Mama Amon
JF-Expert Member
- Mar 30, 2018
- 2,021
- 2,477
Dk. Ayub Chacha Rioba, Mkrugenzi Mtendaji wa TBC
Kwa kuzingatia matakwa ya katiba ya Tanzania, swali hapo juu linatokana na bonde la ufa lililopo kati ya yale ninayoyaona, na yale ninayoyatarajia kuhusiana na uendeshaji wa TBC. Kwa hiyo, kwa kuzingatia mfumo wa hoja yenye muundo wa OPHETAR (Observations, Puzzles, Hypothsis, Theory, Action, and Rebuttals), ninajadili haya:
- Niliyoyaona TBC1,
- Matarajio kwa mujibu wa Katiba,
- Uhalisia wa mambo,
- kitendawili cha mpasuko kati ya matarajio na uhalisia,
- pendekezo kuhusu jawapo la kitendawili hiki,
- Ushahidi unaoweza kujibu kitendawili hiki,
- Mapendekezo kuhusu nadharia sahihi ya mtazamo wa kisera,
- Mapingamizi tarajiwa na
- Majibu ya mapingamizi hayo.
Tangu 15 Novemba 2020 nilipoikosoa TBC katika namna inavyotekeleza dhima yake ya kuelimisha umma juu ya COVID19 kwa kuzingatia misingi ya ukweli, ukweli wote na ukweli pekee, leo tena, tarehe 21 Mei 2021, nimeona matukio mawili yasiyo ya kawaida.
- Asubuhi kabla ya kipindi cha Bunge cha mswali na majibu TBC1 walirusha kipindi cha "Madrasa" kilichokuwa na ujumbe unaotembea kwa upande wa chini ukisomeka "Mashindano ya Kuhifadhi Kurani Tukufu kwa Waislamu Wanawake Yameandaliwa na Taasisi ya Kiislam ya African Relief Foundation." Kurani zilizokuwa zinasomwa zimeandikwa kwa Kiarabu.
- Mchana, mara tu baada ya matangazo ya Maadhimisho ya miaka 40 ya kuanzishwa kwa SADC, ambako Ayub Rioba alikuwa mwongozaji, kilifuata kipindi ncha swala ya Kiislamu. Swala ilianza kwa maelezo ya Kiarabu kwa dakika zipatazo tano.
- Kila alfajiri madhehebu ya dini tofauti hupewa muda wa kusoma sala ya asubuhi.
- Kila usiku wa kati, kabla ya saa sita, madhehebu ya dini tofauti hupewa muda wa kusoma sala ya kufunga siku.
- Kila Jumapili pia, madhehebu ya dini tofauti hupewa muda wa kusoma ibada za Jumapili.
Na ibara ya 4(1) inasema kuwa shughuli zote za Mamlaka ya Nchi katika Jamhuri ya Muungano zitatekelezwa na kudhibitiwa na vyombo vyenye "mamlaka ya utendaji, ... mamlaka ya kutekeleza utoaji haki, ... na mamlaka ya kutunga sheria." Yaani, Serikali, Bunge, na Mahakama.
Hivyo, matarajio yangu ni kwamba, kwa kuwa TBC ni mali inayoendeshwa kwa kodi ya umma chini ya usimamizi wa serikali isiyofungamana na dini yoyote, basi yafuatayo yanapaswa kuonekana:
- Programu zenye sura ya kitaifa katika ngazi ya maudhui
- Programu zenye sura ya kitaifa katika ngazi ya lugha
- Programu zenye sura ya kisekta katika ngazi ya maudhui
- Programu zenye sura ya kisekta katika ngazi ya lugha
Pia, nafahamu kuwa, dini nyingi tayari zinavyo vyombo vyake vya habari kwa ajili ya kuendesha shughuli zake. Kanisa Katoliki wana Tumaini TV, KKKT wana Upendo TV, Waislam wana Iman TV, Wapagani wa "Ramli TV," nk
Nakumbuka kuwa, kwa sehemu kubwa, sala nyingi za madhehebu ya KiIslamu zinatumia lugha ya Kiarabu, jambo ambalo linakiuka sera ya kujenga umoja wa kitaifa kwa kutumia lugha ya Taifa la Tanzania.
Hata ibada kadhaa na litania nyingi za Kikristo zinasomwa kwa lugha ya Kilatini ambayo sio lugha ya Taifa la Tanzania.
Nakumbuka kuna wakati Kardinali pengo alikuwa anaitwa na wazee wetu wa kule Mwenge Parokiani, Dar es Salaam, ili akawaendeshee ibada kwa lugha ya Kilatini, kama walivyokuwa wamezoea zamani, kabla Kanisa Katoliki halijatunga sera ya kuendesha ibada kwa Kiswahili na kimila.
