Tabora. Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk Willibroad Slaa amesema, Chama Cha Mapinduzi (CCM) kisitafute dawa ya mawaziri Mizigo badala yake wamwajibishe aliyewateua hao wanaowaita mzigo.
Alisema badala ya kuwahangaisha Watanzania kwa kujadili majina ya mawaziri mizigo, wanapaswa kuchukua hatua za kinidhamu kama wana uhakika na mawaziri hao na kushauri kuangalia upatikanaji wao hadi kufikia nafasi hizo nyeti za kuwatumikia watu.
Akihutubia mkutano wa hadhara katika Uwanja wa Shule ya Sekondari Uyui mjini Tabora juzi,Dk Slaa alisema kinachoendelea ndani ya Serikali hivi sasa ambacho kinaitwa mawaziri mizigo ni moja ya dalili ya tatizo katika mamlaka ya uteuzi alibainisha pia kuwa, kuwatimua mawaziri hao siyo dawa bali kushughulikia chanzo cha tatizo.
Amesema kwa muda mrefu Serikali ya Rais Jakaya Kikwete imekuwa lawamani kutokana na kushindwa kazi kwa mawaziri wake, jambo ambalo Dk Slaa amesema, limetokana na kutofanyika kwa umakini wa kuzingatia vigezo, bali uswahiba.
Alisisitiza kuwa kinachofanyika sasa kwa Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana kuzunguka nchi nzima na kutaja majukwaani mawaziri mzigo ni njia ya kusukuma agenda ya mabadiliko ya Baraza la Mawaziri,lakini rais anapaswa kuchukua uamuzi sahihi wakati wa kuwawajibisha hao mizigo ambao ni maswahiba.
Dk Slaa anaendelea na ziara ya kuimarisha na kukagua uhai wa chama hicho mkoani Tabora,juzi alitembelea maeneo ya Ugoweko, Kakola na Tabora mjini na kudai kuwa mabadiliko ya mara kwa mara ya Baraza la Mawaziri katika Serikali ya Rais Kikwete hayana tija kwa Watanzania na ni dalili za tatizo la ukosefu wa uwajibikaji.
Soma zaidi: Slaa: Aliyeteua mawaziri mizigo awajibishwe - Siasa - mwananchi.co.tz