Sheria ya Ndoa: Maswali na majibu mbalimbali

JamiiForums

Official JF Response
Nov 9, 2006
6,200
4,984
Marriage Act.jpg

Maana ya ndoa

Kwa mujibu wa Sheria ya ndoa ya mwaka 1971, ndoa ni muungano wa hiari kati ya mwanamme na mwanamke unaokusudiwa kudumu kwa muda wa maisha yao.

Aina za ndoa

Kuna aina mbili za ndoa zinazotambuliwa na sheria hiyo:
1) Ndoa ya mke mmoja - hii ni ndoa ambapo mwanaume ana mke mmoja tu.
2) Ndoa ya wake wengi - hii ni ndoa ambayo mwanaume ana wake zaidi ya mmoja.

Ndoa itokanayo na dhana ya ndoa; hii ni ndoa ambayo mwanamke na mwanamme wamekaa pamoja ndani ya nyumba kama mke na mme kwa muda wa miaka miwili na kuendelea na wote wakapata hadhi ya kuwa wanandoa. Unaweza kusoma zaidi hapa > Majibu ya kisheria: Je, ni kweli mwanaume akiishi na mwanamke kwa kipindi kirefu wanakuwa wameoana? - JamiiForums

Vipengele gani vya kuzingatia ili wanaotaka kufunga ndoa wakubaliwe kisheria kufunga ndoa?

(a) Ni lazima muungano uwe wa hiari

Mume na mke wawe wameamua kuishi pamoja kwa ridhaa yao wenyewe. Hii inamaanisha kusiwe na kulazimishwa, kuhadaiwa kwa aina yoyote kwani muungano kama huo utakuwa batili kisheria. Ni kosa la jinai kushiriki katika shughuli ya ndoa ambayo mmoja wapo au wote wamelazimishwa kufunga ndoa.

(b) Muungano uwe ni kati ya mwanamke na mwanamme

Muungano wa watu wa jinsia moja hata kama ni wa hiari muungano huo hautambuliki kisheria. Pia mtu huhesabika mwanamke au mwanaume kutokana na sehemu za siri alizozaliwa nazo na siyo alizozipata baadaye.

Jamii inachukulia kuwa ndoa ni njia pekee ya kujipanua, upanukaji huku ni kwa kuzaa watoto. Kwa mantiki hiyo ili kupata watoto ni lazima ndoa iwe kati ya mwanamme na mwanamke.

(c) Muungano huo uwe unakusudiwa kuwa wa kudumu

Pamoja na kuwa mwanamke na mwanamme wameamua kuishi pamoja kwa hiari yao lakini siyo kwa kutodumu muungano huo hautambuliki kisheria kama ndoa.

Muungano ni lazima uwe wa kudumu maisha yote au kama mmoja wao amefariki au kama ndoa imekumbwa na matatizo na mahakama ikaona ni bora kutoa talaka kwa yeyote aliyefika kulalamika.

(d) Wanandoa wasiwe maharimu

Maharimu ni watu walio na mahusiano ya karibu ya damu au kindugu.

Wawili wanaoamua kufunga ndoa wasiwe na uhusiano wa karibu kindugu. Inakatazwa katika kifungu cha 14 cha Sheria ya ndoa ya mwaka 1971 mtu kuoa au kuolewa na mzazi wake, mtoto au mjukuu wake, kama ni dada yake, mama au shangazi au baba wa mjomba wake, baba au mama wa kambo na mwanaye aliyemfanya kuwa mtoto wake (adopted child).

(e) Wanandoa wawe wametimiza umri unaokubalika kisheria

Mwanamke na mwanamme wawe wametimiza miaka 18 ili kufunga ndoa.

Hata hivyo mwanamke anaweza kuolewa akiwa na umri wa chini ya miaka18 lakini sio chini ya miaka 15 kama atapata idhini ambayo hutolewa na baba na kama hayupo ni mama au kama wote wamefariki idhini itatolewa na mlezi wa binti huyo.

Kama wote wamefariki basi hatahitaji idhini.

Kuna wakati katika mazingira fulani mahakama inaweza kutoa idhini kwa binti kuolewa akiwa na miaka 14 lakini si chini ya hapo ikiwa ataonekana kwa mfano ana mimba.

Pia mwanaume anaweza kuruhusiwa na mahakama kuoa akiwa na umri wa miaka chini ya 18 lakini lakini si chini ya 16
kama ataonyesha kuelewa jukumu lake kama mtu mzima.

Lakini hii ni pale ambapo kuna tatizo kama la kumpa msichana mimba ndipo mahakama inaweza ikatoa idhini.

Hii inathibitishwa katika ombi la kuoa la Shabiri A. M Virji (1971) HCD no.407 la Mahakama Kuu ya Tanzania, mwombaji alikuwa na miaka 16 lakini alimpa mimba binti wa miaka 18.

Mahakama katika kuchunguza ombi la mvulana la kuoa ilitoa kibali kwa sababu wote wawili walipendana sana na wazazi wao hawakuwa na kipingamizi cha wao kuoana.

(f) Kusiwe na ndoa inayoendelea

Kama mwanamke ana ndoa inayoendelea na inatambulika kisheria haruhusiwi kufunga ndoa nyingine (polyandry).

Kadhalika kama mwanamme ana ndoa ya mke mmoja au kama ni mwislamu ana wake wanne tayari hataruhusiwa kufunga tena ndoa.

(g) Kusiwe na kipingamizi

Kama ndoa imezuiwa na Mahakama au halmashauri ya usuluhishi kutokana na uwezo zilizopewa na ndoa ikaendelea kufungwa kabla ya wenye kupeleka kipingamizi hawajasikilizwa au Mahakama imeshaamua ndoa hiyo isifungwe basi ndoa hiyo itakuwa ni batili.

(h) Mfungishaji ndoa kutokuwa na mamlaka

Kama wanaofunga ndoa wanajua wazi kuwa anayewafungisha ndoa hana mamlaka hayo na kwa makusudu wakakubali awafungishe ndoa basi ndoa hiyo itakuwa ni batili.

Mfungishaji ndoa ili kuwa na mamlaka anapaswa kusajiliwa na Msajili Mkuu wa Ndoa na kupewa leseni ya kufungisha ndoa.

(i) Kutokuwepo kwa wafunga ndoa

Kama ndoa imefungwa bila ya wafunga ndoa wote kuwepo basi ndoa hiyo haitambukuliwa kisheria.

Hata hivyo sheria inaruhusu ndoa kufungwa ikiwa mmoja wa wafunga ndoa hayupo, kama mfunga ndoa ambaye hayupo amewakilishwa na mtu ambaye alikuwepo wakati mfunga ndoa hayupo, alipotoa ridhaa yake ya kuoa au kuolewa.

(j) Mashahidi wa ndoa

Ili ndoa itambulike kisheria ni lazima ishuhudiwe na mashahidi wasiopungua wawili ambao wanaruhusiwa
kisheria yaani umri wao usipungue miaka 18 na wafahamu kinachosemwa na kutendeka wakati wa kufunga ndoa.

(k) Kuwa katika eda

Eda ni kipindi cha kukaa ndani kinachotolewa kwa mwanamke wa kiislamu aliyeachika katika ndoa au aliyefiwa na mumewe, ili taratibu fulani za kidini zifanyike.

Kama mwanamke ambaye ndoa ilifungwa kiislamu anaolewa wakati wa kipindi cha eda hakijaisha basi ndoa hiyo itakuwa batili. Lakini mfaruku hiyo ni pale iwapo mtalikiwa awe anafuata dini ya Kiislamu.

Kama atabadili dini baada ya kufiwa au kupewa talaka masharti ya eda hayatambana na atakuwa huru kuolewa.

Aina za ufungaji ndoa na taratibu za kufuata

Taarifa ya nia ya kuoa

Kwanza kama mwanamke na mwanamme wanataka kufunga ndoa ni wajibu taarifa ya nia ya kufunga ndoa itolewe kwa mfungishaji ndoa siku 21 kabla ya siku ya kufunga ndoa.

Taarifa hiyo ionyeshe mambo yafuatayo:-

(i) Majina kamili na umri wa wanaotaka kuoana.

(ii) Uthibitisho kwamba hakuna kipingamizi dhidi ya hiyo ndoa wanayotarajia kufunga.

(iii) Majina kamili ya wazazi wao na sehemu wanakoishi.

(iv) Hadhi ya wafunga ndoa, yaani kama ni mwanamke ifahamike kama hajaolewa, ametalakiwa au ni mjane na mwanamme pia anapaswa kama hajaoa, au ana mke au/wake wengine (hii ni kwa ndoa za kiserikali na kiislamuu) au kama ametaliki.

(v) Kama muolewaji ana umri chini ya miaka 18, jina la mtu aliyetoa idhini ya yeye kuolewa kama yupo ionyeshwe.

(vi) Kama ni ndoa ya kiserikali au kiislamuu hapana budi kueleza kama ndoa ni ya wake wengi au inatazamiwa kuwa ya wake wengi, majina ya wake waliopo yatajwe.

Pia katika fungu hili kama mtu anataka ndoa iwe ya mke mmoja anapaswa kueleza.

Baada ya taarifa yenye maelezo haya kufikishwa kwa mfungishaji ndoa yeye anawajibika kutangaza hii nia ya kufunga ndoa. Sababu ya kufanya hivyo ni ili kama kuna mwenye kipinganizi na ndoa hiyo atoe taarifa. Matangazo haya hutolewa kama ndoa inatarajiwa kufungwa kidini, sehemu za ibada.

Kama ni ndoa ya kiserikali tangazo litabandikwa nje ya ofisi ya msajili wa Ndoa ambaye ni Mkuu wa Wilaya.

Vipingamizi vya ndoa viko vya aina mbili, cha kwanza ni kile cha kisheria yaani kama ndoa itakayofungwa itakuwa batili.

Kipingamizi cha pili ni kama muoaji ana mke au wake wengine tayari, hivyo mke au wake wanaweza kutoa kipingamizi kama uwezo wa muoaji kifedha ni mdogo kiasi kwamba kuongeza mke mwingine kutazidisha shida.

Mfungishaji ndoa anapopokea taarifa ya kupinga ndoa isifungwe, ataipeleka taarifa hiyo kwenye Baraza la Usuluhishi la Ndoa. Huko aliyewekewa kipingamizi na aliyeweka wataitwa na kila mmoja atajieleza.

Baada ya kusikiliza pande zote Baraza lina uwezo wa kuamua ndoa hiyo ifungwe au isifungwe na mfungishaji ndoa atafuata uamuzi wa Baraza.

Kama mtu atatoa kipingamizi cha uongo na ikithibitika hivyo, adhabu yake anaweza kufungwa kifungo kisichozidi miaka mitatu.

Baada ya kipengele hiki kutimizwa ndoa inaweza kufungwa.

Aina za ndoa

Kama tulivyosema awali kuna aina mbili za ndoa.