Kwa hiyo, katika mazingira ya sasa, yafuatayo ni matarajio yangu:
- Kanisa Katoliki waendeshe programu zao za kisekta kupitia Tumaini TV,
- KKKT waendeshe programu zao za kisekta kupitia Upendo TV,
- Waislam waendeshe programu zao za kisekta kupitia Iman TV,
- Wapagani waendesha programu zao za kisekta kupitia "Ramli TV," nk
- Kanisa Katoliki wanaendesha programu zao za kisekta kupitia TBC1,
- KKKT wanaendesha programu zao za kisekta kupitia TBC1,
- Waislam wanaendesha programu zao za kisekta kupitia TBC1,
- Shughuli za Bunge zinaanza kwa kusoma dua kwa "Mola",
- Viapo vya watumishi wa umma vinamaliziwa kwa maneno "Ewe Mwenyezi Mungu Nisaidie," wakati Katiba ya nchi haitambui neno "Mungu."
Kwa sababu ya maelezo hapo juu, sasa ni wazi kwamba kuna bonde la ufa kati ya matarajio na uhalilsia kama ifuatavyo:
- Wakati Katiba ya Tanzania (1977), ibara ya 4(1) na 19(2) zinasema kuwa, shughuli na uendeshaji wa jumuiya za dini zitakuwa nje ya shughuli za mamlaka ya nchi, programu za vyombo vya dola kama vile TBC zinaonyesha kuwa shughuli na uendeshaji wa jumuiya za dini" ni sehemu ya shughuli za mamlaka ya nchi;
- Wakati Katiba ya Tanzania (1977), ibara ya 4(1) na 19(2) zinasema kuwa, shughuli na uendeshaji wa jumuiya za dini zitakuwa nje ya shughuli za mamlaka ya nchi, programu za vyombo vya dola kama vile matukio ya kuwaapisha viongozi wa umma zinaonyesha kuwa shughuli na uendeshaji wa jumuiya za dini ni sehemu ya shughuli za mamlaka ya nchi;
- Na wakati Katiba ya Tanzania (1977), ibara ya 4(1) na 19(2) zinasema kuwa, shughuli na uendeshaji wa jumuiya za dini zitakuwa nje ya shughuli za mamlaka ya nchi, programu za vyombo vya dola kama vile Bunge zinaonyesha kuwa shughuli za dini, kama vile kusoma dua, ni sehemu ya shughuli za mamlaka ya nchi.
Ni muhimu swali hili lijibiwe ili tujichunguze kama vyombo vya dola vinakweza maslahi ya vikundi na kutweza maslahi ya pamoja kitaifa, au vinginevyo.
Mapendekezo kuhusu sababu za mpasuko husika (Hypothesis)
Napendekeza kwamba ni kosa la kikatiba kutumia kodi ya raia asiye na dini kuhudumia taasisi za kidini. Ni kama ambavyo ni kosa kutumia kodi ya mtu asiye na chama cha siasa kutoa ruzuku kwa chama cha siasa. Kuna tatizo hapo.
Na ni maoni yangu kwamba, kosa hili linafanyika kwa kuwa Tanzania kuna ombwe la kisera na kisheria kuhusu namna bora ya kutenganisha dini na dola
Kutafuta ushahidi unaoweza kueleza kitendawili hiki (Evidence collection)
Nakumbuka kusoma kitabu kinachosema kwamba, kote duniani, sera za kutenganisha dini na dola hugawanyika katika sehemu mbili:
- Sera zinazofuata mtindo wa Kimarekani.
- Sera zinazofuata mtindo wa Kijerumani.
Sera zinazofuata mtindo wa KIjerumani. Hapa, serikali haiyapigi kisogo masuala yote ya dini, kwani kuna senti fulani ya mlipa kodi inatumika kufadhili taasisi za kidini. Kwa mfano, huko Ujerumani, mfumo wa "TRA" yao unatumika kukusanya sadaka kutoka kwa waumini ambao ni waajiriwa, halafu sadaka hiyo inakabidhiwa kwa makanisa yaliyosajili waumini wao. Lakini, mfumo huu unabagua baadhi ya madhehebu ya kidini.
Hapa Tanzania, hakuna sheria wala sera rasmi yenye kutoa mwongozo juu ya kutafsiri ibara ya 4(1), 19(1) na 19(2) ili kila mtu ajue lini, wapi na kwa vipi atenganishe dini na dola.
