Si wote tulishiriki wizi Kapunga

macho_mdiliko

JF-Expert Member
Mar 10, 2008
21,465
38,710
MIMI ni Mtanzania ambaye nafanya kazi nchini Togo Mji Mkuu wa Lome. Naitwa Yahya Msangi na ni msomaji mkubwa wa Raia Mwema. Habari ya Shamba la mpunga la Kapunga (toleo la wiki mbili zilizopita) imenigusa sana kwani nilishiriki mchakato wa kuanzisha shamba hilo.

Hakuna mtu asiyenijua pale Chimala, japo ni miaka mingi sasa imepita. Nilishiriki tangu kusafisha shamba hadi kupanda mbegu za majaribio na baadaye kujengwa miundombinu na kampuni za KAJIMA na WADE ADAMS chini ya usimamizi wa TANCONSULT (Tanzania) na kampuni nyingine kutoka Uingereza (jina limenitoka kidogo).

Baada ya hapo niliteuliwa kuwa Afisa Uzalishaji (tukiwa maafisa wawili mwenzangu akiitwa James Kachumu). Wote tulikuwa wahitimu wa SUA (Sokoine University of Agriculture).

Juu yetu alikuwa Meneja Uzalishaji akiitwa Malisa (jina la kwanza limenitoka) na Meneja Mradi akiitwa Deogratius Kweka (ambaye ametajwa kwenye tuhuma za Twin Towers za BoT).

Habari hii imenigusa kwa kuwa inatoa picha kwamba watumishi wote tuliopewa dhamana ya kuendesha Kapunga Rice Project tulikuwa wabadhirifu! Ukweli ni kwamba ubadhirifu mkubwa ulikuwapo lakini si wote tulishiriki.

Ukweli ni kwamba baadhi yetu tuliupinga kwa nguvu zetu zote na ilitugharimu! Wengine tulifukuzwa kazi, wengine walisingiziwa mashtaka ya uongo wakafungwa (nakumbuka dereva mmoja wa trekta alifia jela!) Wengine walihamishwa na wengine waliacha kazi wenyewe baada ya kusumbuliwa sana.

Historia ya ubadhirifu huo ni ndefu, nitaipitia kwa ufupi. Kwanza niseme tu kwamba mmoja wa watu muhimu katika mradi huo alikataa kuhamia Chimala. Alikuwa anaishi Dar-Es-Salaam! Alikuwa anakuja Kapunga kama mtaliii.

Pale Kapunga alileta jamaa zake wengi na mmoja alimpa madaraka ya kukaimu nafasi yake shambani. Huyu alipoletwa alipewa mamlaka kupita hata sisi aliotukuta kwa kuwa ndiye alikuwa mtekelezaji wa wizi wote uliokuwa unafanywa kupitia kampuni za kigeni na za ndani. Kuna baadhi ya vifaa vya mradi yakiwamo matrekta na magari hayakufika kabisa Kapunga!

Wakati huo ndio kilikuwa kipindi cha ujenzi na makampuni mbalimbali yalihusika. Gharama za kazi na vifaa zilighushiwa na kuna baadhi ya miundombinu kama mifereji haikujengwa kwa kiwango kilichokubalika.

Ujenzi ulipoisha na uzalishaji kuanza mwaka 1991/92 kukaanza wizi mpya! Sumu za mashambani zikaanza kununuliwa kwa wingi kuliko mahitaji na kwa bei za kutisha, mchele ukaanza kuuzwa kwa bei ya kuruka na fedha za ziada zikaingia mifukoni mwa wezi wachache.

Malori ya mchele yakaanza kuchukua mchele bila malipo na kuupeleka kusikojulikana. Hali hii iliwavunja moyo sana wafanyakazi hasa wa shambani ambao walikuwa wakiteseka kwenye vumbi, jua, mvua, majoka, nyuki, sumu n.k., kuzalisha mpunga.

