Siku ya wanawake duniani ina maana gani? Chimbuko, Malengo na Kumbukumbu zisizosahaulika

Mema Tanzania

Member
Feb 23, 2020
66
65
#TatuZaJumatatu

SIKU YA WANAWAKE DUNIANI INA MAANA GANI

| CHIMBUKO LAKE

Mwaka 1908 kulitokea mtafaruku na mjadala mkubwa kuhusiana na wanawake ikumbukwe miaka hiyo kulikuwa na unyanyasaji na kutokutambulika kwa haki za wanawake hali iliyopekea wanawake kuanza kupaza sauti na kuendesha kampeni ili kuleta mabadiliko. Ni mwaka 1908 ambapo wanawake 15,000 waliandamana jijini New York wakitaka kupunguzwa kwa masaa ya kazi, malipo mazuri na haki ya kupiga kura. Mwaka 1909 ikiambatana na azimio la Chama cha Kijamaa cha Amerika (Socialist Party of America) walipitisha Siku ya Kitaifa ya Wanawake (National Women's Day) nchini Marekani tarehe 28 February. Wanawake waliendelea sherehekea siku hii mpaka siku ya mwisho ya Jumapili ya February mwaka 1913, mwaka 1910 mkutano wa pili wa kimataifa kwa wanawake wafanyakazi (International Conference of Working Women) ulifanyika mjini Copenhagen, Denmark.

Katika mkutano huo, mwanamke aitwae Clara Zetkin ambae alikuwa kiongozi wa Women Office kwa chama cha Social Democratic nchini Ujerumani aliwasilisha wazo la Siku ya Kimataifa ya Wanawake Duniani. Pendekezo lake kuu ilikuwa ni kila nchi duniani kila mwaka washerehekee siku moja ili kutambua mahitaji ya wanawake. Ni mkutano uliohudhuriwa na wanawake 100 kutoka mataifa 17 wakiwasilisha vyama vya wafanyakazi, vya ushirika na vya kijamaa. Bunge la Finland ambalo wakati lilikuwa na wanawake watatu, walipitisha wazo la Clara ambalo lilichangia kuanzishwa kwa siku hii. Austria, Ujerumani, Denmark na Switzerland 'Uswissi' ni nchi za mwanzo kusheherekea siku ya wanawake duniani tarehe 18 ya mwezi wa 3 mwaka 1911.

Siku ya wanawake ilianza kupata umaarufu ukanda wa magharibi baada ya mwaka 1977 kufuatia azimio la baraza la umoja wa mataifa ya kuwa machi 8 ni siku ya umoja wa mataifa ya haki za wanawake na amani duniani. Kwa sasa zaidi ya nchi 100 zinaadhimisha siku ya wanawake duniani na baadhi ya nchi wameitangaza kama siku rasmi ya mapumziko.

IWD Women1.png


| MALENGO YA SIKU HII

Malengo ya siku hii ni kuonesha mapenzi na shukrani kwa wanawake. Pia malengo ya siku hii ni kutambua changamoto wanazopitia wanawake maeneo tofauti duniani na kuzitafutia uvumbuzi.

Tangu tumeanza azimisha siku hii unadhani dunia imepiga hatua kiasi katika kuwezesha haki za wanawake duniani? Tupia maoni yako!

| KAULI MBIU YA MWAKA HUU

Mwaka huu kauli mbiu ni #EachforEqual ikiwa na lengo la kulingania kizazi chenye usawa kwa kutambua haki za wanawake.

| MKUTANO WA BEIJING NA HAKI ZA WANAWAKE

Tarehe 8 March 1995, uliitishwa Mkutano wa nne wa wanawake duniani (4th World Conference on Women) ukiwa na kauli mbiu ya vitendo kwa usawa, maendeleo na amani. Mkutano ulifanyika katika mji wa Beijing, China na ndiyo chanzo cha kuitwa Beijing Conference. Mama Gertrude Mongella kutoka Tanzania alipata heshima ya kuongoza kikao hiki kama Katibu mkuu wa mkutano. Mkutano uliambatana na hotuba kutoka kutoka kwa wanawake wenye ushawishi kama Hilary Clinton na Mother Teresa ambaye sehemu ya hotuba yake alinukuliwa akipinga suala la utoaji mimba ambapo baadhi ya mataifa walianza kuruhusu sheria ya utoaji mimba.

| UMUHIMU WA BEIJING CONFERENCE KATIKA HAKI ZA WANAWAKE

Mkutano wa Beijing unatazamiwa km moja ya mikutano mikubwa iliyoweza amsha hali ya wanawake kudai haki zao za msingi. Hotuba ya Bi Hilary Clinton kwa kiasi kikubwa iliweza kushawishi wanawake kuendesha harakati za kupigania haki zao. Maaizimio ya mkutano huo yalipekea kubadilika kwa hali ya wanawake katika nyanja tofauti ikiwemo umaskini, elimu, afya, ukatili, siasa na maamuzi. Mama Gertrude Mongella baada ya mkutano wa Beijing ameendelea kuwa alama kubwa ya kupigania haki za wanawake na amekuwa ni mfano wa kuigwa kwa wanawake na mabinti wengi ndani na nje ya Tanzania. Mwaka huu dunia itaadhimisha miaka 25 ya Beijing Conference na kuangazia namna gani hali ya wanawake imebadilika tangu wakati huo.

| WANAWAKE 5 NA KUMBUKUMBU ZAO ZISIZOSAHAULIKA

IWD Women4.png


1. Gertrude Mongella - Ni mwanasiasa, mwalimu, mwanaharakati, mke na mama wa watoto wa nne aliyezaliwa kisiwa Cha Ukerewe mwaka 1945.
Alizaliwa katika kipindi ambacho wanawake walikuwa wakibaguliwa katika jamii ikiwemo kupata elimu, kuongea mbele ya wanaume, kukatazwa kula baadhi ya vyakula na masuala kadha wa kadha. Licha ya changamoto hizo alipata ushirikiano mkubwa wa wazazi wake ambao walifanikisha ndoto yake ya kufika mpaka chuo kikuu. Mwaka 1995 aliongoza mkutano wa nne wa dunia kuhusu wanawake maarufu Beijing Conference.

Ni Gertrude Mongella pia alikuwa rais wa kwanza wa bunge la afrika lililoundwa mwaka 2004. Ameshika nyifa nyingi na kwa wakati tofauti za kichama na serikali ndani na nje ya Tanzania ikiwemo Msaidizi wa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, waziri wa ardhi, utalii na mali asili na mjumbe wa bodi tofauti tofauti. Mama Gertrude Mongella ni moja ya hazina kubwa kama taifa linajivunia kuwa nae kutokana na uzoefu wake mkubwa na namna alivyoweza kupenyeza katika mifumo dume ya wakati huo na kufanikiwa kushika wadhifa tofauti. Ni mfano wa kuigwa kwa wanawake wengi Tanzania na nje ya Tanzania ambaye ni kichocheo cha wanawake wengi kuthubutu kushika hatamu.

IWD Women5.png


2. Bi Kidude - Si jina geni masikioni mwa watu, alizaliwa miaka ya 1910 na kufariki 17 April 2013. Bi Kidude hakuwa anafahamu tarehe yake ya kuzaliwa isipokuwa alichojua alizaliwa wakati rupia ikitumika kama fedha. Ni mzaliwa wa Zanzibar na aliyekuwa mkongwe wa muziki wa taarabu ya kale. Aina yake ya sauti na namna alivyokuwa akiimba alikonga nyoyo za wapenda muziki duniani kote. Zanzibar ni moja ya visiwa vyenye vivutio vingi vya utalii na wakati wa uhai wake Bi Kidude alikuwa ni kivutio kikubwa kwa wageni kutoka nje na hasa waliofika kumshuhudia katika matamasha ya Sauti za Busara.

Alianza muziki akiwa na miaka kumi na alijifunza toka kwa Sitti Binti Saad. Alipokuwa na miaka 13 alitorekea Tanganyika baada ya kulazimishwa kuolewa, japo aliolewa alipokuwa kigoli lakini ndoa yake ilivunjika baada ya kukimbia manyanyaso na kutorokea kaskazini mwa Misri miaka ya 1930 ambapo ndipo nyota yake ya muziki ilianza kung'ara. Mbali ya muziki, pia alikuwa ni mfanyabiashara wa hina na wanja. Enzi za uhai wake alivunja miiko mingi iliyokuwa ikiwabana wanawake wa kizanzibari ambao walikuwa wakifuata tamaduni za kiarabu kama mavazi ambapo alihusudu kuvaa mavazi yanye kuwasilisha uafrika. Alikuwa na upeo mkubwa na mwerevu sana wa mambo ndiyo maana vitendo vya ukatili wa kijinsia alianza vipinga mapema. Alifanya matamasha makubwa katika mataifa mengi duniani ikiwemo Ulaya na Amerika, moja ya vibao vyake motomoto ni cha Ya Laiti kilichorudiwa na mwanamuziki wa miondoko ya Hip Hop, Mwana FA na alishinda tuzo nyingi ikiwemo ya WOMAX.

IWD Women6.png


3. Harriet Tubman - Alizaliwa mwaka 1822 na kufariki march 1913. Ni raia wa Marekani ambaye alisifika kwa kupambana kuondoa utumwa kwa watu weusi. Kuanzia karne ya 15 waafrika wengi walipelekwa Amerika kufanya kazi katika mashamba na viwanda kama watumwa. Alizaliwa katika utumwa mpaka baadae alipotoroka katika utumwa na kuendesha harakati 13 zilizosaidia kukomboa watumwa takribani 70 ikiwemo marafiki na familia yake kwa kutumia wa wanaharakati wa kuondoa utumwa na nyumba salama zilizo fahamika kama Underground Road. Akiwa mtoto alipata jeraha kubwa kichwani baada ya kumpiga kwa bahati mbaya na chuma kizito kilichorushwa na bwana wa watumwa kuelekezwa kwa mtumwa mwingine. Baada ya jeraha Harriet alianza pata hisia za maono na ndoto za kupigania haki za watu weusi.

Mwaka 1849 alitoroka Philadephia kuelekea Maryland kuikomboa familia yake kutoka utumwani. Alifahamika kama Moses sababu misafara yake ya watu waliokombolewa kutoka utumwani ilikuwa ni mwendo wa usiri na usiku. Mpaka inapitishwa sheria ya kuondoa utumwa mwaka 1850 alikuwa amekomboa zaidi ya watumwa 700. Ulimwengu mzima unamtambua kama ni alama ya ushawishi, kutokata tamaa na uhuru. Mwaka 2016 Marekani waliweka sura yake katika pesa yao ya dola 20. Zimetengenezwa riwaya na hadithi nyingi zenye kuelezea maisha yake ikiwemo filamu kama A Woman Called Moses.

IWD Women7.png


4. Malala Yousafzai- Ni binti wa miaka 22 kutoka taifa la Pakistani. Ni mwanaharakati wa haki ya elimu kwa wanawake na mshindi wa tuzo ya Nobel. Eneo analotoka Swat Valley, Khyber Pakhtunkwa linatawaliwa na wana mgambo wa Taliban ambao huzuia wanawake kwenda shule. Wakati akiwa na miaka 12 tu alianza harakati kwa kuandika katika blogu akielezea namna utawala wa Taliban unavyokandamiza haki za mtoto wa kike kupata elimu. Maandiko yake yalianza pata umaarufu kupitia vyombi vya habari vya kimataifa. Kitendo chake cha kudai haki za wanawake kupata elimu ilipelekea mwaka 2012 kushambuliwa na risasi pamoja na marafiki zake wawili, tukio lake la kushambuliwa lilimpa umaarufu ulimwenguni kote na hata alipopona aliamua kuendeleza harakati za kupigania haki za mwanamke katika elimu ulimwenguni kote.

IWD Women8.png


5. Alaa Salah - Katika ulimwengu wa mataifa ya kiarabu wanawake hawajihusishi sana katika mambo ya kisiasa. Alaa Salah aliyezaliwa mwaka 1997 ni binti mwanafunzi aliyechochea mapinduzi ya kupinga serikali ya Sudan. Alipata umaarufu duniani baada ya picha yake iliyochukuliwa na Lana Haroun kusambaa April 2019 ikimuonyesha kasimama juu ya gari, mbele ya halaiki ya wanaume wengi akiwasisitiza kuendeleza maandamano ya kuipinga serikali. Baada ya mapinduzi, mwezi October 2019 katika kikao cha baraza la usalama la umoja wa mataifa Salah alisisitiza juu ya serikali ya mpito itakayojumuisha uwiano sawa wa kijinsia katika madaraka. Salah anatambulika kama kielelezo kwa wanawake wengine kuwa mstari wa mbele katika kuleta mabadiliko ya kijamii na kisiasa pasipo kujali umezungukwa na mfumo wa jinsia gani.

Tupate tangazo kutoka studio!

IWD Women9.png


Margret Thatcher anasema "If you want something said, ask a man, if you want something done ask a woman"

#IWD2020 #EachforEqual


Tangu tumeanza azimisha siku hii unadhani dunia imepiga hatua kiasi katika kuwezesha haki za wanawake duniani? Tupia maoni yako!

Waweza kutufuata katika tovuti na mitandao yetu:
- Instagram, Medium na Twitter ni @mema_tanzania pia Facebook Mema Tanzania #ExperienceTheChange #IshiKijanja
 
Ninachokijua kwa wanawake waTanzania bado sana kuifikia hamsini kwa hamsini.

Mfano halisi hata hapa JamiiForums nadra sana kukuta michango ya wanawake kwenye majukwaa ya SIASA jamiiintelligence international news ...wao wako MMU na chit chat

Mimi naona hili suala la hamsini kwa hamsini lisitupotezee muda huku Tanzania hawajo tayari
 
Ninachokijua kwa wanawake waTanzania bado sana kuifikia hamsini kwa hamsini.mfano halisi hata hapa jamiiforums nadra sana kukuta michango ya wanawake kwenye majukwaa ya SIASA jamiiintelligence international news ...wao wako MMU na chit chat

Mimi naona hili suala la hamsini kwa hamsini lisitupotezee muda huku Tanzania hawajo tayari
Unajuaje kama hao wanaochangia kwenye majukwaa hayo unayoona wewe bora kama sio wanawake
 
Kwako wanawake wakiwa majukwaa hayo Unadhani hiyo hamsini kwa hamsini itapatikana
Moja ya kufikia 50/50 ni pamoja na mwanamke kujitambua. Kujitambua kwa mwanamke ni pamoja na kuyatimiza majukumu na sio kuwaza ngono tu, halkadhalika kushikiriki kikamilifu katika shughuli za kulijenga taifa kiuchumi na kijamii. Taifa halijengwi na ngono "Hii ni case ya MMU na Chitchat".
 
Moja ya kufikia 50/50 ni pamoja na mwanamke kujitambua. Kujitambua kwa mwanamke ni pamoja na kuyatimiza majukumu na sio kuwaza ngono tu, halkadhalika kushikiriki kikamilifu katika shughuli za kulijenga taifa kiuchumi na kijamii. Taifa halijengwi na ngono "Hii ni case ya MMU na Chitchat".
Majukumu ya mwanamke ni yapi kwa mfano hebu tuelimishe?!

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Back
Top Bottom