Siku Fidel Castro alipofoka akimlaani Abdelaziz Bouteflika

Rubawa

JF-Expert Member
Dec 25, 2015
2,055
3,239
Siku Fidel Castro alipofoka akimlaani Abdelaziz Bouteflika

Na Ahmed Rajab

ABDELAZIZ Bouteflika ni jina ambalo baadhi yetu, wa umri fulani, tumekulia nalo utotoni na tunaendelea kulisikia hadi uzeeni. Zamani lilikuwa jina lililokuwa na heshima fulani. Leo ni jina la mtu anayeadhirika.

Mamilioni ya wananchi wa Algeria, wakiongozwa na vijana, wamemkaa kooni wanamtaka ang’atuke madarakani.

Tulizoea kulisikia jina la Bouteflika tangu alipokuwa waziri wa mambo ya nje wa Algeria (1963-1979). Aliteuliwa kwanza kuishika wizara hiyo alipokuwa na umri wa miaka 26, akiwa waziri kijana kushinda wote wengine duniani kushika wadhifa kama huo.

Enzi hizo kulikuwako katika nchi nyingine mawaziri wa mambo ya nje waliokuwa pia wakivuma kwa muda mrefu. Mifano inayonijia ni ya Adam Malik aliyekuwa waziri wa mambo ya nje wa Indonesia (1966-1977) na Andrei Gromyko aliyeganda kwenye wizara ya mambo ya nje ya Muungano wa Sovieti kwa muda wa miaka 28 (1957-1985).

Bouteflika alijiingiza katika harakati za ukombozi akiwa kijana mbichi wa miaka 19 alipojiunga na jeshi la ukombozi la Armée de libération nationale (ALN), lililokuwa jeshi la chama cha ukombozi wa taifa - Front de libération nationale (FLN).

Alifunzwa kijeshi katika chuo kimoja cha kijeshi nchini Morocco na akiwa na umri wa miaka 23 alipewa dhamana ya kuwaongoza wapiganaji wenzake kusini mwa Algeria karibu na mpaka wa Mali katika mapigano dhidi ya Wafaransa.

Huko ndiko alikopewa jina la Abdelkader al-Mali, jina lake la kivita ambalo baadhi ya watu nchini Algeria hadi leo wanamwita.

Baada ya muda akaibuka kuwa katibu muhtasi wa mambo ya utawala wa Houari Boumédiène, aliyekuwa wakati huo mkuu wa jeshi la ukombozi la ALN. Wawili hao walikuwa na usuhuba mkubwa ulioendelea baada ya uhuru 1962, pale Bouteflika alipoteuliwa waziri wa vijana na michezo na Boumédiène alipokuwa waziri wa ulinzi.

Mwaka uliofuatia Rais Ahmed Ben Bella alimteua Bouteflika waziri wa mambo ya nje. Lakini walikuwa kama paka na chui. Miaka miwili baadaye, 1965, Ben Bella alimkabili Boumédiène na kumwambia kwamba anamfukuza kazi Bouteflika na kwamba atawapangua na kuwapanga upya wakuu wa majeshi.

Boumédiène alinyamaza kimya lakini akishirikiana na Bouteflika aliandaa mapinduzi ya kijeshi yaliyompindua Ben Bella Juni 19, 1965. Fidel Castro, aliyekuwa kiongozi wa Cuba wakati huo alichukizwa na mapinduzi yaliyompindua rafiki yake, Ben Bella. Siku tatu baada ya Ben Bella kupinduliwa Castro aliuhutubia umati wa watu mjini Havana, Cuba.

Aliyaelezea mapinduzi hayo kuwa ya “ndugu kuua ndugu”, ingawa hakuna hata tone moja la damu lililodondoka katika mapinduzi yenyewe. Halafu Castro alianza kumshambulia Bouteflika binafsi akisema kwamba Bouteflika ndiye aliyeyaandaa mapinduzi na kwamba Bouteflika “anajulikana kuwa si mwanamapinduzi bali ni mtu wa mrengo wa kulia…adui wa ushoshalisti na kwa hivyo adui wa mapinduzi ya Algeria.”

