Spika Sitta asema amepata nguvu katika mapambano dhidi ya mafisadi

kasyabone tall

JF-Expert Member
Sep 13, 2009
254
59
Na Ramadhan Semtawa
SPIKA wa Bunge, Samuel Sitta amesema kitendo cha wahisani na Watanzania wengine kumuunga mkono katika uendeshaji vikao vya chombo hicho cha wawakilishi wa wananchi kimempa nguvu zaidi.

Mwakilishi mkazi wa Shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), Alain Noudehou alisema wakati wa maadhimisho ya Siku ya Demokrasia Duniani kuwa shirika lake linampongeza kiongozi huyo wa Bunge kwa jinsi anavyosimamia demokrasi na vita ya ufisadi.

Na jana Spika Sitta alionekana kufurahishwa na msimamo huo wa UN akisema "nimepata nguvu na faraja".

Sitta alifafanua kwamba mtu anapokuwa katika vita na baadaye akaungwa mkono, hujisikia kufarijika sana.

"Kusema changamoto, mimi sioni kama kuna changamoto katika uungwaji mkono huo. Ninachokiona kikubwa ni kwamba, nimefarijika na kupata nguvu zaidi," alisema Sitta ambaye alikuwa mkurugenzi wa kituo cha uwekezaji na ambaye kwa sasa ni mbunge wa Urambo Mashariki.

Kiongozi huyo wa moja ya mihimili mitatu ya dola alifafanua kwamba sifa, nguvu na faraja hiyo inagusa bunge zima ambalo yeye analisimamia kuhakikisha linafuata kanuni na taratibu.

"Ninachosisitiza ni kwamba nimefarijika na kupata nguvu zaidi," alisema.

Sitta alisema tamko hilo la UN ni ishara njema katika usimamizi wa misingi ya utawala bora na kusisitiza kuwa ataendelea kuendesha bunge kwa kusimamia kanuni.

Sitta aliripotiwa kwenye kwenye kiti moto wakati wa kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM (Nec) mjini Dodoma, akituhumiwa kuendesha Bunge kwa kuruhusu mijadala inayokichafua chama na serikali; kupendelea kikundi kidogo cha wabunge katika kutoa nafasi za kuchangia mijadala na kuendesha bunge bila ya kufuata mfumo wa Bunge la Uingereza (westminster) ambalo haliruhusu wabunge wa chama tawala kuikosoa serikali.

Wajumbe wa Nec walidiriki hata kutaka mbunge huyo wa Urambo Mashariki anyanganywe kadi ya uanachama wa CCM na hivyo kupoteza ubunge wake na kiti cha uspika, kabla ya Rais Jakaya Kikwete kumnusuru.

Kikwete pia ndiye aliyetoa ahueni kwa Sitta na wabunge ambao wanajinadi kuwa makamanda wa ufisadi alipoeleza kwenye mazungumzo yake na wananchi kuwa wabunge wanaopambana katika vita hiyo wanaisaidia serikali kujikosoa, kauli ambayo inaonekana hata kubadili msimamo wa CCM.

Sitta aliieleza Mwananchi kuwa wananchi wanaridhishwa na uendeshaji wake wa chombo hicho na michango ya wabunge wengine.

"Wapo Watanzania wanaridhishwa na ninachofanya pamoja na wabunge wengine, wana matumani. Jambo la msingi ni kwamba nitasimamia kanununi," alisisitiza Sitta.

"Maana ukiona unafanya kazi halafu hata nchi wahisani zinakuunga mkono na watu wako katika nchi, ujue ni ishara njema na faraja kubwa kwa bunge letu zima pia, ni sifa kwetu sote."

Spika alisema kwamba baada ya mkutano wa NEC kulikuwa na taarifa nyingi, zikiwemo za yeye kuzimwa jamboa ambalo lilistua wahisani na wakafuatilia kwenye ofisi za chama.

Spika Sitta hakutaka kueleza atakavyoendesha mkutano wa 17 wa Bunge la Jamhuri mwezi Novemba wakati wawakilishi hao wa wananchi watakapokuwa wakitarajia kauli za serikali kuhusu masuala kadhaa yenye utata, likiwemo suala la utoaji wa zabuni ya uzalishaji umeme wa dharura kwa kampuni Richmond Development (LLC).

"Hapana... ni kanuni tu na taratibu ndizo zinazoendesha bunge, hicho ndicho ninachoweza kusema," alijibu swali kuhusu mkutano huo utakaofanyika mwezi Novemba.

"Lakini kama ni mambo mengine, hebu tuache timu ya akina mzee (rais wa serikali ya awamu ya tatu, Ali Hassan) Mwinyi ifanye kazi yake, siwezi; sitaki na nisingependa kuyajadili kabisa, yaacheni, waachieni akina mzee Mwinyi."

Mwinyi anaongoza kamati iliyoundwa na Nec kushughulikia masuala ya kutoelewana baina ya wabunge na wanachama wa CCM ambayo yamekuwa yakisababisha chama hicho kuhusishwa na tuhuma za ufisadi na serikali kuonekana haifanyi kazi kuondoa uchafu huo.
 
Back
Top Bottom