Sitosahau nilikiona cha moto urithi wa mali za babu

Kanungila Karim

JF-Expert Member
Apr 29, 2016
20,744
25,426
f6778344e14e39aa793e68f712ba9a76.jpg

SEHEMU YA 01

Jina langu ni Kassim Fumbwe. Nina umri wa miaka ishirini na minane. Mkazi wa jiji la Dar es Salaam.
Wazazi wangu walifariki dunia wakati nikiwa mdogo. Nakumbuka tulikuwa tunasafiri kutoka Dodoma kuja Dar, basi tulilokuwamo likagongana na lori uso kwa uso.
Baba yangu na mama yangu pamoja na abiria wengine kadhaa walifariki hapo hapo. Mimi nikanusurika.
Nakumbuka nilipata jeraha dogo tu kwenye mkono wangu wa kushoto baada ya kukatwa na vioo vya dirisha vilivyokuwa vimevunjika.
Babu yangu mzaa baba, Mzee Fumbwe Limbunga alipopata habari ya ajali ile alitoka Dar kwa gari lake akaja Morogoro. Majeruhi wa ajali ile tulikuwa tumelazwa katika hospitali ya Morogoro.
Mimi sikuwa nimeumia sana lakini kwa vile wazazi wangu walikuwa wamefariki ilibidi nibaki hapo hospitali ili niweze kutambuliwa na kuchukuliwa na ndugu zangu.
Babu alipokuja akanichukua. Aliichukua pia miili ya marehemu baba yangu na mama yangu.
Siku ya pili yake habari za ile ajali zilichapwa kwenye magazeti. Kila gazeti lilikuwa limechapa picha yangu ikielezea jinsi nilivyonusurika kimiujiza.
Baada ya msiba huo, nikawa ninaishi na babu. Babu yangu alikuwa tajiri lakini alikuwa hana mke. Aliachana na mke wake tangu alipokuwa kijana na hakutaka kuoa tena.
Kwa hiyo alinitafutia mtumishi wa kunihudumia kwa kila kitu ikiwa ni pamoja na kunipeleka shule. Nilipoanza masomo ya sekondari babu akanihamisha katika nyumba yake nyingine. Zote zilikuwa Tegeta lakini zilikuwa mitaa tofauti.
Ile nyumba aliyonihamishia upande mmoja ilikuwa na mpangaji, upande mwingine ndio niliokaa mimi.
Kila jumatatu babu alikuwa akinipa pesa za kutumia kwa wiki nzima. Baadhi ya siku nilikuwa ninapika mwenyewe nyumbani na siku nyingine nilikuwa ninakula kwenye mikahawa..
Baada ya kumaliza masomo yangu nilipata kazi Morogoro. Lakini babu alinishauri niache kazi nifanye biashara. Aliponipa mtaji nikaacha kazi. Nilifungua maduka matatu ya vifaa vya ujenzi pale Morogoro.
Yalikuwa maduka makubwa. Niliajiri karibu wafanyakazi kumi na watano. Kila duka lilikuwa na wafanyakazi watano. Biashara ilianza vizuri. Baada ya miezi sita tu nikaja Dar kununua gari la kutembelea.
Sasa nikawa nafikiria kutafuta mke nioe. Sikumaliza hata mwaka mmoja ile kasi ya biashara ikaanza kupungua. Maduka yangu yaliyokuwa yamejaa vitu yakaanza kuwa matupu. Haukupita muda mrefu nikaanza kupunguza wafanya kazi. Mwisho kila duka likabaki na mfanyakai mmoja.
Nilifikia mahali nikahisi kuwa pengine sikuwa na nyota ya kujiajiri. Nikajuta kuacha kazi niliyokuwa nayo mwanzo. Ikabidi yale maduka mawili niyafunge nikabaki na duka moja ambalo nililisimamia mwenyewe. Duka hilo nalo likafilisika nikalifunga. Nikawa sina kazi.
Nilifikiria kwenda kumueleza babu ili anipe mtaji mwingine lakini nilishindwa kwani nilijua asingekubali tena kunipa pesa zake. Nikauza lile gari. Siku ile nauza gari babu akanipigia simu na kunijulisha kuwa alikuwa anaumwa na alikuwa amelazwa katika hospitali ya Aga Khan.
Nikapanda basi kuja Dar. Nilipofika Dar nilikwenda moja kwa moja katika hospitali katika hospitali ya Aga Khan..
Vile nafika tu na babu yangu anakata roho. Hata sikuwahi kuzungumza naye lolote.
Kifo chake babu hakikunishitua sana kwa sababu alikuwa na mali na mimi ndiye ambaye ningemrithi.
Dereva wake nilimkuta hapo hapo hospitali, alinieleza kuwa Mzee Fumbwe alianza kuumwa siku tatu zilizopita lakini usiku uliopita ndio alizidiwa. Presha ilikuwa juu na sukari ilipanda. Hali ikawa mbaya.
Kwa kushirikiana na dereva huyo tuliuchukua mwili wa Mzee Fumbwe siku ya pili yake kwa ajili ya maziko. Baada ya maziko nikaanza mchakato wa kukagua mali za marehemu.
Nilichokuwa nikikifahamu awali ni kuwa babu yangu alikuwa na maduka kadhaa Dar es Salaam. Alikuwa na vituo vitatu vya mafuta na malori sita.
Pia alikuwa na nyumba alizokuwa amezipangisha ambazo sikujua zilikuwa ngapi.Nilikuwa nikijua nyumba mbili tu, ile aliyokuwa akiishi yeye na ile niliyokuwa nikikaa mimi kabla ya kuhamia Morogoro.
Mali zake nyingine alikuwa akizijua yeye mwenyewe. Niliingia chumbani mwake nikafungua makabati na kuanza kupekuwa nyaraka zake alizozihifadhi kwa lengo la kutambua mali hizo.
Jambo ambalo lilinishangaza, nilikuta hati ya nyumba yake aliyokuwa akiishi na hati za gari alilokuwa akilitumia. Sikukuta hati wala nyaraka nyingine zinazohusu mali zake.
Wakili wake nilikuwa namfahamu. Nikaenda ofisini kwake barabara ya Samora na kumjulisha kuhusu kifo cha mteja wake.
“Oh mzee amefariki?” akaniuliza kwa mshituko.
“Amefariki juzi, tumemzika jana”
“Alikuwa mgonjwa?”
“Wakati anaumwa mimi nilikuwa Morogoro. Juzi akanipigia simu yeye mwenyewe akaniambia kuwa anaumwa na amelazwa hospitali. Muda ule ule nikapanda gari kuja kumuona. Mpaka nafika Dar nikakuta ameshafariki”
“Oh pole sana. Aliwahi kuniambia kuwa mwanawe alifariki dunia”
“Mwanawe ni baba yangu. Alifariki mimi nikiwa mdogo”
“Kwa hiyo mrithi wake utakuwa wewe. Kwa maana hakuwahi kuandika wasia wowote ila alinieleza kuwa hakuwa na ndugu wala mtoto mwingine isipokuwa mjukuu”
Wakili alipoleta suala la urithi akawa amenirahisishia tatizo lililokuwa limenipeleka kwake.
“Hilo ndilo lililonileta kwako”
“Umefanya vizuri kuja kunifahamisha. Sasa unatakiwa ufungue mirathi mahakamani ili uweze kumrithi babu yako”
“Kabla ya kufungua mirathi kuna suala moja ambalo limenishitua sana”
“Suala gani?”
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 02

ILIPOISHIA
“Kuhusu mali za marehemu. Babu yangu alikuwa tajiri lakini katika kumbukumbu zake nimekuta hati ya nyumba moja aliyokuwa anaishi pamoja na hati ya gari alilokuwa akitumia”
“Sasa kama hakuna hati wala nyaraka zozote utazijuaje mali zake nyingine?”
“Kwanza hizo nyaraka zitakuwa zimekwenda wapi?”
“Nenda kapekue vizuri. Inaweekana aliuza baadhi ya mali zake”
Kutokana na ushirikiano alionipa wakili huyo kutafiti mali alizokuwa akimiliki marehemu babu yangu, tuligundua kuwa mpaka marehemu anafariki duniani hakuwa na mali yoyote aliyoacha zaidi ya nyumba aliyokuwa akiishi pamoja na gari lake.
Hata baada ya kufungua mirathi mahakamani na kuthibitishwa kuwa mimi ndiye mrithi wa marehemu, sikukuta pesa ya maana katika akaunti yake ya benki. Akaunti yake ilikuwa na shilingi elfu kumi tu.
SASA ENDELEA
Kwa Kweli mimi na wakili wa marehemu tulishangaa sana. Kila mtu alikuwa akifahamu kuwa Mzee Fumbwe alikuwa ni miongoni mwa matajiri wazawa wa jiji la Dar es Salaam. Jinsi alivyokufa akiwa masikini ni jambo ambalo halikueleweka.
Katika utafiti nilioufanya baadaye niligundua kuwa Mzee Fumbwe alikuwa ameuza baadhi ya mali zake zikiwemo nyumba na vituo vya mafuta siku chache kabla ya kufariki dunia.
Lakini uchunguzi wangu ulishindwa kubaini marehemu alipeleka wapi pesa zake kwani benki hakukuwa na kitu.
Kwa kipindi cha karibu wiki mbili nilikuwa nikiendelea kufanya utafiti kwenye nyaraka za marehemu ili kupata uhakika kwamba kweli babu hakuwa na kitu.
Nikaja kugundua kitabu cha kumbukumbu cha marehemu ambacho alikuwa akiandika mambo yake. Nilipopekua karasa na kitabu hicho niliona kulikuwa na watu ambao walikuwa wakifanya biashara na babu na kwamba babu alikuwa akiwadai wafanyabiahara hao pesa nyingi.
Nilikuta majina ya wafanya biashara wanne. Katika watu hao ni mmoja tu aliyekuwa akiishi hapo Dar, wengine walikuwa wakiishi nchi za nje. Mwenyewe aliandika kama ifuatavyo
Abdul Baraka wa Mbezi Dar es Salaam. Namdai dola milioni moja.
(Aliandika na namba ya simu yake)
Isaac Chusama wa Harare Zimbambwe. Namdai dola milioni mbili na laki tano.
(Aliandika namba ya simu yake na mtaa aliokuwa anaishi)
Benjamin Muhoza wa Gaborone Botswana. Namdai dola milioni moja na laki tano.
(Aliandika namba ya simu yake na mtaa aliokuwa akiishi)
Dumessan Dube wa Cape Town Afrika Kusini. Namdai dola milioni tatu.
(Aliandika namba ya simu yake na mtaa aliokuwa akiishi)
Hapo nikajua kuwa marehemu babu alikuwa akidai fedha nyingi kwa watu waliokuwa wakiishi nje ya nchi.
Kitabu hicho cha kumbukumbu kiliendelea kunjulisha siri ya babu ambayo nilikuwa siifahamu. Babu alikuwa akifanya biashara ya madini. Tena madini ya Tanzanite na kwamba alikuwa akiwauzia wafanya biashara hao.
Kumbukumbu za nyuma za kitabu hicho zilionesha ameshawahi kuwauzia madini wafanyabiashara hao kwa thamani ya dola ya Kimarekani. Na kwamba alikuwa akilipwa kwa awamu.
Nikajiuliza babu alikuwa akipata wapi madini mengi kiasi cha kumpatia mamilioni hayo ya dola?
Swali jingine nililojiuliza ni wapi babu yangu alikokuwa anaficha fedha hizo, isingewezekana afe akiwa hana kitu.
Niliitafuta paspoti yake na nikaipekua. Nikagundua kuwa mara kwa mara alikuwa akitembelea Zimbabwe, Botwana na Afrika kusini.
Nilipopekua zaidi kwenye mafaili yake nikaipata mikataba yake na wafanya biashara hao. Alikuwa amelipwa pesa nusu na nusu alikuwa akiwadai. Tarehe ya kuwafuata wafanya biashara hao wammalizie deni lake ilikuwa imeshapita.
Nikajiambia kama nitafanikiwa kupata fedha hizo nitakuwa tajiri mkubwa hapa Dar kwani kwa pesa za Kitanzania dola hizo zilikuwa ni mabilioni ya shilingi.
Kwa vile marehemu aliandika namba za simu zao, nikaanza kumpigia Abdul Baraka aliyekuwa hapo Dar. Nilimpigia kwa kutumia laini ya marehemu. Simu yake haikupatikana.
Nikampigia Isaac Chusama wa Harare. Simu iliita kwa sekunde chache kisha ikapokelewa.
Nikashangaa kusikia sauti ikinisalimia kwa Kiswahili.
“Habari yako Bwana Fumbwe?”
“Nzuri lakini mimi siye Bwana Fumbwe. Bwana Fumbwe amefariki wiki tatu zilizopita, mimi ni mjukuu wake. Naitwa Kassim Fumbwe”
“Heh! Mzee Fumbwe amefariki?”
“Amefariki. Hivi sasa ni wiki tatu zimeshapita”
“Oh pole sana”
“Asante. Sasa kumbukubu za babu zinaonesha kwamba alikuwa akikudai dola milioni mbili na laki tano. Na mkataba wa makubaliano yenu ninao hapa”
“Ndio ni kweli ananidai”
“Kwa vile tarahe ya kumlipa imeshapita, ninataka nije Harare unipatie hizo fedha. Mimi ndio mrithi wake”
“Sasa nitakuaminije Bwana Fumbwe?”
“Nitakuja na hati zote zikiwemo hati za mahakama zinazoonesha kwamba mimi ndiye mrithi wa marehemu, cheti cha kifo chake na mikataba ya makubaliano yenu”
Pakapita kimya cha sekunde kadhaa kabla ya sauti ya mtu wa upande wa pili kusikika tena.
“Unatarajia kuja lini?”
“Baada ya siku mbili tatu. Hivi sasa ninajiandaa kwa safari”
“Utakapokuja utanijulisha”
“Sawa”
Isaac akatangulia kukata simu.
Hapo hapo nikampigia Benjamin Muhoza. Nilishukuru naye alipopokea simu.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 03