Castro na Ben Bella walikuwa kama chanda na pete. Ben Bella alikuwa na uhusiano mzuri pia na Che Guevara. Mwaka 1963 Algeria ilipokabiliwa na uwezekano wa kuvamiwa na Morocco kwa sababu za ugomvi wa mipaka mbiombio, kwa siri kubwa, Castro alipeleka Algeria ndege mbili zilizojaa wanajeshi wa Kicuba. Pia alipeleka Algeria meli mbili kutoka Cuba zilizokuwa na wanajeshi, silaha bora ilizozipata Cuba kutoka Muungano wa Sovieti, vifaru vya kijeshi, na tani 5,000 za sukari.

Wacuba walikuwa tayari kuingia vitani kuisaidia Algeria na lau Morocco na Algeria zisingelipatana basi Cuba ingepigana barani Afrika kwa mara ya kwanza kuisaidia Algeria dhidi ya Morocco na si Angola kukisaidia chama cha MPLA dhidi ya chama cha Unita.

Kuna sababu nyingine inayotajwa ya kwanini Boumédiène alimpindua Ben Bella. Inasemekana kwamba Ben Bella akitaka kumfungua kutoka gerezani mpinzani Hocine Aït Ahmed. Boumédiène alipinga.

Aït Ahmed, niliyebahatika kukutana naye safari moja katika miaka ya 1980 jijini Paris kwenye ofisi za jarida la Jeune Afrique alikuwa miongoni mwa viongozi kwa kihistoria wa Algeria aliyekuwa akiheshimika.

Baada ya Ben Bella kupinduliwa, Bouteflika aliendelea kuwa waziri wa mambo ya nje hadi Boumédiène alipofariki ghafla 1978. Wakati huo ikifikiriwa kwamba Bouteflika ndiye atayeurithi urais akiwa na mwelekeo wa mrengo wa kulia.

Lakini kulikuwa na mwengine, Kanali Mohamed Salah Yahiaoui, wa mrengo wa kushoto, ambaye pia akiurandia urais. Jeshi likaingilia kati na kutafuta suluhi ya kumweka madarakani Chedli Bendjedid. Kidogokidogo Bendjedid akaanza kumtenga Bouteflika ambaye baadaye alifunguliwa mashtaka ya wizi wa fedha chungu nzima kutoka balozi za Algeria. Bouteflika alizirudisha baadhi ya fedha hizo na mwishowe Bendjedid alimsamahe. Wenzake wawili Bouteflika walifungwa gerezani.

Wakati wa mapigano ya umwagaji damu katika miaka ya 1990 Bouteflika alikuwa kimya na wakati fulani akiishi uhamishoni. Aliibuka tena katika medani ya siasa 199 pale Rais Jenerali Liamine Zéroual alipojiuzulu ghafla na kuitisha uchaguzi mpya. Bouteflika aliyegombea uchaguzi huo akiwa mgombea huru alishinda na aliweza, kwa kiwango kikubwa, kuituliza Algeria na kuirejesha katika hali ya amani. Bouteflika alishinda katika chaguzi tatu nyingine za urais lakini alipotaka kugombea tena urais kwa mara ya tano vijana wakajimwaga barabarani kumpinga.

Walishachoshwa na kikundi kidogo cha watu, kikiwa na wakuu wa kijeshi, nduguye Bouteflika aitwaye Said na wafanyabiashara wachache, wenye kuyahodhi madaraka na kuupalilia ufisadi.


Kila baada ya sala ya Ijumaa Waalgeria wamekuwa wakimiminika barabarani kuyaunga mkono maandamano dhidi ya Bouteflika na mfumo uliompachika madarakani na wenye kujaribu kufanya juu chini aendelee kutawala kwa muhula wa tano, japokuwa hawezi kusema, hawezi kusimama wala hawezi kutembea.

