Simulizi: Tulivyoteswa kwenye mianzi ya kichawi

Kanungila Karim

JF-Expert Member
Apr 29, 2016
20,744
25,425
KIJIJI cha Nangose kipo jirani na mji wa Masasi njiani kuelekea kijijini kuna mimea mingi sana iitwayo mianzi ambayo watu huikata kwa matumizi mbalimbali kama vile kujengea nyumba, kutengenezea ungo au vyombo maalum wenyeji huviita ichinumba ambavyo hutumika kunywea pombe ya kienyeji ya mtama, wengine hutengeneza fimbo maalum ya kutembelea, au mipini ya majembe na kadhalika.

Mimi naitwa Issa Namakoto, nakusimulia simulizi hii nikikurudisha nyuma miaka kadhaa iliyopita tukiwa Dar es Salaam tulipata taarifa kuwa Nangose kuna bustani ya ajabu ya mianzi iliyopandwa kimstari na mtu asiyejulikana.

Siku moja mimi na rafiki zangu 25 tuliamua kwenda kujionea bustani hiyo, tulifunga safari yetu tukitokea Dar es Salaam, tulikuwa vijana watupu wa kike na kiume.
Tuligeuza ziara hiyo kama pikiniki fulani. Wakati tunasafiri tulipofika Nangurukulu, njia panda ya kwenda Kilwa, tulipumzika kwa ajili ya kula chakula cha mchana.

Tulijaribu kuhoji wenyeji tuliokuwa nao kwenye basi na tuliambiwa kuwa ndani ya bustani hiyo kuna maua mazuri yaliyokuwa yamezunguka mianzi hiyo ya ajabu na kulikuwa na mtunzaji ambaye alikuwa ni mtu mwenye umri mkubwa aliyekuwa akisimulia mambo ya bustani hiyo.

Aliyekuwa anatusimulia pale Nangurukulu alitufanya tutamani kufika mapema katika bustani hiyo ili tushuhudie maajabu tuliyoambiwa yapo. Msimuliaji huyo alisema kuwa watu wanaokwenda kujionea maajabu hayo lazima watimize masharti fulani ambayo mtunza bustani huwaambia.

Baada ya kula safari ilianza kwa furaha kubwa, ndani ya basi ‘kosta’ kulikuwa na mazungumzo yanayohusu bustani hiyo ya ajabu na mwenzetu mmoja alisema aliambiwa kuwa ndani yake kuna matunda pori matamu sana ambayo hayana msimu.

Basi letu dogo lilipita Lindi mjini saa nane mchana na dakika chache baadaye tukafika Mnazi Mmoja, njia panda ya Lindi na Masasi na Mtwara.
Hapo pana pilikapilika na kuna mizani ya kupimia magari mazito.
Baada ya kufika hapo, dereva alituambia tushuke kwa ajili ya kununua chochote tulichohitaji na kujisaidia, alitupa dakika kumi na tano.

Kwa kuwa mimi ni mpenzi sana wa korosho, nilinunua za shilingi mia tano na soda.
Muda tuliopewa na dereva ulipoisha tuliingia kwenye gari na kuanza safari na kwenda moja kwa moja hadi Mtama, (Jimbo la Mbunge Nape Nnauye) tukafika saa nane na nusu na njiani kabisa tukakutana na umati ukicheza ngoma, ulikuwa ukikatiza barabara kuu ikabidi dereva asimame, kuwapisha.

“Nadhani hawa wanasherehekea mambo ya jando na unyago kwa sababu kipindi chenyewe kilikuwa cha mavuno,” nilijisemea.

Tulipotoka pale Mtama usingizi ulinishika, nikalala usingizi mzito na nilishtukia nikiambiwa kuwa tumefika Ndanda. Hapa ni maarufu kwa mikoa ya kusini kutokana na kuwa na hospitali kubwa ya misheni na shule ya sekondari.

Nilifikicha macho na kuona mji. Siyo mji mkubwa, una barabara ya lami moja tu na kando ya barabara kuu tunayopita kuna soko. Tulikuta wenyeji wakiuza mbaazi kwa mafungu na abiria waliokuwa wakisafiri kwa mabasi makubwa walikuwa wanajinunulia mbaazi hizo.

Wakati tunatoka Dar tulielezwa kwamba tukifika Ndanda kuna mtu mmoja anaitwa Ngalipambone ataungana nasi na ndiye atakayetuongoza hadi Nangose. Kutokana na urefu wa jina lake watu wanakatiza na kumuita bwana Ngali.

Haikuwa ngumu kumpata kwa sababu alikuwa anawasiliana na dereva wa basi letu mara kwa mara kwa njia ya simu.

“Habari zenu jamani!” Alisalimia bwana Ngali.
“Nzuri, shikamoo!” tuliitikia na kuamkia kwa pamoja kama vile kulikuwa na mtu aliyekuwa akituamuru.
“Marahaba. Mimi naitwa Ngali. Nimeambiwa niwapeleke kwenye bustani ya mianzi ya Nangose.”
“Ni kweli bwana,” alisema dereva.
“Kutoka hapa siyo mbali sana na tutafika leoleo,” akasema bwana Ngali na kuketi kwenye kiti cha mbele kwa dereva msaidizi, ambaye aliinuka na kwenda kusimama mlangoni kama kondakta wa daladala afanyavyo.

Bwana Ngali ndiye alikuwa kinara au dira ya kwenda kwenye bustani hiyo ya ajabu ambayo watu wamekuwa wakiisifia.

Baada ya kufika mjini Masasi hatukukaa, basi lilielekezwa kuifuata barabara ya Nachingwea. Ni mwendo mfupi tu kutoka hapo kwenye njia panda ya kwenda Tunduru ambapo kuna gereza la wilaya tukamsikia bwana Ngali akimuamuru dereva afuate njia ya Nachingwea;

“Pinda kushoto,” tukaiacha barabara kuu na kuifuata ya vumbi. Dakika kama tano bwana Ngali akasema;
“Saa tumefika Nangose, pinda kulia kama tunaelekea Nchoti.”
Lakini baadaye tukaingia barabara yenye vumbi jekundu ilikuwa kama tunaelekea Kijiji cha Nchoti lakini tukapinda tena kulia.

Tulianza kuona bustani ya ajabu na tulipofika eneo fulani bwana Ngali alisimama katikati ya basi akasema:
“Jamani mimi hapa ndiyo mwisho wa safari yangu. Bustani ya mianzi ni hii kuanzia hapa, huko mbele kuna mtu mtamkuta ambaye ndiye atakuwa mwenyeji wenu.”

Nilijiuliza huku ni porini sasa huyu bwana Ngali atarudi kwa njia gani mjini? Hata hivyo, wakati nawaza hayo nilishtukia pikipiki ikitoa mlio, kumbe alimpigia mtu wa bodaboda akawa anatufuata kwa nyuma.

Alishuka kwenye basi letu, akapanda pikipiki na kutoweka. Dereva wetu aliendelea na safari hadi katikati ya bustani ya mianzi. Ilikuwa nzuri sana ambayo sijapata kuona maishani mwangu.

Mianzi ilikuwa imepandwa kwa mstari na pia kulikuwa na maua ya kila aina. Ajabu ni kwamba sehemu zote tulizopita zilikuwa kavu, majani yalikauka lakini katika bustani hiyo ni tofauti sana. Mianzi yote, maua na miti ni ya kijani kibichi.

Alitokea mzee mmoja ambaye alionekana kuwa ni chotara, alikuwa na ndevu nyingi nyeupe na alikuwa na mvi karibu kichwa chote, mashavu yalikuwa yamemshuka kwa uzee.

“Karibuni wajukuu zangu,” alisema mzee huyo tukamuamkia.

Nilimsogelea kwa kuwa mimi ndiye nilikuwa mkuu wa msafara. Alinishika mkono mwilini nikaona kama nimepigwa shoti ya umeme! Nikapiga yowe!

Je, nini kitatokea?
 