Alinisalimia kwa Kingreza kwa kutumia jina la marehemu babu yangu. Na yeye nikamjulisha kuwa Mzee Fumbwe alikuwa amefariki dunia na kwamba mimi nilikuwa mjukuu wake.
“Ulikuwa unataka nini?” akaniuliza.
“Kumbukumbu za babu zinaonesha kwamba anakudai dola milioni moja na laki tano. Mikataba yenu ninayo hapa. Mimi ndiye mrithi wake”
Simu ya upande wa pili ikawa kimya. Nilipoona amenyamaza nilimwambia.
Ninazo hati za mahakama zinazothibitisha kuwa mimi ndiye mrithi wa marehemu. Nina cheti cha kifo chake na nina mkataba wa makubaliano yenu”
“Utakuja kunionesha?” Benjamin akaniuliza.
“Nitakuja kukuonesha ili uthibitishe kuwa Mzee Fumbwe amefariki na kwamba mimi ndiye ninayepaswa kulipwa madeni yake”
SASA ENDELEA
“Utakuja lini?”
“Nitakujulisha siku ambayo nitakuja”
“Sawa”
Nikakata simu kisha nikampigia Dumessan Dube wa Afrika Kusini.
Yeye nilizungumza naye kama nilivyozungumza na wenzake lakini yeye hakushangaa nilipomwambia Mzee Fumbwe amefariki. Aliniambia ameshapata habari.
“Umepata habari hiyo kutoka wapi?” nikamuuliza.
“Nimeipata kutoka kwa marafiki mbalimbali ambao anafanya nao biasharara”
“Ni vyema kama umeshapata habari. Kwa hiyo mimi ndiye mrithi wake. Nimekuta una deni la dola milioni tatu ambazo babu anakudai”
“Umelikuta wapi deni hilo?”
“Kwenye kumbukumbu zake na mkataba wenu wa makubaliano pia ninao hapa”
“Sawa” Dube aliniambia baada ya kimya kifupi kisha akaniuliza.
“Sasa ulitakaje?”
“Nimeona tarehe ya malipo ya hizo pesa imeshapita. Nilitaka nije Afrika Kusini unipatie pesa hizo. Nitakuja na hati zote”
Baada ya kimya kingine kifupi, Dube aliniambia.
“Sawa. Unatarajia kuja lini?”
“Nitakujulisha”
“Sawa”
Kusema kweli baada ya kuzungumza na wafanyabiashra hao waliokuwa nje ya nchi nilifarijika sana. Yule mfanyabiashara aliyekuwa Dar es Salaa ambaye simu yake ilikuwa haipatikani nilimuacha kiporo.
Niliona sasa urithi wa babu ulikuwa unakuja mikononi mwangu taratibu. Nikajiambia kama pesa hizo nitazipata zote ningekuwa miongoni mwa matajiri wakubwa katika jiji hili.
Nilimshangaa marehemu babu yangu kwa kuacha kiasi kikubwa cha pesa nje ya nchi bila kunishirikisha mimi mjukuu wake. Kwa kweli alikuwa msiri sana na pia alikuwa tajiri japokuwa mali alizokuwa akimiliki hapo Dar bado zilikuwa ni kitendawili.
Sikwenda kumueleza wakili kuhusu madeni hayo. Niliacha yabaki kuwa siri yangu. Sasa nikaanza kujiandaa kwa safari ya nchi hizo tatu huku ndoto za utajiri zikiwa zimetawala akili yangu.
Baada ya wiki mbili nikawa nimeshapata pesa za kuniwezesha kuzuru katika nchi hizo. Mipango yangu ya safari ilipokamilika nikaanza safari yangu. Kwanza nilipanga kwenda Harare Zimbabwe. Kabla ya kuondoka nilimpigia simu Isaac Chusama kumjulisha kuwa ninakwenda Zimbabwe.
“Sawa. Ukifika utanipigia simu kunijulisha kuwa umefika” akaniambia.
“Sawa”
Nilifika Harare kama saa nane mchana. Nikiwa katika kiwanja cha ndege cha Harare nilimpigia simu Chusama kumjulisha kuwa nilikuwa uwanja wa ndege wa Harare. Nilitumia simu ya malipo iliyokuwa pale kiwanja cha ndege.
“Kama umeshafika kodi teksi. Mwambie dereva akupeleke Chapachapa Hotel. Nimekukodia chumba namba 35”
“Natumaini madereva wa teksi watakuwa wanaifahamu ilipo hoteli hiyo”
“Wanaifahamu. Ni hoteli maarufu”
“Sawa. Ngoja nikodi teksi”
Baada ya kumaliza kuzungumza na mwenyeji wangu huyo nilitoka nje ya uwanja wa ndege na kukodi teksi. Sasa nilikuwa natumia kingereza kitupu.
Nilimwammbia dereva wa teksi anipeleke Chapachapa Hotel. Baada ya mwendo wa saa moja kasorobo akanifikisha katika hoteli hiyo iliyokuwa katikati ya jiji la Harare.
.
Baada ya kumlipa dereva pesa aliyotaka niliingia hotelini humo. Unapoingia unakutana na ukumbi mwanana uliokuwa na viti na meza.
Kwenye meza moja iliyokuwa karibu na mlango aliketi msichana mmoja mrembo aliyekuwa akinywa soda huku akisoma gazeti. Upande wa kushoto wa ukumbi huo ndio palikuwa mapokezi.
Nikaenda hapo mapokezi na kujitambulisha kuwa nilikuwa mgeni wa Isaac Chusama na kwamba aliniambia kuwa amenikodia chumba namba 35.
“Oh ndiye wewe! Hebu lete paspoti yako tuione” Mhudumu wa mapokezi ambaye alikuwa msichana akaniambia.
Nikampa paspoti yangu iliyokuwa mkononi kama kitambulisho changu huku tukizungumza Kiingereza.
Baada ya kuifungua paspoti yangu na kuiona picha yangu alinirudishia.
Nikapelekwa chumba namba 35 kilichokuwa ghorofa ya kwanza. Nilikuta kiyoyozi, tv na simu ya mezani iliyowekwa kwenye kimeza kilichokuwa kando ya kitanda. Pia kulikuwa na kochi moja refu na kabati la kuwekea nguo pamoja na meza ya kuvalia iliyokuwa na kioo kikubwa.
Nilipoona ile simu niliweka begi langu juu ya kochi nikaketi kitandani na kuinua mkono wa simu.
Simu zilikuwa zinapitia kwa opereta aliyekuwa hapo hoteli ambaye alipopokea simu yangu nilimpa namba ya Isaac Chussama.
Sekunde chache tu baadaye nikaisikia sauti ya Chusama.
“Helow!”
“Mimi ni yule mgeni wako kutoka Tanzania, nimeshafika katika hoteli ya Chapachapa”
“Umepewa chumba?”
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 04

ILIPOISHIA
“Ninaongea na wewe nikiwa chumbani”
“Sawa. Kama utahitaji chakula au kinywaji chochote agiza tu, nimeweka oda kwa ajili yako”
“Sawa”
“Nitakuja kuonana na wewe baada ya dakika chache”
“Nakusubiri”
Baada ya hapo kukawa kimya. Nikaurudisha mkono wa simu kisha nikatoka humo chumbani. Nilifunga mlango kwa funguo nikashuka chini.
Unaposhuka chini unatokea pale mapokezi, nikaenda kukaa kwenye meza moja katika ule ukumbi. Yule msichana niliyemuona ameketi nilipoingia alikuwa bado ameketi akisoma gazeti.
Nilikuwa nimevutiwa na umbile lake la kupendeza na sura yake jamali.
Lakini laiti kama ningetambua tukio ambalo lingetokea hapo hoteli ningeahirisha mapema safari yangu!
SASA ENDELEA
Baada ya kuketi mhudumu alikuja kuniuliza kama nilikuwa nahitaji kitu, akanipa menyu.
Kwenye menyu niliona ugali kwa samaki. Nikatamani kula ugali wa Kizimbabwe. Nikamuagiza mhudumu huyo aniletee ugali kwa samaki.
Wakati nasubiri nilitewe ugali nilioagiza, nilimuona mtu mmoja aliyekuwa amevaa suti nyeusi akiingia hapo hoteli. Alipomuona yule msichana aliyekuwa amekaa karibu na mlango alisita kisha akavuta kiti na kuketi naye. Nikaona wanazunguma ingawa sikuweza kusikia walikuwa wanazungumza nini.
Mhudumu alimfuata yule mtu, nikaona anaagiza kitu. Baadaye kidogo waliletewa chupa mbili za bia na kuanza kunywa. Mimi nilikuwa nimeshaletewa chakula nilichoagiza.
Nilikuwa nikila ugali huku jicho langu likiwa kwa wale watu. Kama sijakosea walikunywa bia mbili mbili. Mimi nilikuwa nimeshamaliza ugali wangu wakati yule mtu alipoinuka na kwenda mapokezi. Alizungumza na mhudumu wa mapokeziki kabla ya kupewa funguo.
Baada ya kupewa funguo alirudi kwa yule msichana akazunguma naye akiwa amesimama. Baada ya muda kidogo msichana aliinuka wakaenda kupanda ngazi.
Nilihisi kama vile yule mtu alikuwa amechukua chumba na alikuwa akielekea chumbani na yule msichana. Huenda walikuwa wakijuana na kwamba yule msichana alikuwa akimsubiri yule jamaa pale.
Niliendelea kuketi pale pale nikiangalia televisheni iliyokuwa imepachikwa katika ukuta. Nilipoona muda unazidi kwenda niliondoka nikarudi chumbani kwangu na kumpigia simu mwenyeji wangu.
Nilitaka kumuuliza mbona hatokei kwani muda mrefu ulikuwa umepita tangu aliponiahidi kuwa anakuja. Simu ikaita kwa muda mrefu bila kupokelewa.
Simu ilipokata nikapiga tena lakini pia haikupokelewa. Nikaamua kusubiri kabla ya kupiga tena.
Kwa vile sikuwa na kingine cha kufanya, niliona nijilaze pale kitandani. Bila kujitambua usingizi ukanipitia hapo hapo.
Nilipozinduka ilikuwa usiku. Niliwasha taa kisha nikatazama saa. Ilikuwa saa mbili na robo usiku. Nikapiga tena simu lakini bado simu ilikuwa ikiita tu bila kupokelewa.
Nikawa nimechukia. Nilihisi huyo mtu aliyefanya niende Zimbabwe hakuwa na ahadi za kweli. Nikaenda kuoga. Niliporudi nilipiga simu tena. Nilipiga mara tatu bila kupokelewa. Simu ilikuwa inaita tu.
Nikashuka chini na kula chakula kisha nikarudi tena juu. Nikapiga tena simu lakini haikupokelewa. Ilikuwa kama vile simu ilikuwa peke yake au mwenye simu aliamua kunisusia.
Kusema kweli nilichanganyikiwa. Nilikuwa sijui la kufanya. Nikalala. Asubuhi nilipoamka kitu cha kwanza kilikuwa kupiga simu. Simu ya Chusama bado ilikuwa ikiendelea kuita tu. Sasa nikaanza kupatwa na wasiwasi.
Nikashuka chini na kupata kifungua kinywa. Wakati naendelea kunywa chai. Nilisikia nung’unung’u hapo hoteli kuwa kuna mtu aliyeuawa akiwa ndani ya chumba cha hoteli.
Tukio hilo liligunduliwa na mhudumu wa usafi ambaye aliingia katika chumba hicho na kukuta maiti ya mwanaume iliyokuwa imelazwa chini.
Baadaye polisi walifika hapo hoteli. Waliongozwa na baadhi ya wafanyakazi wa hoteli hiyo kuelekea katika chumba hicho kilichokuwa ghorofa ya kwanza. Na mimi kwa kutaka kupata ukweli niliinuka nilipokuwa nimeketi nikaelekea huko huko.
Kilikuwa chumba kilichopakana na chumba nilicholala mimi. Mlango ulikuwa umeachwa wazi na polisi pamoja na baadhi ya wafanyakazi walikuwa wameingia ndani.
Sikuweza kumuona vizuri mtu huyo mpaka mwili wake ulipokuwa unatolewa ukiwa kwenye machela. Nilipomuona tu nikamtambua. Alikuwa ni yule mtu ambaye alifika jana yake pale hoteli na kuzungumza na yule msichana na kisha wakaondoka pamoja kuelekea chumbani.
Hata hivyo yule msichana aliyekuwa naye hakuwepo. Ilisemekana kwamba alitoroka kabla ya tukio hilo kugundulika.
Mpaka mwili wa mtu huyo unatolewa, polisi hawakuwa wamegundua mtu huyo alikuwa ameuawa kwa kitu gani. Kwenye pua yake na kwenye pembe moja ya midomo yake kulikuwa na michirizi ya damu iliyoganda.
Kulikuwa na baadhi ya wafanyakazi ambao walichukuliwa na polisi kwenda kutoa maelezo.
Nikajiuliza kama yule mwanamke alikuwa muuaji kweli. Hakuonekana kuwa katili. Niseme ukweli kama ndiye aliyemuua yule mtu, tukio lile lingenikuta mimi kwani jana yake ilibaki kidogo niende nikakae naye.
Nikashukuru kwamba Mungu alikuwa ameninusuru.
Ingawa tukio hilo lilichnaganya akili yangu lakini kitendo cha mwenyeji wangu kutopokea simu kilinichanganya zaidi. Niliingia chumbani na kutafakari nifanye nini. Kwa kweli sikupata jibu.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 05


ILIPOISHIA
Ilipofika saa saba mchana wakati natazama taarifa ya habari kwenye televisheni, lile tukio la mauaji lililotokea pale hoteli lilitangazwa.
Kitu ambacho kilinishitua ni kuwa mtangazaji alimtaja marehemu kuwa ni Isaac Chusama mtu ambaye alikuwa hafahamiki alikuwa akifanya kazi gani. Alitaja mtaa aliokuwa akiishi na kueleza kuwa hakuwa na mke wala watoto.
Taarifa ilieleza kuwa Chusama alifika hapo hoteli majira ya mchana na kuzungumza na msichana mmoja aliyekuwa ameketi kwenye ukumbi wa hoteli hiyo kabla ya kukodi chumba na kuingia chumbani na msichana huyo.
Taarifa ya televisheni iliendelea kueleza kuwa asubuhi ya siku ile mhudumu wa usafi wa hoteli hiyo aliigundua maiti ya Chusama iliyokuwa imelazwa chini na kutoa taarifa kwa uongozi wa hoteli.
SASA ENDELEA
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, uchunguzi wa madaktari umeonesha kuwa marehemu alikabwa koo hadi mauti yakamkuta.
Msemaji wa polisi akaeleza kuwa polisi wanamshuku msichana aliyekuwa naye kuhusika na mauaji hayo na wameanzisha msako wa kumtafuta.
Baada ya taarifa hiyo kutolewa kwenye televisheni, nilibaini kuwa mtu aliyefika hapo hoteli na hatimaye kuuawa alikuwa ni mwenyeji wangu Isaac Chusama!
Hapo niligundua sababu ni kwanini simu nilizokuwa nikipiga zilikuwa hazipokelewi. Zilikuwa haipokelewi kwa sababu Chusama mwenyewe alikuwa ameshauawa. Bila shaka alikuwa ameuawa siku iliyopita.
Sasa nikabaki na maswali kuhusiana na tukio hilo. Nilijiuliza yule msichana alikuwa nani?
Je alikuwa akijuana na Chusama?
Na ni kwanini amemuua?
Pia nilijiuliza baada ya Chusama kuuawa, kulikuwa na uwezekano kweli wa kulipwa pesa zangu? Na ni nani atanilipa?
Baada ya kufikiri kwa kina niliona uwezekano wa kulipwa pesa zangu haukuwepo. Kwani licha ya kuwa ni pesa nyingi nilizokuwa nikimdai Chusama pia nilikuwa si mwenyeji wa hapo na pengine nisiaminike na huyo ambaye atapaswa kulipa deni hilo.
Lakini baya zaidi, nilijiambia kama nitajitia kuwatafuta ndugu na jamaa wa Chusama ili wanilipe deni hilo wanaweza kuniripoti polisi na nikakamatwa na kuhusishwa na mauaji ya Chusama. Hapo nikaingiwa na hofu.
Matumaini ya kupata pesa nilizozifuata huko Zimbabwe yakaanza kuota mbawa. Kule kukata tamaa na kuona safari niliyoifanya ilikuwa ya bure, nilijikuta nikimlaumu Chusama kwa uzembe. Licha ya kutojua kama yule msichana alikuwa na uhusiano naye au la, nilimlaumu Chusama kwa kuonesha kuwa na tamaa ya ngono iliyopitiliza.
Niliamini kuwa Chusama alipokuwa anakuja pale hoteli alikuwa akinifuata mimi lakini ghafla akili yake ilikwenda kwa yule msichana akasahahu kwamba nilikuwa na ahadi naye na hata nilipompigia simu hakupokea. Matokeo yake yalikuwa ni kuuawa.
Lakini ni kwanini auawe? Nikajiuliza na
kuendelea kujiuliza, yule msichana alikuwa nani? Ana kisa naye gani na baada ya kumuua Chusama, alipotelea wapi?
Sikuweza kupata jibu hata la kukisia. Nilikuwa nimeketi pale ukumbini nikainuka na kurudi chumbani.
Wakati ninapanda ngazi nilijiambia ni vizuri niondoke haraka hapo Zimbabwe kwani licha ya kuwa nisingepata faida yoyote kwa kuendelea kukaa hapo bali pia nilitaka kuepuka uchunguzi wa polisi.
Nilihisi kwamba katika uchunguzi wao polisi wanaweza kugundua kwamba Chusama alikuwa amenipangia chumba pale hoteli na ninaweza kukamatwa na kuulizwa nilikuwa na mpango naye gani.
Baada ya kuingia chumbani nilichukua begi langu nikatoka kimya kimya. Nilikodi teksi na kurudi kiwanja cha ndege. Kwa bahati njema nilikuta kulikuwa na ndege inayokwenda Botswana ambayo bado ilikuwa na nafasi.
Nikakata tikiti ya ndege ya kwenda Botswana. Ndege iliondoka maasaa matatu baada ya mimi kufika kiwanja cha ndege. Nilipofika Gaborone, nilimpigia simu Benjamin Muhoza na kumjulisha kuwa nilikuwa katika kiwanja cha ndege cha Gaborone.
“Subiri ninatuma gari ikufuate” Sauti ya Muhoza ikasikika kwenye simu.
“Dereva wako atanitambuaje” nikamuuliza.
“Umevaa mavazi gani?”
“Kwanza mimi ni mrefu wa wastani na mweupe. Nimevaa tisheti ya rangi ya samli, suruali aina ya jinzi ya rangi ya samawati. Nimevaa miwani ya jua”
“Atakutambua. Nitakupa namba ya usajili ya gari atakalokuja nalo”
“Sawa”
Muhoza alinitajia namba ya usajili ya gari hilo, aina yake na rangi yake. Nikamwambia nitalitambua litakapofika.
Saa moja baadaye nikiwa hapo nje ya jengo la uwanja wa ndege nikaliona gari hilo likiwasili. Sikutaka kumpa dereva wa gari hilo taabu ya kunitafuta. Nikamfuata.
Baada ya kujitambulisha kwake kuwa mimi ndiye mgeni wa Chusama aliniambia nijipakie kwenye gari.
Nilijipakia katika siti ya mbele iliyokuwa kando ya dereva. Gari hilo lilinipeleka katika hoteli moja ambapo mwenyeji wangu tayari alikuwa amenichukulia chumba.
“Sasa acha nimfuate mheshimiwa” Dereva akaniambia baada ya kunifikisha hapo hoteli. Akaongeza.
“Aliniambia nikishakufikisha hapa hoteli nimfuate”
“Sawa” nikamjibu. Wakati huo nilikuwa nimekaa katika bustani iliyokuwa mbele ya hoteli ambayo iliwekewa viti na meza.
“Unaweza kuagiza kinywaji unachotaka au chakula”
“Labda kinywaji tu, sitapenda kula kitu chochote kwa sasa” nikamwambia.
Dereva huyo alipoondoka muhudumu alinifuata na kuniuliza kama nilikuwa ninahitaji huduma yoyote.
“Nipatie soda tu” nikamwambia.
“Soda gani?”
“Fanta”
Mhudumu akaondoka. Baada ya muda mfupi alirudi na kuniletea soda niliyomuagiza.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 06

ILIPOISHIA
Wakati namaliza kunywa ile soda nikaona lile gari likisimama kando ya hoteli akashuka dereva wa gari hilo na mtu mwingine aliyekuwa amevaa suti nyeusi. Pia alishuka msichana.
Watu hao watatu wakaingia katika eneo la hoteli. Kitu ambacho kilinishitua na kunipa mshangao ni kuwa yule msichana
alikuwa ndiye yule muuaji wa Isaac Chusama aliyekuwa akitafutwa na polisi kule Zimbabwe.
Kwa kweli nilipomuona kwa mara nyingine nilishituka sana. Yule msichana aliketi katika meza iliyokuwa mbali na meza yangu. Dereva wa lile gari pamoja na yule mtu mwingine wakaja katika meza niliyokuwa nimeketi.
“Mgeni mwenyewe ni huyu hapa” Yule
dereva akamwambia yule mtu ambaye alinipa mkono kunisalimia.
Baada ya kusalimiana naye alikaa kwenye kiti akanitambulisha kuwa yeye ndiye Benjamin Muhoza niliyekuwa ninawasiliana naye.
Na mimi nikamtambulisha jina langu na kumueleza kuwa nilikuwa mjukuu wa marehemu babu yangu mzee Fumbwe Limbunga.
SASA ENDELEA
“Nimefurahi kukufahamu. Uliniambia kuwa ungekuja na hati zote za marehemu Limbunga zilizohusu biashara yetu na pia hati ya mahakama inayokuthibitisha kuwa wewe ndiye mrithi wa marehemu” Mtu huyo aliniambia kwa sauti tulivu.
“Nimekuja na hati zote”
“Nitolee”
Nikafungua mkoba wangu ambao nilikuwa nimeuweka juu ya meza, nikatoa hati mbalimbali. Kwanza nilimuonesha cheti cha kifo cha mzee Fumbwe Limbunga akakitazama kwa makini.
Kisha nilimtolea hati ya mahakama iliyonithibitisha mimi kuwa mrithi wa Fumbwe limbunga. Hati hiyo niliiwekea picha yangu kama mrithi na picha ya marehemu kama mrithiwa.
Muhoza aliitazama hati hiyo kwa unagalifu.
Nilimuachia sekunde thelathini ili amalize kuisoma hati hiyo iliyokuwa imeandikwa kwa kingreza kisha nikamtolea mkataba
ambao aliwekeana saini yeye na babu.
Alipouona ule mkataba alinitazama akatingisha kichwa chake kuonesha kunikubalia.
“Nafikiri nimeweza kukuthibitishia” nikamwambia wakati akiupekua ule mkataba.
“Hakuna tatizo. Nimeona hapa kuwa mzee Fumbwe amefariki na wewe ndiye mrihi wake ambaye unapaswa kulipwa madeni ya marehemu”
Aliponiambia hivyo alinyamaza kimya kwa sekunde kadhaa kabla ya sauti yake kusikika tena.
“Hivi unaiendeleza ile biashara ya marehemu babu yako?”
Nikatikisa kichwa.
“Hapana. Ile biashara ilikuwa ni yake mwenyewe. Mimi sikuhusika nayo”
“Huwezi kuyapata yale madini ya Tanzanite?”
“Sijui marehemu alikuwa akiyapata wapi”
“Na hakuna mtu yeyote unayenfahamu anayefanya biashara ile huko Tanzania?”
“Labda nikuulizie halafu nikufahamishe kwenye simu”
Nilipomwammbia hivyo mtu huyo alinyamaza tena kama aliyekuwa akiwaza.
Baada kimya cha sekunde kadhaa aliniambia.
“Sasa sikiliza, nipe muda niweze kukutayarishia pesa zako”
“Muda gani?” nikamuuliza.
“Muda wa siku moja tu, yaani kesho asubuhi ninakupatia pesa zako uende zako”
“Naweza kusubiri mpaka kesho. Hata hivyo nisingeweza kuondoka leo”
“Sawa. Nimekuchukulia chumba hapa hoteli, utakula, utakunywa. Gharama ni juu yangu. Wewe hutalipa chochote hadi hapo kesho tutakapomalizana mimi na wewe”
“Sawa”
“Nitakufuata kesho saa tatu”
Aliniambia na kuinuka kwenye kiti. Tukaagana kisha akaondoka pamoja na dereva wake. Walikwenda kwenye ile meza aliyoketi yule msichana. Yule mtu alikaa kwenye kiti lakini dereva wake aliondoka.
Niliona wakiagiza vinywaji. Wakaendelea kunywa na kuzungumza kwa karibu masaa matatu kabla ya kuondoka.
Kitu ambacho kilitia shaka katika moyo wangu ni kuhusu yule msichana muuaji ambaye alidaiwa kumuua mtu kule Zimbabwe na hatimaye kuibukia hapo Botswana.
Nilijiuliza yule msichana ni nani na ni kwanini alipotoka kumuua Chusama, mtu ambaye nilikuwa na mipango naye, amekwenda huko Boswana kwa mtu mwingine ambaye pia nilikuwa na mipango naye.
Nikaendelea kujiuliza iwapo Muhoza alikuwa na uhusiano na yule msichana na kama alikuwa anajua kama msichana huyo alikuwa anatafutwa na polisi wa Zimbabwe kwa mauaji.
Kusema kweli sikupata jibu licha ya kujiuliza maswali kadhaa kichwani mwangu.
Mwenyeji wangu alipoondoka na yule msichana na mimi niliondoka na kwenda chumbani kwangu. Nikajilaza kwenye kitanda huku mawazo yangu yakiwa kwenye utajiri.
Nilijiambia ingawa nilizikosa pesa a Chusama baada ya kuuawa, nitaziata pesa za Muhoza ambazo nikichanganya na pesa nitakazopata kutoka kwa Dube wa Afrika Kusini nitakuwa tajiri.
Nikajiwazia mipango ya maendeleo. Nilijiambia nitakaporudi Tanzania nitanunua gari la kifahari pamoja na kuanzisha miradi mikubwa ya biashara. Baada ya hapo nitatafuta mke nioe.
Wakati nikiwaza hayo nilisikia mlango ukibishwa, nikainuka na kwenda kuufungua. Niliona wasichana wawili waliokuwa wamejipodoa huku nyuso zao ziking’ara kwa mkorogo.
Walikuwa wamesimama kando ya mlango wakiwa wamevaa nguo fupi huku matiti yao yaliyokuwa yametuna kama mipira yakiwa nusu nje.
“Naweza kuwasaidia? Nikawambia.
Walinisalimia kwa heshima na kuanza kujitambulisha majina yao lakini sikujua mara moja kitu walichokuwa wanahitaji.
Nikawambia kuwa nimefurahi kuwafahamu. Mmoja wapo akaniuliza jina langu. Nikamtajia.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 07

ILIPOISHIA
Walipoona uso wangu ulikuwa umeota alama ya kuuliza waliniambia.
“Tulitaka kukuchangamsha tu mgeni wetu. Tunaona umekuwa kimya chumbani, huna mwenzako”
Hapo ndipo nilipoelewa kuwa wale walikuwa changu doa waliokuwa wakijiuza kwenye mahoteli.
Mawazo yangu yalikuwa tofauti na wao kwa upande mmoja na yalikuwa yanalingana na wao kwa upande mwingine.
Yalikuwa tofauti na wao kwa upande mmoja kwa sababu kilichonipeleka Botswana hakikuwa kufuata machangudoa na yalilingana na wao kwa upande mwingine kwa sababu wao walikuwa wakitafuta pesa kwa njia zao na mimi vile vile nilikuwa natafuta pesa.
Nilipowaza hivyo nilijikuta nikitabasamu.
“Karibuni” nikawambia huku nikijiambia mwenyewe kuwa si vibaya kuzungumza nao mawili matatu kupitisha wakati.
Wasichana hao wakaingia mle chumbani.
SASA ENDELEA
Wote wawili walikimbilia kukaa kitandani wakaniwekea nafasi nikae katikati yao. Nikakaa.
“Kwanini unataka kulala peke yako wakati sisi tupo?” Msichana mmoja aliyeonekana kuwa na macho ya juu aliniuliza.
“Nimekuja peke yangu, nitalala peke yangu. Mlitaka nilale na nani?” nikamjibu.
“Uchague mmojawapo kati yetu sisi” Msichana wa pili akaniambia.
Kusema kweli hawakuwa malaya wa kuweza kunishawishi. Mkorogo ulikuwa umewaharibu. Lakini nilitaka kuzungumza nao tu nichangamshe akili yangu.
“Je kama nitawachagua nyote itakuwaje?’ nikawauliza huku nikiwatazama kwa zamu.
“Utatuweza?” Mmojawapo akaniuliza.
“Nisiwaweze kwani nyie ni vyuma?”
“Sawa. Utatupa dola ngapi?”
“Tatizo litakuwa hapo kwenye dola”
\
“Utatupa dola ngapi?”
“Sina hata dola moja”
“Si kweli. Huoneshi kuwa huna pesa, usingekaa katika hoteli hii”
“Kwani unatokea wapi?” Msichana mwingine akaniuliza.
“Natokea Zimbabwe”
“Wewe ni Mzimbabwe?”
“Hapana. Mimi ni Mbongo”
Wasichana hao wakaonesha kushituka.
“Mbongo ni mtu wa nchi gani?”
“Mtanzania”
“Kumbe unatoka Tananzia?”
“Unakufahamu?”
“Sijafika lakini tumefundishwa shuleni kwamba Tanzani ilikuwa moja ya nchi zilizokuwa mstari wa mbele kupigania uhuru wa Afrika ikiwemo nchi yetu chini ya uongozi wa Mwalimu Nyerere”
“Sasa kama mnajua hivyo kwanini mnanitoza dola?”
“Ulitaka bure?”
“Ikiwezekana”
Wasichana hao walicheka kisha wakainuka na kusimama. Bila shaka waligundua kuwa nilikuwa nikiwapotezea wakati wao bure.
“Mbona mnakwenda zenu?” nikawauliza.
“Sisi tuko kazini bwana. Hamna bure hapa. Wewe hutaki kutoa pesa yako. Kwaheri” Msichana mmoja akanniambia.
Walitoka na kuniacha. Na mimi niliinuka nikafunga mlango wangu kisha nikarudi kitandani.
Siku ile ikapita nikiwa hapo hoteli.
Asubuhi ya siku iliyofuata nikiwa kwenye mkahawa wa hoteli hiyo nikipata kifungua kinywa, nilimuona dereva wa mwenyeji wangu Muhoza akinifuata. Uso wake ulikuwa umetaharuki.
Akanisalimia kisha akaniambia.
“Bwana Muhoza ameuawa!”
Mshituko ulinifanya niinuke kwenye kiti na kusimama.
“Bwana muhoza ameeuawa?” nikamuuliza kwa mshangao.
“Jana alipoondoka hapa alikwenda katika hoteli nyingine ambako alilala na yule msichana aliyekuwa naye. Aliniambia nimfuate asubuhi. Asubuhi nilipomfuata nikakuta taarifa hiyo. Maiti yake ilikutwa chumbani hii asubuhi”
Nikajiambia, ni yale yale yaliyotokea Botswana.
“Kwani yule msichana aliyekuwa naye ni nani?” nikamuuliza yule dereva.
Dereva huyo akabetua mabega yake.
“Simfahamu na sijui walikutana wapi”
“Yule ndiye aliyehusika na mauaji hayo!”
“Inaaminika hivyo kwa sababu amekimbia”
“Hebu kaa nikueleze kitu” nikamwambia Yule mtu huku na mimi nikikaa.
“Unajua mimi natokea Botswana. Yule msichana nilimkuta katika hoteli niliyofikia pale Botswana. Baadaye nilimuona akiwa na mwenyeji wangu na wakachukua chumba pale pale hoteli. Asubuhi yake mwenyeji wangu akakutwa ameuawa katika chumba cha hoteli na yule msichana hakuonekana. Sasa nilipofika hapa Zimbabwe nilishangaa kumuona tena akiwa na Muhoza” nikamueleza yule mtu.
“Kwanini hukutuambia tangu jana?”
“Nilishindwa kuwambia, nilijua labda wanajuana”
“Sasa yule msichana atakuwa ni nani na anatokea wapi?”
Nikaguna na kushusha pumzi ndefu.
“Hicho ni kitendawili na sidhani kama atapatikana”
“Anaweza kupatikana”
“Nilikuwa namdai Muhoza pesa nyingi na tulikubaliana kwamba angenilipa hii asubuhi. Sasa sijui nitafanyaje?”
“Huyu jamaa kama ulikuwa na mipango naye ya pesa ni bora usamehe. Kwanza mimi siwajui ndugu zake na isitoshe alishatengana na mke wake miaka mingi iliyopita”
Nikatikisa kichwa change kusikitika.
“Mkosi gani huu jamani…!” nilijisemea kimoyomoyo.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 08

ILIPOISHIA
Yule dereva wa Muhoza alipoondoka pale hoteli sikumuona tena. Nikalala pale hoteli hadi siku iliyofuata ambapo nililazimika kujilipia mwenyewe chumba.
Nikafanya mipango ya usafiri wa kwenda Afrika Kusini. Nikagundua kuwa ulikuwepo usafiri wa treni wa kutoka Zimbabwe hadi hadi Afrika Kusini.
Nikasafiri kwa treni hadi Cape Town. Nilipofika kwenye kituo cha treni cha Cape town, nikampigia simu Domesan Dube kumjulisha kuwa nilikuwa nimewasili kwa treni kutokea Zimbabwe.
Dube akaniambia kuwa anamtuma dereva wake anifuate. Baada ya kupita kama saa moja hivi, dereva huyo akawasili na gari. Alinipakia akanipeleka nyumbani kwa Dube.
Wakati anasimamisha gari mbele ya jumba lake la kifahari nilimuona yule msichana muuaji akitoka katika jumba hilo. Alipungia mkono teksi iliyokuwa inapita barabarani. Teksi iliposimama akajipakia na kuondoka.
Yule dereva hakushituka kumuona msichana huyo lakini mimi nilishituka sana.
SASA ENDELEA
Mimi nilishituka kwa sababu nilikuwa namfahamu na nilikuwa nafahamu visa alivyovitenda kule Botswana na Zimbabwe.
Lakini pia nilishituka vile nilivyomkuta Afrika Kusini wakati jana yake tu aliuaa mtu Zimbabwe.
Kitu kingine kilichonifanya nishituke ni kuona msichana huyo alikuwa akinifuatia kwa wale wadaiwa wangu ambapo kile nchi niliyokuwa ninakwenda nilikuwa namkuta akiwa na mtu niliyekuwa namfuata.
Baada ya gari kusimama, dereva alishuka na mimi nikafungua mlango haraka na kushuka. Tayari uso wangu ulikuwa umeshatahariki baada ya kumuona yule msichana.
Dereva alitangulia kuingia ndani ya jumba hilo akaniambia.
“Karibu ndani”
Nikaingia ndani. Tulitokea kwenye sebule pana iliyokuwa imepambwa vizuri.
Mimi na yule dereva tulishituka tulipomuona mtu aliyekuwa amelala chini akiwa ametoa macho karibu na mlango.
“Oh Bwana Dube!” Dereva alitoa sauti ya kimako kisha akachutama na kumtazama yule mtu.
“Bwana Dube…Bwana Dube…!” akamuita huku akijaribu kumtikisa.
Mtu huyo alikuwa kimya huku macho yake yakitazama dari bila kupepesa. Sikuwa daktari na sikuwa na uzoevu wa kutazama miili ya watu waliokufa lakini nilipotazama yale macho, niligundua mara moja kuwa mtu huyo alikuwa ameshakufa.
“Huyo ndiye Bwana Dumesan Dube?” nikamuuliza yule dereva.
“Ndiye yeye. Sijui amepatwa na nini!”
“Kuna msichana alitoka humu ndani wakati tunafika, ni nani?”
Dreva akatikisa kichwa.
“Sikumfahamu. Ngoja nimuite daktari wake, labda ni presha”
Dereva huyo aliyekuwa ametaharuki aliinuka akatoa simu yake na kutafuta namba ya daktari wa Dube kasha akampigia.
“Bwana Dube ameaguka chini, sijui amepatwa na nini?” alisema baada ya simu kupokelewa.
Niliisikia sauti ya upande wa pili ikiuliza.
“Ameanguka wapi?”
“Nyumbani kwake. Nilikuwa nimetoka kidogo niliporudi nilimkuta yuko chini lakini hasemi na inaonekana hana fahamu”
“Subiri, ninakuja”
Dereva akakata simu na kunitazama.
“Daktari wake anakuja. Tumsubiri”
“Kwani Bwana Dube ana tatizo la presha?” nikamuuliza.
“Presha ni tatizo linaloweza kutokea ghafla tu, si lazima uwe nalo siku za nyuma”
Huyo daktari alliyeitwa aliharakisha kufika. Baada ya dakika thelathini tu aliusukuma mlango na kuingia ndani.
Alipomuona Dube akiwa chini hakuuliza chochote, alichutama na kuanza kumpima. Alianza kumpima presha kwa kutumia kipimo cha kufunga kwenye mkono.
Alipomaliza aliinuka na kutuambia.
“Nasikitika kuwambia kuwa Bwana Dube ameshakufa. Apelekwe hospitali kwa uthibitisho zaidi”
“Ameshakufa!” Dereva wa Dube alimaka uso wake ukionesha kutoamini.
“Apelekwe hospitali” Daktari akasisitiza.
“Lakini ni jambo la kushangaza sana kwa sababu niliachana naye muda mchache tu uliopita”
“Umeniambia kwamba alianguka?” Daktari akamuuliza.
“Itakuwa alianguka kwani tulipokuja tulimkuta hapo chini”
“Ana dalili kama ya kukabwa kwenye shingo yake”
Dereva alizidi kupata taharuki.
“Amekabwa? Amekabwa na nani? Humu ndani hakuna mtu. Au aliingia mtu na kumkaba?’
“labda ni yule msichana tuliyemuona akitoka?” nikamwambia.
“Msichana anaweza kumkaba?”
“Anaweza”
“Mimi naondoka. Nimewambia mumpeleke hospitali. Huko atafanyiwa uchunguzi na sababu ya kifo chake itajulikana” Daktari akatuambia na kutoka.
Nikajiambia kwamba kwa vile suala hilo linahusu mauaji, ingebidi lifike polisi na likifika huko, mimi na dereva wa Dube tutakuwa ndio watuhumiwa wa kwanza.
Kwa sababu ya kuogopa ushahidi, sikueleza chochote kuhusu yule msichana, nikamuacha yule dereva akishughulikia suala hilo. Mimi nikatafuta hoteli nikapanga chumba.
Kwa kweli suala la yule msichana muuaji lilisumbua akili yangu. Nilishindwa kujua msichana huyo alitokea wapi na kwanini alikuwa akiwaua wale watu. Pia nilikuwa nikijiuliza alikuwa akiwaua kwa namna gani?
Kile kitendo cha kumuona akitoka katika jumba la Dube kilitosha kunithibitishia kuwa ndiye aliyemuua Dube.
Nilikuwa nina pesa chache ilizobaki ambazo zilitosha kukata tikiti ya kurudi Dar. Asubuhi kulipokucha nikaenda kukata tikiti na kuondoka. Safari yangu haikuwa na mafanikio yoyote. Zaidi ilikuwa ni kupata hasara tu na kupotea muda.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 09


Ndege ilipaa hewani kwa takribani saa sita kabla ya kutua katika kiwanja cha ndege cha Dar es Salaam.
Ndege ilipotua, abiria walianza kushuka. Nilikuwa miongoni mwa abiria wa mwisho mwisho. Nilikuwa nimechoka na nilionesha wazi kukata tamaa.
Wakati namalizia kushuka ngazi ya ndege, macho yangu yalimuona mtu aliyenishitua akiwa mbele yangu.
Alikuwa ni yule msichana muuaji! Alikuwa miongoni mwa abiria waliokuwa wamepanda ile ndege wakitokea Afrika Kusini. Alikuwa amefuatana na mwanamme mmoja aliyekuwa amevaa suti nyeusi wakizungumza.
Kusema kweli sikutambua kama yule msichana alikuwemo ndani ya ndege ile. Nilimgundua wakati ule wa kushuka. Yule mtu aliyekuwa amefuatana naye sikuweza kumtambua.
Tulipotoka nje ya jengo la kiwanja cha ndege, msichana huyo pamoja na yule mtu aliyekuwa amefuatana naye walikodi teksi na kuondoka. Na mimi nikakodi teksi na kumwambia dereva awafuate.
SASA ENDELEA
“Una maana niifuate hii teksi ya mbele yangu?” Dereva wa teksi akaniuliza.
“Ndiyo ifuate hiyo hiyo”
“Inaelekea wapi?”
“Popote itakapoelekea”
“Ina maana wewe hujui inaeleka wapi?”
“Kwani tatizo lako ni nini, hapo tutakapofika utanitoza kiasi utakachotaka”
“Sawa. Nilitaka tupatane tu”
“Hatuwezi kupatana kwa sababu sijui wanakwenda wapi”
“ Nimekuelewa”
Dereva wa teksi akaanza kuiandama teksi iliyokuwa mbele yetu. Wakati mwingine gari lilitinga katikati yetu lakini dereva alijitahidi kuhakikisha teksi hiyo haitupotei.
Wakati tunaendelea kuiandama teksi hiyo, mawazo yangu yalikuwa kwa yule msichana. Bado nilikuwa nikijiuliza msichana yule ni nani na kwanini nakutana naye katika kila nchi ninayokwenda. Pia nilijiuliza yule mtu aliyenaye ni nani na anatoka wapi.
Nilihisi kwamba kwa vile msichana huyo alikuwa katika jiji ambalo nilikuwa nikilijua vyema, ningeweza kufanya uchunguzi na kumgundua.
Hata hivyo jambo moja nilikuwa na uhakika nalo moyoni mwangu kwamba msichana huyo alikuwa wa hatari na muuaji aliyeonekana kuwa na uzoevu wa kuua.
Mara moja niligundua kuwa teksi iliyowapakia ilikuwa ikielekea Mbezi. Tuliendelea kuifuata hadi iliposimama mbele ya jumba moja la kifahari. Dreva wa teksi niliyopanda alitaka kusimama nikamwambia apitilize moja kwa moja.
“Sitaki wagundue kuwa ninawafuata” nikamwambia dereva huyo na kuongeza.
“Utasimama kule mbele”
“Nimekuelewa”
Wakati teksi ikiendelea kwenda, mimi nilikuwa nikitazama nyuma kwenye kioo. Nilimuona yule msichana akishuka kwenye ile teksi pamoja na yule mwanaume aliyekuwa naye. Teksi iliondoka na wao wakafungua geti na kuingia ndani.
Kwa vile nilikuwa nimeshaikariri ile nyumba, nilimwambia dereva wa teksi ageuze anipeleke nyumbani kwangu.
“Umeshawaona?” akaniulia wakati akiigeuza teksi.
“Nimewaona. Nilitaka kujua wanaishi wapi?”
“Kwani ni kina nani wale?”
“Nilisafiri nao kutoka Afrika Kusini. Nilitaka kujua wanaishi wapi hapa dar”
Dereva alitaka kuendelea kuniuliza
lakini alibadili mawazo akanyamaza kimya.
Baada ya nusu saa tu alinifikisha katika mtaa ninaoishi. Aliisimamisha teksi mbele ya nyumba yangu nikamuuliza gharama yake ni kiasi gani.
Alinitajia kiasi alichotaka nikatoa pochi yangu na kumpa kiasi hicho bila kusita.
“Asante sana” nilimwambia huku nikifungua mlango wa teksi na kushuka.
Huku nikiwa na begi langu nilikwenda kufungua mlango wa nyumba yangu nikaingia ndani. Niliondoka kwenda nje ya nchi kwa matumaini ya utajiri lakini nimerudi kama masikini. Safari yangu haikuwa na mafanikio yoyote, nilijiambia kwa huzuni.
Mbali ya kutokuwa na mafanikio, ilikuwa safari ya balaa na iliyonitia hofu kutokana na wale watu niliowafuata kuuawa mmoja baada ya mwingine, tena wameuawa na msichana huyo huyo ambaye aliwafuata Botswana, Zimbabwe na Afrika Kusini.
Msichana yule sasa amekuwa ni kitendawili ambacho nilihitaji kukitegeua kadiri itakavyowezekana. Kwa vile nilikuwa nimeikariri sura yake pamoja na nyumba aliyoingia, niliamini kwamba ningewea kumfuatilia na kumjua vizuri.
Siku ile ikapita. Asubuhi ya siku iliyofuata wakati nimeketi sebuleni nikitazama televisheni, niliona kitu kilichonishitua.
Kilikuwa ni kipinidi cha taarifa ya habari. Habari ya kwanza kutangazwa na kuoneshwa ilikuwa ya mauaji ya mkazi mmoja wa Mbezi aliyetajwa kwa jina la Abdul Baraka.
Hilo jina lilinishitua kwa sababu lilikuwa katika orodha ya wale wadaiwa wa marehemu babu yangu. Jina hilo lilikuwa la kwanza na mtu huyo ndiye niliyeanza kumpigia simu lakini simu yake haikupatikana nikaamua nimuache kiporo.
Yeye hasa ndiye aliyekuwa tegemeo langu baada ya wale watu niliowafuata nje ya nchi kuuawa na kusababisha nisipate kitu.
Taarifa hiyo ya televisheni ilieleza kwamba mwili wa Abdul Baraka ulikutwa mchana wa jana yake nyumbani kwake ukiwa umelazwa sebuleni.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 10

Uchunuzi wa madaktari wa hospitali ya Muhimbili ulionesha kuwa marehemu aliuawa kwa kukabwa koo na kukosehwa pumzi kwa zaidi ya dakika tano jambo lililosababisha moyo wake kusimama na hivyo kusababisha kifo chake.
Sasa mshituko mkubwa niliupata wakati picha ya Abdul Baraka ilipooneshwa. Alikuwa ni yule mtu niliyemuona amefuatana na yule msichana muuaji jana yake.
Hapo hapo nikajua kwamba aliuawa na yule msichana ambaye alitoweka baada ya kufanya mauaji hayo.
Nikajiuliza ni kwanini hawa watu wanaodaiwa na marehemu babu yangu wanauawa na anayewaua ni mtu mmoja tena msichana, amezunguka nchi zote kuwafuata?
Jambo jingine la ajabu nililoliona ni kuwa mauaji hayo yanafanyika wakati ule ninafuatilia madeni hayo. Kulikoni!
Nilitamani kwenda polisi kueleza nilichokuwa ninakifahamu kuhusu yule msichana lakini niliogopa kwa sababu sikuwa nikijua yule msichana alikuwa nani. Angeweza kuwa gaidi au ni mtu aliyetumwa kufanya mauaji.
Nikajiambia kama nitajitia kimbele mbele cha kumripoti polisi ningeweza kuuawa. Nikaamua kuwa kimya.
Wiki moja ikapita. Siku hiyo nilikuwa nimekaa nyumbani kwangu nikiwaza, simu yangu ikaita.
SASA ENDELEA
Namba iliyokuwa ikinipigia ilikuwa ngeni kwangu. Nikaipokea ile simu.
“Hello!”
“Hello, nazungumza na Kassim Fumbwe?’ Sauti ya mwanamke ikaniuliza.
“Ndiyo. Kassim Fumbwe. Nani mwenzangu”
“Naitwa Ummy. Nilikuwa na mazungumzo na wewe. Nilihitaji tukutane”
Moyo wangu ulishituka kidogo.
“Tukutane wapi?”
Mimi niko Suzy Hotel hapa Masaki. Niko chumaba namba 35. Ukifika utanikuta”
Nikasita kidogo kabla ya kumuuliza.
“Unanifahamu vipi?”
“Ninakufahamu. Kama unataka kujua zaidi nitakufahamisha utakapofika”
“Hayo mazungumzo yanahusu nini?”
“Yanahusu mali za marehemu babu yako”
Aliponiambia hivyo sikutaka kuendelea kumhoji, nikamwambia.
“Nisubiri ninakuja sasa hivi”
Simu ya upande wa pili ikakatwa. Nilikuwa nimeketi sebuleni nikainuka na kutoka. Gari langu ambao nililirithi kwa babu nilikuwa nimeliegesha nje. Nikajiapakia na kuliwasha.
Gari lilipowaka nilitia gea na kuelekea Masaki huku nikijiuliza huyo mwanamke aliyenipigia simu alikuwa nani na alitaka kunieleza nini kuhusu mali za marehemu babu yangu.
Kilichonifanya nikurupuke na kumfuata haraka haraka ni ule utata wa mali za marehemu babu. Babu alikuwa tajiri lakini baada ya kufa alionekana hakuwa na mali yoyote.
Nilitarajia kuwa mwanamke huyo alikuwa akijua siri ya mali za marehemu babu na angenifichulia.
Nilipofika Suzy Hotel iliyokuwa Masaki niliegesha gari katika eneo la kuegeshea kisha nikatoa simu na kumpgia yule mwanamke.
“Nimeshafika?” nikamwambia.
“Uko wapi?” Sauti ya mwanamke ikauliza kwenye simu.
“Niko hapa mbele ya hoteli”
“Njoo chumba namba 35 kipo ghorofa ya kwanza”
“Sawa”
Nikashuka kwenye gari na kuingia hotelini humo. Nilipanda ngazi hadi ghorofa ya kwanza, nikakitafuta chumba namba 35. Nilipokiona nikakifuata na kubisha mlango.
Baada ya sekunde chache tu mlango
ulifunguliwa na msichana.
“Karibu ndani” akaniambia huku akitabasamu.
Nilipomtazama vizuri, sura yake ikanijia akilini mmwangu.
Alikuwa ni yule msichana muuaji niliyekutana naye Botswana, Zimbabwe na kisha Afrika Kusini.
Nilipogundua kuwa alikuwa ni yeye nilishituka nikarudi nyuma hatua moja
kisha nikageuka na kutoka mbio.
“Mbona unakimbia?” Niliisikia sauti yake ikiniuliza kwa nyuma.
Sikujibu wala sikusimama. Nilishuka ngazi mbili mbili nikafika chini. Pale chini niliona nikikimbia nitawatia watu wasiwasi nikatembea taratibu na kutoka
nje ya hoteli. Nikajipakia kwenye gari langu na kuliondoa kwa kasi.
Bila shaka yule mwanamke alitaka kunimaliza na mimi, nilijiambia kimoyomoyo huku nikizidi kukanyaga mafuta.
Nilishindwa kujua aliipataje namba yangu na alijuaje kuwa ninaitwa Kassim Fumbwe kwani aliponipigia simu aliniuliza kama mimi ni Kassim Fumbwe.
Aliponipigia simu sikutarajia kama alikuwa ni yeye. Si kwa sababu ya kunitambua kuwa mimi ni Kassim Fumbwe bali vile alivyoniambia kuwa ana mazungumzo na mimi kuhusu mali ya babu yangu.
Nikahisi kwamba likuwa akijua mengi kuhusu mimi hasa vile ambavyo alihusika katika safari yangu nzima kutoka Botswana, Zimbabwe, Afrika Kusini hadi kurudi tena Tanzania.
Sasa nikapata wazo moja kwamba ni kweli alikuwa akiifahamu siri ya mali ya marehemu babu yangu kwa sababu yeye ndiye aliyeifanya safari yangu isiwe na mafanikio. Yeye ndiye aliyewaua watu wote waliokuwa wakidaiwa na babu yangu. Sababu za kuwaua alikuwa akizijua mwenyewe.
Nikaendelea kujiambia, kwangu mimi msichana huyo atabaki kuwa adui. Ingawa sikuweza kujua ni kwanini aliwaua wale watu lakini nilijenga hofu kwamba alitaka kuniua na mimi.
Hii ndio sababu nilimkimbia pale hoteli.
Nilipofika nyumbani nilikaa sebuleni na kuendelea kujiwazia kuhusu yule mwanamke. Ghafla simu yangu ikaita. Nilipotazama namba nikaona ni ile ya yule msichana. Nikaipokea.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 11

ILIPOISHIA
“Mbona umekimbia?” Sauti ya msichana ikaniuliza.
“Hebu niambie ukweli wewe ni nani?” nikamuuliza.
“Kama ulikuwa hunijui kwanini umenikimbia?”
“Nimekukimbia kwa sababu”
“Sababu gani?”
“Wewe si nilikukuta Botswana siku chache ziliopita halafu nikakuona tena Zimbabwe na jana ulikuwa Afrika Kusini?”
“Kumbe umenikariri vizuri”
“Nimekukariri kwa sababu nimeona kila nchi niliyokwenda nilikuwa nakuona”
“Ndiyo sababu nilitaka kukutana na wewe”
“Kwani wewe ni nani? Unamjuaje marehemu babu yangu na umenijuaje mimi?”
SASA ENDELEA
“Sasa hayo ndiyo mambo ambayo tutazungumza tutakapokutana ”
Nikatikisa kichwa changu ingawa niliyekuwa nikizungumza naye hakuwa karibu yangu.
“Hilo la kukutana na wewe litakuwa gumu kidogo”
“Hutaki kujua zilipo mali za marehemu babu yako”
“Ninataka sana lakini kuna mambo
ambayo yamenishitua”
“Niambie ni mambo gani?”
“Kuna watu ambao ulikuwa karibu nao.
Hao watu waliuawa katika mazingira ya kutatanisha” nikamwambia.
“Wapi huko?”
“Botswana, Zimbambwe na Afrika Kusini”
“Umetaja lakini bado mmoja”
“Abdul Baraka wa Mbezi hapa Dar aliuawa pia”
“Waliuawa na nani?”
“Nilikuona wewe na Abdul Baraka mkishuka kwenye ndege kutoka Afrika
Kusini”
“Swali nililokuuliza, wameuawa na nani?”
Hapo niligwaya kujibu. Niliona kama
nitamwambia aliwaua yeye anaweza kukasirika na akajua kuwa nina ushahidi kuwa yeye nndiye muuaji. Akipata uhakika huo nilihofia kuwa anaweza kunisaka kwa udi na uvumba ili aniue.
Nikamuuliza. “Uliponiambia bado mmoja ulikuwa na maana gani?”
“Nilikuwa nina maana unayoijua wewe”
“Mimi sijui kitu”
“Haiwezekani kuwa hujui kitu. Usingeniambia kuwa kuna watu walikuwa karibu na mimi na wameuawa. Ulikuwa na maana gani?”
“Usinielewe vibaya. Nilimaanisha hao watu walikuwa na wewe kabla ya kuuawa”
“Hao watu wanakuhusu?”
“Walikuwa wakidaiwa na marehemu babu yangu”
“Tunarudi pale pale katika mali ya marehemu babu yako. Bado hutaki kujua kile kilicho nyuma ya pazia”
“Ninataka”
“Sasa naomba kukutana na wewe kwa mara nyingine”
Nikafikiri kidogo kisha nikamwambia.
“Kwanini tusizungumze kwenye simu?”
“Hatuwezi kuzungumza kwenye simu kila
kitu. Kuna maongezi mengine ni lazima tukutane mimi na wewe”
“Ungejitambulisha kwanza ili niweze kukujua vizuri, wewe ni nani na
unamjuaje babu yangu?”
“Sasa ili unijue vizuri mimi, nitakuelekeza mahali ambapo utapata habari zangu kikamilifu na tutaweza kuonana mimi na wewe”
“Nielekeze ni mahli gani??”
Msichana akanielekeza mtaa mmoja ulioko eneo la Mwananyamala. Pia akanitajia namba ya nyumba.
“Ukifika uliza Sharif Nasri” akaniambia.
“Huyo Sharif Nasri ni nani?”
“Ni baba yangu”
“Umeniambia wewe unaitwa nani?”
“Naitwa Ummy Sharif Nasri”
“Wewe ni sharifu?”
“Hilo ni jina tu”
“Kwa hiyo kama nitampata huyo mzee nimuulize kuhusu wewe?”
“Ndiyo muulize na mimi utanipata hapo hapo”
“Sawa. Nitafanya hivyo”
“Basi nakutakia mchana mwema”
Msichana akakata simu.
Aliniacha na mawazo yaliyochanganyika na fadhaa. Nilijiuliza maswali mengi sana yaliyokosa majibu.
Imani niliyokuwa nayo ni kuwa huyu
msichana ndiye aliyewaua wale watu niliowafuata kule Botswana, Zimbbabwe na Afrika Kusini. Na ndiye pia aliyemuua Baraka Abdul aliyeuawa nyumbani kwake Mbezi.
Kama kweli ndiye aliyewaua, ilikuwa ni lazima niwe na hofu naye na ni lazima nishuku kuwa pengine alitaka kuniua na
mimi ingawa sababu za kufanya mauaji hayo nilikuwa sizijui.
Sasa kwa kunielekeza kwa mtu mwingine ambaye aliniambia ni baba yake, alizidi kunichanganya. Nilijiuliza huyo mtu atanieleza nini kuhusu msichana huyu aliyeonesha kila dalili ya kupata mafunzo ya uuaji.
Nikaendelea kujiuliza, huyo mzee anajua nini kuhusu watu hao waliouawa na mwanawe na anajua sababu za mauaji hayo?
Au mzee huyo anamjua babu yangu au ananijua mimi?
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 12


ILIPOISHIA
Vile vile nilitaka kujua jinsi yule msichana anavyohusika na mali za babu yangu. Amejuaje kama mali za babu yangu zimepotea?
Au ana maelezo gani ambayo anataka kunipa kuhusu mali hizo na ameyapata wapi?
Suala la mali lilinipa shauku lakini suala la mauaji lilinitia hofu. Ilibidi nigwaye na nifikiri vya kutosha kabla ya kuamua kwenda huko Mwananyamala.
Baada ya kuwaza kwa muda mrefu nilitoka pale nyumbani, nikaenda
kwenye mkahawa uliokuwa jirani. Niliagiza chakula nikala huku nikiwaza.
Nilipomaliza kula niliitoka. Siku ile kulikuwa na mechi kati ya Simba na Yanga. Nikaenda uwanja wa taifa. Nilikuwa mpenzi wa mpira wa miguu na shabiki wa moja ya timu hizo.
Niliangalia mpira hadi saa kumi na mbili jioni. Sikupata furaha kwa vile timu zilitoka sare bila kufungana. Nikarudi nyumbani.
Mpaka muda huo nilikuwa nimepuuza kwenda Mwananyamala kumuulizia
Sharif Nasri.
Asubuhi ya siku ya pili yake yule msichana akanipigia simu.
“Mbona hukwenda kule nilikokuelekeza?” akaniuliza.
“Nitakwenda leo”
“Ni muhimu. Tafadhali usipuuze”
SASA ENDELEA
Baada ya kunywa chai niliona niende huko Mwananyamala alikonielekeza huyo msichana ili nikapate taarifa zake. Nilitarajia si tu ningeweza kugundua
msichana huyo alikuwa nani pia ningeweza kujua sababu ya kuwaua wale watu.
Hata hivyo wakati nikienda huko Mwananyamala nilikuwa nikijua fika kwamba yule msichana alikuwa mtu wa hatari.
Lakini kubwa zaidi lililonisukuma niende, ni vile alivyoniambia kuwa alikuwa na
tarifa ya malli za babu yangu ambazo mpaka muda ule zilikuwa ni kitendawili nilichoshindwa kukitegua.
Kadhalika mauaji yale ya watu wanne ambao walikuwa wakidaiwa na babu yangu yalizidi kunipa shauku ya kutaka kumjua vyema msichana huyo ambaye mpaka muda ule nilikuwa nikiamini kwamba ndiye aliyewaua.
Nilipofika Mwananyamala niliutafuta mtaa niioelekezwa hadi nikaupata.
Nikaitafuta nyumba yenye namba aliyonitajia yule msichana. Nilipoiona nilijisikia kuanza kupata hofu nikajiambia kuwa nami leo naenda kufa.
Sikujua ni kwanini nilipata hofu. Lakini nilihisi nilipata hofu kwa sababu nilipagundua mahali ambapo ningepata taarifa za yule msichana ambazo zilikuwa zikiumiza kichwa changu.
Mbele ya ile nyumba nilikuta mzee aliyekuwa amekaa kwenye kiti cha uvivu akivuta mtemba.
Alikuwa mzee mrefu na mwembamba aliyekuwa na ndevu nyingi nyeupe. Alikuwa amevaa shati jeupe na suruali nyeupe. Kichwani alikuwa amevaa kofia ya darize.
Jinsi nilivyomsoma kutokana na mavazi yake na sura yake, alikuwa mswahili wa pwani aliyekuwa amechanganya na ushirazi. Umri wa mzee huyo haukuwa chini ya miaka sabini na mitano ingawa bado alionekana kuwa na nguvu za kutosha.
Nilisimamisha gari karibu na baraza ya nyumba hiyo nikaizima moto na kutoa gea zote na kuvuta hand break na kushuka.
Vile nilivyomuuona mswahili nikamtolea salaam.
“Asalaam alaykum”
“Waalayka salaam” aliniitikia. Ingawa alikuwa mwembamba, sauti yake ilikuwa nzito inayokwaruza.
“Habari za hapa?” niliendelea kumsalimia nikiwa nimesimama mbele yake.
“Nzuri. Karibu” akanikaribisha huku akinitazama kwa macho ya udadisi.
Macho yake yalikuwa madogo yaliyokuwa na kope nyeupe.
“Samahani mzee wangu, kulikuwa na mtu ninamuulizia. Aliniambia ninaweza kumpata hapa”
“Ni nani?”
“Anaitwa Ummy Sharif Nasri”
Mzee nilipomtajia jina hilo alishituka akautoa mtemba wake midomoni kisha akaniuliza tena huku akiwa amenikazia macho.
“Unasema nani?”
“Ummy Sharif Nasri”
Mzee aliendelea kunikazia macho.
“Wewe unatokea wapi?”
“Natokea hapa hapa Dar”
“Unamfahamuje Ummy?”
“Sikuwa nikimfahamu tangu zamani ila
jana nilipigiwa simu na msichana aliyejitambulisha kwa jina hilo akaniambia nikutane naye kwa sababu ana taarifa za mali za marehemu babu yangu”
“Alikwambia anaitwa Ummy Sharifu Nasri?”
“Ndiyo”
“Alikuelekeza uje kwenye nnyumba hii?”
“Ndiyo”
“Uliwahi kumuona yeye mwenyewe?”
“Nilimuona jana”
“Una hakika kwamba ulimuona Ummy?”
“Ndiyo nnilimuonna”
“Nikikuonesha picha yake unaweza kumtambua”
“Ndiyo nitamtambua”
“Hebu subiri”
Mzee alionesha wazi nilimchanganya akili. Aliinuka kwennye kiti akaingia
ndani.
Sikujua ni kwanini alitaharuki. Baada ya muda kidogo alitoka akiwa ameshika kitabu cha picha.
“Hebu sogea hapa karibu” akanniambia huku akifungua karasa za kile kitabu.
“Hebu angalia hii picha. Msichana uliyemuona ndiye huyo?”
Mzee alinionesha picha moja ya ukubwa wa bahasha ya barua. Ilikuwa ikumuonesha yule msichana akitabasamu.
“Ndiye huyu?” Mzee akaniuliza.
“Ndiye yeye”
“Mtazame vizuri”
“Nimemtazama vizuri, ndiye yeye Ummy Sharif Nasri”
“Unaponiambia hivyo unanichanganya…!”
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 13

ILIPOISHIA
Kama vile magoti yalimnyong’onyea, mzee alirudi ghafla kwenye kiti chake.
“Kwanini ninakuchanganya mzee wangu?” nikamuuliza kwa sauti tulivu nikiwa sijui nililokuwa ndani ya moyo wa mzee huyo..
“Mimi ndiye Sharif Nasri. Huyu ni binti
yangu na alishakufa miaka mitano iliyopita!”
Kauli ya yule mzee ikanishitua na mimi.
“Umesema alishakufa miaka mitano iliyopita?” nikamuuliza.
“Ndiyo alishakufa. Hivi sasa ni marehemu. Uliponiambia ni huyu umenichanganya sana”
“Kama alishakufa miaka mitano iliyopita, mbona nimemuona na ameniambia nije kumuulizia hapa?”
Nikaona mama mmoja na binti mmoja aliyekuwa amefanana na Ummy, wakitoka pale barazani. Pengine ni baada ya kusikia yale maneno.
“Kuna nini?” Yule mama akauliza.
SASA ENDELEA
“Huyu kijana amekuja na habari za kushangaza kidogo” Yule mzee alianza kumueleza.
“Kwani yeye ni nani?”
“Sikiliza nikueleze. Yeye amekuja kumuulizia Ummy”
Yule mama akanitazama kisha akaurudisha uso wake kwa yule mzee.
“Yeye hajui kama Ummy hivi sasa ni marehemu? Amekuja kutukumbushia msiba tuliokwishausahau”
“Anasema alikutana naye na alimuagiza aje hapa nyumbani!”
“Alikutana naye lini?” Yule mama aliuliza kwa mshituko.
“Eti mlikutana llini??” Yule mzee akaniuliza.
“Nilikkutana naye jana na leo niliongea naye asubuhi kwa simu” nikamjibu.
Mama akatikisa kichwa.
“Huyo siye Ummy. Ummy alikwishakufa mmika mitano iliyopita” Mama alisema.
“Nimemuonesha hii picha ya marehemu. Ameniambia Ummy aliyekutana naye ndiye huyo”
“Haiwezekani. Huyo aliyekutana naye si Ummy”
Yule msichana aliyetokana yule mama akanitazama.
“Umesema uliongea naye kwenye simu leo?” akaniuliza.
“Ndiyo niliongea naye”
“Ulimpigia au alikupigia?”
“Alinipigia yeye”
“Hebu tuoneshe namba yake”
Nikatoa simu yangu na kuitafuta namba aliyonipigia yule msichana, nikamuonesha.
Msichana aliisoma ile namba kisha akagutuka.
“Mama hii ndiyo iliyokuwa namba ya marehemu dada!” akasema kwa sauti ya
kutaharuki.
“Kwani unaikumbuka vizuri?”Yule mama akamuuliza.
“Naikumbuka” Msichana alisema na kurudia kuitaja ile namba kwa kuikariri
kisha akaongeza.
“Ni namba ya marehemu kweli”
Nyuso za watu wote watatu zikawa zimebadilika. Nilijuta kufika pale nyumbani na kukuta niliyoyakuta.
“Hebu tueleze vizuri unajuana naye vipi huyu Ummy?” Yule mama akaniuliza.
Ikanibidi nieleze ukweli wote tangu babu yangu alipofariki mpaka nikaenda
katiika nchi nilizokwenda kufuatilia madeni ya babu. Nikaeleza jinsi msichana huyo alivyowaua watu niliowafuata katika kila nchi niliyokwenda. Na mtu wa mwisho aalimuua Dar es Salaam mara tu niliporudi kutoka Afrika Kusini.
Niliwaeleza kwamba niliporudi nilimuona
huyo msichana akishuka kwenye ndege akiwa amefuatana na mtu mmoja.
“Niliwafuatilia hadi Mbezi ambako niliona wakiingia katika nyumba moja. Siku ya piili yake nikaona kwenye vyomba vya
habari yule mtu ameuawa na alikuwa ni mmoja wa watu waliokuwa wanadaiwa na
babu yangu”
Mama alitoa mguno mzito akamtazama yule binti kisha akamtazama yule mzee ambaye nilikwisahisi kuwa alikuwa mume wake.
“Huyu kijana amekuja na habari kubwa” akawambia kisha akanitazama na kuniuliza.
“Sasa mlikutana wapi na huyu msichana mkiwa hapa Dar”
“Tulikutana jana. Sijui alipataje namba yangu akanipigia simu…”
“Wewe ulijuaje kuwa ni yeye aliyekupigia simu?”
“Sikujua kama alikuwa yeye. Aliniambia nimfuate katika hoteli moja pale Masaki, akaniambia alikuwa na taarifa kuhusu mali za babu yangu. Nikafika
hapo hoteli. Nikaingia katiika chumba alichoniambia ananisubiri.
“Nilipoingia humo chumbani nikamuona yeye. Kwa vile nilivyojua kuwa ndiye aliyeua wale watu, nilidhani alitaka
kuniua na mimi nikatoka mbio bila kumsikiliza. Niliporudi nyumbani alinipigia simu akaniuliza kwanini nilimkimbia”
Niliendelea kuwaeleza jinsi nilivyojibizanana na msichana huyo hadi akanitajia jina lake na ubinti wake na akanitaka nifike nyumbani kwao Mwananyamala ili nionane naye.
“Namba ya nyumba hii alikutajia
yeye?”
“Ndiyo alinitajia yeye. Jana sikufika. Leo asubuhi akanipigia simu na kunisisitiza kuwa nifike kumuulizia. Ndio nikafika
na kukutana na huyu mzee hapa”
Palipita kimya cha karibu robo dakika. Wenyeji wangu hao walikuwa wameduwaa wakinitazama. Sikuweza kujua walikuwa wananiwazia nini.
Nikahisi kijasho chembamba kikinitiririka kwenye mfereji wa uti wa mgongo wangu.
Nilikuwa nikijiuliza kama ule ulioua watu Botswana, Zimbabwe na Afrika Kusini uulikuwa ni mzuka wa Ummy na kwamba nilikutana na kuzungumza na mzuka?
Maswali hayo yalikuwa yakipita akilini mwangu kimya kimya huku nikikabiliwa na kazi ya kukwepa macho ya wale wazee waliokuwa wakinitazama.
Ni vyema niseme ukweli kwamba wakati ule tunazungumza, miguu yangu ilikuwa inatetemeka kwa hofu.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 14


ILIPOISHIA
“Sasa mwanangu, huyu msichana uliyekuja kutueleza kwamba ulikutana naye na kuzungumza naye alishakufa na mdogo wake amethibitisha kwamba namba ya simu uliyopigiwa ni ya marehemu kweli, je mpaka sasa una wazo gani?” Yule mama akaniuliza lakini swali lake lilikuwa ni gumu kulijibu.
“Sijui nikujibu nini mama yangu. Hiyo taarifa kwamba huyu msichna alikufa
miaka mitano iliyopita imenichanganya akili yangu” nikamjibu.
“Kwani alipokupigia simu alikueleza alikuwa na uhusiano gani na babu yako?” Yule mzee naye akaniuliza.
“Hakuniambia kama alikuwa na
uuhusiano wowote na babu yangu isipokuwa aliniambia alitaka anipe taarifa za mali ya babu yangu”
“Na mimi nina wazo langu” Yule msichana naye akasema na kuongeza.
“Hebu mpigie simu hapa hapa tumsikie”
“Hilo ni wazo zuri” nikasema na kuitazama simu yangu ambayo nilikuwa nayo mkononi.
Nikampigia Ummy Sharif Nasri.
SASA ENDELEA
Simu ilikuwa inaita lakini ilikuwa haipokelewi.
“Simu inaita lakini haipokelewi” nikawambia.
Niliiondoa simu sikioni mwangu na kuielekeza kwa yule msichana.
“Sikiliza simu inaita” nikamwambia.
Msichana aliishika ile simu akaiweka kwenye sikio lake na kusikiliza.
“Ndiyo simu inaita kweli” akasema.
Aliendelea kuiweka sikioni kwake hadi simu ikakata yenyewe. Akaiondoa sikioni
na kunipa.
“Simu inaita lakini hapokei” akasema tena.
“Una maana kwamba Ummy yuko hai?” Mama yake akamuuuliza.
Msichana akabetua mabega.
“Tunachojua sisi ni kuwa amekufa, sasa hii habari kuwa dada yuko hai hatuijui. Kama angekuwa hai si angekuja
nyumbani”
“Ni miujiza hii!” Mzee akasema huku uso wake ukiwa umefadhaika.
“Hebu piga tena” Yule mama akaniambia.
Nikapiga tena ile namba.
Safari hii simu haikupatikana.
“Inaita” Mama akaniuliza.
“Simu haipatikani tena” nikawambia.
“Mara moja hii!” Mama akashangaa.
“Inawezekana ameizima” nikawambia.
“Huyo Ummy ndiyo ameizima?”
“Ndiyo yeye. Mnaponiambia kuwa amekufa niinashangaa kwa sababu nimemuona na nimezungumza naye”
“Huyu huyu ambaye umemuona kwenye picha?”
“Ndiye huyo huyo”
“Sasa ili uamini kuwa amekufa twende nikakuoneshe kaburi lake. Makaburi hayako mbali” Mzee akaniambia.
Mzee huyo alinichukua hadi katika eneo la makaburi ambalo halikuwa mbali sana. Akanionesha kaburi la Ummy Nasri. Lilikuwa na kibao kilichoandikwa jina lake, tarehe aliyokufa na aliyozikwa.
“Kaburi lake ni hili hapa”
Sikuwa hata na la kusema. Nilibaki kushangaa tu.
Mzee aliendelea kuniambia.
“Marehemu amelala ndani”
“Sasa mzee huyu atakuwa nani?” nikamuuliza.
“Sisi hatumjui. Sisi tunachojua ni kuwa binti yetu alishakufa na aliyekufa hafufuki”
“Lakini mzee fikiria kwamba alinielekeza yeye mwenyewe kuwa nije pale nyumbani nimuulizie”
“Mtu yeyote hawezi kukubaliana na maelezo yako” Mzee akaniambia huku akiondoka.
“Nimekuja kukuonesha hili kaburi ili uthibitishe kuwa Ummy alikwishakufa” akaongeza.
“Na mimi nathibitisha kuwa nilimuona”
“Basi itakuwa ni miujiza mikubwa”
Tukarudi pale nyumbani.
“Ni vizuri kama utakutana naye tena uje naye hapa mguu kwa mguu” Mzee akaniambia wakati akiketi kwenye kiti chake cha uvivu.
Wakati narudi na gari langu nilianza kuzikumbuka zile safari za kimiujiza za yule msichana amabaye kwanza nilimkuta Botswana. Halafu nikaenda kumuona Zimbabwe. Nilipokwenda Afrika Kusini nikakutana naye tena. Bado wakati narudi Tanzania nikashuka naye kwenye ndege moja ingawa wakati wa kupanda ndege sikumuona.
Na huko kote alikuwa akiwaua watu niliokuwa nimewafuata. Mtu wa mwisho alikuwa mkazi wa hapa hapa Dar ambaye alishuka naye kwenye ndege.
Watu wote aliowaua walikuwa wakidaiwa na marehemu babu yangu na mauaji yalifanyika wakati ule nafanya ziara yakufuatilia madeni.
Mwisho wa siku msichana huyo alinipigia simu na kuniambia kuwa ana mazungumzo na mimi kuhusu mali za babu yangu.
Aliniona Botswana. Aliniona Zimbabwe. Aliniona Afrika Kusini lakini hakuniambia kuwa ana mazungumzo na mimi.
Katika nyumba aliyonielekeza niende nimeambiwa kwamba msichana huyo wanamfahamu lakini alikwisha kufa miaka mitano iliyopita.
Sasa napata picha kwamba msichana huyu hakuwa wa kawaida. Zile safari alizozifanya kule Botswana, Zimbabwe na Afrika Kusini pia hazikuwa za kawaida. Niliona kama alikuwa akiibuka tu katika zile nchi nilizomkuta. Hakuwa akisafiri. Hakukuwa na hadi leo hakuna usafiri wa haraka kiasi kile.
Pia yale mauaji aliyokuwa akiyafanya hayakuwa ya kawaida. Kwa mwanamke kuwaua wanaume kirahisi rahisi namna ile haikuwa kawaida.
Baada ya kuwaza hayo nikajiuliza, yule msichana alikuwa shetani au mzuka wa Ummy niliyeelezwa kuwa alikwishakufa?
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 15

ILIPOISHIA
Nikajiambia kama hatakuwa shetani atakuwa ni mzuka. Lakini sikuelewa ni kwanini mzuka huo uliwaua wale watu na kwanini uliniambia kuwa unajua siri za mali za babu yangu.
Kwa vile suala la msichana huyo lilikuwa limenipa dukuduku, nilipofika nyumbani nikapata wazo moja. Wazo hilo lilikuwa ni kufanya utafiti ili kumjua huyo Ummy niliyemabiwa kuwa alikufa, alikuwa msichana wa aina gani. Alikuwa
akifanya kazi gani na pia nijue kama alikuwa na uhusiano na marehemu babu yangu.
Sikutaka tena kumpigia simu Ummy kwa sababu huenda angeipokea na kunieleza maneno ya kunitisha.
Ili kuanza upelelezi wangu niliona niende katika mtaa ule ule aliokuwa anaishi Ummy nitafute mtu aliyekuwa anamfahamu nifanye naye urafiki na kisha nianze kumhoji kuhusu maisha ya Ummy mpaka kufa kwake.
Ule mtaa nilikuwa mgeni nao, nilijua isingekuwa kitu rahisi kumpata rafiki wa kunipa habari za Ummy lakini
nilijiambia ni lazima nijitahidi kwa kadiri ya uwezo wangu nimpate mtu ambaye ataweza kunifumbulia kitendawili cha Ummy Nasir.
SASA ENDELEA
Siku ile yule msichana hakunipigia simu na mimi sikumpigia. Mimi sikumpigia kwa hofu niliyoipata baada ya kuelezwa kuwa msichana huyo alishakufa. Na kama alishakufa na nimekuja kukutana naye, basi atakuwa ni mzuka.
Asubuhi ya siku ya pili yake nikaenda katika ule mtaa niliyokwenda jana yake kumuulizia Ummy. Safari hii sikwenda na gari langu. Nilipanda daladala.
Sikutaka kufika tena pale nyumbani kwa mzee Nasir. Nilizuga zuga katika nyumba zilizokaribiana na nyumba yake nikitafuta mtu ambaye ningeweza kufanya naye urafiki na kumuuuliza kuhusu marehemu Ummy.
Katika kutupatupa macho nikaona
sehemu iliyokuwa na meza ya kahawa na kashata. Kulikuwa na mabenchi matatu ya kukalia. Muuza kahawa aliyekuwa amevaa kofia kubwa lililosukwa kwa minyaa kama la mvuvi wa samaki, alikuwa amekaa upande wa pili wa meza yake akiwa na ndoo mbili, jiko na birika la kahawa lililokuwa likifuka moshi jikoni.
Muda ule kulikuwa na mtu mmoja tu aliyekuwa amekaa akinywa kahawa. Nikaona niende nikakae mahali hapo ili nifikirie la kufanya.
Mara tu nilipoketi akaja mtu mwingine. Tukawa watu watatu.
Muuza kahawa akatutilia kahawa bila hata kutuuliza. Ukishakaa kwenye benchi lake maana yake ni kuwa unataka kahawa.
Nilichomsikia akiuliza ni. “Nikutilie tangawizi?”
Alikuwa akimtazama yule mwenzangu aliyekuja baada ya mimi.
“Ndiyo tia” Mtu huyo akamjibu.
“Na wewe?” akaniiuliza mimi.
Wakati ananitazama, sura yake ikanijia akilini mwangu. Zilinichukua kama nukta tatu hivi kumkumbuka Selemeni Mzaramu.
Wakati namkumbuka, yeye alishanikumbuka zamani.
“Ah! Kasim Fumbwe… kumbe ni wewe?” akaniuliza kwa mshangao.
“Mzaramu! Bado upo Dar hii!” nikamuuliza.
“Twende wapi ndugu yangu. Tunabangaiza humu humu. Makamba alituambia tutabanana hapa hapa”
Tukacheka.
“Nikuwekee tangawizi?’ akaniiuliza tena.
“Ndiyo niwekee”
Selemani Mzaramu alikuwa rafiki yangu wa miaka mingi. Nilisoma naye shule ya msingi hadi darasa la saba. Wakati mimi
naendelea na masomo ya sekondari, mwenzangu hakuchaguliwa. Na baada ya hapo sikuwahi kukutana naye tena hadi siku ile nilipomuona amevaa kofia la minyaa akiuza kahawa.
Mzaramu alinisogezea kikombe cha
kahawa akaniuliza.
“Uko wapi Kasim?”
“Mimi niko hapa hapa Dar. Nilikuwa Morogoro , maisha yakanishinda, nikarudi hapa Dar”
“Unafanya kazi wapi, nije unipe kibarua?”
“Bado nipo nipo tu, sifanyi kazi popote. Nilikuwa na duka Morogoro, duka likafa, nikarudi Dar baada ya babu yangu kufariki. Na ndiyo nimeamua niendelee kuwa hapa”
“Mimi baada ya masomo nilihangaika na malori mpaka yamenitia kilema. Sasa
nipo hapa?”
“Alah! Umepata ulemavu?”
“Mguu wangu ulivunjika mara tatu. Mfupa ulisagika vibaya. Nimeokolewa na vyuma…”
Mzaramu alinionesha mguu wake wa kushoto baada ya kuisega suruali yake. Mguu huo ulikuwa hautazamiki kwa mishono!
“Nje unaouna ni mguu lakini ndani ni vyuma vitupu, yaani ulikuwa ukatwe lakini kaka yangu alijitahidi sana kunipeleka hospitali za pesa ambako niliwekewa vyuma. Nikasema sasa malori basi”
“Loh! Pole sana rafiki yangu. Ulikuwa dereva?”
“Nilikuwa taniboi. Basi nilikaa hospitali karibu mwaka mzima”
Nikatikisa kichwa changu kumsikitikia.
“Pole sana rafiki yangu lakini kama unapata riziki yako na maisha yanakwenda, shukuru Mungu”
“Nashukuru. Nimeoa na nina watoto
wawili lakini mke wangu alinikimbia aliposikia nitakatwa mguu. Kaniachia watoto lakini nimewalea mwenyewe na hivi sasa wanasoma”
“Kumbe ulipata mkasa mkubwa rafiki yangu….”
“Kula kashata” Mzaramu akaniambia.
Nikaokota kashata moja na kuing’ata.
“Unazitengeza mwenywe?” nikamuuliza.
“Nazitengeza mwenyewe usiku. Asubuhi nakuja nazo”
“Kwani unaishi wapi??’
“Naishi hapa hapa Mwananyamala”
“Mtaa huu?”
“Ndiyo naishi mtaa huu huu lakini ni kule mwisho”
“Umeishi mtaa huu kwa miaka mingapi?’
“Nina miaka kumi na mitano sasa”
Nikajiambia kimoyomoyo kuwa atakuwa anamjua Ummy ambaye alikufa miaka mitano tu iliyopita.
“Katika mtaa huu alikuwa akiishi msichana mmoja aliyekuwa akiitwa Ummy Nasri…”
“Nyumba yao ile paleee lakini huyo msichana alikwisha kufa zamani ila namfahamu sana”
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 16

ILIPOISHIA
“Maana yake mtu amekufa halafu anakuja kuonekana tena”
“Sasa yule si mtu yule yule”
“Ni nani sasa?”
“Kwanza mtu akifa hawezi kuonekana tena”
“Mbona mimi nimemuona Ummy?”
“Uliyemuona si Ummy”
“Ni yeye. Licha ya kunielekeza kwao alinipa namba ya simu yake na nilimuonesha ndugu yake pale nyumbani kwao akasema ni namba ya Ummy kweli”
“Kwani ulifika kwao kumuulizia?’
“Ndiyo, nilifika jana”
“Wakakuambia nini?”
“Wakaniambia hivyo hivyo kwamba Ummy alikufa”
“Si ndiyo nilivyokueleza mimi?”
SASA ENDELEA
Nilihisi kwamba maelezo ya Mzaramu badala ya kunisaidia yalizidi kunichanganya. Mzaramu hakutaka
kukubaliana na miimi kwamba niliyemuona alikuwa ni Ummy wakati nilikuwa na imani kuwa niliyekutana naye alikuwa ni Ummy Nasri.
Kitu muhimu kilichonifanya niamini kuwa niliyemuona ni Ummy Nasri aliyedaiwa kufa ni ile picha ya Ummy niliyooneshwa na baba yake huku mdogo wake akikiri kwamba namba ya simu niliyopigiwa na Ummy ilikuwa namba ya Ummy kweli. Mdogo wake huyo alikuwa ameikariri.
Sasa kulikuwa na vitu viwili vilivyonitia mawazo. Kwanza ni yale maelezo ya Mzaramu kwamba Ummy kabla ya kufa alikuwa na uhusiano na mzee mmoja
ambaye Mzaramu alinithibitishia kuwa ndiye yule niliyemuonesha katika picha iliyokuwa kwenye simu yangu.
Picha hiyo ilikuwa ni ya babu yangu marehemu mzee Limbunga. Hivyo maelezo ya Mzaramu yalionesha kwamba babu yangu alikuwa na uhusiano na Ummy.
Kitu cha pili kilichoniitia mawazo ni maelezo ya Ummy kwamba anazijua siri za malli ya babu yangu. Inawezekana kweli anaijua siri ya mali ya babu yangu kwa vile alikuwa na uhusiano naye. Ila kinachotatanisha hapo ni kuwa Ummy mwenyewe anadaiwa kuwa alishakufa.
Yakanijia mawazo yale yale kwamba niliouona ulikuwa mzuka wa Ummy, yaani iliwezekana kuwa Ummy alishakufa kweli lakini nilichokutana nacho kilikuwa kivuli chake. Nilishasikia hadithi nyingi za watu waliokufa kuonekana tena ikidaiwa kuwa ni mizuka ya watu hao.
Lakini mara nyingi mizuka hiyo
inapotokea inakuwa na sababu.
Sasa nikajiambia labda nijaribu kutafuuta sababu ya kutokea kwa mzuka wa Ummy ambaye aliwaua watu wote waliokuwa wakidaiwa na babu yangu na kusababisha nisilipwe pesa ambazo ningelipwa na watu hao.
Nikajiuliza kama Ummy alikuwa mzuka ni kwanini aliwaua watu hao halafu aniambie kuwa anaijua siri ya mali ya babu yangu na kutaka nikutane naye?
Kwa kweli kila nilivyowaza niliona sivyo na kila nilivyojiuliza sikupata jibu. Hapo ndipo nilipozidi kuchanganyikiwa.
“Mbona umeduwaa rafiki yangu?”
Mzaramu akaniuliza akiwa hajui yaliyokuwa yanapita akilini mwangu.
Nikazinduka kutoka katika mawazo yangu na kumwambia.
“Nilikuwa nafikiria hadithi uliyonieleza”
“Kahawa imekutosha?” akaniuliza.
“Imetosha. Ni kiasi gani?”
“Sijakuuzia, nimekupa kiurafiki kwa vile siku nyingi hatujaonana”
“Asante, nakushukuru sana. Naona nikuage, tutaonana siku nyingine”
Nilipoondoka kwa Mzaramu nilikusudia nipite pale nyumbani kwa kina Ummy na kama nitakutana na yule mzee nisalimiane naye.
Wakati nipo barabarani nikitembea kwa miguu kuelekea upande ule ilikokuwa nyumba ya mzee Nasri, nikakutana na mdogo wake Ummy akitokea dukani.
Msichana huyo aliponiona akasimama.
“Kaka wewe ndiye uliyekuja nyumbani jana ukatuambia kuwa ulimuona dada?” akaniuliza.
“Ndiye mimi”
“Jana ulitutia wasiwasi sana. Ilibidi mama aende kwa mganga kumueleza kuhusu kuonekana kwa Ummy ambaye alishakufa. Mganga akamwambia kwamba huyo aliyeonekana alikuwa Ummy kweli, amechukuliwa msukule”
“Amechukuliwa msukule na nani?” nikamuuliza.
“Huyo mganga alimwambia amechukuliwa msukule na mwanamke mmoja ambaye aliwahi kugombana naye”
“Waligombania nini?”
“Huyo mwanamke alikuwa akidai kuwa marehemu alikuwa anatembea na mume wake”
Nikayakumbuka yale maelezo ya Mzaramu. Nikafikiri kidogo kisha nikamuuliza.
“Kama alichukuliwa msukule mbona yuko vizuri tu, anaongea kwenye simu na nilikutana naye Botswana, Zimbabwe na Afrika Kusini. Mtu aliyechukuliwa msukule anapanda ndege?”
“Hayo ni maelezo ya huyo mganga lakini baba alipoelezwa amesema hataki mambo ya kishirikina, anachojua yeye ni kuwa mwanawe amekufa, huyo aliyeonekana siye mwanawe”
“Mimi pia hayo madai ya kuchukuliwa msukule sikubaliani nayo. Waganga wengine wanakisia tu”
“lakini wewe una hakika kuwa ulimuona dada?”
“Nilimuona na ni yeye aliyenielekeza nije kwenu. Mimi nilikuwa sijui kwamba amekufa”
“Na tangu jana hajakupigia simu?”
“Hajanipigia bado”
“Na wewe hujampigia?”
“Sijampigia”
“Ungempigia umuulize vizuri”
“Kusema kweli nimetishika baada ya kusikia kuwa alishakufa”
“Hebu jaribu kumpigia sasa hivi?”
Nikatoa simu na kuitafuta namba ya Ummy, nilipoipata nikampigia.
Simu ikaita. Nikajua itapokelewa ili nimpe mdogo wake azungumze naye lakini simu haikupokelewa. Ilipokata nikapiga tena.
“Hapokei simu?” nikamwambia yule msichana.
“Labda alikudanganya tu?”
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 17

ILIPOISHIA
“Hakunidanganya. Baba yako alinionesha picha yake, ndiye yeye
niliyemuona na hata namba ya simu anayotumia ulisema ni yake”
“Namba ya simu ni yake kweli, niliikariri
kichwani mwangu”
“Basi ndiyo ujue niliyemuona alikuwa ni Ummy kweli”
“Sasa mbona hapokei simu?”
“Tena mwanzo alikuwa akinipigia yeye, ndiyo nikaipata hii namba yake”
“Basi atakapokupigia tena utakuja kutuambia”
Nikaagana na yule msichana. Sikwenda kwao tena. Nikaenda kupanda daladala na kurudi nyumbani.
Vile nafika nyumbani tu, simu yangu ikapigwa. Nilipoangalia namba inayonipigia, nikaona namba ya Ummy.
Nilishituka halafu mwili ulinisisimka.
SASA ENDELEA
Nikajiuliza niipokee au nisiipokee? Kama nitaipokea msichana huyo atanieleza nini? Nikajiambia chochote ambacho ataniambia kitazidi kuniweka njia panda kwa vile nimeshathibitisha kuwa msichana huyo alikuwa ameshakufa.
Vile vile tayari nilikuwa na hofu ya kuzungumza na mtu ambaye kuna ushahidi kuwa alikuwa amekufa.
Lakini kwa upande mwingine nilikuwa na shauku ya kumsikia yeye mwenyewe atakachojibu kuhusu madai kuwa alikuwa ameshakufa miaka mitano iliyopita.
Nikajiambia nisipopokea simu yake, bado nitabaki kuwa njia panda kwani sitapata mtu mwingine wa kunipa ufafanuzi kuhusu madai ya kufa kwake.
Mbali na hayo, bado nilitaka kujua ni siri gani ambayo alitaka kunieleza kuhusu mali za babu yangu. Nikaamua kupokea ile simu.
“Hello!” Nikasema kwa sauti ya kujikaza ili nisioneshe hofu niliyokuwa nayo.
“Hello! Kassim unajua nimekupenda sana, ninataka uwe mume wangu!”
Maneno hayo yalinishitua. Niwe mume wa mtu aliyekwisha kufa!
“Natumaini kuwa naongea na Ummy?” nikamuuliza.
“Mimi ni Ummy Nasri”
“Uliniambia nifike nyumbani kwenu Mwananyamala, nimefika jana na leo lakini sikukuona”
“Ulimkuta nani?”
“Nilimkuta baba yako mzee Nasri”
“Vizuri sana. Alikuambia nini?”
“Aliniambia maneno ya kunishitusha sana”
“Kama yapi”
“Aliniambia kwamba mwanawe anayeitwa Ummy alikwishakufa miaka mitano iliyopita”
“Na mimi ni nani?”
“Umeniambia kuwa wewe ni Ummy Nasri”
“Na uliyembiwa amekufa ni nani?”
“Ni Ummy Nasri”
“Sasa una shaka gani?”
“Kwanza nataka unieleze ni kwanini nimeambiwa kuwa umekufa?”
“Kuna umuhimu wa mimi na wewe kukutana”
“Kwanza nataka ujibu, kwanini nimeambiwa kuwa umekufa?”
“Ndiyo maana nikakwambia kuna umhimu tukutane ili tuzugumzie hilo pamoja na kukueleza kuhusu mali za babu yako”
Nikanyamaza kwa sekunde kadhaa nikifukiria la kumjibu.
“Lakini ni kweli kuwa ulikufa?” nikamuuliza baada ya kimya kifupi.
“Ni kweli?”
“Sasa wewe ni nani?”
“Ni Ummy”
“Umekubali kuwa ulishakufa, sasa mbona uko hai?”
“Mimi ni kivuli cha Ummy”
“Sijakuelewa. Kivuli maana yake nini?”
“Maana yake ni mzuka wa Ummy!”
Moyo wangu ulipiga kwa nguvu kisha ukaanza kunienda mbio. Nikahisi mkono ulioshika simu ulikuwa ukitetemeka.
“Kassim tutakapokutana kila kitu utakielewa vizuri”
“Unadhani nitakutanaje na mzuka?”
“Tutakutana tu na tutazungumza, usijali”
“Mmmh…!”
Pakapita kimya kingine.
“Niambie nikiuone wapi na muda gani?” Sauti ya Ummy ikautanzua ukimya uliokuwepo.
“Acha nifikirie kwanza”
“Ufikirie nini Kassim?”
“Umenitisha. Umeniambia kwamba wewe ni mzuka”
“Sasa unataka ufikirie nini?”
Sikujibu.
“Kassim!” Sauti ya Ummy ikaita kwenye simu.
Sikujibu. Nilibaki nimeduwaa kama gogo.
“Nitakupa muda wa kufikiria lakini usizidi saa arobaini na nane”
“Sawa” nikamuitikia.
Ummy akakata simu.
Yale maneno ya kwanza ya Ummy kuwa ananipenda na anataka niwe mume wake, yalipita katika akili yangu.
Nikajiambia hata wale watu aliowaua kule Buswana. Zimbabwe , Afrika Kusini na hapa Dar, inaelekea walianzana kwenye mapenzi,
Kitendo cha kuniambia anataka niwe mume wake si tu kimebadili mada yake ya kwanza ya kutaka tukutane ili anieleze ziliko mali za babu yangu bali pia nilifikiri kwamba ilikuwa ni hatua ya kutaka kuniua.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 18

ENDELEA....
Niliendelea kujiambia kama msichana huyo amekiri kuwa ni mzuka, atakuwa ni muuaji tu. Pengine alikuwa na kisasi na
babu yangu ambaye niliambiwa alikuwa mwanamke wake.
Nitakutanaje na kuzungumza na mzuka? Nilijiuliza huku nikifikiria niende Mwananyamala nikamjulishe mzee Nasri kuhusu yale maelezo ya Ummy.
Hata hivyo upande mmoja wa akili yangu ulinikataza kwenda Mwananyamala kwa vile nilijua yule mzee atapuuza maelezo yangu kwa ile imani yake kuwa Ummy alishakufa na aliyekufa hawezi kurudi tena duniani.
Sasa nifanye nini, huyu msichana ataendelea kuniandama?” nikajiuliza
Sikuweza kupata jibu la haraka kwa vile akili yangu ilikuwa imetaharuki. Nilijiambia nitakapotulia na kurudi katika hali ya kawaida, huenda nitajua nitafanya nini.
Wakati nazungumza na Ummy nilikuwa nimesimama kwa kutaharuki, nikakaa kwenye kochi na kuendelea kuwaza.
Hisia zangu tangu nianze kumfahamu Ummy sasa zilikuwa zimebadilika. Mwanzo nilikuwa nikihisi kuwa Ummy alikuwa binaadamu anayetumia miujiza kuua watu. Nilijua hivyo tangu nilipoanza kumuona kule Botswana.
Na hata pale nilipomkimbia katika chumba cha hoteli aliponiita, nilimkimbia kwa hofu kuwa alitaka kuniua kama alivyowaua wale wadeni wa marehemu babu.
Lakini sasa mtazamo haukuwa huo. Hisia zangu zilikuwa upande mwingine kwamba Ummy hakuwa muuaji mwenye miujiza kama nilivyokuwa nikidhani bali alikuwa mzuka wa mtu aliyekwisha kufa
miaka mitano iliyopita.
Kama Ummy aliyekufa alikuwa binadamu, huyu Ummy wa sasa si binaadamu tena. Huu ni mzuka kama alivyoniambia wenyewe. Hauna akili ya kibinaadamu. Mara nyingi mzuka
unapotokea unakuja kuua watu halafu unapotea.
Niliwaza kwamba mimi pia nilikuwa katika orodha ya kuuawa na mzuka huo kwani wale waliouawa kwanza walikuwa wako pamoja na mzuka huo kiurafiki wakidhani alikuwa binaadamu mwenzao. Na wote waliuawa katika mazingira ya kimapenzi.
Sasa kama mzuka huo wa Ummy umeanza kuniambia kuwa umenipenda, ndio unataka kunitia kamba ili uniue kirahisi.
Lakini wakati nawaza hivyo suala la mali za babu lilikuwa likitikisa kichwa changu. Kwanini mzuka huo aliniambia unazijua siri za mali ya babu yangu?.
Ilikuwa ni muhimu nikutane naye lakini niliogopa. Huenda hapo tutakapokutana ndio nikauawa hapo hapo.
Nikajiuliza niende nikaripoti polisi ili Ummy akamatwe na kuhojiwa? Au, niliendelea kujiuliza, niende kwa mganga ili anieleze ukweli kuhusu kiumbe huyu na nia yake kwangu?
Wazo la kwenda polisi sikuafikiana nalo. Nilijiambia polisi hawashughulikii masuala ya mizuka. Ningeweza kudai kuwa huyu msichana anadaiwa kuwa alikufa miaka mitano iliyopita lakini ninamuona na ananipigia simu kutaka nikutane naye.
Madai hayo yanaweza kuwavutia polisi wamuandalie mtego na kumkamata. Lakini nikajiuliza kama Ummy ni mzuka kweli, anaweza kukamatika au ninajidanganya?
Wazo zuri, niliendelea kujiambia, ni la kwenda kwa mganga. Mganga anaweza kunitegulia kitendawili hiki.
Baadaya kuwaza hivyo nikaamua niende kwa mganga mmoja wakati ule alikuwa akikaa Chanika. Alikuwa mzigua wa Handeni. Alikuwa akifahamiana na babu na kuna siku niliwahi kwenda kwake nikiwa na babu. Babu yangu licha ya utajiri aliokuwa nae alikuwa mshirikina sana.
Siku ambayo nilikwenda naye kwa mganga huyo alikwenda kumroga mfanyabiashara mwenzake ambaye naye alikuwa na vituo vya mafuta. Walikuwa wakishindana kibiashara na babu akaamua kuingiza na uchawi.
Siku hiyo nakumbuka, mganga alizika mbuzi watatu wakiwa hai kwenye kaburi la mwanamke aliyekufa zamani. Juu ya kaburi pakamwagwa mchanga wa alama za viatu za mfanyabiashara aliyekuwa akishindana na babu yangu.
Babu alikuwa ametuma watu kuzitafuta alama za viatu za mfanyabiashara huyo kwa dau la shilingi milioni tatu kwa mtu atakayefanikisha kuzipata. Watu hao wakawa wanamuandama mfanyabiashara huyo usiku na mchana mpaka wakafanikiwa kupata alama zake.
Alama hizo walizipata aliposhuka kwenye gari na kukanyaga mchanga kabla ya kwenda kulikagua eneo ambalo alitaka kulinunua pale Ubungo.
Baada ya mchanga huo kumwagwa juu ya kaburi hilo palikutwa kibao kilichokuwa na jina lake. Baada ya siku saba mfanyabiashara huyo aliaga dunia baada ya gari lake kugongwa na lori la mafuta! Babu akafurahi.
Mganga huyo alikuwa mzigua aliyetoka Handeni. Wenyeji wa Chanika walimpa jina la “mashine ya kuua”
Tangu kipindi hicho miaka mingi ilikuwa imepita na sikuwahi kwenda kwake tena kwa vile sikuwa na tabia za kwenda kwa waganga wa kienyeji. Hiyo tabia alikuwa nayo babu yangu.
Nikaona niende nikamueleze matatizo yangu nikiamiini kuwa anaweza kunipatia ufumbuzi.
Nikaenda kwa gari langu
Nilipofika niliikuta ile nyumba yake ambayo wakati ule ilikuwa ikiendelea kujengwa, ilikuwa imeshakamilika. Lakini nilikuta msururu wa watu.
Ikabidi na mimi nipange msitari. Hadi nafanikiwa kuingia katika chumba chake cha uganga ilikuwa karibu saa kumi na moja jioni. Nilikuwa na matumaini madogo sana kama angelishughulikia suala langu kwa vile muda ulikuwa umekwenda sana.
Mganga mwenyewe alikuwa amenisahau, nikamkumbusha. Mara moja akamkumbuka babu yangu lakini mimi hakunikumbuka.
“Wewe ni mjukuu wa yule mzee?” akaniuliza.
“Ni mimi lakini babu mwenyewe alishakufa”
Mganga akashituka.
“Kumbe mzee Limbunga alikufa?”
“Alikufa”
“Alikufa mwaka gani?”
“Alikufa mwaka huu”
“Kwa hiyo wewe ndiye umesimamia shughuli zake?”
“Ni mimi lakini kuna matatizo yamejitokeza”
“Matatizo gani?”
“Wewe unajua kuwa mzee Limbunga alikuwa tajiri lakini alipokufa mali zake hazikuonekana”
“Kwanini?”
“Sijui”
ITAENDELEA
 

Similar Discussions

8 Reactions
Reply
Back
Top Bottom