Sitta mzoefu wa kuvuruga Bunge?

asha ngedere

Member
Nov 6, 2009
92
11
Wadau mnaichukuliaje hii. Inaashiria nini katika miaka mitano ya Spika Sitta hadi sasa!

Sitta mzoefu wa kuvuruga Bunge

MWANDISHI WETU

Imebainika kuwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samuel Sitta ni mwanasiasa mzoefu wa kuvuruga Bunge.

Siri hiyo nyeti imebainika kufuatia matukio mbalimbali ambayo Spika huyo amewahi kuyafanya katika kipidi chake cha uongozi wa kisiasa nchini.

Uchunguzi wa waandishi wetu umebaini kuwa Rais wa Kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mwalimu Julius Nyerere alishawahi kukasirishwa na mwenendo wa Sitta, ambapo alielezea maono yake kupitia kitabu chake cha Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania.


Imebainika pia kuwa suala la kutaka mashauriano na mwafaka ili kuzuia mgawanyiko katika asasi nyeti ambazo anaziongoza au anafanyia kazi si jambo kubwa kwa mheshimiwa Sitta.

Kupitia dondoo mbalimbali zilizotumika katika kufanya uchunguzi, lililo kubwa kwa mheshimiwa Sitta ni kupambana na kupima mambo kwa viwango na mizania yake kama anavyoona.

Aidha, imebainika kuwa kama mheshimiwa huyo angelikuwa anatambua ukubwa na hadhi ya ofisi yake, basi angelikuwa bahiri wa kufanya siasa zake kwenye vyombo vya habari na katika makanisa.

Inaonyesha kuwa kwa wale wanaojua historia ya Sitta, yanayotokea leo hii na yeye akiwa katikati ya matukio hayo, hawawezi kushangaa.

Uchunguzi wetu unarudi katika miaka ya nyuma ambapo kama kiongozi wa Wanafunzi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Samuel Sitta alishiriki na kupanga maandamano ya kupinga kuanzishwa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).

Hata hivyo, tukio hilo liliishtua serikali aliyoongoza Mwalimu Julius Nyerere, serikali ya TANU na pia Taifa zima, ambapo vijana wake waliotumia pesa za wakulima na wafanyakazi walitakiwa kuwa na moyo wa kujitolea kuijenga nchi yao na pia kuchangia kwa namna yoyote maendeleo ya nchi.

Watu mbalimbali waliohojiwa na gazeti hili ambao wanalikumbuka tukio hilo walisema kuwa wanafunzi hao walioandaliwa na akina Sitta waandamane walibeba mabango ya kuikejeli serikali ya Mwalimu Nyerere na mabango yenyewe yalikuwa na maandishi yaliyosomeka, "Afadhali ya mkoloni".

"Tukio hilo lilimuudhi sasa Mwalimu Nyerere mpaka akakifunga Chuo Kikuu cha Dar es Salaam," anakumbusha profesa mmoja wa Chuo Kikuu ambaye alilishuhudia tukio hilo wakati huo.

Wakati Samuel Sitta anasema alitaka kunyang'anywa kadi ya Chama cha Mapinduzi na anamtaka Edward Lowassa awaombe radhi Watanzania kwa sakata la Kampuni ya mkataba wa kufua Umeme ya Richmond, yeye mpaka sasa hajaomba radhi kwa yale yaliyotokea 1966 ambapo taifa na serikali ilidhalilishwa na wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kukosa uzalendo.

Aidha, uchunguzi wa gazeti hili unabainisha kuwa, akiwa Waziri wa Sheria na Katiba, katika Serikali ya Awamu ya Pili, chini ya uongozi wa Rais Ali Hassan Mwinyi, Samuel Sitta alishiriki kwa kiasi kikubwa kulivuruga Bunge, kwa kuishauri serikali kukubali hoja za kundi la G 55 la kubadilisha Mfumo wa Muungano na kuanzisha Mfumo wa Shirikisho wa serikali tatu, ikiwa ni pamoja na kufufua serikali ya Tanganyika.

Taarifa hizo za kiuchunguzi zinaonyesha kuwa kiini cha pendekezo hilo kilitokana na fikra za wanasiasa na wabunge ambao walikuwa na kiburi cha kuona kwamba Wazanzibar wanabebwa na kuwa na kauli kubwa kwa uongozi na utawala wa sehemu hii ya Jamhuri na hivyo kuundwa kwa serikali ya Tanganyika kungelikomesha hali hiyo.

