SIMULIZI YA KWELI:Niliolewa na wanaume watatu

Kanungila Karim

JF-Expert Member
Apr 29, 2016
20,744
25,425
a1b42940d8d9b7dc280fd7346ec77ace.jpg

SEHEMU YA 01:

Ninaposema niliolewa na wanaume watatu, nataka nieleweke vizuri kwamba walinioa na niliishi nao kwa miaka kadhaa bila wao wenyewe kujuana. Kwa maneno mengine ni kwamba nilikuwa mke wa wanaume watatu kwa wakati mmoja, wanaume wenyewe wakiwa hawajui.
Sijui niseme ulikuwa uhuni au ni tamaa ya maisha au ulikuwa ni ujinga, sijui.Tukio hilo nililifanya miaka michache iliyopita wakati huo nikiwa bado msichana mwenye matumaini ya maisha.
Kielimu sikuwa nimesoma zaidi ya ile elimu ya kufuta ujinga, yaani kujua kusoma na kuandika. Niliishia darasa la saba tu. Na nilikomea darasa hilo kutokana na utoro wangu shuleni.
Sikuwahi hata kufanya mtihani wa taifa, nilikuwa siendi shule. Baba na mama yangu walikuwa wameshafariki dunia. Mama alifariki dunia nikiwa darasa la tano na baba alimfuata nikiwa darasa la saba ambalo sikulimaliza.
Nilielezwa kuwa nilikuwa na akili lakini sikuwa nikipenda masomo hata kidogo. Wanafunzi wenzangu niliokuwa nao darasa la saba waliniambia laiti ningefanya mtihani wa darasa la saba ningefaulu kwenda sekondari kutokana na akili yangu.
Licha ya kuishia darasa la saba, ujanja wangu uliniwezesha kuzungumza lugha ya kiingereza kwa ufasaha mzuri ila kwenye kuandika ndiyo ilikuwa balaa lakini nilikuwa ninaweza kusoma vitabu na magazeti yaliyoandikwa kwa lugha hiyo.
Watu wengi wasionijua vizuri walikuwa wakinidhania nilikuwa na elimu ya chuo, kumbe ni ya msingi.
Wakati naacha masomo nilikuwa na umri wa miaka kumi na tatu. Nilikuwa nikiishi na shangazi yangu maeneo ya Ilala jijini Dar. Shangazi alinichukua baada ya wazazi wangu wote kufariki dunia.
Jina langu ni Mishi. Baba yangu alikuwa anaitwa Ramadhani Mzaka, Mdigo wa Tanga. Mama yangu ndiye alikuwa Mwarusha. Alikuwa mwanamke mweupe kama Mwarabu. Mimi ndiye nilishabihiana naye kwa sura, weupe na uzuri.
Vile vishawishi vya wanaume ndivyo vilivyoniingiza katika balaa nikiwa na umri mdogo. Kulikuwa na kijana mmoja aliyekuwa akiitwa Sele, maarufu kama Sele Msela. Yeye ndiye aliyeniingiza katika mapenzi.
Nilikuwa nimesoma naye katika shule ya msingi darasa moja. Mimi nilipoacha masomo, yeye aliendelea hadi akafika kidato cha nne.Miaka miwili baadaye alifanikiwa kupata kazi Shirika la Bandari. Nilikuwa nikikutana naye karibu kila siku kwa vile tulikuwa tunaishi mtaa mmoja.
Sele alikuwa kijana wa kwanza kunitamkia kuwa alitaka kunichumbia baada ya kuwa naye kwa muda mrefu. Miezi michache baadaye Sele akakamatwa na vitu vya wizi bandarini. Alikuwa na mchezo wa kukwapua-kwapua vitu na kuja kuviuza mjini.
Ingawa alishinda kesi, alifukuzwa kazi na kurudi kijiweni. Kwa vile alishazoea kushika pesa, maisha yalimshinda akakimbilia Sauzi kutafuta maisha. Siku za kwanza-kwanza tulikuwa tukiwasiliana kwa simu akinipa matumaini kwamba dhamira yake ya kuja kunioa ilikuwa palepale lakini siku zilivyozidi kwenda mawasiliano yetu yakakatika.
Siku zikazidi kwenda. Nikamsahau Sele kwani hatukuwa na mawasiliano tena.Siku moja nilikuwa natoka Kigoma. Basi liliharibika njiani. Tulikaa hadi usiku, basi lilikuwa bado likishughulikiwa. Likapita lori likielekea Dar. Nilikuwa nimesimama peke yangu pembeni mwa barabara.
Dereva wa lori hilo aliponiona alifunga breki akatoa kichwa kwenye dirisha na kuniuliza.
“Unakwenda Dar?”
Nilikuwa kwenye lindi la mawazo yaliyochanganyika na uchovu. Ile sauti ya dereva ikanishitua.
“Unasemaje?” nikamuuliza.
“Unakwenda Dar?” Akaniuliza tena.
“Ndiyo ninakwenda Dar lakini basi letu limeharibika.”
“Uko tayari kusafiri kwa lori?”
“Acha lori, hata kwa trekta niko tayari. Nimechoka sana.”
“Njoo ujipakie twende.”
Kwa vile sikuwa na mzigo wowote zaidi ya mkoba wangu ambao nilikuwa nao begani nikasogea kwenye lori hilo. Taniboi alifungua mlango akashuka na kunipisha. Nikaingia kwenye lori.
Nikawekwa katikati. Kulia kwangu kulikuwa na dereva. Kushoto kulikuwa na taniboi.
Tukaanza safari.
“Unatokea wapi?” Dereva akaniuliza.
“Natoka Kigoma,” nikamjibu na kuongeza:
“Lakini najuta kupanda lile basi, limeharibika njiani mara tatu.”
“Pole sana. Sasa wewe ni mkazi wa Kigoma au Dar?”
“Ni mkazi wa Dar. Kigoma nilienda tu mara moja.”
Wenyewe walikuwa wakitafuna mahindi ya kuchemsha waliyonunua njiani. Wakanipa moja na mimi nikawa natafuna.Ilipofika saa 2:00 usiku. Lori likasimama katika kijiji kimoja. Tukashuka kwa ajili ya kupumzika na kupata maakuli. Mimi nilikataa kula kwa sababu nilikuwa nimechoka na sikuwa nikitamani kula kutokana na ile fadhaa ya safari.
Lakini dereva wa lori hilo alinilazimisha nile.
“Tutafika alfajiri, hutapata chakula tena,” akaniambia.
Nikaamua nile. Nikala kuku mzima na wali. Wakati nataka kulipa dereva akaniambia nisilipe. Akalipa yeye. Nikamshukuru kwa wema wake.
Baada ya kula tulipumzika kwa muda mrefu tukizungumza kile na hiki. Tulipoanza tena safari nililala ndani ya lori. Mpaka nakuja kuzinduka tupo Chalinze.
“Tuko wapi hapa?” Nikamuuliza dereva.
“Tuko Chalinze,” dereva akanijibu.
“Kumbe nimelala sana. Ni saa ngapi sasa?”
“Inakaribia kuwa saa 9:00 usiku.”
Pale Chalinze lori lilisimama tena. Tukashuka. Tuliingia kwenye mgahawa mmoja tukanywa chai. Dereva akamtuma taniboi wake akanunue mirungi.
Sisi tulibaki kwenye mgahawa hadi taniboi alipokuja na bahasha iliyofungwa mirungi. Nikamsikia dereva akimuuliza taniboi huyo.
“Umepata gati au shambarungu?”
“Nimepata gati.”
Dereva akaifungua palepale na kuitazama.
“Hii ni giza halafu ni kilalo,” akasema baada ya kuiangalia.
“Saa hizi huwezi kupata ya leo.”
Vilikuwa vichanga sita. Dereva alichagua vichanga vitatu akachukua yeye, vitatu akampa taniboi wake.“Umenunua bigijii?” Akamuuliza.
“Ndiyo hizi hapa.”
Zilikuwa kwenye mfuko. Taniboi akatia mkono mfukoni na kutoa bigjiii hizo za ubani zipatazo kumi.
Dereva alichukua tano na tano nyingine akamuachia taniboi.
Itaendelea
 
SEHEMU YA 02:

Vilikuwa vichanga sita. Dereva alichagua vichanga vitatu akachukua yeye, vitatu akampa taniboi wake.
“Umenunua bigijii,” akamuuliza.
“Ndiyo hizi hapa.”
Zilikuwa kwenye mfuko. Taniboi akatia mkono mfukoni na kutoa peremende hizo za ubani zipatazo kumi.
Dereva alichukua tano na tano nyingine akamuachia taniboi. SASA ENDELEA…

Turudi kwenye gari,” dereva akamwambia taniboi wake.
Dereva huyo niliyekuwa nimekaa naye akanyanyuka na kuniambia.
“Twende.”
Na mimi nikanyanyuka, tukatoka na kurudi kwenye gari. Hawakuondoka hapohapo, kwanza walianza kutafuna mirungi yao huku wakivuta sigara.
Walikuwa wamenikera sana kutokana na ule moshi wa sigara. Ni vile walinisaidia tu ndiyo sababu niliwavumilia.
“Kwani hii mirungi inawapa ladha gani?” nikawauliza.
“Inatupatia zaidi ya ladha,” dereva akanijibu.
“Nini sasa?”
“Inatupatia handas!”
“Nimekuwa nikiwasikia walaji mirungi pale Dar wakitaja hiyo handas lakini sijui maana yake.”
Nilipowaambia hivyo wakanicheka.
“Sasa mnacheka nini jamani wakati mimi nauliza?”
“Handas ndiyo kilevi cha hii mirungi. Kwanza unajisikia raha na pili inakupa hisia fulani ya kukuburudisha,” dereva akaniambia.
“Inawapa hisia gani?”
“Kila mtu inampa hisia ya namna yake. Kuna watu wanapata hisia za utajiri wanapokula mirungi. Wanajenga majumba na kununua magari ya kifahari mawazoni mwao.”
Nikaangua kicheko.
“Yaani wanawaza tu kuwa wananunua magari na kujenga nyumba wakati si kweli?” nikawauliza huku nikiwatazama kwa zamu dereva na taniboi wake.
“Hebu jaribu kutafuna utaona mwenyewe na hutauliza tena,” dereva akaniambia na kunipa majani kadhaa ya mirungi.
Nikaanza kutafuna nikiwaigiza vile wanavyokula. Nilihisi ilikuwa michungu na ilikuwa na ukakasi.
Nikakunja uso.
“Kumbe ni michungu namna hii?”
“Kula na bigijii,” dereva akaniambia.
“Nipe basi.”
Dereva akanipa bigijii moja. Nikaifungua na kuimega kidogo. Utamu wake ukapunguza ule uchungu niliokuwa nikiusikia. Nikaendelea kutafuna.
“Halafu nasikia inarusha usingizi,” nikawauliza.
“Ndiyo maana unaona madereva wengi wa malori wanakula,” dereva akaniambia.
“Hata baadhi ya madereva wa daladala pia wanatafuna. Nimeshawaona.”
“Ile kazi yenyewe ni pasua kichwa, lazima wale mirungi.”
Dereva akatazama saa yake kisha akasema;
“Tuondoke.”
Akaliwasha gari na kuliingiza barabarani. Tukaanza safari ya kuelekea Dar.
Dereva huyo alikuwa akiendesha huku akiendelea kula mirungi. Wakati ule ndiyo nilitambua kuwa mirungi ilikuwa ikifanya kazi ndani ya kichwa chake kwani mazungumzo yake yalianza kubadilika.
“Unajua tangu tumekupakia sijakuuliza jina lako, unaitwa nani?” akaniuliza.
“Naitwa Mariam,” nikamdanganya kisha nikamuuliza.
“Na wewe unaitwa nani?”
“Naitwa Musa. Unaishi Dar sehemu gani?”
Sikutaka kumtajia mahali ninapoishi lakini niliona kama nitamtajia anaweza kunipeleka hadi nyumbani, nikamwambia;
“Naishi Ilala.”
Musa akanitazama usoni kisha akanitazama kifuani.
“Hivi unafanya shughuli gani?”
“Biashara tu,” nikaendelea na uongo wangu. Sikuwa na biashara yoyote.
“Unafanya biashara gani?”
Nikafikiri kidogo kisha nikamwambia;
“Huwa naleta mchele kutoka Mbeya.”
“Kutoka Mbeya au Kigoma?”
“Kutoka Mbeya, Kigoma nilikwenda tu kwa matatizo yangu mengine.”
Ukapita ukimya mfupi kabla ya dereva huyo kuniuliza tena;
“Una watoto?”
“Sina hata mmoja.”
“Kumbe hujaolewa?”
“Bado kwanza.”
Nilipoona mazungumzo yake hayaingii kichwani mwangu nikajidai kumuuliza;
“Mmepakia nini?”
“Bidhaa tu za Wahindi.”
“Mkifika Dar, kesho mnaondoka tena?”
“Inategemea.”
“Inategemea nini?”
“Kupatikana kwa mzigo, kama mzigo upo tunaondoka tena.”
“Sasa nyinyi mnalala muda gani? Au ndiyo mnakula mirungi usiku na mchana?”
“Tunalala. Kama tunafika hii alfajiri tunasubiri kuche, tunashusha mzigo wa watu halafu narudisha gari, tunakwenda kulala. Kama kuna safari nyingine tunaweza kuondoka usiku au asubuhi ya kesho kutwa.”
“Kumbe mna kazi!”
“Wewe ndiye unaona tuna kazi lakini sisi wenyewe tumeshazoea.”
Baada ya kumkatisha yale mazungumzo yake ya kunidadisi maisha yangu nikawa nimemchanganya kidogo, hakunidadisi tena mpaka tuliposimamishwa na polisi wa usalama barabarani.
Walikuwa polisi wanne waliokuwa wameegesha gari lao pembeni na kusimama kando ya barabara. Nikaogopa.
“Wakikuuliza wewe nani, wambie ni mke wangu. Usiseme ni abiria. Haturuhusiwi kuchukua abiria,” dereva Musa akaniambia.
Nikamkubalia kwa kichwa.
“Ficha hiyo mirungi.”
Nikaificha chini ya siti. Ile iliyokuwa midomoni nikaitema haraka. Dereva naye alifanya hivyohivyo.
Je, nini kiliendelea? Fuatilia
 
1 Reactions
Reply
Back
Top Bottom