(a) Ndoa ya mke mmoja

Huu ni muungano unaoruhusu mwanamme kuoa si zaidi ya mke mmoja, mfano wa aina hii ya ndoa ni ndoa ya Kikiristo.

(b) Ndoa ya zaidi ya mke mmoja

Huu ni muungano unaoruhusu mwanamme kuoa mke zaidi ya mmoja, mfano wa aina hii ya ndoa ni ndoa za Kiislamu na ndoa za kimila.

Sheria ya ndoa inatambua aina tatu za ufungaji wa ndoa yaani kiserikali, kidini na kimila. Ndoa hizo zaweza kufungwa kwa kufuata taratibu za kidini au za kiserikali. Utaratibu huo utafuata au kuzingatia kama wanandoa ni waumini wa dhehebu
fulani au la.

(a) Ndoa ya kidini

Ndoa hii hufungwa kwa mujibu wa taratibu ya dini husika hivyo ni lazima masharti yote yatimizwe kisheria na taarifa ya nia ya kufunga ndoa itolewe na ndoa ifungiwe mahali pa wazi panapokubalika kisheria na mfungishaji awe na mamlaka hayo kisheria.

(b) Ndoa ya kiserikali

Ndoa hii hufungwa mbele ya Mkuu wa Wilaya ambaye ndiye Msajili wa Ndoa.

Ndoa itafungwa katika ofisi ya Msajili au mahali pengine popote palipotajwa katika leseni yake ya kufungisha ndoa.

(c ) Ndoa ya kimila

Ndoa inaweza kufungwa kimila iwapo mmoja wa wafunga ndoa au wote wawili wanafuata sheria za mila za kabila fulani ambapo mwandishi wa ndoa za kimila ni Katibu Tarafa.

Ndoa ya kimila hufungishwa na mtu anayetambulika kimila kuwa ana uwezo huo.

Ni muhimu sana Katibu Tarafa kuhudhuria kwenye ufungishaji huo wa ndoa kwani ndiye atakayehusika na kuleta vyeti vya ndoa kutoka kwa msajili.

Ufungaji ndoa nje ya nchi

Kifungu cha 8 cha sheria kinampa mamlaka Waziri wa Sheria kuteua baadhi ya maofisa ubalozi kuwa wasajili wa ndoa.

Ni lazima msajili aridhike kuwa masharti yote yametimizwa ndipo afungishe ndoa.

Kuna masharti ya nyongeza kama angalau mmoja wa wafunga ndoa awe ni Mtanzania. Pia kama mmoja wa wafunga ndoa si Mtanzania ni lazima Msajili aridhike kuwa ndoa inayokusudiwa kufungwa itatambulika kisheria katika nchi ambayo huyo mmoja wa wafunga ndoa ni mkazi.

Utaratibu unaotumika kufungisha ndoa hizi ni sawa na ule unaotumika katika kufungisha ndoa za kiserikali.

Dhana ya kuchukulia ndoa

Kuna dhana inayokanushika (rebuttable presumption) kuwa mwanamme na mwanamke wakiishi pamoja kwa miaka miwili au zaidi huchukuliwa kuwa ni mke na mume mbele ya sheria japokuwa hawakuwahi kufunga ndoa. Dhana hii imeelezwa katika kifungu cha 160 cha Sheria ya Ndoa.

Ili dhana hii iwepo ni lazima yafuatayo yathibitishwe:-

(i) Lazima ithibitike kwamba mwanamke na mwanamme wameishi pamoja kwa muda wa miaka miwili au zaidi kwa mfululizo.

(ii) Lazima pia ithibitike kuwa umma unaowazunguka unawachukulia na kuwapa heshima kama mke na mume.

(iii) Lazima ithibitishwe kuwa watu hao walikuwa na uwezo wa kuwa mke na mume wakati walipoanza kuishi pamoja kama
umri ulikubalika kisheria.

(iv) Ni lazima pia ithibitishwe kuwa kati ya hao wawili au wote hakuna aliye na ndoa inayoendelea.

Ndoa batili na sababu zinazoweza kuifanya ndoa kuwa batili

Ndoa batili ni ndoa ambayo itachukuliwa kisheria kuwa ni ndoa halali hadi hapo amri ya kuivunja itakapotolewa.

Ndoa batili ni halali kama ndoa nyingine isipokuwa ina kasoro fulani. Wanandoa katika ndoa hiyo wana haki na wajibu sawa kama ilivyo katika ndoa nyingine zisizo na kasoro. Kadhalika watoto waliozaliwa katika ndoa ya namna hii ni halali
na wana haki zote kisheria.

Ni vitu gani vinavyofanya ndoa kuwa batili?

1. Maradhi ya zinaa

Kama wakati wa kufunga ndoa mmoja wa wafunga ndoa alikuwa na maradhi ya zinaa na yule asiye na ugonjwa kama wakati wa kufunga ndoa alikuwa hajui lolote anaweza kulalamika mahakamani na ndoa ikavunjwa.

2. Kukataa makusudi kutimiza ndoa

Kama baada ya kufunga ndoa mmoja wa wafunga ndoa atakataa kuitimiliza ndoa anayekataliwa ana haki ya kuiomba mahakama kuvunja ndoa hiyo.

Maingiliano yanayotambulika kisheria ni yale yanayofanyika siku ya ndoa na kuendelea na siyo kabla ya ndoa.

Kukataa kuitimia ndoa kunakuwa sababu ya kubatilisha ndoa ikiwa mwenye kukataa hana sababu yoyote ya msingi na mwenye kukataliwa ametumia kila mbinu kumshawishi aliyekataa lakini ikashindikana kufanya tendo la ndoa.

3. Mimba ya mwanamme mwengine

Kama wakati wa kufunga ndoa mke atathibitika ana mimba aliyopata kwa mwanamme mwingine, mume anaweza kuiomba mahakama ivunje ndoa hiyo.

Kama itathibitika kuwa mume alijua hivyo hali wakati wa kufunga ndoa, lalamiko lake halitasikilizwa.

4. Wazimu au kifafa cha kipindi

Mmoja wa wafunga ndoa kama ana wazimu au kifafa cha kurudia rudia na mwenzake alikuwa hajui hilo hali wakati wa kufunga ndoa, atakuwa na haki ya kuiomba mahakama kuivunja ndoa hiyo.

Ieleweke kuwa ugonjwa ni lazima uwe unarudia rudia na siyo mtu awe aliugua na akapona.

5. Kushindwa kutimiza ndoa

Kama mmoja wa wafunga ndoa atashindwa kuitimiliza ndoa basi ndoa hiyo inaweza kubatilishwa.

Kwa mwanamme kama anashindwa kuitimiliza ndoa kwa sababu ya kukosa nguvu za kiume basi ana haki ya
kuiomba mahakama kuibatilisha ndoa. Ili kukosa nguvu za kiume kuwe sababu ya kubatilisha ndoa ni lazima ithibitike kuwa hali hiyo ilitokea kabla au wakati wa kufunga ndoa na siyo baada ya kufunga ndoa wakati kitendo cha kuitimiliza ndoa kilishafanyika.

Ili ndoa iweze kubatilika ni lazima kukosa nguvu huko kuthibitishwe na daktari kuwa hakuponi au kunapona lakini mwanamme hataki matibabu.

Mwanamke anaweza kuwa na maumbile ambayo yanaweza kufanya ndoa ishindwe kutimilizika.

Ikithibitika hali hiyo lakini mwanamke hataki tiba mwanamme anaweza kuomba mahakamani ndoa kubatilishwa.

Ili mahakama iweze kusikiliza shauri la kuomba kubatilisha ndoa ni lazima shauri hilo lipelekwe haraka.

Kama shauri litakwenda mahakamani baada ya mwaka mmoja tangu tarehe ya ndoa Mahakama haitalipokea.

Pia ni lazima ithibitike kuwa mlalamikaji alikuwa hajui kasoro hiyo wakati wa kufunga ndoa na baada ya kuigundua kasoro hiyo hajawahi kuingiliana na mwenzie mwenye kasoro hiyo.

Ndoa batili huvunjwa na mahakama pekee baada ya kupokea malalamiko toka kwa mmoja wa wanandoa.

Kama hakutakuwa na malalamiko yatakayopelekwa mahakamani na anayedhurika na kasoro hizo, ndoa hiyo itadumu ama labda mmoja afariki au kama kuna talaka itatolewa na mahakama.

Watu waliooana wana uhuru wa kugeuza ndoa yao kuwa ya mke mmoja au ya wake wengi pale wanapofuata taratibu zinazokubalika kisheria.

Kabla ya kufanya uamuzi wa kugeuza ndoa ni hapanabudi wanandoa wakubaliane kuhusu uamuzi huo.

Kitendo cha kugeuza ndoa hufanywa mbele ya Hakimu wa Wilaya au Jaji ambapo wanandoa watatoa tamko la maandishi lenye saini zao na Hakimu au Jaji aliyeshuhudia naye hutia sahihi yake.

Katika kugeuza ndoa, ndoa ya kiserikali ya kienyeji au ya Kiislamu inaweza kugeuzwa kuwa ya mke mmoja kama kabla ya kugeuza hizi zinaweza kugeuzwa kuwa ya wake wengi.

Ikumbukwe kuwa kubadilisha dini pekee hakubadilishi hadhi ya ndoa.

Vilevile ndoa ya kikristo haiweza kugeuzwa kuwa ya wake wengi wala ndoa ya wake wengi inayodumu kuwa ya mke mmoja.
Talaka na taratibu zake. Talaka ni ruhusa au amri ya mahakama ya kisheria ambayo mume au mke hupewa wakati anapomwacha mwenzake.

Chombo chenye mamlaka ya kutoa talaka ni mahakama tu. Mahakama hiyo itatoa talaka kwa ndoa ambayo imedumu kwa muda wa miaka miwili au zaidi.

Mahakama inaweza kutoa talaka kwa ndoa ambayo haijafikisha muda huo endapo mlalalmikaji atatoa sababu za msingi mahakamani.

Kutengana

Kutengana si talaka, kutengana maana yake ni hali ambayo mke na mume hukaa mbalimbali.

Kukaa mbalimbali au kutengana kwaweza kuwa kwa mapatano kati ya wanandoa hao au kutengana kwaweza kuwa kwa amri ya mahakama.

Mahakama itatoa amri hiyo endapo mmoja wao atapeleka maombi mahakamani.

Faida ya kutengana wote au mmoja wao waweza au aweza kutambua makosa na baadaye kukata shauri kurudiana au kuishi tena. Kutengana kwa mapatano, ni kutengana kwa hiari yao wenyewe bila shuruti, mapatano hayo yaweza kuwa ya maandishi au ya mdomo.

Mambo kadha yaweza kuzingatiwa wakati wa makubaliano kama; heshima kwa kila mmoja, matumizi au matunzo,watoto kama wapo watakaa na nani, mali ya pamoja je itatunzwa namna gani na kutobughudhiana.

