Libya
JF-Expert Member
- Nov 11, 2016
- 783
- 1,918
John Shibuda amezungumza kwenye Kongamano la maombi na maridhiano ya amani lililofanyika Mjini Dodoma. Shibuda amenukuu maneno ya baba wa taifa iliyosema 'watanzania hatuwezi kutatua matatizo yetu kwa kujidanganya hayapo' au kutumia mbinu za kifalsafa za kuyafubaza lakini yapo. Anasema Rais Magufuli alipiga msumari kwa kusema watanzania sio wajinga. Wanaweza wakakaa kimya lakini wewe unaeongea wanakupa jina 'Kubwa Jinga'.
SHIBUDA: Maneno haya najua hayana ladha tamu lakini kama una ugonjwa wa malaria, huwezi ukaondoa ugonjwa kwa ladha tamu ya machungwa lazima utumie ladha chungu ya quinine ndipo itatoka malaria. Mimi bado mdogo kwa mzee Butiku lakini nami nimesonga niko alasiri, nina deni kwa Mwenyezi Mungu nimetimize wajibu wangu alieniusia heri kujikwaa kidole kuliko kujikwaa ulimi.
Viongozi wote tujitahadhari na hatari ya kujikwaa ulimi ukawa wewe ukawa mafuta ya taa kwenye moto ukachochea ukalipuka na kutengeneza janga. Huwezi ukapata amani kama hakuna haki, mapinduzi ya Zanzibar yalisababishwa na dhulma, hapakuwa na hak, volcano likalipuka chini ya jemedari hodari mzalendo haki ikazaliwa.
Dumisheni mahubiri ya haki kwa sababu ukiwa na haki una thawabu kwa mwenyezi Mungu. Uchaguzi uwe na uwazi, ukweli na usawa ili tukamilishe dhamira njema ya mheshimiwa Rais. Usione chaelea kimeundwa, wako watu wanatafuta kiki wanaojipendekeza, wanafiki wasiokuwa na udhu katika matendo yao alafu wanasema mimi mzalendo, uzalendo gani wa jehanamu?
Naikumbusha TAMISEMI, uchaguzi wa serikali za mitaa ulichafua taswira ya Tanzania na ulimchafua Rais wetu. Kuna watu walienda maovu ya kutafsiriwa, natafuta tafsiri kwamba ni wazalendo na kinga kwa ya upendo mkubwa kwa Rais Magufuli, acheni uongo. Rais Magufuli si mnafiki na hana hulka ya unafiki. Anapenda ukweli ndio sifa na hulka yake.
Tendeni mema ya kujenga historia ya Rais Magufuli ya kujenga legacy atakayoiacha baada ya miaka 10 panapo majaaliwa. We DC unasababisha taswira potofu na nyie ndugu zangu wanaCCM mkikaa kimya inakuwa kama mmewatuma.
Kila upendacho wewe, Mwajuma sio lazima akipende. Mfumo wa vyama vingi ni ushindanishaji nguvu za hoja na ni kazi ya udobi ya kung'arisha ustawi na maendeleo ya wananchi, ni kushindanisha dawa ya kuondoa maumivu. Uchaguzi ukifika tunakwenda kuuza ubora wa dawa, niwakumbushe wanasiasa tukashindanishe utamu wa nguvu za hoja lakini na nyinyi serikali, wanasheria wana lugha zao, madaktari wana zao na wanasiasa tuna zetu.
Kitoweo bila chumvi hakuna kionjo na ukitia pilipili manga kwenye biriani ina ladha tamu na wanasiasa tuna vionjo vyetu. Tusigeuze kila atalosema mwanasiasa kwamba ni uchochezi, kwa mwanasiasa tunakwenda kushindanisha kauli mbiu zetu na kuna vijembe, chama gani hakitumii vijembe? Marehemu Komba alikuwa anaimba wapinzania wako wapi waje hapa tuwachinje, haikuwa na maana ya kuwatoa roho maana yake wachinjiwe kwa kura. Ukisema wimbo ule ni kichochezi cha kumwaga damu ni yako.
Naiomba serikali ikumbuke kwamba mfumo wa vyama vingi ulianzishwa na CCM na mimi nilikuwa ni mjumbe wa NEC tulipokuwa tukipitisha, kama mmakonde haogopi kinyago chake naomba serikali isiogope kivuli cha vyama vingi.
Niwaambie vyombo vya dola, katika siasa kuna uongo mmoja. Anaweza watu wa CCM hawakutuma vijana kwenda kuvamia chama fulani lakini watu wamevaa T-shirts za CCM aidha Tshirt za chama fulani kwenda kuchokoza CCM ili kuwachonganisha, naomba vyombo vya dola muwe makini sana na wanaoitwa kamati za ufundi za kutengeneza fitna za kisiasa.
Uchaguzi ni kaa la moto, ukikanyaga unaungua. Moto hula kuni, hakuna mtu timamu atiae miba katika njia ya kutoka na kurejea nyumbani kwake. Nimeyasema haya kwa sababu siasa za uchaguzi ni kaa la moto. Naomba kuhimiza tupendane na tuhistamiliane.