Alitokea mzee mmoja ambaye alikuwa chotara, alikuwa na ndevu nyingi nyeupe na karibu kichwa chake chote kilikuwa na mvi.
“Karibuni wajukuu zangu,” alisema mzee huyo.
Kwa kuwa mimi ndiye nilikuwa mkuu wa msafara nilimsogelea. Aliponishika mkono mwilini nikaona kama nimepigwa shoti ya umeme! Nikapiga yowe!
Je, nini kitatokea?
SONGA NAYO…
Nilimuangalia usoni baada ya kuniachia akawa anatabasamu, nikajua kuwa alikuwa na mapengo na meno yake yalikuwa meusi kama vile anakula ugoro.
“Nisikilizeni. Mimi naitwa Mzee Mavaka. Huyu kiongozi wenu nimemuonesha kuwa katika bustani hii hakuna mchezo. Kila unachokiona kiheshimu. Ukitaka kuchuma chochote ni lazima uniambie mimi ili niweze kutoa baraka za kufanya hivyo.
Hii ni bustani iliyohifadhiwa na himaya ingine ili kutoa funzo kuwa mazingira yanapaswa kutunzwa hivi. Kwa hiyo usichume kitu bila ruhusa yangu, nawajua nyinyi vijana wa Dar mlivyo wabishi, ubishi wenu uishie kulekule kabla ya kuingia katika bustani hii tukufu ya Nangose, sawa?”
Tukaitikia kwa pamoja “Sawaaa.” Ilikuwa kama vile tuliambiana.
“Mianzi hii mnayoiona ni ya aina yake, imepandwa kwa mstari na kwa umaridadi kama mnavyoona na kila kitu kilichomo ndani ya bustani hii ni fahari ya dunia hii. Ogopeni, heshimuni. Ona jinsi nyasi zilivyofyekwa na vipepeo wanavyofurahia mandhari hii.
aribuni zingatieni sheria hiyo ya kutochuma chochote bila ruhusa yangu,” alionya.
Alitupeleka kwenye mgahawa wa bustani tukala chakula bure. Ajabu ni kwamba tulikuta ‘bufee’ yenye kila aina ya chakula na kila mtu alikuwa anajipakulia mwenyewe chakula akipendacho.
Pia kulikuwa na vinywaji baridi vya kila aina. Tulimuuliza yule mzee Mavaka nani analipia bili ya chakula, akasema hiyo analipa mwenye bustani. Tulimuuliza ni nani? Hakujibu akawa anatabasamu tu!
Vijana wa Dar kama unavyowajua ni wabishi, wakaanza kuchuma ‘maembe ya kusini’ wenyewe huziita embe mali, wakawa wanakula, ulikuwa ni msimu wa maembe. Wengine hasa wasichana wakawa wanachuma maua yenye harufu nzuri na kuyatunga kwenye nyuzi zao kisha kuzivaa shingoni bila kupata idhini ya yule mzee.
Tuliendelea kutembelea bustani ile na kugundua kuwa kulikuwa na sehemu ambayo ilikuwa na maji yametuama ni kama bwawa kubwa na kulikuwa na mtu ameketi kando yake, tulikwenda kuangalia anafanya nini, kumbe alikuwa anavua samaki ajabu ni kwamba alikuwa hatuangalii, alikuwa anavua samaki mmojammoja kwa kutumia ndoana na kuwaweka kwenye kapu kubwa.
“Mzee shikamoo.” Nilimuamkia.
“Siwezi kukujibu salamu yako,” alijibu kijeuri yule mzee.
“Sasa mzee mbona unajibu hivyo, tumekukosea nini? Sisi ni wageni hapa.”
“Makosa mliyoyafanya mnajifanya hamyajui mpaka mimi niwaambie?”
“Tuambie mzee, sisi ni kama wajukuu zako.”
“Kwanza ondokeni hapa kwenye bwawa la samaki, watoto wajinga sana nyie, wajukuu zangu gani msiosikiliza mnachoambiwa na wakubwa wenu? Nasema ondokeni!” alizidi kufoka, alituangalia, macho yake yalikuwa mekundu kama mtu aliyevuta bangi!
Tuliondoka eneo hilo, mbele yake tuliona kuna mianzi mizuri sana na watu wanaikata ile iliyokomaa tu na kuipakia kwenye gari.
“Jamani habari za hapa,” niliwasalimia watu wale.
“Nzuri. Mnataka mianzi? Kuna masharti ya kuikata,” alijibu mmoja wa wale vijana waliokuwa wakikata na wengine walikuwa wakiipakia kwenye gari aina ya Canter.
“Masharti gani? Hayo ni mambo ya kizamani bwana,” mwenzetu mmoja akasema.
“Siyo mambo ya kizamani, kuna masharti msipoyatekeleza mtapata madhara mazito. Tunaambiwa ni hatari na unaweza kupoteza wenzako wote uliofuatana nao.”
“Watapoteaje? Acheni hayo, uongo mtupu,” akadakia kijana mwingine miongoni mwetu.
“Wewe unayetueleza habari hizo umewahi kushuhudia mtu akiadhibiwa kwa kula matunda au kukata mianzi katika bustani hii tangu uzaliwe?” akadakia dada mwingine.
“Mimi sijashuhudia lakini kuna simulizi nzito sana nimesimuliwa na wazee kuhusu bustani hii ya mianzi ya Nangose.”
“Kwanza tueleze kwa nini inaitwa bustani ya mianzi ya Nangose wakati kuna matunda mengi kama vile miembe na maua ya kila aina?”
“Hilo mimi siwezi kujibu, kwa kuwa mimi siye mwenye bustani,” alijibu kijana huyo.
Yupo kijana miongoni mwetu alichuchumaa na kuchukua mundu na kwenda kukata mianzi michanga ili aone kama inatoa pombe ya ulanzi kwani yeye ni mtu wa Iringa.
Mara nilimuona mzee Mavaka aliyetupokea akitoka kwenye ule mgahawa akiwa ametoa macho na mwili kumtetemeka.
“Nani kakata mianzi michanga na kuchuma maembe na maua bila idhini yangu? Nyinyi vijana wa Dar habari zenu nimezisikia ndiyo maana nikawaonya kabla, nimeona kwenye chombo ndani mkichuma embe na maua na sasa mmekata mianzi, sasa mtaona cha mtema kuni,” alifoka mzee Mavaka.
Huku akitetemeka, sekunde chache tukashuhudia tetemeko la ardhi! Bustani yote ikawa inatetemeka! Mianzi ikawa inatupiga, yowe zilikuwa nyingi na hatukuwa na uwezo wa kukimbilia kwenye basi.
Nilishuhudia ardhi ikizama huku baadhi ya wenzangu wakiwa wamezimia kutokana na kupigwa na mianzi. Kipande cha ile bustani kiliendelea kuzama huku tukiwa juu yake, nikawa naona giza linaanza kuingia kadiri tulivyokuwa tunazama nuru ya jua ikawa inapotea machoni mwangu badala yake nikawa nasikia sauti za kutisha.
Mshangao uliniingia baada ya kuona kutitia huko kwa bustani kuliendelea kwa saa nzima nikawa sioni chochote isipokuwa giza lilikuwa totoro. Moyo wangu ulinienda mbio nikijua kuwa sasa utakuwa mwisho wa maisha yetu.
Nilianza kutetemeka wakati ardhi ikizidi kuzama, ilikuwa kama tupo kwenye lifti na tunashushwa chini kutoka ghorofani, swali likawa tunazamishwa na nani na je, tutapona au mwisho wa yote ni kufunikwa na ardhi? Moyoni niliwalaumu wenzangu kwa kutofuata masharti ya bustani ile ya Mianzi ya Nangose.
Je nini kitatokea?
 
SEHEMU YA 03



Nilianza kutetemeka wakati ardhi ikizidi kuzama, ilikuwa kama tupo kwenye lifti na tunashushwa chini kutoka ghorofani, swali likawa tunazamishwa na nani na je tutapona au mwisho wa yote ni kufunikwa na ardhi? Niliwalaumu wenzangu kimoyomoyo kwa kutofuata masharti ya bustani ile ya Mianzi ya Nangose.
Je, huo ndiyo mwisho wa vijana hao?


SONGA NAYO…


Ajabu ni kwamba pamoja na ardhi kuendelea kuzama, sikusikia sauti yoyote kuonesha kuna mashine inaendesha kipande kile cha ardhi kukipeleka chini zaidi ya ardhi.


Kwa kuwa saa yangu ilikuwa inatoa mwanga kwenye giza nene, niliiangalia nikagundua kuwa sasa ni saa mbili tukizama ardhini, sekunde kama kumi hivi nilianza kuona mwanga unajitokeza ukitokea chini ya ardhi.


Nilihisi kwamba tutatokea kwenye ardhi nyingine ambayo hata hivyo sijui kama ni mauzauza au kitu gani.Niliangalia kwa makini nikagundua kwamba bado nilikuwa ndani ya bustani ya Mianzi ya Nangose na mwanga ule hafifu ulioanza kujitokeza ulinifanya niwaone wenzangu wote kuwa bado walikuwa hawajarejewa na fahamu.
Nilikuwa na wazo lingine kabisa kuwa inawezekana wenzangu walifariki dunia wakati mimi nikiamini kuwa walikuwa wamezimia.


Woga ukazidi kunipanda, nikaamua nimsogelee mwenzetu mmoja aliyekuwa karibu na pale nilipokuwa nimeketi kuona kama anapumua au tayari ameshafariki dunia.
Nilikuwa sijawahi hata siku moja kumgusa mtu aliyefariki dunia, sasa nilikuwa sijui anakuwaje. Lakini nikakumbuka simulizi za wazee kwamba mtu akishapoteza uhai mwili wake unakuwa baridi.


Nilimgusa mwenzangu yule na kukuta mwili wake una vuguvugu, hivyo nikaamini kwamba hakufariki. Nilikumbuka kitu kingine, kumgusa kwenye mshipa mkubwa unaopeleka damu kichwani. Kweli nilisikia mapigo ya moyo wake kwa kuhisi kwa mikono kuwa damu inatembea kupelekwa kichwani.


Nilimtikisa huku nikimuita jina “Hamadi, Hamadi, Hamadiii,” akawa kimyaa.
Nilimsogelea msichana mmoja anayeitwa Helena naye nikafanya kama nilivyofanya kwa Hamadi. Nilijaribu kumuita, haikusaidia kitu.


Mkononi mwangu nilikuwa na saa yenye uwezo wa kuonesha muda hata kwenye giza, yaani mishale yake ilikuwa inatoa mwanga, ilinionesha kuwa tangu tuanze kuzama chini ya ardhi tumeshatumia saa tatu. Nilipigwa na butwaa nisijue la kifanya.


Mwanga ulikuja ghafla na kujikuta tupo katika dunia nyingine. Baadaye nilisikia ardhi tuliyokuwa juu yake ikigonga kama vile huko chini yake kuna bati ikawa kama bustani imetua ardhini lakini ajabu ni kwamba kulikuwa na mwanga wa kutosha na tulionekana kama vile tupo juu ya dunia mpya!


Dakika chache baadaye tulishtukia tukiwa tumezungukwa na wanaume wenye ndevu ndefu ambao waliwapulizia dawa wenzangu waliozirai, wakazinduka wote, wakashangaa zaidi yangu kuona tulikuwa dunia nyingine!


Tulipangwa mstari mmoja na kuamriwa kutembea, hatukujua tunapelekwa wapi, wasichana tuliokuwa nao walikuwa wakilia kwa woga!
Japokuwa nilijikaza niliwaangalia wale watu wenye ndevu ndefu waliokuwa wakitusimamia. Tulipangwa mistari miwili na tukaambiwa kuwa tunakwenda kwa mfalme wa nchi ile.


“Tunakwenda kufanya nini?” Niliingiwa na ujasiri nikahoji.
“Ina maana nyinyi ni mataahira. Hamjui kosa hadi sasa?” mmoja wa watu wale aliyekuwa akionekana kama kamanda wao alisema.


“Tunaomba utusamehe,” alidakia kijana mwingine.
“Hakuna kusamehewa hapa. Unajua umetumia nini kufika huku?” akasema yule kamanda.


“Hatujui, kwani huku ni wapi?” niliuliza tena.
“Huku ni nchi ya Ntukuruku.”
Kimyaa kilitanda kwa sekunde kama tano hivi na tukabaki kuangaliana, Nilikuwa najiuliza nchi ya Ntukuruku ni nchi gani? Nilijitahidi kujikumbusha Jiografia, sikumbuki kama kuna nchi yenye jina hilo niliwahi kukutana nalo katika kusoma kwangu.


“Nisiwafiche, nitawaambia kosa lenu.”
“Tafadhali kamanda usitufiche, tuambie nini kosa letu hadi tukaletwa nchi hii ya chini ya ardhi?”
“Wakati mnaingia kwenye bustani ile ya Mianzi ya Nangose, hamkuambiwa miiko?” alihoji kamanda yule.


“Tuliambiwa,” nikajibu.
“Sasa kama ni hivyo, kwa nini hamkutii?”
Kimyaa.
“Nawauliza kwa nini hamkutii?”
“Hatukujua,” alijibu kijana mmoja.


“Hamkujua wakati mlijulishwa kuwa pale nidhamu inatakiwa.”
“Tunaomba sana utusamehe, hatutarudia tena. Sisi tulidhani ni utani tu.”
“Utani? Unaweza kutaniana na mtu mzima kama mzee Mavaka anayetunza bustani ile?”
“Kweli ilikuwa kama anatutania.”


“Hamna adabu kabisa. Kwenu mnataniana na mzee mkubwa kama yule? Hamna hata chembe ya adabu. Mnastahili kabisa kupelekwa kwa mfalme ili iwe fundisho.”
Kutoka pale ‘tulipotua’ na bustani ya mianzi hadi kwa mfalme ni mwendo mrefu. Tulitembea kwa nusu saa na sikuona dalili ya kufika. Tulizidi kuingia kwenye misitu minene yenye miti mikubwa na majani mengi ya kijani.


Moyoni nilikuwa najiuliza kama tutakuwa salama. Nilihisi tunakwenda kuuawa. Njia tuliyokuwa tunapita ilikuwa na alama ya matairi ya magari lakini hatukuona gari lolote likitupita.


Baadaye kwa mbali tukaona watu wengi sana walikuwa wamekusanyika huku wakipiga ngoma na wengine wakiimba.


Hatukuzielewa nyimbo zile zilikuwa na maana gani kwa kuwa walikuwa wakiimba kwa lugha ambayo hatukuijua. Kijana mmoja ambaye alikuwa nyuma yangu nilimhoji kama anaelewa chochote maana ya maneno yaliyokuwa yakiimbwa na watu wale, akasema hajui.


Hata hivyo, kijana mwingine ambaye alikuwa mbele yangu alisema anaelewa lugha hiyo. Nilimuuliza ni lugha gani wanatumia akasema ni Kimeto.
“Kimeto?”


“Ndiyo hicho ni Kimeto, lugha moja inayotumika Kaskazini ya Msumbiji.”
“Wanasema nini?”


“Wanasema hawa ni waharibifu, mfalme wape adhabu kali, ikibidi wafe.”
“Kha! Wanataka kutuua? Hawa watu mbona wakatili sana.”
Tulikaribia jumba la mfalme, tulimuona akiwa amesimama kwenye lango kuu.
Je, nini kitafuata?
 
SEHEMU YA 05


ILIPOISHIA
Wakati yote hayo yanafanyika mimi nilikuwa bado nimepigishwa magoni na kwa hakika magoti yalianza kuniuma kwa sababu pale chini palikuwa na changarawe na sikuthubutu kusimama au kukaa kwani niliwaza kwamba nikifanya hivyo, watanimaliza kwa mikuki yao.

SONGA NAYO…

Niliwaza hivyo kwa sababu nilijua kuwa kilichotufikisha pale ni kutotii sheria za kwenye bustani ya mianzi ya Nangose , sasa kutotii sheria mbele ya mfalme nilijiridhisha kuwa adhabu yake itakuwa kali na ya papo kwa hapo, yaani ama nikatwe kwa panga shingoni au kukitwa mkuki kifuani au mgongoni na kufa palepale.

Baadaye ngoma zilizokuwa zikipigwa zilisimama na nikamuona mfalme au chifu wa mji ule akishuka jukwaani alipokuwa huku akiwa bado ana panga mkononi. Nilihisi moyo kuchomoka kwa jinsi ulivyokuwa ukidunda kwani nilijua kuwa sasa anakuja kunikata kichwa.

Lakini nilijisemea moyoni kwamba akija kwa kusudio hilo sitakubali kuuawa kinyonge, kwamba ni lazima nitapambana naye. Nilijisemea hivyo kwa sababu hadi chifu au mfalme huyo anashuka, sikuwa nimefungwa mikono wala miguu, hivyo ningeweza kujitetea japokuwa nilijua kuwa kifo sitaweza kukiepuka kwa sababu wale watu wapo wengi na wanaume karibu wote walikuwa na mikuki.

Niliwaona wale wanawake kumi na mbili waliokuwa wakicheza wakiwa na mitungi kichwani, wakiitua na kuiweka mbele yangu.

Mfalme badala ya kunijia mimi aliiendea ile mitungi na kuteka maji kisha kumpa yule mzee Mavaka tuliyemkuta katika bustani ya Nangose aliyekuwa amesimama karibu yangu.

Wazo lingine lilikuja na kujiuliza hawa jamaa wanataka kuniua kwa kuninywesha maji yaliyokuwa kwenye mitungi yote kumi na mbili? Sikupata jibu.

Badala yake yule mzee Mavaka alichukua kata iliyokuwa na maji aliyokabidhiwa na mfalme na kupanda jukwaani ambapo kulikuwa kumelazwa wale wasichana wawili tuliokuwanao waliokuwa wamezimia na akaanza kuwamwagia mwilini.

Wa kwanza alipomwagiwa, alizinduka na akakaa palepale juu jukwaani. Msichana wa pili ilitumika mitungi zaidi ya mitatu kumwagiwa mpaka nikawa na wasiwasi kwamba inawezekana ameshakata roho.

Wakati nakata tamaa, mara nilisikia akikohoa, hapo moyo wangu ukatulia, nikaona Mungu amemponya. Wakati hayo yanafanyika, uwanja mzima ulikuwa kimya na aliyekuwa akitembea huku akiwa na kata yenye maji na akiwa anafanya kazi ya kuwamwagia maji wale wasichana ni mzee Mavaka tu.

Baada ya wale mabinti kuzinduka, mfalme alimuita mzee Mavaka na kumuuliza kama yupo tayari kuyasema makosa yetu sisi watu ishirini na sita.

“Ndiyo mfalme, nipo tayari kueleza makosa yao,” akasema mzee Mavaka.

“Eleza sasa,” mfalme akaamuru.

“Hawa vijana walikuja katika bustani yetu ya Nangose na kupata maelezo yote kuhusu masharti. Ajabu ni kwamba walikuwa wabishi na wajeuri. Wakaanza kuchuma matunda na maua na kukata mianzi bila ruhusa tena ile michanga.”

“Kha! Walikata mianzi michanga kweli?”

“Kweli mfalme na ndiyo maana nimewaleta hapa mbele yako.”

“Uliwaambia adhabu ya kukata mianzi michanga?”

“Sikuwaambia, lakini niliwaambia ni marufuku kufanya hivyo.”

“Baada ya kula matunda na kuchuma maua kisha kukata mianzi ulichukua hatua gani?”

“Hatua ya kwanza ilikuwa ni kuwafokea ili waone kile walichokifanya ni kitu kibaya lakini kwa kuwa kukata mianzi michanga hukumu yake unaitoa wewe, niliona ni vema kuwaleta kwako na ndiyo maana wako mbele yako sasa hivi.”

“Sawa, huyu aliyepiga magoti ni nani?”

“Walijitambulisha kwangu kuwa huyu ni kiongozi wao, anaitwa Issa Namakoto.”

“Bwana Namakoto, umesikia mashtaka yenu?”

“Mheshimiwa mfalme nimesikia, lakini nakuomba sana tusamehe, hatutarudia tena.”

“Hakuna cha kusamehewa. Kuna sheria hapa na sheria ni msumeno. Adhabu yake wote nyinyi ni kifo.”

Mfalme baada ya kusema hayo wenzangu wote wakaangua kilio, isipokuwa mimi. Nilikuwa nafikiria njia ya kujiokoa na kuwaokoa wenzangu.

“Mfalme nimesikia ulichokisema kwamba tunastahili kufa. Nakuomba sana, mimi kiongozi wao ni mtume wa Mungu, nakuomba sana tuepushie na adhabu yako mtukufu na utaona faida yake!” Nilisema kwa ujasiri huku nikijua kuwa nadanganya, sikuwa mtume.

“Nyinyi ni lazima mfe ili iwe fundisho kwa watu wanaofanya vitendo kama vyenu.”

“Tafadhali mfalme…” alinikatiza.

“Nisikilize. Adhabu yenu itakuwa ni kutumbukizwa kwenye shimo refu na humo kila mmoja wenu atajifia kwa wakati wake.”

“Lakini mfalme, ungetusikiliza kwanza…”

“Hakuna cha kuwasikiliza. Wote mtatupwa kwenye shimo refu, hiyo adhabu itaanza kutekelezwa kesho.”

Mwili wangu ulianza kutetemeka tena maana sikujua hilo shimo litachimbwa saa ngapi na sisi kufukiwa kesho au lilishachimbwa tayari.

Baada ya maneno yale ya mfalme, ngoma zilianza kupigwa tena na wale wanaume wenye mikuki wakaanza kucheza kwa kurukaruka kama Wamasai waliopandwa mori.

Wale wasichana wawili waliokuwa juu ya jukwaa waliozinduka walishushwa na wanawake wenzao na kuunganishwa na wengine wakaambiwa wawafuate wale wasichana kumi na mbili waliokuwa na mitungi.

Sisi wavulana tuliambiwa tuwafuate wale wanaume wenye mikuki. Nilijua hakutakuwa na mauaji tena ya kutumia mikuki kwa kuwa adhabu yetu ilishatangazwa kuwa ni kutupwa kwenye shimo siku iliyofuata.

Wavulana tulipelekwa kwenye nyumba moja ndefu kama ‘godauni’. Tuliketishwa chini mle ndani na baada ya muda kikaletwa chakula, kilikuwa chakula kingi na ni tofauti, tuliambiwa tuchague. Kulikuwa na pilau, wali mweupe na nyama.

Zile nyama zilikuwa za aina mbalimbali, zipo tulizoambiwa ni za ng’ombe, ngamia, mbuzi, kuku na bata. Mimi niliamua kujipakulia wali na nyama ya kuku.

Hata hivyo, hakuna aliyekuwa na hamu ya kula kwa kuwa tulijua kesho yake tungeuawa.

Je,nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 07


ILIPOISHIA
Nilifurahi sana kimoyomoyo kupata nafasi hiyo, nikajiambia “lazima nipange ya kumuambia mfalme ili kujiokoa, hiyo ni last chance yaani nafasi ya mwisho kwangu na jamaa zangu kuweza kujiokoa.
“Vipi, mbona kama unataka kuniambia kitu?”
“Nihakikishie tu kwamba mfalme nitaongea naye?”
“Utaongea naye, ni sheria, kuna wengi sana wanaokoka kwa kusema maneno ya mwisho hayo wakiyapangilia vizuri na kumuingia mfalme, mnaweza kupunguziwa adhabu.”
“Nitashukuru sana kupata nafasi hiyo.”
“Sawa. Nenda kalale usubiri kesho, siku ya kufa na kupona,” alizidi kunishauri.SONGA NAYO…
Tulijitenga na askari huyo na kukaa pembeni huku tukimchungulia kupitia nondo zilizowekwa mlangoni.
Niliingia kwenye sala ya kimoyomoyo kumuomba Mungu atuepushie balaa la kufukiwa tukiwa hai.
Kwa kweli sikupata hata lepe la usingizi na hali ilikuwa hivyohivyo kwa watu wengine ambao walikuwa wamekaa hatua chache kutoka nilipokuwa mimi hasa baada ya kuwaambia tumuombe Mungu kwa pamoja bila kujali dini zetu.
Waswahili wanasema saa hazigandi, hivyo nilianza kusikia majogoo yakianza kuwika. Mawazo yalikuwa mengi na nilikuwa nafikiria jinsi ya kujinasua na kifo pamoja na wenzangu.
Nilijua kuwa mfalme au chifu yule alikuwa hatanii, kweli kesho yake atatutupa shimoni kutuua.
Niliwaza tena lile wazo langu la awali la kujifanya mimi ni mtume wa Mungu. Nilijiuliza kimoyomoyo nitamshawishi nini ili aamini kuwa naweza kuwa mtume wa kweli?
Kwa kuwa nilikuwa mwanamazingaombwe niliwaza kwamba nimuombe kumuonesha maajabu fulani ya kimazingaombwe labda yanaweza kusaidia akasadiki kuwa mimi ni mtu wa Mungu na akaacha kutuua.
Niliwaita wenzangu na kuwaambia wazo langu hilo. Wote waliniunga mkono lakini tukasema ni mchezo gani wa mazingaombwe unaoweza kumteka akili akaogopa kutuua?
Mawazo yalikuwa mengi, kuna waliosemsa nimuoneshe jinsi ya kubadili mchanga na kuwa sukari, wapo waliosema nibadili majani kuwa vitambaa na wapo waliosema nigeuze maji kuwa majivu, kwa kuwa michezo yote hiyo naimudu.
Hata hivyo, kuna jamaa mmoja alisema tumuoneshe mchezo wa kumchinja mtu kisha kumfufua. Hilo wazo nililiafiki.Sasa kivumbi kilikuwa je tutapata nafasi ya kuonana tena na huyo mkuu wa pale na kupata nafasi hiyo kabla ya kwenda kutumbukizwa shimoni ili tufe?
Baada ya majadiliano hayo niliangalia saa yangu mishale ilikuwa inaonesha ni saa 10 alfajiri, wote tulikuwa tumejikunyata sehemu moja mithili ya kuku wa kufugwa wanavyojikusanya kwenye taa wakati wa usiku ili wapate joto.
Wote walijua kuwa mkombozi wao katika sakata hilo la kufukiwa kwenye shimo tukiwa hai ni mimi. Swali lililokuwa likigonga kwenye vichwa vyetu ni je, tutapata nafasi ya kumuomba huyo mfalme ili tumuoneshe manjonjo hayo?
Alfajiri hiyo nilisikiliza kwa makini kama nitasikia adhana, lakini sikusikia, hata ilipofika saa kumi na mbili nilisikiliza kama nitasikia kengele ya kanisani ikigongwa, pia nayo sikuisikia.
Nikajua kuwa watu wa pale hawana dini tunazozijua sisi. Yaani hawaujui Uislamu au Ukristo.
“Ndiyo maana hawana ubinadamu,” nilijishtukia nikisema kwa sauti.
“Unazungumza na nani?” alinihoji kijana mmoja.
“Ahh, nimewaza sana na kujishtukia nikisema hivyo, hawa jamaa wanaotushikilia hawana dini.”
“Kwa nini unasema hivyo?” aliniuliza kijana yule.
Nikamweleza sababu kutokana na mawazo yangu na kuunganisha na kutosikia viashiria vya dini tulizozizoea wakati wa alfajiri au asubuhi kama hiyo.
Yule kijana nilipomwambia hivyo hakunijibu badala yake alijikunyata na kuegemea ukuta uliokuwa na baridi kali kutokana na hali ya hewa ya siku hiyo. Kulikuwa na baridi kali na bahati mbaya sana hatukuwa na shuka za kujifunika.
Walioteseka zaidi kwa baridi ni baadhi ya vijana ambao walivaa mafulana maarufu kama ‘kaawoshi’, niliwasikia baadhi yao wakitetemeka na meno yao kugongana. Niliwahurumia sana lakini nadhani waliingiwa na woga zaidi kwa kujua kuwa bado saa chache uhai wetu ukatishwe.
“Kweli. Sasa kumepambazuka, kifo chetu kinakaribia,” nilisema na kuwaangalia wenzangu walioonekana kukata tamaa.“Kaka saa ngapi?”Mmoja wao aliniuliza. Niliangalia saa nikamwambia kuwa ni saa kumi na mbili na robo na tukiangalia nje tuliona mwanga wa jua ukianza kuchomoza.
Haukupita muda mrefu tangu yule kijana aniulize swali kwani alitokea askari ambaye hakuwa yule wa usiku na akaja moja kwa moja kwenye geti letu na kulifungua.
“Wote tokeni nje,” alisema kwa amri. Alionekana ni mnene na mrefu pia alikuwa akionekana kana kwamba ni mcheza kareti kwa sababu niliangalia mikono yake nikaona ina sugu kwenye vidole na pia misuli yake ya kwenye mikono na kifua ilikuwa mikubwa.
Tulitolewa nje na baada ya kutoka niligundua kuwa kumbe kulikuwa na askari wengi na wote walikuwa wakituangalia, walipangwa mistari miwili na sisi tukawekwa kati.
Upande wetu wa kushoto ndipo kulipokuwa na godauni ambalo wasichana walilazwa, nao walitolewa nje na kuamriwa kusimama msitari mmoja kama tulivyokuwa tumesimama.
Wengi wao walikuwa na macho mekundu bila shaka kutokana na kulia usiku kucha kwa sababu ya hofu ya kifo tulichotangaziwa jana yake.
“Nisikilizeni kwa makini. Mimi naitwa Kamanda Ben Mtwanga,” alisema yule askari mwenye miraba minne ambaye nilihisi alikuwa kamanda wao.“Wote tutawapeleka kwa mfalme ili mkaagane naye kabla ya kupelekwa kwenye shimo la kifo ambako mtatupwa humo.
“Mkifika kwa mfalme kila mmoja wenu atapewa nafasi ya kuzungumza na kumwambia mfalme kile alichonacho moyoni na hasa kuhusu maisha yako huko unakotoka.
“Unatakiwa uwe huru kuzungumza na usiwe na wasiwasi kwa sababu hiyo ni nafasi yako ya pekee.
“Kama unataka kusamehewa utamwambia na utatoa sababu nzito ambayo unafikiria inaweza au zinaweza kukutoa katika janga hili zito ambalo adhabu yake ni kupoteza maisha, ukiwa makini unaweza kupona na adhabu hii, kuna mwenye swali?” aliuliza yule kamanda.
“Ndiyo, tunalo,” nikasema.
“Uliza, wewe si ndiye kiongozi wa wahalifu hawa?”
 
SEHEMU YA 08


ILIPOISHIA

“Kila mmoja wenu atapewa nafasi ya kuzungumza na kumwambia mfalme kile alichonacho moyoni.
“Kama unataka kusamehewa utamwambia na utatoa sababu, mnaweza kuiepuka adhabu ya kupoteza maisha iliyopo mbele yenu mkiwa makini kujieleza kwake, kuna mwenye swali?” aliuliza kamanda yule.
“Ndiyo, tunalo,” nikamjibu.
“Uliza, wewe si ndiye kiongozi wa wahalifu hawa?”

SONGA NAYO…

Nauliza, tutakapokutana na mfalme, kila mmoja ataongea kivyake au mimi nitawakilisha wote?”

“Kisheria inatakiwa kila mmoja ajitetee mwenyewe, aeleze matatizo yake ili mfalme aone nani atamsamehe au nani adhabu yake iendelee na sisi huwa tunatekeleza huko kwenye shimo la kifo. Mwingine mwenye swali?”
Kijana mmoja alisimama na kufuta machozi kisha kuuliza: “Kwani tunaweza kutumbukizwa shimoni wote kwa pamoja au mmoja mmoja?”
“Hilo swali lako nikikujibu litakusaidia nini? Uliza maswali ya maana, au hamjanielewa?”
Kimyaa.

Yule kamanda akaendelea: “Nia ya kujieleza ni kupima uzito wa matatizo yenu kwani huwa yanatofautiana. Kwa mfano, msichana anaweza kuwa na ujauzito, akijieleza pale anaweza kusamehewa kwa sababu kisheria mwanamke mjamzito hairuhusiwi kutumbukizwa kwenye shimo la kifo.”
“Kama yule msichana anadanganya?” aliulizwa msichana mwingine.

“Akidanganya atakuwa anajidanganya mwenyewe kwa sababu mimba huwa haitumbukizi tumbo ndani badala yake huwa tumbo linachomoza, hivyo kama atadanganya ni lazima atakuja kujulikana. Umeelewa?”
“Nimeelewa, lakini mtu kama huyo anapewa adhabu gani?”
“Ukijulikana kuwa umemdanganya mfalme, adhabu huwa ni kukatwa kichwa palepale.”
Baada ya kusema hayo niliwaona wasichana wengi wakiinamisha vichwa vyao, bila shaka walitegemea uongo huo kuwaokoa.
Baadaye yule kamanda aliuliza kama kuna mtu mwingine mwenye swali lakini ikaonekana hakukuwa na aliyekuwa na swali pengine watu walikuwa na hofu ya kifo maana dakika zilikuwa zinazidi kusonga mbele.

Msafara ulianza kuelekea kwa mfalme na tulikuwa katika mistari miwili, mmoja wa sisi wavulana na wa pili ulikuwa wa wasichana na wao ulikuwa na watu wasiopungua nane, wetu ulikuwa na watu ishirini na moja.

Safari kuelekea kwa mfalme ilianza kwa mwendo wa taratibu huku tukiongozwa na ngoma iliyokuwa ikipigwa kadiri tulivyokuwa tukipiga hatua na tuliambiwa awali kuwa tufuate mapigo ya ngoma hiyo kubwa ambayo shuleni tulikuwa tukiita mdundo.
Baada ya mwendo wa dakika kumi niliona mbele yangu umati ukiwa umezunguka jukwaa nikatambua kuwa pale ndipo alipo mfalme.

Mawazo yangu yalikuwa mengi kadiri tulivyokuwa tunakaribia umati ule na nikawa najiaminisha kuwa mfalme yupo pale.
Tulipokaribia umati ule, wananchi wenyewe walitupisha njia na baada ya kuacha uwazi nilimuona mfalme akiwa ameshika mkuki wa rangi ya shaba ambao ni ishara ya mamlaka aliyokuwanayo.
Tulisimamishwa mbele yake na ile ngoma iliyokuwa ikipigwa iliacha kuvuma kuashiria tulifika. Tuliambiwa tugeuke kulia ambapo mfalme alikuwa ameketi kwenye kiti chake cha enzi.
Yule Kamanda Ben Mtwanga aliyetuleta pale alimtaarifu mfalme kwamba mbele yake kuna watu ishirini na tisa ambao wamefanya makosa kwenye bustani ya Nangose na wanasubiri amri yake ya kutupwa kwenye shimo la kifo.

Mfalme alisimama na kuanza kusema: “Wananchi wangu kama ilivyo ada kabla ya hawa watu hawajatupwa kwenye shimo la kifo ni lazima niwasikilize utetezi wao wa mwisho wa kwa nini wapunguziwe adhabu. Utetezi huu hufanywa sehemu ya wazi kama hivi.”
“Sawa mkuu. Utaratibu ni kwamba tuanze na kiongozi wao wa msafara Bwana Issa Namakoto,” alisema Kamanda Mtwanga.
“Sawa. Issa Namakoto nenda kasimame pale alipo mfalme ujieleze.”
Nilianza kutetemeka mwili kama vile nina homa kali. Nilikwenda taratibu na kusimama mbele yake, nilihisi nitashindwa kutoa maneno.

“Ehee, adhabu yako ni kutupwa ndani ya shimo la kifo, una utetezi wowote?” Mfalme akaniuliza.
“Ndiyo mfalme mtukufu.”Nilikohoa kidogo ili kuweka sawa sauti yangu, nikaendelea:
“Mimi unayeniona maulana mfalme ni Mtume wa Mungu. Sijui katika nchi hii mnajua maana yake.”
“Hatujui na mimi binafsi sijui.”
“Mtukufu mimi nina uwezo wa kufanya mengi ambayo binadamu hawezi kwa mfano naweza kumchinja mtu kisha nikarudishia kichwa chake kwenye shingo yake na akawa hai tena kama kawaida.”
Baada ya kutamka hayo nilimuona mfalme akiwageukia wasaidizi wake akawauliza:
“Ni ya kweli hayo?”
“Hatujui maulana.”
“Hebu fanya tuone.”
Nilimuita kijana mmoja aitwaye Chambilecho ambaye tulikuwanaye katika msafara wetu na tumekuwa tukifanya naye mchezo huo wa mazingaombwe mara nyingi.
Nilifanya mazingaombwe yangu na watu wote pamoja na mfalme wakapigwa na butwaa nikajua kuwa hawa watu wa sehemu hii hawajawahi kuona wala kusikia mambo hayo.
Baadaye nikawaambia nimemchinja rafiki yangu Chambilecho na sasa namrejeshea uhai wake. Nilifanya vitu vyangu na mara akawa mzima.

Nilimuambia arukeruke ili kuthibitishia umma ule kwamba yu mzima, akafanya hivyo na kuzidi kushangaza watu.
Niliomba yaletwe maji kwenye mitungi, nikafanya mazingaombwe na maji yale yakawa divai tamu, niliwaambia watu wainywe, wakainywa na kuzidi kushangaa huku wengine wakisema hakika huyu ni nabii.

Kama vile hiyo haitoshi, nilimchukua ndege na kumuweka kwenye kopo na wote wakashuhudia nikilipondaponda lile kopo lakini nilipofunua kikapu kilichozibwa juu ili ndege asiruke alikutwa mle akiwa hai. Watu walipigwa na butwaaa na kusema mimi ni nabii kweli na kwamba nikitupwa kwenye shimo la kifo, nchi itatikisika.
Mfalme alisimama akautazama umati uliokuwa ukinishangaa huku wengine wakisema sikuwa mtu wa kawaida.
“Sikilizeni,” yule mfalme akaanza kuhutubia.
“Katika maisha yangu sijaona mambo ya ajabu kama haya.”
Je, Namkoto na wenzake watasalimika kutupwa shimoni?
 
SEHEMU YA 09


Tuliamriwa kusimama na kuanza safari na kuelekea kwenye shimo ambalo limeandaliwa kwa shughuli hiyo.

Yule msichana aliyekuwa mjamzito alikuwa akilia kwa sauti huku akipunga mikono ishara ya kutuaga.

Kilio chake kilifanya hata sisi wanaume tuanze kulia, mimi huwa mgumu sana kulia lakini yowe za yule dada zilinifanya nitokwe na machozi.

Nini kilifuata?



SONGA NAYO…

Dereva Limbende na utingo wake ambao nao walisalimika kutupwa kwenye shimo la kifo, niliwaona wakibubujikwa na machozi kutulilia.

Vijana wenzangu tuliokuwa tumepangwa kwenye mstari wote walishindwa kusema chochote kwa kujua kwamba sasa tunakwenda kufa.

Wasichana tuliohukumiwa nao ambao walikuwa watano wote walikuwa wakilia. Mmoja aliishiwa nguvu kabisa za kutembea tukaamriwa tumbeba.

Kazi hiyo niliifanya mimi nikisaidiwa na kijana Kwiimukaga.

Hata hivyo, kazi ya kumbeba msichana ambaye alizimia wakati tunakwenda kutupwa shimoni ilikuwa ngumu ilibidi kupokezana kwa sababu msichana huyo alikuwa pandikizi la mtu.

Lakini pia kazi hiyo ilikuwa ngumu kwa kuwa tuliishiwa nguvu hasa kwa kuwa usiku uliopita hatukuweza kula chakula kutokana na hofu ya kifo ambacho sasa tunakwenda kukabiliana nacho.

Wakati wa msafara huo, kulikuwa na kikundi cha wapiga ngoma waliokuwa wamezifunga viunoni mwao.

Mwendo kutoka pale kwenye kiwanja cha mikutano hadi kwenye shimo ilichukua saa nzima ni mbali kutoka makazi ya watu na ni kwenye msitu mnene.

Tulipofika pale ajabu ya kwanza tuliyoiona ni kwamba shimo lile ni pango kubwa ambalo sijajua lilitokana na nini lakini lilikuwa na mfuniko mkubwa wa jiwe.

Kwa wale wasoma maandishi ya vitabu vya dini, niwakumbushe kuwa jiwe lile linafanana na lile ambalo lilitumika kufunikia kaburi la Yesu.

Tofauti na zama hizo ambapo jiwe hilo kubwa lilivingirishwa na askari, lile la pale lilitolewa na winji maalum ya kunyanyulia vitu vizito.

Ajabu ya pili ni kwamba kulikuwa na kiti maalum cha chuma ambacho kilikuwa na minyororo ambacho kilikuwa pale, kando kidogo na ile winji.

Nilijiuliza, kiti kile cha chuma, tunauawa kwanza kwa umeme baada ya kukikalia kisha tunatupwa shimoni?

Hilo lilikuwa swali langu kichwani na sikuwa na uwezo wa kupata jibu wakati ule.

Ajabu ya tatu ni kwamba karibu na kile kiti kulikuwa na askari wanne ‘walioshiba’ ambao nilikuwa sijajua walikuwa pale kwa kazi gani.

Baadaye aliitwa kijana wa kwanza aanze kutekeleza adhabu yetu, alichukuliwa na askari walioshiba na kukalishwa kwenye kile kitu cha chuma.

Baadaye alinyanyuliwa huku akimwaga machozi na kuwekwa kwenye mlango wa lile pango.

Alishushwa taratibu kwa ile winji. Ilielekea kuwa shimo lile ni refu sana kwa sababu minyororo iliyokuwa imeshikilia kiti ilikuwa mirefu na iliisha yote.

Baadaye nilishuhudia ile minyororo minne ikirudi ardhini na kipande kimoja kimoja cha kile kiti cha chuma kilichoshuka chini na kijana wetu.

Zoezi hilo liliendelea mpaka wote wakaisha nami nikawa mtu wa mwisho kushushwa chini ya shimo.

“Wewe Issa Namakoto tumekufanya kuwa wa mwisho kushushwa kwenye hili shimo la kifo ili utoe neno lako la mwisho kwetu,” alisema Kamanda Ben Mtwanga aliyeoongoza zoezi hilo la kututumbukiza shimoni.

Nilifikiria haraka japokuwa akili ilikuwa siyo yangu lakini niliamua kuwatisha tu.

“Mimi naitwa Namakoto au ukienda kijijini kwetu huwa naitwa Maharage ya Zambia. Nawaahidi kwamba sisi hatutakufa na tutakuja kutokea tena katika nchi hii. Mtashangaa lakini hiyo ndiyo ahadi yangu.”

Baada ya kusema hayo niliona watu waliokuwa pale wakishangazwa na kile nilichokisema.

“Anasemaje? Watakuja tena? Wangapi wametumbukizwa kwenye shimo hilo na hawajawahi kurudi duniani?” nilisikia mtu mmoja akiuliza.

Hapohapo nikajua kuwa kumbe lile shimo limewahi kutumika kufunika watu wengine tofauti na tulivyokuwa tukidhani kwamba tungefukiwa kwenye shimo kwa mchanga.

Mimi tofauti na wenzangu ambao walikuwa wakiishiwa nguvu na kubebwa kuketishwa kwenye kile kiti cha chuma, nilikwenda na kukaa mwenyewe.

“Kwa kawaida kila anayetupwa ndani ya chimo hili hupewa chakula cha siku saba na maji ili atumie muda huo kumuomba Mola wake kabla ya kifo, hivyo, baada ya wewe kutiwa shimoni kuna chakula na maji tutawaletea, muwe tayari kuvipokea,” alisema Kamanda Mtwanga.

Sikuwa na la kusema zaidi ya kumuitikia “Sawa.” Winji iliwashwa na nikaanza kuteremshwa shimoni na kwa kuwa nilikuwa mtu wa mwisho, ngoma ambazo zilitulia wakati wa zoezi zima, zikaanza kupigwa tena.

Nilifika chini ya shimo na kukuta wenzangu wakiwa wamejikunyata huku wengi wakilia na baadhi yao wakiwa wamezimia.

Kwa kuwa jiwe lilikuwa halijafunikwa, tuliweza kuonana vizuri kwa sababu mwanga ulikuwa ukiingia.

Niliweza kuona kando ya pale tulipokuwa tumeketi kuna mifupa ya watu, hiyo iliashiria kuwa watu waliotupwa ndani ya shimo hilo walifariki dunia na kwamba siyo utani.

Baada ya dakika kadhaa niliona kile kiti kikishuka, kilikuwa na maboksi kumi ya maji. Nilishusha, yakaletwa tena mara saba baadaye ililetwa mikate mingi, sikuwa na sababu ya kujua ilikuwa mingapi kwa sababu nilijua walaji watakosekana.

Wasichana ambao walikuwa wakilia tukiwa mle shimoni waliruka ghafla:“ Nini?” nilihoji.

“Kuna panya,” alijibu msichana mmoja.

Akili yangu ilifanya kazi haraka na kujiuliza, ‘huyu panya anaishije kwenye shimo hilo refu? Je, inawezekana hutoka nje kupitia lile tundu lililotumika kutushushia sisi humu?”

Jibu sikupata kwa sababu panya mwenyewe hakuwepo aliingia shimoni lakini hata kama angekuwepo nisingeweza kumuuliza kwa kuwa ni panya.

Nilisimama na kwenda kuangalia lile tundu aliloingia panya, akili zikanituma kwamba utafiti wangu uanzie pale.

Je, nini kiliendelea?
 
SEHEMU YA 10



Akili yangu ilifanya kazi haraka na kujiuliza, ‘huyu panya anaishije kwenye shimo hilo refu? Je, inawezekana hutoka nje kupitia lile tundu lililotumika kutushushia sisi humu?”
Jibu sikupata kwa sababu panya mwenyewe hayupo kaingia shimoni lakini hata kama angekuwepo nisingeweza kumuuliza kwa kuwa ni panya.
Nilisimama na kwenda kuangalia lile tundu aliloingia panya, akili zikanituma kwamba utafiti wangu uanzie pale.

SASA ENDELEA:
Nilisimama kwenye lile tundu kwa dakika tano hivi, wenzangu wakawa wananiangalia wasijue nilikuwa nawaza nini.

“Mbona kaka Namakoto unaangalia tundu la panya kisha huseni lolote?” alinihoji Kwiimuka.
“Nadhani wote au baadhi yenu mmemuona panya hapa.”
“Ndiyoo,” waliitikia baadhi ya vijana niliotupwa nao kwenye shimo lile la kifo.
“Nani ana wazo kuhusu panya huyu?”
Kimyaa. Ukimya wao ulinifanya nigundue kuwa hakuna mtu mwenye mawazo, walimuona kama walivyokuwa wanamuona tukiwa nje ya pango lile.
“Hamuoni kuwa panya huyu anaweza kutuokoa?”
“Kivipi?” aliuliza tena Kwiimuka.
“Huyu panya kwa mawazo yangu naamini anatoka nje ya shimo hili na inawezekana huwa anakwenda kujitafutia chakula nje ya pango hili.”
Baada ya kusema hayo kuna baadhi ya wenzangu walikasirika, bila shaka waliona wazo langu ni la kipuuzi na nawapotezea muda.
Lakini nilijiuliza kupoteza muda ili wafanye nini kwa sababu sikuona hata mmoja ambaye alikuwa na wazo lolote la kuweza kujiokoa.
“Sasa kaka Namakoto unafikiri panya huyu kachimba shimo hadi bustani ya Nangose?”
Kabla sijajibu mwingine akadakia:
“Sasa hata kama huyu panya kachimba shimo kutoka bustani ya Nangose, sisi tunaweza kupita katika tundu lake?”
Huyu wa swali la pili nilimuona kama alitaka kuelekea kule nilipokuwa nawaza, lakini akashindwa kufikiri zaidi.
“Niwaambieni jambo?” nilianza kuongea nao, nikanyamaza kidogo ili kumeza mate.
“Huyu panya inawezekana ni Mungu ameamua kutuonesha ili kutuokoa, mnasemaje?”
“Atatuokoaje?” aliuliza msichana mmoja.
“Sikiliza. Ni lazima tutumie mifupa ya watu waliotangulia waliotupwa humu ili kujinasua. Wazo langu ni kwamba tuchimbue kufuata njia hii ya panya. Tuchimbe taratibu na kwa bidii naamini tutatoka nje ya pango hili. Kuna mwenye swali?”
Wote nikawaona wanakunjuka sura zao na kuonesha nyuso za matumaini.
“Ni wazo zuri na hiyo kazi tuianze sasa hivi,” alichombeza kijana mmoja aliyekwenda moja kwa moja kuchukua mfupa wa maiti na kuja pale kwenye shimo la panya.
Kazi ya kuchimbua haikuwa ngumu sana kwa sababu udongo ulikuwa tifutifu na hali hiyo ilitushangaza.
“Hapa inavyoelekea shimo hili lilikuwa likitumika zamani kwa kazi fulani na hii ilikuwa njia ya watu kufika shimoni,” nilisema.
“Lakini sasa kwa nini walifukia?” mwingine alihoji.
“Huwezi kujua labda walikuwa na sababu maalum, labda za kivita enzi hizo. Inawezekana walikuwa wakijificha watu hapa wakiona maadui enzi hizo za ujima,” akadakia kijana mwingine.
“Msifurahie jamani, huwezi kujua, panya anaweza kupita katikati ya miamba iliyoungana, hivyo, tutafurahi kama tutatoboa juu ya ardhi,” nilisema na baada ya kutamka hivyo nyuso za watu niliona zimekunjamana.
“Sisemi hivyo ili kuwakatisha tamaa, la hasha. Nataka tuzidi kumuomba Mungu ili tusikutane na mwamba ambao utatuzuia kuendelea na kuchimba njia,” niliona niwape moyo.
Kazi ilikuwa ngumu kwa sababu ilikuwa ni kufa na kupona. Kwamba tukifanikiwa kutoboa ardhi itakuwa ndiyo kupona kwetu na tusipofanikiwa itakuwa ndiyo kifo chetu.
Kubwa kuliko yote ni kwamba nilitaka tufanye kazi kwa bidii kabla ya chakula tulichopewa hakijaisha.
Siyo chakula tu, bali hata maji tulipewa kidogo ili tufe haraka na kwa kazi nzito tuliyokuwa tukifanya huku tukivuja jasho, ilikuwa ni hatari sana kama tungeishiwa maji.
Ni kwamba kuishiwa maji maana yake tungeshindwa kazi ya kuchimba mtaro wa kutuwezesha kutoka ndani ya lile shimo la kifo.
Tatizo lingine ambalo tulikumbana nalo ndani ya shimo lile ni vitendea kazi. Ile mifupa ambayo tulikuwa tukiitumia kuchimbulia ardhi ilikuwa ikilika.
Hilo lilinitia hofu sana na nilipoichunguza baadhi ya mifupa niligundua kuwa ni ya watu wa zamani sana hivyo haikuwa na uwezo wa kuhimili ardhi ambayo licha ya baadhi ya sehemu kuwa tifutifu, kuna sehemu zilikuwa ngumu.
Changamoto nyingine ni baadhi ya vijana kuchubuka viganja, yaani kuota mafindofindo kutokana na kutozoea kazi ngumu kama ile tuliyokuwa tukiifanya kwa vifaa duni, mifupa ya watu.
Lakini changamoto nyingine ni vifaa vya kusombea mchanga kwani tulikuwa tumeshachimba umbali wa hatua ishirini za mtu mzima.
Hatukuwa na makarai au ndoo badala yake tukawa tunatumia mafuvu ya watu ambayo kwa kweli yalitusaidia.
Wakati naanza kuwahimiza kutumia mavufu hayo baadhi ya wasichana walikwa waoga.
“Mnaogopa nini? Haya mafuvu hayadhuru, tumieni kusombea mchanga,” niliwaambia.
“Lakini mimi naogopa sana,” alisema msichana mmoja. Ni wazi kwamba wasichana karibu wote tuliokuwa nao ndani ya shimo lile la kifo ilikuwa mara yao ya kwanza kuona mifupa ya watu waliokufa.
Baada ya kuwapa somo kuhusu mifupa ile, wengi walipata ujasiri na wakawa wanatumia kama vitendea kazi. Niliwaambia wazi kwamba bila kufanya hivyo, tutafia kwenye shimo hilo kama walivyokuwa hao ambao mifupa yao sasa tunaitumia kama vifaa vya kuchimbia njia yetu ya kujinasua.
Je, watafanikiwa kujiokoa?
 
SEHEMU YA 11


ILIPOISHIA

…tutafia kwenye shimo hilo kama walivyokuwa hao ambao mifupa yao sasa tunaitumia kama vifaa vya kuchimbia njia yetu ya kujinasua.

SASA ENDELEA
Mwongozo wetu kama nilivyosema awali ni njia ya panya ambayo kwa bahati nzuri ilikuwa siyo ya kupindapinda.

Kazi hiyo tuliifanya kwa siku mbili mfululizo, mchana.
Ilikuwa kazi kubwa kwa sababu kwenye tundu tulilokuwa tunalichimba kulikuwa na giza na joto sana.
“Inabidi tuingie kwa zamu kwenye hili tundu tunalolichimba,” nilishauri.
Kilichosaidia ni kwamba ndani ya shimo hilo la kifo kulikuwa na upana wa kutosha na tulitumia nafasi fulani kulundika mchanga unaotolewa kwenye tundu.
Hata hivyo, kuliongezeka joto ndani ya shimo kutokana na kupungua nafasi baada ya sehemu nyingi kumezwa na mchanga uliokuwa ukisomwa kwa mafuvu ya watu.
Changamoto nyingine ambayo tulikumbana nayo ni ya kuuguliwa kwa mwenzetu mmoja wa kike.
“Kaka mimi najisikia kuumwa,” alisema msichana huyo.
“Unaumwa nini?”
“Naumwa sana na tumbo na mwili wote najisikia homa,” alisema.
Nilikwenda kumgusa kwa kutumia kiganja change nikakuta kweli ana homa kali. Niliogopa japokuwa sikutaka wenzangu waone kuwa nina woga.
Woga huo uliniingia kwa sababu kuu mbili. Moja, nilihofu kwamba kama ni malaria anaweza kufa.
Pili nilijua kwamba akifa tukiwa kwenye pango lile ambalo lilikuwa na joto kali, ataharibika, hali itakayosababisha kuwe na harufu kali na kwa vyovyote watu wataishiwa nguvu ya kufanya kazi, hivyo wote kufia kwenye shimo hilo la kifo.
“Jamani huyu anayeumwa akandwe kwa maji, haya wasichana fanyeni kazi hiyo,” niliamuru.
Bila ajizi wasichana wakawa wanamkanda mwenzo mgonjwa kwa kutumia khanga zao.
“Angalieni, mtumie maji kwa uangalifu kwa sababu hatuna maji zaidi ya hayo,” niliwaonya.
Nilihesabau chupa za maji ambayo yalibaki zilikuwa kama kumi na tano tu. Niliogopa sana.
Mikate tuliyopewa na wale watu ili ikiisha tufe kwa njaa ilikuwa mingi kuliko maji.
Lakini nilijua kuwa kama maji yatakwisha hata kama tuna mikate mia moja, tutailaje? Kwa vyovyote tutashindwa.
Wakati tunajitahidi kuchimba mtaro huo ili tuweze kutoka nje kijana mmoja aliyekuwa ndani aliniita:
“Kaka Namakoto, kaka namakoto njoo upesiii!”
Nikajikusanya kutoka katika kundi la yule msichana mgonjwa na kuinama ili kwenda ndani ya tundu ilikotokea sauti.
“Kaka Namakoto njooo,” alisema kijana mwingine, staili ya uitaji wao ilinitia wasiwasi na kunifanya nijiulize mara mbili, hao wameona mwanga au kitu gani kimewafanya wapagawe!
Nilikuwa na kibiriti mkononi, nikakiwasha baada ya kuwafikia.
“Nini?”
“Kuna majimaji hapa,” mmoja alisema.
Niliwasha kibiriti na kugundua kuwa kweli kulikuwa na unyevunyevu.
Tulizidi kuchimba sasa badala ya kutia mchanga kwenye mafuvu ya kichwa tukawa tunatia tope yaani mchanganyiko wa maji na udongo.
Wakati wenzangu walikuwa wakifurahia hali ile, akili yangu haikukaa sawa, nilihofu kwamba kutokana na majimaji yale tunaweza kufunikwa na udongo.
Vijana walikuwa wakiendelea kuchimbua licha ya mikono yao kuwa na malengelenge kutokana na kutozoea kazi za sulubu walizokuwa wakifanya.
“Ngojeni kidogo, kuna kitu nimewaza,” nilisema.
“Umewaza nini tena? Tujitahidi jamani tunaweza kuibuka juu ya ardhi,” alisema Kwimuka.
“Hapana. Akili hainitumi kuendelea mbele.”
“He, kaka Namakoto ina maana tuache, kisha iweje?” aliuliza tena Kwimuka.
“Simahanishi kwamba tuache kazi ya kuchimba hapana.”
“Ila?”
“Tumchimbe sasa kuelekea juu, si mnaona jinsi kulivyojaa tope hapa chini?”
“Ndiyo.”
“Mnajua kwa nini nasema hivyo?”
“Hatujui.”
“Tuelekee juu kwa sababu tukiendelea mbele kuna hatari ya hili tundu kutufunika.”
“Kwa hiyo tufanye nini?”
“Nimeshasema tuchimbe kwenda juu ili kama kutokeza basi tutokeze juu ya ardhi.”
“Kuna mwenye wazo zaidi ya langu?”
“Hakuna,” alijibu haraka haraka Kwimuka.
“Hapana, haya mambo siyo ya mtu mmoja, inafaa kila mmoja akatafakari kabla ya kujibu,” nikawapa wosia.
Baada ya kukaa kwa sekunde karibu kumi bila kupata jibu mmbadala, tukaanza kazi ya kuchimba kwenda juu.
Kasi hiyo ilikuwa nyepesi kidogo kwa sababu kila ukichimbua ardhi ilikuwa inaanguka kutokana na kulowana na maji.
Usiku ulipoingia tulitengeneza kama kisima ili kukinga maji ambayo yangeweza kutusaidia ikiwa tutaishiwa kabisa maji.
Kulipopambazuka nilikwenda kuona kama maji yamepatikana, nikawasha kibiriti na kukuta yamejaa ya yamejikusanya kwenye shimo tulilolitengeneza maalum kwa ajili ya kazi hiyo.
Niliwaambia wenzangu wachukua chupa zote tupu na wajaze maji yale ili yatusaidie siku zijazo.
Wakati huo hali ya mgonjwa wetu ilizidi kuwa mbaya na hatukuwa na dawa yoyote ya kumpa sipokuwa maji.
Wakati natia maji kwenye chumba niliona mzizi fulani ambayo ilinipa ishara kwamba tunakaribia kutoboa juu ya ardhi.
Rangi ya mzizi hiyo ilinikumbusha zamani wakati nikiwa na marehemu babu yangu ambaye alikuwa na kawaida ya kunionesha mizizi mbalimbali ambayo alikuwa akiitumia kutibu watu.
“Huu mzizi kama wa mti mmoja unaitwa Nrokochi. Babu alikuwa akiutumia kutibu maradhi mbalimbali.”
“Una uhakika?” alinihoji kijana mmoja.
“Ngoja kwanza tuufuatilie.” Tulichimba kuufuata na baadaye kuukata.
Je, watafanikiwa kujiokoa?
 
SEHEMU YA 12


Tulifanikiwa kutoka kwenye shimo la kifo salama japokuwa msichana mmoja alikuwa mgonjwa. Tulitumia siku saba kuchimba tundu la kututoa shimoni.

Niliwaacha wenzangu pale kwenye pango na kwenda kwa mkuu wa nchi ile aliyeamuru tutupwe shimoni tufe, walinzi waliponiona walinishangaa na kuingiwa na woga lakini mkuu mwenyewe pia aliponiona alipigwa na butwaa. Nilimsalimia kwa heshima zote.

“Kwani wewe ni Issa Namakoto au ni macho yangu?” aliuliza.
“Ni mimi mtukufu. Kama nilivyokueleza, mimi ni mtume wa Mungu na ndiye aliyenitoa. Kesho nitawaleta wote uliowatupa shimoni.”
Nilijifanya natoweka, nikaenda kwa wenzangu, tulilala na kesho yake tukafika kwa kiongozi yule. Tulipikiwa vyakula vya kila aina, tukala kisha wote tulirudishwa katika Bustani ya Nangose, tulikuta basi letu, tulipanda na kurudi Dar na hivyo ndivyo nilivyoteseka kwenye mianzi ya kichawi Nangose. Ilikuwa safari ya hatari!
Mwisho.

Wiki iliyopita nilipata simu na sms nyingi kutoka kwa wasomaji wangu wakihoji kwa nini hadithi ni fupi sana, niwaombe radhi kwamba tumeifupisha kutokana na sababu za kiufundi.
 
3 Reactions
Reply
Back
Top Bottom