Shivji achambua sheria ya madini

Keil

JF-Expert Member
Jul 2, 2007
2,214
803
Shivji achambua sheria ya madini

*Asema mikataba iliyosaniwa chini ya sheria ya 1998 inakiuka Katiba

*Asema inazuia uhuru wa Bunge kuifanyia mabadiliko

*Ataka sheria ifanyiwe marekebisho kulinda maslahi ya umma

Na Kizitto Noya


MWANASHERIA Maarufu nchini Profesa Issa Shivji, amechambua sheria ya madini ya mwaka 1998 na kueleza mapungufu kadhaa na athari zake kwa uchumi wa taifa.

Shivji amechambua sheria hiyo katika makala maalum aliyoichapisha kwenye gazeti la The Citizen linalochapishwa na kusambazwa na Kampuni ya Mwananchi Communications Ltd la Oktoba 13 mwaka huu.

Alisema utajiri wa madini nchini utakuwa laana kwa taifa badala ya neema endapo jitihada za kuzifanyia marekebisho sheria zilizopo hazitafanyika kwa lengo la kuwapa wabunge nguvu ya sheria ili kufanya mabadiliko mikataba mibovu ya madini.

Alisema sheria hizo ambazo nyingi zilitungwa katika kipindi cha serikali ya Awamu ya Tatu ni mbovu kwa vile haziwapi uwezo wabunge kufanyia mabadiliko mikataba ya madini kabla ya kumalizika muda wake.

Kwa mujibu wa Profesa Shivji, utata wa mkataba wa mgodi wa madini ya dhahabu wa Buzwagi umetokana na upungufu huo unaopatikana kwenye kufungu cha 10 cha sheria ya madini ya mwaka 1998.

Kifungu hicho kinamruhusu Waziri anayeshughulika na madini kuingia mkataba kwa niaba ya Serikali na kutoa kibali maalum cha kufanya shughuli za uchimbaji wa madini ambacho kinazuia mkataba huo kufanyiwa marekebisho baada ya kusainiwa.

Alisema utata katika mkataba huo umetokana na sheria hiyo kumpa nguvu Waziri wa Madini na Nishati kuridhia mapendekezo ya mwekezaji badala ya kazi hiyo kufanywa na Bunge.

Alisema kusingekuwa na upungufu katika sheria hiyo, mapendekezo hayo yalitakiwa kuridhiwa na Bunge badala ya waziri na kuleta utata katika jamii.

Alisema kitendo cha sheria hiyo kuwaondolea wabunge haki ya kufanya mabadiliko ya mikataba ya madini, ni upungufu unaotakiwa kufanyiwa marekebisho haraka ili kuwa na uwakilishi wa wananchi katika maamuzi mazito ya mabadiliko ya mikataba ya madini kwa manufaa ya taifa na ni kinyume na Katiba ya nchi.

"Katika sheria hiyo Bunge halina uwezo wa kubadilisha mkataba wa madini baada ya kuupitisha na viwango vya kodi vilivyopitishwa bungeni vitaendelea kubaki hivyo hivyo mpaka mwisho wa mkataba hata kama kuna mabadiliko ya serikali, " alisema Shivji ambaye alikuwa Mhadhiri wa Sheria katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kabla ya kustaafu. Pia Shivji ni Wakili Mwandamizi wa Mahakama Kuu.

Alisema sheria hiyo iliyopitishwa bungeni mwezi Augosti,1998 haitoi uwezo kwa Bunge kujadili, na kufanyia mabadiliko mikataba ya madini kulingana na mahitaji badala yake uwezo huo amepewa waziri mwenye dhamana.

"Bunge lina haki kikatiba kutunga, kujadili na kupitisha sheria, lakini haki hiyo haionekani kwenye mikataba ya madini jambo ambalo linasababisha utata katika sekta ya madini," alisema Shivji.

Alisema sheria hiyo inakiuka katiba ambayo ndio msingi wa sheria, inayowapa wabunge uwezo wa kutunga, kujadili, kushauri na kupitisha na kuzifanyia marekebisho sheria mbalimbali zinazoonekana kuwa mbovu katika kipindi fulani.

Alisema ili kuondokana na utata wa mikataba ya madini, sheria inatakiwa kuangaliwa upya na Bunge linatakiwa kupewa uwezo wa kuhoji na kuifanyia mabadiliko mikataba kabla ya muda uliwekwa kumalizika.

Alisema nguvu ya Bunge kupitisha sheria inatakiwa kuonekana kwa vitendo katika kuibadilisha sheria hiyo hasa katika kipindi ambacho linaona kuwa kuna umuhimu kufanya hivyo kwa maslahi ya umma.

Aliongeza kuwa sheria ya madini inapaswa kufanyiwa marekebisho kwa lengo la kudhibiti mikataba mibovu ya madini baina ya serikali na wawekezaji kwa faida ya umma.

Alisema ni wajibu wa Bunge kuhoji na kufanya mabadiliko ya haraka katika mikataba inayozua utata katika jamii ili kulinda amani na maslahi ya Taifa.

Alisema kitendo cha sheria ya madini kuwaondolea wabunge uwezo wa kuhoji mikataba kabla ya muda wa makubaliano ya awali na kumpa waziri mwenye dhamana kusaini makubaliano mapya na wawekezaji kinahatarisha uchumi wa nchi.

Alisema kuna haja kwa sheria hizo kufanyiwa marekebisho kwa vile ni vigumu kwa Bunge kutabiri hali ya baadaye wakati wa kupitisha mikataba kama hiyo ili kuondoa fursa ya migogoro.

Shivji alisema Watanzania bado wana nafasi ya kubadilisha sheria na mikataba mirefu ya madini ili iwe na manufaa kwao.

"Sidhani kwamba mahakama yenye wajibu wa kulinda sheria imeshindwa kubadili sheria zinazonyima uhuru wa Bunge na kulifanya lishindwe kutekeleza majukumu yake,"alisema.

Source: Mwananchi
 
kwa hiyo mkataba wa buzwagi hata wananchi wakipigia kelele ndo imetoka hiyo ama ?
 
kwa hiyo mkataba wa buzwagi hata wananchi wakipigia kelele ndo imetoka hiyo ama ?

Wananchi hawana sababu ya kuupigia 'kelele' kwani EL alishasema kuwa mkataba ni babu kubwa na JK amekwambia umelinda maslahi yetu.
 
"Sidhani kwamba mahakama yenye wajibu wa kulinda sheria imeshindwa kubadili sheria zinazonyima uhuru wa Bunge na kulifanya lishindwe kutekeleza majukumu yake,"alisema.

Wataalamu wengine wa sheria wanaweza kutusaidia ktk hili. ikiwezekana basi watu waende mahakamani kupinga sheria hii.
 
Tuanze kampeni za ngumu za One On One za kuweza kuvipa vyama vya upinzani zaidi ya 50% ya viti Bungeni ili Bunge liwe na uwezo wa kutunga sheria zinazo tufaa na kutupilia mbali sheria zinazo kumbatia Ukoloni Mamboleo.

Vyama vya upinzani vikipata viti vingi ni vema kuwapendekeza watu kama Shivji kuwa Wabunge wa taifa ili kusaidia kuweka sawa mambo ya kisheria Bungeni.
 
Back
Top Bottom