Matatizo yanayojitokeza leo hasa kuhusiana na Muungano ni matokeo ya Wazanzibari walijifunza nini kutokana na matukio katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hasa kuhusiana na jinsi kundi la wabunge (G 55) lilivyoibuka na jinsi serikali ilivyoshughulikia suala hilo.

John Malecela ambaye alikuwa Waziri Mkuu alilazimishwa kuachia nafasi yake na kuwa Waziri asiye na wizara maalum huku nafasi yake ikichukuliwa na Cleopa David Msuya, lakini cha ajabu Waziri wa Sheria na Katiba, Samuel Sitta ambaye kwa nafasi yake alitoa ushauri mbaya kwa serikali na hakujali chama, Baraza la Wawakilishi la Zanzibar na wala serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, hakujiuzulu.

"Wakati akijiuzulu nafasi ya Uwaziri Mkuu Edward Lowassa, Waziri wa sekta husika (Nishati na Madini) walijiuzulu. Baadhi ya watu wanahoji kwa nini Sitta hakujiuzulu mwaka 1994 akaondoka na Malecela?" wamehoji watu hao.

Nafasi ya Waziri wa Sheria na Katiba ni nafasi nyeti hasa katika kipindi cha mabadiliko ya kusimika mfumo wa demokrasi ya vyama vingi, maandiko yote ya kubadilisha mfumo wa jamii, ambayo ni pamoja na mfumo wa vyama vya siasa na uongozi wa dola.

Inaonyesha kuwa kilichokuwa kimetokea mwaka 1993 ni sawa na yale yaliyokuwa yametokea mwaka 1968 ambapo wabunge wa chama cha TANU walikuwa wanataka bunge na serikali kuwa juu ya chama na kukinyima chama tawala nafasi ya kuelekeza siasa na sera za nchi.

Wabunge, akina marehemu Wilfrem Mwakitwange na Dk. Lyantika Masha na wengine walifukuzwa kwenye nyadhifa zao, wabunge walifanya hivyo kwa kutaka kuiga mfumo wa demokrasi wa nchi za Magharibi, bila kujali nafasi ya chama katika kuleta uhuru na pia kuelekeza taifa katika kuamirisha uhuru.

Akina Mwakitwange na wenzake walikumbatia matakwa ya demokrasi ya Magharibi bila kujali tofauti zilizopo katika nchi ambazo ubepari na matabaka yamekomaa na demokrasi kujengeka kwa zaidi ya miaka 300 na nchi changa ambapo maendeleo ya nchi hizo ni duni.

"Baada ya miaka 15, wanasiasa wa mrengo wa kulia ndani ya Bunge wakiongozwa zaidi na hisia zao, bila kujali nini kitatokea kuhusiana na umoja wa chama na Bunge, walijichukulia dhamana ya kuanzisha zali kubwa kutishia muungano na mustakibali wa nchi kwa ujumla, kilichowatuma kufanya hivyo ni kiburi cha baadhi ya wabunge na mawaziri wa serikali kujiona ni bora kwa kupanga hoja na kuamini katika mantiki ya hoja zao," anakumbusha mchambuzi mmoja wa masuala ya siasa nchini aliyeomba hifadhi ya jina lake.

Mchambuzi huyo anasema, Wabunge na baadhi ya mawaziri walinogewa dhana ya utanganyika na hivyo kuanzisha na kuridhia hoja ya kuundwa kwa serikali ya Tanganyika.

Kuwa na Rais wa Serikali ya Muungano Mzanzibari na pia kuwa na Rais wa Serikali ya Mapinduzi ambaye ni Mzanzibari na madai mengine kutoka kwa viongozi wa siasa uchwara kutoka Zanzibar kuliwasumbua sana baadhi ya viongozi kutoka Tanzania Bara ambao waliona wajipatie madaraka kwa kuvunja misingi ya Muungano. Vile vile waliuona uongozi wa Rais Ali Hassan Mwinyi, kwa haiba yake, kama Kiongozi Mkuu mwenye uwezo pungufu.

Mwalimu Nyerere katika kitabu chake anawalaumu sana aliyekuwa Waziri Mkuu wakati ule, Mzee John Samuel Malecela ambaye alikuwa Mkuu wa shughuli za serikali Bungeni na Horace Kolimba, ambaye alikuwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi na Waziri wa Serikali ya Muungano kwa kutojali maslahi ya chama na hatima ya Taifa.

Katika kuchambua mlolongo wa matukio, ni wazi baadhi ya wabunge na mawaziri walifanya makusudi na kusaidia kupitishwa kwa Azimio ambalo lilitaka muundo wa Muungano ubadilishwe na kutaka Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi ikubali hoja ya wabunge.