Kubwa ya yote ni pale ambapo mavuno ya shamba lililokuwa likiitwa la wafanyakazi (Block Farm) yalipotakiwa yapelekwe Makao Makuu Dar es Salaam kwa Meneja Mkuu na Wakurugenzi. Baadhi yetu tuliokuwa wajumbe wa Menejimenti uzalendo ulitushinda tukaamuru wafanyakazi wachukue haki yao!

Hii ni kwa mujibu wa Staff Regulation ya shirika la NAFCO lililokuwa linamiliki mashamba nchini. Kitendo hiki kiliwaudhi wakubwa Dar es Salaam pamoja na viongozi wa Mkoa wa Mbeya! Masikini hatukujua kumbe uongozi mkoani nao ulikuwa fedhuli na mbakaji wa mali za mradi! Tunaposikia kuwa wakuu hao wa zamani sasa ni waheshimiwa sana huko nyumbani tunashangaa sana.

Afadhali Mkuu wa Wilaya alitimuliwa zama za Mzee Ruksa akiwa katika mkoa mmoja nchini.

Huyo Mkuu wa Wilaya sitamsahau. Kwani siku moja nikiwa shambani (hiyo small holder) naelekeza maji kwenye kashamba kangu. Alikuja na Landrover nyeupe inapepea bendera ya Jamhuri akasimama kama mita 100 kutoka nilipo.

Mara nikaona mgambo anakuja kwa kasi na kuniambia naitwa kwenye gari! Mimi nililitambua gari na nilikwisha kubonyezwa picha yote na wasamaria wema kutoka ofisini kwake.

Nilimwambia yule mgambo kwamba huyo aliyeko kwenye gari nadhani ana macho na miguu miwili hivyo anaweza kuja kama alivyokuja yeye!

Akataka kunizoa mzobemzobe, lakini alhamdulilah wakati huo na mimi si haba, akagonga mwamba! Alichonitaabisha ni harufu ya gongo iliyotoka kinywani mwake! Kule kwenye gari walipoona mjumbe anakaribia kugalagazwa wakaja kwa gari mbio! Mkuu wa Wilaya akawa wa kwanza kuruka tuta la mfereji kunifuata! Mkuu huyu wa wilaya alikuwa mwanamke.

Aliponikaribia akaniuliza 'wewe ndiye Msangi?'
Nikamwambia muulize aliyekupa jina langu, maana mie na wewe hatujawahi kukutana.

Alibadilika sura, akavimba na kusema ' unajua mimi nina mamlaka ya kukuweka ndani masaa 24 bila kuhojiwa?' Nikamjibu ' inawezekana lakini mumeo ana mamlaka ya kukuweka ndani milele bila kuhojiwa na mtu yeyote pia' kwa hiyo mamlaka yako si ya ajabu sana'!

Akabadilisha somo kwa kunituhumu amepata mashtaka ya kuwa nawanyima wakulima wenzangu maji, eti nimetoboa mfereji maji yote yanaingia shambani mwangu ndiyo maana navuna vizuri kuliko wengine!

Kweli alinikuta natoboa mfereji, lakini hapo small holder hakuna mkulima ambaye hakuwahi kutoboa mfereji kwa kuwa kazi ya kusawazisha shamba ililipuliwa na mkandarasi. Hata shambani kwake Mkuu wa Wilaya alikuwa katoboa hivyo hivyo. Nilimshauri twende kwenye shamba lake ajionee mwenyewe mambo yalivyo na jinsi mimi nilivyojifunza kutoboa mfereji kutoka kwake kama Mkuu wa Wilaya! Alianza kufoka, na kusema atamwamuru Meneja wangu akate mshahara wangu kufidia gharama za safari yake na ujumbe aliofuatana naye!

Nilimjibu kwamba mimi nazijua sheria za kazi (nilikuwa Katibu wa Chama cha Wafanyakazi Kapunga), asithubutu. Aliondoka kwa hasira yeye na ujumbe wake. Masikini Mkuu wa Wilaya yule hakujua ndani ya gari mlikuwa na mtonyaji wangu! Alinipa stori yote na mazungumzo yote waliyofanya kabla na baada ya safari. Mungu amkirimu mtumishi yule, aliona ukweli na akaamua kuulinda.