Mapendekezo kuhusu nadharia mwafaka ya kisera (Theorising)
Mpaka hapa, swali lililo mbele yetu ni hili hapa:
Ni kwa jinsi gani kundi la watu waliozaliwa wakiwa na usawa katika ngazi ya urazini na uhuru wa kuchagua linaweza kujipanga na kuendelea kuishi kama Taifa lenye umoja japokuwa kuna ukweli usiopingika kwamba ndani ya Taifa hilo kuna tofauti za maumbile, mitazamo ya kisayansi, kiteolojia, kisiasa, kifalsafa na kimaadili?
Kihistoria, kuna majibu mawili kwa swali hili. Jawabu la kwanza linahusu utaratibu wa mpito wenye kutumika kulingana na mazingira yaliyopo. Huu ni utaratibu wa kupuuzia uvumilivu pale hali inaporuhusu na kusisitiza uvumilivu pale hali inapolazimisha hivyo . Yaani: “intolerance whenever possible” and “tolerance whenever necessary,” yaani, "modus vivend doctrine."
Na jawabu la pili linaendana na ujenzi wa misingi ya umoja wa Taifa ambalo linaunganishwa na majukwaa ya umma wote (civic spaces), ambako kanuni pekee inayotumika kuleta umoja ni jumla ya tunu zinazoendana na urazini wa umma (public reason).
Kwa mujibu wa kanuni ya urazini wa umma hoja ya kitaifa inakuwa ni hoja mtambuka kwa kuwa inakubalika kisayansi, kifalsafa, kiteolojia na kihistoria. Kwa mujibu wa wanazuoni huu ni mwafaka wa kitaifa, yaani "overlapping consensus doctrine."
Rex Martin (2015), katika makala yake, “Overlapping consensus,” kama lilivyochapishwa katika kitabu kilichohaririwa na Jon Mandle akishirikiana na David A. Reidy, “The Cambridge Rawls lexicon (UK: Cambridge Universirt Press; 2015, p.588-89),” ameeleza vizuri sana jambo hili.
Kwa sababu ya ushahidi uliotajwa hapo juu, sasa mambo yafuatayo yanafuata kimantiki:
Sera zinazotenganisha dini na dola kwa kufuata mtindo wa Kijerumani zina ubaguzi, kwani, madhehebu ya dini yaliyosajiliwa na serikali huwa mengi zaidi ya 500 kiasi kwamba, yote hayawezi kupata fursa sawa za kiserikali. Hizi zinaendana na "modus vivend doctrine"
Sera zinazotenganisha dini na dola kwa kufuata mtindo wa Kimarekani hazina ubaguzi, kwani, kwa sababu ya serikali kuzipiga kisogo dini zote, inakuwa imezitendea kwa usawa dini zote. Hizi zinaendana na "overlapping consensus doctrine."
Mapendekezo kuhusu namna ya kusonga mbele (Action recommended)
Hivyo basi, kwa kuwa Sera zinazotenganisha dini na dola kwa kufuata mtindo wa Kijerumani zina ubaguzi; na kwa kuwa sera zinazotenganisha dini na dola kwa kufuata mtindo wa Kimarekani hazina ubaguzi, napendekeza yafuatayo:
- Kwamba, programu zote za kidini, ambazo kwa sababu hiyo ni programu za kisekta ziondolewe katika TBC;
- Kwamba, programu zote za kidini, ambazo kwa sababu hiyo ni programu za kisekta ziendeshwe kupitia vituo binafsi vya madhehebu ya kidini;
- Kwamba, TBC ijielekeze katika programu zenye kujenga umoja wa kitaifa kwa kueneza lugha ya Taifa, na sio lugha nyinginezo;
- Kwamba, utaratibu wa kusoma dua mwanzoni mwa shughuli za Bunge ufutwe.
- Kwamba, Bunge litunge sheria inayotoa mwongozo rasmi kuhusu sera ya kutenganisha dini na dola hapa nchini Tanzania. Yaweza kuitwa "The Separation of Religion and State Act of 2021."
Kuna pingamizi moja kuu naona laweza kuibuka dhidi ya hoja yangu hapo juu. Linahusu tafsiri potofu ya tunu ya uvumilivu. Kwa hiyo nalijibu mapema kabla halijaibuka.
Kuna watu watasema kuwa kwa sababu ya tunu ya uvumilivu tunayoikubali wote, basi inabidi haya yafanyike:
- Kwamba, madhehebu tofauti yapeane zamu ya kuhubiri katika vyombo vya habari vya Taifa;
- Kwamba, madhehebu tofauti yapeane zamu ya kuhubiri katika vituo vya mabasi barabarani;
- Kwamba, madhehebu tofauti yapeane zamu ya kuhubiri katika mabasi ya wasafiri;
- Kwamba, madhehebu tofauti yapeane zamu ya kuhubiri katika darasa lenye wanafunzi wale wale ndani ya shule moja;
- Kwamba, madhehebu tofauti yapeane zamu ya kufungua mkutano ule ule wa kiserikali;
- Kwamba, madhehebu tofauti yapeane zamu ya kusoma dua ya kufungua vikao vya Bunge;
- Na mifano mingine kama hiyo;
Napinga tafsiri hii ya neno "uvumilivu" kwa sababu ya maelezo yafuatayo, na ambayo yanakubaliana na kile ambacho tumekuwa tunafanya katika baadhi ya sehemu za maisha yetu ya kila siku.
Fikiria kwamba, kuna mtu A anayeamini kuwa kitendo X ni haramu kidini, na hivyo kuamini kuwa kitendo hiki kinapaswa kupingwa.
Lakini, kwa mujibu wa tunu ya uvumilivu, mtu A anatakiwa kuamini kwamba ni sahihi kujizuia kupinga kitendo X, endapo kitafanywa na mtu baki B, kwa sababu kitendo hicho ni miongoni mwa matendo yanayopaswa kuvumiliwa na wanajamii.
Kwa hiyo, uamuzi wa mtu A kuvumilia kitendo cha mtu B unaonekana kumaanisha kwamba, mtu A anakubali imani kwamba “X ni kitendo kinachopaswa kupingwa” na anakubali imani kwamba “X ni kitendo kisichopaswa kupingwa,” ambazo ni imani mbili zinazopingana kimantiki.
Hata hivyo, kama tunu ya uvumilivu ikitafsiriwa vizuri haitaonekana kuwa na mkanganyiko huu wa kimantiki. Kwa mujibu wa tafsiri sahihi ya tunu ya uvumilivu, kukubalika na kukataliwa kwa kitendo X kunategemea mazingira ya kitendo hicho.
Yaani, uvumilivu wa mtu A kuhusu imani X, katika mazingira M, haumaanishi kwamba mtu A anapaswa kuonyesha uvumilivu kuhusu imani X, katika kila mazingira mbali na mazingira M.
Ndio kusema kwamba, kitendo X sio haramu kila wakati, kila mahali na kwa kila mtendaji. Yaani, wema wa kitendo X, au ubaya wake, unategenea mazingira ambako kitendi hicho kitafanyika.
Kwa hiyo, tafsiri sahihi ya tunu ya uvumilivu iko hivi: fikiria kwamba kuna mtu A anayemaini kuwa kitendo X ni haramu kidini, na hivyo kuamini kuwa kitendo hiki kinapaswa kupingwa katika mazingira M.
Lakini, kwa mujibu wa tunu ya uvumilivu, mtu A anatakiwa kuamini kwamba ni sahihi kujizuia kupinga kitendo X, endapo kitafanywa na mtu baki B, kwa sababu kitendi hicho ni miongoni mwa matendo yanayopaswa kuvumiliwa katika mazingira N.
Kwa hiyo, uamuzi wa mtu A kuvumilia kitendo cha mtu B unamaanisha kwamba, mtu A anakubali imani kwamba “X ni kitendo kinachopaswa kupingwa” katika mazingira M na anakubali imani kwamba “X ni kitendo kisichopaswa kupingwa,” katika mazingira N.
Ukitumia somo hili katika mjadala wa sasa, maana yake ni hii: “X ni kitendo kinachopaswa kupingwa” katika mazingira M na anakubali imani kwamba “X ni kitendo kisichopaswa kupingwa,” katika mazingira N, ambapo:
- X ni kitendo cha kuendesha programu za kisekta katika TV
- M ni mazingira yanayohusisha TV ya Taifa TBC
- N ni mazingira yanayohusisha TV ya taasisi ya kidini kama vile Tumaini TV, Iman TV, Upendo TV, nk.
- Ambapo, mazingira M na mazingira N yote yanapatikana ndani ya nchi moja ya Tanzania.
Katika Taifa moja, lenye mseto wa kidini, lazima kuwepo na sehemu za umma mpana ambako programu za kisekta hazikanyagi. Maeneo hayo ni pamoja na:
- Vyombo vya habari vya Taifa (Hapa, lugha ya Taifa ni alama na nyenzio ya kujenga Utaifa)
- Shule za Taifa (Hapa sare ni alama na nyenzio ya kujenga Utaifa)
- Vyuo vya Taifa (Hapa mtaala mmoja ni alama na nyenzio ya kujenga Utaifa)
- Vituo vya usafiri wa umma (Hapa vituo vya mabasi ni mfano wa uwepo wa maslahi ya pamoja Kitaifa)
- Maktaba za Taifa Hapa vitabu mmoja ni mfano wa uwepo wa maslahi ya pamoja Kitaifa)
- Barabara za Taifa (Hapa barabara ni mfano wa uwepo wa maslahi ya pamoja Kitaifa)
- Na kadhalika