Kutengana kwa amri ya mahakama, hii ni hali ya mume na mke kutengana kwa amri ya mahakama na mahakama imeridhika kuwa ndoa imevunjika.

Ushahidi wa kuwa ndoa imevunjika ni ushahidi ambao unaweza kutolewa mbele ya mahakama kunapokuwepo na maombi au shauri la talaka.

Sababu za kutoa talaka mahakamani

Kabla ya kupeleka shauri au maombi mahakamani ya talaka, mwanandoa husika hana budi kufuata au kuzingatia hatua zifuatazo;

a) Kufungua au kupeleka malalamiko kwenye Baraza la Usuluhishi la Ndoa kwa mfano BAKWATA, Kanisani, Ustawi wa Jamii au Baraza la Kata.

b) Baraza litasikiliza, na endapo litashindwa mapatano au muafaka kati ya wanandoa hao, basi baraza litatoa cheti ambacho kitaeleza kuwa limeshindwa kusuluhisha mgogoro wa ndoa na kuomba mahakama kuendelea kutoa talaka.

c) Baada ya mwanadoa mmoja kupata cheti hicho basi atatakiwa atayarishe madai ya
talaka akionyesha kuwa kulikuwa na ;- ndoa halali, kuna mgogoro kati yao, watoto, mali walizochuma wakati wa ndoa yao,.

Muombaji huyo ataiomba mahakama hiyo itoe amri ya talaka, mgawanyo wa mali zilizochumwa kwa nguvu za pamoja, mamlaka ya kukaa na watoto na matunzo yao, gharama za madai au shauri.

Ili mahakama itoe talaka sababu kadha huangaliwa na mahakama.

Sababu hizo ni mambo ambayo yatakayofanya ndoa ionekane kuwa imevunjika kiasi kwamba haiwezi kurekebishika tena, mambo hayo ni kama ifuatavyo;

a) Ugoni; hii ni zinaa ambayo hufanywa na mwanaume na mwanamke ambao hawajaoana.

Hii hutokea ambapo mwanamme ana mke wake au mwanamke ana mume wake, hivyo mmoja wapo anamwacha mke/mume na kufanya zinaa na mtu mwingine.

b) Ukatili; ukatili ni kuumiza nafsi nyingine, kuharibu mwili au kuwa na hofu ya kuumizwa.

c) Kulawiti; kulawiti ni kumwingilia mtu kinyume na maumbile,

d) Kichaa; ni kutokuwa na akili timamu, na hali hii lazima iwe imethibitishwa na madaktari bingwa wa akili.

e) Kuzembea wajibu kwa makusudi; haya ni majukumu ya mume, majukumu hayo ni kama haya; kumtunza mke kwa kumpa chakula, malazi na mavazi.

f) Uasi; ni hali ya mke au mume kuhama nyumba ya ndoa na kwenda kuishi mahala pengine bila sababu yoyote ya msingi,

g) Kutengana; kukaa mbalimbali kwa mume na mke kwa muda wa miaka isiyo pungua mitatu, kutengana kwao ni sababu tosha ya talaka.

h) Dhana ya kifo; hii ni hali ambayo mmoja wa wana ndoa amekufa, na hii hutokea iwapo mojawapo hataonekana / ametoroka kwa muda mrefu, kama miaka 5, hapo mahakama hutoa tangazo kuwa fulani amekufa.

i) Kifungo; hii ni hali ambayo mume au mke ametenda kosa la jinai na ametiwa hatiani na mahakama imemfunga miaka 5 au maisha basi mahakama inaweza kutoa talaka kwa mwombaji.

j) Tofauti za imani za kidini, endapo mwanandoa mmoja atabadili dini basi ni sababu tosha ya kuomba
mahakama ivunje ndoa na kutoa talaka.

Haki na wajibu katika ndoa

Baada ya kufunga ndoa na ikaonekana haina kasoro yoyote, mke ana haki mbalimbali kisheria anazostahili
kuzipata.

Haki hizi ni kama:- Matunzo; mke au wake wana haki ya kutunzwa na mume wao kwa kuwapatia mahitaji muhimu kama
chakula, malazi, mavazi, matibabu, n.k kulingana na uwezo alionao mume.

- Kumiliki mali; mke ana haki ya kumiliki mali aliyoipata kabla na baada ya ndoa kama aliipata kwa fedha yake mwenyewe.

- Mke ana haki ya kuingia mikataba, kushitaki na kushitakiwa.

- Makubaliano yaweza kufanywa na wanandoa hiyo jinsi ya kumiliki mali iliyopatikana kabla ya ndoa yao jinsi gani waimiliki. Kwa mali iliyopatikana wakati wa ndoa, mali hiyo ni mali ya wanandoa wote, kwa sababu imepatikana kwa mchango wa nguvu za pamoja.

Hii haijalishi kuwa mmoja wa wanandoa (mke) hachangii pesa tasilimu au anakaa nyumbani na kufanya shughuli za nyumbani tu. Kufanya shughuli za nyumbani ni mchango mkubwa na ameokoa fedha nyingi. Umiliki wa mali kwa wanandoa haujalishi kuwa mmoja wapo amemiliki mali hiyo kwa jina lake au la.

Haki ya kukopa kwa dhamana ya mume; jukumu la kutunza mke na watoto ni jukumu la mume au baba. Kwa msingi huo, endapo baba amesafiri, au ametoroka na baadaye matatizo yakajitokeza yanayohitaji fedha, basi mke ana haki ya kukopa fedha kwa jina la mume au kuweka rehani mali yamumewe.

- Haki ya kuishi katika nyumba ya ndoa;
Nyumba ya ndoa ni nyumba ambayo mke na mume wanaishi wakati wa ndoa. Hata kama wanandoa wana nyumba nyingi, basi wanayoishi au kutumia kama makazi ndiyo nyumba ya wanandoa.

Nyumba hii haiwezi kuuzwa, kuweka rehani au kuchukuliwa na mtu mwingine kama zawadi bila ya makubaliano ya wanandoa wote.(bila ridhaa ya wanandoa).

Mwanandoa ana haki ya kuishi kwenye nyumba hiyo mpaka amri ya mahakama ya kuvunja ndoa, au kutengana itakapotolewa.

Talaka kisheria

Neno talaka linaweza kuwa mojawapo ya maneno yaliyozoeleka midomoni au masikioni mwa watu wengi katika ulimwengu wa sasa.

Kwa lugha nyepesi, talaka ni kitendo cha wanandoa kuachana na mahusiano ya kindoa yaliyokuwa baina yao.
Lakini kisheria, ingawa maana ya talaka inaakisiwa na maana hii ya Kiswahili, lakini katika maana ya sheria kuna mambo mengine zaidi ya kuzingatia.

Tafsiri ya sheria ya ndoa ya Tanzania, sura ya 29 ya marekebisho ya sheria ya mwaka 2002, talaka ni kitendo cha mahakama yenye mamlaka katika shauri linalohusika, kutoa tamko la kuivunja ndoa iliyokuwapo, kwa sababu mbalimbali.
Hivyo, tukiangalia kwa mtazamo wa kihistoria, ndoa kwa mujibu wa sheria ya Kiingereza (common law) ambayo imeakisiwa sana na sheria ya ndoa ya Tanzania, ilikuwa haitambui sababu ya aina yeyote katika kuivunja ndoa kwa msingi wa talaka.
Lakini baada ya miaka mingi kupita, sheria ya talaka ilianza kutumika nchini Uingereza baada ya sababu kadhaa za kisheria za kuvunja ndoa kwa talaka kuanzishwa.

Sheria ya Talaka (The Divorce Act) ya mwaka 1969 ilianzishwa nchini Uingereza kufuatia ripoti ya askofu Kent wa nchini humo.

Mwaka mmoja baadaye yaani mwaka 1969 serikali ya Tanzania kupitia tamko la serikali (Government Notice) namba 1 ya mwaka huo, iliyojulikana kama White Paper ilichukua msimamo na mtazamo huu wa sheria ya Kiingereza juu ya talaka.
Hadi mwaka 1971 tulipochukua msimamo huu wa sheria ya Uingereza juu ya talaka, mabadiliko makubwa ya kimsingi ya sheria juu ya talaka yalitokea katika sheria yetu hapa nchini nayo ni pamoja na kuwa na sababu moja tu inayoweza kuifanya ndoa kuvunjwa na mahakama kwa tamko la talaka, sababu hiyo ni kuwa mahakama itakapothibitisha kwamba ndoa hiyo imevunjika kabisa na haiwezi kurekebishika kutokana na kasoro zisizo weza kurekebishika.

Hivyo, sheria ya Tanzania katika hili nayo ikachukua sababu moja inayoweza kuifanya ndoa kuvunjwa na talaka.
Hata hivyo, wakati tunaangalia sheria hii, tunatakiwa kujua kwamba sababu moja ya kuivunja ndoa kwa talaka ipo Tanzania bara pekee.

Baadhi ya watu wanadhani sababu za kuvunja ndoa ni zile zinazoelezewa na sheria hii kama hali au mazingira ya kuthibitisha kwamba ndoa hiyo ina tofauti zisizorekebishika.

Sababu hizo ni pamoja na uzinifu nje ya ndoa, ukatili pamoja na kumkimbia/kumtelekeza mwanandoa mwezako. Uzinifu ni mojawapo ya sababu zinazoipa mahakama mamlaka kisheria kuivunja ndoa yoyote. Hata hivyo, unatakiwa kujua uzinifu una maana nyingi kutegemea na eneo husika.

Kimsingi uzinifu ni kitendo cha mwanandoa mmoja kufanya ngono nje ya mahusiano yake ya ndoa iliyo halalishwa.
Hapa katika kuondokana na wasiawasi wa kuweza kushindwa kuthibitisha uzinifu, sheria imetoa dhana kwamba pale tu itakapokutwa mume na mke wamelala pamoja na wako watupu, basi dhana hapa ni kwamba wametoka au wanataka kufanya ngono.

Dhana hii kama ilivyoanzishwa na mahakama katika shauri la Denise dhidi ya Denise, Jaji Single anasisitiza kwamba dhana hii ni ngumu kuipinga isipokuwa kama itathibitika kwamba mwanaume aliyekutwa ni hanithi au mwanamke huyo ni bikira.
Na uthibitisho wa uzinifu nje ya ndoa ni kama uthibitisho wa katika kesi ya jinai ambapo anayelalamika anatakiwa kuithibitishia mahakama pasi na shaka kwamba uzinifu umetokea.

Kwa upande wa Uingereza, kama itathibitika kwamba kulikuwa na uzinifu na kwamba mtoto alizaliwa nje ya ndoa, pia atahesabika ni mtoto haramu na hivyo kukosa haki zake zote kwa mzazi wake wa pili.

Hata hivyo, mara nyingi uzinifu unaweza kuthibitishwa na ushahidi wa mazingira kama vile mmoja wa wanandoa kuwa na ugonjwa wa zinaa na kadhalika.

Kifungu cha 170(2) cha sheria ya ndoa ya Tanzania, kinatoa maelekezo juu ya ushahidi wa aina hii.

Hata hivyo, uzinifu si lazima uwe sababu ya mahakama kutoa talaka. Mahakama kwa kuzingatia mazingira ya kesi husika inaweza kuamuru mtu aliyefanya uzinifu na mmoja wa wanandoa kumlipa fidia muathirika wa uzinifu huo.

Ukatili pia ni sababu mojawapo ya sababu zinazoweza kuithibitishia mahakama kwamba ndoa hii ina kasoro zisizoweza kurekebishika.

Kuharamisha, kubatilisha ndoa katika Sheria ya Ndoa

NENO kuharamisha ni la kawaida katika lugha ya Kiswahili ambalo linalotokana na neno ‘haramu’ likimaanisha kitu kisichofaa, kwa maana iliyo nyepesi.

Aidha kuharamisha ndoa kisheria ni kitendo cha mahakama kutoa tamko kwamba ndoa ambayo iliyodhaniwa kuwa imefungwa haikufungwa wala haikuwapo.

Hapa tunatakiwa tujue mantiki ya kitendo hiki ni kuharamisha (nullify) ndoa ambayo ilidhaniwa ni halali wakati wa kufungwa, lakini kumbe katika jicho la sheria ndoa hiyo “haipo na wala haikuwahi kuwapo”.

Hii siyo talaka kama ambavyo watu wengine wanaweza kufikiri. Somo la talaka tutalizungumzia baadae katika makala nyingine.

Kama ambavyo nadharia nyingi za sheria zetu zimetoka katika sheria za mahakama za nchini Uingereza, yaani Common law, nadharia hii imetoka huko huko, wakati wa mageuzi baada ya kuanguka kwa dola ya utawala wa kifalme wa Kirumi huko Ulaya.

Wakati wa utawala wa kirumi huko Ulaya, sheria za Kanisa Katoliki zilikuwa zinatumika kwa kiwango kikubwa, imani na mafundisho ya Kanisa Katoliki ndoa ni Sakramenti iliyoanzishwa na Mwenyezi Mungu.

Hii ilikuwa na maana kuwa ndoa ni takatifu hivyo talaka ni kitu ambacho hakitambuliki katika sheria za Kanisa, kusisitiza maneno ya bwana Yesu katika Injili ya Marko 10:7-8 kwamba mwanaume na mwanamke wakiungana wanakuwa mwili mmoja na kwamba alichokiunganisha Mungu mwanadamu yeyote asikitenganishe.

Kwa mantiki hiyo, njia pekee ya watu kutoka ndani ya ndoa wakati huo ilikuwa ni kuiharamisha na si talaka, kwani ilikuwa haitambuliki kama tulivyoona hapo awali. Baada ya kuanguka kwa dola ya Rumi huko Ulaya, tawala za kifalme zikawa maarufu sehemu nyingi huko Ulaya na kusababisha sheria za kanisa (Canon law) kupotea na kwa upande wa Uingereza, sheria za mahakama za Uingereza yaani Common law zikashika kasi.

Hivyo basi athari ya sheria hizi za mahakama za Uingereza ilikuwa ni pamoja na kuleta mafundisho mengine ikiwemo kuanzisha upya talaka.

Kwa Tanzania, vifungu vya 39 na 49 vya Sheria ya Ndoa, 1971; vinaelezea njia mbili kuu za kuharamisha ndoa. Njia hizi ni zile ambazo ikithibitika mahakamani, basi mahakama itatoa tamko la kuharamisha ndoa.

Njia hizi ni pamoja na ndoa haramu (void marriage) na ndoa isiyo haramu lakini pia si halali kwa kuwa imekosa mahitaji kadhaa ya kisheria yaani ndoa batili (voidable marriage).

Kwa ndoa haramu, hii ni ndoa ambayo tangu mwanzo ilikuwa ni haramu katika jicho la sheria; wakati aina ya pili ya ndoa isiyo haramu ila imekosa kutimiza masharti kadhaa ya kisheria kuifanya iwe halali na hivyo kuifanya batili.

Kwa mfano kwa mwanamme asieweza kufanya tendo la ndoa na mkewe, ndoa yake itakuwa batili kama mkewe atakwenda mahakamani kuomba ndoa yake ibatilishwe kwa kuwa mumewe hawezi kufanya tendo hilo ambalo ni hitaji la kisheria ili ndoa iwe halali; lakini kama mwanamke huyo atavumilia hali hiyo, ndoa yao itakuwa ni halali.

Hivyo basi, kwa mujibu wa kifungu cha 39 na 49 vya Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971, kuna sababu mbalimbali ambazo zinaweza kusababisha ndoa isiwe halali, kwa sababu hizo mume au mke anaweza kuomba mahakama itoe tamko la kubatilisha ndoa yake.

Kwa wanandoa kushindwa kufanya tendo la ndoa wakati wameoana, kwa mujibu wa kifungu cha 39(e) cha Sheria hii, pindi mwanandoa yeyote (mwanamme au mwanamke) wakati wameshafunga ndoa na mwenzake atashindwa kufanya tendo la ndoa hiyo itakuwa sababu kwa mmojawapo kuomba tamko la kubatilisha ndoa hiyo.

Huu pia ni uamuzi uliotolewa katika shauri la Dralge dhidi ya Dralge , (1947)1 All.ER 29), la nchini Uingereza,ambapo mahakama ilitafsiri kimantiki kwamba tendo la ndoa ndilo haswa linalomaanishwa katika kile ambacho kifungu cha 39 cha Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971.


Kwa MASWALI na MAJIBU, fuatilia kuanzia post ya 2 katika thread hii. Pia, kwa ufafanuzi zaidi wa kisheria, soma viambatanishi katika PDF format kwenye bandiko hili

Pia, unashauriwa kusoma:

1) Ijue Sheria: Mke asiye wa Ndoa na Mtoto wa nje ya Ndoa hawarithi Kisheria - JamiiForums

2) Sheria ya ndoa: Mke ana wajibu wa kumtunza mume akiyumba kiuchumi - JamiiForums

3) Kuvunja ahadi ya kuoa au kuolewa: Sheria inasemaje? - JamiiForums

4) Unajua sheria ya ndoa inaruhusu watoto wa miaka 14 kuoana? - JamiiForums

5) Je, mwanaume anaweza kumbaka mke wake wa ndoa? - JamiiForums
 

Attachments

  • SHERIA YA NDOA-Kwa UFUPI.pdf
    181 KB · Views: 160
  • sheria_ya_ndoa_na_mirathi.pdf
    325.4 KB · Views: 179
  • Sheria-ya-Ndoa-na-Talaka-Tanzania.pdf
    1.1 MB · Views: 186
Salaam,

Kuna kipengele katika sheria ya ndoa kinachosema kua pindi ndoa inapovunjika Mtoto atakaa kwa mama yake mpaka afikishe miaka saba then baba anaweza kumchukua.

Sasa kuna rafiki yangu mmoja ana experience hii kitu so kwa maoni yake anasema hii sheria inabidi ibadilishwe kwani unakuta mtu unaingia gharama kubwa kumtunza mtoto akiwa kwa mama yake na pili kuna wazazi wengine ndo wanafanya mtoto kama fimbo ya kukukomoa.

Sasa kwa maoni yake anaona kipengele hiki kibadilishe kiweze kusomeke kua "ikiwa kama baba ana uwezo basi aruhusiwe kumchukua mtoto pindi tu amalizapo kunyonya na sio baada ya miaka saba! Wandugu hapo mnasemaje?

BAADHI YA MASWALI YA WADAU WENGINE

Msaada wa kisheria jamani. Nina mke tumetengana zaid ya miaka miwili. tulioana 2008 na tuna mtoto mmoja. Hatukubahatika kuwa na maelewano mazuri kwani kwao wana jeuri, pesa na mali nyingi nami sina elimu wanayohitaji mume wa mtoto wao awe nayo.

Mwez mmoja baada ya ndoa mke aliniaga anaenda Nje kusoma. sikumuelewa na alichokifanya ni kuondoka bila kuaga na akaacha pete ya uchumba na ndoa mezani.

Amerudi nimempeleka baraza la usuruhish ili tutengane rasmi.kwa sasa kesi iko mahakaman. nimempa kila kitu cha ndan. nimebaki na kitanda tu ila bado anadai kibanda changu (nyumba) iuzwe tugawane sawa. ukweli nyumba alinikuta nayo naye hakua na kazi ila kilicho ongezeka ni umeme na maji tu navyo niliuweka kipindi hayupo.

Hapo haki ikoje? na naskia fununu kwamba baba mkwe ndo anataka kuinunua ili anikomeshe. Naombeni Msaada wa kisheria wanajamii wenzangu mtoto yupo kwao ila napeleka pesa ya matunzo kila mwezi.
======
Nianze kueleza kifupi

Niliajiriwa miaka kadhaa hapo nyuma na wakati naajiriwa nilikuwa desperate na ndoa hivyo nilipofika kazini tu 1st date yangu nikaamua kuishi nae.

Baada ya muda nikaona kukaa na mtoto wa watu kimya sio vizuri nikaamua kwenda kumlipia mahari. Baada ya kumlipia akaanza kuforce ndoa(cheti). Mwanzoni sikujua nia yake hivyo nikaridhia tukafunga ndoa(kupewa cheti serikali) tukiwa mimi na yeye na rafiki yangu na mpenzi wake.

Aisee baada ya kupata cheti hapo ndo matatizo yalipoanzia (siwezi kusema hapa mapungufu ya mwenzangu maana hata mimi pia na mapungufu) but ndoa ilikuwa chungu(nilichukua mkopo kufanya biashara but haikwenda vizuri ikafa so mke akawa na mshahara mkubwa zaid yangu).

Hali ilikuwa mbaya sana kwangu mpaka ikafika hatua nikaamua kuacha kazi na kila kitu nikamwachia na kuja Dar kuanza moja maisha. Kwa bahati nzuri Mungu akanijalia hapa mjini. Ingawa mwanzo hali ilikuwa ngumu zaidi ya ugumu wa kawaida kulala na kula ilikuwa mtihani kwelikweli but nikaanza kufanikiwa taratibu.

Mpaka sasa naweza sema nimepata vitu viwili vitatu(biashara/nyumba kadhaa na usafiri). Sasa huku nina binti nilianzisha nae mahusiano na amekuwa bora sana kwangu kwa ushauri na kunijali.

Yule mke aliyeko mkoani nimekuwa nikitunza mtoto kwa juhudi zote hivyo kwenye hilo hana malalamiko kabisa.

Juzijuzi ameanzisha maada ya talaka anataka kuwa huru na mimi nikaona ni jambo jema ili na me nimuoe huyu niliyenae.

Tatizo mahakama imeandika muda wa talaka ambao mimi sitakuwa nchini hivyo siwezi kwenda. Yule mke kashauri niandike barua ya kupokea wito wa mahakama na pia kuruhusu aendelee na process ya talaka iendelee huku nikikubali kutunza mtoto kwa maandishi na amedai mahakamni ndio wamemshauri hivyo(kwenye mabaraza ya usuluhishi alitoa pesa barua zake zikapita).

Swali langu ni je kisheria ni sahihi kesi inavyoenda bila uwepo wangu? Mahakama itatoa hukumu?

Swali la pili kwenye mali; kila kitu tulichopata wakati naishi nae nilipoondoka nilimuachia vyote. Hizi nilizonazo sijachuma nae bora hata huyu dada niliyenae aseme tumechuma wote ila yule hana hata 10 aliyochangia hapa. Swali ni je hizi mali zangu za sasa zitahesabika kwenye talaka?(nimejaribu kumdadis akadai hana shida nazo)

Naomba wataalam wa sheria wanipe ushauri.
======
Naomba kama kuna watu humu ndani wanazijua sheria zinazohusu talaka hapa Tanzania wanifafanulie kidogo.

Je, kuna sheria moja kuhusu mgawanyo wa mali kwa ndoa zote, I mean za Kiislam, Kikristo na za serikali?

Je, kuna sheria kuhusu pre nuptial agreement?

Je, watu wakiwa wa dini tofauti mali zinagawanywa vipi?

Je, mtu akiwa mfano ana kampuni yenye thamani ya milioni kumi na akafunga ndoa,na akaja kuachana na mwenzie wakati mali zimekuwa bilioni kumi kwa mfano?

Je, mali zinagawanywa vipi?

Wanaojua wanieleweshe.
======
Habari zenu wadau,

Kuna kaka angu amefikia kikomo cha uvumilivu kwenye ndoa yake (ya Kiksristo) na ameamua kuivunja. Hajui taratibu za kufuata ili afanikiwe kutoa talaka. Msaada please kwa waijuao sheria.
=====
Labda mme ameoa na wamekaa wote na kuzaa watoto lakini mke amekuwa chanzo cha kutoelewana ndani ya ndoa kwa miaka, na ugomvi husioisha ukianzishwa na mke na mme akaamua kukaa naye bila mahusiano kwa miaka 5 na hataki kwenda mahamakani, je anaweza kuoa mke mwingine akiwa ndani ya inactive marriage hiyo? Je, Mke wake halali akikataa kuruhusu ndoa hiyo mpya kuna sheria itamzuia mme kuoa kwa kutumia lazima?
======
Je, Sheria ya ndoa inazungumziaje mambo ya pre-nup na post-nup?

Je, hiyo sheria ya ndoa inaruhusu ubatilishwaji wa ndoa?

Kama inaruhusu, ni mazingira au hali gani ndo zaweza kusababisha ndoa kubatilishwa?

Na ni kwa baada ya muda gani, baada ya ndoa kufungwa, ndo inaweza kubatilishwa?


BAADHI YA MAJIBU YA WADAU
Ili mahakama ivunje ndoa lazima mmepitia baraza la usuluhishi la ndoa (marriage conciliation board) ikashindikana kusuluhisha ndoa..kutoka kwenye baraza la usuluhishi mtapewa certificate kwamba usuluhishi umefeli kwahyo muende mahamakani.

Mahakama ktk kuvunja ndoa inakuwa inaongozwa na sheria ya ndoa ya Mwaka 1973 japo kuna revised edition ya 2002 ambayo inasema ndoa mpk ivunjwe n lazima iwe imefikia hatua ambayo haiwezi kurekebishika(the marriage has broken down irreperably) kumaanisha mmeenda usuluhishi wa bodi imeshndkana na mnaweza pewa separation period Kwa muda almost miaka 2 muangalie km mtaweza kusuluhisha.

Vyote vikishindikana basi mtafile petition for divorce itasikilizwa then ndoa itavunjwa na kubaki kuangalia mambo mengine kama division of matrimonial asset and custody of the children yani mgawanyo wa mali na matunzo ya watoto kama wapo.
======
Nimeona sana huku watu wameandika "Baraza la kata" sijaelewa kabisa limehusikaje Sheria ya ndoa imetaja Marriage conciliatory board na kwa uelewa wangu zipo ustawi wa jamii, makanisani kwa wakristu na bakwata kwa waislamu. Anyway ngoja niendelee. Hakuna ndoa ambayo haivunjiki; narudia "HAKUNA" nitachambua kwa muktadha ufuatao

CHRISTIANITY

"alichounganisha Mungu mwanadamu asitenganishe" ndio lakini Mungu anapenda usafi/utakatifu hivyo basi ndoa yaweza kuvunjwa endapo yoyote Kati ya haya likitokea, uhusiano wa kindugu mf. baada ya kuona ikagundulika nyie ni ndugu au mna uhusiano wa damu basi hiyo ndoa ni batili naitavunjwa. Mwenzako akibadilisha dini na mwisho uasherati.

MUSLIM

"talaka ni mojawapo ya halali zinazo mchukiza Allah" hivyo basi talaka ni halali kw mujibu wa waislam

KIMILA

hili pia halina utata ndoa zinavunjwa tu

BOMANI/KISERIKALI

ndio ndo zinavunjwa

TARATIBU za KUFATA

ili ndo ivunjwe kisheria yafuatayo ni muhimu:

1. Muwe mmeishi pamoja kwa muda usiopungia Miaka miwili (though kuna exception)

2. Cruelity/unyanyasaji/mateso yawezakuwa physical or mental mf. kipigo, kunyimwa chakula na tendo la ndoa au kulawitiwa

3. Adultry/ uzinzi

4. Desertion/kutelekezwa

Iwapo yote au mojawapo Kati ya hayo hapo juu yamejitokeza basi mhusika atapitia Hizo Marriage Board nimezitaja hapo juu, Nashuri Kama ni Mkristo usipitie kanisani ni kupoteza muda nenda ustawi moja kwa moja onyesha kwamba hamuwezi kuishi Tena pamoja kivyovyote vile utapata Certificate ambayo utaitumia kufungua shauri mahakamani.

NB: Baada ya talaka kutoka ni mgawanyo wa Mali

"Ndoa na iheshimiwe na watu wote"
======
The Law is the reflection of peoples culture, when the law comes into being it intends to be a servant of man and not making men servants of the law thus the law will regulate the conduct of the society,protect individuals and also give retribution or redress to the people whose rights are violated, therefore I will speak on the issue of law being the custodian of marriage.

First of all family is one of the most basic pillar of the society, strong nations are built on firm families therefore the state has a sacred duty to protect families. It allows for divorce just as the Tanzanian Law of Marriage Act says but it has made it a very hard thing to attain, it starts with the requirement of two years prolonged cohabitation.

Also it demands the families to visit the marriage reconciliation board which is vested with power under the Act to give room for couples to talk openly on issues pertaining their marriage, remember the marriage reconciliation board is created by the Minister Responsible and if the board fails to keep the marriage intact there will be a presumption that the board if failing to do the job it was assigned to do.

But comes circumstance where one party suffers unnecessarily and excessively that he or she cannot bear it anymore, here also the Act mentions of things like cruelty and many things just find the Act. Kumbuka ndoa inalindwa sana na serikali hivyo huwezi kuamua kutoka bila kutoa sababu za msingi za kwanini unataka talaka na pia hiyo bodi ya usuluhishi ni laziama iwe imeridhia kwamba ndoa yenu haiwezi kuendelae teena hivyo kuwaruhusu muende mahakamani kwa ajili ya talaka.

Kama nilivyosema kwamba serikali inalinda saana ndoa ndiyo maaana kabla hata ya kutoa talaka wanandoa wanaweza kukubaliana kupeana mapumziko ambayo kwa lugha ya kiingereza we call it Separation,haya yanaweza kuwa ni uamuzi wenu au mahakama yenyewe ikawaamulia. This action have a psychological impact on the both couples kwasababu kama mnapendana mtatafutna Japo kama muda wa zaidi ya miaka mitatu itapita bila nyinyi wajamaa kukumbukana then tutajua marrige is irreparably broken down therefore lazima talaka itolewe kama moja atadai.

Suala la mali siku hizi limekuwa utata because women are highly protected na kumbuka kabla hamjaona kama huna nia ya kuifanya mali yako kuwa ya familia or Matrimonial property then inabidi utamke kabisa na kama hutasema basi kwenye kugawana ni lazima mwanamke aangaliwe saana kwasababu kumbuka hata kama umejenga nyumba wakati wa ndoa ikatokea upepo makali ukaja ukavunja madirisha basi mke wako akanunua vioo vipya then her contribution will be put into consideration ila hii ni pale ambapo mali haijasemwa ni ya nani.

On the other hand kumbuka hata pale ambapo unaenda kazini mkeo anakuamsha na kukwambia baba fulani maji tayari,kakunyooshea nguo na unakuta chai iko mezani unakunywa unaondoka na kwenda kazini kwa furaha na unapata mshahara by one way or another her contribution made you get the salary running through your wallet therefore lazima alindwe.

Pia mtoto kama ni mdogo kama ni chini ya miaka saba lazima akakae na mama yake huko hata kama atampendaje baba yake here what is put into consideration is the best interest of a child lakini kama ni zaidi ya hapo pia itaangaliwa ni mzazi yupi ambaye anaweza kuishi vizuri na mtoto kumbuka kama mama ni wa hovyo kama mlevi sugu hawezi kukaa na mtoto hapo mahakama itaweza kumruhusu baba kama utakuwa na uwezo ila kwa

Uingereza mtoto akiwa mdogo halafu wazazi hamueleweki then serikali itamchukua kwa nguvu mtoto akikaa na mama ni lazima uwe unapeleka hela za mahitaji, tafuat Marriage Act na Usome yote ni rahisi kueleweka saaana.
======
Kinachoangaliwa zaidi katika sheria za familia (family laws) hususani pale ndoa inapovunjika au mume na mke kutengana, ni haki za wahusika katika familia hiyo (yaani baba, mama na mtoto). Kama familia ilikuwa na mali iliyochumwa pamoja akiwemo mtoto, sheria inatembeza mgawo kati ya wahusika, miongoni mwa mali za wazazi ni mtoto/ watoto wakati mali ya mtoto ni "matunzo bora".

Kanuni ya jumla ni kwamba baba ndie mwenye mtoto. Mtoto anakuwa kwa mama pale tu mazingira ya ustawi wake (walfare of the child) yatapothibitishwa kuwa yatalindwa na kumwezesha mtoto huyo kukua vyema.

Sheria ya ndoa inahusu zaidi wana ndoa na watoto waliopatikana ndani ya ndoa. Kwa wale ambao hawapo kwenye ndoa, bado sheria inatambua kuwa mtoto ni mali ya Baba. Kwa mfano sheria ya "Affiliation" inampa haki mama wa mtoto anayetarajiwa kuzaliwa au aliekwishazaliwa kuwasilisha ombi maalumu katika mahakama (Mahakama ya Wilaya) kutaka utambuzi wa baba wa mtoto husika na kumtaka baba huyo (putative father) kutoa matunzo kwa mtoto aliyezaliwa ambaye kwa mujibu wa sheria hii anatambulika kama mtoto haramu (illegitimate child). Matunzo kwa mtoto aliyezaliwa nje ya ndoa (out of wedlock) yanaweza kukoma ikwa baba wa mtoto ataiomba mahakama ifanye hivyo kwa kuthibitisha kuwa mtoto ametimiza miaka 14 au mama husika wa mtoto ameolewa au kuingia kwenye mahusiano ya "ki unyumba (cohabitation)" na mwanaume ambaye alikuwa ameacha.

Pia mahakama ikijiridhisha kwa sababu nyingine. Amri ya mahakama ya kumtaka baba wa mtoto atoe matunzo kwa sheria ya "Affiliation" inapoteza nguvu mara baada ya mtoto kutimiza miaka 16. (kuna dhana kuwa atakuwa ameanza kujitegemea).

Ni sawia kuwa mtoto akiwa na umri usiozidi miaka saba (7) akakaa kwa mama lakini uzoefu umeonyesha kuwa akina mama wengi wamekuwa wakitumia fursa hiyo kuchuma kupitia mgongo wa mtoto. Utakuta mama ameolewa na mume mwingine au yupo nje ya eneo ambalo mtoto yupo anapiga "uchangu" na ana mbwaga mtoto kwa bibi au ndugu, lakini bado anataka apewe matunzo ya mtoto huyo ambayo hayamfikii mtoto.

Katika mazingira kama haya, baba wa mtoto anayo haki ya kuomba mahakama apewe hifadhi ya mtoto na matunzo kukatishwa kwani kanuni ya jumla ya mtoto kuwa kwa mama itakuwa imekiukwa!.
======
Kwa upande wa mgawanyo wa mali baada ya talaka Sheria ya Ndoa ya Mwaka 1971 imeelezea katika Kifungu cha 114 kama ifuatavyo:

"114. Power of court to order division of matrimonial assets
(1) The court shall have power, when granting or subsequent to the grant of a decree of separation or divorce, to order the division between the parties of any assets acquired by them during the marriage by their joint efforts or to order the sale of any such asset and the division between the parties of the proceeds of sale.
(2) In exercising the power conferred by subsection (1), the court shall have regard–
(a) to the customs of the community to which the parties belong;
(b) to the extent of the contributions made by each party in money, property or work towards the acquiring of the assets;
(c) to any debts owing by either party which were contracted for their joint benefit; and
(d) to the needs of the infant children, if any, of the marriage,
and subject to those considerations, shall incline towards equality of division.
(3) For the purposes of this section, references to assets acquired during the marriage include assets owned before the marriage by one party which have been substantially improved during the marriage by the other party or by their joint efforts."


Katika kuelezea kifungu hicho Mahakama ya Rufani katika Kesi ya Bi Hawa Muhamed v. Ally Seif [1983] TLR 32 (CA) iliangalia "contribution" ya kila mwanandoa katika mgawanyo wa mali. Mahakama ilienda mbali zaidi kwa kusema kwamba hata zile kazi za "ugolikipa" za nyumbani zinachangia katika mali za familia! Katika ukurasa wa 44 Mahakama ilisema, pamoja na mambo mengine, kama ifuatavyo:

"Guided by this objective of the Act, we are satisfied that the "joint efforts" and "work towards the acquiring of the assets" have to be construed as embracing the domestic "efforts" or "work" of husband and wife."
======
Ili kuweza kufungua shauri la talaka Mahakamani yakupasa kwanza kwenda kwenye baraza la usuluhishi (Mariage Reconciliation Board) baada ya kufika kwenye Baraza la usuluhishi mtasikilizwa wakishindwa kuwasuluhisha ndipo mtaenda Mahakamani. Mahakamani utaenda na hati kutoka Baraza la Usuluhishi Ikionyesha kuwa limeshindwa kuwasuluhisha (kuna mazingira tofauti kuwa Imeshindikana kuwasuluhisha) Baraza la usuluhishi kupitia ni takwa la sheria japo kuna exceptional.

Ukifika Mahakamani baada ya kufungua shauri lazima uoneshe kuwa ndoa imevunjika na hairekebishiki tena (breakdown beyond repair) na vigezo vinavyotumika miongoni mwao kuonyesha kuwa hairekebishiki tena vinaweza kuwa vifuatvyo 1. Ugoni 2. Kutelekezwa 3. Ukatili n.k Lakini pia mahakama yaweza kwa mtazamo wake kwa kuzingatia mazingira ya ndoa na namna mambo yanavoenenda ikaona ndoa imevunjika beyond repair japo mmbo yaliyotajawa na sheria hayapo.

Mahakama itatoa talaka kuvunja ndoa na kufuatia kugawa Mali iliyo ya Ndoa na kuzingatia Malezi ya watoto.
Kwa Ujumla Mtoto chini ya Miaka saba anastahili kukaa na Mama ake Lakini Mahakama yaweza kuamua vinginevyo Kuzingatia mwenendo na Tabia ya mama na Kigezo cha Kuweka mtoto kwa Baba au Mama ni Maslahi Bora ya Mtoto katika ukuaji wake(Welfare of the child).

Kwa kifupi nimeona nichangie ivyo.
 
Wafanye some editing kwa zamani miaka saba ata darasa la kwanza bado kwa sasa wangefanya miaka 5 inatosha
 
Salaam!
Kuna kipengele katika sheria ya ndoa kinachosema kua pindi ndoa inapovunjika Mtoto atakaa kwa mama yake mpaka afikishe miaka saba then baba anaweza kumchukua!!...

Sheria haisemi hivyo, sheria iko wazi kwamba mtoto anaweza kutunzwa na baba au mama wakati wowote :

The court may, at any time, by order, place an infant in the custody of his or her father or his or her mother or, where there are exceptional circumstances making it undesirable that the infant be entrusted to either parent, of any other relative of the infant or of any association the objects of which include child welfare.

Hiyo unayosema wewe ni dhana inayopingika "rebuttable pressumption" kwa hiyo huyo rafikiyo alichotakiwa kufanya ni kupinga dhana hiyo kwamba ni vizuri mtoto akakaa na baba yake badala ya mama pamoja na kuwa mtoto ni chini ya miaka saba.

There shall be a rebuttable presumption that it is for the good of an infant below the age of seven years to be with his or her mother but in deciding whether that presumption applies to the facts of any particular case, the court shall have regard to the undesirability of disturbing the life of the infant by changes of custody.

Hata hivyo zingatia kuwa kwenye kufikia uamuzi wa aina yoyote mahakama inaangalia vigezo vingi ikiwemo vifuatavyo:

In deciding in whose custody an infant should be placed the paramount consideration shall be the welfare of the infant and, subject to this, the court shall have regard to
(a) the wishes of the parents of the infant;
(b) the wishes of the infant, where he or she is of an age to express an independent opinion; and
(c) the customs of the community to which the parties belong.
 
Kimey,

Lakini kwanza tujiulize mswali yafuatayo:

1. Mtoto ni wa nani? Mama? Baba? Wote?
2. Kama ni wa wote, ni vipi mmoja wao awe na haki zaid ya kukaa na mtoto kuliko mwingine?

Suala la mtoto mdogo kukaa na mama sio automatic!Inategemea na mazingira ya huyo mama. Mahakama/sheria inamtizama zaidi mtoto kuliko wazazi. Je mtoto atafaidika (kiafya, malezi nk) zaidi wapi? kwa baba au kwa mama? Kama wote hawafai, wote wanapoteza haki ya kukaa na mtoto!
 
Ngambo Ngali,
Mkuu thanx ngoja nitamwambia kuhusu hichi kifungu maana si unajua tena si sheria tunazisikia tu juu juu.....
 
Mie naona angekaa tu na mama yake mpaka afikie umri wa kujitambua mwenyewe sasa na kuamua akae na nani.
 
Mama anafanya mtoto mtaji na kumkomoa jamaa!!

Kumbuka kuwa hii ni sheria ya kizamani kidogo ambayo ilifikiria kuwa mama atakuwa nyumbani kila siku kwa sasa mama ni mbangaizaji.

Kama baba na matunzo ya watoto muda mwingi ni day care centre, nursery school, bording school to university.

Kama mtoto anaweza kwenda day care kwa nini asikae na baba hata kama ana miaka 3 au minne?
 
Mie naona angekaa tu na mama yake mpaka afikie umri wa kujitambua mwenyewe sasa na kuamua akae na nani

Kinachoangaliwa zaidi katika sheria za familia (family laws) hususani pale ndoa inapovunjika au mume na mke kutengana, ni haki za wahusika katika familia hiyo (yaani baba, mama na mtoto). Kama familia ilikuwa na mali iliyochumwa pamoja akiwemo mtoto, sheria inatembeza mgawo kati ya wahusika, miongoni mwa mali za wazazi ni mtoto/ watoto wakati mali ya mtoto ni "matunzo bora".

Kanuni ya jumla ni kwamba baba ndie mwenye mtoto. Mtoto anakuwa kwa mama pale tu mazingira ya ustawi wake (walfare of the child) yatapothibitishwa kuwa yatalindwa na kumwezesha mtoto huyo kukua vyema.

Sheria ya ndoa inahusu zaidi wana ndoa na watoto waliopatikana ndani ya ndoa. Kwa wale ambao hawapo kwenye ndoa, bado sheria inatambua kuwa mtoto ni mali ya Baba. Kwa mfano sheria ya "Affiliation" inampa haki mama wa mtoto anayetarajiwa kuzaliwa au aliekwishazaliwa kuwasilisha ombi maalumu katika mahakama (Mahakama ya Wilaya) kutaka utambuzi wa baba wa mtoto husika na kumtaka baba huyo (putative father) kutoa matunzo kwa mtoto aliyezaliwa ambaye kwa mujibu wa sheria hii anatambulika kama mtoto haramu (illegitimate child).

Matunzo kwa mtoto aliyezaliwa nje ya ndoa (out of wedlock) yanaweza kukoma ikwa baba wa mtoto ataiomba mahakama ifanye hivyo kwa kuthibitisha kuwa mtoto ametimiza miaka 14 au mama husika wa mtoto ameolewa au kuingia kwenye mahusiano ya "ki unyumba (cohabitation)" na mwanaume ambaye alikuwa ameacha.

Pia mahakama ikijiridhisha kwa sababu nyingine. Amri ya mahakama ya kumtaka baba wa mtoto atoe matunzo kwa sheria ya "Affiliation" inapoteza nguvu mara baada ya mtoto kutimiza miaka 16. (kuna dhana kuwa atakuwa ameanza kujitegemea).

Ni sawia kuwa mtoto akiwa na umri usiozidi miaka saba (7) akakaa kwa mama lakini uzoefu umeonyesha kuwa akina mama wengi wamekuwa wakitumia fursa hiyo kuchuma kupitia mgongo wa mtoto. Utakuta mama ameolewa na mume mwingine au yupo nje ya eneo ambalo mtoto yupo anapiga "uchangu" na ana mbwaga mtoto kwa bibi au ndugu, lakini bado anataka apewe matunzo ya mtoto huyo ambayo hayamfikii mtoto.

Katika mazingira kama haya, baba wa mtoto anayo haki ya kuomba mahakama apewe hifadhi ya mtoto na matunzo kukatishwa kwani kanuni ya jumla ya mtoto kuwa kwa mama itakuwa imekiukwa!.
 
Kimey,

Mara nyingi tumekuwa na migogoro ya hapa na pale ndani ya nyumba na nimekuwa nikifikiri kuwa endapo itatokea ikafikia tunaachana nini hatima ya mtoto nimekuwa nikitafuta suluhu kwasababu ya mtoto wetu, mwanzoni mamaa alikuwa ananiambia anaondoka na alikuwa nataka kuondoka na mtoto na kwa sababu nampenda sana mtoto wangu na sitaki ateseke.

Nimekuwa nikimzuia mama asiondoke ila mara ya mwisho ambapo tukuwa na utata mama alikuwa tayari kuondoka na kuniachia mtoto kutokana na kwamba nilimtishia usalama wa mtoto iwapo ataondoka naye ingawa tulifika muafana na bado tuko pamoja ila nimeamua kwasasa akilianzisha n itamruhusu aondoke na aniachie mtoto kwasababu nina hakika hana uwezo wa kumtunza.
 
Ngambo Ngali,
Asante sana mkuu kwa ufafanuzi wa kisheria. Ila pia nitapenda utuuleze kuwa kwa mfano baba aliwatelekeza au kutelekeza mtoto na mama kwa kuda mrefu bila sababu ya msingi. Na hasa pale ambako hakuzuiwa kuwaona au kumwoana mtoto na mzazi mweziwe. Na kuwa mama huyo anatunza mtoto/watoto peke yake in everything. Je naomba usaidie yafuatayo:

1. Baba huyo anaweza kuomba custody ya mtoto hata kama ni over 7 or 14 years na akakubaliwa wakati hana upendo na interest na mtoto/watoto?

2. Kwa kisheria mtoto/watoto hao watakuwa chini ya nani?


3. Je, haiwezekani akina baba wa aina hiyo wakanyang'anywa ile haki ya kuwa bilogical father? Naamini baba unaheshimika kwa kumtunza mtoto na si kumzaa na kumtelekeza kwa makusudi

4. Je, na talaka inaweza kutolewa kwa baba ambaye kaitelekeza familia kwa kuwa amepata kimada na kwa kuwa anataka aoe kimada kile basi anawahi mahakamani kupata talaka. Je mke huyo hawezi kuweka pingamizi kwa kuwa mume huyo not innocent as he descerted the family?

Mkuu leta utaalam hapa ili tuisaidie jamii. Kuna ndoa na akina mama wanapata shida na hawajui sheria itawasaidiaje.
 
@Maane,
Mkuu pata ufafanuzi huu wa kina na bure kabisa. Kama kuna zaidi usisite kurudi JF kuuliza hii ndo huduma kwa mteja, ukiridhika kumbuka kuchangia JF ili iendelee kuwepo na kuwahudumia wadau wake:

<U>
A: WAJIBU KATIKA NDOA

Sheria ya ndoa ya Tz ya Mwaka 1971 inaweka wajibu ufuatao:

..Except where the parties are separated by agreement or by

decree of the court and subject to any subsisting order of the court,

(a) it shall be the duty of every husband to maintain his wife or
wives and to provide them with such accommodation, clothing
and food as may be reasonable having regard to his means and
station in life

(b) it shall be the duty of every wife who has the means to do so,
to provide in similar manner for her husband if he is incapacitated,

wholly or partially, from earning a livelihood by r n of mental
or physical injury or ill-health

MATUNZO KWA MKE AU MUME

Iwapo wanandoa wametenganishwa au kuachanishwa kwa amri ya Mahakama sheria inasema:

Where a decree of separation or divorce is granted, it shall include provision for the maintenance and custody of the infant children, if any, of the marriage


***Ikumbukwe kuwa amri ya kutengana (separation) kunazuia tu kwa wahusika kukutana kinyumba (cohabitation) na sio kuvunja ndoa kama ilivyo kwa amri ya kuachana au talaka.

Kuhusu matunzo sheria inatoa mamlaka kwa mahakama kutoa amri ya kumtaka mwanaume kutoa matunzo kwa mkewe (kwa kuzingatia kipato cha huyo mume) katika mazingira yafuatayo:




  • Kama hampi huduma wakati bado wapo pamoja;
  • Kama amemtelekeza (if he has deserted her, for so long as the desertion continues)
  • Katika kipindi ambapo shauri la ndoa linashughulikiwa mahakamani
  • Wakati watakapo tenganishwa
  • Katika kipindi cha talaka (divorce) ambapo mahakama itazingatia mazingira ya hasili ya mwanamke huyo na kuwa matunzo yatakoma tu baada ya mke huyo kuolewa na mume mwingine au pale mahakama itakapo tengua amri hiyo ya matunzo.
:confused:*******Ikumbukwe kuwa ikiwa mke ametelekezwa, yeye ndie anapaswa kuomba matunzo kwa kuwasilisha maombi maalumu Mahakamani.

Amri ya matunzo inaweza kutolewa pia dhidi ya mwanamke ambaye ana dhamana ya kumhudumia mume asiye na uwezo.

B: HIFADHI NA MATUNZO KWA MTOTO

Kuhusu hifadhi ya watoto sheria inaeleza ifuatavyo:

The court may, at any time, by order, place an infant in the custody of his or her father or his or her mother or, where there are exceptional circumstances making it undesirable that the infant be entrusted to either parent, of any other relative of the infant or of any association the objects of which include child welfare


There shall be a rebuttable presumption that it is for the good of an infant below the age of seven years to be with his or her mother but in deciding whether that presumption applies to the facts of any particular case, the court shall have regard to the undesirability of disturbing the life of an infant by changes of custody.

Where there are two or more children of a marriage, the court shall not be bound to place both or all in the custody of the same person but shall consider the welfare of each independently.

An order for custody may be made subject to such conditions as the court may think fit to impose, and subject to such conditions, if any, as may from time to time apply, shall entitle the person given custody to decide all questions relating to the upbringing and education of the infant.

MASHARTI YA KUTUNZA MTOTO

Kuhusu kumtunza mtoto sheria inasema:


an order for custody may-
(a) contain conditions as to the place where the infant is to reside, as to the manner of his or her education and as to the religion in which he or she is to be brought up;


(b) provide for the infant to be temporarily in the care and control of some person other than the person given custody;

(c) provide for the infant to visit a parent deprived of custody or any member of the family of a parent who is dead or has been deprived of custody at such times and for such periods as the court may consider reasonable;

(d) give a parent deprived of custody or any member of the family of a parent who is dead or has been deprived of custody the right of access to the infant at such times and with such frequency as the court may consider reasonable; or

(e) prohibit the person given custody from taking the infant out of Tanzania.


MZAZI WA MTOTO KUPOTEZA HAKI YA KUMTUNZA MTOTO

Ili kumlinda mtoto, Sheria ya ndoa ina mpa pia ndugu wa mume au mke kuomba hifadhi ya mtoto na pia mzazi wa mtoto anaweza kuhesabika hana uwezo wa kukaa na mtoto. Sheria inasema yafuatayo:


The court may, when granting a decree of separation or divorce or at any time thereafter, on the application of the father or the mother of any infant of the marriage, or where the father or mother is dead, on the application of a relative of the deceased parent, make an order declaring either parent to be a person unfit to have the custody of the infant and may at any time rescind any such order

Kuhusu nani ana haki ya kukaa na mtoto ndoa inapobatilishwa sheria ina sema:

Where a marriage is a nullity or is annulled,..(..) the mother shall, in the absence of any agreement or order of court to the contrary, be entitled to the custody of the infant child, if any, of the marriage


Matunzo ya mtoto:

Save where an agreement or order of court otherwise provides, it shall be the duty of a man to maintain his infant children, whether they are in his custody or the custody of any other person, either by providing them with such accommodation, clothing, food and education as may be reasonable having regard to his means and station in life or by paying the cost thereof


it shall be the duty of a woman to maintain or contribute to the maintenance of her infant children if their father is dead or his whereabouts are unknown or if and so far as he is unable to maintain them.

C: HAKI YA MAMA KUOMBA MATUNZO:

Mwana ndoa yeyote anaweza kuomba matunzo kwa kuwasilisha maombi maalumu kwa ajili hiyo Mahakamani, ikiwa ana sababu za msingi kama kutelekezwa na wenzi wake. Sheria inaelekeza hivi:

The court may at any time order a man to pay maintenance for the benefit of his infant child-

a) if he has refused or neglected to adequately provide for him or
her; or
(b) if he has deserted his wife and the infant is in her charge; or
(c) during the pendency of any matrimonial proceedings; or
(d) when making or subsequent to the making of an order placing
the infant in the custody of any other person.

The court shall have the corresponding power to order a woman to pay or contribute towards the maintenance of her infant child where it is satisfied that having regard to her means it is reasonable so to order.

The court may, in its discretion, when ordering payment of maintenance for the benefit of an infant, order the person liable to pay such maintenance to secure the whole or any part of it by vesting any property in trustees upon trust to pay such maintenance or part thereof out of the income from such property, and subject
thereto, in trust for the settlor

MUDA WA KUTOA MATUNZO:

Save where an order for custody or maintenance of an infant and is expressed to be for any shorter period or where any such order has been rescinded, it shall expire on the attainment by the infant of the age of eighteen years.


D: TALAKA

Kuhusu taraka sheria ya ndoa inaweka bayana haki ya mwana ndoa yeyote kuomba talaka au kutenganishwa. Kuhusu taraka, Mahakam inaweza kutoa pale itakaporidhika kuwa ndoa kati ya mwombaji na mjibu maombi imevunjika na haiwezi tenga kutengamaa au kurekebishika(broken down irreparable). Sheria inaelekeza ifuatavyo:

Any married person may petition the court for a decree of separation or divorce on the ground that his or her marriage has broken down. but no decree of divorce shall be granted unless the court is satisfied

that the breakdown is irreparable.

Sheria inaweka vigezo vifutavyo kutambua kuwa ndoa haiwezi kutenga maana na ndio sababu zinazomwezesha mwanandoa kuomba talaka;

(a) pale mwomba talaka atakapothibitisha kuwa mwezake ametenda uzinzi (adultery) zaaidi ya mara moja na anaendelea kufanya hivyo;

(b)
mjibu maombi/ mdaiwa ni msumbufu katika ndoa (sexual perversion)

(c) mjibu maombi/ mdaiwa ametenda vitendo vya kikatili kwa mfano kumpiga mdai au watoto vipigo visivyo cha kawaida au kumnyima chakula nk (cruelty) ;

(d) mjibu maombi/ mdaiwa kutokuwa tayari kwa makusudi kutoa unyumba au kushiriki tendo la ndoa.

(e) mjibu maombi/ mdaiwa kumtelekeza mdai au familia kwa zaidi ya miaka mitatu


(f) iwapo mjibu maombi/ mdaiwa atakuwa amehukumiwa kifungo cha maisha zaidi ya miaka mitano jela (ili litazingatia zaidi aina ya kosa alilotenda na kifungo anachotumikia) si wakati wote inaweza kusaidia.

(g) Iwapo itathibitishwa na madaktari zaidi ya mmoja wenye uzoefu na magonjwa ya akili kuwa mjibu maombi/ mdaiwa anasumbuliwa na ugonjwa wa akili ambao hawezi kupona.

(h)
Iwapo mjibu maombi/ mdaiwa atakuwa amebadili dini ikiwa wahusika wote walikuwa wakifuata dini moja wakati walipooana na ikiwa kwa sharti la dini hiyo inaweka sharti kuwa kubadili dini kunaweza kuvunja ndoa (change of religion by the respondent, where both parties followedthe same faith at the time of the marriage and where accordingto the laws of that, faith a change of religion dissolves or is aground for the dissolution of marriage) .


UTARATIBU WA KUWASILISHA MAOMBI YA TARAKA MAHAKAMANI


Sheria ya Ndoa inatafsri ndoa kuwa ni muungano wa hiyari kati ya mtu mke na mtu mume ambao wamedhamiria kuishi pamoja katika maisha yao yote. Adidha, ndoa inachukuliwa kama mkataba ambao unaweza pia kuvunjika iwapo kuna tatizo au kutokuelewana kwenye masharti ya makubaliano hayo au mmoja kati ya wahusika kushindwa kuheshimu au kutotimiza wajibu wake katika makubalinao.

Hata hivyo, ndoa haiwezi kuvunjwa iwapo haijaikisha umri unaotambulika kisheria na maombi ya kuivunja hayajazingatia utaratibu wa kuyawasilisha Mahakamani. Sheria ya ndoa inasema:

*******No person shall, without the prior leave of the court, petition for divorce before the expiry of two years from the date of the marriage which it is sought to dissolve. Leave shall not be granted to petition for divorce within two years of marriage except where it is shown that exceptional hardship is being suffered by the person applying for such leave******



No person shall petition for divorce unless he or she has first referred the matrimonial difficulty to a Board 'and the Board has certified that it has failed to reconcile the parties: (Board Mabaraza ya ndoa au Marriage Reconciliatory Boards)

Mabaraza ya usuluhishi ya ndoa ni yale yanayotambulika kisheria kwa mfano kupitia madhebu ya Dini kuna mabaraza yab ndoa.

Sharti la kuanzia kwenye Baraza la Usuluhisi wa ndoa linaweza lisizingatiwe katika mazingira yafuatayo:

(a) where the petitioner alleges that he or she has been deserted by, and does not know the whereabouts of, his or her spouse; or


(b) where the respondent is residing outside Tanganyika and it is unlikely that he or she will enter the jurisdiction within the six months next ensuing after the date of the petition; or

(c) where the respondent has been required to appear before the Board and has wilfully failed to attend; or

(d) where the respondent is imprisoned for life or for a term of at least five years or is detained under the Preventive Detention Act, and has been so detained for a period, exceeding six months, or

(e) where the petitioner alleges that the respondent is suffering from an incurable mental illness; or

(f) where the court is satisfied that there -are extraordinary circumstances which make reference to the Board impracticable.

E: NDOA BATILI

Sheria ya ndoa inatambua ndoa zifutazo kuwa batili:


(a) iwapo mmoja kati ya wanandoa ana umri usistahili kuingia kwenye ndoa, ambayo ni miaka chini ya miaka 15 kwa mwanamke na kumi na nane kwa mwanaume ispiokuwa kama kuna ridhaa ya wazazi au Mahakama)
(b) ndoa kati ya watu ambao wanazuiliwa na sheria kuoana au kuingia kwenye mahusiano ya ndoa, kwa mfano sheria inasema:

o No person shall marry his or her grandparent, parent, child or grandchild, sister or brother, great-aunt or great-uncle, aunt or uncle, niece or nephew, as the case may be.

oNo person shall marry the grandparent or parent, child or grandchild of his or her spouse or former spouse

oNo person shall marry the former spouse of his or her grandparent or parent, child or grandchild.

oNo person shall marry a person whom he or she has adopted or by whom he or she was adopted.

(c)Ndoa iliyofanyika na mtu ambaye kisheria anazuiliwa kuoa kutokana na kuwa na ndoa nyingine. Kwa mfano sheria inasema:

oNo man, while married by a monogamous marriage, shall contract another marriage

oNo man, while married by a polygamous or potentially polygamous marriage, shall contract a marriage in any monogamous form with any person.

oNo woman who is married shall, while that marriage subsists, contract another marriage

(d) Ndoa ambayo ilifanyika pasipo ridhaa ya mmoja wa wana ndoa kwa mfano kuhusu ridhaa sheria inasema:

No marriage shall be contracted except with the consent, freely and voluntarily given, by each, of the parties thereto.consent shall not be held to have been freely or voluntarily given if the party who purported to give it- was influenced by coercion or fraud; or was mistaken as to the nature of the ceremony; or was suffering from any mental disorder or mental defect, whether permanent or temporary, or was intoxicated, so as not fully to appreciate the nature of the ceremony, and references in this Act to ''consent'' or ''consent freely


(e) iwapo katika mahusiano ya ndoa mmoja wa wanandoa hawezi kushiriki tendo la ndoa (incapable of consummating)


(f) iwapo kuna pingamizi ambalo mahakama au Baraza la ndoa limeridhia kuwa ndoa husika haipaswi kufungwa lakini wahusika wakaamua kinyemela kufunga ndoa hiyo.

(g) Ndoa iliyofungwa wakati mmoja wa wanandoa hayupo katika eneo la kufungisha ndoa husika na hakuna shahidi anayeweza kuthibitihs uhiyari wake.

(h) Ikiwa anayehusika kufungisha ndao hakuwa na uwezo wa kufanya hivyo na wanadoa wakawa wanajua na kukaa kimya kwa makusudi.

(i) Ndoa iliyofungwa pasipo kuwepo kwa mashahidi angalau wawili

(j) Iwapo ndoa husika imeleezwa bayana na wahusika kuwa ni ya muda maalumu

(k) Ikiwa mke alifunga ndoa ya kiislamu na mumewe alipofariki akaingia kwenye ndoa nyingine akiwa bado katika kipindi cha eda (iddat)

Ndoa pia inaweza kuhesabika batili kwa hiyari ya wahusika kuachana au kuendelea (voidable marriage) katika mazingira yafuatayo:

(a) pale inapotoke mmoja wa wanadoa hawezi kutimiza tendo la ndoa (incapable of consummating)

(b) au amepata ugonjwa wa akili au kifafa
(c) au mmoja wa wanandoa anaugua ugonjwa wa zinaa wenye kuambukiza
(d) au mmoja wa wanandoa hataki kwa makusudi kushiriki tendo la ndoa
(e) Iwapo mke hajafikia miaka 18 na ridhaa ya mzazi haikupatikana wakati alipokuwa akiolewa
(f) Ikiwa itabainika kuwa Mke alipewa mimba na mwanaume mwingine.
</U>
 
Haiwezekani kukukomoa kwani hata mahakama au ustawi wa jamii wenyewe wanazingatia kipato chako kabla ya kukupangia kiasi cha kutoa matunzo.

Na isitoshe kama mama anao uwezo hapaswi kupewa chochote. Na zaidi ya hayo mtoto anapokuwa ameacha kunyonya mama akikataa kukaa nae na ikiwa ana uwezo wa kifedha anpaswa kutoa pesa za matunzo kwa baba.
 
I love this . Hivi kuna website ambapo tunaweza kupata more information? It makes for some very good reading.
 
Helo ndugu Great Thinkers naomba mnijuze unaposema mke katika sheria ya ndoa tanzania ni yupi anayetambulikana, je ukizaa na mtu na ukakaa naye bila kufunga ndoa sheria itamtambua kuwa ni mke wako, na je unapotaka kudai talaka kwa huyu ambaye hukufunga naye ndoa inakubalika kwenda mahakamani.
 
Kwa mujibu wa Sheria ya Ndoa ya Tanzania..Act No. 5 of 1971 [CAP 29 RE:2002]

Kifungu cha 9 cha sheria hii kimeifafanua ndoa kama ifuatavyo.
Meaning of marriage
(1) Marriage means the voluntary union of a man and a woman, intended to last for their joint lives.
(2) A monogamous marriage is a union between one man and one woman to the exclusion of all others.
(3) A polygamous marriage is a union in which the husband may, during the subsistence of the marriage, be married to or marry another woman or women.

Unapozungumzia mke katika ndoa ni yule ambaye mmefunga naye ndoa halali kwa mujibu wa sheria ya ndoa ya Tanzania.

Mtu ambaye umezaa naye tu bila kufunga ndoa huyo si mkeo bali ni hawara (concubine), kuzaa nae hakufanyi uhusiano wenu kuwa na hadhi ya ndoa, hivyo ukitaka mtambulike kama wanandoa ni lazima mfuate taratibu za kufunga ndoa kama sheria inavyotaka.

Talaka inatolewa na mahakama kwa wale ambao ni wanandoa halali tu (wenye cheti cha ndoa) lakini hata hivyo kifungu cha 160(1) cha sheria hii kinasema hivi;

Presumption of marriage
(1) Where it is proved that a man and woman have lived together for two years or more, in such circumstances as to have acquired the reputation of being husband and wife, there shall be a rebuttable presumption that they were duly married.

Kwa kutumia kifungu hiki basi, kama mmeishi chini ya paa moja kwa muda wa miaka miwili au zaidi na jamii inayowazunguka imekuwa ikiwatambua nyie kama wanandoa mahakama inaweza kuleta dhana ya ndoa kati yenu, lakini hii haitosaidia kupata talaka isipokuwa tu kama kuna chochote unachostahili kutokana na kuishi kwenu pamoja muda wote huo dhana hii inaweza kukusaidia kupata haki yako.
 
8 Reactions
Reply
Back
Top Bottom