Haya maandamano ya nidhamu ya hali ya juu ambayo tumekuwa tukiyashuhudia wiki hizi chache siyo ya kwanza yaliyowafanya Waalgeria wamiminike barabarani katika miji yote ya nchi hiyo wakidai mageuzi ya kisiasa nchini mwao. Walianza kwanza kuandamana namna hivyo 1988 wakati wananchi wa nchi nyingine za Afrika ya Kaskazini walipokuwa wamejikunyata wakizihofia nafsi zao na wakiogopa kupambana na watawala wao wa kimabavu.

Wakati huo kulikuwa na matumaini makubwa kwamba hali ya mambo nchini Algeria itabadilika. Wengi wakitumai kwamba patapatikana demokrasia endelevu na wengi walifurahi wakaanza kushangilia palipopatikana katiba mpya ya kidemokrasia mwanzoni mwa 1989.

Kabla ya hapo, siasa za Algeria zilikuwa zikidhibitiwa na vyombo vitatu: jeshi, dola na chama cha FNL ambacho pekee kilikuwa halali tangu nchi hiyo iwe huru 1962 hadi 1989 palipoanzishwa mfumo wa vyama vingi. Hali ilikuwa hivyo kwa kipindi chote hicho.

Uchumi wa Algeria wenye kutegemea sana mauzo ya mafuta ya petroli na gesi asili ulidhibitiwa na dola (serikali) iliyoweza kuutumia kuwapatia ajira na huduma idadi kubwa ya watu. Waalgeria wakila unyunyu na kustarehe hadi bei za petroli zilipoanza kuanguka na madeni yakazidi kuyaelemea mabega ya serikali. Watawala wakaanza kushindwa kuyakidhi mahitaji ya wananchi.

Hapo ndipo wananchi walipoanza kuyahisi makali ya maisha. Wakaanza kulalamika. Manunguniko yakazidi. Wanaharakati wakatafuta njia za kuwaunganisha wananchi, hasa wa matabaka ya chini, na hatimaye mnamo Oktoba 1988 wananchi wakaanza kufanya fujo barabarani wakidai haki za kimsingi za kidemokrasia.

Utawala ulitikisika. Haukuweza kulizuia wimbi la ghadhabu za umma. Wananchi waliendelea kushikilia lazima pawepo mageuzi katika mfumo wa utawala. Mwishowe watawala hawakuwa na budi ila kuanzisha mfumo wa vyama vingi vya siasa.

Kuanzishwa kwa mfumo huo kuliiangusha moja ya nguzo tatu muhimu za utawala wa Algeria yaani FLN, chama pekee cha siasa kilichokuwako nchini humo. Siasa za vyama vingi zilianzishwa Algeria katika wakati ambapo vuguvugu la Kiislamu likianza kuchomoza na kupata nguvu.

Mwanzoni vuguvugu hilo halikuwa la kisiasa. Lilikuwa likijishughulisha na masuala ya kijamii kuwasaidia wa tabaka la nchi katika mambo ya elimu, afya na mambo mingine ya kijamii.

Maandamano na uasi dhidi ya watawala ni moja ya mambo yanayotufanya tuikumbuke vyema historia ya Algeria. Kwa kumpinga Bouteflika Waalgeria wamekuwa wakiudai tena utu wao na utawala wa haki. Watawala nao, kwa upande wao, wamekuwa wakizitumia taasisi za dola kuendelea kuwakandamiza. Bado umma wa Algeria haukuvunjika moyo na kukata tamaa.

Hatujui patuzuka nini kesho au hata miezi michache ijayo. Baada ya maandamano ya wiki tatu mfululizo watawala walimteua Noureddine Bedoui awe waziri mkuu mpya, Uteuzi wake nadhani ni njama ya kuwababaisha wananchi wahisi kuwa kuna mageuzi katika ngazi za juu za utawala.

Sidhani kama ataweza kuleta mageuzi endelevu yatayoutuliza umma. Labda atachojaribu kufanya ni kuutia viraka mfumo wa utawala uliochakaa na ulioanza kufumka. Ni muhali kwamba kwa kufanya hivyo ataweza kuwaridhisha wananchi.

