Tafsiri Yangu: NCCR-Mageuzi Imenasa Kwenye Gea Ya Reverse!

maggid

JF-Expert Member
Dec 3, 2006
1,084
1,246
Ndugu zangu,


Kuna mengi yametokea katika siku za karibuni. Ni mengi yenye kuhitaji tafsiri. Nitaanza na hili lililomkumba David Kafulila ambalo kimsingi ni mgogoro unaoendelea ndani ya NCCR- Mageuzi.

Katika dunia ya magari ya kizamani usiombe unase kwenye gea ya reverse. Kutoka kwake ni shughuli pevu. NCCR – Mageuzi imenasa kwenye gea ya reverse. Ni gea ya kurudia nyuma.

Ishara zilishaonekana. Kilichotokea ndicho kilichokuwa kinasubiriwa. Kilichotokea ndani ya NCCR- Mageuzi si kwamba chama kimemfukuza mwanachama, bali, kundi moja ndani ya chama limefanikiwa kumfukuza mwanachama mwenzao.


Tumemwona Katibu Mkuu wa NCCR- Mageuzi, Sam Ruhuza akitamka kwenye TBC1, kuwa NCCR- Mageuzi inaona uchungu sana kumpoteza Kafulila. Kwamba NCCR- Mageuzi wanawatunza wabunge wao kama mboni ya jicho. Naam, katika siasa, alichofanya Sam Ruhuza ni kutoa machozi ya mamba.


Na tukaambiwa haraka, kuwa NCCR- Mageuzi sasa imeomba kwenda Ikulu kukutana na JK kuhusiana na Katiba. Tafsiri; Kafulila ndiye aliyekuwa akipanga magogo kwenye njia ya kwenda kwa JK, pale Ikulu ya Magogoni .

Tulidhani , baada ya purukushani ile ya mpaka mwanachama tena mbunge mwandamizi katika chama kunyang'anywa kadi, NCCR- Mageuzi wangeianza safari ya kwenda kwa wanachama na wapenzi wao. Kufanya mikutano ya ndani na nje kuwaeleza kilichotokea na kujibu maswali n a hoja za wanachama na wapenzi wa chama hicho.

Ndugu zangu,
Kinachotokea ndani ya NCCR- Mageuzi ni mgogoro wa ndani ya chama. Inahusu kuwania mamlaka ya uongozi wa chama na inaweza kuunganishwa, kwa mbali, na mbio za urais wa 2015. Hilo la mwisho linahitaji uchambuzi wake.
Na kinachotokea NCCR- Mageuzi ni pigo na huzuni kwa tunaopenda uwepo wa siasa za upinzani wa vyama vingi hapa nchini. Hofu yangu siku zote ni pale itakapotokea, CCM ikaondoka madarakani na kuiacha Chadema ikishika hatamu za dola huku tukiwa na CCM dhaifu kama chama cha upinzani na vyama vingine aina ya NCCR- Mageuzi na CUF vilivyojifia kwa kujitundika vyenyewe vitanzi vya ' CCM B na CCM C'. Kuna ishara zinazonyesha hatari ya kufika huko.

Kwa hapa tulipo, NCCR- Mageuzi inahitajika kama chama kamili na kinachoaminika cha upinzani. Tulipo sasa kila mbunge wa upinzani na hususan kila sauti ya mbunge wa upinzani yenye kujenga ni muhimu sana katika bunge ambalo walio wengi ni Wabunge wa Chama Cha Mapinduzi. David Kafulila alikuwa ni mmoja wa watu hao.


Sam Ruhuza wa NCCR- Mageuzi anajua, kuwa katika siasa tunaamini kila kitu kinawezekana. Hivyo basi, kama hakukufanyika jitihada zozote za kumbakisha ndani ya chama David Kafulila, mwanasiasa huwezi kusimama na kusema unaona uchungu kumpoteza mbunge wenu.


Na hapa tunajifunza, kuwa wakati umefika wa kuangalia upya taratibu za kuwapata na kuwavua ubunge wabunge wetu. Umefika wakati tuweke katika Katiba yetu mpya. Kuwa mbunge aliyechaguliwa na wananchi , hata kama atafukuzwa uanachama wa chama chake, bado atabaki kuwa ' Mbunge Pori' mpaka uchaguzi utakaofuata. Kwamba hatutakuwa na uchaguzi mdogo.


Kinahitajika nini kwa sasa NCCR- Mageuzi?



Usuluhishi, usuluhishi, usuluhishi. Ni usuluhishi utakaopelekea Kafulila kumaliza muda wake wa Ubunge. Na Msajili wa Vyama John Tendwa hawezi tu kusimama pembeni na kuongea na media kwamba kufukazana kwenye vyama ni ufisadi. Ndio, Tendwa hawezi kuingilia mambo ya ndani ya NCCR-Mageuzi, lakini, kama mlezi wa vyama vya siasa, Tendwa anaweza kushiriki kazi ya usuluhishi. Pamoja na mgogoro uliopo kati ya David na James ifike mahali wawili hao wasaidiwe kutanguliza hekima. Kwamba wawili hao , James Mbatia na David Kafulila, waishi kwa kuikubali hali hadi 2015. Maana, baada ya hapo, kama hawatapata muafaka wa kwao wenyewe na wa kirafiki, basi, mmoja wao lazima atoke zizini.


Na kikubwa, NCCR- Mageuzi watangulize maslahi ya taifa. Wakae sasa kama chama. Watambue kuwa chama kina mgogoro mkubwa. Kama Tendwa atashindwa kuwasaidia, waombe mtu au watu wenye hekima waende wakafanye kazi ya usuluhishi. Ndio, David na James wanahitaji kusuluhishwa. Maana, kikubwa hapa ni kuwafikiria pia wananchi wa Kigoma Kusini wenye kuhitaji uwakilishi wa mbunge wao waliomchagua.


Nape Nnauye Naye?

Alianza vema kuzichanga karata za kisiasa kwa kinachotokea NCCR- Mageuzi. Gazeti Tanzania Daima linamnukuu Nape akisema kuwa; " Sipendi tabia ya kuwafukuza wanasiasa wanaohoji mambo na hasa wakiwa vijana. " Hapo Nape alicheza haswa karata za siasa huku akiligeukia kundi kubwa la vijana waliokipa mgongo chama chake.


Lakini, kama ilivyo mgema ukimsifia sana. Nape anamalizia vibaya kuchanga karata zake za siasa kwa kusema; " Nakishukuru Chama cha NCCR- Mageuzi kwa kuturudishia jimbo letu, nina uhakika wa jimbo hilo kurudi CCM".- (Nape Nnauye, Tanzania Daima, Desemba 20, 2011.)


Ni kauli hiyo ya Nape inayokinzana na kauli yake ya ; " Nchi kwanza, Chama Baadae". Nape angepaswa kufahamu, kuwa kwa NCCR- Mageuzi kumfukuza Kafulila kwa sasa ni suala lisilo na maslahi kwa nchi. Angesubiri sana kuzungumzia chama chake kitakavyonufaika na jambo hilo.

Ni tafsiri yangu tu.

Maggid Mjengwa,

Iringa
Jumatano, Desema 21, 2011
Mjengwa Blog::Habari,Picha,Matangazo
 
Vyama vingine vya siasa vimekaa kama magenge ya wahguni au vijiwe vya wapiga soga na waganga njaa.
 
huu uchambuzi upo finyu kwa mtu wa hadhi yako.
Tendwa hukumwandika ipasavyo kwani analalamika wakati KATIBA ZA VYAMA ANAZO KABATINI tena kabla hajasajili.
Tendwa angekuwa mwazi kwa kuwaeleza wanainchi kilichotokea NCCR ni sahihi 100% kwa mujibu wa KATIBA ya sasa kwa hiyo ni serikali ya CCM iliyopora ushindi wa kesi ya Mtikila ya mgombea binafsi.
kwa hiyo tendwa alalamikie KATIBA na siyo NCCR
 
huu uchambuzi upo finyu kwa mtu wa hadhi yako.
Tendwa hukumwandika ipasavyo kwani analalamika wakati KATIBA ZA VYAMA ANAZO KABATINI tena kabla hajasajili.
Tendwa angekuwa mwazi kwa kuwaeleza wanainchi kilichotokea NCCR ni sahihi 100% kwa mujibu wa KATIBA ya sasa kwa hiyo ni serikali ya CCM iliyopora ushindi wa kesi ya Mtikila ya mgombea binafsi.
kwa hiyo tendwa alalamikie KATIBA na siyo NCCR

Marytina,
Asante sana kwa maoni yako. Hivi ni wewe Marytina uliyekuwa ukinitukana jana na leo unasema mimi ni mtu mwenye hadhi. Mtu mzima hutafakari kabla ya kuandika na si kinyume chake.
Maggid,
Iringa.
 
Good work Majid, kufa kwa NCCR na vyama vingine ni pigo kwa taifa hili.....sipati picha tungekuwa na chadema tatu!!
 
Marytina,
Asante sana kwa maoni yako. Hivi ni wewe Marytina uliyekuwa ukinitukana jana na leo unasema mimi ni mtu mwenye hadhi. Mtu mzima hutafakari kabla ya kuandika na si kinyume chake.
Maggid,
Iringa.

Take it easy Dude,
nimekubaliana na uchambuzi wako..
 
Good work Majid, kufa kwa NCCR na vyama vingine ni pigo kwa taifa hili.....sipati picha tungekuwa na chadema tatu!!

Exactly mkuu, i wish sana vyama vya Upinzani vyote viwe na nguvu na lengo moja.
Inakera pale unapoona Upinzani wakivuana nguo kwa hoja ambazo kimsingi walitakiwa wasimame pamoja..
 
Marytina,
Asante sana kwa maoni yako. Hivi ni wewe Marytina uliyekuwa ukinitukana jana na leo unasema mimi ni mtu mwenye hadhi. Mtu mzima hutafakari kabla ya kuandika na si kinyume chake.
Maggid,
Iringa.

Hasira!!
 
Marytina,
Asante sana kwa maoni yako. Hivi ni wewe Marytina uliyekuwa ukinitukana jana na leo unasema mimi ni mtu mwenye hadhi. Mtu mzima hutafakari kabla ya kuandika na si kinyume chake.
Maggid,
Iringa.

jana ??????sidhani
nilitumia lugha khali dhidi yako ulipoleta kwa mara ya kwanza UPIGAJI KURA WA WABUNGE VIJANA
 
jana ??????sidhani
nilitumia lugha khali dhidi yako ulipoleta kwa mara ya kwanza UPIGAJI KURA WA WABUNGE VIJANA

Marytina, umeshasahau, mapema hivi. Mimi nilishakusamehe kwa matusi yako kwangu. Nilishangaa tu leo kuniita mtu mwenye hadhi. Nashukuru kuwa u mwepesi wa kusahau. Ni sifa njema hiyo kwa mwanadamu.
Maggid
 
huu uchambuzi upo finyu kwa mtu wa hadhi yako.
Tendwa hukumwandika ipasavyo kwani analalamika wakati KATIBA ZA VYAMA ANAZO KABATINI tena kabla hajasajili.
Tendwa angekuwa mwazi kwa kuwaeleza wanainchi kilichotokea NCCR ni sahihi 100% kwa mujibu wa KATIBA ya sasa kwa hiyo ni serikali ya CCM iliyopora ushindi wa kesi ya Mtikila ya mgombea binafsi.
kwa hiyo tendwa alalamikie KATIBA na siyo NCCR
Although I hate what you have just vomited, but I will defend to death you right of vomiting it.
Maggid is very right, hii kitu inatakiwa ipingwe na wapenda haki. What Mbatia and Co. did is hindrance to right of expression and free speech within the party. Adhabu iliyotolewa ni kubwa mno, nahisi kuna wivu, chuki ukizingatia baadhi ya viongozi wa NCCR waliukosa ubunge.
 
E bwana kumbe NCCR wabunge wake wote wanatoka kigoma? maskini! wamekwisha kisiasa! Mbatia na genge lake walifanya ujinga wa hali ya juu!
 
Kaka Maggid, kwa namna fulani nakubaliana na wewe na kwa upande mwingine napingana na hoja zako kabisaa, Hebu fikiria mara mbili au zaidi; Lengo la kila chama ni kuwa kifanye kazi zake ili kufikia makusudio yake, ndani ya nccr kafulila amedaiwa kukichafua chama chake kuwa ni cha ki ccm ccm na hivyo hakifai,anakitukana kichaka kilichomuhifadhi. Unategemea nini maggid? Binafsi nilitegemea utueleze kafulila na wenzake kafukuzwa kwa nini na siyo ushabiki wako kwa kafulila,unadhihirisha wazi kuwa wewe ni shabiki wa kafulila,kwa nini? kwa sababu hutaki kujihusisha na makosa yaliyomfukuzisha kafulila na badala yake unataka watu waamini kuwa kafulila eti kaonewa, kaonewa namna gani wakati amekiuka sheria na kanuni za chama chake? Hivi wewe hata kama una matatizo na mkeo halafu anatoka kwenda kuyaeleza na kukukashifu nje ya ndoa yako na tena ya kukuzushia ili kukidhi malengo yake utajisikiaje? Hicho ndicho kulicomgharimu kfulila na wenzake? Alionywa na kushauliwa zaidi ya mara ishirini kuchana na tabia ya kwenda kuzungumzia mambo ya chama nje ya chama tena ambayo ni ya kizushi yaani ya uwongo, hakusikia akaona kuwa yeye ni bora kuliko wengine. Kaka,najua unampenda kafulila lakini katika hili kakosea na hastahili kutetewa kwa kuwapotosha watu kama unavyofanya hapa. Sasa nakueleza kuwa kafulila alipoulizwa juu ya kashfa zote alizombebesha mbatia kwenye vyombo vya habari alisema kuwa Mbatia hana hatia naaendelee na uenyekiti,kwa kinywa chake alizungumza, wewe unamtetea,kwa lipi kaka?Punguza ushabiki na ujaribu kuwa focussed na kuzungumza ukweli. Sasa kama alikiri kuwa madai yote baada ya kuuliza kuwa ni ya uwongo, na huku ikizingatiwa kuwa alishaonywa (kafulila) asirudie tena kwenda kuzungumza mambo ya chama na ya uongo tena yanayokichafua chama nje ya taratibu za chama,kwa nini unataka asiadhibiwe kama alivyoadhibiwa? Au unataka kutuambia kuwa watu aina ya kaufalila wasiadhibiwe eti kwa sababu ni watu maarufu? Hakika itakuwa hakuna tofauti na ccm, Ni lazima tujifunze kuwashughurikia watovu wa nidhasmu bila kujali nani ni nani, hii ni kwa sababu haki haipaswi kuwa ya kibaguzi. Kilichomfuzisha kafulila ni kukiuka onyo na au karipio la chama la kukichafua chama nje ya chama husika jambo linalopelekea chama kishindwe kuaminika.

GHARAMA ZA MATUSI ua KASHFA ZA Kafulila NA WENZAKE KWA nccr ni kubwa kuliko Kuwaacha ndani ya chama;
Napenda kukuthibishia kuwa kwa mwaka mzima mzima sasa nccr kimeshindwa kufanya kazi zake barabara kwa sababu ya migogoro ya kafulila na wenzake wachache ndani ya nccr, lakini pia kafulila amekuwa msemaji tu ambaye siyo mtekelezaji wa yale anayokiahidi chama kilichomtimua. Hivi ukifanya analysis huoni kuwa ni hasara kubwa sana kwa chama kusindwa kufanya kazi zake kwa mwaka mzima kwa sababu ya kushughulikia mgogoro ulioanzishwa na kafulila halafu alipohojiwa na NEC ya nccr akasema kuwa Mbatia hana hatia na kashfa zote alikuwa akizitoa hazima msingi wowote tena kwa maandishi siku hiyo alipofukuzwa uanachama? YAANI UNATAKA CHAMA KIKAE MWAKA AU MIAKA KIKISHUGHURIKIA MGOGORO WA KAFULILA!??
hata hivyo naona NCCR kuwa chama kilichokomaa kisiasa kuliko vyama vingine hapa nchini kikifuatiwa na CDM, kwa sababu kina wabunge wachache lakini hakikusita kufanya maamuzi magumu ya kumvua ubunge kafulila ili kujenga nidhamu miongonimwake. Usidhani ni nidhamu ya woga, la hasha!kinataka watu wawe na Discipline na siyo vinginevyo, Kmbuka kuwa watu wanalia kila siku sheria zinavunjwa zinavunjwa, sasa leo imetokea kafulila amekamatwa pabaya tena kwa haki,lakini watu mnajifanya vipofu eti hamuoni kafulila kakosea, kasome katiba na kanuni za nccr utagundua kuwa kafulila kakosea na kama unampenda utamshauri next time popote aepuke tabia ya kujifanya yeye anajua kila kitu na kuwapuuza wenzake hadi kuwakashifu kwa kuwaonea, muuleze kuwa itamgharimu sana, Mimi ni miongoni mwa mashabiki wa kafulila, nimefuatilia hadi chamani nccr kujua ukweli huu nikagundua kakosea kwa mujibu wa katiba na kanuni za chama chao,tena ilipaswa wawe wamemfukuza mapema lakini ni wavumilivu mnooooooooo. Kweli ni msemaji kafulila lakini hapa alikosea chama chake, na hii inapswa kuigwa na vyama vingine ili kuhakikisha tunajenga nchi yenye waadilifu wa hali ya juu, nchi yetu inabaki nyuma kimaendeleo kwa sababu ya kuoneana haya au aibu, hatuwezi kuendelea ni lazima tuache kuoneana aibu,sawa maggid na wengineo? Tusiangalie uzuri wa kafulila, tuangalie na mabaya yake,
Tatizo kubwa watu wanaharaka ya kwenda ikulu na kucukua dola. Naona nccr wao wanataka kujenga taasisi ya itakayokuwa na watu waadilifu na hivyo hawana haraka ya kwenda ikulu, na hili ndilo muhimu sana badala unafanikiwa kuingia ikulu na kucukua dola halafu unakuwa na rasilimali watu iliyo ya hovyo,umefanya nini yale yale kama ya ccm kwa hivi sasa, Tuache haraka na kubeza maamuzi sahihi ya nccr mageuzi kwa sababu ya ushabiki.

Nakaribisha mawazo tujadili
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom