Sitta afungwa mdomo

nyabhingi

JF-Expert Member
Oct 12, 2010
15,508
19,981
SAKATA LA DOWANS: Sitta afungwa mdomo
• Baraza la Mawaziri chini ya JK lamshambulia yeye na Mwakyembe

na Mwandishi wetu


amka2.gif

RAIS Jakaya Kikwete amemfunga mdomo Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki Samuel Sitta aliyeingia katika mzozo na waziri mwenzake wa Nishati na Madini, William Ngeleja.
Mzozo huo uliibuka baada ya Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi (ICC), kuamua Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) iilipe Dowans fidia ya sh bilioni 94 kutokana na TANESCO kuvunja mkataba nayo.
Uamuzi wa kumziba mdomo Sitta, ulifikiwa jana katika kikao cha Baraza la Mawaziri, kilichofanyika Ikulu, jijini Dar es Salaam, chini ya Rais Kikwete, ambapo pamoja na mambo mengine, mjadala wa malipo ya Dowans ulitawala kikao hicho.
Mwingine aliyepigwa kufuli katika kikao hicho ni Naibu Waziri wa Miundombinu, Dk. Harrisson Mwakyembe, ambaye naye aliungana na Sitta kumpinga Ngeleja kuilipa Dowans.
Vyanzo vyetu vya habari vilisema Sitta na Mwakyembe walikuwa na wakati mgumu kutetea hoja ya kutaka serikali isiilipe Dowans na kwamba hata Rais alisema hafurahishwi na hukumu ya malipo hayo.
“Kikao bado kinaendelea, lakini Sitta na Mwakyembe walibanwa sana na mawaziri na hata Bwana mkubwa (Rais) aliungana na mawaziri wengine kuwalaumu kwa kupeleka mjadala huo hadharani,” kilisema chanzo chetu cha habari.
Kwa mujibu wa habari hizo, kuanzia sasa Sitta na Dk. Mwakyembe, wamefungwa mdomo kuzungumzia suala la malipo ya Dowans hadharani na kwamba wanapaswa kuwa kitu kimoja kuhakikisha mipango ya serikali inatekelezwa kama ilivyopangwa.
Kabla ya kibano hicho jana, wiki iliyopita katika kikao cha kamati ndogo ya mawaziri uliibuka msuguano wa hoja kati ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema na Waziri Sitta.
Habari kutoka ndani ya kikao hicho ambacho kilifanyika chini ya uenyekiti wa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, zinaeleza kuwa Jaji Werema alieleza kusikitishwa na matamshi ya Sitta katika vyombo vya habari.
Taarifa kutoka ndani ya kikao hicho zimemkariri Werema akieleza kushangazwa na hatua ya Sitta kuwashambulia yeye na Ngeleja huku akijua kuwa walichokifanya na kuamua kilikuwa kinagusa moja kwa moja mamlaka yao ya kiwajibu na kimamlaka.
Jaji Werema amekaririwa akimweleza Waziri Sitta kwamba iwapo kweli alikuwa ana uchungu na suala la Dowans, basi wakati kesi ikiendelea alipaswa kuisaidia serikali katika kuwasilisha utetezi dhidi ya malalamiko 17 yaliyokuwa yamewasilishwa na kampuni hiyo.
Habari zinaeleza kwamba hatua ya Sitta ambaye alikuwa akitambua fika namna kesi hiyo ilivyokuwa ikiendelea kutochangia jambo lolote wakati shauri hilo likiwa ICC na badala yake kusubiri hadi serikali ishindwe ndipo aanze kutoa matamshi katika vyombo vya habari ilikuwa ni ya kuchochea hasira za wananchi dhidi ya viongozi pasipo sababu zozote.
Wakati Jaji Werema akimshushia lawama Sitta kwa muda usiopungua dakika 15, Waziri Mkuu Pinda alikuwa kimya muda wote.
Baada ya kumaliza hoja yake, Waziri Mkuu aliwataka wajumbe wa kamati hiyo ya mawaziri iliyokuwa ikijadili kuhusu Muswada wa Mabadiliko ya Sheria ya Manunuzi unaotarajiwa kuwasilishwa katika Bunge lijalo kuendelea na mjadala.
Awali kabla ya Werema kuzungumza, Sitta alichangia kuhusu muswada huo na akaeleza haja ya kuwekwa kwa masharti magumu zaidi ili kuzuia uwezekano wa makampuni ya kitapeli kujipenyeza nchini na kuigharimu serikali mamilioni ya fedha kauli ambayo ilionekana kumkera Werema.
Awali hofu ilitawala kwamba Sitta na Mwakyembe, wangeweza kupoteza nafasi zao za uwaziri kutokana na hatua yao ya kuibua mjadala dhidi ya mawaziri wenzao nje ya Baraza la Mawaziri kuhusu uamuzi wa serikali kukubali kuilipa Kampuni ya Dowans Holdings SA.
Mkanganyiko wa kauli ya Sitta na Mwakyembe, ulisababisha Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Utawala Bora), Mathias Chikawe, kutoa matamshi makali ya karipio kwa mawaziri hao wawili.
Ukali wa matamshi hayo ya Chikawe ambaye anadaiwa kupata baraka za Rais Kikwete, uliongezwa na tamko lake la kuwataka Sitta na Mwakyembe iwapo wanataka kuendeleza malumbano hayo nje ya utaratibu wa kawaida wa mawasiliano wa mawaziri, wajiondoe serikalini.
Chikawe amekaririwa akisema kitendo cha Sitta kumtuhumu Ngeleja kwamba alitangaza kulipwa kwa Dowans kabla suala hilo halijafikishwa katika Baraza la Mawaziri kinakwenda kinyume cha miiko ya uwaziri kinachomtaka kutotoa siri za baraza.
Kwa mujibu wa Chikawe, Waziri Ngeleja kwa mamlaka aliyonayo kama waziri mwenye dhamana na masuala ya nishati alikuwa na mamlaka ya kutoa tamko alilotoa baada ya kufanya mashauriano na wataalamu mbalimbali wa masuala ya sheria serikalini.
Chikawe alisema iwapo Sitta na Mwakyembe walikuwa hawajaridhishwa na uamuzi wa Waziri Ngeleja walikuwa na njia za kuwasilisha hoja zao pasipo kutumia vyombo vya habari.
Kwa upande wake, Mwakyembe ameingia matatani kutokana na kunukuliwa na gazeti la Uhuru linalomilikiwa na Chama cha Mapinduzi (CCM) akieleza kushangazwa na hukumu ya Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Migogoro ya Uwekezaji (ICC) iliyoipa ushindi Dowans dhidi ya serikali na kutakiwa kulipwa fidia ya shilingi bilioni 94. ICC iliamua katika hukumu yake Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) iilipe Dowans fidia ya sh bilioni 94 kutokana na TANESCO kuvunja mkataba nayo.


h.sep3.gif


juu
blank.gif
 
Dawa siyo kuwafumba watu midomo, swala ni kusimama kwenye reality. Kwamba wanayosema ni sawa au siyi sawa. Siyo kukaripia wapiganaji wetu wenye uchungu na hii inji
 
Back
Top Bottom