Tuachane na mwanamama yule. Basi kama ilivyo kwenye wizi wowote lazima watu wazidiane akili. Pale makao makuu NAFCO kulikuwa na timu mbili. Moja ikiongozwa na Mkurugenzi wa Fedha na Utawala, nyingine ikiongozwa na Mkurugenza wa Mipango. Mkurugenzi wa Fedha alikuwa amewaweka kundini mameneja wa mashamba ya Ruvu, Kahe Mbozi Maize, n.k., wa Mipango alikuwa na mameja wa Kapunga, Dakawa Rice Farm na Hanang Wheat Complex. Kwa kifupi waligawana mashamba kwa manufaa yao.

Mameneja wakuu wote waliopita pale NAFCO walikuwa wanawekwa sawa na makundi haya mawili. Haijambo nao walinufaika sana. Lakini hawa wakurugenzi wawili kila mmoja alikuwa anamlia timing mwenzie, mmoja akizubaa tu anazidiwa kete.

Sasa wakati ule mashamba mengi ya NAFCO yalikuwa hoi bin taaban. Shamba pekee lililokuwa 'linalipa' ni Kapunga. Mmoja wa wale wakurugenzi wetu wawili alikuwa mlafi wa kupindukia, actually mwizi mharibifu kuliko mwenzake. Yeye hata ikibidi trekta liwe cannibalised alikuwa tayari kuchukua vipande vipande!

Huu ndio mkasa uliolikumba shamba dada liliokuwa linaitwa Madibira Rice Project. Hapo alikuwa na meneja wake mmoja, walihamisha kila kitu mpaka mradi ukafa! Mkurugenzi huyo akafanya mbinu akabadili uongozi pale Kapunga.

Kwa mabadiliko hayo wimbi jipya la wizi pale Kapunga likaanza. Huyu ndiye alikuja kuipeleka Kapunga kaburini. Aliiba, akaiba, akaiba, akanyanyasa wafanyakazi (mimi mwenyewe alinisukia uhamisho mara mbili. Mara ya kwanza ilifutiliwa mbali na Mwenyekiti wa Bodi, Mzee Brown Ngwililupi – Mungu amlaze pema kwani alikuwa mtu wa haki tupu yule). Alipojiunga na NCCR Mageuzi akaondolewa, badala yake akaletwa Matheo Qaresi.

Qaresi mwanzoni alizuia uhamisho wangu wa pili, lakini baadaye akaruhusu nifukuzwe kazi kabisa! Lakini kabla sijapewa uhamisho, bosi wangu alikuwa mtu wa visa na mikasa!

Mwaka 1992 nilipata ajali ya gari mjini Mbeya, nilimgonga mtu akafariki. Iliniuma sana. Baada ya kumaliza taratibu zote za Polisi nilitafuta nyumbani kwa marahemu nikaenda na rafiki zangu kutoa pole na ubani. Kwa kweli nilisikitika sana kusikia yule marehemu alikuwa mlowezi kutoka Malawi na hakuwa na ndugu ila alikuwa na mwanamke rafiki waliyekutana hapo Mbeya.

Ubani wetu tulimpa yule mama ingawa naye hakuwa mkewe. Alipofika bosi wangu mpya mwaka 1994 akaamua kutumia ajali hiyo kunitafutia matatizo. Siku moja nikiwa ofisini kwangu alikuja mzee mmoja nisiyemjua, akajitambulisha kuwa yeye ni ndugu wa marehemu niliyemgonga kwa gari (yeye alisema niliyemuua) na amekuja kufuata fidia.

Msingi wa madai yake (alinipa karatasi iliyochapishwa vizuri na kompyuta) ni kwamba marehemu alikuwa na watoto anawasomesha, mashamba yenye ukubwa wa ekari 200 na mifugo. Watoto hawasomi kwa kukosa ada na mifugo na mashamba imeteketea kwa kukosa huduma! Anataka fidia ya milioni 2, wakati ule nyingi kwa kiwango chake.