Kutokana kwamba Mhe. Samuel Sitta alikuwa Waziri wa Sheria na Katiba, maandiko makuu mawili yaani "TAARIFA YA SERIKALI JUU YA AZIMIO LA BUNGE KUHUSU HAJA YA KUUNDA SELIKALI YA TANGANYIKA NDANI YA MUUNDO WA MUUNGANO" na hotuba ya Waziri wa Sheria na Katiba ya kuwasilisha makadirio ya Wizara ya Sheria na Katiba katika kikao cha bajeti 1993/94 ambapo "Serikali ilielezea kusudio la kuandaa Waraka wa Serikali (White Paper) kutafuta maoni ya wananchi kuhusu Muundo wa Muungano".

"Ni jambo la ajabu katika historia ya Tanzania kwa serikali kukitaka chama kiridhie maamuzi ya kisiasa ambayo hayakutokana na vikao vyake vikuu vya Kamati Kuu, Halmashauri Kuu na Mkutano Mkuu wa Taifa," anasema mwanasiasa mmoja mkongwe ndani ya CCM.

Aidha, anasema kilichokuwa kinaendelea ni kutafsiri matukio kisheria bila kujali athari zake kisiasa kwa kuzingatia matakwa ya mshikamano wa chama na uongozi wa dola kwa ujumla.

Serikali ya Rais Mwinyi ilikuwa ni serikali iliyogawanyika na pia chama kilikuwa kimetekwa na urasimu kiasi kwamba dhana ya dola kushika hatamu ndiyo ilikuwa imetamalaki.

Ni dhahiri kwamba ukuu wa chama katika kuonyesha dira na mwelekeo wa taifa ulikuwa unakabiliana na changamoto kubwa.

Inaelezwa kwamba ni katika kipindi hiki ambapo Chama kilianza kupoteza nafasi yake ya kuwa chama cha wanachama na badala yake kikaanza kuwa chama cha viongozi.

Hoja za wabunge kutaka kubadilishwa muundo wa Muungano na kupelekea kuundwa kwa serikali tatu ikiwemo serikali mpya ya Tanganyika ni jambo lililotazamwa kirasimu bila wahusika kuingia kwenye mjadala wa kina na kuibua sababu zenye uzito wa kubeba hoja.

Mwalimu Nyerere alishindwa hoja zilizokuwa na utaratibu uliokuwa unatumiwa na serikali kuhusiana na kuwasilisha hoja hiyo nzito.

"Kwanza lazima ieleweke kwamba Muungano ni wa pande mbili, kwa vipi Bunge la Jamhuri ya Muungano lilikuwa linajichukulia mamlaka bila kujali kwamba kuna Baraza la Wawakilishi na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na wananchi wa Zanzibar ambao wana nafasi yao katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano hasa kuhusu mabadiliko katika mfumo wa muungano?" anahojia mchambuzi wa masuala ya siasa.

Pia ikumbukwe kwamba kabla hoja haijaingia katika utaratibu wa kutungiwa sheria lazima kuwepo na mashauriano na wadau mbalimbali ndani na nje ya mfumo wa dola.

"Hayo yote Mheshimwia Sitta ambaye alikuwa ndiye msimamizi mkuu wa masuala ya ufundi (ya kisheria) hakuyaona na badala yake akagubikwa na ushabiki wa kisiasa pamoja na uhafidhina wa kuamini kwamba sheria ndiyo mwanzo na mwisho wa mambo yote," anaongeza.

Hivyo, Sitta hawezi kukwepa lawama kazi zile walizotupiwa akina Malecela na Kolimba na kwa hakika Sitta ilikuwa ajiuzulu au aondolewe kwenye nafasi yake kama waziri wa Sheria na Katiba kama Malecela alivyo ondolewa kwenye nafasi ya Waziri Mkuu.

Mapungufu ya serikali ya awamu ya pili chini ya Rais Mwinyi kwa kiasi fulani yalikuwa yanachochewa na baadhi ya mawaziri waliokuwa na agenda zao binafsi ambao walikuwa wanajiona kwamba wao ni bora kuliko wengine.

Na wakati huo huo kama siyo Mwalimu Nyerere kuingilia kati na kunusuru hali basi upepo mbaya lazima ungezamisha jahazi na vinginevyo tungekuwa tunagawana mbao.

Mwalimu Nyerere analiweka vizuri suala hilo pale anaposema: "13 Kwa kuwa suala la muundo wa nchi ni zito na ni la Kikatiba ushirikishwaji wa wananchi ni jambo lisiloweza kuepukwa.

Aidha, kwa uzoefu wetu na hali halisi ya nchi yetu ni lazima utaratibu wowote utakaokubalika uwezeshe Serikali ya Jamhuri ya Muungano kushauriana na chama na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar".

Haya tunayoyaona katika Bunge la sasa linaloongozwa na Spika Samuel Sitta, yanaturejesha nyuma kwamba Sitta ana mwelekeo wa siasa za kirasimu, ambazo daima hupendelea kukitupa chama kando bila kujali matokeo yake ya muda mrefu.

Ni wazi jambo la Bunge kuwa na makundi na Chama Cha Mapinduzi kudhoofika, havimsumbui Sitta.

"Tunachopata kutoka kwake ni kwamba yeye yuko sahihi, wengine wote wanaompinga ni mafisadi na kwa namna yoyote ile "anaongozwa na Yesu". Yesu, wa wote anaweza kubinafsishwa?" anahoji Profesa wa Chuo Kikuu.

SOURCE: TAIFA TANZANIA
 
Majungu kibao hakuna lolote hapo mtu atavuruga vipi bunge ? Bunge hilo hilo likiongozwa na Sitta ndilo lilofanya kwa mara ya kwanza waziri mkuu na mawaziri kuanchia ngazi sasa sijui mnaandika nini ?na lazima mkumbuke hakuna mtu perfect ndio maana kila mtu anakasoro zake kwa hiyo kama kuna kitu amechemka lakini pia muangalie pia aliyoyafanya.jamani mijitu mingine khaa
 
..Sitta aliteuliwa lini kuwa waziri wa sheria na katiba? kabla, au baada ,ya sakata ya hoja ya kuundwa kwa serikali ya Tanganyika?
 
Ni hulka ya kila binadamu kubadilika kubalika hivyo kwa sita ni mtu ambaye mara zote huwa anasimamia ukweli ambao anajua yeye mwenyewe
 
yawezekana ni majungu hasa tunapoelekea kwenye uchaguzi mkuu. lakini wadau, ni kweli haya mengine yaliyosemwa i.e kushawishi mgomo wa wanafunzi wa chuo kikuu 1966 kupinga jkt na kuunga mkono serikali ya tanganyika ndani ya muungano? pengine wenye data wanaweza kutujuza ili tumwelewe vizuri, achilia mbali hayo majungu.
 
Ni bahati mbaya kwamba habari ndefu lakini haina chochote cha maana zaidi ya kuanza kampeni kabla ya wakati. Kuna haja ya kujua mmiliki wa gazeti na uhusiano wake na makundi yanayo hasimiana ndani ya CCM na Bunge.
 
ha ha ha wacha niende nikanywe chai manake mambo yamekuwa si mambo tena au ndio ule msemo wa kikwetu kwamba kama unaishi nyumba ya nyasi wacha kutupa vishungi vya tumbaku unayovuta hovyo ha ha ha si unajua tena
 
Majungu tupu hizi ni kampeni za kisiasa zaidi tumezizoea Sitta kama unanisikia chukua glass yako ya wine telemshia polepole tulisubiri kwa muda mrefu bunge hili la viwango na spidi kama kuna mtu asiyeweza kukabili viwango aachie bomba

Mwandishi amejaribu kumhusisha Sitta na matukio mbali mbali wangapi huwa wanaunga mkono maandamano pale chuoni na wapo madarakani tutajane kwa majina ni kina nani walikuwa G55 na wako madarakani muulize Marmo mbona Malecela alikuwa mmoja wao

Halafu mwandishi anaonekana hana data vizuri ndiyo maana anaishia kusema eti anahoji Profesa mmoja wa chuo kikuu yupi mbona hutukumbushi kuwa naye Nyerere aliwahi kufungwa jela regardless ya sababu hata Sitta inawezekana alikuwa na sababu kwa wakati ule kuunga maandamano

hakuna kitu hapa ni wale wale wapinzani wake walioandaa hii taarifa yeye kama Spika anatetea wananchi wao wanatetea maslahi yao wanataka kumgeuzia kibao aonekane kama yeye ndiye msaliti tusahau kwamba wao ndio mafisadi wakubwa Sitta tuko pamoja
 
Well elaborated with some vivid examples, It seem that the writer is good in making explaination, well done.

Believe or not, ukimuona mtu anahubiri siasa mpaka makasani, basi huyo mtu ni mbinafsi mna mpenda sifa tena za kijinga. Hill halihitaji mtu kuwa na degree ndo alione, kwani ni nani asijua kuwa kanisani huwa kuna mjumuiko wa watu wenye itikadi tofauti za kisiasa?

Mimi bado nina imani kubwa sana kati ya wanasiasa wanaopenda hili taifa na rasilimali zake kama Mh.Dr.Slaa, huyu anaonekana kwa matendo na siyo akina ndugu zangu wanaojipambanua kuwa wanapinga ufisadi kumbe na behind the background, ni wapuuzi watupu.

Tanzania itajengwa na moyo safi na siyo na watu walafi na wanaopenda sifa.
 
Ni vizuri kuangalia huyo mwandishi ana mahusiano gani na maendeleo ya taifa la watanzania.

Kifupi kutokana mtazamo wangu naona huyu mwandishi pengine katumwa tu kuleta ujumbe wa aina hii, lakini nikiri tu kwamba hili jungu halijapikwa vizuri, labda kwa maamuma wa siasa zetu
 
- Hilo gazeti ni la nani kwani maana siku hizi ni lazima kuuliza kwanza, especially gazeti linapokuwa limejaa sumu na majungu kama hayo juu ni lazima kujua ni kambi gani ya siasa au kundi gani CCM wanamiliki hilo gazeti!

- Maendeleo hakuna ila majungu tu na fitina ndio vimetawala hili taifa, article lirefu kama lina ideas za maendeleo kwa wananchi, kumbe ni majungu tu na fitina! Hili taifa sijui tumelogwa na nani! siku hizi ni Zitto, Zitto, Sitta, sitta, Lowassa, Lowasa, Mwakyembe, Mwakyembe, Kikwete Kikwete, maendeleo hakuna maneno tuuuu!

Respect.


FMEs!
 
- Hilo gazeti ni la nani kwani maana siku hizi ni lazima kuuliza kwanza, especially gazeti linapokuwa limejaa sumu na majungu kama hayo juu ni lazima kujua ni kambi gani ya siasa au kundi gani CCM wanamiliki hilo gazeti!

- Maendeleo hakuna ila majungu tu na fitina ndio vimetawala hili taifa, article lirefu kama lina ideas za maendeleo kwa wananchi, kumbe ni majungu tu na fitina! Hili taifa sijui tumelogwa na nani! siku hizi ni Zitto, Zitto, Sitta, sitta, Lowassa, Lowasa, Mwakyembe, Mwakyembe, Kikwete Kikwete, maendeleo hakuna maneno tuuuu!

Respect.

FMEs!

You have nailed mkuu, kuna viumbea umbea na vimajungu ambavyo havitusaidii kama taifa, kusema watu na sio ideas. Yaani unawaza mpaka unafikia point na kusema , kweli viongozi hawa they are exactly like us! maana huoni input, challenges, new ideas and free thinking kutoka kwa waandishi wa habari wengi sana.unaamini waandishi wanawatakiwa kuwa smart kwa sababu ya kujisomea na exposure lakini wapi bwana!
 
Umekosea pa kupeleka, hapa ulipozileta hizo chai zako wala hakuna wanywaji. Try elsewhere
 
...mhn, wameshindwa kumpa kashfa ya ufisadi sasa wanajaribu kutupa karata ya historia. Lol, kuna mbwembwe kwelikweli kwenye siasa.
 
Majungu kibao hakuna lolote hapo mtu atavuruga vipi bunge ? Bunge hilo hilo likiongozwa na Sitta ndilo lilofanya kwa mara ya kwanza waziri mkuu na mawaziri kuanchia ngazi sasa sijui mnaandika nini ?na lazima mkumbuke hakuna mtu perfect ndio maana kila mtu anakasoro zake kwa hiyo kama kuna kitu amechemka lakini pia muangalie pia aliyoyafanya.jamani mijitu mingine khaa

we ndo utumbo mtupu...huyu mzee ni mshenzi na hafai kuwa kiongozi ,ana chuki na majungu...hafai
 
Kwani amelivurugaje Bunge? Maneno ni mengi halafu hiyo source si mnaiona kuwa haiaminiki manake ni ileile ya kuwalinda mafisadi. Mwacheni 6 bwana. Kama ni kuvuruga nadhani anavuruga ukiritimba wa ccm ndani ya bunge na si bunge kama institution!
 
Nina wasiwasi na yaliyoandikwa hapa, ila nina wasiwasi kibao na yale ambayo hayajaandikwa hapa!
 
Sitta zama zake kisiasa ndo zinazoyoyoma hivyoo kwani naye kutwa malumbanoo magazetinii akisaidiwaa na nipashee kuchocheaa story mbofu mbofuuuuuuuuuuuuuuuuuuuuu....namhurumiaaa.
 
Back
Top Bottom