Pia watawala walimteua Lakhdar Brahimi kusimamia kipindi cha mpito na mchakato wa kulipatia taifa katiba mpya kupitia Mkutano wa Kitaifa. Huenda mwanadioplomasia huyo aliyebobea akafanikiwa. Lakini haielekei kwa sasa kwamba waandamanaji wataweza kuupindua mfumo mzima wa watawala wanaowakandamiza.

Watawala wataendelea kuchukua hatua ambazo wanahisi zitawaghilibu wananchi. Hatahivyo, wananchi wa Algeria, kama walivyo wananchi wanaokandamizwa katika nchi nyingine, hawawezi kughilibika kila uchao.

Wenye kuhodhi madaraka kwa sasa ni wale wenye bunduki, vifaru vya kijeshi na wenye kuvitumia vyombo vya dola dhidi ya umma wenye kutaka mageuzi. Hata hivyo, kuna siku watawala hao watadata pamoja na vyombo vyao vya dola.

Kitachoibuka baada ya hapo hatukijui.


Baruapepe: aamahmedrajab @icloud.com; Twitter: @ahmedrajab









Sent using Jamii Forums mobile app
 
mbongo ukiandamana ikatokea ukapata tatizo kidogo majirani wanakaa kukusengenya kwamba ndo ukome umejitakia matatizo wanaibuka ma misemo yao 'mwana kulitaka,mwanakulipata"

sisi kubadirika bado sana.
 
Mtu yupo Kwenye Wheel chair kwa maradhi kwa zaid ya Miaka 10 lakin bado anang'ang'ania Madarakani
Labda aliweka nadhiri atoke Ikulu Siku anapelekwa Kaburini

Uchaguzi uliopita umefanyika akiwa ICU France 'akashinda' kwa Kishindo
 
Ahmed Rajabu taarifa za international relations toka madai ya Uhuru kabla hata ya miaka 1950's ziko kwenye viganja vya mikono yake. Hata akina Babangida aliwahi kutoa makala yake , nilimkubali. Na makala zake za RAIA mwema no darasa Tosha. Ila anaamini msimamo ya kuwa mchango Wa waislamu kuleta Uhuru Wa Tanganyika Nyerere na system yake hawakuuthamini. Lakini haimuondolei ukweli kuwa ni mwanazuoni mahiri Wa kiwango cha juu huyu mzanzibar. Lakini kama kuna ndugu zake ( ni shombe) waliumizwa na Sera za Karume had I akaishi nje ya nchi yake maisha yote tangu namsoma miaka 1970's asasmehewe mpemba Wa watu. Hongera Ahmed Rajab.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Mtu yupo Kwenye Wheel chair kwa maradhi kwa zaid ya Miaka 10 lakin bado anang'ang'ania Madarakani
Labda aliweka nadhiri atoke Ikulu Siku anapelekwa Kaburini

Uchaguzi uliopita umefanyika akiwa ICU France 'akashinda' kwa Kishindo
Sisi yeye, ni wanaomzunguka wanaofaidi utawala wake. Inawezekana kabisa hata hana habari na kinachoendelea

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Chocho
Siku Fidel Castro alipofoka akimlaani Abdelaziz Bouteflika

Na Ahmed Rajab

ABDELAZIZ Bouteflika ni jina ambalo baadhi yetu, wa umri fulani, tumekulia nalo utotoni na tunaendelea kulisikia hadi uzeeni. Zamani lilikuwa jina lililokuwa na heshima fulani. Leo ni jina la mtu anayeadhirika.

Mamilioni ya wananchi wa Algeria, wakiongozwa na vijana, wamemkaa kooni wanamtaka ang’atuke madarakani.

Tulizoea kulisikia jina la Bouteflika tangu alipokuwa waziri wa mambo ya nje wa Algeria (1963-1979). Aliteuliwa kwanza kuishika wizara hiyo alipokuwa na umri wa miaka 26, akiwa waziri kijana kushinda wote wengine duniani kushika wadhifa kama huo.

Enzi hizo kulikuwako katika nchi nyingine mawaziri wa mambo ya nje waliokuwa pia wakivuma kwa muda mrefu. Mifano inayonijia ni ya Adam Malik aliyekuwa waziri wa mambo ya nje wa Indonesia (1966-1977) na Andrei Gromyko aliyeganda kwenye wizara ya mambo ya nje ya Muungano wa Sovieti kwa muda wa miaka 28 (1957-1985).

Bouteflika alijiingiza katika harakati za ukombozi akiwa kijana mbichi wa miaka 19 alipojiunga na jeshi la ukombozi la Armée de libération nationale (ALN), lililokuwa jeshi la chama cha ukombozi wa taifa - Front de libération nationale (FLN).

Alifunzwa kijeshi katika chuo kimoja cha kijeshi nchini Morocco na akiwa na umri wa miaka 23 alipewa dhamana ya kuwaongoza wapiganaji wenzake kusini mwa Algeria karibu na mpaka wa Mali katika mapigano dhidi ya Wafaransa.

Huko ndiko alikopewa jina la Abdelkader al-Mali, jina lake la kivita ambalo baadhi ya watu nchini Algeria hadi leo wanamwita.

Baada ya muda akaibuka kuwa katibu muhtasi wa mambo ya utawala wa Houari Boumédiène, aliyekuwa wakati huo mkuu wa jeshi la ukombozi la ALN. Wawili hao walikuwa na usuhuba mkubwa ulioendelea baada ya uhuru 1962, pale Bouteflika alipoteuliwa waziri wa vijana na michezo na Boumédiène alipokuwa waziri wa ulinzi.

Mwaka uliofuatia Rais Ahmed Ben Bella alimteua Bouteflika waziri wa mambo ya nje. Lakini walikuwa kama paka na chui. Miaka miwili baadaye, 1965, Ben Bella alimkabili Boumédiène na kumwambia kwamba anamfukuza kazi Bouteflika na kwamba atawapangua na kuwapanga upya wakuu wa majeshi.

Boumédiène alinyamaza kimya lakini akishirikiana na Bouteflika aliandaa mapinduzi ya kijeshi yaliyompindua Ben Bella Juni 19, 1965. Fidel Castro, aliyekuwa kiongozi wa Cuba wakati huo alichukizwa na mapinduzi yaliyompindua rafiki yake, Ben Bella. Siku tatu baada ya Ben Bella kupinduliwa Castro aliuhutubia umati wa watu mjini Havana, Cuba.

Aliyaelezea mapinduzi hayo kuwa ya “ndugu kuua ndugu”, ingawa hakuna hata tone moja la damu lililodondoka katika mapinduzi yenyewe. Halafu Castro alianza kumshambulia Bouteflika binafsi akisema kwamba Bouteflika ndiye aliyeyaandaa mapinduzi na kwamba Bouteflika “anajulikana kuwa si mwanamapinduzi bali ni mtu wa mrengo wa kulia…adui wa ushoshalisti na kwa hivyo adui wa mapinduzi ya Algeria.”

Castro na Ben Bella walikuwa kama chanda na pete. Ben Bella alikuwa na uhusiano mzuri pia na Che Guevara. Mwaka 1963 Algeria ilipokabiliwa na uwezekano wa kuvamiwa na Morocco kwa sababu za ugomvi wa mipaka mbiombio, kwa siri kubwa, Castro alipeleka Algeria ndege mbili zilizojaa wanajeshi wa Kicuba. Pia alipeleka Algeria meli mbili kutoka Cuba zilizokuwa na wanajeshi, silaha bora ilizozipata Cuba kutoka Muungano wa Sovieti, vifaru vya kijeshi, na tani 5,000 za sukari.

Wacuba walikuwa tayari kuingia vitani kuisaidia Algeria na lau Morocco na Algeria zisingelipatana basi Cuba ingepigana barani Afrika kwa mara ya kwanza kuisaidia Algeria dhidi ya Morocco na si Angola kukisaidia chama cha MPLA dhidi ya chama cha Unita.

Kuna sababu nyingine inayotajwa ya kwanini Boumédiène alimpindua Ben Bella. Inasemekana kwamba Ben Bella akitaka kumfungua kutoka gerezani mpinzani Hocine Aït Ahmed. Boumédiène alipinga.