Lakini wakati ananieleza hayo nilikuwa naona vikaragosi wa meneja wakipita na kutupa jicho ofisini kwangu! Nikajua huyu mzee amesukwa!

Basi kwanza nilimweleza fidia hulipwa na Bima ya gari aende akadai Bima. Pili nikamwomba twende Polisi kituo cha Chimala akaandikishe maelezo yake!

Hakutaka suala la kwenda Polisi ndipo nikampasulia jipu pwaaa! Nikamweleza ninavyomjua marehemu na kwamba anachofanya ni kutaka kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu! Alitoka ofisini mbio, kwa kiwewe alichokuwa nacho, moja kwa moja akakimbilia ofisini kwa meneja wangu!

Nilimfuata huko huko na kumwambia meneja wangu kuwa nashukuru kwa kuniletea mgeni!

Alifedheheka sana. Baada ya hapo meneja wetu akaanza mkakati wa kuwaondoa watumishi wote waliokuwa na msimamo. Hapo ndipo wengine walisingiziwa wizi au ubakaji. Kuna waliokamatwa Jumatatu, wakapelekwa mahakamani na kesi kusikilizwa Jumatatu, wakahaukumiwa Jumatatu na kupelekwa jela ya Ruanda mjini Mbeya Jumatatu hiyo hiyo!

Namkumbuka mmoja alikuwa anaitwa George Kinyamagoha. Alisingiziwa kubaka, akakamatwa, akahukumiwa, akafungwa siku hiyo hiyo na akafia jela pale Ruanda! Tuliambiwa alipatwa malaria lakini hakuruhusiwa kwenda hospitali hadi akafa! Sijui hata ndugu zake wanajua kilichomsibu ndugu yao!? Kisa alitoboa siri kwamba kigogo mmoja ndiye aliyemtuma kulimia watu mashamba yao na kutia pesa mfukoni!

Ni kweli kigogo yule alimtuma, lakini naye alichepuka akalima heka mbili tatu akatia pesa mfukoni, lakini wakati akirudi kwenye safari hiyo haramu akapinduka na kuua trekta la thamani ya shilingi milioni 70 wakati ule! Alikuwa anajaribu ku save muda asigundulike baada ya kufanya kazi haramu ya bosi naye alifanya kaharamu kake!

Hatimaye siku moja wafanyakzi baada ya kutaabika waliamua kuwafungia milango wabadhirifu wote. Mkuu wa Mkoa akamwaga FFU kibao. Nyumba yangu na familia ikazingirwa na FFU! Familia ikapata hofu kwelikweli. Lakini si FFU wote wanatenda kwa kupenda! Nilipofika nyumbani na kukuta imezingirwa, wengi wa FFU waliniambia bila woga kwamba 'ndugu Msangi, usihofu hata kidogo, hapa tumefuata posho tu sie ni binadamu na tunaona unachotetea ni haki'. Nilifarijika kupita kiasi!

Majira ya usiku saa tatu nilisikia wakizozana na kamanda wao kuhusu kuzingira nyumba yangu! Wakimwambia kamanda ingefaa wahamie kantini kwani si vyema kumzingira mtu asiye na tatizo!

Kamanda alikubaliana nao. Walikaa siku tatu huku Mkuu wa Mkoa na viongozi wabadhirifu wakiendesha jitihada za kufungua milango ili warejee ofisini kinyume cha matakwa ya wafanyakazi. Walirejea kwa mtutu wa bunduki!

Serikali kupitia Wizara ya Kilimo (wakati huo chini ya Frederick Sumaye) ikaamua kuunda tume ya uchunguzi. Kiongozi wa tume alikuwa mzee mmoja kutoka TFTU/OTTU. Ile haikuwa tume huru, kwanza walilipwa posho na NAFCO! Walipofika tu wakakutana CCM Bar (ipo pale Chimala) na uongozi wa mradi. Ni bahati mbaya tu miaka ile vinasa sauti havikuwa vingi, lakini tulisikiliza mazungumzo yao yote. Yalikuwa ni ya jinsi gani wataandika ripoti nzuri!

