoja za wazi na za kweli mnaanza kumtia kash kash,mara mmeparamia.Mpo kwa maslahi ya Nchi,tendeni wajibu wenu kwa haki hata kama ni huyo aliyewachagua kakosea mpeni ukweli asije tutumbukiza wote bahari pamoja na nyie mkiwemo maana wote tnasafiri chombo kimoja kiitwacho TZ.
Au hamjui hata hayo majengo mnayokaa hapo Kijito,Mbwe na OSTA n.k ni kodi za hawa mnaowatia kash kash?
 
Uslama wa taifa umebaki kuwa Ulinzi wa viongozi, usalama wa taifa sasa hivi uko very vulnerable, thank God wabongo wengi bado kuamka na kucapitalize kwenye weakness zilizopo!
 
Labda sasa hivi kwa vile wamepata mtu wao kwenye premia basi watatulia na kula huku wakipulizia!

Mie Nadhani tuangalie ni jambo lipi ambalo wameshindwa.tuwasaidie ,TISS wanafanya kazi zao kwa ufanisi na tatizo ni siasa kuingizwa katika suala la TISS.wao hawawezi kulisemea sabbu wapo chini ya ofisi ya Rais.Tatizo ni mfumo wa serikali yetu a sio TISS wala PCCB sababu wanawajibika moja kwa moja kwa Ofisi ya Rais.

tuweke mapendekezo ya nini kifanyike kuhsu hili.MWanakijiji makala yao imetulia.Nimeamua kujiunga na nyie.
angalia ibara ya 5 kifungu cha pili cha THE TANZANIA INTELLIGENCE AND SECURITY SERVICE ACT
(2) It shall not be a function of the Service-
(a) to enforce measures for security; or
(b) to institute surveillance of any person or category of persons by
reason only of his or their involvement in lawful protest, or dissent
in respect of any matter affecting the Constitution, the laws or
the Government of Tanzania.
 
Gembe hicho kifungu cha pili (a) ndicho kinatatiza.. sasa hawa jamaa wanapofanya ulinzi wa Rais au kushiriki katika ulinzi wa Rais wamepata wapi madaraka hayo?
 
Gembe hicho kifungu cha pili (a) ndicho kinatatiza.. sasa hawa jamaa wanapofanya ulinzi wa Rais au kushiriki katika ulinzi wa Rais wamepata wapi madaraka hayo?

Things as usual (mazoea Mzee). Wala siyo kumlinda Rais tu pia Viongozi wa mbio za Mwenge.
 
oh snap.. yaani hata viongozi wa mbio za mwenge!! yaani nimecheka hadi nusura nipaliwe.. great!
 
Mie Nadhani tuangalie ni jambo lipi ambalo wameshindwa.tuwasaidie ,TISS wanafanya kazi zao kwa ufanisi na tatizo ni siasa kuingizwa katika suala la TISS.wao hawawezi kulisemea sabbu wapo chini ya ofisi ya Rais.Tatizo ni mfumo wa serikali yetu a sio TISS wala PCCB sababu wanawajibika moja kwa moja kwa Ofisi ya Rais.

tuweke mapendekezo ya nini kifanyike kuhsu hili.MWanakijiji makala yao imetulia.Nimeamua kujiunga na nyie.
angalia ibara ya 5 kifungu cha pili cha THE TANZANIA INTELLIGENCE AND SECURITY SERVICE ACT
[/LEFT]

Haya mambo tumeyajadili hapa
 
Hapa panahitajika nguvu za kijeshi japo miezi sita ,hakuna cha msali mtume la si hivyo basi mbio za vijiti zitachachamaa na safari hii naona kutakuwa na ule mtindo wa Nchi ya Afrika ya kati ambayo mtu na kaka yake walikuwa wakipinduana kila baada ya miaka mitatu ,yaani anapindua anenda kukaa ulaya baada ya miaka mitatu anarudi na kumpindua ndugu yake mpaka jamaa wameshitukia hilo dili.
 
Mzee mwanakijiji, this is a good one!!

Kwa hiyo kama mambo yenyewe ndio haya...ni balaa. Every move is a check mate.
1. Pinda,after reading this one na habari na facts zingine, kazi ipo..

2. Bi Meghji, one of very few respected x minister, kumnyamazisha kazi imefanyika hapa..

3. Mangufuli,another respected minister, sawa tunaitaji mifugo...lakini serikali ilipofikia hapa huyu jamaa alistahili sehemu nyingine nyeti

4. Sasa tuna kina Mkullo, Masha nk. mbona orodha ni ndefu.

Mchawi ni nani hapa??
 
Mzee mwanakijiji, this is a good one!!

Kwa hiyo kama mambo yenyewe ndio haya...ni balaa. Every move is a check mate.
1. Pinda,after reading this one na habari na facts zingine, kazi ipo..

2. Bi Meghji, one of very few respected x minister, kumnyamazisha kazi imefanyika hapa..

3. Mangufuli,another respected minister, sawa tunaitaji mifugo...lakini serikali ilipofikia hapa huyu jamaa alistahili sehemu nyingine nyeti

4. Sasa tuna kina Mkullo, Masha nk. mbona orodha ni ndefu.

Mchawi ni nani hapa??

Magufuli angekuwa respected Minister si ange toa pendekezo hizo nyumba Zisiuzwe na Hiyo Government Agenycy s ya kushughulikia Nyumba inge zikodisha on commercial rate.
Hivyo zingeweza kujiendesha na kuzi fanyia matengenezo.
 
Kijiji nashukuru kwa hii issue ulioandka hapa, na naomba kuongezea kwamba ili tuendele na tuenzi Professionalism, iwepo kamati ya kusaili viongozi muhimu wa taasisi za umma , kuanzia Jeshi, Polisi na Hata Mabalozi ili kuepuka uswahiba na vinavyo endana na uswahiba.
Jingine ajira katika usalama wa taifa wenyewe ufanyike kwa vigezo vinavyo eleweka kuliko inavyo tokea sasa hivi matokea wafanyakazi wa usalama wa taifa wana watumikia walio waajira, badala ya taifa
 
Wakati mwingine ukimya una maana ya kukubali.

MMK,
Mtalii alikutuhumu hapa kwamba unajihusisha na biashara haramu ya madawa ya kulevya kwenye ile thread ya Mtanzania aliyeuwawa UK, nilikuomba utoe tamko kuhusu tuhuma hizo lakini hadi leo umekaa kimya, I think we should all practise what we are preaching here.

NB:UGAIDI and not UGHAIDI- Apart from that, a very good article I must say, congratulations!I wish I could write like you.
 
1 Reactions
Reply
Back
Top Bottom