Aït Ahmed, niliyebahatika kukutana naye safari moja katika miaka ya 1980 jijini Paris kwenye ofisi za jarida la Jeune Afrique alikuwa miongoni mwa viongozi kwa kihistoria wa Algeria aliyekuwa akiheshimika.

Baada ya Ben Bella kupinduliwa, Bouteflika aliendelea kuwa waziri wa mambo ya nje hadi Boumédiène alipofariki ghafla 1978. Wakati huo ikifikiriwa kwamba Bouteflika ndiye atayeurithi urais akiwa na mwelekeo wa mrengo wa kulia.

Lakini kulikuwa na mwengine, Kanali Mohamed Salah Yahiaoui, wa mrengo wa kushoto, ambaye pia akiurandia urais. Jeshi likaingilia kati na kutafuta suluhi ya kumweka madarakani Chedli Bendjedid. Kidogokidogo Bendjedid akaanza kumtenga Bouteflika ambaye baadaye alifunguliwa mashtaka ya wizi wa fedha chungu nzima kutoka balozi za Algeria. Bouteflika alizirudisha baadhi ya fedha hizo na mwishowe Bendjedid alimsamahe. Wenzake wawili Bouteflika walifungwa gerezani.

Wakati wa mapigano ya umwagaji damu katika miaka ya 1990 Bouteflika alikuwa kimya na wakati fulani akiishi uhamishoni. Aliibuka tena katika medani ya siasa 199 pale Rais Jenerali Liamine Zéroual alipojiuzulu ghafla na kuitisha uchaguzi mpya. Bouteflika aliyegombea uchaguzi huo akiwa mgombea huru alishinda na aliweza, kwa kiwango kikubwa, kuituliza Algeria na kuirejesha katika hali ya amani. Bouteflika alishinda katika chaguzi tatu nyingine za urais lakini alipotaka kugombea tena urais kwa mara ya tano vijana wakajimwaga barabarani kumpinga.

Walishachoshwa na kikundi kidogo cha watu, kikiwa na wakuu wa kijeshi, nduguye Bouteflika aitwaye Said na wafanyabiashara wachache, wenye kuyahodhi madaraka na kuupalilia ufisadi.


Kila baada ya sala ya Ijumaa Waalgeria wamekuwa wakimiminika barabarani kuyaunga mkono maandamano dhidi ya Bouteflika na mfumo uliompachika madarakani na wenye kujaribu kufanya juu chini aendelee kutawala kwa muhula wa tano, japokuwa hawezi kusema, hawezi kusimama wala hawezi kutembea.

Haya maandamano ya nidhamu ya hali ya juu ambayo tumekuwa tukiyashuhudia wiki hizi chache siyo ya kwanza yaliyowafanya Waalgeria wamiminike barabarani katika miji yote ya nchi hiyo wakidai mageuzi ya kisiasa nchini mwao. Walianza kwanza kuandamana namna hivyo 1988 wakati wananchi wa nchi nyingine za Afrika ya Kaskazini walipokuwa wamejikunyata wakizihofia nafsi zao na wakiogopa kupambana na watawala wao wa kimabavu.

Wakati huo kulikuwa na matumaini makubwa kwamba hali ya mambo nchini Algeria itabadilika. Wengi wakitumai kwamba patapatikana demokrasia endelevu na wengi walifurahi wakaanza kushangilia palipopatikana katiba mpya ya kidemokrasia mwanzoni mwa 1989.

Kabla ya hapo, siasa za Algeria zilikuwa zikidhibitiwa na vyombo vitatu: jeshi, dola na chama cha FNL ambacho pekee kilikuwa halali tangu nchi hiyo iwe huru 1962 hadi 1989 palipoanzishwa mfumo wa vyama vingi. Hali ilikuwa hivyo kwa kipindi chote hicho.

Uchumi wa Algeria wenye kutegemea sana mauzo ya mafuta ya petroli na gesi asili ulidhibitiwa na dola (serikali) iliyoweza kuutumia kuwapatia ajira na huduma idadi kubwa ya watu. Waalgeria wakila unyunyu na kustarehe hadi bei za petroli zilipoanza kuanguka na madeni yakazidi kuyaelemea mabega ya serikali. Watawala wakaanza kushindwa kuyakidhi mahitaji ya wananchi.

Hapo ndipo wananchi walipoanza kuyahisi makali ya maisha. Wakaanza kulalamika. Manunguniko yakazidi. Wanaharakati wakatafuta njia za kuwaunganisha wananchi, hasa wa matabaka ya chini, na hatimaye mnamo Oktoba 1988 wananchi wakaanza kufanya fujo barabarani wakidai haki za kimsingi za kidemokrasia.

Utawala ulitikisika. Haukuweza kulizuia wimbi la ghadhabu za umma. Wananchi waliendelea kushikilia lazima pawepo mageuzi katika mfumo wa utawala. Mwishowe watawala hawakuwa na budi ila kuanzisha mfumo wa vyama vingi vya siasa.

Kuanzishwa kwa mfumo huo kuliiangusha moja ya nguzo tatu muhimu za utawala wa Algeria yaani FLN, chama pekee cha siasa kilichokuwako nchini humo. Siasa za vyama vingi zilianzishwa Algeria katika wakati ambapo vuguvugu la Kiislamu likianza kuchomoza na kupata nguvu.

Mwanzoni vuguvugu hilo halikuwa la kisiasa. Lilikuwa likijishughulisha na masuala ya kijamii kuwasaidia wa tabaka la nchi katika mambo ya elimu, afya na mambo mingine ya kijamii.

Maandamano na uasi dhidi ya watawala ni moja ya mambo yanayotufanya tuikumbuke vyema historia ya Algeria. Kwa kumpinga Bouteflika Waalgeria wamekuwa wakiudai tena utu wao na utawala wa haki. Watawala nao, kwa upande wao, wamekuwa wakizitumia taasisi za dola kuendelea kuwakandamiza. Bado umma wa Algeria haukuvunjika moyo na kukata tamaa.

Hatujui patuzuka nini kesho au hata miezi michache ijayo. Baada ya maandamano ya wiki tatu mfululizo watawala walimteua Noureddine Bedoui awe waziri mkuu mpya, Uteuzi wake nadhani ni njama ya kuwababaisha wananchi wahisi kuwa kuna mageuzi katika ngazi za juu za utawala.

Sidhani kama ataweza kuleta mageuzi endelevu yatayoutuliza umma. Labda atachojaribu kufanya ni kuutia viraka mfumo wa utawala uliochakaa na ulioanza kufumka. Ni muhali kwamba kwa kufanya hivyo ataweza kuwaridhisha wananchi.

Pia watawala walimteua Lakhdar Brahimi kusimamia kipindi cha mpito na mchakato wa kulipatia taifa katiba mpya kupitia Mkutano wa Kitaifa. Huenda mwanadioplomasia huyo aliyebobea akafanikiwa. Lakini haielekei kwa sasa kwamba waandamanaji wataweza kuupindua mfumo mzima wa watawala wanaowakandamiza.

Watawala wataendelea kuchukua hatua ambazo wanahisi zitawaghilibu wananchi. Hatahivyo, wananchi wa Algeria, kama walivyo wananchi wanaokandamizwa katika nchi nyingine, hawawezi kughilibika kila uchao.

Wenye kuhodhi madaraka kwa sasa ni wale wenye bunduki, vifaru vya kijeshi na wenye kuvitumia vyombo vya dola dhidi ya umma wenye kutaka mageuzi. Hata hivyo, kuna siku watawala hao watadata pamoja na vyombo vyao vya dola.

Kitachoibuka baada ya hapo hatukijui.


Baruapepe: aamahmedrajab @icloud.com; Twitter: @ahmedrajab









Sent using Jamii Forums mobile app
Ahsante sana. Chochote toka kwa nguli wa siasa na habari kwetu ni tunu.
 
Back
Top Bottom