Viongozi wa kijiji cha Chimala ambao leo hii ndio wako mstari wa mbele kuilalmikia Serikali kwa kuwatelekeza wanapaswa wajilaumu wao wenyewe. Ile tume feki ilikutana nao, wakatoa ushahidi kwamba utawala ni mzuri ila kundi letu sisi ndilo lina ukorofi na ingefaa tuhamishwe au kufukuzwa kazi ili mradi uendelee. Hata hakimu wa Mahakama ya Chimala aliyekuwapo (sasa marehemu nasikia) naye akatoa ushahidi kutetea viongozi wabadhirifu.

Tume iliwahoji vibaraka wa wabadhirifu na maoni yao yakafanywa ndiyo maoni ya wafanyakazi wote wa Kapunga. Hapo ndipo Kapunga ilipewa pasipoti ya kwenda kaburini.

Hao viongozi wa kijiji cha Chimala wanapaswa kujilaumu wenyewe badala ya kulaumu Serikali. Madhara haya walijitakia wenyewe!

Hata wananchi wa Chimala hawapaswi kulalamika sana kwani wakati ule alifika Agustine Mrema pale kijijini. Wakati huo Waziri wa Mambo ya Ndani na Naibu Waziri Mkuu! Kwa hofu ya Mrema (wakati ule Mzee wa Kiraracha si mchezo) wakaanza kupangwa wasemeje kwenye mkutano.

Nilihudhuria mkutano huo pale uwanja wa sekondari ya Chimala. Waliozungumza hawakueleza matatizo ya mradi na maendeleo ya kijiji chao. Wengi walisifu uongozi wa NAFCO na kutuponda wakorofi wachache! Sasa wanaula wa chuya, siye bado tunapeta, pale hapakuwa kwetu! Ni kwao, sisi riziki ilipokoma tuliondoka tukwaachia zigo lao!

Hatimaye Bodi ya Qaresi ambaye iliagiza nijieleze kwenye Bodi ndogo ya Shamba. Mimi nilikataa kwenda huko kwa kuwa Mkuu wa Mkoa (ambaye naye alikuwa mshiriki wa ubadhirifu alikuwa mjumbe wa Bodi hiyo pamoja na maofisa wengine mkoani). Pili mimi sikuwa mtumishi niliyekuwa nawajibika kwa Bodi ya Shamba, mimi nilikuwa nawajibika kwa Bodi Kuu ambayo Mwenyekiti alikuwa Qaresi.

Nikafukuzwa, tena kwa kupewa barua siku ya Eid El Haji! Nilikuwa najiandaa na familia yangu kwenda msikitini kusali alipokuja mjumbe mahsusi kutoka Makao Makuu Dar es Salaam akaona ni wakati muafaka wa kunikabidhi barua ya kufukuzwa kazi. Naambiwa baadaye walifanya sherehe eti wamepata dawa ya kirusi cha UKIMWI! Kirusi hicho mimi YAHYA MSANGI!

Lakini Mwenyezi Mungu hamtupi mja wake. Mimi bado niko hai na ni mfanyakazi katika taasisi ya kimataifa! Wengi wa kundi la wabadhirifu na waovu wametangulia mbele ya haki. Sijui kama waliwahi kutubu maovu yao, lakini ningekuwa nasaidiana na Muumba ningemshauri awarejeshee maombi yao kwani walikuwa waovu mno! Wengine, hata hivyo, Mungu ameamua kuwalipa hapa hapa!

Nimeandika kwa kirefu kwa kuwa nimeudhika sana na taswira aliyotoa Mwandishi wa Makala yenu kwamba wote tuliokabidhiwa dhamana na Taifa hatukuwa waaminifu. Si kweli, wengine tulipata madhara tunayoyakumbuka leo na milele. Kama kuna niliyemtaja humu na anabisha nilichosema na athubutu kuomba uchunguzi!


