Siri kali za serikali

albuluushiy

JF-Expert Member
Oct 2, 2013
1,405
685
ASUBUHI moja, Aprili 1947, mwanamke mmoja alipenya na kuingia makao makuu ya Ofisi ya Makoloni jijini London. Baridi ilikuwa imeshtadi kwelikweli asubuhi hiyo.

Bibi huyo,kwa upole na kwa sauti nyororo, alimuomba mlinzi amruhusu aingie ndani ajibanze kuikimbia baridi. Mlinzi alimkubalia bila ya mushkili wowote.Ofisi ya Makoloni ilikuwa wizara iliyoyashughulikia makoloni yote ya Uingereza.

Baada ya kuingia ndani, mwanamke huyo akateremka ngazi na kufululiza chooni. Humo akaacha bomu lililovingirishiwa magazeti.Lilikuwa na baruti 24. Polepole akapanda ngazi kurudi juu na akatoka nje akichanganyika na umati wa watu barabarani. Aliyayuka katika zahma za asubuhi, akatoweka, asionekane.

Bomu hilo liligunduliwa baadaye. Kwa bahati halikulipuka kwa sababu mtambo uliotegeshwa ulilipue uliharibika. Lingelipuka lingesababisha mauaji ya halaiki ya watu na vurumai isiyosemeka katikati ya eneo la Whitehall.

Hapo ndipo penye takribani wizara zote za Uingereza pamoja na nyumba ya Namba 10 Downing Street ambayo ni ofisi na makazi ya Waziri Mkuu.

Magaidi waliohusika na jaribio hilo hawakukata tamaa. Mwaka huohuo waliwapelekea wanasiasa wa Uingereza bahasha za barua zilizokuwa na baruti kali.

Ilipotokea kadhia hiyo ya bomu kuwekwa chooni, Ofisi ya Makoloni,Polisi wa Uingereza walikuwa hawamjui mwanamke aliyelitega bomu hilo ni nani. Idara ya ujasusi ya MI5 nayo pia haikumjuwa.Kumbe alikuwa ni gaidi wa shina la Uingereza la Gengi la Stern.Hilo lilikuwa ni gengi la magaidi, moja ya makundi mawili ya kigaidi yaliyokuwa yakipigana na watawala wa Kiingereza nchini Palestina. Jingine likiitwa "Irgun."

Baruti zilizotumiwa kutengenezea bomu alipewa huyo mwanamke na gaidi mwingine wa Gengi la Stern. Huyo alikuwa ni Yahudi wa Kifaransa aliyejeruhiwa vitani. Mguu wake mmoja ulikuwa wa bandia. Aliweza kuziingiza Uingereza hizo baruti kwa kuzificha ndani ya huo mguu wa bandia. Alibandikwa lakabuya ‘Bwana Baruti.'

Lengo la magaidi wa Stern waliokuwa Uingereza lilikuwa ni kufanya mashambulizi nchini humo ili kuilazimisha serikali ya Uingereza iunde taifa huru la Kiyahudi nchini Palestina.

Huyo mwanamke wa Gengi la Stern aliyeacha bomu chooni katika Ofisi ya Makoloni hatimaye alikamatwa Ubelgiji. Alifichuliwa baada ya idara kuu za kijasusi na upelelezi za Uingereza kufanya upelelezi mkali na msako mkubwa katika bara la Ulaya. Idara hizo ni za MI5, MI6 na kitengo cha "askari kanzu" wa idara ya polisi ya London.

Kadhalika, Idara ya Ujasusi ya MI5 iliweza kuwatambua magaidi wa kundi la Irgun waliokuwa Uingereza. Wote waliojulikana wakawa wanapelelezwa na kuchunguzwakwa makini. Hata hivyo kiongozi wao, "kubwa lao," hakupatikana. Aliendelea kuandaa na kupanga mashambulizi ya kigaidi dhidi ya Waingereza, Palestina kwenyewe na hata katika nchi za Ulaya.

Kiongozi huyo wa Irgun akiitwa Menachem Begin. Alizaliwa 1913 upande wa Poland ambao wakati huo ulikuwa sehemu ya Urusi chini ya utawala wa kifalme.

Ajabu ya mambo ni kwamba gaidi huyo wa Kizayuni aliyeutia mguu wake kwa mara ya kwanza Palestina akiwa na umri wa miaka 29 baadaye alikuwa Waziri Mkuu wa sita wa Israel.

Na ajabu ya maajabu ni kwamba gaidi huyu alitunukiwa Tuzo ya Amani ya Nobel yeye pamoja na Rais wa zamani wa Misri Anwar Sadat eti kwa sababu wao walikuwa viongozi wa Israel na Misri nchi hizo zilipoandikiana Mkataba wa Amani.

Ajabu ni kwamba hadi leo hakuna amani Misri wala hakuna amani Israel. Na wala hakuna amani Mashariki ya Kati nzima.

Ajabu nyingine ni kwamba Tuzo ya Amani alitunukiwa mtu kama yeye, gaidi aliyesababisha mauaji ya idadi kubwa ya watu tangu alipokuwa akipigania kuanzishwa kwa dola ya Israel hadi alipokuwa kiongozi wa dola hiyo ya Kizayuni. Na hii ni dola ambayo inazidi kuonekana kuwa ni dola ya kibaguzi mithili ya Afrika ya Kusini ilipokuwa ikitawaliwa na makaburu.

Hayo ni kati ya maajabu ya historia. Au labda itakuwa sahihi zaidi tukisema kwamba hayo ni kati ya maajabu ya unafiki uliozagaa katika historia.

Ni hivi karibuni tu ambapo Serikali ya Uingereza iliidhinisha kwamba watu waruhusiwe kuzisoma nyaraka za siri za idara zake za kijasusi za toka mwaka 1945.

Kwenye nyaraka hizo ndipo utapoweza kuziona habari hizo za jinsi idara za kijasusi za Uingereza zilivyokuwa zikipambana na magaidi kutoka Mashariki ya Kati katika miaka ya 1940 na 1950.

Nyaraka hizo pia zinathibitisha kwamba katika zama za ‘Vita Baridi' kati ya nchi za Kikomunisti na za Magharibi, kitisho kikubwa kwa usalama wa Uingereza hakikuwa Muungano wa Sovieti na Urussi yake bali kilikuwa magaidi wa Mashariki ya Kati.

Siku hizo magaidi hao hawakuwa Wapalestina wala hawakuwa wa Kiislamu. Walikuwa magaidi wa Kiyahudi au wa Kizayoni. Kwa hivyo, ugaidi kutoka Mashariki ya Kati si jambo geni katika historia ya ugaidi.

Siku hizi vita dhidi ya ugaidi wa kimataifa hutumiwa kuhalalisha maovu mengi yanayotendwa na serikali za madola makubwa na za makwetu. Mapambano hayo yanazipa serikali zetu visingizio vya "kuwashughulikia" wapinzani wao wa kisiasa. Kila sababu hutafutwa ya kuwafungamanisha wapinzani na ugaidi au na shutuma za ugaidi.

Mara nyingi tunaona kuwa watuhumiwa wa ugaidi wanapotiwa nguvuni serikali huwa hazizijali haki zao za kimsingi. Haki za binadamu hupuuzwa kwa vile watuhumiwa huonekana kama si binadamu. Wanapotiwa nguvuni watuhumiwa wa ugaidi hufanyiwa mambo ya kinyama na serikali zinazowashika.

Tumesikia wiki iliyopita unyama waliokuwa wakifanyiwa watuhumiwa wa ugaidi waliokuwa mikononi mwa Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA). Kuna wanaodai kwamba vitendo kama hivyo vingali vikiendelea hadi hii leo.

Zamani katika zama za Vita Baridi Marekani na washirika wake wa Ulaya ya Magharibi walikuwa haweshi kuzishutumu idara za kijasusi za nchi za Kikomunisti za Ulaya ya Mashariki kwa kuwatesa mahabusu.

Stasi, Idara ya Usalama au Polisi ya Siri, ya iliyokuwa Ujerumani ya Mashariki, ilipata jina baya duniani kwa uovu wake.Mbinu zake za utesaji zilipindukia mpaka kwa jinsi zilivyokuwa zikikirihisha. Hatujasahau kwamba hao "mastadi wa mateso" wa Stasi, kwa mfano, ndio waliowafunza watesaji wa nchi kadhaa za Kiafrika, zikiwa pamoja na wale wa Zanzibar katika zama za ukatili baada ya Mapinduzi ya 1964.

Ile ripoti iliyotolewa wiki iliyopita kuhusu utesaji wa CIA inaonyesha kwamba Marekani nayo inafanya yaleyale iliyokuwa ikiyakemea yalipokuwa yakifanywa na Stasi. Kwa hakika shirika la CIA limefurutu ada kwa utesaji wake.

Shirika hilo la kijasusi linasaidiwa na vyombo vya vya usalama vya nchi kadhaa za Kiafrika katika mipango yao ya kuwadhibiti na kuwatesa wananchi wa nchi hizo wenye kushukiwa kwamba wanahusika na vitendo vya ugaidi au kwamba wana mahusiano na magaidi.

Ushirikiano uliopo baina ya vyombo vya usalama vya mataifa yetu na mashirika ya kijasusi ya madola makubwa hasa lile la CIA umegeuka kuwa ngao yeye kuzipa kinga serikali zetu ziwafanye watakavyo wananchi wenzetu wenye kudhaniwa kwamba wana harufu ya kigaidi.

Ndio ukaona polisi wa Kenya wakawa hawana muhali kuua watu misikitini wakijuwa kwamba hakuna litalowafika. Au ukaona wapinzani wa serikali ya Tanzania mbiombio wakipakwa rangi ya ugaidi, wakitiwa ndani na kuteswa kwa vile serikali inajua namna itavyoweza kujikosha wafadhili watapowasaili kuhusu ukiukwaji wa haki za binadamu.

Hao wafadhili nao wanakuwa hawana ubavu wa kuzisaili serikali zetu endapo wao wenyewe wanazikiuka haki za binadamu za washutumiwa wa ugaidi. Tunaishi katika mazingira ya hofu na yenye kutisha.

Serikali za wakubwa na za kwetu zinatuingilia mpaka vyumbani mwetu tunamolala. Zinatupiga darubini wenyewe tukiwa hatujui, zinasikiliza simu zetu, zinaziingilia kompyuta zetu na kusoma baruapepe zetu.

Hakuna tufanyalo ambalo serikali hizo hazilijui. Na juu ya yote hayo, juu ya teknolojia yao ya hali ya juu basi serikali hizo zinafanya makosa. Zinawatia watu hatiani kwa makosa na zinawaadhibu bure bila ya kuwa na hatia.

Mfano mzuri ni ule wa kisa cha mvuvi wa Zanzibar Suleiman Salim. Kijana huyu alitekwa nyara na wenye kuwasaka magaidi na halafu "akauzwa" na madalali kwa shirika la CIA kwa dola za Marekani zaidi ya nusu milioni. Alisafirishwa hadi Djibouti, kwenye kambi kuu ya jeshi la Marekani la Africom. Huko aliteswa. Halafu akapelekwa Afghanistan kwenye kambi nyingine ya jeshi la Marekani.

Aliteswa mateso ya kila aina na hatimaye aliachiwa baada ya miaka mitano ushei bila ya kupatikana thibitisho lolote kwamba alikuwa gaidi. Inasemekana kwamba waliomteka nyara walikosea.Wakimfikiria ni Myemeni anayeshutumiwa kuwa ni gaidi wa Al Qae'da.

Bila ya shaka serikali zetu – ya Muungano na ya Zanzibar - ni lazima ziwe macho na ziwachukulie hatua magaidi kwa vile kitisho cha ugaidi nchini ni cha kweli. Si kitisho cha mchezo. Lakini vyombo vyetu vya usalama pamoja na mahakama vinawajibika vichukuwe hatua zao kwa insafu. Visikubali hata siku moja kutumiwa na serikali au na chama kinachotawala kwa dhamiri za kisiasa za kupambana na mahasimu wao wa kisiasa.

Chanzo:Raia Mwema
 
Back
Top Bottom