Source: Raia Mwema
 
Duh pole sana, inaelekea bwana msangi una mengi ya kueleza lakini unayaeleza kama kwa uoga au kutojiamini nadhani ulipaswa kuandika kitabu kuhusu hiyo project, na watanzania wengi waweze kupata hiyo habari katika mtiririko mzuri na wa kujenga hoja za msingi

Kumbe Qares na Sumaye ni wazamani kwenye hizi game?
 
Ndugu Msangi,
Mwenyezi Mungu ataendelea kukubariki. Tunahitaji Watanzania zaidi wenye kuthubutu kupambana na uhaini wa aina hii.
 
Tanzania zaidi ya uijuavyo mi nakwambia yaani hawa viongozi wetu hakuna mwenye background safi hata moja nani aje kutuokoa?
 
Msangi hii nchi iache tu mwl Nyerere alianzisha mengi lakini ni machache tulonyo kwa sasa, sasa kwa shamba tu uwe mpole ila mara nyinginekuwa na Confidence katika kujieleza huu ni uwanja wa uhuru wa mawazo BUT matusi mwiko!
 
waandishi wa habari utawaweza bongo? wameshauza hivoooooo!

ukijibu wanauza tena!!!!

Pole Msangi
 
Msangi watu kama nyie ndio mnaonekana hamna heshima na adabu. Sio uwongo kwa miaka ya story yako watu mlikuwa wachache saaaana.

Hata elimu zetu kuanzia chekechea mapka vyuoni simetulea hivyo wa juu hakoselewi. Sasa watu kama kina msangi nina hakika wengi kwenye jamii tunawashangaa.

Ni vizuri umeijibu hiyo hoja na itakuwa vizuri ukifanya jitihada za wana chimala wayajue haya ya upande mwingine wa shilingi. wao wataamua. Sijui ni njia gani ukiwa na nia ya kuwafikishia habari wanakijiji inafaa hili swali huwa sijapata jibu.

Njia pekee ya kuwasiliana na wanakijiji wengi no only through politician. Huu mtandao ni wa wachache. Hii ni changamoto ya kujaribu kuwafikishia habari kama hii wadau wanachimala kazi kwao iakuwa kujua nani kinyonga, nani nyoka wa kijani asiye na sumu na nani cobra.
 
miaka yooote huwa nawaaambia jamani maishapopote..........heb cheki jamaa alipotoka! chedi avae msangi
 
Msangi,
we need a complete report here ( a book as someone suggested will do)
Otherwise utakuwa huitendei haki jamii yako.
We need to know the WHOLE thing.
You have hide it for a long enough time.
Let it out NOW.
 
Mambo yaliyompata Yahaya Msangi ni ya kawaida sana kutokea kwenye mashirika ya umma.

Sisi tuliobahatika kufanyakazi kwenye mashika ya umma ambayo yalikuja kufa kama ilivyotokea kwenye mashamba ya NAFCO story ni hizo hizo wabadhirifu mara nyingi wanapata kinga kutoka mamlaka za juu.

Mwl Nyerere alijitahidi sana kuijenga Tanzania kwa kadri ya uwezo wake wote lakini alikuwa na bahati mbaya sana ya kuzungukwa na viongozi ambao hawakutaka kumsaidia.

Project zote alizozianzisha zilishindwa kuendelea kwasababu ya ubadhirifu na uongozi mbovu.Wiki mbili zilizopita nilitembelea TEMDO kwaajili ya kutengenezewa mashine ya kukamua juice,nilichojionea kwa kweli roho iliniuma kila idara niliyopita wafanyakazi wanafikiria jinsi kuiba.

Mwisho wa ziara yangu nilimwambia mfanyakazi mmoja ambae tulikuwa tukifahamiana siku nyingi atafute kazi mahali pengine kwasababu kulikuwa na kila dalili TEMDO itakufa muda si mrefu.
 
Mambo yaliyompata Yahaya Msangi ni ya kawaida sana kutokea kwenye mashirika ya umma.Sisi tuliobahatika kufanyakazi kwenye mashika ya umma ambayo yalikuja kufa kama ilivyotokea kwenye mashamba ya NAFCO story ni hizo hizo wabadhirifu mara nyingi wanapata kinga kutoka mamlaka za juu.

Mwl Nyerere alijitahidi sana kuijenga Tanzania kwa kadri ya uwezo wake wote lakini alikuwa na bahati mbaya sana ya kuzungukwa na viongozi ambao hawakutaka kumsaidia.Project zote alizozianzisha zilishindwa kuendelea kwasababu ya ubadhirifu na uongozi mbovu.Wiki mbili zilizopita nilitembelea TEMDO kwaajili ya kutengenezewa mashine ya kukamua juice,nilichojionea kwa kweli roho iliniuma kila idara niliyopita wafanyakazi wanafikiria jinsi kuiba.Mwisho wa ziara yangu nilimwambia mfanyakazi mmoja ambae tulikuwa tukifahamiana siku nyingi atafute kazi mahali pengine kwasababu kulikuwa na kila dalili TEMDO itakufa muda si mrefu.

TEMDO ndio shirika gani hilo mkuu? Vipi je wanatengeneza pia mashine za kukamulia mafuta ya alizeti? Wanapatikana wapi?

Back to the topiki: Ukiangalia VISION ya Mwl Nyerere katika uchumi wa nchi hii ililenga zaidi kwenye kuwa taifa za wazalishaji na si taifa la wachuuzi kama lilivyo sasa! Laiti kama pale alipokosea Mwalimu pangepata mtu akaparekebisha kitalaamu zaidi, sasa hivi tungekuwa mbali sana!
 
TEMDO ndio shirika gani hilo mkuu? Vipi je wanatengeneza pia mashine za kukamulia mafuta ya alizeti? Wanapatikana wapi?

Back to the topiki: Ukiangalia VISION ya Mwl Nyerere katika uchumi wa nchi hii ililenga zaidi kwenye kuwa taifa za wazalishaji na si taifa la wachuuzi kama lilivyo sasa! Laiti kama pale alipokosea Mwalimu pangepata mtu akaparekebisha kitalaamu zaidi, sasa hivi tungekuwa mbali sana!

Heshima kwako Masaki,

Mkuu wangu Masaki TEMDO [Tanzania Engineering and Manufacturing Design Organisation] wana uwezo wa kutengeneza mashine aina nyingi kama mashine za kukamulia juice,mafuta,mashine za kupukuchua mahindi na nk pia inahusiaka sana kutoa utaalamu wa kiuandisi kwenye viwanda vya sukari,minjingu,migodi viwanda vya chai na nk.Hii taasisi iko chini ya wizara ya viwanda biashara na masoko makao makuu ya TEMDO yako Njiro jijini Arusha.
 
Inaelekea huyu Deogratias Kweka ni fisadi mzoefu, mbona kila alipopita panafuka moshi? Wakuu kama kuna mwenye data zake zaidi atupe manake anaonekana kuwa msaada mkubwa kufichua waliokuwa wakimtuma..
 
Heshima kwako Masaki,

Mkuu wangu Masaki TEMDO [Tanzania Engineering and Manufacturing Design Organisation] wana uwezo wa kutengeneza mashine aina nyingi kama mashine za kukamulia juice,mafuta,mashine za kupukuchua mahindi na nk pia inahusiaka sana kutoa utaalamu wa kiuandisi kwenye viwanda vya sukari,minjingu,migodi viwanda vya chai na nk.Hii taasisi iko chini ya wizara ya viwanda biashara na masoko makao makuu ya TEMDO yako Njiro jijini Arusha.

Asante mkubwa!
 
Pole sana Bw.Msangi... Bila shaka mmiliki wa Raia mwema inabidi atume watu huko Chimala na Mbeya ili kuunganisha dots...
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom